-
Rumania2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kumsifu Yehova Katika Kambi na Magereza
Mbali na magereza, Rumania ilikuwa na kambi tatu kubwa za kazi ngumu. Moja ilikuwa karibu na mlango wa Mto Danube, nyingine kwenye Kisiwa Kikubwa cha Braila, na ile ya tatu ilikuwa karibu na mfereji unaounganisha Mto Danube na Bahari Nyeusi. Mwanzoni mwa utawala wa Wakomunisti, Mashahidi waliofungwa walijikuta mara nyingi pamoja na watu waliowatesa hapo awali, ambao walikamatwa kwa sababu waliunga mkono serikali ya zamani. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alijikuta pamoja na makasisi 20! Haikosi walikuwa na mazungumzo yenye kusisimua.
Kwa mfano, ndugu katika gereza moja aliongea kwa undani na profesa wa dini ambaye hapo awali aliwahoji watu waliotaka kusomea ukasisi. Ndugu alitambua mara moja kwamba profesa huyo hakujua chochote kuhusu Biblia. Mkuu wa jeshi wa ile serikali iliyoanguka alikuwa miongoni mwa wafungwa waliosikiliza.
Mkuu huyo wa jeshi alimuuliza yule profesa: “Inakuwaje kwamba mafundi wanajua Biblia vizuri kuliko wewe?”
Yule profesa akajibu: “Kwenye vyuo vikuu vya dini tunafundishwa desturi za kanisa na mambo mengineyo, lakini si Biblia.”
Huyo mkuu wa jeshi hakuvutiwa, kwa hiyo akasema: “Tulitegemea ujuzi wako, lakini sasa ninaona kwamba tumedanganyika vibaya sana.”
Hatimaye, wafungwa kadhaa walikubali kweli na wakajiweka wakfu kwa Yehova, akiwemo mtu mmoja aliyekuwa amehukumiwa kifungo cha miaka 75 kwa wizi. Utu wa mtu huyo ulibadilika sana hivi kwamba wenye mamlaka gerezani walitambua mabadiliko hayo, nao wakampa kazi mpya ambayo kwa kawaida mtu ambaye amefungwa kwa wizi hangepewa. Alipewa kazi ya kwenda mjini bila mlinzi kununua vitu vilivyohitajika gerezani!
Hata hivyo, maisha yalikuwa magumu gerezani na chakula kilikuwa haba. Wafungwa hata waliomba viazi vyao visitolewe maganda. Walikula pia viazi-sukari, nyasi, majani, na mimea mingineyo ili tu kujaza tumbo. Wafungwa kadhaa walikufa hatimaye kwa sababu ya kukosa chakula kizuri na wote waliugua ugonjwa wa kuhara damu.
Katika majira ya kiangazi ndugu walioishi karibu na mlango wa Mto Danube walichimba na kuhamisha udongo kwa ajili ya ujenzi wa bwawa fulani. Katika majira ya baridi kali walifanya kazi ya kukata matete wakisimama juu ya barafu mtoni. Walilala katika meli kuukuu ya chuma nao wakavumilia baridi, uchafu, chawa, na walinzi wasio na huruma ambao hawakujali hata mfungwa alipokufa. Lakini katika hali yoyote ile, ndugu walitiana moyo na kusaidiana kudumisha nguvu za kiroho. Fikiria kilichompata Dionisie Vârciu.
Kabla tu ya kuachiliwa, ofisa mmoja alimuuliza Dionisie: “Je, kifungo chako kimebadili imani yako, Vârciu?”
Dionisie akajibu: “Samahani! Je, wewe ungebadili suti bora kwa suti duni?”
Ofisa huyo akajibu: “La.”
Dionisie akasema: “Vivyo hivyo, gerezani humu hakuna mtu hata mmoja aliyenipa chochote kilicho bora kuliko imani yangu. Kwa nini basi niibadili?”
Ndipo ofisa huyo akampa Dionisie mkono na kusema: “U huru Vârciu. Usiache imani yako.”
Ndugu na dada kama Dionisie ni wanadamu tu. Ujasiri na nguvu zao za kiroho zilitokana na imani katika Yehova, waliyoidumisha kwa njia za ajabu.—Met. 3:5, 6; Flp. 4:13.
Kujifunza kwa Kutegemea Kumbukumbu
András Molnos anasema hivi: “Nilipata mazoea mazuri ya kiroho gerezani.” Vipi? Aliona umuhimu wa kukusanyika pamoja na ndugu kila juma ili kujifunza Neno la Mungu. András anasema: “Mara nyingi, hatukuwa na vitabu wala magazeti, kwa hiyo tulitegemea kumbukumbu. Ndugu walijitahidi kukumbuka makala za Mnara wa Mlinzi walizojifunza kabla ya kufungwa. Ndugu wachache walikumbuka kila kitu katika gazeti, hata maswali ya makala za funzo!” Baadhi yao walikumbuka vizuri makala hizo kwa sababu walikuwa wamezinakili kwa mkono kabla ya kukamatwa.—Ona sanduku, “Njia za Kufanya Nakala,” kwenye ukurasa wa 132-133.
Walipopanga mikutano ya Kikristo ndugu wenye madaraka walitangaza habari ambayo ingezungumziwa, na kila mfungwa alijitahidi kukumbuka yote aliyojua kuhusu habari hiyo kama vile maandiko na mambo aliyokuwa amesoma katika vitabu vya Kikristo vya kujifunzia Biblia. Hatimaye, wote walikutana ili kuzungumzia habari hizo. Kiongozi aliyeteuliwa kwenye mkutano alifungua kwa sala na kuongoza mazungumzo kwa kuuliza maswali. Baada ya wengine wote kutoa maelezo, ndugu huyo alitoa maelezo yake, kisha akauliza swali lingine.
Majadiliano kama hayo hayakuruhusiwa katika magereza fulani. Lakini ndugu hawakushindwa kujifunza. Ndugu mmoja anasema hivi: “Tulikuwa tukitoa kioo cha dirisha la bafu, na kukipaka mchanganyiko wa maji, sabuni, na chokaa tuliyokuwa tumetoa ukutani. Kilipokauka, tuliandika somo la siku hiyo kwenye kioo hicho. Ndugu mmoja alinong’ona maneno, huku mwingine akiyaandika.
“Tulikaa katika seli kadhaa za gereza, na vikundi vya funzo vilipangwa katika seli hizo. Kila somo lilipitishwa kutoka ndugu mmoja hadi mwingine katika ile seli yenye kioo. Ndugu katika zile seli nyingine walipataje habari hizo? Mmoja wetu aliziwasilisha kwa mfumo wa mawasiliano wa Morse kwa kugongagonga polepole ukuta au mabomba ya kupasha joto. Wakati huohuo, kila ndugu katika zile seli nyingine alitumia kikombe chake kama kifaa cha kukuza sauti kwa kukiweka ukutani au kwenye mabomba na kuweka sikio kwenye kikombe hicho. Wale ambao hawakujua mfumo wa Morse hawakuwa na budi kujifunza mfumo huo.”
Ndugu katika magereza fulani waliletewa chakula cha kiroho na dada wenye akili waliobuni mbinu mbalimbali. Kwa mfano, walipooka mikate dada hao walificha magazeti au vijitabu ndani ya donge. Ndugu waliita chakula hicho mkate kutoka mbinguni. Akina dada waliingiza hata sehemu za Biblia magerezani kwa kukunja-kunja kurasa za Biblia na kuziweka ndani ya mipira midogo ya plastiki kisha kuipaka rojo ya chokoleti na kakao.
Hata hivyo, ndugu waliweza kusoma tu walipoenda chooni. Hakuna mahali pengine ambapo askari waliwaruhusu kuwa peke yao hata kwa dakika chache. Baada ya kusoma, walificha kile walichosoma nyuma ya tangi la maji la choo. Hata wafungwa wasiokuwa Mashahidi walijua maficho hayo, na wengi wao walifurahia kusoma kwa utulivu pia.
-
-
Rumania2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/picha katika ukurasa wa 124, 125]
Tulikumbuka Mistari 1,600 ya Biblia
Dionisie Vârciu
Alizaliwa: 1926
Alibatizwa: 1948
Maelezo mafupi kumhusu: Kuanzia mwaka wa 1959, alikaa katika magereza mbalimbali na kambi za kazi ngumu kwa zaidi ya miaka mitano. Alikufa mwaka wa 2002.
Tulipokuwa gerezani, tuliruhusiwa kuwasiliana na familia zetu, na kila mwezi waliruhusiwa kutuletea kifurushi cha zawadi chenye uzani wa kilo tano. Wale tu waliomaliza kazi zao ndio waliopewa vifurushi vyao. Tulikuwa tukigawanya chakula katika sehemu 30 hivi ili kila mmoja wetu apate kiasi sawa na mwenzake. Pindi moja tuligawanya matofaa mawili katika sehemu 30 hivi. Ni kweli kwamba kila sehemu ilikuwa ndogo, hata hivyo ilipunguza njaa yetu.
Hata ingawa hatukuwa na Biblia au vichapo vya kujifunzia Biblia, tulidumisha hali yetu ya kiroho kwa kujikumbusha mambo tuliyokuwa tumejifunza kabla ya kutiwa gerezani na kwa kuyazungumzia pamoja na wengine. Tulipanga kwamba kila asubuhi ndugu mmoja akumbuke na kukariri mstari fulani wa Biblia. Kisha tukaurudia-rudia kwa sauti ya chini na kuutafakari asubuhi tulipokuwa katika matembezi ya kulazimishwa yaliyochukua dakika 15 hadi 20. Tuliporudi kwenye seli yetu yenye upana wa meta mbili na urefu wa meta nne ambapo 20 kati yetu tulikuwa tukikaa, tulitumia dakika 30 hivi kutoa maelezo kuhusu mstari huo. Tulikumbuka jumla ya mistari 1,600 ya Biblia. Alasiri, tulizungumzia habari mbalimbali kutia ndani maandiko 20 hadi 30 yanayohusiana na habari hizo. Sote tuliziweka habari hizo akilini.
Mwanzoni ndugu fulani alifikiri kwamba alikuwa mzee sana asiweze kukariri maandiko mengi ya Biblia. Lakini alikuwa tu akipuuza uwezo wake. Baada ya kutusikia tukikariri maandiko mara 20 hivi, yeye pia aliweza kukumbuka na kukariri maandiko mengi, na jambo hilo likamfurahisha sana!
Naam, tulikuwa wenye njaa na dhaifu kimwili, lakini Yehova aliendelea kutulisha na kutuimarisha kiroho. Hata baada ya kuachiliwa, tulihitaji kudumisha hali yetu ya kiroho kwa kuwa maofisa wa Idara ya Upelelezi waliendelea kutunyanyasa wakitarajia kwamba tutakana imani yetu.
-