-
Rwanda2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MAISHA GEREZANI
Maisha yalikuwa magumu gerezani. Wafungwa walipewa chakula cha mhogo na maharagwe mara moja kwa siku. Nyama ililiwa mara moja hivi kwa mwezi. Matandiko yalikuwa na kunguni, lakini kwa sababu ya msongamano, wafungwa wengi walilala sakafuni. Haikuwa rahisi kupata maji. Akina ndugu waliishi pamoja na wahalifu sugu na wajeuri. Mara nyingi walinzi wa gereza walikuwa wakali, ingawa mmoja wao, Jean Fataki, alikuwa mwenye fadhili. Alikubali kujifunza Biblia, hatimaye akabatizwa, na ni painia mwaminifu hadi sasa.
Ndugu Rwakabubu akumbuka: “Tulipokuwa gerezani, askofu huyo alifanya Misa huko gerezani. Aliwaambia wasikilizaji wake wajihadhari na Mashahidi wa Yehova. Baadaye, baadhi ya Wakatoliki waliomsikiliza wakatuuliza ni kwa nini askofu mkuu alisema hivyo, kwa kuwa waliwaona Mashahidi wa Yehova kuwa wenye amani.”
Punde si punde, Roger na Noella Poels wakawasili mjini Kigali kutoka Ubelgiji. Roger alikuwa na kandarasi ya kazi. Wale ndugu watatu walikuwa bado gerezani, hivyo, Roger akaomba kuzungumza na Waziri wa Haki ili amweleze kuhusu imani yetu na kuuliza kwa upole sababu inayofanya serikali iwachukie Mashahidi wa Yehova. Waziri huyo alikatiza mazungumzo kwa kusema: “Bwana Poels, nimekusikiliza vya kutosha! Utarudi kwenu Brussels. Hutaendelea kukaa nchini Rwanda!”
Kwa kuwa wale ndugu watatu waliendelea kuwa imara bila kutishika, walilazimika kukamilisha kifungo chao cha miaka miwili, ingawa katika mwaka wa pili walihamishiwa gereza lililokuwa afadhali kidogo. Wakaachiliwa mnamo Novemba 1984.
-
-
Rwanda2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka uliofuata, Palatin Nsanzurwimo na mkewe, Fatuma, walikamatwa na maajenti wa shirika la usalama wa Serikali. Baada ya kuhojiwa kwa saa nane na nyumba yao kupekuliwa sana, walipelekwa gerezani pamoja na watoto wao watatu. Wakiwa njiani kwenda gerezani, ndugu mdogo wa Palatin, aliyekuwa akiwafuata kwa ukaribu, akamchukua mwana wao mwenye umri wa miaka mitano na binti mwenye umri wa miaka minne ili awatunze. Palatin na Fatuma wakafungwa pamoja na mtoto wao mchanga mwenye umri wa miezi 14. Baadaye Fatuma alihamishiwa gereza lingine ambamo alikaa kwa miezi tisa.
Wakati huo, watoto wanne wa Jean Tshiteya walifukuzwa shuleni. Baadaye kidogo, aliporudi nyumbani, alipata mke wake amekamatwa, nyumba yake imepekuliwa, huku watoto wakiachwa peke yao. Muda mfupi baadaye, Ndugu Tshiteya akakamatwa na kutupwa gerezani huko Butare, akajiunga na mke wake na ndugu wengine. Baadaye, Mashahidi wote waliokuwa wamefungwa katika magereza mbalimbali huko Butare wakahamishwa na kupelekwa katika gereza kuu la Kigali. Wakati huo, watoto wa Ndugu Tshiteya walikuwa wakitunzwa na akina ndugu mjini Kigali.
Ndugu Tshiteya akumbuka: “Akina ndugu na dada walipoletwa katika gereza kuu la Kigali kutoka magereza ya maeneo mengine, walisalimiana kwa shangwe, wakisema ‘Komera!’ yaani, ‘Jipe moyo!’ Mlinzi mmoja wa gereza aliposikia salamu hiyo, alisema hivi kwa ukali: ‘Mna wazimu! Watu wanawezaje kujipa moyo gerezani?’”
-