-
Je, Tumlaumu Mungu kwa Matatizo Yetu?Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 1
-
-
Je, Tumlaumu Mungu kwa Matatizo Yetu?
WAKATI binti ya Marion, aliye mtu mzima, alipopata jeraha baya la ubongo, Marion alifanya jinsi ambavyo wengi wetu tungefanya.a Alimwomba Mungu amsaidie. “Sikumbuki wakati mwingine wowote ambapo nimewahi kuhisi nikiwa mpweke hivyo na bila msaada,” asema Marion. Baadaye, hali ya binti yake ilizorota, naye Marion akaanza kuwa na shaka kumhusu Mungu. “Kwa nini jambo hilo lilitukia?” akauliza. Hangeweza kuelewa kwa nini Mungu mwenye upendo na mwenye kujali angeweza kumwacha.
Ni jambo la kawaida kabisa kuhisi jinsi Marion alivyohisi.Watu wengi duniani wamehisi kwamba Mungu amewaacha wakati wa uhitaji. “Bado sijui ‘kwa nini MUNGU huruhusu mambo mabaya yatokee,’” asema Lisa baada ya mjukuu wake kuuawa. “Bado sijapoteza imani kabisa katika Mungu, lakini imepungua.” Pia, mwanamke mmoja alisema hivi baada ya mtoto wake mchanga wa kiume kuhusika katika msiba fulani wa kipumbavu: “Mungu hakunifariji kwa yaliyotokea. Hakunionyesha kama ananijali au kunihurumia.” Aliongeza kusema: “Sitamsamehe Mungu kamwe.”
Wengine hujawa na uchungu kumwelekea Mungu wanapotazama ulimwengu wanamoishi. Wao huona nchi zilizolemewa na umaskini na njaa, wakimbizi wa vita wasio na tumaini, watoto wengi waliopoteza wazazi kwa sababu ya UKIMWI, na mamilioni ya watu wanaosumbuliwa na magonjwa mengine. Kwa sababu ya misiba hiyo na mingineyo, wengi humlaumu Mungu kwa kuwa inaonekana kama hajali.
Hata hivyo, ukweli ni kwamba si Mungu anayesababisha matatizo yanayowapata wanadamu. Kwa kweli, kuna sababu zifaazo za kuamini kwamba hivi karibuni Mungu atabatilisha madhara yote ambayo yamewapata wanadamu. Tunakualika usome makala inayofuata na uone kwamba Mungu anatujali kwelikweli.
[Maelezo ya Chini]
a Majina yamebadilishwa.
-
-
Mungu Anakujali KwelikweliMnara wa Mlinzi—2004 | Julai 1
-
-
Je, Mungu Ndiye Husababisha Matatizo Yetu?
Mwanadamu ndiye husababisha mengi ya matatizo yanayompata. Kwa mfano, tunajua vizuri sana hatari zinazotokana na vitendo fulani. Na bado, watu hufanya uasherati, hutumia vibaya pombe na dawa nyingine, hutumia tumbaku, hushiriki katika michezo hatari, kuendesha gari kwa kasi, na kadhalika. Tumlaumu nani ikiwa mtu atateseka kwa sababu ya mazoea hayo hatari? Mungu au yule anayetenda kipumbavu? Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linasema: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.
Pia, mara nyingi wanadamu huumizana. Taifa linapotangaza vita, bila shaka, Mungu hawezi kulaumiwa kwa mateso yanayotokea. Mhalifu anapomshambulia raia mwenzake, je, tumlaumu Mungu kwa majeraha yoyote yanayotokea au kifo? La! Je, tumlaumu Mungu wakati mtawala wa kimabavu anapokandamiza, kutesa, na kuwaua watu anaotawala? Hilo halingekuwa jambo la akili.—Mhubiri 8:9.
Lakini namna gani mamilioni ya wale wanaoishi maisha ya ufukara au wana njaa? Je, tumlaumu Mungu? La, kwa kuwa dunia yetu huzalisha chakula cha kutosha kulisha kila mtu. (Zaburi 10:2, 3; 145:16) Kuna njaa na umaskini mwingi kwa sababu vitu ambavyo Mungu ametupatia havigawanywi kwa usawa. Na tatizo hilo haliwezi kutatuliwa kwa sababu ya ubinafsi wa mwanadamu.
Sababu ya Msingi
Lakini je, tumlaumu nani mtu anaposhikwa na ugonjwa au anapokufa kwa sababu ya uzee? Je, ungeshangaa kujua kwamba hatupaswi kumlaumu Mungu kwa mambo hayo? Mungu hakumuumba mwanadamu awe akizeeka na kufa.
Wakati wenzi wa kwanza, Adamu na Hawa, walipowekwa katika bustani ya Edeni, Yehova aliwapa taraja la kuishi milele katika paradiso duniani. Hata hivyo, ni wazi kwamba alitaka dunia ikaliwe na watu ambao wangethamini urithi wao. Hivyo, matarajio ya uhai wao wa wakati ujao yangetegemea sharti fulani. Adamu na Hawa wangeishi katika Paradiso ikiwa tu wangeendelea kumtii Muumba wao mwenye upendo.—Mwanzo 2:17; 3:2, 3, 17-23.
Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa waliasi. Hawa aliamua kumsikiliza Shetani Ibilisi. Shetani alimdanganya na hivyo akaonyesha kwamba Mungu alikuwa akimnyima Hawa kitu fulani kizuri. Hivyo, akaanza kujitegemea na kujaribu ‘kuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ Adamu aliungana naye katika uasi huo.—Mwanzo 3:5, 6.
Kwa kutenda dhambi hiyo, Adamu na Hawa walionyesha kwamba hawastahili kuishi milele. Walipatwa na matokeo mabaya ya dhambi. Nguvu zao zilipungua, na mwishowe wakafa. (Mwanzo 5:5) Hata hivyo, uasi wao ulikuwa na matokeo mabaya zaidi. Tungali tunateseka kutokana na dhambi ya Adamu na Hawa. Mtume Paulo aliandika: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Naam, kwa sababu ya uasi wa Adamu na Hawa, dhambi na kifo vilienea kati ya wanadamu wote kama ugonjwa wenye kuua.
-