Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Walikabiliana na Miiba Katika Miili Yao
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Februari 15
    • Walikabiliana na Miiba Katika Miili Yao

      “Nilipewa mwiba katika mwili, malaika wa Shetani, afulize kunipiga kofi.”—2 WAKORINTHO 12:7.

      1. Ni matatizo gani yanayokabili watu leo?

      JE, UNAPAMBANA na jaribu lenye kuendelea? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayepambana na jaribu kama hilo. Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ Wakristo waaminifu wanakabiliana na mnyanyaso mkali, matatizo ya kifamilia, magonjwa, mahangaiko ya kifedha, maumivu ya kihisia-moyo, kufiwa na wapendwa, na magumu mengine. (2 Timotheo 3:1-5) Katika nchi fulani, njaa na vita vinatisha maisha ya watu wengi.

      2, 3. Ni mtazamo upi usiofaa unaoweza kutokezwa na matatizo yaliyo kama miiba ambayo tunakabili, na kwa nini huenda jambo hilo likawa hatari?

      2 Matatizo hayo yanaweza kumfanya mtu ajihisi hoi kabisa, hasa ikiwa atapatwa na matatizo kadhaa kwa wakati mmoja. Ona vile lisemavyo andiko la Mithali 24:10: “Ukizimia [“ukivunjika moyo,” NW] siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” Naam, kuvunjika moyo kwa sababu ya majaribu kunaweza kufanya tukose nguvu tunazohitaji sana na kunaweza pia kudhoofisha azimio letu la kuvumilia hadi mwisho. Jinsi gani?

      3 Huenda kuvunjika moyo kukatufanya tukose usawaziko. Kwa mfano, ni rahisi sana kutilia chumvi matatizo yetu na kuanza kujihurumia. Huenda wengine hata wakamlilia Mungu, “Kwa nini unaruhusu jambo hili linipate?” Mtu akiruhusu mtazamo kama huo usiofaa usitawi moyoni mwake, basi utamkosesha furaha na uhakika. Mtumishi wa Mungu anaweza kuvunjika moyo sana hivi kwamba huenda hata akaacha kupigana “pigano bora la imani.”—1 Timotheo 6:12.

      4, 5. Katika hali fulani, Shetani anahusikaje na matatizo yetu, lakini tunaweza kuwa na uhakika gani?

      4 Bila shaka, Yehova Mungu hasababishi majaribu ambayo hutupata. (Yakobo 1:13) Matatizo mengine hutupata kwa sababu tu tunajitahidi kuwa waaminifu kwake. Kwa kweli, wote wanaomtumikia Yehova hushambuliwa na Shetani Ibilisi, adui yake mkubwa. Katika wakati wake mfupi unaosalia, ‘mungu huyo mwovu wa huu mfumo wa mambo’ anajaribu kufanya yeyote anayempenda Yehova aache kufanya mapenzi Yake. (2 Wakorintho 4:4) Shetani hutesa kadiri awezavyo ushirika mzima wa ndugu zetu ulimwenguni pote. (1 Petro 5:9) Ni kweli kwamba matatizo yetu yote hayasababishwi moja kwa moja na Shetani, lakini anaweza kutumia isivyofaa matatizo tunayokabili, akitaka kutudhoofisha zaidi.

      5 Hata Shetani au silaha zake ziwe zenye nguvu kadiri gani, tunaweza kumshinda! Tunawezaje kuwa na uhakika huo? Kwa sababu Yehova Mungu hutupigania. Mungu amehakikisha kwamba watumishi wake wanafahamu mbinu za Shetani. (2 Wakorintho 2:11) Kwa kweli, Neno la Mungu hutueleza mengi kuhusu majaribu ambayo huwasumbua Wakristo wa kweli. Kwa habari ya mtume Paulo, Biblia inatumia usemi “mwiba katika mwili.” Kwa nini? Na tuchunguze jinsi ambavyo Neno la Mungu hufafanua usemi huo. Kisha tutaona kwamba si sisi tu tunaohitaji msaada wa Yehova ili kushinda majaribu.

      Kwa Nini Majaribu Ni Kama Miiba?

      6. Paulo alimaanisha nini kwa usemi “mwiba katika mwili,” na huenda mwiba huo ulikuwa nini?

      6 Baada ya kujaribiwa vikali, Paulo alipuliziwa kuandika: “Nilipewa mwiba katika mwili, malaika wa Shetani, afulize kunipiga kofi, ili nisipate kukwezwa kupita kiasi.” (2 Wakorintho 12:7) Mwiba huo uliokuwa katika mwili wa Paulo ni nini? Bila shaka, mwiba ambao umepenya sana kwenye ngozi unasababisha maumivu. Kwa hiyo mfano huo wa mwiba unadokeza kitu ambacho kilimletea Paulo maumivu—yawe ya kimwili, ya kihisia-moyo, au yote mawili. Huenda ikawa Paulo alisumbuliwa na ugonjwa wa macho au ugonjwa mwingine. Au huenda mwiba huo ulimaanisha watu waliopinga kustahili kwake kuwa mtume na kutilia shaka thamani ya kazi yake ya kuhubiri na kufundisha. (2 Wakorintho 10:10-12; 11:5, 6, 13) Hata huo mwiba uwe ulikuwa nini, ulibaki palepale na haungeweza kuondolewa.

      7, 8. (a) Usemi ‘kufuliza kupiga kofi’ unamaanisha nini? (b) Kwa nini ni muhimu kukabiliana na miiba yoyote inayotusumbua leo?

      7 Ona kwamba mwiba huo ulifuliza kumpiga Paulo kofi. Ona pia kwamba kitenzi cha Kigiriki ambacho Paulo alitumia hapa kinatokana na neno linalotafsiriwa “konzi za vidole.” Neno hilo linatumiwa kihalisi kwenye Mathayo 26:67 na kwa njia ya mfano kwenye 1 Wakorintho 4:11. Katika mistari hiyo, neno hilo lina maana ya kupigwa ngumi. Kwa kuwa Shetani anamchukia sana Yehova na watumishi Wake, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Ibilisi alifurahi kwamba mwiba fulani ulifuliza kumpiga Paulo kofi. Leo, Shetani hufurahi tunapotaabishwa vilevile na mwiba fulani katika mwili.

      8 Kwa hiyo, kama Paulo, tunahitaji kujua jinsi ya kukabiliana na miiba hiyo. Hilo ni jambo la kufa na kupona! Kumbuka kwamba Yehova anataka kutupatia uhai wa milele katika ulimwengu mpya, ambako hatutapatwa kamwe na matatizo yaliyo kama miiba. Ili kutusaidia kupata zawadi hiyo nzuri, Mungu ametupatia mifano mingi katika Neno lake takatifu, Biblia, ambayo inaonyesha kwamba watumishi wake waaminifu walifanikiwa kukabiliana na miiba katika miili yao. Hao walikuwa watu wa kawaida, wasio wakamilifu kama vile sisi. Huenda kufikiria watu fulani miongoni mwa ‘wingu hilo kubwa la Mashahidi’ kukatusaidia “tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 12:1) Kutafakari juu ya mambo waliyovumilia kunaweza kuimarisha uhakika wetu kwamba tunaweza kukabiliana na miiba yoyote ambayo Shetani anaweza kutumia dhidi yetu.

      Miiba Iliyomsumbua Mefiboshethi

      9, 10. (a) Mefiboshethi alipataje kuwa na mwiba katika mwili wake? (b) Mfalme Daudi alimwonyeshaje fadhili Mefiboshethi, nasi tunawezaje kumwiga Daudi?

      9 Mfikirie Mefiboshethi, mwana wa Yonathani aliyekuwa rafiki ya Daudi. Mefiboshethi alipokuwa na umri wa miaka mitano, habari zilifika kwamba babake, Yonathani, na babu yake Mfalme Sauli, walikuwa wameuawa. Kwa kushtuka, yaya wa Mefiboshethi ‘alimchukua na ikawa, alipokimbia kwa haraka, huyo mtoto alianguka, akawa kilema.’ (2 Samweli 4:4) Ni lazima ulemavu huo ulikuwa mwiba kwelikweli ambao Mefiboshethi alivumilia alipokuwa akikua.

      10 Miaka kadhaa baadaye, Mfalme Daudi alimwonyesha Mefiboshethi fadhili-upendo. Alifanya hivyo kwa sababu alimpenda sana Yonathani baba ya Mefiboshethi. Daudi alimpa Mefiboshethi shamba lote la Sauli na kumweka Siba mtumishi wa Sauli alitunze. Daudi pia alimwambia Mefiboshethi hivi: ‘Utakula chakula mezani pangu daima.’ (2 Samweli 9:6-10) Yaelekea fadhili-upendo za Daudi zilimfariji Mefiboshethi na zilimpunguzia mateso yaliyotokana na ulemavu wake. Ni somo zuri kama nini! Sisi pia tunapaswa kuwaonyesha fadhili wale wanaopambana na mwiba katika mwili.

      11. Siba alidai nini kuhusu Mefiboshethi, na tunajuaje kwamba dai lake lilikuwa la uwongo? (Ona kielezi-chini.)

      11 Baadaye Mefiboshethi alilazimika kupambana na mwiba mwingine katika mwili wake. Mtumishi wake Siba alimchongea mbele ya Mfalme Daudi, ambaye alikuwa akikimbia Yerusalemu kwa sababu ya uasi wa Absalomu, mwana wa Daudi. Siba alisema kwamba Mefiboshethi si mwaminifu na alikuwa amebaki Yerusalemu akitumaini kujitwalia utawala.a Daudi aliamini uchongezi wa Siba na kumpa mwongo huyo shamba lote la Mefiboshethi!—2 Samweli 16:1-4.

      12. Mefiboshethi alitendaje kuhusu mambo yaliyompata, naye anatuwekea mfano gani mzuri?

      12 Hata hivyo, Mefiboshethi alipokutana na Daudi hatimaye, alimweleza mfalme huyo yale yaliyotokea. Mefiboshethi alikuwa akijitayarisha kujiunga na Daudi wakati Siba alipojitolea kwenda kwa niaba yake. Je, Daudi alirekebisha mambo? Si kabisa. Aligawanya lile shamba kati ya wanaume hao wawili. Jambo hilo lingeweza kuwa mwiba mwingine katika mwili wa Mefiboshethi. Je, alivunjika moyo sana? Je, alipinga uamuzi wa Daudi akilalamika kwamba haukuwa wa haki? La, alikubali kwa unyenyekevu uamuzi wa mfalme. Alizingatia mambo yafaayo, akifurahi kwamba mfalme aliyestahili kutawala Israeli alikuwa amerudi salama. Bila shaka, Mefiboshethi aliweka mfano bora sana kwa kuvumilia ulemavu, uchongezi, na kivunja-moyo.—2 Samweli 19:24-30.

      Nehemia Alikabiliana na Majaribu Yake

      13, 14. Nehemia alilazimika kuvumilia miiba gani aliporudi kujenga upya kuta za Yerusalemu?

      13 Fikiria miiba ya mfano ambayo Nehemia alivumilia aliporudi katika jiji la Yerusalemu lisilokuwa na kuta mnamo karne ya tano K.W.K. Alikuta jiji hilo likiwa bila ulinzi wowote, nao Wayahudi waliorudishwa walikuwa hawana utaratibu, wamevunjika moyo, na wasio safi mbele za Yehova. Baada ya muda mfupi, Nehemia alitambua kwamba hata ingawa Mfalme Artashasta alimruhusu kujenga upya kuta za Yerusalemu, ujenzi huo uliwachukiza magavana wa nchi jirani. Magavana hao ‘walihuzunika sana, kwa kuwa amekuja mtu kuwatakia heri wana wa Israeli.’—Nehemia 2:10.

      14 Wapinzani hao wa kigeni walifanya yote wawezayo kusimamisha kazi ya Nehemia. Lazima vitisho, uwongo, na uchongezi wao—kutia ndani wapelelezi waliotumwa kumvunja moyo—ulikuwa kama miiba yenye kudumu katika mwili wake. Je, mbinu za adui hao zilimshinda? La! Alimtumaini Mungu kabisa na kusimama imara. Hivyo, Nehemia alipomaliza kujenga upya kuta za Yerusalemu, kuta hizo zilitoa ushuhuda wenye kudumu kwamba Yehova alimwunga mkono kwa upendo.—Nehemia 4:1-12; 6:1-19.

      15. Ni matatizo gani ya Wayahudi yaliyomsumbua sana Nehemia?

      15 Akiwa gavana, Nehemia alilazimika kupambana na matatizo mengi miongoni mwa watu wa Mungu. Matatizo hayo yalikuwa kama miiba iliyomsumbua sana kwa sababu yaliathiri uhusiano wao na Yehova. Matajiri walikuwa wanatoza riba ya juu sana, nao ndugu zao maskini walilazimika kuacha mashamba yao yachukuliwe na wengine na hata kuwauza watoto wao kuwa watumwa ili kulipa madeni na pia kulipa kodi kwa Waajemi. (Nehemia 5:1-10) Wayahudi wengi walivunja Sabato na hawakuwategemeza Walawi wala hekalu. Pia, wengine walioa wake “wa Ashdodi, na Amoni, na Moabu.” Jambo hilo lilimwumiza Nehemia kama nini! Lakini miiba hiyo haikumfanya aache kazi yake. Akiwa mtetezi mwenye bidii wa sheria za uadilifu za Mungu, Nehemia alikabiliana na hali hiyo kikamilifu. Kama Nehemia, na tusiruhusu mwenendo mbaya wa wengine utuzuie kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu.—Nehemia 13:10-13, 23-27.

      Waaminifu Wengine Wengi Walikabiliana na Miiba Katika Mwili

      16-18. Isaka na Rebeka, Hana, Daudi, na Hosea walipatwa na matatizo gani ya kifamilia?

      16 Biblia ina mifano mingine mingi ya watu waliokabiliana na hali zenye kutaabisha zilizokuwa kama miiba. Matatizo ya kifamilia ndiyo sanasana yaliyosababisha miiba hiyo. Wake wawili wa Esau “waliyafanya maisha ya Isaka na Rebeka [wazazi wa Esau] kuwa machungu.” Rebeka hata alisema kwamba alichukia maisha yake kwa sababu ya wake hao. (Mwanzo 26:34, 35; 27:46, Biblia Habari Njema) Fikiria pia Hana na jinsi mke mwenza Penina ‘alivyomchokoza sana’ kwa sababu Hana alikuwa tasa. Labda hata alimchokoza mara nyingi wakiwa nyumbani. Penina pia alimchokoza hadharani—yaelekea mbele ya watu wa ukoo na marafiki—wakati familia hiyo ilipohudhuria msherehekeo huko Shilo. Uchokozi huo ulikuwa kama kushindilia mwiba katika mwili wa Hana.—1 Samweli 1:4-7.

      17 Hebu fikiria yale ambayo Daudi alivumilia kwa sababu ya wivu wa kipumbavu wa Mfalme Sauli, baba mkwe wake. Ili kuokoa uhai wake, ilimbidi Daudi aishi mapangoni katika nyika ya En-gedi, ambako alilazimika kupanda miamba hatari yenye miinuko mikali. Lazima ukosefu huo wa haki uwe ulimtia uchungu mwingi kwa kuwa hakuwa amemkosea Sauli. Hata hivyo, ilimbidi Daudi aishi maisha ya utoro kwa sababu ya wivu wa Sauli.—1 Samweli 24:14, 15; Mithali 27:4.

      18 Wazia matatizo ya kifamilia yaliyompata nabii Hosea. Mke wake alikuwa mzinzi. Ni lazima uzinzi huo ulikuwa kama miiba katika moyo wa Hosea. Na ni lazima awe aliumia kama nini mke wake alipozaa watoto wawili haramu kutokana na uasherati wake!—Hosea 1:2-9.

      19. Ni mnyanyaso gani uliompata nabii Mikaya?

      19 Mnyanyaso ni mwiba mwingine katika mwili. Fikiria yaliyompata nabii Mikaya. Ni lazima Mikaya mwadilifu awe aliumia sana kuona kwamba Mfalme Ahabu aliamini uwongo wa wazi wa manabii wasio wa kweli waliomzunguka. Naye kiongozi wa wadanganyifu hao alifanya nini wakati Mikaya alipomwambia Ahabu kwamba manabii hao wote walikuwa wakizungumza kwa “pepo wa uongo”? “Alimpiga Mikaya kofi la shavu”! Jambo baya hata zaidi ni jinsi Ahabu alivyotenda alipoonywa na Yehova kwamba vita vyake vya kutwaa tena Ramoth-Gileadi havingefanikiwa. Ahabu aliagiza Mikaya atiwe gerezani na apewe posho lililopunguzwa. (1 Wafalme 22:6, 9, 15-17, 23-28) Kumbuka pia Yeremia na jinsi alivyotendewa na wanyanyasi wake wakatili.—Yeremia 20:1-9.

      20. Naomi alilazimika kuvumilia miiba gani, naye alithawabishwaje?

      20 Kufiwa na wapendwa pia ni hali nyingine yenye kuumiza ambayo inaweza kuwa kama mwiba katika mwili. Naomi alilazimika kuvumilia kifo cha mumewe na cha wanawe wawili kilichomwumiza sana. Vifo hivyo vilikuwa vingali vinamwumiza aliporudi Bethlehemu. Aliwaambia marafiki wake wasimwite Naomi bali wamwite Mara, jina lililoonyesha uchungu aliokuwa nao kwa sababu ya mambo yaliyompata. Hata hivyo, kwa sababu ya uvumilivu wake, hatimaye Yehova alimthawabisha kwa kumpa mjukuu wa kiume ambaye alikuja kuwa mmoja wa mababu wa Mesiya.—Ruthu 1:3-5, 19-21; 4:13-17; Mathayo 1:1, 5.

      21, 22. Yobu alipoteza nini, naye alitendaje?

      21 Fikiria jinsi Yobu alivyoshtuka alipopata habari za vifo vya ghafula na vya ukatili vya watoto wake kumi wapendwa pamoja na kupoteza mifugo na watumishi wake wote. Ghafula, maisha yake yalionekana kana kwamba yamefikia mwisho! Kisha, hata kabla Yobu hajapata nguvu kutokana na mapigo hayo, Shetani akampiga kwa ugonjwa. Huenda Yobu alifikiria kwamba ugonjwa huo mbaya ungemwua. Maumivu yake yalikuwa makali sana hivi kwamba aliona kwamba kifo kingemletea kitulizo.—Ayubu 1:13-20; 2:7, 8.

      22 Na kana kwamba Yobu hakuwa ameteseka vya kutosha, mke wake alimjia akiwa mwenye huzuni na uchungu na kumwambia: “Umkufuru Mungu, ukafe!” Huo ulikuwa mwiba ulioje katika mwili wake wenye maumivu! Kisha, marafiki watatu wa Yobu wakamshambulia kwa hoja zao za uwongo badala ya kumfariji, wakimshutumu kwamba amefanya dhambi kisiri na kusema kwamba dhambi hiyo ndiyo iliyofanya apatwe na magumu hayo. Ni kana kwamba hoja zao zenye makosa zilishindilia miiba katika mwili wake. Kumbuka pia kwamba Yobu hakujua ni kwa nini mambo hayo mabaya yalikuwa yakimpata; wala hakujua kama angenusurika. Lakini, “katika mambo hayo yote Ayubu [“Yobu,” NW] hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.” (Ayubu 1:22; 2:9, 10; 3:3; 14:13; 30:17) Ingawa alisumbuliwa na miiba mingi kwa wakati mmoja, aliendelea kuwa mwaminifu. Hicho ni kitia-moyo kilichoje!

      23. Ni nini kilichowawezesha watu waaminifu ambao tumezungumzia, wavumilie miiba mbalimbali katika mwili?

      23 Bila shaka, Biblia ina mifano mingine mingi kama hiyo ambayo imetajwa. Watumishi wote hao waaminifu walilazimika kupambana na miiba yao ya mfano. Nao walikuwa na matatizo ya aina nyingi. Hata hivyo, kuna jambo moja ambalo wote walizingatia. Wote waliendelea kumtumikia Yehova. Licha ya majaribu yao yenye kutaabisha, walimshinda Shetani kwa nguvu za Yehova. Jinsi gani? Makala ifuatayo itajibu swali hilo na kutuonyesha jinsi sisi pia tunavyoweza kukabiliana na jambo lolote lililo kama mwiba katika mwili wetu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Haielekei kwamba mtu aliyekuwa mwenye shukrani na mnyenyekevu kama Mefiboshethi angepanga njama kama hiyo kwa kujitakia makuu. Inaelekea alijua sifa ya uaminifu ya babake Yonathani. Ingawa alikuwa mtoto wa Mfalme Sauli, Yonathani alitambua kwa unyenyekevu kwamba Daudi alikuwa amechaguliwa na Yehova kuwa mfalme wa Israeli. (1 Samweli 20:12-17) Yonathani hangemfunza mwanawe mchanga kutamani mamlaka ya kifalme kwa kuwa alikuwa mzazi aliyemhofu Mungu na rafiki mwaminifu-mshikamanifu wa Daudi.

  • Kukabiliana na “Mwiba Katika Mwili”
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Februari 15
    • Kukabiliana na “Mwiba Katika Mwili”

      “Fadhili yangu isiyostahiliwa yakutosha wewe.”—2 WAKORINTHO 12:9.

      1, 2. (a) Kwa nini tusishangae kwamba tunapatwa na majaribu na matatizo? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika tunapopatwa na majaribu?

      “WOTE wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Kwa nini wanyanyaswe? Kwa kuwa Shetani hudai kwamba mwanadamu humtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi tu, naye anataka sana kuthibitisha dai lake. Pindi moja Yesu aliwaonya mitume wake waaminifu hivi: “Shetani amedai kuwapata nyinyi watu ili awapepete kama ngano.” (Luka 22:31) Yesu alijua vizuri kwamba Mungu humruhusu Shetani atujaribu kupitia matatizo yenye kuumiza. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba kila tatizo linalotupata maishani husababishwa moja kwa moja na Shetani au roho wake waovu. (Mhubiri 9:11) Lakini Shetani yu tayari kutumia njia yoyote ile awezayo ili kuvunja uaminifu-maadili wetu.

      2 Biblia hutuambia kwamba hatupaswi kushangazwa na majaribu yanayotupata. Majaribu yoyote ambayo huenda yakatupata, ni ya kawaida na yenye kutazamiwa. (1 Petro 4:12) Kwa kweli, “mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu [zetu] katika ulimwengu.” (1 Petro 5:9) Leo, watumishi wote wa Mungu wanapata mkazo mkali sana kutoka kwa Shetani. Ibilisi hufurahia kuona tukiteseka kwa matatizo mengi iwezekanavyo ambayo ni kama miiba. Ili kufanya hivyo, yeye hutumia mfumo wake wa mambo ambao inaelekea unazidisha au kuifanya miiba yoyote tuliyo nayo ‘katika miili yetu’ iwe mibaya hata zaidi. (2 Wakorintho 12:7) Hata hivyo, si lazima mashambulio ya Shetani yavunje uaminifu-maadili wetu. Kama vile Yehova ‘atakavyotufanyia njia ya kutokea’ ili tuvumilie kishawishi, atafanya vivyo hivyo tunapokabili matatizo yaliyo kama miiba katika miili yetu.—1 Wakorintho 10:13.

      Jinsi ya Kukabiliana na Mwiba

      3. Yehova alimjibuje Paulo alipomwomba aondoe mwiba uliokuwa mwilini mwake?

      3 Mtume Paulo alimwomba Mungu aondoe mwiba uliokuwa mwilini mwake. “Kwa ajili ya hilo mara tatu nilimsihi sana Bwana kwamba upate kuniondoka.” Yehova alijibuje ombi la bidii la Paulo? “Fadhili yangu isiyostahiliwa yakutosha wewe; kwa maana nguvu yangu inafanywa kamilifu katika udhaifu.” (2 Wakorintho 12:8, 9) Na tuchanganue jibu hilo la Mungu ili tuone jinsi liwezavyo kutusaidia tukabiliane na matatizo yoyote yaliyo kama miiba yanayotusumbua.

      4. Paulo alinufaika kwa njia zipi kutokana na fadhili isiyostahiliwa ya Yehova?

      4 Ona kwamba Mungu alimtia Paulo moyo awe mwenye shukrani kwa fadhili isiyostahiliwa ambayo alikuwa ameonyeshwa kupitia Kristo. Bila shaka, Paulo alikuwa amebarikiwa sana katika njia nyingi. Kwa upendo, Yehova alimpa pendeleo la kuwa mwanafunzi ingawa hapo awali Paulo aliwapinga vikali wafuasi wa Yesu. (Matendo 7:58; 8:3; 9:1-4) Baadaye, kwa fadhili Yehova alimpa Paulo migawo na mapendeleo mengi yenye kusisimua. Hapa tunajifunza somo lililo wazi. Hata wakati hali ni mbaya kabisa, bado tuna baraka nyingi na tunapaswa kushukuru kwa ajili ya baraka hizo. Matatizo yetu hayapaswi kamwe kutufanya tusahau wema mwingi ambao Yehova hutuonyesha.—Zaburi 31:19.

      5, 6. (a) Yehova alimfunzaje Paulo kwamba nguvu za Mungu ‘hufanywa kamili katika udhaifu’? (b) Mfano wa Paulo ulithibitishaje kwamba Shetani ni mwongo?

      5 Fadhili ya Yehova isiyostahiliwa inatosha kwa njia nyingine. Nguvu za Mungu ni nyingi sana hivi kwamba zinaweza kutusaidia kushinda majaribu yetu. (Waefeso 3:20) Yehova alimfunza Paulo kwamba nguvu zake ‘hufanywa kamilifu katika udhaifu.’ Jinsi gani? Kwa upendo alimpa Paulo nguvu zote alizohitaji ili kukabiliana na jaribu lake. Hivyo, uvumilivu wa Paulo na tumaini lake thabiti katika Yehova ziliwadhihirishia wote kwamba nguvu za Mungu zilikuwa zinashinda kuhusiana na mwanamume huyu dhaifu na mwenye dhambi. Sasa fikiria jinsi Ibilisi, ambaye hudai kwamba wanadamu humtumikia Mungu wakati hawana matatizo yoyote, alivyohisi kuhusiana na uvumilivu huo. Uaminifu-maadili wa Paulo ulimfedhehesha sana mchongezi huyo!

      6 Hapo awali, Paulo alishirikiana na Shetani kupiga vita dhidi ya Mungu. Alikuwa pia mnyanyasaji fidhuli wa Wakristo, Farisayo mwenye bidii ambaye, yaelekea wakati mmoja aliishi maisha ya starehe kwa sababu familia yake ilikuwa tajiri. Sasa Paulo alikuwa akimtumikia Yehova na Kristo kama “mdogo zaidi sana kati ya wale mitume.” (1 Wakorintho 15:9) Hivyo, alikuwa anajitiisha kwa unyenyekevu chini ya mamlaka ya baraza linaloongoza la Kikristo la karne ya kwanza. Naye alikuwa akivumilia kwa uaminifu licha ya mwiba uliokuwa katika mwili wake. Shetani aliudhika sana kwa kuwa majaribu ambayo Paulo alipata maishani hayakupunguza bidii yake. Paulo hakusahau lile tumaini kwamba angeshiriki katika Ufalme wa mbinguni wa Kristo. (2 Timotheo 2:12; 4:18) Hata hivyo, hakuna mwiba, hata uwe wenye maumivu kadiri gani, ambao ungeweza kupunguza bidii yake. Nasi vilevile tuzidishe bidii yetu! Yehova hututegemeza wakati wa majaribu na kutukweza kwa kutupatia pendeleo la kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo.—Mithali 27:11.

      Maandalizi ya Yehova Ni Muhimu

      7, 8. (a) Yehova huwaimarisha watumishi wake leo kwa njia gani? (b) Kwa nini kusoma Biblia kila siku na kujifunza ni muhimu sana ili kuvumilia mwiba katika mwili wetu?

      7 Leo, Yehova huwatia nguvu Wakristo waaminifu kupitia roho yake takatifu, Neno lake, na udugu wetu wa Kikristo. Kama mtume Paulo, tunaweza kumtwika Yehova mizigo yetu kupitia sala. (Zaburi 55:22) Ingawa huenda Mungu asituondolee majaribu, anaweza kutupatia hekima ya kukabiliana nayo, hata yale ambayo si rahisi kuyastahimili. Yehova pia anaweza kutupatia uwezo—“nguvu ipitayo iliyo ya kawaida”—ili tuweze kuvumilia.—2 Wakorintho 4:7.

      8 Tunapataje msaada huo? Ni lazima tujifunze Neno la Mungu kwa bidii, kwa kuwa katika Neno lake tutapata faraja yake ya kweli. (Zaburi 94:19) Tunasoma katika Biblia maneno yenye kugusa moyo ya watumishi wa Mungu walipomwomba awasaidie. Tunaweza kutafakari majibu ya Yehova ambayo mara nyingi yanatia ndani maneno yenye kufariji. Kujifunza Neno la Mungu kutatuimarisha ili “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.” Kama vile tunavyohitaji kula chakula kila siku ili tupate nguvu, vivyo hivyo ni lazima tujifunze Neno la Mungu kwa ukawaida. Je, tunafanya hivyo? Ikiwa ndivyo, basi tutaona kwamba kupokea “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” hutusaidia kuvumilia miiba yoyote ya mfano ambayo huenda inatusumbua sasa.

      9. Wazee wanawezaje kuwategemeza wale walio na matatizo?

      9 Wazee Wakristo wanaomhofu Mungu wanaweza kuwa “mahali pa kujificha na upepo” wa taabu na “mahali pa kujisitiri na dhoruba” ya matatizo. Wazee, ambao wanataka kutimiza maneno hayo yaliyopuliziwa, humwomba Yehova kwa unyenyekevu na kwa unyofu awape “ulimi wa hao wafundishwao” ili waweze kujua jinsi ya kuwajibu kwa maneno yanayofaa wale wanaoteseka. Maneno ya wazee yanaweza kuwa kama mvua inayonyesha polepole na yanaweza kutuliza na kufariji akili zetu wakati wa magumu. Kwa kuzungumza “kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo,” wazee kwa kweli huwategemeza ndugu na dada zao wa kiroho ambao huenda wanachoka au kuvunjika moyo kwa sababu ya mwiba fulani katika mwili wao.—Isaya 32:2; 50:4; 1 Wathesalonike 5:14.

      10, 11. Watumishi wa Mungu wanawezaje kuwatia moyo wengine ambao wanavumilia majaribu makali?

      10 Watumishi wote wa Yehova ni sehemu ya familia yake ya Kikristo yenye umoja. Naam, sisi ni “viungo ambavyo kila kimoja ni cha kile kingine,” na tuko “chini ya wajibu kupendana.” (Waroma 12:5; 1 Yohana 4:11) Sisi hutimizaje wajibu huo? Kulingana na 1 Petro 3:8, sisi hufanya hivyo kwa ‘kuonyesha hisia-mwenzi, kuwa na shauku ya kidugu, na kuwa wenye huruma kwa njia ya wororo’ kwa wote ambao katika imani ni jamaa zetu. Sote tunaweza kuwapa ufikirio wa pekee wale wanaovumilia mwiba wenye maumivu makali katika mwili, wawe wachanga au wazee. Jinsi gani?

      11 Tunapaswa kujitahidi kuwa wepesi kutambua mateso yao. Ikiwa hatuna huruma na hatujali, tunaweza kuzidisha mateso yao bila kujua. Kufahamu majaribu yao kwapasa kutuchochea tuwe waangalifu kuhusu yale tusemayo, jinsi tuyasemavyo, na jinsi tutendavyo. Tukiwa wenye kujenga na kutia moyo, tunaweza kupunguza maumivu makali ya mwiba wowote unaowasumbua. Hivyo, tunaweza kuwa kwao msaada wenye kutia nguvu.—Wakolosai 4:11.

      Jinsi Ambavyo Wengine Wamefanikiwa Kukabiliana na Mwiba

      12-14. (a) Mkristo mmoja alifanya nini ili kukabiliana na kansa? (b) Ndugu na dada wa kiroho wa mwanamke huyu walimtegemeza na kumtia moyo jinsi gani?

      12 Tukaribiapo mwisho wa siku hizi za mwisho, “maumivu makali ya ghafula ya taabu” yanaongezeka kila siku. (Mathayo 24:8) Hivyo, yaelekea majaribu yatawapata watu wote duniani, hasa watumishi waaminifu wa Yehova, wanaojitahidi kufanya mapenzi yake. Kwa mfano, fikiria Mkristo mmoja aliyekuwa mhudumu wa wakati wote. Alipimwa na kupatikana na ugonjwa wa kansa na ikawa lazima apasuliwe ili tezi zake za mate na za limfu ziondolewe. Wakati yeye na mumewe walipojua kwamba alikuwa na ugonjwa huo, walimwendea Yehova mara moja kwa sala ndefu ya kumsihi. Baadaye alisema kwamba walipata amani nyingi ajabu. Hata hivyo, hali yake haikuwa shwari wakati wote, hasa alipokuwa anakabiliana na matatizo yaliyotokana na matibabu yake.

      13 Ili kukabiliana na ugonjwa wake, dada huyo alijaribu kujifunza mengi awezavyo kuhusu kansa. Alishauriana na madaktari wake. Alisoma katika Mnara wa Mlinzi, Amkeni!, na vichapo vinginevyo vya Kikristo, masimulizi ya maisha yanayoonyesha jinsi watu fulani walivyokabiliana kihisia-moyo na ugonjwa huo. Alisoma pia maandiko ya Biblia yanayoonyesha uwezo wa Yehova wa kutegemeza watu wake wakati wa matatizo, na habari nyingine zenye manufaa.

      14 Makala moja iliyozungumzia jinsi ya kukabiliana na hali ya kukata tamaa ilitaja maneno haya yenye hekima: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe.” (Mithali 18:1) Kwa hiyo, makala hiyo ilitoa ushauri huu: “Usijitenge.”a Dada huyo anaeleza hivi: “Wengi waliniambia kwamba walikuwa wanasali kwa ajili yangu na wengine walinipigia simu. Wazee wawili walinipigia simu kwa ukawaida ili kunijulia hali. Nilipokea maua na kadi nyingi sana. Wengine hata walipika chakula na wengi wakajitolea kunipeleka hospitali.”

      15-17. (a) Mkristo mmoja alikabilianaje na matatizo yaliyosababishwa na aksidenti? (b) Washiriki wa kutaniko walimsaidiaje?

      15 Dada mmoja kutoka New Mexico, Marekani, ambaye alikuwa amemtumikia Yehova kwa muda mrefu, alipatwa na aksidenti ya gari mara mbili. Alijeruhiwa shingo na mabega, hali iliyozidisha ugonjwa wake wa yabisi-kavu ambao alikuwa ameuvumilia kwa miaka 25. Anaeleza hivi: “Ilikuwa vigumu sana kwangu kuinua kichwa au kubeba kitu chochote chenye uzito unaozidi kilogramu mbili. Sala yangu ya bidii kwa Yehova na pia makala tunazojifunza katika gazeti la Mnara wa Mlinzi zimenitegemeza sana. Gazeti moja lilieleza andiko la Mika 6:8 na kusema kwamba kuwa wanyenyekevu katika kutembea na Mungu humaanisha kutambua udhaifu wetu. Jambo hilo lilinisaidia kuelewa kwamba licha ya ugonjwa wangu, sipaswi kuvunjika moyo, hata ingawa wakati niliotumia katika huduma ya shambani ulikuwa mchache kuliko nilivyotaka. Kumtumikia Mungu kwa nia nzuri ndilo jambo muhimu zaidi.”

      16 Pia anaripoti: “Siku zote wazee walinipongeza kwa jitihada zangu za kuhudhuria mikutano na kuhubiri. Wachanga walikuwa wakinisalimu kwa kunikumbatia. Wahudumu hao mapainia walinionyesha subira nyingi na mara nyingi walibadilisha mipango yao nilipokuwa mgonjwa sana nisiweze kwenda kuhubiri. Hali ya anga ikiwa mbaya, kwa fadhili wangenipeleka kwenye ziara za kurudia au kunialika kwenye mafunzo yao ya Biblia. Na kwa kuwa singeweza kubeba mfuko wa vitabu, wahubiri wengine waliweka vichapo vyangu kwenye mifuko yao nilipoenda kuhubiri.”

      17 Ona jinsi wazee wa kutaniko na waamini wenzao walivyowasaidia dada hao wawili kukabiliana na magonjwa yao yaliyokuwa kama miiba. Waliwasaidia kwa matendo na kwa fadhili ili watimize mahitaji hususa ya kiroho, kimwili, na kihisia-moyo. Je, jambo hilo halikutii moyo kuwasaidia ndugu na dada wengine walio na matatizo? Enyi wachanga, mnaweza pia kuwasaidia washiriki wa kutaniko lenu wanaopambana na miiba katika miili yao.—Mithali 20:29.

      18. Tunaweza kupata kitia-moyo gani katika masimulizi ya maisha yanayochapishwa katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!?

      18 Magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yamechapisha masimulizi mengi ya maisha na pia mambo yaliyowapata Mashahidi ambao wamekabiliana, na bado wanakabiliana na matatizo maishani. Unaposoma makala hizo kwa ukawaida, utaona kwamba wengi wa ndugu na dada zako wa kiroho ulimwenguni pote wanavumilia magumu ya kiuchumi, kufiwa na wapendwa katika majanga, na hali za vita zenye hatari. Wengine wana magonjwa yenye kulemaza. Wengi hawawezi kufanya mambo rahisi ambayo watu wengine wenye afya nzuri huyaona kuwa ya kawaida tu maishani. Wao hupatwa na majaribu makali kwa sababu ya magonjwa yao, hasa wanaposhindwa kushiriki katika kazi za Kikristo kwa kadiri ambavyo wangependa. Wanashukuru kama nini kwa msaada na utegemezo ambao ndugu na dada zao, wachanga kwa wazee, huwapa!

      Uvumilivu Huleta Furaha

      19. Kwa nini Paulo aliweza kufurahi licha ya udhaifu wake mbalimbali na majaribu yaliyokuwa kama miiba?

      19 Paulo alifurahi kuona jinsi Mungu alivyomtia nguvu. Alisema: “Kwa mteremo zaidi sana afadhali nijisifu kwa habari ya udhaifu wangu, ili nguvu ya Kristo ipate kubaki juu yangu kama hema. Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, katika matusi, katika visa vya uhitaji, katika minyanyaso na magumu, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana niwapo dhaifu, ndipo niwapo mwenye nguvu.” (2 Wakorintho 12:9, 10) Kwa sababu ya mambo yaliyompata, Paulo angeweza kusema hivi kwa uhakika: “Si kwamba ninasema kwa habari ya kuwa katika uhitaji, kwa maana nimejifunza, kuwa mwenye ujitoshelevu, mwenyewe katika hali zozote nilimo. Kwa kweli najua jinsi ya kupungukiwa na maandalizi, kwa kweli najua jinsi ya kuwa na wingi. Katika kila jambo na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji. Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:11-13.

      20, 21. (a) Kwa nini tunaweza kupata furaha kwa kutafakari juu ya “vitu visivyoonekana”? (b) Ni ‘vitu gani visivyoonekana’ unavyotarajia kuona katika Paradiso ya kidunia?

      20 Hivyo basi, kwa kuvumilia miiba yoyote iliyo katika miili yetu, tunaweza kupata furaha kubwa kwa kuonyesha kila mtu kwamba nguvu za Yehova zinafanywa kamilifu katika udhaifu wetu. Paulo aliandika hivi: “Hatufi moyo . . . Hakika mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku kwa siku. Kwa maana ingawa dhiki ni ya dakika na ni nyepesi, yafanyiza kwetu utukufu ulio na uzito wenye kuzidi zaidi na zaidi na ni wa kudumu milele; huku tukifuliza kuweka macho yetu . . . juu ya vitu visivyoonekana. Kwa maana . . . vitu visivyoonekana ni vya kudumu milele.”—2 Wakorintho 4:16-18.

      21 Leo watu wa Yehova walio wengi wanatumaini kuishi katika Paradiso yake ya kidunia na kufurahia baraka ambazo ameahidi. Tunaweza kusema kwamba ‘hatuoni’ baraka hizo leo. Hata hivyo, hivi karibuni sana tutaziona kwa macho yetu wenyewe, naam, na kuzifurahia milele. Mojawapo ya baraka hizo itakuwa kitulizo cha kuishi pasipo matatizo yaliyo kama miiba! Mwana wa Mungu ‘atavunja-vunja kazi za Ibilisi’ na “kumfanya kuwa si kitu yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo.”—1 Yohana 3:8; Waebrania 2:14.

      22. Tunapaswa kuwa na uhakika na vilevile azimio gani?

      22 Kwa hiyo, hata tuwe na mwiba gani katika mwili unaotuletea maumivu leo, na tuendelee kukabiliana nao. Kama Paulo, tutakuwa na nguvu za kufanya hivyo kwa njia ya Yehova, ambaye hutupatia nguvu kwa wingi. Wakati tutakapoishi katika Paradiso ya kidunia, tutamsifu Yehova Mungu wetu kila siku kwa mambo mazuri atakayotutendea.—Zaburi 103:2.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona makala “Maoni ya Biblia: Jinsi ya Kukabiliana na Hali ya Kukata Tamaa,” katika toleo la Amkeni! la Mei 8, 2000.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki