-
‘Mkashangilie Daima kwa Ajili ya Hivi Niviumbavyo’Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
“Tazama, Watumishi Wangu Watafurahi”
16. Yehova atawabariki watumishi wake waaminifu kwa njia zipi, lakini itakuwaje kwa wale ambao wamemwacha?
16 Unabii unaeleza kwamba kuna thawabu tofauti-tofauti ambazo zinawangoja wale wanaomwabudu Mungu kwa moyo mweupe na wale wanaofanya hivyo kwa unafiki. Unafanya hivyo kwa kuwakaripia wale ambao wamemwacha Yehova: “Bwana MUNGU asema hivi, Tazama, watumishi wangu watakula, bali ninyi mtaona njaa; tazama, watumishi wangu watakunywa, bali ninyi mtaona kiu; tazama, watumishi wangu watafurahi, bali ninyi mtatahayarika; tazama, watumishi wangu wataimba kwa furaha [“hali njema,” “NW”] ya moyo, bali ninyi mtalia kwa huzuni ya moyo; mtapiga kelele kwa sababu ya uchungu wa roho zenu.” (Isaya 65:13, 14) Yehova atawabariki watumishi wake waaminifu. Wakiwa na mioyo inayofurika shangwe, watabubujika kelele za furaha. Kula, kunywa, na kufurahi ni maneno yanayoonyesha kwamba Yehova atatosheleza mahitaji ya waabudu wake kwa vitu kemkemu. Tofauti na hivyo, wale ambao wamechagua kumwacha Yehova wataona njaa na kiu ya kiroho. Mahitaji yao hayatatoshelezwa. Watalia kwa sauti kubwa na kupiga makelele ya kuomboleza kwa uchungu na msononeko.
17. Kwa nini watu wa Mungu leo wana sababu nzuri ya kuimba kwa furaha?
17 Maneno ya Yehova yanaieleza vizuri hali ya kiroho ya watu ambao leo wanadai kwa maneno tu kwamba wanamtumikia Mungu. Hata ingawa mamilioni ya watu wa Jumuiya ya Wakristo wana uchungu wa roho, waabudu wa Yehova wanaimba kwa furaha. Nao wana sababu nzuri ya kushangilia. Wanalishwa vema kiroho. Yehova huwaandalia chakula kingi cha kiroho kupitia vichapo vya Kibiblia na makusanyiko ya Kikristo. Kwa hakika, zile kweli zenye kujenga na ahadi zenye faraja zilizo katika Neno la Mungu hutupatia ‘hali njema ya moyo’!
-
-
‘Mkashangilie Daima kwa Ajili ya Hivi Niviumbavyo’Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
“Ninaumba Mbingu Mpya na Dunia Mpya”
20. Ahadi ya Yehova ya “mbingu mpya na dunia mpya” ilitimizwaje mwaka wa 537 K.W.K.?
20 Sasa Yehova anaieleza kwa mapana na marefu ahadi yake ya kuwarudishia hali nzuri wale mabaki wenye toba wakiisha kurejea kutoka uhamishoni Babiloni. Kupitia Isaya, Yehova anasema hivi: “Tazama, mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya, na maneno ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17, “Zaire Swahili Bible”) Ni hakika kwamba ahadi ya Yehova ya kurudishwa kwa hali za kwanza itatimizwa, kwa hiyo yeye anaongea kana kwamba tukio hilo la wakati ujao la kurudishwa kwa hali za kwanza limekwisha anza. Unabii huu ulitimizwa mara ya kwanza mwaka wa 537 K.W.K. wakati mabaki Wayahudi waliporudishwa Yerusalemu. “Mbingu mpya” zilikuwa nini wakati huo? Zilikuwa ugavana wa Zerubabeli ulioungwa mkono na Kuhani wa Cheo cha Juu, Yoshua, mahali pakuu pa ugavana huo pakiwa ni Yerusalemu. Mabaki Wayahudi waliorudishwa ndio waliokuwa “dunia mpya,” yaani jamii iliyosafishwa, nao walijitiisha chini ya utawala huo na kusaidia kuanzisha upya ibada safi nchini. (Ezra 5:1, 2) Shangwe ya kurudishwa huko ilifunika mateso yote ya zamani; misononeko ya zamani hata haikukumbukwa.—Zaburi 126:1, 2.
21. Ni mbingu mpya zipi zilizotokea mwaka wa 1914?
21 Hata hivyo, kumbuka kwamba Petro alirudia maneno ya unabii wa Isaya akaonyesha kwamba ungetimizwa wakati ujao. Mtume huyo aliandika hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Mwaka wa 1914 zile mbingu mpya zilizokuwa zimengojewa sana zilitokea. Ufalme wa Kimesiya uliozaliwa mwaka huo unatawala kutoka mbinguni kwenyewe, na Yehova ameupa ufalme huo mamlaka ya kuitawala dunia yote. (Zaburi 2:6-8) Serikali hiyo ya Ufalme, iliyo chini ya Kristo na watawala wenzake 144,000, ndio mbingu mpya.—Ufunuo 14:1.
22. Dunia mpya itafanyizwa kwa watu gani, na watu wanatayarishwaje hata sasa ili wawe kiini cha mpango huo?
22 Namna gani dunia mpya? Kwa kufuata kielelezo cha utimizo wa kale, dunia mpya itafanyizwa kwa watu wanaofurahia kujitiisha chini ya utawala wa serikali mpya ya kimbingu. Hata sasa, mamilioni ya watu mmoja-mmoja wenye mwelekeo unaofaa wananyenyekea chini ya serikali hiyo na kujitahidi kufuata sheria zake zilizo katika Biblia. Wanatoka katika taifa zote, lugha zote, na jamii zote, nao hushirikiana kumtumikia Mfalme Yesu Kristo anayetawala. (Mika 4:1-4) Mfumo mwovu wa mambo uliopo ukiisha kupita, kikundi hicho ndicho kitakachofanyizwa kuwa kiini cha dunia mpya na hatimaye kiwe jamii ya wanadamu wenye kumhofu Mungu watakaokuwa kila mahali ulimwenguni, wakiwa warithi wa makao ya kidunia ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 25:34.
23. Ni habari zipi tunazozipata katika kitabu cha Ufunuo kuhusu “mbingu mpya na dunia mpya,” na unabii huo utatimizwaje?
23 Kitabu cha Ufunuo kinaelezea njozi ambayo mtume Yohana aliona kuhusu siku ya Yehova inayokuja, wakati ambao mfumo huu wa mambo utaondolewa. Halafu Shetani atafungwa ndani ya abiso. (Ufunuo 19:11–20:3) Baada ya maelezo hayo, Yohana anayarudia maneno ya kiunabii ya Isaya, akiandika hivi: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya.” Mistari inayofuata ya masimulizi ya njozi hii tukufu inaeleza juu ya wakati ambao Yehova Mungu atabadili kabisa hali za dunia hii ziwe nzuri zaidi. (Ufunuo 21:1, 3-5) Ni wazi kwamba ahadi ya Isaya ya “mbingu mpya na dunia mpya” itatimizwa vizuri ajabu katika ulimwengu mpya wa Mungu! Jamii mpya ya kidunia itafurahia paradiso ya kiroho na hata ya kihalisi, ikiwa chini ya mbingu mpya za kiserikali. Ile ahadi ya kwamba “maneno ya kwanza [magonjwa, mateso, na ole mwingine mwingi unaopata wanadamu] hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni” inafariji kweli kweli. Ikiwa wakati huo tutakumbuka jambo lolote lile, halitatutia madhara wala maumivu yanayolemea mioyo ya wengi wakati wa sasa.
24. Kwa nini Yehova atashangilia kurudishwa kwa Yerusalemu, na ni nini ambacho hakitasikiwa tena katika barabara za jiji?
24 Unabii wa Isaya unaendelea kusema hivi: “Furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha. Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza.” (Isaya 65:18, 19) Si Wayahudi peke yao watakaoshangilia kurudishwa kwenye nchi yao, bali Mungu mwenyewe atashangilia pia, kwa maana atarembesha jiji la Yerusalemu—ambalo kwa mara nyingine litakuwa limekuwa mahali pakuu pa ibada ya kweli duniani. Ile sauti ya kulia kwa sababu ya maafa, iliyosikiwa katika barabara za jiji miongo kadhaa mapema, haitasikiwa tena.
25, 26. (a) Katika siku zetu, Yehova anafanyaje Yerusalemu liwe “shangwe”? (b) Yehova atatumia Yerusalemu Jipya kwa njia gani, na kwa nini sisi tunaweza kushangilia leo?
25 Leo, pia, Yehova anafanya Yerusalemu liwe “shangwe.” Jinsi gani? Kama vile tumekwisha kuona, hatimaye zile mbingu mpya zilizotokea mwaka wa 1914 zitahusisha pia watawala wenzi 144,000, wenye kushiriki katika ile serikali ya kimbingu. Mbingu hizo zinatajwa kiunabii kuwa “Yerusalemu Jipya.” (Ufunuo 21:2) Yerusalemu Jipya ndilo linalomaanishwa wakati Mungu anaposema hivi: “Tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.” Yerusalemu Jipya litatumiwa na Mungu kuwamiminia wanadamu watiifu baraka zisizo na kifani. Haitasikiwa tena sauti ya kulia wala ya maombolezo, kwa maana Yehova atatosheleza “haja za moyo [wetu].”—Zaburi 37:3, 4.
26 Kwa kweli, sisi leo tuna sababu kamili ya kufurahi sana! Karibuni Yehova atatakasa jina lake maarufu kwa kuwaharibu wapinzani wote. (Zaburi 83:17, 18) Kisha mbingu mpya peke yake zishike usukani kusimamia mambo yote. Lo, hizo ni sababu nzuri kama nini za kufurahi sana na kukishangilia milele kile kinachoumbwa na Mungu!
Ahadi ya Wakati Ujao Wenye Usalama
27. Isaya anaelezaje kuhusu usalama ambao wale wenye kurudi wataufurahia katika nchi yao?
27 Katika utimizo wa kwanza, maisha yatakuwaje kwa Wayahudi wenye kurudi wakiwa chini ya mbingu mpya? Yehova anasema hivi: “Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa.” (Isaya 65:20) Hiyo inaonyesha vizuri kama nini usalama ambao wahamishwa wenye kurudi watafurahia katika nchi yao iliyorudishwa! Kifo kisichotazamiwa hakitampata mzaliwa-juzi, maana yake kitoto cha siku chache tu. Wala kifo cha jinsi hiyo hakitammaliza mzee asiyetimiza maisha yake.d Maneno ya Isaya yanawafariji kweli kweli Wayahudi watakaorudi Yuda! Wakiisha kuwa salama nchini mwao, hawana tena haja ya kufanya wasiwasi eti adui zao watasomba watoto wao wachanga au kuchinja mashujaa wao.
28. Tunajifunza nini kutokana na maneno ya Yehova juu ya maisha katika ulimwengu mpya chini ya Ufalme wake?
28 Maneno ya Yehova yanatuambia nini juu ya maisha katika ulimwengu mpya unaokuja? Chini ya Ufalme wa Mungu, kila mtoto atakuwa na tarajio la kupata wakati ujao ulio salama. Kifo hakitaua tena mwanamume anayemhofu Mungu akiwa katika umri wake wa ufanisi mkubwa. Bali, wanadamu watiifu watakuwa salama salimini, na wataweza kufurahia maisha. Namna gani watu wowote wanaochagua kumwasi Mungu? Watapoteza pendeleo la uhai. Hata ikiwa mtenda-dhambi anayeasi ana “umri wa miaka mia,” atakufa. Hapo yeye atakuwa “mtoto wa siku chache” akilinganishwa na vile angaliweza kuwa—mtu mwenye maisha yasiyo na kikomo.
29. (a) Watu wa Mungu walio watiifu watapata shangwe zipi katika nchi ya Yuda iliyorudishwa? (b) Kwa nini miti ni mfano unaofaa wa maisha marefu? (Ona kielezi-chini.)
29 Yehova anaendelea kueleza juu ya hali zitakazokuwako katika nchi iliyorudishwa ya Yuda: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.” (Isaya 65:21, 22) Baada ya kuirudia nchi ya Yuda, ambayo bila shaka haikuwa na nyumba wala mizabibu, watu wa Mungu walio watiifu watakuwa na shangwe ya kuishi katika nyumba zao wenyewe na kula matunda kutoka mashamba yao wenyewe ya mizabibu. Mungu ataibariki kazi yao, na wataishi maisha marefu—marefu kama siku za mti—wafurahie matunda ya kazi zao.e
30. Watumishi wa Yehova wanafurahia hali gani leo, na watafurahia nini katika ulimwengu mpya?
30 Unabii huu umepata utimizo fulani katika siku zetu. Watu wa Yehova walitoka kwenye uhamisho wa kiroho mwaka wa 1919, wakaanza kurudisha hali za kwanza katika “nchi” au makao yao ya utendaji na ibada. Walijenga makutaniko na kusitawisha hali ya kuzaa matunda ya kiroho. Matokeo ni kwamba, hata sasa watu wa Yehova wanafurahia paradiso ya kiroho na amani waliyopewa na Mungu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba amani hiyo itaendelea mpaka ndani ya ile Paradiso halisi. Hata haiwezekani kuwaza kwa usahihi ni maajabu gani ambayo Yehova atafanya katika ulimwengu mpya kwa kuitumia mioyo na mikono ya waabudu wake wenye nia ya kufanya kazi. Itakuwa shangwe iliyoje kujenga nyumba yako mwenyewe kisha kuishi ndani yake! Chini ya utawala wa Ufalme, hakutakuwako upungufu wa kazi ya kuridhisha. Utafurahi kama nini “kujiburudisha kwa mema” ya matunda ya kazi zako mwenyewe sikuzote! (Mhubiri 3:13) Je, tutapata wakati wa kutosha kuifurahia sana kazi ya mikono yetu? Kabisa! Maisha yasiyo na kikomo ya wanadamu waaminifu yatakuwa “kama siku za mti”—maelfu ya miaka, na hata zaidi!
31, 32. (a) Wahamishwa wanaorudi watafurahia baraka zipi? (b) Wanadamu waaminifu watakuwa na tazamio gani katika ulimwengu mpya?
31 Yehova anaeleza juu ya baraka zaidi zinazowangoja wahamishwa wanaorudi: “Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na BWANA, na watoto wao pamoja nao.” (Isaya 65:23) Wayahudi hao waliorudishwa watabarikiwa na Yehova, na kwa hiyo hawatafanya kazi ya bure. Wazazi hawatazaa watoto ili tu wapatwe na kifo cha mapema. Watu wale waliokuwa uhamishoni hawatafurahia baraka za kurudishwa wakiwa peke yao; wazao wao watakuwa pamoja nao. Mungu ana hamu nyingi ya kutimiza mahitaji ya watu wake kiasi cha kuahidi hivi: “Itakuwa ya kwamba, kabla hawajaomba, nitajibu; na wakiwa katika kunena, nitasikia.”—Isaya 65:24.
32 Yehova atatimizaje ahadi hizo katika ulimwengu mpya unaokuja? Tungoje tuone. Yehova hajaeleza jinsi kila kitu kitakavyokuwa, lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba wanadamu waaminifu “hawatajitaabisha kwa kazi bure” tena. Umati mkubwa wa waokokaji wa Har-Magedoni na watoto wowote ambao huenda wakawazaa watakuwa na tazamio la maisha marefu ya kuridhisha—uhai wa milele! Hata wale watakaofufuliwa kisha wachague kuishi kupatana na viwango vya Mungu watapata shangwe ya kuwa katika ulimwengu mpya. Yehova atayasikia na kuyatimiza mahitaji yao, hata kuyatazamia. Kwa kweli, Yehova ataufungua mkono wake na kuridhisha “kila kilicho hai matakwa yake.”—Zaburi 145:16.
33. Wayahudi watakapoirudia nchi yao, wanyama wataishije kwa amani?
33 Amani na usalama ambazo zimeahidiwa zitakuwa za kiasi gani? Yehova anamalizia sehemu hii ya unabii kwa kusema hivi: “Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng’ombe; na mavumbi yatakuwa chakula cha nyoka. Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema BWANA.” (Isaya 65:25) Wakati mabaki ya Wayahudi waaminifu watakapoirudia nchi yao, watakuwa chini ya utunzaji wa Yehova. Itakuwa ni kama simba anakula majani kama ng’ombe, kwa maana simba hatawadhuru Wayahudi wala wanyama wao wa kufugwa. Ahadi hiyo ni hakika, kwa maana inamalizika kwa kusema, ‘asema Yehova.’ Na neno lake hutimia daima!—Isaya 55:10, 11.
34. Maneno ya Yehova yana utimizo gani wenye kusisimua leo na katika ulimwengu mpya?
34 Leo maneno ya Yehova yanatimizwa kwa njia ya kusisimua miongoni mwa waabudu wa kweli. Tangu mwaka wa 1919, Mungu ameibariki nchi ya kiroho ya watu wake, akaigeuza kuwa paradiso ya kiroho. Wale wanaoingia katika paradiso hii ya kiroho hufanya mabadiliko ya ajabu katika maisha yao. (Waefeso 4:22-24) Watu mmoja-mmoja ambao wakati mmoja walikuwa na nyutu za kinyama—ambao labda waliwatumia vibaya wanadamu wenzao au wakawadhulumu kwa njia nyinginezo—wanafanya maendeleo ya kuyamaliza makali ya tabia zisizopendeza kwa msaada wa roho ya Mungu. Matokeo ni kwamba, wanafurahia amani na umoja wa ibada pamoja na waamini wenzao. Baraka zinazofurahiwa sasa na watu wa Yehova katika paradiso yao ya kiroho zitaendelea mpaka ndani ya Paradiso halisi, ambamo amani itakuwamo miongoni mwa wanadamu, na hali kadhalika miongoni mwa wanyama. Tunaweza kuwa na hakika kwamba lile agizo ambalo Mungu aliwapa wanadamu hapo awali litatimizwa kabisa kwa njia inayofaa, yaani: ‘Kuitiisha nchi; kutawala samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.’—Mwanzo 1:28.
35. Kwa nini tuna sababu nzuri sana ya ‘kushangilia daima’?
35 Tunashukuru kama nini kwa ajili ya ahadi ya Yehova ya kuumba “mbingu mpya na dunia mpya”! Ahadi hiyo ilitimizwa mwaka wa 537 K.W.K., na inatimizwa zaidi leo. Utimizo huo wa mara mbili unaonyesha jinsi wanadamu watiifu wanavyoweza kupata wakati ujao ulio mtukufu. Yehova ametufadhili kwa kutupatia sisi, kupitia unabii wa Isaya, kionjo cha mambo ambayo amewawekea wale wanaompenda. Kwa kweli tuna sababu nzuri sana ya kuyatii maneno haya ya Yehova: “Mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo”!—Isaya 65:18.
-