Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mabadiliko Ya Maisha
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SEHEMU 2

      Mabadiliko Ya Maisha

      Je, unaridhika na jinsi mwili wako unavyokua?

      □ Ndiyo □ Hapana

      Je, mabadiliko ya kipindi cha kubalehe yamekufanya uwe mpweke, uchanganyikiwe, au uwe mwoga?

      □ Ndiyo □ Hapana

      Je, nyakati zote wewe hufikiria kuhusu watu wa jinsia tofauti?

      □ Ndiyo □ Hapana

      Ikiwa umejibu “ndiyo” katika yoyote ya maswali yaliyo juu, usiwe na shaka​—hilo halimaanishi kwamba una kasoro yoyote! Ukweli ni kwamba, mabadiliko ya kimwili na kihisia wakati wa kubalehe yanaweza kukusisimua au kukuvunja moyo au kukufanya uwe na hisia nyinginezo. Bila shaka, kwa muda mrefu umetamani kuwa mtu mzima, lakini sasa kwa kuwa hatua za kuwa mtu mzima zimeanza, unaweza kuingiwa na woga! Sura ya 6-8 zitakusaidia kushughulika na mabadiliko ya maisha.

      [Picha katika ukurasa wa 56, 57]

  • Kwa Nini Mwili Wangu Unabadilika?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 6

      Kwa Nini Mwili Wangu Unabadilika?

      “Nilirefuka haraka sana. Nilikuwa na maumivu mengi. Ingawa nilipenda kuwa mrefu, nilikuwa na maumivu ya miguu. Hilo halikunifurahisha hata kidogo!”—Paul.

      “Unajua kwamba mwili wako unabadilika, hata hivyo hungependa yeyote atambue. Kisha, mtu fulani anakuambia kwamba una kiuno cha mwanamke aliyekomaa—unatamani dunia ipasuke na kukumeza!”—Chanelle.

      UMEWAHI kuhamia eneo lingine pamoja na familia yenu? Yalikuwa mabadiliko makubwa, sivyo? Uliacha kila kitu ulichokuwa umezoea—nyumba yenu, shule yenu, na marafiki wako. Yaelekea ilikuchukua muda mrefu kuzoea mazingira yako mapya.

      Mwanzoni mwa kipindi cha kubalehe—wakati ambapo mwili wako unaanza kukomaa—unaingia katika kipindi cha baadhi ya mabadiliko makubwa zaidi maishani. Ni kana kwamba unahamia “eneo” jipya. Bila shaka ni jambo lenye kusisimua! Lakini kuingia katika kipindi cha utu uzima kwaweza kukutatanisha na huenda isiwe rahisi kwako kuzoea hali hiyo. Ni nini kinachotukia katika kipindi hicho kigumu maishani?

      Mabadiliko ya Wasichana

      Kipindi cha kubalehe ni wakati wa mabadiliko makubwa. Mabadiliko mengine yataonekana wazi. Kwa mfano, homoni zitasababisha nywele ziote kwenye maeneo ya viungo vyako vya uzazi. Pia, matiti, kiuno, mapaja, na makalio yatakuwa makubwa. Mwili wako utaanza kubadilika na kuchukua umbo la mwanamke mkomavu. Usiwe na wasiwasi. Hupaswi kushangazwa—mabadiliko hayo ni mambo ya kawaida kabisa. Na yanaonyesha kwamba mwili wako unajitayarisha kwa ajili ya wakati ambapo utaweza kupata mtoto!

      Muda fulani baada ya kuanza kubalehe, utaanza kupata hedhi. Usipojitayarisha vya kutosha, badiliko hilo kubwa maishani mwako linaweza kuogopesha. “Nilipoanza kupata hedhi, sikuwa tayari hata kidogo,” asema Samantha. “Nilijiona kuwa mchafu. Nilikuwa nikijisugua sana nilipokuwa nikioga. Nilijiona kuwa ‘mwenye kuchukiza sana.’ Niliogopa sana nilipofikiria kwamba kwa miaka mingi nitakuwa nikipata hedhi kila mwezi!”

      Hata hivyo, kumbuka kwamba kupata hedhi kunaonyesha kwamba nguvu zako za uzazi zinakua. Ijapokuwa miaka mingi itapita kabla hujawa mzazi, unaendelea kukomaa na kuwa mwanamke. Vyovyote vile, kuanza kupata hedhi kunaweza kuwa jambo la kuhangaisha. “Jambo kubwa zaidi nililolazimika kukabili ni kubadilika-badilika kwa hisia,” asema Kelli. “Nilifadhaika sana kwa kuwa sikujua kwa nini ningeweza kuwa na furaha mchana kutwa, na kulia kwelikweli usiku wa siku hiyohiyo.”

      Ikiwa hivyo ndivyo unavyohisi sasa, uwe na subira. Baada ya muda utazoea. Annette, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Nakumbuka wakati nilipofikia hatua ya kukubali kwamba ili niwe mwanamke mkomavu mabadiliko hayo lazima yatokee na kwamba Yehova amenipa zawadi ya uzazi. Inachukua muda kukubali jambo hilo, na inakuwa vigumu sana kwa wasichana fulani; lakini baada ya muda unajifunza kukubali mabadiliko hayo.”

      Je, umeanza kujionea yoyote kati ya mabadiliko hayo ambayo yamezungumziwa? Katika nafasi zilizo hapa chini, andika maswali yoyote uliyo nayo kuhusu mabadiliko yanayokupata.

      ․․․․․

      Mabadiliko ya Wavulana

      Ikiwa wewe ni mvulana, kipindi cha kubalehe kitabadili sana sura yako. Kwa mfano, huenda mara nyingi ngozi yako ikawa na mafuta mengi na kutokeza chunusi.a “Inafadhaisha na kuvunja moyo sana kuwa na chunusi,” asema Matt mwenye umri wa miaka 18. “Unahitaji kupigana vita vikali na chunusi hizo. Huwezi kujua ikiwa zitakwisha au zitaacha makovu au ikiwa watu watakudharau kwa sababu una chunusi.”

      Kwa upande mwingine, huenda ukaona kwamba unazidi kuwa mkubwa na mwenye nguvu na kwamba mabega yako yanaanza kupanuka. Pia, wakati wa kubalehe, nywele zinaweza kuota kwenye miguu, kifua, na uso wako, na pia kwenye makwapa yako. Hata hivyo, kumbuka kwamba kuwa na nywele nyingi hakumaanishi kwamba wewe ni dume sasa; hilo ni jambo linalotegemea urithi tu.

      Kwa kuwa sehemu mbalimbali za mwili wako hukua kwa viwango tofauti, unaweza kuhisi kwamba sura yako haipendezi. Dwayne anasema hivi kuhusu wakati alipobalehe: “Nilionekana kama ngamia mwenye miguu ya twiga. Ilionekana kana kwamba ujumbe kutoka kwenye ubongo wangu ungechukua juma moja kabla ya kufika kwenye miguu!”

      Katika miaka ya katikati ya utineja sauti yako inakuwa nzito zaidi hatua kwa hatua. Kwa muda fulani, sauti nzito inaweza kukatizwa-katizwa na sauti nyembamba na kali, jambo ambalo linaweza kukufanya uaibike. Hata hivyo, usijali. Baada ya muda, sauti yako itasawazika. Kwa sasa, kujifunza kutohangaishwa na hali hiyo kutakupunguzia aibu.

      Mfumo wako wa uzazi unapozidi kukomaa, viungo vyako vya uzazi vitakuwa vikubwa na nywele zitaota kandokando. Pia vitaanza kutokeza umajimaji unaoitwa shahawa. Umajimaji huo huwa na mamilioni ya mbegu za uzazi zisizoweza kuonekana kwa macho, ambazo hupitishwa wakati wa ngono. Mbegu moja inaweza kutungisha mimba yai la mwanamke na kutokeza mtoto.

      Umajimaji huo unapoongezeka mwilini, kiasi fulani hufyonzwa mwilini, lakini mara kwa mara, mwingine unatoka usiku unapolala. Hilo ni jambo la kawaida. Hata Biblia hulizungumzia. (Mambo ya Walawi 15:16, 17) Jambo hilo linaonyesha kwamba mfumo wako wa uzazi unafanya kazi na kwamba unaelekea kuwa mwanamume mkomavu.

      Je, umeanza kujionea yoyote kati ya mabadiliko hayo ambayo yamezungumziwa? Katika nafasi zilizo hapa chini, andika maswali yoyote uliyo nayo kuhusu mabadiliko yanayokupata.

      ․․․․․

      Kushughulika na Mabadiliko ya Kihisia

      Mfumo wa uzazi unapoendelea kukomaa, wavulana na wasichana huanza kuvutiwa na watu wa jinsia tofauti. “Nilipoingia kipindi cha kubalehe, ghafula nilianza kuona wasichana wengi kuwa warembo,” anasema Matt. “Lilikuwa jambo lenye kuvunja moyo sana, kwa kuwa singeweza kufanya lolote mpaka wakati ambapo ningekuwa na umri mkubwa zaidi.” Sura ya 29 ya kitabu hiki itazungumzia zaidi hali hiyo. Hata hivyo, kwa sasa unapaswa kutambua kwamba unahitaji kujifunza kuzuia tamaa zako za ngono. (Wakolosai 3:5) Amini usiamini, unaweza kuamua kutozitosheleza!

      Kuna hisia nyingine pia ambazo hutokea katika kipindi cha kubalehe. Kwa mfano, huenda ukajiona kuwa mtu asiyefaa kitu. Vijana wengi huwa wapweke na kushuka moyo mara kwa mara. Pindi hizo, ni vizuri kuzungumza na mzazi au mtu mwingine mzima unayemwamini. Andika jina la mtu mzima ambaye wewe unaweza kuzungumza naye kuhusu hisia zako.

      ․․․․․

      Ukuzi wa Maana Zaidi

      Ukuzi wa maana zaidi si wa kimo, umbo, wala sura yako, bali utu wako, yaani, ukuzi wa kiakili, kihisia na, zaidi ya yote, wa kiroho. Mtume Paulo alisema hivi: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa nikisema kama mtoto, nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.” (1 Wakorintho 13:11) Ndiyo, haitoshi tu kuonekana kama mtu mzima. Lazima ujifunze kutenda, kuzungumza, na kufikiri kama mtu mzima. Usijihangaishe sana na mabadiliko ya mwili hivi kwamba umpuuze yule mtu wa ndani!

      Pia, kumbuka kwamba Mungu “huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Biblia inasema kwamba Mfalme Sauli alikuwa mrefu na mwenye sura nzuri, lakini hakupata mafanikio akiwa mfalme wala maishani. (1 Samweli 9:2) Tofauti naye, Zakayo alikuwa “mfupi,” hata hivyo alikuwa na ujasiri wa kubadili maisha yake na kuwa mwanafunzi wa Yesu. (Luka 19:2-10) Ni wazi kwamba jinsi mtu alivyo kwa ndani ndilo jambo la maana.

      Ukweli ni kwamba: Hakuna njia yoyote salama ya kuharakisha au kukawiza jinsi mwili unavyokua. Kwa hiyo, badala ya kuchukia na kuogopa mabadiliko hayo, jipe moyo na usihangaishwe na mambo kupita kiasi. Kubalehe si ugonjwa, wala wewe si mtu wa kwanza kubalehe. Uwe na hakika kabisa kwamba maisha yako hayako hatarini hata kidogo. Dhoruba ya kubalehe itakapokuwa imepita, utaibuka ukiwa mtu mzima aliyekomaa!

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Namna gani ikiwa hufurahishwi na kile unachoona unajipotazama kwenye kioo? Unaweza kufanya nini ili uwe na maoni yanayofaa kuhusu sura yako?

      [Maelezo ya Chini]

      a Wasichana pia hupata chunusi. Tatizo hilo linaweza kupunguzwa kwa kutunza ngozi ifaavyo.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”—Zaburi 139:14.

      PENDEKEZO

      Mwili wako unapoanza kukua, epuka kuvalia mavazi yanayochochea hamu ya ngono. Sikuzote, valia kwa “kiasi na utimamu wa akili.”—1 Timotheo 2:9.

      JE, WAJUA . . . ?

      Kipindi cha kubalehe chaweza kuanza mapema sana, kuanzia umri wa miaka minane hivi, au kinaweza kuchelewa na kuanza mtu anapokuwa katika miaka ya katikati ya utineja. Hata mtu aanze kubalehe wakati gani, haimaanishi kwamba ana kasoro.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ninapozidi kukomaa na kuwa mtu mzima, sifa ninayohitaji kufanyia kazi sana ni ․․․․․

      Ili kukua kiroho, nita ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini ni vigumu sana kushughulika na mabadiliko ya kimwili na ya kihisia wakati wa kipindi cha kubalehe?

      ● Ni nini unachoona kuwa kigumu sana katika mabadiliko hayo?

      ● Kwa nini huenda upendo wako kwa Mungu ukaelekea kupungua katika kipindi cha kubalehe, lakini unaweza kuzuia jinsi gani jambo hilo lisitokee?

      [Blabu katika ukurasa wa 61]

      Kuna hali nyingi zenye kutia wasiwasi katika kipindi cha kubalehe, na huenda usijue jinsi mwili wako utakavyokuwa siku inayofuata. Lakini kadiri unavyokua, unajifunza kukubali mabadiliko hayo na hata kuyafurahia.’’—Annette

      [Sanduku katika ukurasa wa 63, 64]

      Ninaweza Kuzungumza Namna Gani na Baba Yangu au Mama Yangu Kuhusu Ngono?

      “Nikiwa na swali lolote kuhusu ngono, siwezi kamwe kuwauliza wazazi wangu.”—Beth.

      “Siwezi hata kupata ujasiri wa kutaja mambo hayo.”—Dennis.

      Ikiwa uko kama Beth au Dennis, uko katika hali ngumu sana. Ungependa kujua kuhusu ngono, lakini watu walio na majibu ndio watu ambao hungependa kuwauliza—wazazi wako! Una maswali mengi yanayokuhangaisha:

      Wataniona namna gani?

      “Sitaki waanze kunishuku kwa sababu ya kuuliza.”—Jessica.

      “Wanataka uendelee kuwa mtoto asiyejua chochote milele, na siku utakapoanza kuzungumza nao kuhusu ngono, mambo kwisha.”—Beth.

      Watafikiri nini?

      “Naogopa kwamba wazazi wangu watanihukumu na kuanza kunigombeza hata kabla sijamaliza kuzungumza.”—Gloria.

      “Wazazi wangu hawajui kuficha hisia zao, kwa hiyo, naogopa kwamba sura zao zitaonyesha kwamba wamevunjika moyo. Kwanza, huenda hata baba yangu akaanza kufikiria jinsi ya kunigombeza huku nikiendelea kuzungumza.”—Pam.

      Je, watakosa kunielewa?

      “Huenda wakakasirika na kuanza kuuliza maswali kama vile, ‘Kuna mtu anayekushawishi mfanye ngono?’ au ‘Rafiki zako wanakushinikiza?’ Lakini huenda tu unataka kujua.”—Lisa.

      “Kila mara nikitaja tu mvulana yeyote, baba yangu huingiwa na wasiwasi. Kisha anaanza kunionya kuhusu ngono. Kisha nawaza, ‘Ni nani aliyesema kuhusu ndoa au ngono? Nimesema tu kwamba ana sura ya kuvutia.’”—Stacey.

      Huenda ikakuliwaza kujua kwamba wazazi wako pia wanaona ugumu kuzungumza na wewe kuhusu ngono, kama vile tu unavyoona ugumu kuzungumza nao! Huenda ndiyo sababu uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 65 ya wazazi walidai kwamba wamezungumza na watoto wao kuhusu ngono, hali ni asilimia 41 tu ya watoto wanaokumbuka mazungumzo hayo kati yao na wazazi wao.

      Ukweli ni kwamba, huenda wazazi wako wakasita kuzungumzia ngono. Kama ilivyo katika visa vingi, huenda wazazi wao hawakuzungumza nao kamwe kuhusu ngono! Hata sababu iwe gani, waelewe wazazi wako. Labda hata wewe mwenyewe unaweza kuanzisha mazungumzo hayo. Ingawa kufanya hivyo kunahitaji ujasiri mwingi, ninyi nyote, wewe na wao pia, mtafaidika. Jinsi gani?

      Kuanzisha Mazungumzo

      Wazazi wako wana hekima na mashauri mengi kuhusu ngono. Unachohitaji tu ni njia ya kuanzisha mazungumzo hayo. Jaribu njia inayofuata:

      1 Eleza wasiwasi wako tangu mwanzo. “Nasita kuongea nawe kuhusu habari hii kwa kuwa huenda ukafikiri . . . ”

      2 Kisha mwambie mzazi wako kwa nini umemwendea yeye. “Hata hivyo nina swali, na nimeona afadhali nikuulize wewe kuliko kumwuliza mtu mwingine yeyote.”

      3 Halafu taja jambo linalokusumbua. “Swali langu ni . . . ”

      4 Mwishoni mwa mazungumzo, hakikisha kwamba kuna nafasi ya kuendeleza mazungumzo hayo wakati ujao. “Nikiwa na swali lingine lolote, je, naweza kukuuliza tena?”

      Hata ikiwa unajua atajibu ndiyo, kumsikia mzazi wako akisema hivyo kwaweza kufanya iwe rahisi kuzungumzia habari hiyo wakati ujao uhitaji utakapotokea. Basi jaribu njia hiyo! Huenda ukakubaliana na Trina. Sasa, akiwa na umri wa miaka 24, anasema: “Mimi na mama yangu tulipokuwa tukizungumza, nakumbuka nikitamani dunia ipasuke. Lakini sasa, nafurahi kwamba mama yangu aliniambia mambo waziwazi. Huo umekuwa ulinzi kwelikweli!”

      [Picha katika ukurasa wa 59]

      Kuyaaga maisha ya utotoni ni kama kuhamia eneo lingine—lakini unaweza kuzoea mabadiliko hayo

  • Nifanye Nini Ikiwa Sipendi Umbo Langu?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 7

      Nifanye Nini Ikiwa Sipendi Umbo Langu?

      Je, mara nyingi unavunjwa moyo na umbo lako?

      □ Ndiyo □ Hapana

      Je, umewahi kufikiria kufanyiwa upasuaji au kufuata ratiba kali ya kula ili kurekebisha kasoro fulani ya kimwili?

      □ Ndiyo □ Hapana

      Ikiwa ungeweza, ungebadili nini katika mwili wako? (Chora duara kuzunguka kile ambacho ungependa kubadili.)

      Kimo

      Uzito

      Umbo

      Nywele

      Rangi

      Sauti

      IKIWA umejibu ndiyo maswali ya kwanza mawili na kuchora duara kuzunguka vitu vitatu au zaidi katika swali la tatu, usife moyo. Kumbuka kwamba: Kuna uwezekano mkubwa kwamba wengine hawalioni umbo lako kuwa lenye kuchukiza kama unavyoliona. Ni rahisi kuhangaikia umbo lako kupita kiasi. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba mara nyingi wasichana wanaogopa kunenepa kuliko wanavyoogopa vita vya nyuklia, kansa, au hata kufiwa na wazazi wao!

      Bila shaka, umbo lako linaweza kuathiri jinsi unavyojiona na jinsi wengine wanavyokutendea. Maritza mwenye umri wa miaka 19 anasema: “Nilipokuwa nikikua, dada zangu wawili wakubwa walikuwa warembo sana, nami nilikuwa mnene-mnene. Nilidhihakiwa sana shuleni. Zaidi ya hayo, shangazi yangu alinibandika jina Chubs (Kibonge), jina la mbwa wake mdogo aliyekuwa mnono sana!” Julie, mwenye umri wa miaka 16, alikuwa pia katika hali kama hiyo. “Msichana mmoja shuleni alinidhihaki akisema nina meno kama ya sungura. Hata ingawa halikuwa jambo zito, bado nilijisikia vibaya, na hata sasa sipendi meno yangu!”

      Je, Unahangaikia Umbo Lako Kupita Kiasi?

      Si vibaya kuhangaikia umbo lako. Hata Biblia inataja wanawake na wanaume fulani waliokuwa wenye kuvutia kama vile Sara, Raheli, Yosefu, Daudi, na Abigaili. Biblia inasema kwamba msichana fulani aliyeitwa Abishagi alikuwa “mrembo zaidi.”—1 Wafalme 1:4.

      Hata hivyo, vijana wengi wanahangaikia umbo lao kupita kiasi. Kwa mfano, wasichana fulani wanaamini kwamba ili uwe mwenye kuvutia lazima uwe mwembamba. Na kwa kweli, ni kana kwamba magazeti yenye picha za wanamitindo wembamba kupita kiasi hukazia jambo hilo. Wasichana hao husahau kwamba picha hizo zimeboreshwa kwenye kompyuta na kwamba wanamitindo hao hulazimika kujitesa kwa kujinyima sana chakula ili kudumisha umbo lao! Zaidi ya hilo, kujilinganisha na picha zilizo kwenye magazeti kwaweza kukuvunja moyo sana. Hata hivyo, unaweza kufanya nini ikiwa bado hupendi umbo lako? Kwanza, unahitaji kujichunguza kwa unyoofu.

      Je, Maoni Yako Yana Kasoro?

      Je, umewahi kujitazama kwenye kioo kinachopotosha umbo? Kioo hicho kinaweza kukufanya uonekane mkubwa au mdogo kuliko ulivyo kihalisi. Vyovyote vile, unachoona si sahihi.

      Vivyo hivyo, vijana wengi wana maoni yenye kasoro kuhusu umbo lao. Fikiria hili: Katika uchunguzi mmoja uliofanywa, asilimia 58 ya wasichana walidai kwamba wao ni wanene sana, ijapokuwa asilimia 17 tu kati yao ndio waliokuwa wanene sana. Katika uchunguzi mwingine, asilimia 45 ya wanawake ambao ni wembamba sana walifikiri kwamba wao ni wanene sana!

      Wachunguzi fulani wanasema wasichana wengi wanaohangaikia uzito wao hawana sababu ya kufanya hivyo. Huenda hilo lisikutulize sana hasa ikiwa una mwili mkubwa. Ikiwa kweli una mwili mkubwa, sababu inaweza kuwa nini?

      Huenda sababu moja ni chembe za urithi. Kiasili, watu fulani ni wembamba na mifupa yao inatokeza. Lakini ikiwa chembe zako za urithi zimekufanya uwe mnene na mwenye mafuta mengi, basi kiasili hukukusudiwa uwe mwembamba. Hata unapokuwa na uzito ambao unapendekezwa na wanatiba, huenda bado ukaonekana kuwa mnene kuliko vile ambavyo ungependa. Kufanya mazoezi na kula chakula kinachofaa kunaweza kusaidia, hata hivyo, huwezi kubadili sana umbo ambalo umerithi.

      Sababu nyingine inaweza kuwa mabadiliko ya kawaida ya kipindi cha kubalehe. Msichana anapobalehe, mafuta yaliyo mwilini mwake huongezeka kutoka asilimia 8 mpaka asilimia 22 hivi. Mara nyingi hali hiyo inabadilika kadiri muda unavyosonga, na msichana kibonge mwenye umri wa miaka 11 au 12 hivi anaweza kubadilika na kuwa tineja aliye na umbo lenye kuvutia. Kwa upande mwingine, unaweza kufanya nini ikiwa umbo lako linatokana na mazoea mabaya ya kula au kutofanya mazoezi? Na unaweza kufanya nini ikiwa kwa kweli unahitaji kupunguza uzito kwa sababu ya afya?

      Maoni Yenye Usawaziko

      Biblia inapendekeza watu wawe na “kiasi katika mazoea.” (1 Timotheo 3:11) Kwa hiyo, inafaa kuepuka mazoea ya kujinyima chakula au kufuata ratiba kali ya kula. Labda njia bora ya kupunguza uzito ni kuwa na ratiba nzuri ya kula chakula kinachofaa na kufanya mazoezi ya kutosha.

      Hakuna haja ya kufuata ratiba fulani ya kula eti kwa sababu inafuatwa na watu wengi. Kwa mfano, kwa muda fulani vidonge vinaweza kupunguza hamu yako ya kula; lakini muda si muda mwili huvizoea, na hamu yako ya kula inarudi. Au uwezo wa mwili wako wa kutumia chakula hupungua na hivyo kufanya uongeze uzito au hata kupatwa na madhara fulani ambayo wengine hupatwa nayo, kama vile kizunguzungu, kupanda kwa shinikizo la damu, kushikwa na wasiwasi ghafula, na labda kutegemea sana vidonge hivyo. Ndivyo ilivyo pia na vidonge vinavyoondoa maji mwilini au vile vinavyoongeza uwezo wa mwili wako wa kutumia chakula.

      Tofauti na hilo, kufuata utaratibu wa kula wenye usawaziko na kufanya mazoezi ya kiasi kwa ukawaida kutaboresha umbo na afya yako. Kufanya mazoezi ya viungo kwa kiasi mara kadhaa kwa juma kutaboresha sana afya yako. Hata huenda ikatosha kufanya mazoezi yasiyohusisha mambo mengi kama vile kutembea haraka au kupanda ngazi.

      Jihadhari na Ugonjwa wa Kujinyima Chakula!

      Vijana fulani wametamani sana kupunguza uzito hivi kwamba wamepata ugonjwa wa kujinyima chakula ambao unahatarisha uhai, unaoitwa anoreksia. Baada ya kutibiwa ugonjwa huo kwa miezi minne, Masami anasema hivi: “Watu wanaponiambia, ‘Unaonekana mwenye afya,’ mimi hujiambia, ‘Haikosi nimeanza kunenepa.’ Nyakati kama hizo mimi hulia sana na kusema, ‘Laiti ningaliweza kurudia uzito niliokuwa nao miezi minne iliyopita!’”

      Ugonjwa huo unaweza kuanza bila mtu kutambua. Huenda msichana akaamua kufuata ratiba fulani ya kula ambayo haielekei kuwa na madhara, labda ili kupunguza kilo chache tu. Hata hivyo, anapofikia uzito aliotaka, hatosheki. Anapojitazama kwenye kioo, huenda akasema hivi: “Bado mimi ni mnene sana!” Hivyo, anaamua kupunguza kilo nyingine chache. Kisha nyingine chache. Halafu nyingine chache. Tayari zoea limeanza, na hivyo ndivyo ugonjwa huo unavyotokea.

      Ikiwa una dalili za anoreksia au ugonjwa mwingine unaohusiana na chakula, unahitaji msaada. Zungumza na mzazi wako au mtu mwingine mzima anayeaminika. Methali moja ya Biblia inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

      Urembo wa Kweli Ni Nini?

      Biblia haikazii sana sura au umbo la mtu. Badala yake, jinsi mtu alivyo ndani humfanya awe mwenye kupendeza au asiyependeza machoni pa Mungu.—Methali 11:20, 22.

      Mfikirie Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi. Biblia inasema: “Hakuna mwanamume aliyekuwa na sura nzuri sana katika Israeli yote kuweza kusifiwa sana hivyo. Hakuwa na kasoro yoyote, kuanzia wayo wa mguu wake mpaka kipaji cha kichwa chake.” (2 Samweli 14:25) Lakini, kijana huyo alikuwa mwenye hila. Kwa sababu ya kiburi na kujitakia makuu, alijaribu kunyakua kiti cha ufalme cha mfalme aliyewekwa na Yehova. Kwa hiyo, Biblia haimsifu Absalomu, badala yake, inamtaja kuwa mtu asiye mshikamanifu hata kidogo na mwenye chuki ya uuaji.

      Jambo kuu ni kwamba “Yehova anaipima mioyo”—bali si kiuno cha msichana wala misuli ya mvulana. (Methali 21:2) Kwa hiyo, ingawa si vibaya kutamani kuwa na umbo lenye kupendeza, jambo la maana zaidi ni utu wako. Kwa kweli, kuwa na sifa za kiroho kutakufanya uwe mwenye kupendeza zaidi machoni pa wengine kuliko kuwa na misuli yenye nguvu au umbo zuri!

      PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 10

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Vijana wengi wana ugonjwa wa kudumu au ulemavu fulani. Ikiwa wewe ni mmoja wao, unaweza kushughulika na hali hiyo jinsi gani?

      MAANDIKO MUHIMU

      “Mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.”—1 Samweli 16:7.

      PENDEKEZO

      Unapojaribu kupunguza uzito . . .

      ● Usikose kifungua- kinywa. Hilo linaweza kufanya ule zaidi kwa sababu ya njaa.

      ● Kunywa glasi moja kubwa ya maji kabla ya kila mlo. Kufanya hivyo kutapunguza hamu yako ya kula na kukusaidia ule kwa kiasi.

      JE, WAJUA . . . ?

      Wataalamu fulani huonya kwamba ukijinyima sana chakula ili kupunguza uzito, huenda mwili wako ukafikiri kwamba kuna hatari na hivyo kuhifadhi chakula badala ya kukitumia na kusababisha uongeze tena uzito haraka!

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ninaweza kutunza vizuri zaidi afya yangu kwa ․․․․․

      Ratiba yangu ya kufanya mazoezi kwa kiasi inaweza kutia ndani ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Una maoni gani kuhusu sura yako?

      ● Ni hatua gani zinazofaa ambazo unaweza kuchukua ili kufanya sura yako iwe nzuri zaidi?

      ● Unaweza kumwambia nini rafiki yako ambaye amepata ugonjwa fulani unaohusiana na chakula?

      ● Ni kwa njia gani unaweza kumsaidia ndugu au dada yako mdogo awe na maoni yenye usawaziko kuhusu umbo lake?

      [Blabu katika ukurasa wa 69]

      “Kwa muda mrefu nilidhihakiwa kwa sababu macho yangu ni makubwa. Nilijifunza kucheka wengine waliponitania na vilevile kujiamini. Sasa nimetosheka na sura yangu. Nimejikubali jinsi nilivyo.’’—Amber

      [Picha katika ukurasa wa 68]

      Huenda maoni yako kuhusu sura yako yakawa kama ya mtu anayejitazama kwenye kioo kinachopotosha umbo

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki