Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kufuatia Kusudi Lenye Maana Maishani
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Oktoba 1
    • Kufuatia Kusudi Lenye Maana Maishani

      “Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah.”—ZABURI 150:6.

      1. Eleza jinsi kijana mmoja alivyotafuta kusudi maishani.

      “NILISOMEA udaktari kwa sababu nilitaka kutumia maisha yangu kuwasaidia watu. Pia, nilifikiri kwamba umashuhuri na pesa nyingi ambazo ningepata nikiwa daktari zingeniletea furaha,” anakumbuka Seung Jin, ambaye alilelewa huko Korea.a “Nilivunjika moyo nilipotambua kwamba daktari anaweza kuwasaidia watu kwa kadiri ndogo sana. Kisha niliamua kufuatia kazi ya usanii, lakini jitihada zangu hazikuwafaidi wengine sana, nami nilijiona kuwa mwenye ubinafsi tu. Halafu nikaamua kuwa mwalimu lakini muda si muda niligundua kwamba nilikuwa nikiwapa wengine ujuzi tu wala si mwongozo ambao ungewaletea furaha ya kweli.” Kama watu wengi wanavyofanya, Seung Jin alikuwa akitafuta kusudi lenye maana maishani.

      2. (a) Kuwa na kusudi maishani kunamaanisha nini? (b) Tunajua jinsi gani kwamba Muumba alituweka duniani akiwa na kusudi?

      2 Kuwa na kusudi la kweli maishani kunamaanisha kuwa na sababu ya kuishi, lengo lililo wazi, kuwa na mradi ambao tunajitahidi kufikia. Je, kweli wanadamu wanaweza kuwa na kusudi kama hilo? Ndiyo! Uhakika wa kwamba tumeumbwa tukiwa na akili, dhamiri, na uwezo wa kufikiri unaonyesha kwamba Muumba alituweka duniani akiwa na kusudi fulani zuri. Hivyo basi, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba tunaweza kupata na kutimiza kusudi la kweli la maisha kwa kuishi tu kupatana na kusudi la Muumba.

      3. Kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu linatia ndani nini?

      3 Biblia inafunua kwamba kusudi la Mungu kwa ajili yetu linatia ndani mambo mengi. Kwa mfano, tuliumbwa kwa njia nzuri na hilo linaonyesha kwamba kwa kweli Mungu ana upendo usio wa kichoyo. (Zaburi 40:5; 139:14) Kwa hiyo, kuishi kupatana na kusudi la Mungu kunamaanisha kuwapenda wengine bila uchoyo kama Mungu anavyowapenda. (1 Yohana 4:7-11) Kunamaanisha pia kutii maagizo ya Mungu ambayo yanatusaidia kuishi kupatana na kusudi lake lenye upendo.—Mhubiri 12:13; 1 Yohana 5:3.

      4. (a) Ni nini kinachohitajiwa ili kuwa na kusudi la kweli maishani? (b) Ni kusudi gani bora kabisa ambalo mtu yeyote anaweza kufuatia?

      4 Pia, Mungu alikusudia kwamba wanadamu waishi pamoja kwa furaha na amani na kuishi hivyo pia na uumbaji mwingine wote. (Mwanzo 1:26; 2:15) Hata hivyo, tunahitaji kufanya nini ili tuwe na furaha, usalama, na amani ya akili? Kama mtoto ambaye anajihisi akiwa salama na mwenye furaha anapojua kwamba wazazi wake wako karibu, tunahitaji kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Baba yetu wa mbinguni ili tupate kusudi la kweli na lenye maana maishani. (Waebrania 12:9) Mungu anatuwezesha kuwa na uhusiano kama huo pamoja naye kwa kuturuhusu tumkaribie na kwa kusikiliza sala zetu. (Yakobo 4:8; 1 Yohana 5:14, 15) ‘Tukitembea pamoja na Mungu’ kwa imani na kuwa marafiki wake, tunaweza kumletea Baba yetu wa mbinguni shangwe na sifa. (Mwanzo 6:9; Methali 23:15, 16; Yakobo 2:23) Hilo ndilo kusudi bora kabisa ambalo mtu yeyote anaweza kufuatia. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah.”—Zaburi 150:6.

      Una Kusudi Gani Maishani?

      5. Kwa nini si jambo la hekima kutanguliza mapendezi ya kimwili?

      5 Kusudi la Mungu kwa ajili yetu linatia ndani kujitunza vizuri sisi wenyewe pamoja na familia zetu. Hilo linatia ndani kutimiza mahitaji yetu ya kimwili na ya kiroho. Lakini, tunahitaji kufanya hivyo kwa usawaziko ili mambo ya kimwili tunayopendezwa nayo na mahangaiko yetu yasifunike mambo ya kiroho ambayo ni ya maana zaidi. (Mathayo 4:4; 6:33) Inasikitisha kwamba jambo kuu katika maisha ya watu wengi ni kutafuta vitu vya kimwili. Hata hivyo, si jambo la hekima kujaribu kutosheleza mahitaji yetu yote kwa kutafuta tu vitu vya kimwili. Uchunguzi wa hivi karibuni wa mamilionea huko Asia unafunua kwamba wengi wao “hawajihisi salama na wanahangaika, hata ingawa wamekuwa maarufu na wametimiza mengi kwa sababu ya utajiri wao.”—Mhubiri 5:11.

      6. Yesu alitoa shauri gani kuhusu kufuatia utajiri?

      6 Yesu alizungumza kuhusu “nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Marko 4:19) Utajiri unadanganya kwa njia gani? Unamfanya mtu aonekane kuwa na furaha, ijapokuwa hana furaha. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha.” (Mhubiri 5:10) Lakini je, mtu anaweza kufuatia miradi ya kimwili na wakati uleule amtumikie Mungu kwa nafsi yake yote? Bila shaka hawezi. Yesu alieleza hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” Yesu aliwahimiza wafuasi wake wajiwekee “hazina mbinguni,” wala si vitu vya kimwili duniani, yaani, wajifanyie jina zuri pamoja na Mungu, ambaye ‘anajua ni vitu gani wanavyohitaji hata kabla hawajamwomba.’—Mathayo 6:8, 19-25.

      7. Tunaweza jinsi gani ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli’?

      7 Mtume Paulo alitoa shauri zito kuhusu jambo hilo alipomwandikia Timotheo, mfanyakazi mwenzake. Alimwambia Timotheo hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri . . . waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie . . . , wawe wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.”—1 Timotheo 6:17-19.

      “Uzima Ulio wa Kweli” Ni Nini?

      8. (a) Kwa nini watu wengi wanajitahidi kutafuta utajiri na umaarufu? (b) Watu hao hawatambui nini?

      8 Watu wengi wanafikiri kwamba maneno “uzima ulio wa kweli” yanamaanisha maisha ya raha na starehe. Gazeti moja la Asia linasema hivi: “Wale wanaotazama sinema au televisheni wanaanza kutamani yale wanayoona na kuota kuhusu vitu ambavyo wanaweza kuwa navyo.” Wengi wanafanya kutafuta utajiri na umaarufu kuwe kusudi kuu maishani mwao. Wengi wanapoteza maisha yao ya ujana, wanaacha kufuatia viwango vya kiroho, na afya yao na maisha yao ya familia yanaharibika kwa sababu ya kufuatia vitu hivyo. Ni watu wachache sana wanaotambua kwamba maisha ya raha na starehe yanayotangazwa na vyombo vya habari yanaonyesha tu “roho ya ulimwengu,” yaani, njia ya kufikiri ambayo ina uvutano juu ya mabilioni ya watu duniani na ambayo inawasukuma watende kinyume cha kusudi la Mungu kwa ajili yetu. (1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2) Haishangazi kwamba kuna watu wengi sana ambao hawana furaha leo!—Methali 18:11; 23:4, 5.

      9. Wanadamu hawawezi kutimiza nini, na kwa nini?

      9 Namna gani wale wanaojitahidi sana kuwasaidia wengine bila uchoyo, kumaliza njaa, magonjwa, na ukosefu wa haki? Kwa kawaida, jitihada zao nzuri na za kujitolea zinawafaidi watu wengi. Lakini, hata wakijitahidi kadiri gani, hawawezi kamwe kubadili mfumo huu wa mambo uwe mzuri na wenye haki. Kwa nini? Kwa sababu ukweli ni kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” Shetani, naye hataki ubadilike.—1 Yohana 5:19.

      10. Watu waaminifu watapata “uzima ulio wa kweli” wakati gani?

      10 Inahuzunisha sana mtu kuweka tumaini lake lote katika ulimwengu huu! Paulo aliandika hivi: “Ikiwa ni katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi ndio wa kusikitikiwa zaidi kati ya watu wote.” Watu wengi wanaoamini kwamba maisha ndiyo haya tu, wana mtazamo huu: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:19, 32) Lakini kuna ahadi ya wakati ujao, yaani, ‘mbingu mpya na dunia mpya, ambazo tunangojea kulingana na ahadi ya Mungu, na humo uadilifu utakaa.’ (2 Petro 3:13) Wakati huo, Wakristo watafurahia “uzima ulio wa kweli,” yaani, “uzima wa milele” kwa ukamilifu, ama mbinguni au chini ya utawala wenye upendo wa serikali ya Ufalme wa Mungu!—1 Timotheo 6:12.

      11. Kwa nini kujitahidi kuendeleza mambo ya Ufalme wa Mungu ni jambo lenye kusudi?

      11 Ufalme wa Mungu tu ndio utakaosuluhisha kabisa matatizo ya wanadamu. Kwa hiyo, kujitahidi kuendeleza mambo ya Ufalme wa Mungu ndilo jambo lenye kusudi zaidi ambalo mtu anaweza kufuatia. (Yohana 4:34) Tunaposhiriki katika kazi hiyo, tunakuwa na uhusiano wenye thamani pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Pia, tunafurahia kutumika pamoja na mamilioni ya ndugu na dada zetu wa kiroho ambao wanafuatia kusudi kama letu maishani.

      Kujidhabihu kwa Njia Inayofaa

      12. Eleza tofauti iliyopo kati ya maisha katika mfumo wa sasa na “uzima ulio wa kweli.”

      12 Biblia inasema kwamba ulimwengu huu “unapitilia mbali na pia tamaa yake.” Kila sehemu ya ulimwengu wa Shetani itaharibiwa, kutia ndani umaarufu na utajiri wake, “lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:15-17) Tofauti na utajiri usio hakika, utukufu wa muda, na raha zisizoridhisha za mfumo huu, “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele chini ya Ufalme wa Mungu, utadumu na tunapaswa kujidhabihu kwa ajili yake, maadamu tunajidhabihu kwa njia inayofaa.

      13. Mume na mke fulani walijidhabihu kwa njia gani inayofaa?

      13 Wafikirie Henry na Suzanne. Wanaamini kabisa ahadi ya Mungu ya kwamba atawasaidia wote wanaotanguliza Ufalme maishani mwao. (Mathayo 6:33) Kwa hivyo, badala ya wote wawili kufanya kazi ya kuajiriwa, waliamua kuishi katika nyumba ya hali ya chini ili wawe na wakati zaidi wa kufuatia mambo ya kiroho pamoja na mabinti wao wawili. (Waebrania 13:15, 16) Rafiki yao mmoja mwenye nia nzuri hakuelewa kwa nini waliamua hivyo. Alimwambia Suzanne hivi: “Mpendwa, ikiwa unataka kuishi katika nyumba nzuri zaidi, ni lazima ujinyime kitu fulani.” Hata hivyo, Henry na Suzanne walijua kwamba kumtanguliza Yehova ‘kuna ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.’ (1 Timotheo 4:8; Tito 2:12) Mabinti wao walikuja kuwa waeneza-injili wenye bidii sana. Wakiwa familia wanahisi kwamba hawakukosa kitu chochote; badala yake walifaidika sana kwa kufanya mradi wa kufuatia “uzima ulio wa kweli” uwe kusudi lao.—Wafilipi 3:8; 1 Timotheo 6:6-8.

      ‘Usiutumie Ulimwengu kwa Ukamili’

      14. Kuacha kukazia fikira kusudi la kweli kunaweza kuongoza kwenye misiba gani?

      14 Hata hivyo, kuna hatari kubwa tukiacha kukazia fikira kusudi la kweli na kuacha kushika imara “uzima ulio wa kweli.” Tunakabili hatari ya “kuchukuliwa na mahangaiko na utajiri na raha za maisha haya.” (Luka 8:14) Tamaa zisizozuiwa na pia “mahangaiko ya maisha” yanaweza kutufanya tujihusishe kupita kiasi katika mfumo huu wa mambo. (Luka 21:34) Inahuzunisha kwamba watu fulani wamenaswa na tamaa inayoenea sasa ya kuwa matajiri na “wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi,” hata wamepoteza uhusiano wao wenye thamani pamoja na Yehova. Wamepata hasara kubwa kama nini kwa sababu ya ‘kutoshika imara uzima wa milele!’—1 Timotheo 6:9, 10, 12; Methali 28:20.

      15. Familia moja ilipata faida gani kwa sababu ya ‘kutoutumia ulimwengu kwa ukamili’?

      15 Paulo aliwashauri “wale wanaoutumia ulimwengu wawe kama wale wasioutumia kwa ukamili.” (1 Wakorintho 7:31) Keith na Bonnie walitii shauri hilo. Keith anasema hivi: “Niliamua kuwa Shahidi wa Yehova nilipokuwa nikikamilisha masomo yangu katika chuo cha udaktari wa meno. Nilihitaji kufanya uamuzi. Ningeweza kuwatibu wagonjwa wengi na kupata pesa nyingi, lakini kufanya hivyo kungeharibu hali yetu ya kiroho. Niliamua kutibu wagonjwa wachache ili nipate wakati zaidi wa kushughulikia mahitaji ya kiroho na ya kihisia ya familia yangu ambayo baadaye ilikuwa na mabinti watano. Ingawa mara nyingi hatukuwa na pesa nyingi, tulijifunza kupunguza gharama, na sikuzote tulikuwa na vitu tulivyohitaji. Familia yetu ilikuwa na uhusiano wa karibu, wenye uchangamfu, na ilikuwa yenye furaha sana. Mwishowe, sisi sote tuliingia katika huduma ya wakati wote. Sasa mabinti wetu wana ndoa zenye furaha, na watatu kati yao wana watoto. Familia zao pia zina furaha zinapoendelea kutanguliza kusudi la Yehova maishani.”

      Kutanguliza Kusudi la Mungu Maishani Mwako

      16, 17. Biblia inataja mifano gani ya watu ambao walikuwa na vipawa, na kwa nini wanakumbukwa?

      16 Biblia inataja mifano ya watu ambao waliishi kupatana na kusudi la Mungu na wale ambao hawakufanya hivyo. Mambo tunayojifunza kutokana na mifano hiyo yanawafaa watu wa kila umri, utamaduni, na hali. (Waroma 15:4; 1 Wakorintho 10:6, 11) Nimrodi alijenga majiji makubwa, lakini alifanya hivyo kwa kumpinga Yehova. (Mwanzo 10:8, 9) Hata hivyo, watu wengine wengi waliweka mifano mizuri. Kwa mfano, Musa hakufanya kusudi lake maishani liwe kudumisha cheo chake akiwa Mmisri mwenye kuheshimiwa. Badala yake, alithamini sana mapendeleo yake ya kiroho na kuyaona “kuwa ni utajiri mkubwa kuliko hazina za Misri.” (Waebrania 11:26) Inaelekea kwamba daktari Luka alimsaidia Paulo na wengine katika magonjwa yao. Lakini Luka aliwafaidi wengine sana kwa kuwa mweneza-injili na mwandikaji wa Biblia. Naye Paulo, hakujulikani kuwa mtaalamu wa Sheria, bali mmishonari, “mtume kwa mataifa.”—Waroma 11:13.

      17 Daudi anakumbukwa hasa kwa sababu ya kuwa ‘mtu aliyekubalika kwa moyo wa Mungu,’ wala si kama kiongozi wa jeshi au mwimbaji na mtungaji wa muziki. (1 Samweli 13:14) Tunamjua Danieli kwa sababu ya utumishi wake akiwa nabii mshikamanifu wa Yehova wala si ofisa wa serikali ya Babiloni; tunamkumbuka Esta kwa sababu ya mfano wake wa ujasiri na imani wala si kwa sababu alikuwa malkia wa Uajemi; tunawakumbuka Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana kama mitume wa Yesu wala si wavuvi hodari. Na mwishowe, tunamkumbuka Yesu akiwa “Kristo” wala si “seremala.” (Marko 6:3; Mathayo 16:16) Wote hao walielewa wazi kwamba hata iwe walikuwa na vipawa, mali, au cheo gani, walipaswa kutanguliza utumishi wa Mungu maishani mwao wala si kazi za kimwili. Walijua kwamba kusudi bora zaidi na lenye kuthawabisha zaidi ambalo wangeweza kuwa nalo ni kuwa wanaume au wanawake wanaomwogopa Mungu.

      18. Kijana mmoja Mkristo aliamua kutumia maisha yake kwa njia gani, na mwishowe alitambua nini?

      18 Mwishowe Seung Jin, aliyetajwa mwanzoni, alielewa jambo hilo pia. Anasema hivi: “Badala ya kutumia nguvu zangu zote katika udaktari, usanii, au ualimu, niliazimia kutumia maisha yangu kupatana na wakfu wangu kwa Mungu. Sasa ninatumika katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa walimu wa Biblia, nikiwasaidia watu watembee katika njia ya uzima wa milele. Mwanzoni nilifikiri kwamba huduma ya wakati wote haisisimui sana. Sasa maisha yangu yanasisimua sana kuliko wakati mwingine wowote kadiri ninavyojitahidi kuboresha utu wangu na uwezo wangu wa kuwafundisha watu wenye utamaduni mbalimbali. Ninaona kwamba kufanya kusudi la Yehova liwe kusudi letu ndiyo njia pekee ya maisha yenye maana.”

      19. Tunaweza kupata jinsi gani kusudi la kweli maishani?

      19 Tukiwa Wakristo, tumebarikiwa kuwa na ujuzi wenye kuokoa uhai na tumepata tumaini la wokovu. (Yohana 17:3) Basi acheni ‘tusipokee fadhili zisizostahiliwa za Mungu kisha tukose kusudi lake.’ (2 Wakorintho 6:1) Badala yake, acheni tutumie siku zetu na miaka yetu ambayo ni yenye thamani kumsifu Yehova. Acheni tueneze ujuzi unaoleta furaha ya kweli sasa na unaoongoza kwenye uzima wa milele. Tukifanya hivyo, tutaona maneno haya ya Yesu yakitimia katika maisha yetu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Na tutapata kusudi la kweli maishani.

      [Maelezo ya Chini]

      a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

  • Kufuatia Kusudi La Mungu Leo
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Oktoba 1
    • Kufuatia Kusudi La Mungu Leo

      “[Kristo] alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe.”—2 WAKORINTHO 5:15.

      1. Simulia jambo lililoonwa na mmishonari mmoja katika mgawo wake.

      “GARI letu ndilo lililokuwa gari la kwanza lisilo la kivita kuingia katika kijiji fulani cha Waafrika baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe kuisha,” alikumbuka mmishonari mmoja anayeitwa Aaron.a “Mawasiliano pamoja na kutaniko dogo la huko yalikuwa yamekatizwa, na tulilazimika kushughulikia mahitaji ya akina ndugu. Tulibeba chakula, mavazi, na vichapo vya Biblia, na vilevile video ya Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name (Les Témoins de Jéhovah: un nom, une organisation).b Tulihitaji kuonyesha video hiyo mara mbili kwa sababu watu wengi wenye kupendezwa walijaa katika nyumba kubwa ya nyasi iliyotumiwa kama jumba la sinema katika kijiji hicho. Nyumba hiyo ilikuwa na mashini ya video na televisheni. Tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia kwa sababu ya maonyesho hayo. Ni wazi kwamba jitihada zote tulizofanya hazikuwa za bure.”

      2. (a) Kwa nini Wakristo wanaazimia kutumia maisha yao katika utumishi wa Mungu? (b) Sasa tutazungumzia maswali gani?

      2 Kwa nini Aaron na wenzake walifanya utumishi huo mgumu? Kwa sababu wameweka maisha yao wakfu kwa Mungu ili kuonyesha kwamba wanathamini dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, nao wanataka kutumia maisha yao kupatana na kusudi la Mungu. Kama Aaron na wenzake, Wakristo wote waliojiweka wakfu wameazimia ‘kutoishi tena kwa ajili yao wenyewe’ bali kufanya yote wanayoweza “kwa ajili ya habari njema.” (2 Wakorintho 5:15; 1 Wakorintho 9:23) Wanajua kwamba mfumo huu wa mambo utakapofikia mwisho wake, umaarufu na pesa zote katika ulimwengu hazitakuwa na thamani yoyote. Kwa hiyo, wanataka kutumia uhai na afya yao kupatana na kusudi la Mungu. (Mhubiri 12:1) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Tunaweza kupata wapi ujasiri na nguvu za kufanya hivyo? Na tuna nafasi gani za kupanua utumishi wetu?

      Kuchukua Hatua Zinazofaa za Kufanya Maendeleo

      3. Kufanya mapenzi ya Mungu kunatia ndani hatua gani za msingi?

      3 Kufanya mapenzi ya Mungu ni jambo ambalo Wakristo wa kweli wanafuatia katika maisha yao yote. Kwa kawaida, tunaanza na hatua za msingi kama vile kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kusoma Biblia kila siku, kushiriki katika kazi ya kuhubiri, na kufanya maendeleo kufikia ubatizo. Tunapofanya maendeleo, tunakumbuka maneno haya ya mtume Paulo: “Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yawe wazi kwa watu wote.” (1 Timotheo 4:15) Hatufanyi maendeleo hayo ili tujitukuze lakini tunaonyesha azimio letu la kufanya mapenzi ya Mungu bila ubinafsi. Kuchukua hatua hiyo kunaonyesha kwamba tunamruhusu Mungu aongoze hatua zetu katika mambo yote maishani, naye anafanya hivyo kwa njia bora kuliko tunavyoweza kujiongoza.—Zaburi 32:8.

      4. Tunaweza kushinda jinsi gani wasiwasi usiofaa?

      4 Hata hivyo, kusitasita au kujihangaikia kupita kiasi kunaweza kutuzuia kufanya maendeleo katika utumishi wa Mungu. (Mhubiri 11:4) Kwa hiyo, ili tupate shangwe ya kweli katika kumtumikia Mungu na wengine, huenda tukahitaji kwanza kushinda wasiwasi wetu. Kwa mfano, Erik alikuwa akifikiria kutumika katika kutaniko la lugha ya kigeni. Lakini alikuwa na wasiwasi: ‘Je, kweli watanikubali? Je, nitawapenda ndugu hao? Je, watanipenda?’ Anasema hivi: “Mwishowe nilitambua kwamba nilihitaji kuwafikiria zaidi ndugu hao kuliko kujifikiria mwenyewe. Niliamua kuacha kuhangaikia mambo yaliyonifanya niwe na wasiwasi na badala yake kujitoa tu bila ubinafsi katika njia yoyote niliyoweza. Nilisali ili nipate msaada kisha nikaendelea na mipango yangu. Sasa ninafurahia sana utumishi wangu.” (Waroma 4:20) Ndiyo, kwa kadiri ambavyo tunamtumikia Mungu na wengine bila ubinafsi, ndivyo tunavyopata shangwe na kuridhika.

      5. Kwa nini tunahitaji kupanga mambo yetu kwa uangalifu ili kufuatia kusudi la Mungu? Toa mfano.

      5 Ili kufuatia kusudi la Mungu kwa mafanikio tunahitaji pia kupanga mambo yetu kwa uangalifu. Kwa hekima, tunaepuka kuwa na madeni mengi ambayo yanaweza kutufanya tuwe watumwa wa mfumo huu na kutuzuia kufanya kazi ya Mungu. Biblia inatukumbusha hivi: “Mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.” (Methali 22:7) Kumtegemea Yehova na kutanguliza mambo ya kiroho kutatusaidia kuona mambo kwa njia inayofaa. Kwa mfano, Guoming na dada zake wawili wanaishi pamoja na mama yao mahali ambapo gharama za nyumba ziko juu na kazi hazipatikani kwa urahisi. Kwa kutumia pesa zao kwa uangalifu na kugawana gharama, wanatimiza mahitaji yao hata wakati ambapo wengine wao hawana kazi. Guoming anasema hivi: “Nyakati nyingine, wengine wetu hatupati mshahara. Hata hivyo, tunaendelea na huduma yetu ya upainia na pia tunamtunza vizuri mama yetu. Tunashukuru kwamba Mama yetu hataki tuache mambo ya kiroho ili tumtafutie mambo ya kustarehesha maishani.”—2 Wakorintho 12:14; Waebrania 13:5.

      6. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba tunaweza kubadili maisha yetu ili yapatane na kusudi la Mungu?

      6 Ikiwa unafuatia sana mambo ya kimwili, kutafuta pesa au mambo mengine, huenda ukahitaji kufanya marekebisho makubwa ili utangulize kusudi la Mungu. Kwa kawaida, mabadiliko hayo hayawezi kufanywa mara moja, na hupaswi kufikiri kwamba umeshindwa ukikosea mwanzoni. Mfikirie Koichi, ambaye alikuwa na tatizo la kutumia wakati mwingi sana katika tafrija. Koichi alijifunza Biblia akiwa kijana, lakini kwa miaka mingi, alitumia wakati mwingi sana kucheza michezo ya video. Siku moja Koichi alijiuliza hivi: ‘Ninafanya nini? Nina umri wa miaka 30 hivi nami situmii maisha yangu kwa njia yoyote yenye kusudi!’ Koichi alianza tena kujifunza Biblia naye akakubali msaada kutoka kwa kutaniko. Ijapokuwa alibadilika polepole, hakukata tamaa. Kwa kusali sana na kwa utegemezo wenye upendo kutoka kwa wengine, mwishowe aliacha kabisa zoea lake. (Luka 11:9) Sasa Koichi anafurahia kutumika akiwa mtumishi wa huduma.

      Jifunze Kuwa na Usawaziko

      7. Kwa nini tunahitaji kuwa na usawaziko tunapofanya kazi ya Mungu?

      7 Kufuatia kusudi la Mungu kunastahili jitihada zetu za nafsi yote. Hatupaswi kamwe kujihurumia au kuwa wavivu tunapofanya hivyo. (Waebrania 6:11, 12) Hata hivyo, Yehova hataki tujichoshe kabisa kimwili, kiakili, au kihisia. Kukubali kwa unyenyekevu kwamba hatuwezi kutimiza kazi ya Mungu kwa nguvu zetu wenyewe kunamletea utukufu na kunaonyesha kwamba tuna usawaziko. (1 Petro 4:11) Yehova anaahidi kutupa nguvu tunazohitaji ili tufanye mapenzi yake, lakini hatupaswi kujisukuma kupita tunavyoweza, tukijaribu kufanya yale ambayo Yehova hatutarajii tufanye. (2 Wakorintho 4:7) Ili tuendelee kumtumikia Mungu bila kujichosha, tunahitaji kutumia nguvu zetu kwa hekima.

      8. Ni nini kilichotukia wakati kijana mmoja Mkristo alipojaribu kumtumikia Yehova na ulimwengu kwa nguvu zake zote, naye alifanya mabadiliko gani?

      8 Kwa mfano, kwa miaka miwili Ji Hye, ambaye anaishi Asia Mashariki, alifanya kazi yenye shughuli nyingi sana huku akifanya upainia. Anasema hivi: “Nilijaribu kumtumikia Yehova na ulimwengu kwa nguvu zangu zote, lakini nilikuwa nikilala kwa saa tano tu kila usiku. Mwishowe, sikuwa na nguvu zozote za kukazia fikira kweli, na mambo ya kiroho hayakuniletea shangwe ya kutosha.” Ili amtumikie Yehova kwa ‘moyo, nafsi, akili, na nguvu zake zote,’ Ji Hye alitafuta kazi isiyo na shughuli nyingi. (Marko 12:30) Anasema hivi: “Ingawa familia yangu ilinisukuma ili nitafute pesa nyingi, nilijitahidi kutanguliza kusudi la Mungu. Bado ninapata pesa za kutosha kushughulikia mambo ya msingi, kama vile kununua mavazi mazuri. Ninafurahi kuwa na wakati wa kutosha wa kulala! Ninapata shangwe katika huduma yangu nami nina nguvu zaidi kiroho sasa. Hiyo ni kwa sababu sivutiwi na sikengeushwi fikira na vitu vya ulimwengu.”—Mhubiri 4:6; Mathayo 6:24, 28-30.

      9. Jitihada zetu katika huduma zinaweza kuwa na matokeo gani kwa watu?

      9 Si kila mtu anaweza kumtumikia Mungu akiwa mweneza-injili wa wakati wote. Ikiwa unapambana na uzee, afya mbaya, au udhaifu mwingine, kumbuka kwamba Yehova anathamini sana uaminifu wako na utumishi mwingine wa moyo wote ambao unaweza kutoa. (Luka 21:2, 3) Kwa hiyo, kila mmoja wetu hapaswi kupuuza matokeo mazuri ya jitihada zetu kwa wengine, hata ikiwa ni jitihada ndogo. Kwa mfano, tuseme kwamba tumetembelea nyumba chache na hatukupata mtu yeyote anayependezwa na ujumbe wetu. Baada ya kuondoka, huenda wenye nyumba wakaongea kuhusu ziara yetu kwa saa au siku nyingi, hata ikiwa hawakutukaribisha nyumbani mwao! Hatutazamii kwamba kila mtu ambaye anasikia habari njema atakubali ujumbe wetu, lakini wengine watakubali. (Mathayo 13:19-23) Huenda wengine wakakubali ujumbe wetu baadaye wakati maisha yao au hali za ulimwengu zinapobadilika. Kwa vyovyote vile, tunapofanya yote tunayoweza katika huduma yetu ya hadharani, tunafanya kazi ya Mungu. Sisi ni “wafanyakazi wenzi wa Mungu.”—1 Wakorintho 3:9.

      10. Washiriki wote wa kutaniko wana nafasi gani?

      10 Kwa kuongezea, sote tunaweza kuwasaidia watu wa familia yetu, na ndugu na dada zetu wa kiroho. (Wagalatia 6:10) Uvutano wetu mzuri kwa wengine unaweza kuwa na matokeo makubwa sana na yenye kudumu. (Mhubiri 11:1, 6) Wazee na watumishi wa huduma wanapotimiza migawo yao kwa bidii, wanalisaidia kutaniko kuwa na afya nzuri ya kiroho na kuwa imara, na utendaji wa Kikristo unaongezeka. Tunahakikishiwa kwamba ‘tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana,’ kazi yetu haitakuwa “ya bure.”—1 Wakorintho 15:58.

      Kufuatia Kusudi la Mungu Kama Kazi ya Maisha

      11. Mbali na kutumika katika kutaniko letu, huenda tukapata nafasi gani nyingine?

      11 Tukiwa Wakristo, tunapenda uhai, na tungependa kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu. (1 Wakorintho 10:31) Tunapojitahidi kwa uaminifu kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuwafundisha wengine kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru, tutapata mapendeleo mengi ya utumishi yenye kuthawabisha. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Zaidi ya kutumika katika kutaniko letu, huenda tukapata nafasi za kutumika mahali penye uhitaji mkubwa zaidi, iwe katika eneo lingine, katika lugha ya kigeni, au nchi nyingine. Wazee na watumishi wa huduma wanaostahili ambao hawajaoa wanaweza kualikwa wahudhurie Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, na baadaye kutumika katika makutaniko ambayo yana uhitaji wa Wakristo waliokomaa, iwe ni katika nchi yao au nchi nyingine. Wenzi wa ndoa ambao wako katika huduma ya wakati wote wanaweza kustahili kupata mazoezi ya umishonari katika shule ya Gileadi na kutumika katika nchi nyingine. Na kuna uhitaji mkubwa zaidi na zaidi wa wajitoleaji ambao wanaweza kufanya kazi mbalimbali Betheli, na pia kujenga na kutunza majumba ya mikutano na ofisi za tawi.

      12, 13. (a) Unaweza kuchagua jinsi gani mapendeleo ya utumishi ya kufuatia? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi uzoefu tunaopata katika mgawo mmoja unavyoweza kutusaidia katika migawo mingine.

      12 Unapaswa kufuatia mapendeleo gani ya utumishi? Ukiwa mtumishi aliyejiweka wakfu kwa Yehova, sikuzote tafuta mwongozo wake na wa tengenezo lake. ‘Roho yake njema’ itakusaidia kufanya uamuzi unaofaa. (Nehemia 9:20) Mara nyingi, mgawo mmoja unaongoza kwenye mgawo mwingine, na uzoefu na ustadi ambao unapata katika mgawo fulani wa utumishi unaweza kukusaidia katika mgawo mwingine baadaye.

      13 Kwa mfano, Dennis na mke wake, Jenny, wanashiriki kwa ukawaida katika miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Baada ya Kimbunga Katrina kukumba eneo la kusini mwa Marekani, walijitolea katika kazi ya kutoa msaada. Dennis anasema hivi: “Kutumia ufundi ambao tulijifunza katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme kuwasaidia ndugu zetu kumetuletea shangwe kubwa sana. Kwa kweli, shukrani ambazo tunapokea kutoka kwa wale ambao tumewasaidia zinagusa moyo sana. Vikundi vingine vya kutoa misaada havijafanikiwa sana katika kazi ya kurekebisha majengo ambayo yaliharibiwa. Tayari Mashahidi wa Yehova wamerekebisha au kujenga upya nyumba zaidi ya 5,300 na Majumba mengi ya Ufalme. Watu wanaona kazi hiyo nao wanapendezwa zaidi na ujumbe wetu.”

      14. Unaweza kufanya nini ikiwa unatamani kufuatia huduma ya wakati wote?

      14 Je, unaweza kufuatia kusudi la Mungu kwa kuchagua huduma ya wakati wote iwe kazi yako ya maisha? Bila shaka, utapata baraka nyingi ukifanya hivyo. Ikiwa hali zako za sasa hazikuruhusu, labda unaweza kuzibadili. Sali kama Nehemia alivyosali alipotamani kuanza mgawo muhimu: “Ah, tafadhali, Yehova, . . . mpe mafanikio mtumishi wako.” (Nehemia 1:11) Kisha, tenda kupatana na sala yako huku ukimtegemea “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Ili Yehova abariki jitihada zako za kumtumikia kikamili zaidi, ni lazima kwanza utie bidii. Mara tu unapoamua kuanza huduma ya wakati wote, shikamana na uamuzi wako. Kadiri wakati unavyopita ndivyo utakavyopata uzoefu zaidi, na shangwe yako itaongezeka.

      Maisha Yenye Kusudi Kwelikweli

      15. (a) Tunafaidika jinsi gani tunaposoma masimulizi ya wale ambao wamemtumikia Mungu kwa muda mrefu na tunapozungumza nao? (b) Taja simulizi la maisha ambalo limekutia moyo sana.

      15 Unaweza kutazamia kupata matokeo gani ukifuatia kusudi la Mungu? Zungumza na watumishi ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu, hasa wale ambao wamefanya huduma ya wakati wote kwa miaka mingi. Wana maisha yenye kuridhisha na yenye kusudi kwelikweli! (Methali 10:22) Watakwambia kwamba Yehova hajakosa kamwe kuwasaidia kupata vitu wanavyohitaji sana na vitu vingine zaidi hata wanapokuwa katika hali ngumu. (Wafilipi 4:11-13) Tangu mwaka wa 1955 mpaka 1961, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilikuwa na mfululizo wa masimulizi ya maisha ya watu waaminifu. Mfululizo huo ulikuwa na kichwa, “Kufuatia Kusudi Langu Maishani.” Kuanzia wakati huo, mamia ya masimulizi mengine ya maisha yamechapishwa. Kila simulizi linaonyesha roho ya bidii na shangwe ambayo inatukumbusha yale yanayosemwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo ya Mitume. Ukisoma masimulizi hayo yenye kusisimua utachochewa kusema hivi: ‘Hayo ndiyo maisha ninayotaka!’

      16. Ni nini kinachofanya maisha ya Mkristo yawe yenye kusudi na furaha?

      16 Aaron ambaye alitajwa mwanzoni mwa habari hii, anakumbuka hivi: “Nikiwa Afrika, mara nyingi nilikutana na vijana ambao walikuwa wakitanga-tanga kila mahali nchini wakitafuta maisha yenye kusudi. Wengi wao hawakupata kamwe kusudi lolote. Lakini sisi tulikuwa tukifuatia kusudi la Mungu kwa kueneza habari njema ya Ufalme, na tulifurahia sana maisha mapya na yenye kusudi. Tumejionea wenyewe kwamba kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

      17. Kwa nini tunapaswa kufuatia kusudi la Mungu sasa?

      17 Namna gani wewe? Unafuatia kusudi gani? Ikiwa huna mradi wowote wa kiroho ulio wazi, utaanza kufuatia mambo mengine. Kwa nini upoteze uhai wako wenye thamani ukifuatia ndoto za mchana za ulimwengu wa Shetani? Hivi karibuni, “dhiki kuu” itakapotokea, utajiri wa kimwili na vyeo vya ulimwengu havitakuwa na maana yoyote. Jambo la maana litakuwa uhusiano wetu pamoja na Yehova. Tutashukuru kama nini kwamba tumemtumikia Mungu na wengine na tumefuatia kikamili kusudi la Mungu katika maisha yetu!—Mathayo 24:21; Ufunuo 7:14, 15.

      [Maelezo ya Chini]

      a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

      b Imetayarishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki