Kufuatia Kusudi La Mungu Leo
“[Kristo] alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe.”—2 WAKORINTHO 5:15.
1. Simulia jambo lililoonwa na mmishonari mmoja katika mgawo wake.
“GARI letu ndilo lililokuwa gari la kwanza lisilo la kivita kuingia katika kijiji fulani cha Waafrika baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe kuisha,” alikumbuka mmishonari mmoja anayeitwa Aaron.a “Mawasiliano pamoja na kutaniko dogo la huko yalikuwa yamekatizwa, na tulilazimika kushughulikia mahitaji ya akina ndugu. Tulibeba chakula, mavazi, na vichapo vya Biblia, na vilevile video ya Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name (Les Témoins de Jéhovah: un nom, une organisation).b Tulihitaji kuonyesha video hiyo mara mbili kwa sababu watu wengi wenye kupendezwa walijaa katika nyumba kubwa ya nyasi iliyotumiwa kama jumba la sinema katika kijiji hicho. Nyumba hiyo ilikuwa na mashini ya video na televisheni. Tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia kwa sababu ya maonyesho hayo. Ni wazi kwamba jitihada zote tulizofanya hazikuwa za bure.”
2. (a) Kwa nini Wakristo wanaazimia kutumia maisha yao katika utumishi wa Mungu? (b) Sasa tutazungumzia maswali gani?
2 Kwa nini Aaron na wenzake walifanya utumishi huo mgumu? Kwa sababu wameweka maisha yao wakfu kwa Mungu ili kuonyesha kwamba wanathamini dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, nao wanataka kutumia maisha yao kupatana na kusudi la Mungu. Kama Aaron na wenzake, Wakristo wote waliojiweka wakfu wameazimia ‘kutoishi tena kwa ajili yao wenyewe’ bali kufanya yote wanayoweza “kwa ajili ya habari njema.” (2 Wakorintho 5:15; 1 Wakorintho 9:23) Wanajua kwamba mfumo huu wa mambo utakapofikia mwisho wake, umaarufu na pesa zote katika ulimwengu hazitakuwa na thamani yoyote. Kwa hiyo, wanataka kutumia uhai na afya yao kupatana na kusudi la Mungu. (Mhubiri 12:1) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Tunaweza kupata wapi ujasiri na nguvu za kufanya hivyo? Na tuna nafasi gani za kupanua utumishi wetu?
Kuchukua Hatua Zinazofaa za Kufanya Maendeleo
3. Kufanya mapenzi ya Mungu kunatia ndani hatua gani za msingi?
3 Kufanya mapenzi ya Mungu ni jambo ambalo Wakristo wa kweli wanafuatia katika maisha yao yote. Kwa kawaida, tunaanza na hatua za msingi kama vile kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kusoma Biblia kila siku, kushiriki katika kazi ya kuhubiri, na kufanya maendeleo kufikia ubatizo. Tunapofanya maendeleo, tunakumbuka maneno haya ya mtume Paulo: “Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yawe wazi kwa watu wote.” (1 Timotheo 4:15) Hatufanyi maendeleo hayo ili tujitukuze lakini tunaonyesha azimio letu la kufanya mapenzi ya Mungu bila ubinafsi. Kuchukua hatua hiyo kunaonyesha kwamba tunamruhusu Mungu aongoze hatua zetu katika mambo yote maishani, naye anafanya hivyo kwa njia bora kuliko tunavyoweza kujiongoza.—Zaburi 32:8.
4. Tunaweza kushinda jinsi gani wasiwasi usiofaa?
4 Hata hivyo, kusitasita au kujihangaikia kupita kiasi kunaweza kutuzuia kufanya maendeleo katika utumishi wa Mungu. (Mhubiri 11:4) Kwa hiyo, ili tupate shangwe ya kweli katika kumtumikia Mungu na wengine, huenda tukahitaji kwanza kushinda wasiwasi wetu. Kwa mfano, Erik alikuwa akifikiria kutumika katika kutaniko la lugha ya kigeni. Lakini alikuwa na wasiwasi: ‘Je, kweli watanikubali? Je, nitawapenda ndugu hao? Je, watanipenda?’ Anasema hivi: “Mwishowe nilitambua kwamba nilihitaji kuwafikiria zaidi ndugu hao kuliko kujifikiria mwenyewe. Niliamua kuacha kuhangaikia mambo yaliyonifanya niwe na wasiwasi na badala yake kujitoa tu bila ubinafsi katika njia yoyote niliyoweza. Nilisali ili nipate msaada kisha nikaendelea na mipango yangu. Sasa ninafurahia sana utumishi wangu.” (Waroma 4:20) Ndiyo, kwa kadiri ambavyo tunamtumikia Mungu na wengine bila ubinafsi, ndivyo tunavyopata shangwe na kuridhika.
5. Kwa nini tunahitaji kupanga mambo yetu kwa uangalifu ili kufuatia kusudi la Mungu? Toa mfano.
5 Ili kufuatia kusudi la Mungu kwa mafanikio tunahitaji pia kupanga mambo yetu kwa uangalifu. Kwa hekima, tunaepuka kuwa na madeni mengi ambayo yanaweza kutufanya tuwe watumwa wa mfumo huu na kutuzuia kufanya kazi ya Mungu. Biblia inatukumbusha hivi: “Mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.” (Methali 22:7) Kumtegemea Yehova na kutanguliza mambo ya kiroho kutatusaidia kuona mambo kwa njia inayofaa. Kwa mfano, Guoming na dada zake wawili wanaishi pamoja na mama yao mahali ambapo gharama za nyumba ziko juu na kazi hazipatikani kwa urahisi. Kwa kutumia pesa zao kwa uangalifu na kugawana gharama, wanatimiza mahitaji yao hata wakati ambapo wengine wao hawana kazi. Guoming anasema hivi: “Nyakati nyingine, wengine wetu hatupati mshahara. Hata hivyo, tunaendelea na huduma yetu ya upainia na pia tunamtunza vizuri mama yetu. Tunashukuru kwamba Mama yetu hataki tuache mambo ya kiroho ili tumtafutie mambo ya kustarehesha maishani.”—2 Wakorintho 12:14; Waebrania 13:5.
6. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba tunaweza kubadili maisha yetu ili yapatane na kusudi la Mungu?
6 Ikiwa unafuatia sana mambo ya kimwili, kutafuta pesa au mambo mengine, huenda ukahitaji kufanya marekebisho makubwa ili utangulize kusudi la Mungu. Kwa kawaida, mabadiliko hayo hayawezi kufanywa mara moja, na hupaswi kufikiri kwamba umeshindwa ukikosea mwanzoni. Mfikirie Koichi, ambaye alikuwa na tatizo la kutumia wakati mwingi sana katika tafrija. Koichi alijifunza Biblia akiwa kijana, lakini kwa miaka mingi, alitumia wakati mwingi sana kucheza michezo ya video. Siku moja Koichi alijiuliza hivi: ‘Ninafanya nini? Nina umri wa miaka 30 hivi nami situmii maisha yangu kwa njia yoyote yenye kusudi!’ Koichi alianza tena kujifunza Biblia naye akakubali msaada kutoka kwa kutaniko. Ijapokuwa alibadilika polepole, hakukata tamaa. Kwa kusali sana na kwa utegemezo wenye upendo kutoka kwa wengine, mwishowe aliacha kabisa zoea lake. (Luka 11:9) Sasa Koichi anafurahia kutumika akiwa mtumishi wa huduma.
Jifunze Kuwa na Usawaziko
7. Kwa nini tunahitaji kuwa na usawaziko tunapofanya kazi ya Mungu?
7 Kufuatia kusudi la Mungu kunastahili jitihada zetu za nafsi yote. Hatupaswi kamwe kujihurumia au kuwa wavivu tunapofanya hivyo. (Waebrania 6:11, 12) Hata hivyo, Yehova hataki tujichoshe kabisa kimwili, kiakili, au kihisia. Kukubali kwa unyenyekevu kwamba hatuwezi kutimiza kazi ya Mungu kwa nguvu zetu wenyewe kunamletea utukufu na kunaonyesha kwamba tuna usawaziko. (1 Petro 4:11) Yehova anaahidi kutupa nguvu tunazohitaji ili tufanye mapenzi yake, lakini hatupaswi kujisukuma kupita tunavyoweza, tukijaribu kufanya yale ambayo Yehova hatutarajii tufanye. (2 Wakorintho 4:7) Ili tuendelee kumtumikia Mungu bila kujichosha, tunahitaji kutumia nguvu zetu kwa hekima.
8. Ni nini kilichotukia wakati kijana mmoja Mkristo alipojaribu kumtumikia Yehova na ulimwengu kwa nguvu zake zote, naye alifanya mabadiliko gani?
8 Kwa mfano, kwa miaka miwili Ji Hye, ambaye anaishi Asia Mashariki, alifanya kazi yenye shughuli nyingi sana huku akifanya upainia. Anasema hivi: “Nilijaribu kumtumikia Yehova na ulimwengu kwa nguvu zangu zote, lakini nilikuwa nikilala kwa saa tano tu kila usiku. Mwishowe, sikuwa na nguvu zozote za kukazia fikira kweli, na mambo ya kiroho hayakuniletea shangwe ya kutosha.” Ili amtumikie Yehova kwa ‘moyo, nafsi, akili, na nguvu zake zote,’ Ji Hye alitafuta kazi isiyo na shughuli nyingi. (Marko 12:30) Anasema hivi: “Ingawa familia yangu ilinisukuma ili nitafute pesa nyingi, nilijitahidi kutanguliza kusudi la Mungu. Bado ninapata pesa za kutosha kushughulikia mambo ya msingi, kama vile kununua mavazi mazuri. Ninafurahi kuwa na wakati wa kutosha wa kulala! Ninapata shangwe katika huduma yangu nami nina nguvu zaidi kiroho sasa. Hiyo ni kwa sababu sivutiwi na sikengeushwi fikira na vitu vya ulimwengu.”—Mhubiri 4:6; Mathayo 6:24, 28-30.
9. Jitihada zetu katika huduma zinaweza kuwa na matokeo gani kwa watu?
9 Si kila mtu anaweza kumtumikia Mungu akiwa mweneza-injili wa wakati wote. Ikiwa unapambana na uzee, afya mbaya, au udhaifu mwingine, kumbuka kwamba Yehova anathamini sana uaminifu wako na utumishi mwingine wa moyo wote ambao unaweza kutoa. (Luka 21:2, 3) Kwa hiyo, kila mmoja wetu hapaswi kupuuza matokeo mazuri ya jitihada zetu kwa wengine, hata ikiwa ni jitihada ndogo. Kwa mfano, tuseme kwamba tumetembelea nyumba chache na hatukupata mtu yeyote anayependezwa na ujumbe wetu. Baada ya kuondoka, huenda wenye nyumba wakaongea kuhusu ziara yetu kwa saa au siku nyingi, hata ikiwa hawakutukaribisha nyumbani mwao! Hatutazamii kwamba kila mtu ambaye anasikia habari njema atakubali ujumbe wetu, lakini wengine watakubali. (Mathayo 13:19-23) Huenda wengine wakakubali ujumbe wetu baadaye wakati maisha yao au hali za ulimwengu zinapobadilika. Kwa vyovyote vile, tunapofanya yote tunayoweza katika huduma yetu ya hadharani, tunafanya kazi ya Mungu. Sisi ni “wafanyakazi wenzi wa Mungu.”—1 Wakorintho 3:9.
10. Washiriki wote wa kutaniko wana nafasi gani?
10 Kwa kuongezea, sote tunaweza kuwasaidia watu wa familia yetu, na ndugu na dada zetu wa kiroho. (Wagalatia 6:10) Uvutano wetu mzuri kwa wengine unaweza kuwa na matokeo makubwa sana na yenye kudumu. (Mhubiri 11:1, 6) Wazee na watumishi wa huduma wanapotimiza migawo yao kwa bidii, wanalisaidia kutaniko kuwa na afya nzuri ya kiroho na kuwa imara, na utendaji wa Kikristo unaongezeka. Tunahakikishiwa kwamba ‘tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana,’ kazi yetu haitakuwa “ya bure.”—1 Wakorintho 15:58.
Kufuatia Kusudi la Mungu Kama Kazi ya Maisha
11. Mbali na kutumika katika kutaniko letu, huenda tukapata nafasi gani nyingine?
11 Tukiwa Wakristo, tunapenda uhai, na tungependa kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu. (1 Wakorintho 10:31) Tunapojitahidi kwa uaminifu kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuwafundisha wengine kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru, tutapata mapendeleo mengi ya utumishi yenye kuthawabisha. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Zaidi ya kutumika katika kutaniko letu, huenda tukapata nafasi za kutumika mahali penye uhitaji mkubwa zaidi, iwe katika eneo lingine, katika lugha ya kigeni, au nchi nyingine. Wazee na watumishi wa huduma wanaostahili ambao hawajaoa wanaweza kualikwa wahudhurie Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, na baadaye kutumika katika makutaniko ambayo yana uhitaji wa Wakristo waliokomaa, iwe ni katika nchi yao au nchi nyingine. Wenzi wa ndoa ambao wako katika huduma ya wakati wote wanaweza kustahili kupata mazoezi ya umishonari katika shule ya Gileadi na kutumika katika nchi nyingine. Na kuna uhitaji mkubwa zaidi na zaidi wa wajitoleaji ambao wanaweza kufanya kazi mbalimbali Betheli, na pia kujenga na kutunza majumba ya mikutano na ofisi za tawi.
12, 13. (a) Unaweza kuchagua jinsi gani mapendeleo ya utumishi ya kufuatia? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi uzoefu tunaopata katika mgawo mmoja unavyoweza kutusaidia katika migawo mingine.
12 Unapaswa kufuatia mapendeleo gani ya utumishi? Ukiwa mtumishi aliyejiweka wakfu kwa Yehova, sikuzote tafuta mwongozo wake na wa tengenezo lake. ‘Roho yake njema’ itakusaidia kufanya uamuzi unaofaa. (Nehemia 9:20) Mara nyingi, mgawo mmoja unaongoza kwenye mgawo mwingine, na uzoefu na ustadi ambao unapata katika mgawo fulani wa utumishi unaweza kukusaidia katika mgawo mwingine baadaye.
13 Kwa mfano, Dennis na mke wake, Jenny, wanashiriki kwa ukawaida katika miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Baada ya Kimbunga Katrina kukumba eneo la kusini mwa Marekani, walijitolea katika kazi ya kutoa msaada. Dennis anasema hivi: “Kutumia ufundi ambao tulijifunza katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme kuwasaidia ndugu zetu kumetuletea shangwe kubwa sana. Kwa kweli, shukrani ambazo tunapokea kutoka kwa wale ambao tumewasaidia zinagusa moyo sana. Vikundi vingine vya kutoa misaada havijafanikiwa sana katika kazi ya kurekebisha majengo ambayo yaliharibiwa. Tayari Mashahidi wa Yehova wamerekebisha au kujenga upya nyumba zaidi ya 5,300 na Majumba mengi ya Ufalme. Watu wanaona kazi hiyo nao wanapendezwa zaidi na ujumbe wetu.”
14. Unaweza kufanya nini ikiwa unatamani kufuatia huduma ya wakati wote?
14 Je, unaweza kufuatia kusudi la Mungu kwa kuchagua huduma ya wakati wote iwe kazi yako ya maisha? Bila shaka, utapata baraka nyingi ukifanya hivyo. Ikiwa hali zako za sasa hazikuruhusu, labda unaweza kuzibadili. Sali kama Nehemia alivyosali alipotamani kuanza mgawo muhimu: “Ah, tafadhali, Yehova, . . . mpe mafanikio mtumishi wako.” (Nehemia 1:11) Kisha, tenda kupatana na sala yako huku ukimtegemea “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Ili Yehova abariki jitihada zako za kumtumikia kikamili zaidi, ni lazima kwanza utie bidii. Mara tu unapoamua kuanza huduma ya wakati wote, shikamana na uamuzi wako. Kadiri wakati unavyopita ndivyo utakavyopata uzoefu zaidi, na shangwe yako itaongezeka.
Maisha Yenye Kusudi Kwelikweli
15. (a) Tunafaidika jinsi gani tunaposoma masimulizi ya wale ambao wamemtumikia Mungu kwa muda mrefu na tunapozungumza nao? (b) Taja simulizi la maisha ambalo limekutia moyo sana.
15 Unaweza kutazamia kupata matokeo gani ukifuatia kusudi la Mungu? Zungumza na watumishi ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu, hasa wale ambao wamefanya huduma ya wakati wote kwa miaka mingi. Wana maisha yenye kuridhisha na yenye kusudi kwelikweli! (Methali 10:22) Watakwambia kwamba Yehova hajakosa kamwe kuwasaidia kupata vitu wanavyohitaji sana na vitu vingine zaidi hata wanapokuwa katika hali ngumu. (Wafilipi 4:11-13) Tangu mwaka wa 1955 mpaka 1961, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilikuwa na mfululizo wa masimulizi ya maisha ya watu waaminifu. Mfululizo huo ulikuwa na kichwa, “Kufuatia Kusudi Langu Maishani.” Kuanzia wakati huo, mamia ya masimulizi mengine ya maisha yamechapishwa. Kila simulizi linaonyesha roho ya bidii na shangwe ambayo inatukumbusha yale yanayosemwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo ya Mitume. Ukisoma masimulizi hayo yenye kusisimua utachochewa kusema hivi: ‘Hayo ndiyo maisha ninayotaka!’
16. Ni nini kinachofanya maisha ya Mkristo yawe yenye kusudi na furaha?
16 Aaron ambaye alitajwa mwanzoni mwa habari hii, anakumbuka hivi: “Nikiwa Afrika, mara nyingi nilikutana na vijana ambao walikuwa wakitanga-tanga kila mahali nchini wakitafuta maisha yenye kusudi. Wengi wao hawakupata kamwe kusudi lolote. Lakini sisi tulikuwa tukifuatia kusudi la Mungu kwa kueneza habari njema ya Ufalme, na tulifurahia sana maisha mapya na yenye kusudi. Tumejionea wenyewe kwamba kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
17. Kwa nini tunapaswa kufuatia kusudi la Mungu sasa?
17 Namna gani wewe? Unafuatia kusudi gani? Ikiwa huna mradi wowote wa kiroho ulio wazi, utaanza kufuatia mambo mengine. Kwa nini upoteze uhai wako wenye thamani ukifuatia ndoto za mchana za ulimwengu wa Shetani? Hivi karibuni, “dhiki kuu” itakapotokea, utajiri wa kimwili na vyeo vya ulimwengu havitakuwa na maana yoyote. Jambo la maana litakuwa uhusiano wetu pamoja na Yehova. Tutashukuru kama nini kwamba tumemtumikia Mungu na wengine na tumefuatia kikamili kusudi la Mungu katika maisha yetu!—Mathayo 24:21; Ufunuo 7:14, 15.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Imetayarishwa na Mashahidi wa Yehova.
Je, Unaweza Kueleza?
• Yehova anahisi namna gani kuhusu utumishi tunaomtolea?
• Kuona mambo kwa njia inayofaa na kuwa na usawaziko kunatusaidia jinsi gani kumtumikia Mungu na kuwatumikia wengine?
• Tuna nafasi gani za kupanua utumishi wetu?
• Tunaweza kuishi maisha yenye kusudi la kweli sasa kwa kufanya nini?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Tunahitaji usawaziko ili tuendelee kumtumikia Yehova kwa nafsi yetu yote
[Picha katika ukurasa wa 24]
Kuna njia nyingi za kufanya utumishi mtakatifu