Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yehova Ni Fungu Langu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 15
    • Yehova Ni Fungu Langu

      “Mimi ni fungu lako na urithi wako katikati ya wana wa Israeli.”​—HES. 18:20.

      1, 2. (a) Walawi walikuwa katika hali gani kuhusiana na urithi wa nchi? (b) Yehova aliwapa Walawi ahadi gani?

      BAADA ya Waisraeli kuchukua sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi, Yoshua alianza kazi ya kugawa nchi hiyo kwa kura. Alifanya kazi hiyo akishirikiana na Kuhani Mkuu Eleazari pamoja na wakuu wa makabila. (Hes. 34:13-29) Walawi hawakupaswa kupewa urithi wa nchi kama ule ambao yale makabila mengine yalipewa. (Yos. 14:1-5) Kwa nini kabila la Lawi halikuwa na eneo, au fungu, katika ile Nchi ya Ahadi? Je, walisahauliwa?

      2 Jibu linapatikana katika maneno ambayo Yehova aliwaambia Walawi. Ili kukazia kwamba hakuwa amewaacha, Yehova aliwaambia hivi: “Mimi ni fungu lako na urithi wako katikati ya wana wa Israeli.” (Hes. 18:20) Aliwapa ahadi yenye kutia moyo sana: “Mimi ni fungu lako”! Ungehisi namna gani ikiwa Yehova angekwambia hivyo? Huenda mwanzoni ungejiuliza hivi: ‘Ninastahili kweli kuhakikishiwa hivyo na Mweza-Yote?’ Pia, huenda ukajiuliza hivi: ‘Je, Yehova anaweza kweli kuwa fungu la Mkristo yeyote asiye mkamilifu leo?’ Maswali au maulizo hayo yanakuhusu wewe na wapendwa wako. Basi, acheni tuone maana ya maneno hayo ya Mungu. Kufanya hivyo kutatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyoweza kuwa fungu la Wakristo leo. Anaweza hasa kuwa fungu lako, iwe una tumaini la kuishi mbinguni au tumaini la kuishi katika paradiso duniani.

      Yehova Aliwatunza Walawi

      3. Ni nini kilichomfanya Mungu awachukue Walawi kwa ajili ya utumishi wake?

      3 Kabla Yehova hajawapa Waisraeli Sheria, vichwa vya familia walitumikia wakiwa makuhani katika familia zao. Mungu alipowapa Sheria, alichagua watu fulani kutoka katika kabila la Lawi ili watumike daima wakiwa makuhani na wasaidizi. Alifanya hivyo jinsi gani? Mungu alipowaangamiza wazaliwa wa kwanza huko Misri, aliwatakasa wazaliwa wa kwanza wa Israeli, na kuwaweka kando ili wawe wake, wawe mali yake. Kisha Mungu akafanya badiliko hili kubwa: “Nawachukua Walawi . . . mahali pa wazaliwa wote wa kwanza katikati ya wana wa Israeli.” Kwa kuwa hesabu ya watu ilionyesha kwamba wazaliwa wa kwanza wa Israeli walikuwa wengi kuliko Walawi, bei ya fidia au ukombozi ililipwa ili kujazia tofauti hiyo. (Hes. 3:11-13, 41, 46, 47) Hivyo, Walawi wangeweza kutimiza daraka lao la kumtumikia Mungu wa Israeli.

      4, 5. (a) Mungu alimaanisha nini aliposema kwamba alikuwa fungu la Walawi? (b) Mungu aliwatunza Walawi jinsi gani?

      4 Mgawo huo ulimaanisha nini kwa Walawi? Yehova alisema kwamba angekuwa fungu lao kumaanisha kwamba badala ya kupewa urithi wa nchi, walikabidhiwa pendeleo lenye thamani sana la utumishi. Wangepata urithi wa kuwa “ukuhani wa Yehova.” (Yos. 18:7) Mistari mingine inayozunguka andiko la Hesabu 18:20 inaonyesha kwamba jambo hilo halikufanya wawe maskini kimwili. (Soma Hesabu 18:19, 21, 24.) Walawi walipaswa kupewa “kila sehemu ya kumi katika Israeli iwe urithi wao kwa sababu ya utumishi wao.” Wangepokea asilimia 10 ya mazao yote ya Waisraeli na ya wanyama walioongezeka. Kisha Walawi walipaswa kutoa sehemu ya 10 ya vitu walivyopokea kuwa mchango, “ule ulio bora zaidi,” ili kutegemeza ukuhani.a (Hes. 18:25-29) Makuhani walipewa pia “michango yote mitakatifu” ambayo wana wa Israeli walimletea Mungu mahali pake pa Ibada. Hivyo, washiriki wa ukuhani walikuwa na sababu nzuri za kuamini kwamba Yehova angewatunza.

      5 Inaonekana kwamba Sheria ya Musa iliwaagiza Waisraeli watoe sehemu nyingine ya kumi. Familia za Waisraeli zilitumia sehemu hiyo kununua vyakula na vinywaji na pia kujifurahisha wakati wa makusanyiko matakatifu kila mwaka. (Kum. 14:22-27) Hata hivyo, mwishoni mwa kila mwaka wa tatu na wa sita wa mzunguko wa sabato wa miaka saba, sehemu hiyo ya kumi iliwekwa kwenye malango ili kuwasaidia maskini na pia Walawi. Kwa nini Walawi walipewa pia msaada huo? Kwa sababu ‘hawakuwa na fungu wala urithi’ katika Israeli.—Kum. 14:28, 29.

      6. Kwa kuwa kabila la Lawi halikuwa na fungu la nchi katika Israeli, Walawi wangeishi wapi?

      6 Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Walawi hawakugawiwa nchi yoyote, wangeishi wapi?’ Mungu aliwapa mahali pa kuishi. Aliwapa majiji 48 pamoja na viwanja vya malisho vilivyozunguka majiji hayo. Majiji hayo yalitia ndani majiji sita ya makimbilio. (Hes. 35:6-8) Hivyo, Walawi walikuwa na mahali pa kuishi wakati ambapo hawakuwa wakitumika katika patakatifu pa Mungu. Yehova aliwatunza kabisa wale ambao walijitoa wenyewe katika utumishi wake. Ni wazi kwamba Walawi walionyesha kuwa Yehova ni fungu lao kwa kutegemea uwezo na utayari wake wa kuwatunza.

      7. Walawi walihitaji kuwa na nini ili Yehova awe fungu lao?

      7 Sheria haikutaja adhabu yoyote ambayo Mwisraeli angepata ikiwa angekosa kutoa sehemu ya kumi. Watu walipopuuza kutoa sehemu ya kumi, makuhani na Walawi waliumia. Ndivyo ilivyokuwa katika siku za Nehemia. Matokeo yalikuwa kwamba Walawi walilazimika kufanya kazi katika mashamba yao, na kupuuza huduma yao. (Soma Nehemia 13:10.) Ni wazi kwamba Walawi walipata tu mahitaji yao wakati taifa hilo lilipotii Sheria ya Yehova. Zaidi ya hayo, makuhani na Walawi wenyewe walihitaji kuwa na imani katika Yehova na njia yake ya kuwaandalia mahitaji yao.

      Watu Mmoja-Mmoja Ambao Yehova Alikuwa Fungu Lao

      8. Eleza tatizo ambalo Asafu alikuwa nalo.

      8 Kwa ujumla, Yehova angekuwa fungu la kabila lote la Walawi. Hata hivyo, ni vizuri kuona kwamba Walawi wakiwa mtu mmoja-mmoja walitumia maneno “Yehova ni fungu langu” ili kuonyesha kwamba walijitoa kwa Mungu na kumtegemea yeye. (Omb. 3:24) Mlawi mmoja aliyesema hivyo alikuwa mwimbaji na mtungaji wa nyimbo. Tutamwita Asafu, ingawa huenda alikuwa mshiriki wa familia ya Asafu, yule Mlawi ambaye aliongoza waimbaji katika siku za Mfalme Daudi. (1 Nya. 6:31-43) Katika Zaburi ya 73 tunasoma kwamba Asafu (au mmoja wa wazao wake) alishangaa. Aliwaonea wivu watu waovu ambao walikuwa na maisha mazuri na akafikia hatua ya kusema hivi: “Hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia.” Inaonekana kwamba alikosa kuthamini pendeleo lake la utumishi; hakuthamini kwamba Yehova alikuwa fungu lake. Aliteseka kiroho ‘mpaka alipoingia katika patakatifu pakuu pa Mungu.’—Zab. 73:2, 3, 12, 13, 17.

      9, 10. Kwa nini Asafu alisema kwamba Mungu ni ‘fungu lake mpaka wakati usio na kipimo’?

      9 Akiwa katika patakatifu, Asafu alianza kuona mambo kama Mungu alivyoyaona. Labda umewahi kuwa na maoni kama ya Asafu. Labda wakati fulani ulikosa kuthamini kwa kadiri fulani mapendeleo yako ya kiroho na kuanza kukazia fikira vitu vya kimwili ambavyo hukuwa navyo. Lakini ulipojifunza Neno la Mungu na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ulianza kuona mambo kama Yehova anavyoyaona. Asafu alitambua jambo ambalo mwishowe lingewapata waovu. Alifikiria kuhusu hali yake na kutambua kwamba Yehova angeushika mkono wake wa kuume na kumwongoza. Hivyo, Asafu alimwambia Yehova hivi: “Isipokuwa wewe sina mapendezi mengine duniani.” (Zab. 73:23, 25) Kisha akasema kwamba Mungu ni fungu lake. (Soma Zaburi 73:26.) Hata kama ‘mwili na moyo wa mtunga-zaburi huyo ungeshindwa,’ Mungu angekuwa ‘fungu lake mpaka wakati usio na kipimo.’ Mtunga-zaburi huyo alikuwa na hakika kwamba Yehova angemkumbuka akiwa rafiki. Utumishi wake mwaminifu haungesahauliwa. (Mhu. 7:1) Bila shaka, Asafu alitiwa moyo sana na jambo hilo. Aliimba hivi: “Mimi, kumkaribia Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”—Zab. 73:28.

      10 Asafu aliona kwamba Yehova kuwa fungu lake ni jambo la maana zaidi kuliko vitu vya kimwili ambavyo alipewa akiwa Mlawi. Alikazia hasa pendeleo lake la utumishi na uhusiano wake pamoja na Yehova, na urafiki ambao alikuwa amesitawisha pamoja na Aliye Juu Zaidi. (Yak. 2:21-23) Ili kulinda uhusiano huo, mtunga-zaburi huyo alihitaji kuendelea kuwa na imani katika Yehova na kumtegemea. Asafu alipaswa kuwa na uhakika kwamba mwishowe angepata thawabu maishani ikiwa angeishi kulingana na viwango vya Mungu. Unaweza kuwa na uhakika kama huo katika Mweza-Yote.

      11. Ni swali gani ambalo Yeremia aliuliza, na lilijibiwa jinsi gani?

      11 Nabii Yeremia ni Mlawi mwingine aliyemwona Yehova kuwa fungu lake. Acheni tuone alichomaanisha alipotumia maneno hayo. Yeremia aliishi huko Anathothi, jiji la Walawi ambalo lilikuwa karibu na Yerusalemu. (Yer. 1:1) Pindi moja, Yeremia alishangaa na kuuliza: Kwa nini waovu walikuwa wakifanikiwa huku waadilifu wakiteseka? (Yer. 12:1) Baada ya kuona mambo yaliyokuwa yakitokea Yerusalemu na Yuda, alihisi kwamba alipaswa ‘kulalamika’ kuhusu mambo aliyoona. Yeremia alijua kwamba Yehova ni mwadilifu. Swali la nabii Yeremia lilijibiwa kwa hakika kupitia mambo ambayo Yehova alimwongoza nabii huyo kutabiri baadaye kwa uwezo wa roho takatifu na jinsi Yehova alivyoyatimiza. Kulingana na unabii mbalimbali kutoka kwa Mungu, wale ambao walitii mwongozo wa Yehova ‘walipata nafsi yao kama nyara,’ lakini watu waovu waliokuwa matajiri walipuuza onyo na kuangamia.—Yer. 21:9.

      12, 13. (a) Ni nini kilichomchochea Yeremia atangaze hivi: “Yehova ni fungu langu,” na alikuwa na mtazamo gani? (b) Kwa nini makabila yote ya Israeli yalihitaji kusitawisha mtazamo wa kungojea?

      12 Baadaye Yeremia alipoangalia nchi yake iliyobaki ukiwa, alihisi kana kwamba alikuwa akitembea katika giza. Ilikuwa ni kana kwamba Yehova alimfanya ‘aketi mahali penye giza kama watu waliokufa zamani.’ (Omb. 1:1, 16; 3:6) Yeremia alikuwa ameliambia taifa hilo lenye kuasi limrudie Baba yao wa mbinguni, lakini ubaya ulikuwa mwingi hivi kwamba Mungu alilazimika kuruhusu Yerusalemu na Yuda kuangamizwa. Yeremia aliumia alipoona hivyo, hata ingawa kosa halikuwa lake. Alipokuwa akiteseka, nabii huyo alikumbuka rehema za Mungu. Alisema hivi: “Hatujaisha.” Kwa kweli, rehema za Yehova ni mpya kila asubuhi! Ndipo Yeremia alipotangaza hivi: “Yehova ni fungu langu.” Aliendelea kuwa na pendeleo la kumtumikia Yehova akiwa nabii.—Soma Maombolezo 3:22-24.

      13 Kwa miaka 70, Waisraeli hawangekuwa na nchi yao. Ingeachwa ukiwa. (Yer. 25:11) Lakini maneno “Yehova ni fungu langu” yaliyosemwa na Yeremia yalionyesha alikuwa na uhakika kwamba Mungu angewarehemu, na hilo lilimpa sababu ya kuwa na “mtazamo wa kungojea.” Makabila yote ya Israeli yalikuwa yamepoteza urithi wao, hivyo yalihitaji kusitawisha mtazamo kama wa nabii huyo. Yehova peke yake ndiye aliyekuwa tumaini lao. Baada ya miaka 70, watu wa Mungu walirudishwa katika nchi yao na wakapata pendeleo la kumtumikia huko.—2 Nya. 36:20-23.

      Wengine Wangeweza Kumfanya Yehova Kuwa Fungu Lao

      14, 15. Zaidi ya Walawi, ni nani ambaye alimfanya Yehova kuwa fungu lake, na kwa nini?

      14 Asafu na Yeremia walikuwa wa kabila la Lawi, lakini je, ni Walawi peke yao ambao wangekuwa na pendeleo la kumtumikia Yehova? Hapana! Kijana Daudi, ambaye baadaye angekuwa mfalme wa Israeli, alimwita Mungu “fungu langu katika nchi ya walio hai.” (Soma Zaburi 142:1, 5.) Daudi alipotunga zaburi hiyo, hakuwa katika nyumba ya mfalme au hata katika nyumba yoyote. Alikuwa ndani ya pango, akijificha maadui wake. Katika pindi mbili hivi, Daudi alikimbilia katika mapango—pango moja lilikuwa karibu na Adulamu na lingine lilikuwa katika jangwa la En-gedi. Huenda alitunga Zaburi ya 142 akiwa ndani ya moja la mapango hayo.

      15 Ikiwa ndivyo ilivyokuwa, basi Mfalme Sauli ndiye aliyekuwa akimuwinda Daudi, akitafuta kumuua. Daudi alikimbia na kuingia ndani ya pango ambalo halingeweza kufikiwa kwa urahisi. (1 Sam. 22:1, 4) Katika eneo hilo lililojificha, huenda Daudi alihisi kwamba hakuwa na rafiki kando yake ambaye angeweza kumtegemeza kwa kumlinda. (Zab. 142:4) Huo ndio wakati ambao Daudi alimwomba Mungu msaada.

      16, 17. (a) Ni sababu gani zilizomfanya Daudi akate tamaa? (b) Daudi angeweza kumwomba nani msaada?

      16 Kufikia wakati ambapo Daudi alitunga Zaburi ya 142, huenda alipata habari kuhusu jambo lililompata Kuhani Mkuu Ahimeleki, ambaye bila kujua alimsaidia Daudi alipokuwa akimkimbia Sauli. Mfalme Sauli mwenye wivu aliagiza Ahimeleki pamoja na watu wa nyumba yake wauawe. (1 Sam. 22:11, 18, 19) Daudi aliona kwamba ni yeye aliyesababisha vifo vyao. Alihisi ni kana kwamba alimuua kuhani ambaye alikuwa amemsaidia. Kama ungekuwa katika hali ya Daudi, je, ungejiona kuwa na hatia? Daudi alipata mkazo zaidi kwa sababu hakupumzika kwa kuwa Sauli aliendelea kumfuata.

      17 Muda mfupi baadaye nabii Samweli alikufa, ambaye alikuwa amemtia Daudi mafuta ili awe mfalme. (1 Sam. 25:1) Huenda hilo lilimfanya Daudi akate tamaa zaidi. Hata hivyo, Daudi alijua kwamba Yehova ndiye angemsaidia. Daudi hakuwa na pendeleo la utumishi kama la Walawi, lakini alikuwa tayari ametiwa mafuta ili kutimiza utumishi wa aina nyingine, mwishowe angekuwa mfalme wa watu wa Mungu. (1 Sam. 16:1, 13) Kwa hiyo, Daudi alimimina moyo wake mbele za Yehova na kuendelea kufuata mwongozo wa Mungu. Wewe pia unaweza na unapaswa kumfanya Yehova kuwa fungu lako na kimbilio lako unapojikaza katika utumishi wake.

      18. Watu ambao tumezungumzia katika habari hii walionyesha jinsi gani kwamba Yehova alikuwa fungu lao?

      18 Watu ambao tumezungumzia walimfanya Yehova kuwa fungu lao katika maana ya kwamba walipokea mgawo wa kazi katika utumishi wake. Walimtegemea Mungu awatunze walipokuwa wakimtumikia. Walawi na pia Waisraeli wa makabila mengine, kama vile Daudi, wangeweza kumfanya Mungu kuwa fungu lao. Wewe pia unaweza jinsi gani kumfanya Yehova awe fungu lako? Tutazungumzia jambo hilo katika habari inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ukuhani ulivyotegemezwa, ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 684 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 655.

  • Je, Unamfanya Yehova Awe Fungu Lako?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 15
    • Je, Unamfanya Yehova Awe Fungu Lako?

      “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—MT. 6:33.

      1, 2. (a) “Israeli wa Mungu” wanaotajwa katika Wagalatia 6:16 wanafananisha nani? (b) Katika andiko la Mathayo 19:28, ni nani wanaofananishwa na “yale makabila kumi na mawili ya Israeli”?

      UNAPOSOMA jina Israeli katika Biblia, unafikiria nini? Je, unamfikiria Yakobo mwana wa Isaka, ambaye jina lake lilibadilishwa na kuwa Israeli? Au unawafikiria wazao wake, taifa la kale la Israeli? Namna gani kuhusu Israeli wa kiroho? Jina Israeli linapotumiwa kwa njia ya mfano, kwa kawaida linahusu “Israeli wa Mungu,” wale 144,000, ambao wametiwa mafuta kwa roho takatifu ili kuwa wafalme na makuhani mbinguni. (Gal. 6:16; Ufu. 7:4; 21:12) Lakini fikiria jinsi makabila 12 ya Israeli yanavyozungumziwa kwa njia ya pekee katika andiko la Mathayo 19:28.

      2 Yesu alisema hivi: “Katika uumbaji-mpya Mwana wa binadamu atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili, mkiyahukumu yale makabila kumi na mawili ya Israeli.” Katika mstari huo, “yale makabila kumi na mawili ya Israeli” ni wale ambao watahukumiwa na wanafunzi watiwa-mafuta wa Yesu na ambao wanatumaini kupata uzima wa milele katika Paradiso duniani. Watafaidika kutokana na utumishi wa kikuhani wa wale 144,000.

      3, 4. Watiwa-mafuta waaminifu wameweka mfano gani mzuri?

      3 Kama makuhani na Walawi wa zamani, watiwa-mafuta leo wanaona utumishi wao kuwa pendeleo. (Hes. 18:20) Watiwa-mafuta hawatazamii kupewa eneo au mahali fulani duniani kuwa urithi wao. Badala yake, wanatazamia kuwa wafalme na makuhani mbinguni pamoja na Yesu Kristo. Wataendelea kumtumikia Yehova katika mgawo huo, kama inavyoonyeshwa na mambo tunayosoma katika andiko la Ufunuo 4:10, 11 kuhusu watiwa-mafuta wakiwa katika cheo chao mbinguni.—Eze. 44:28.

      4 Wakiwa duniani, watiwa-mafuta wanaishi kwa njia ambayo inaonyesha kwamba Yehova ni fungu lao. Pendeleo lao la kumtumikia Mungu ni la maana sana kwao. Wanaonyesha imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo na wanaendelea kumfuata, na hivyo ‘kufanya mwito na kuchaguliwa kwao kuwe hakika.’ (2 Pet. 1:10) Kila mmoja wao ana hali na uwezo tofauti. Hata hivyo, hawatumii udhaifu wowote walio nao kuwa kisingizio cha kufanya machache tu katika utumishi wa Mungu. Badala yake, wanatanguliza kabisa utumishi wa Mungu, na kufanya yote wanayoweza. Nao wanawawekea mfano mzuri wale ambao wanatumaini kuishi katika paradiso duniani.

      5. Wakristo wote wanaweza kumfanya Yehova kuwa fungu lao jinsi gani, na kwa nini huenda isiwe rahisi kufanya hivyo?

      5 Iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au la kuishi duniani, ni lazima ‘tujikane wenyewe na kuuchukua mti wetu wa mateso na kumfuata Kristo sikuzote.’ (Mt. 16:24) Mamilioni ya watu ambao wanatazamia kuishi katika Paradiso duniani wanamwabudu Mungu na kumfuata Kristo kwa njia hiyo. Hawatosheki kufanya mambo machache tu ikiwa wanaona kwamba wanaweza kutimiza mengi zaidi. Wengi wamechochewa kurahisisha maisha yao na wamekuwa mapainia. Wengine wao wanafanya upainia miezi fulani kila mwaka. Na kuna wengine, ingawa hawawezi kufanya upainia, wanajikaza kabisa katika huduma. Watu hao ni kama Maria aliyejitoa, ambaye alimmiminia Yesu mafuta yenye marashi. Yesu alisema hivi: “Amenifanyia tendo zuri. . . . Alifanya jambo ambalo aliweza.” (Marko 14:6-8) Huenda isiwe rahisi kwetu kufanya yote tunayoweza, kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu ambao unatawaliwa na Shetani. Hata hivyo, tunajikaza wenyewe kabisa na kumtegemea Yehova. Fikiria jinsi tunavyofanya hivyo katika sehemu nne hasa.

      Kuutafuta Kwanza Ufalme wa Mungu

      6. (a) Watu kwa ujumla wanaonyesha jinsi gani kwamba fungu lao liko katika maisha haya tu? (b) Kwa nini ni jambo bora zaidi kuwa na mtazamo kama wa Daudi?

      6 Yesu aliwafundisha wafuasi wake watafute kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu. Watu wa ulimwengu wana mwelekeo wa kutafuta kwanza faida zao binafsi kama “watu wa mfumo huu wa mambo, ambao fungu lao liko katika maisha haya.” (Soma Zaburi 17:1, 13-15.) Watu wengi wanampuuza Muumba wao na kujitoa wenyewe kutafuta maisha ya raha, kuwa na familia, na kuacha urithi. Fungu lao liko katika maisha haya tu. Lakini Daudi alitaka kujifanyia jina zuri mbele za Yehova, kama vile baadaye mwana wake alivyopendekeza watu wote wafanye. (Mhu. 7:1) Kama tu Asafu, Daudi aliona kwamba kuwa Rafiki ya Yehova lilikuwa jambo bora zaidi kuliko kutanguliza faida zake mwenyewe maishani. Alipata shangwe katika kutembea pamoja na Mungu. Leo, Wakristo wengi wametanguliza utendaji wa kiroho badala ya kazi yao ya kimwili.

      7. Ndugu mmoja alipata baraka gani kwa kutanguliza Ufalme?

      7 Mfikirie Jean-Claude, anayeishi katika Jamhuri ya Afrika ya Kati. Ni mzee wa kutaniko aliye na mke na watoto watatu. Katika nchi hiyo, ni vigumu kupata kazi, na watu wengi wanafanya jambo lolote lile ili wasipoteze kazi yao. Siku moja, msimamizi wa kazi alimwambia Jean-Claude aanze kufanya kazi usiku, kuanzia saa kumi na mbili na nusu jioni, siku saba kwa juma. Jean-Claude alimweleza kwamba zaidi ya kuitunza familia yake kimwili, alihitaji pia kutunza hali yao ya kiroho. Pia, alisema kwamba alikuwa na daraka la kulisaidia kutaniko. Msimamizi huyo alimwambia nini? “Ikiwa umefanikiwa kupata kazi, ni lazima usahau mambo mengine yote, kutia ndani mke wako, watoto wako, na matatizo yako. Ni lazima ujitoe kabisa katika kazi yako—usijitoe kwa kitu kingine chochote ila kazi yako. Chagua jambo moja: dini yako au kazi yako.” Wewe ungefanya nini? Jean-Claude alitambua kwamba ikiwa angepoteza kazi yake, Mungu angemtunza. Bado angekuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu, na Yehova angemsaidia kutosheleza mahitaji ya kimwili ya familia yake. Kwa hiyo, alihudhuria mkutano uliofuata wa katikati ya juma. Kisha, akajitayarisha kwenda kazini, lakini hakuwa na hakika kwamba angeendelea kufanya kazi hiyo. Kwa ghafula, alipigiwa simu. Yule msimamizi alikuwa amefutwa kazi, lakini ndugu yetu akaendelea na kazi yake.

      8, 9. Tunaweza kuwaiga makuhani na Walawi jinsi gani katika kumfanya Yehova awe fungu letu?

      8 Watu fulani ambao wamekuwa katika hatari ya kupoteza kazi yao wamejiuliza hivi: ‘Nitatimiza jinsi gani daraka langu la kuiandalia familia yangu mahitaji?’ (1 Tim. 5:8) Iwe umewahi kujikuta katika hali kama hiyo au hapana, inaelekea kutokana na mambo uliyojionea una hakika kwamba wale ambao wanamfanya Mungu kuwa fungu lao na kuthamini sana pendeleo la kumtumikia hawawezi kamwe kukata tamaa. Yesu alipowaambia wanafunzi wake waendelee kutafuta kwanza ufalme, aliwahakikishia hivi: “Nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote,” kama vile chakula, kinywaji, au mavazi.—Mt. 6:33.

      9 Fikiria Walawi, ambao hawakupata urithi wa nchi. Kwa kuwa walihangaikia hasa ibada safi, ili kupata mahitaji yao walihitaji kumtegemea Yehova, ambaye aliwaambia hivi: “Mimi ni fungu lako.” (Hes. 18:20) Ingawa hatutumikii katika hekalu halisi kama makuhani na Walawi walivyofanya, tunaweza kuiga roho yao, tukiwa na uhakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu. Kadiri tunavyozidi kuingia katika siku za mwisho, ndivyo linavyokuwa jambo la maana zaidi kutegemea nguvu za Mungu za kutuandalia mahitaji yetu.—Ufu. 13:17.

      Kuutafuta Kwanza Uadilifu wa Mungu

      10, 11. Watu fulani wamemtegemea Yehova jinsi gani inapohusu kazi ya kimwili? Toa mfano.

      10 Yesu aliwatia moyo pia wanafunzi wake ‘waendelee kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu.’ (Mt. 6:33) Hilo linamaanisha kutanguliza kiwango cha Yehova cha mambo yanayofaa na yasiyofaa badala ya desturi za wanadamu. (Soma Isaya 55:8, 9.) Huenda unakumbuka kwamba zamani, watu fulani walipanda au kuuza tumbaku, waliwafundisha wengine kupigana vitani, au walitengeneza na kuuza silaha za vita. Baada ya kupata ujuzi wa ile kweli, wengi wao waliamua kubadili kazi yao na hivyo kustahili kubatizwa.—Isa. 2:4; 2 Kor. 7:1; Gal. 5:14.

      11 Mfano mmoja ni Andrew. Wakati yeye na mke wake walipojifunza kumhusu Yehova, waliazimia kumtumikia. Andrew aliipenda sana kazi yake lakini akaiacha. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa akifanya kazi katika shirika ambalo liliunga mkono vita na alikuwa ameazimia kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu. Andrew alipoacha kazi hiyo, alikuwa na watoto wawili, na alikuwa na pesa za kutumia kwa miezi michache tu na hakuwa na mshahara wowote. Kwa maoni ya wanadamu, huenda ilionekana kwamba hakuwa na ‘urithi’ wowote. Alitafuta kazi huku akimtegemea Mungu. Yeye na familia yake wanapofikiria wakati huo wanaweza kusema kwa hakika kwamba mkono wa Yehova si mfupi. (Isa. 59:1) Kwa kurahisisha maisha yao, Andrew na mke wake hata wamepata pendeleo la kufanya utumishi wa wakati wote. Andrew anasema hivi: “Nyakati fulani tumehangaika sana kwa sababu ya pesa, nyumba, afya, na kuzeeka. Lakini sikuzote Yehova ametutegemeza. . . . Tunaweza kusema bila shaka yoyote kwamba, kumtumikia Yehova ndilo jambo bora na lenye kuthawabisha zaidi katika maisha ya wanadamu.”a—Mhu. 12:13.

      12. Ni sifa gani inayohitajiwa ili kutanguliza viwango vya Mungu? Toa mifano ya kwenu.

      12 Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mkiwa na imani inayotoshana na mbegu ya haradali, mtauambia mlima huu, ‘Ondoka hapa uende pale,’ nao utaondoka, na hakuna jambo litakalowashinda.” (Mt. 17:20) Je, utatanguliza viwango vya Mungu hata ikiwa utapata matatizo kwa kufanya hivyo? Ikiwa huna uhakika kwamba unaweza kufanya hivyo, zungumza na washiriki wengine wa kutaniko. Bila shaka, utaburudishwa kiroho ukiwasikia wakisimulia mambo waliyojionea maishani.

      Kuthamini Maandalizi ya Kiroho Kutoka kwa Yehova

      13. Tunapojikaza kabisa katika utumishi wa Yehova, tunaweza kutazamia nini kuhusu maandalizi ya kiroho?

      13 Ikiwa unathamini sana pendeleo lako la kumtumikia Yehova, unaweza kuwa na hakika kwamba atatosheleza mahitaji yako ya kimwili na ya kiroho, kama vile tu alivyowatunza Walawi. Mfikirie Daudi. Ingawa alikuwa ndani ya pango, alikuwa na hakika kwamba Mungu angemwandalia mahitaji yake. Sisi pia tunaweza kumtegemea Yehova hata inapoonekana kwamba hakuna njia ya kutokea. Kumbuka kwamba wakati Asafu ‘alipoingia katika patakatifu pakuu pa Mungu,’ ndipo alipoelewa vizuri jambo ambalo lilikuwa likimhangaisha. (Zab. 73:17) Sisi pia, tunahitaji kutafuta msaada kutoka kwa Mungu ambaye ni Chanzo cha utegemezo wetu wa kiroho. Hivyo, tunaonyesha kwamba tunathamini pendeleo letu la kumtumikia Mungu katika hali yoyote ile tunayokabili. Kwa njia hiyo tunamfanya Yehova awe fungu letu.

      14, 15. Tunapaswa kutenda jinsi gani nuru inapoongezeka kuhusu maandiko fulani, na kwa nini?

      14 Unatenda jinsi gani wakati Yehova, ambaye ni Chanzo cha elimu ya kiroho, anapofunua nuru zaidi kuhusu “mambo mazito ya Mungu” yaliyo katika Biblia? (1 Kor. 2:10-13) Mtume Petro alituwekea mfano bora kabisa wakati Yesu alipowaambia hivi wasikilizaji Wake: “Ninyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu wenyewe.” Wanafunzi wengi walielewa maneno hayo kihalisi na kusema hivi: “Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?” Kisha “wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma.” Lakini Petro akasema: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—Yoh. 6:53, 60, 66, 68.

      15 Petro hakuelewa kabisa Yesu alimaanisha nini aliposema kuhusu kula mwili Wake na kunywa damu Yake. Lakini mtume huyo alimtegemea Mungu ili amwelimishe kiroho. Nuru ya kiroho kuhusu jambo fulani inapozidi kuongezeka, je, unajitahidi kuelewa sababu za Kimaandiko za marekebisho hayo? (Met. 4:18) Waberoya wa karne ya kwanza walilipokea neno “kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku.” (Mdo. 17:11) Ukiwaiga utathamini hata zaidi pendeleo lako la kumtumikia Yehova, na kumfanya kuwa fungu lako.

      Kuoa au Kuolewa Katika Bwana Tu

      16. Mungu anaweza kuwa fungu letu jinsi gani inapohusu amri iliyo katika 1 Wakorintho 7:39?

      16 Pia, Wakristo wanahitaji kukumbuka makusudi ya Mungu kuhusu kufuata mwongozo wa Biblia wa kuoa au kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Wengi wameamua kubaki waseja badala ya kupuuza shauri hilo kutoka kwa Mungu. Mungu anawatunza vizuri wale wanaofanya hivyo. Daudi alifanya nini alipohisi upweke na kuona ni kana kwamba hakuwa na mtu wa kumsaidia? Alisema hivi: “Mbele [za Mungu] niliendelea kumwaga hangaiko langu; mbele zake niliendelea kutangaza juu ya taabu yangu mwenyewe, roho yangu ilipozimia ndani yangu.” (Zab. 142:1-3) Huenda nabii Yeremia ambaye alimtumikia Mungu kwa uaminifu kwa makumi ya miaka akiwa mseja alihisi hivyo pia. Unaweza kuchunguza mfano alioweka ambao umezungumziwa katika sura ya 8 ya kitabu Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia.

      17. Dada mmoja mseja anapambana jinsi gani na upweke wa mara kwa mara?

      17 Dada mmoja huko Marekani anasema hivi: “Sijawahi kamwe kuazimia kubaki mseja. Nitaolewa ikiwa nitampata mtu anayefaa. Mama yangu ambaye si mwamini alijaribu kunisadikisha niolewe na mtu yeyote yule ambaye ningempata. Nilimuuliza ikiwa angekubali kulaumiwa ikiwa ndoa yangu ingeharibika. Baada ya muda, aliona kwamba nilikuwa na kazi nzuri, nilikuwa nikijitunza mwenyewe, na nilikuwa na furaha. Akaacha kunisukuma niolewe.” Nyakati nyingine dada huyo anahisi upweke. Anasema hivi: “Wakati huo, ninajitahidi kumtegemea Yehova. Haniachi kamwe.” Ni nini ambacho kimemsaidia kumtegemea Yehova? “Sala inanisaidia kutambua kwamba Mungu ni halisi na kwamba siko peke yangu. Ikiwa Aliye Juu Zaidi katika ulimwengu mzima anasikiliza, je, ninaweza kweli kukosa shangwe na kuhisi siheshimiwi?” Akiwa na uhakika kabisa kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea,” dada huyo anasema hivi: “Ninajitahidi kujitoa kuwasaidia wengine, bila kutazamia kulipwa. Ninapojiuliza, ‘Ninaweza kumsaidia namna gani mtu huyu?’ Ninapata shangwe moyoni.” (Mdo. 20:35) Ndiyo, Yehova ni fungu lake, naye anafurahia pendeleo la kumtumikia.

      18. Yehova anaweza kukufanya jinsi gani uwe fungu lake?

      18 Hata ukipatwa na hali gani, unaweza kumfanya Mungu kuwa fungu lako. Ukifanya hivyo, utahesabiwa kati ya watu wake wenye furaha. (2 Kor. 6:16, 17) Kisha, unaweza kuwa fungu la Yehova, kama ilivyokuwa kwa watu wengine zamani. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:9, 10.) Kama taifa la Israeli lilivyokuwa fungu la Mungu kati ya mataifa, anaweza kukuchagua uwe mali au fungu lake na kukutunza kwa upendo.—Zab. 17:8.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona gazeti Amkeni! la Novemba 2009, ukurasa wa 12-14.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki