-
Kuenea kwa Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za KidiniMnara wa Mlinzi—1997 | Machi 1
-
-
Kuenea kwa Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za Kidini
HARAKATI YA KUFUATA KANUNI ZA MSINGI—miongo michache iliyopita upesi, hiyo ilikuwa harakati ndogo tu katika Uprotestanti. Mambo yamebadilika kama nini! Bruce B. Lawrence, mwelezaji juu ya dini, aliandika kwamba miaka 30 iliyopita, ni wachache ambao wangaliona kwamba mwishoni mwa karne ya 20, harakati ya kufuata kanuni za msingia ingekuwa kichwa cha maana sana na hata cha kupita kiasi cha vyombo vya habari na cha utafiti wa vyuo vikuu.
Hata hivyo, hilo ndilo jambo ambalo limetokea. Ripoti za magazeti ya habari juu ya maandamano ya jeuri mitaani, visa vya uuaji kimakusudi, harakati za kupinga utoaji-mimba, werevu mbalimbali wa kisiasa wa vikundi vya kidini vyenye uvutano juu ya umma, na mioto mikubwa ya hadharani ya kuchomea vitabu vionwavyo kuwa vyenye ukufuru, ni vikumbusha vya daima vya matendo ya washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Jarida la kila juma la habari za fedha Mondo Economico la Kiitalia lilitaarifu kwamba karibu kila mahali harakati ya kufuata kanuni za msingi “inashambulia kisiasa kwa kutumia jina la Mungu.”
Washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi mara nyingi huonyeshwa kuwa wenye kupita kiasi na washupavu, wakitunga njama mbalimbali na kufanya mashambulio ya kiharamia. Watu wanatiwa hofu na kule kuongezeka kwa vikundi vya aina hiyo kama vile Comunione e Liberazione katika Ukatoliki wa Kiroma, Gush Emunim katika Dini ya Kiyahudi, na Muungano wa Kikristo katika Uprotestanti wa Amerika Kaskazini. Kwa nini harakati ya kufuata kanuni za msingi inaenea? Inachochewa na nini? Je, labda ni “kisasi cha Mungu,” kama adokezavyo mwanasoshiolojia Mfaransa Gilles Kepel?
[Maelezo ya Chini]
a Mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi ni mtu ashikamanaye sana na kanuni za msingi za kidini zenye kuhifadhi mambo na desturi za kale. Maana ya “harakati ya kufuata kanuni za msingi” itazungumziwa zaidi kikamili zaidi katika makala ifuatayo.
-
-
Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za Kidini—Hiyo ni Nini?Mnara wa Mlinzi—1997 | Machi 1
-
-
Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za Kidini—Hiyo ni Nini?
HARAKATI ya kufuata kanuni za msingi ilianza wapi? Mwishoni mwa karne iliyopita, wanatheolojia wasioshikamana na desturi za zamani walikuwa wakibadili itikadi zao ili zilingane na uhakiki wa Biblia na nadharia za kisayansi, kama vile mageuzi. Tokeo ni kwamba, uhakika wa watu katika Biblia ulidhoofishwa. Viongozi wa kidini wenye kushikamana na desturi za zamani katika Marekani waliitikia kwa kuanzisha zile walizoita kanuni za msingi za imani.a Mapema katika karne ya 20, walichapisha mazungumzo juu ya kanuni hizo za msingi katika mfululizo wa mabuku wenye kichwa The Fundamentals: A Testimony to the Truth (Kanuni za Msingi: Ushuhuda wa Kweli). Usemi “harakati ya kufuata kanuni za msingi” watokana na kichwa hicho.
Katika nusu ya kwanza ya karne ya 20, harakati ya kufuata kanuni za msingi ilizungumziwa mara kwa mara. Kwa kielelezo, mwaka wa 1925, washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi katika dini walipeleka mahakamani mwalimu wa shule aitwaye John Scopes wa Tennessee, Marekani, katika ile iliyokuja kuitwa kesi ya Scopes. Uhalifu wake ulikuwa nini? Alikuwa akifundisha mageuzi, na hilo lilipingana na sheria ya jimbo. Siku hizo, watu fulani waliamini kwamba harakati ya kufuata kanuni za msingi isingedumu. Mwaka wa 1926, Christian Century, gazeti la Kiprotestanti, lilisema kwamba harakati hiyo ilikuwa “ya kijuujuu tu na si halisi” na “yenye kukosa kabisa sifa za utimizo wenye kujenga au wenye kudumu.” Kadirio hilo lilikosea kama nini!
Tangu miaka ya 1970, harakati ya kufuata kanuni za msingi imekuwa katika habari daima. Profesa Miroslav Volf, wa chuo cha Fuller Theological Seminary, California, Marekani, asema hivi: “Harakati ya kufuata kanuni za msingi za kidini haijadumu tu, bali imesitawi pia.” Leo, maneno “harakati ya kufuata kanuni za msingi za kidini” hutumiwa si kuhusu harakati za Kiprotestanti tu, bali pia kuhusu wale katika dini nyingine, kama vile Ukatoliki, Uislamu, Dini ya Kiyahudi, na Dini ya Hindu.
Itikio kwa Nyakati Zetu
Kwa nini harakati ya kufuata kanuni za msingi yaenea? Wale wanaochunguza harakati hiyo husema kwamba inasababishwa, angalau kwa sehemu, na ugeugeu wa kiadili na wa kidini wa nyakati zetu. Katika miaka ya mapema jamii zilizo nyingi ziliishi katika mazingira yenye uthabiti wa kiadili uliotegemea itikadi za kidesturi. Sasa itikadi hizo zinapingwa au kukataliwa mbali. Watu wengi wenye akili hudai kwamba hakuna Mungu na kwamba mwanadamu yuko peke yake katika ulimwengu wote mzima usiojali. Wanasayansi wengi hufundisha kwamba wanadamu wametokana na mageuzi ya kinasibu, si kutokana na matendo ya Muumba mwenye upendo. Maoni yenye uendekevu yaenea. Ulimwengu unakumbwa na hali ya kupoteza kanuni za kiadili katika sehemu zote za jamii.—2 Timotheo 3:4, 5, 13.
Washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hutamani sana ule uthabiti mbalimbali wa zamani, na baadhi yao hujitahidi kurudisha jumuiya zao na mataifa yao kwenye ile waonayo kuwa misingi ifaayo ya kiadili na ya kimafundisho. Wao hufanya vyovyote wawezavyo kuwalazimisha wengine waishi kulingana na sheria ya kiadili na utaratibu wa itikadi za kimafundisho ulio “sahihi.” Mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi husadiki kwa uthabiti kwamba yeye yuko sahihi na wengine wamekosea. Profesa James Barr, katika kitabu chake Fundamentalism, asema kwamba harakati ya kufuata kanuni za msingi “mara nyingi huonwa kuwa usemi wenye uhasama na wa kudharau, unaodokeza hali ya kushika sana maoni ya kibinafsi, ushupavu, unyimivu wa ujuzi na ugumu.”
Kwa kuwa hakuna yeyote apendaye kuitwa mwenye kushika sana maoni ya kibinafsi, mshupavu, au mgumu, si wote wanaokubaliana juu ya ni nani aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi na ni nani asiye mshiriki wa harakati hiyo. Hata hivyo, kuna mambo fulani yanayoonyesha tabia za harakati ya kufuata kanuni za msingi katika dini.
Kumtambulisha Mshiriki wa Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi
Kwa kawaida harakati ya kufuata kanuni za msingi kidini ni jaribio la kuhifadhi zile zionwazo kuwa desturi au itikadi za kidini za awali za utamaduni fulani na kupinga ile ionwayo kuwa roho ya kilimwengu ya ulimwengu. Hilo si kusema kwamba washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hupinga mambo yote yaliyo ya kisasa. Baadhi yao hutumia njia za uwasiliano za kisasa kwa matokeo sana ili kuendeleza maoni yao. Lakini wanapiga vita dhidi ya kufanywa kilimwengu kwa jamii.b
Baadhi ya washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi wanaazimia si kujihifadhia wenyewe tu muundo wa kidesturi wa mafundisho au wa njia ya maisha bali pia kulazimisha wengine waufuate, wapate kubadili miundo ya kijamii ili ipatane na itikadi za washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Kwa hiyo, Mkatoliki aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi, hatakazia tu upingaji wa utoaji-mimba. Yamkini atawasonga wanasheria wa nchi yake waendeleze sheria zinazokataza utoaji-mimba. Katika Poland, kulingana na gazeti la habari La Repubblica, ili sheria inayopinga utoaji-mimba ikubaliwe, Kanisa Katoliki liliongoza “‘vita’ ambayo katika hiyo lilitumia mamlaka na nguvu zalo zote.” Katika kufanya hivyo, wenye mamlaka wa kanisa walikuwa wakitenda sawa sana na washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Ule Muungano wa Kikristo wa Kiprotestanti katika Marekani hupiga “vita” vya aina hiyohiyo.
Washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hutambulika hasa kwa masadikisho yao ya kidini yenye msingi imara. Hivyo, Mprotestanti aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi atakuwa muungaji-mkono mwenye kusadikishwa wa ufafanuzi wa halisi wa Biblia, yamkini kutia ndani itikadi ya kwamba dunia iliumbwa katika siku sita halisi. Mkatoliki aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hana shaka zozote juu ya ukamilifu wa papa.
Basi, yaeleweka ni kwa nini usemi “harakati ya kufuata kanuni za msingi” hutokeza maoni ya ushupavu usio wenye kukubali sababu na kwa nini wale wasio washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi huhangaika waonapo harakati ya kufuata kanuni za msingi ikienea. Tukiwa mtu mmoja-mmoja, huenda tusikubaliane na washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi na huenda tukafadhaishwa na werevu wao mbalimbali wa kisiasa na matendo yao yenye jeuri ya mara kwa mara. Kwa kweli, washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi wa dini moja huenda wakashtuliwa na matendo ya wale wa dini nyingine! Bado, watu wengi wenye kufikiri wanahangaikia mambo yanayosababisha kuenea huko kwa harakati ya kufuata kanuni za msingi—kule kuongezeka kwa ulegevu wa kiadili, hali ya kupoteza imani, na kule kukatalia mbali hali ya kiroho katika jamii ya kisasa.
Je, harakati ya kufuata kanuni za msingi ndiyo njia pekee ya kuitikia mielekeo hiyo? Ikiwa sivyo, njia nyingine ni ipi?
[Maelezo ya Chini]
a Zile ziitwazo kwa kawaida Hoja Tano za Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi, zilizofasiliwa mwaka wa 1895, zilikuwa “(1) upulizio wa kamili na ukamilifu wa Andiko; (2) uungu wa Yesu Kristo; (3) kuzaliwa kwa Kristo na bikira; (4) ufuniko wa badala wa Kristo juu ya msalaba; (5) ufufuo wa kimwili wa Kristo na kuja kwake kwa pili duniani, kibinafsi na kimwili.”—Studi di teologia (Masomo ya Kitheolojia).
b “Kufanywa kilimwengu kwa kitu” kwamaanisha kukazia mambo ya kilimwengu, badala ya mambo ya kiroho au mambo matakatifu. Mambo ya kilimwengu hayahusiani na dini wala na itikadi za kidini.
-
-
Njia BoraMnara wa Mlinzi—1997 | Machi 1
-
-
Njia Bora
MASHAHIDI WA YEHOVA wanahangaikia mmomonyoko wa hali ya kiroho ulimwenguni na ukosefu wa adili na ugeugeu wa kidini unaoenea katika jamii. Tokeo ni kwamba, nyakati nyingine wao huitwa washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Lakini je, wao ni washiriki wa harakati ya aina hiyo? La. Ingawa wana masadikisho thabiti ya kidini, wao si washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi katika maana ambayo usemi huo umekuja kutumiwa. Wao hawasongi viongozi wa kisiasa ili waendeleze maoni fulani, nao hawafanyi maandamano na vitendo vya jeuri dhidi ya wale ambao hawakubaliani nao. Wamepata njia bora. Wanamwiga Kiongozi wao, Yesu Kristo.
Mashahidi wa Yehova wanasadiki kwamba kuna kweli ya kidini, inayopatikana katika Biblia. (Yohana 8:32; 17:17) Lakini Biblia hufundisha Wakristo wawe wenye fadhili, wema, wapole, na wenye kukubali sababu—sifa zisizoruhusu ushupavu. (Wagalatia 5:22, 23; Wafilipi 4:5) Katika kitabu cha Biblia cha Yakobo, Wakristo wanatiwa moyo kusitawisha “hekima ya kutoka juu,” inayofafanuliwa kuwa ‘kwanza kabisa safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema.’ Yakobo aliongeza hivi: “Tunda la uadilifu hupandwa mbegu yalo chini ya hali zenye amani kwa ajili ya wale wanaofanya amani.”—Yakobo 3:17, 18.
Mashahidi wa Yehova wanakumbuka kwamba Yesu alihangaikia sana ile kweli. Alimwambia Pontio Pilato hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Ingawa alikuwa mteteaji hodari wa ile kweli, hakujaribu kulazimisha wengine wafuate masadikisho yake. Badala ya hivyo, alivuta akili na mioyo yao. Alijua ya kwamba Babaye wa kimbingu, aliye Mungu “mwema, [na] mwenye adili,” angeamua jinsi ya kuondolea mbali mambo yasiyo ya kweli na udhalimu kutoka usoni pa dunia na wakati wa kufanya hivyo. (Zaburi 25:8) Kwa sababu hiyo, hakujaribu kuwanyamazisha wale ambao hawakukubaliana naye. Kinyume cha hilo, ni viongozi wa kidini wenye imani ya kidesturi wa siku yake waliojaribu kumnyamazisha Yesu.—Yohana 19:5, 6.
Mashahidi wa Yehova wana masadikisho thabiti juu ya mafundisho ya kidini, nao wanadhihirisha kanuni imara kwa habari ya maadili. Sawa na mtume Paulo, wanasadiki kwamba kuna “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja,” tu. (Waefeso 4:5) Wana habari pia juu ya maneno haya ya Yesu: “Lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Hata hivyo, hawajaribu kuwalazimisha wengine wafuate itikadi zao. Badala ya hivyo, wanamwiga Paulo na ‘kuwaomba’ wote wanaotamani ‘wawe wenye kupatanishwa na Mungu.’ (2 Wakorintho 5:20) Hiyo ndiyo njia bora. Ndiyo njia ya Mungu.
Harakati ya kufuata kanuni za msingi katika dini ni tofauti sana, kulingana na jinsi ambavyo usemi huo hutumiwa leo. Washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hutumia mbinu nyingi—kutia ndani jeuri—ili kulazimisha jamii ifuate kanuni zao. Katika kufanya hivyo, wanakuwa sehemu muhimu ya mfumo wa kisiasa. Lakini, Yesu alisema kwamba wafuasi wake hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:16; Yakobo 4:4) Kwa kupatana na maneno hayo, Mashahidi wa Yehova hudumisha hali ya kutokuwamo kabisa katika ubishi mbalimbali wa kisiasa. Na, sawa na vile gazeti la habari la Kiitalia Fuoripagina lilivyokiri, “hawamlazimishi mtu yeyote afuate jambo lolote lile; kila mtu yuko huru kukubali au kukataa yale wasemayo.” Tokeo ni nini? Ujumbe wa Biblia wenye amani wa Mashahidi huvuta watu wa aina zote, hata wale ambao wakati mmoja walikuwa washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi.—Isaya 2:2, 3.
Ulimwengu Wenye Kanuni Imara
Mashahidi hutambua kwamba wanadamu hawawezi kusuluhisha matatizo yanayowahangaisha washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Huwezi kumlazimisha mtu amwamini Mungu au akubali itikadi zako binafsi. Kuamini kwamba jambo hilo lawezekana kuliongoza kwenye baadhi ya mambo yenye kuchukiza sana katika historia, kama zile Krusedi, yale Mabaraza ya Kuhukumu Wazushi ya enzi za kati, na kule “kugeuzwa imani” kwa Wahindi wa Amerika. Hata hivyo, ikiwa una itibari katika Mungu, utakuwa tayari kumwacha ashughulikie mambo.
Kulingana na Biblia, Mungu amewekea mpaka ule wakati ambao awaruhusu wanadamu wavunje sheria zake na hivyo kusababisha kuteseka na umivu. Wakati huo karibu umeisha. Tayari, Yesu anatawala akiwa Mfalme katika Ufalme wa Mungu wa kimbingu, na upesi Ufalme huo utatenda ili kuondoa serikali za kibinadamu na kutwaa uongozi wa kila siku juu ya wanadamu. (Mathayo 24:3-14; Ufunuo 11:15, 18) Tokeo litakuwa paradiso ya ulimwenguni pote ambamo amani na uadilifu utakuwa kwa wingi. Wakati huo hakutakuwa na ugeugeu juu ya jinsi Mungu wa kweli apasavyo kuabudiwa. “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Kanuni za milele kama vile fadhili-upendo, kweli, haki, na wema zitashinda kwa faida ya wanadamu watiifu wote.
Akitazamia wakati huo, mtunga-zaburi asema hivi katika njia ya kishairi: “Fadhili na kweli zimekutana, haki na amani zimehusiana. Kweli imechipuka katika nchi, haki imechungulia kutoka mbinguni. Naam, BWANA atatoa kilicho chema, na nchi yetu itatoa mazao yake. Haki itakwenda mbele zake, nayo itazifanya hatua zake kuwa njia.”—Zaburi 85:10-13.
Ingawa hatuwezi kuubadili ulimwengu, sisi tukiwa mtu mmoja-mmoja twaweza kusitawisha kanuni za kimungu hata leo. Hivyo, twaweza kujaribu kuwa aina ya watu ambao Mungu atataka wawe waabudu wake katika ulimwengu huo mpya. Ndipo tutakapokuwa miongoni mwa wale wasikivu wanaorejezewa na mtunga-zaburi hivi: “Wenye upole [“wasikivu,” NW] watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Mungu hutegemeza na kuwabariki wale wafanyao mapenzi yake, naye aahidi mambo ya ajabu kwa wakati ujao wao. Mtume Yohana alisema hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17.
-