-
Uadilifu Wachipuka Katika SayuniUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Wale wa mwisho wa “miti” hiyo yenye fahari wamesitawi katika miaka ya tangu 1919, wakati Yehova alipowahuisha mabaki wa Israeli wa Mungu kutoka kwenye hali yao ya kutotenda kwa muda. Kwa kuwapa maji tele ya kiroho, inaweza kusemwa kwamba Yehova ametokeza msitu wa miti ya haki, yenye kuzaa matunda.—Isaya 27:6.
14, 15. Waabudu wa Yehova waliofunguliwa walianza miradi gani kuanzia mwaka wa (a) 537 K.W.K.? (b) 33 W.K.? (c) 1919?
14 Akikazia kazi ya “miti” hii, Isaya anaendelea kusema hivi: “Nao watajenga mahali pa kale palipoharibiwa, watapainua mahali palipokuwa ukiwa zamani, watatengeneza miji iliyoharibiwa, mahali palipoachwa kizazi baada ya kizazi.” (Isaya 61:4)
-
-
Uadilifu Wachipuka Katika SayuniUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Vivyo hivyo, kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, Yesu Kristo alisababisha mabaki ya ndugu zake watiwa-mafuta wajenge upya “mahali palipoachwa kizazi baada ya kizazi.” Kwa muda wa karne nyingi, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walikuwa wameshindwa kuwapa watu ujuzi wa Yehova, wakawapa mapokeo ya kibinadamu na mafundisho yasiyo ya Kimaandiko. Wakristo watiwa-mafuta walisafisha makutaniko yao kwa kuondoa mazoea yenye madoa ya dini ya uwongo ili kazi ya kurudisha ibada ya kweli isonge mbele. Halafu wakaanza shughuli ambayo ingekuja kuwa kubwa kuliko shughuli zote za kutoa ushahidi ulimwenguni.—Marko 13:10.
16. Ni nani wamekuwa wakiwasaidia Wakristo watiwa-mafuta katika kazi yao ya kurudisha ibada safi, na wamekabidhiwa majukumu yapi?
16 Huo ulikuwa utume mkubwa sana. Wale mabaki wa Israeli wa Mungu walio wachache kwa ulinganisho wangetimizaje jukumu hilo? Yehova alimpulizia Isaya kutangaza hivi: “Wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu.” (Isaya 61:5) Kwa njia ya mfano, wageni hao na watu walio wa kabila nyingine wamekuwa “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Yesu.a (Ufunuo 7:9; Yohana 10:11, 16) Wao hawatiwi mafuta kwa roho takatifu kupata urithi wa kimbingu. Bali, wana tumaini la kupata uhai wa milele katika dunia-paradiso. (Ufunuo 21:3, 4) Na bado, wanampenda Yehova na wamekabidhiwa wajibu wa kiroho wa kufanya uchungaji, ukulima, na utunzaji wa mizabibu. Utendaji huo si kazi za hali ya chini. Chini ya mwelekezo wa mabaki wa Israeli wa Mungu, wafanyakazi hawa husaidia kuchunga, kulea, na kuvuna watu.—Luka 10:2; Matendo 20:28; 1 Petro 5:2; Ufunuo 14:15, 16.
17. (a) Washirika wa Israeli wa Mungu wataitwaje? (b) Ni dhabihu gani moja tu inayohitajiwa ili kuwe na msamaha wa dhambi?
17 Namna gani juu ya Israeli wa Mungu? Yehova anawaambia hivi, kupitia Isaya: “Bali ninyi mtaitwa makuhani wa BWANA; watu watawaiteni wahudumu wa Mungu wetu; mtakula utajiri wa mataifa, na kujisifia utukufu wao.” (Isaya 61:6) Katika Israeli ya kale, Yehova alifanya uandalizi ili ukuhani wa Kilawi utoe dhabihu kwa niaba ya makuhani wenyewe na Waisraeli wenzao. Hata hivyo, mwaka wa 33 W.K., Yehova alikoma kutumia ukuhani wa Kilawi na kuanzisha mpango mzuri zaidi. Aliukubali uhai mkamilifu wa Yesu kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi za wanadamu. Tangu wakati huo, hakuna dhabihu nyingine yoyote ambayo imehitajiwa. Dhabihu ya Yesu ina nguvu za kutumika daima dawamu.—Yohana 14:6; Wakolosai 2:13, 14; Waebrania 9:11-14, 24.
18. Israeli wa Mungu wanakuwa ukuhani wa aina gani, na wana utume gani?
18 Basi, washirika wa Israeli wa Mungu ni ‘makuhani wa Yehova’ jinsi gani? Akiwaandikia Wakristo wenzake watiwa-mafuta, mtume Petro alisema hivi: “Nyinyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu kwa ajili ya miliki ya pekee, kwamba mpate kutangaza kotekote sifa bora kabisa’ za yeye aliyewaita nyinyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Petro 2:9) Kwa hiyo, wakiwa kikundi, Wakristo watiwa-mafuta wanakuwa ukuhani wenye utume hususa: kuyaambia mataifa juu ya utukufu wa Yehova. Wanapaswa kuwa mashahidi wake. (Isaya 43:10-12) Muda wote wa siku za mwisho, Wakristo watiwa-mafuta wameutimiza utume huo muhimu kwa uaminifu. Matokeo ni kwamba, sasa mamilioni ya watu wanashirikiana nao katika kazi ya kutoa ushahidi juu ya Ufalme wa Yehova.
19. Wakristo watiwa-mafuta watapendelewa kufanya utumishi gani?
19 Zaidi ya hilo, washirika wa Israeli wa Mungu wana tazamio la kutumikia wakiwa makuhani kwa njia nyingine. Wakiisha kufa, wanafufuliwa mbinguni wakiwa roho wasioweza kufa. Licha ya kutumikia wakiwa watawala pamoja na Yesu katika Ufalme wake huko, wanatumikia pia wakiwa makuhani wa Mungu. (Ufunuo 5:10; 20:6) Katika hali hiyo, watapendelewa kutumia faida za dhabihu ya fidia ya Yesu kuelekea wanadamu waaminifu duniani. Katika njozi ya mtume Yohana iliyoandikwa katika Ufunuo sura ya 22, wanatajwa tena kuwa “miti.” “Miti” yote 144,000 inaonwa ikiwa mbinguni, ikitokeza ‘mazao kumi na mawili ya matunda, ikitoa matunda yake kila mwezi. Na majani ya hiyo miti yalikuwa ya kuponya mataifa.’ (Ufunuo 22:1, 2) Lo, huo ni utumishi wa kikuhani ulio mzuri kama nini!
Aibu na Fedheha, Kisha Furaha
20. Ijapokuwa kuna upinzani, ni baraka gani ambayo ukuhani wa kifalme unaingojea?
20 Tangu 1914, wakati mwaka wa Yehova wa nia njema ulipoanza, ule ukuhani wa kifalme umekuwa ukipingwa-pingwa tu na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. (Ufunuo 12:17) Hata hivyo, hatimaye jitihada zote za kukomesha kuhubiriwa kwa habari njema zimeshindwa kabisa kufanikiwa. Unabii wa Isaya ulitabiri hilo, ukisema hivi: “Badala ya aibu yenu mtapata maradufu, na badala ya fedheha wataifurahia sehemu yao; basi katika nchi yao watamiliki maradufu; furaha yao itakuwa ya milele.”—Isaya 61:7.
21. Wakristo watiwa-mafuta walikujaje kufurahia baraka maradufu?
21 Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, mabaki watiwa-mafuta waliaibishwa na kutiwa fedheha na Jumuiya ya Wakristo yenye utukuzo wa taifa. Makasisi walikuwa miongoni mwa wale waliowashtaki ndugu wanane waaminifu wa makao makuu jijini Brookyln kwa kuwasingizia eti ni wachochezi waliopinga serikali. Ndugu hao walitiwa gerezani bila haki kwa muda wa miezi tisa. Mwishowe, katika Machi ya mwaka wa 1919, waliwekwa huru, na baadaye mashtaka yao yote yakaondolewa. Hivyo, njama ya wapinzani ya kukomesha kazi ya kuhubiri ikawarudia wao wenyewe. Badala ya kuwaacha waabudu wake waaibishwe daima, Yehova aliwakomboa, akawarudisha kwenye makao yao ya kiroho, yaani “nchi yao.” Wakiwa humo, walipokea baraka maradufu. Mateso yao yakawa si kitu kwa kulinganishwa na baraka tele za Yehova. Hakika walikuwa na sababu ya kupaaza sauti ya shangwe!
22, 23. Wakristo watiwa-mafuta wamemwigaje Yehova, naye amewathawabishaje?
22 Maneno ya Yehova yanayofuata yana sababu nyingine ya kuwafanya Wakristo leo washangilie: “Mimi, BWANA, naipenda hukumu ya haki, nauchukia wivi na uovu; nami nitawalipa malipo katika kweli, nitaagana nao agano la milele.” (Isaya 61:8) Kupitia funzo lao la Biblia, mabaki watiwa-mafuta walijifunza kupenda haki na kuchukia uovu. (Mithali 6:12-19; 11:20) Walijifunza ‘kufua panga zao ziwe majembe,’ wakabaki bila kuwamo katika vita vya wanadamu na katika misukosuko ya kisiasa. (Isaya 2:4) Pia waliacha mazoea ya kumvunjia Mungu heshima, kama vile uchongezi, uzinzi, wivi, na ulevi.—Wagalatia 5:19-21.
23 Kwa sababu Wakristo watiwa-mafuta wanapenda haki kama Muumba wao, Yehova amewapa ‘malipo yao katika kweli.’ Mojawapo ya “malipo” ya jinsi hiyo ni agano la kudumu kwa wakati usiojulikana—lile agano jipya—ambalo Yesu aliwatangazia wafuasi wake usiku uliotangulia kufa kwake. Agano hilo ndilo lililoweka msingi wa kuwa kwao taifa la kiroho, watu wa pekee wa Mungu. (Yeremia 31:31-34; Luka 22:20) Chini ya agano hilo, Yehova atatumia faida zote za dhabihu ya fidia ya Yesu, kutia na msamaha wa dhambi kwa ajili ya watiwa-mafuta na wanadamu wengine wote waaminifu.
Kufurahia Sana Baraka za Yehova
24. “Kizazi” kinachotoka katika mataifa na kubarikiwa ni akina nani, nao wamekuwaje “kizazi”?
24 Wengine miongoni mwa mataifa wametambua kwamba baraka ya Yehova iko juu ya watu wake. Hiyo ilitabiriwa na ahadi hii ya Yehova: “Kizazi chao kitajulikana katika mataifa, na uzao wao katika kabila za watu; wote wawaonao watakiri ya kuwa wao ni kizazi kilichobarikiwa na BWANA.” (Isaya 61:9) Washirika wa Israeli wa Mungu, yaani Wakristo watiwa-mafuta, wamekuwa watendaji miongoni mwa mataifa wakati wa mwaka wa Yehova wa nia njema. Leo, mamilioni ya watu wameikubali huduma ya hao watiwa-mafuta. Kwa kushirikiana karibu-karibu na Israeli wa Mungu, wale wanaotoka katika mataifa wana pendeleo la kuwa ‘kizazi kilichobarikiwa na Yehova.’ Hali yao ya furaha inaonekana na wanadamu wote.
25, 26. Wakristo wote wanaonyeshaje maoni yale yale yanayotajwa katika Isaya 61:10?
25 Wakristo wote, watiwa-mafuta na kondoo wengine, wanatazamia kumsifu Yehova milele hata milele. Wanakubaliana kwa moyo wote na nabii Isaya, anayesema hivi kwa kupuliziwa: “Mimi nitachachawa katika Yehova bila kukosa. Nafsi yangu itakuwa na shangwe katika Mungu wangu. Kwa maana yeye amenivika mavazi ya wokovu; amenizungushia joho la uadilifu, kama bwana-arusi ambaye, kwa njia ya kikuhani, huvaa vazi la kichwani, na kama bibi-arusi anayejipamba kwa vitu vyenye mapambo.”—Isaya 61:10, “NW.”
26 Wakiwa wamevaa “joho la uadilifu,” Wakristo watiwa-mafuta wamepiga moyo konde kubaki wakiwa wenye utakato na usafi machoni pa Yehova. (2 Wakorintho 11:1, 2) Wakiisha kutangazwa na Yehova kuwa waadilifu kwa kusudi la kurithi uhai wa kimbingu, hawatayarudia kamwe makao yenye ukiwa ya Babiloni Mkubwa, ambaye wamekombolewa kutoka kwake. (Waroma 5:9; 8:30) Kwao, yale mavazi ya wokovu ni ya thamani sana. Vivyo hivyo waandamani wao ambao ni kondoo wengine wamepiga moyo konde kufuata viwango vya juu vya ibada safi ya Yehova Mungu. Wakiisha ‘kufua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo,’ wanatangazwa kuwa waadilifu na wataiokoka “dhiki kubwa.” (Ufunuo 7:14; Yakobo 2:23, 25) Hadi wakati huo, wanawaiga waandamani wao watiwa-mafuta kwa kuepuka kuchafuliwa na Babiloni Mkubwa.
27. (a) Ni ‘uoteshaji’ gani wenye kutazamisha utakaokuwako wakati wa Utawala wa Milenia? (b) Tayari haki inaoteshwaje miongoni mwa jamii ya wanadamu?
27 Leo waabudu wa Yehova wanafurahia kuwa katika paradiso ya kiroho. Karibuni watafurahia Paradiso halisi pia. Kwa mioyo yetu yote, tunautazamia wakati huo unaoelezwa dhahiri katika maneno ya kumalizia ya Isaya sura ya 61: “Kama nchi itoavyo machipuko yake, na kama bustani ioteshavyo vitu vilivyopandwa ndani yake; ndivyo Bwana MUNGU atakavyootesha haki na sifa mbele ya mataifa yote.” (Isaya 61:11) Wakati wa Milenia ya Kristo, dunia ‘itaoteshwa haki.’ Wanadamu watapaaza sauti kwa shangwe, na haki itapanuka hadi miisho ya dunia. (Isaya 26:9) Hata hivyo, si lazima tuingoje siku hiyo tukufu ndipo tutoe sifa mbele ya mataifa yote. Tayari haki inaoteshwa miongoni mwa mamilioni ya watu wanaompa utukufu Mungu wa mbinguni na kuzitangaza habari njema juu ya Ufalme wake. Hata sasa imani na tumaini letu zinatupa kila sababu ya kufurahia baraka za Mungu wetu.
-