-
Ujumbe Wenye Tumaini kwa Mateka Walioshuka MoyoUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 239]
Yesu alijithibitisha kuwa “kiongozi na jemadari” kwa kabila za watu
-
-
Ujumbe Wenye Tumaini kwa Mateka Walioshuka MoyoUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Sura Ya Kumi Na Sita
Ujumbe Wenye Tumaini kwa Mateka Walioshuka Moyo
1. Eleza jinsi hali ya wahamishwa Wayahudi ilivyokuwa huko Babiloni.
GIZA la huzuni lilikuwa limeingia katika historia ya Yuda. Watu wa agano la Mungu walikuwa wameng’olewa katika nchi yao na sasa walikuwa wakiteseka utekwani Babiloni. Ni kweli kwamba walipewa uhuru wa kiasi fulani ili kuendeleza shughuli zao za kila siku. (Yeremia 29:4-7) Wengine walijifunza ufundi wa mambo mbalimbali na wengine wakafanya biashara.a (Nehemia 3:8, 31, 32) Hata hivyo, maisha ya mateka Wayahudi hayakuwa rahisi. Walikuwa utumwani kimwili na kiroho. Acheni tuone ilikuwaje.
2, 3. Uhamisho ulikuwa na matokeo gani juu ya ibada ambayo Wayahudi walimtolea Yehova?
2 Wakati majeshi ya Babiloni yalipoangamiza Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., yaliipiga ibada ya kweli pigo kali, licha ya kufanya taifa hilo ukiwa. Yalisomba vyombo vyote vya hekalu la Yehova na kuliangamiza, yakauharibu kabisa mpangilio wa ukuhani kwa kuteka baadhi ya watu wa kabila la Lawi na kuua wengine. Bila nyumba ya ibada, bila madhabahu, na bila mpangilio mzuri wa ukuhani, haikuwezekana Wayahudi wamtolee Mungu wa kweli dhabihu kwa njia iliyoagizwa na Sheria.
3 Bado Wayahudi waaminifu wangeweza kudumisha utambulisho wao wa kidini kwa kufuata tohara na kufuata Sheria kwa kadiri ilivyowezekana. Kwa mfano, wangeweza kuepuka vyakula vilivyokatazwa na pia kuishika Sabato. Lakini kwa kufanya hivyo, wangeweza kudhihakiwa na watekaji wao kwa maana Wababiloni waliziona desturi za kidini za Wayahudi kuwa upumbavu. Kuonyesha kwamba wahamishwa hao walishuka moyo, maneno ya mtunga-zaburi yanasema hivi: “Kando ya mito ya Babeli ndiko tulikoketi, tukalia tulipoikumbuka Sayuni. Katika miti iliyo katikati yake tulivitundika vinubi vyetu. Maana huko waliotuchukua mateka walitaka tuwaimbie; na waliotuonea walitaka furaha; tuimbieni baadhi ya nyimbo za Sayuni.”—Zaburi 137:1-3.
4. Kwa nini ingekuwa kazi bure ikiwa Wayahudi wangetegemea mataifa mengine ili kupata ukombozi, lakini wangeweza kugeukia nani awasaidie?
4 Basi, mateka Wayahudi wangeweza kupata faraja kwa kugeukia nani? Wokovu wao ungetoka wapi? Ni wazi haungetoka kwa mataifa yaliyowazunguka! Mataifa hayo yote yalikuwa hoi mbele ya majeshi ya Babiloni, na mengi yaliwachukia Wayahudi. Hata hivyo kulikuwa na tumaini. Yehova, ambaye walikuwa wamemwasi wakiwa watu huru, aliwakaribisha kwa uchangamfu ingawa walikuwa uhamishoni.
“Njoni Majini”
5. Maneno “njoni majini” yana maana gani?
5 Yehova anamtumia Isaya kutoa unabii ili kuwaambia hivi mateka Wayahudi walioko Babiloni: “Haya, kila aonaye kiu, njoni majini, naye asiye na fedha; njoni, nunueni mle; naam, njoni, nunueni divai na maziwa, bila fedha na bila thamani.” (Isaya 55:1) Maneno hayo yana semi nyingi za ufananisho. Kwa mfano, fikiria mwaliko huu: “Njoni majini.” Bila maji, haiwezekani kuwa hai. Sisi wanadamu tukikosa maji, tunaweza kuishi juma moja hivi tu. Hivyo, inafaa kwamba Yehova anatumia maji kama mfano ili kuonyesha maneno yake yatakuwa na matokeo gani juu ya mateka Wayahudi. Ujumbe wake utawaburudisha, kama kinywaji baridi wakati wa joto kali la mchana. Utawafanya waache kushuka moyo na kuzima kiu yao ya kutamani ukweli na uadilifu. Tena utawajaza tumaini la kuja kuwekwa huru kutoka utekwani. Hata hivyo, ili hao wahamishwa Wayahudi wapate faida, ni lazima wanywe ujumbe wa Mungu kama maji, wausikilize, na kutenda vile unavyosema.
6. Wayahudi watapataje faida wakinunua “divai na maziwa”?
6 Vilevile, Yehova anawatolea “divai na maziwa.” Maziwa hufanya watoto wapate nguvu na kukua. Vivyo hivyo, maneno ya Yehova yatawatia watu wake nguvu za kiroho na kuwawezesha kuimarisha uhusiano wao naye. Namna gani divai? Mara nyingi divai hutumiwa nyakati za sherehe. Katika Biblia, inahusianishwa na ufanisi na shangwe. (Zaburi 104:15) Kwa kuwaambia watu wake ‘wanunue divai,’ Yehova anawapa uhakikisho kwamba ‘watafurahi kabisa,’ wakiirudia ibada ya kweli kwa moyo wote.—Kumbukumbu la Torati 16:15; Zaburi 19:8; Mithali 10:22.
7. Kwa nini huruma ya Yehova kuwaelekea wahamishwa inastahili kusifiwa, nayo inatufundisha nini juu yake?
7 Lo, Yehova ni mwenye rehema kama nini kwa kuwatolea Wayahudi wahamishwa burudiko hilo la kiroho! Huruma yake inastahili kusifiwa hata zaidi tunapokumbuka kwamba Wayahudi wamekuwa wapotovu na waasi. Si kwamba wanastahili kibali cha Yehova, hapana. Hata hivyo, mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi karne nyingi mapema: “BWANA amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. Yeye hatateta sikuzote, wala hatashika hasira yake milele.” (Zaburi 103:8, 9) Yehova havunji kamwe uhusiano na watu wake, bali ndiye anayechukua hatua ya kwanza ya upatanisho. Kwa kweli, yeye ni Mungu ambaye “hufurahia rehema.”—Mika 7:18.
Tumaini Lisilofaa
8. Wayahudi wengi wameweka tumaini lao wapi, ijapokuwa wamepewa onyo gani?
8 Kufikia sasa, Wayahudi wengi hawajamtumainia Yehova kabisa ili wapate wokovu. Kwa mfano, kabla ya Yerusalemu kuanguka, watawala wake walitegemea mataifa yenye nguvu yawaunge mkono, wakawa ni kama wanafanya ukahaba na Misri na Babiloni. (Ezekieli 16:26-29; 23:14) Yeremia alikuwa na sababu nzuri ya kuwaonya hivi: “Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake na moyoni mwake amemwacha BWANA.” (Yeremia 17:5) Lakini watu wa Mungu walifanya vivyo hivyo!
9. Huenda ikawa Wayahudi wengi ‘wanatoa fedha kwa ajili ya kitu ambacho si chakula’ jinsi gani?
9 Sasa wamekuwa watumwa wa mojawapo la mataifa waliyokuwa wameyatumainia. Je, wamepata somo? Huenda ikawa wengi hawajapata, kwa maana Yehova anauliza hivi: “Kwani kutoa fedha kwa ajili ya kitu ambacho si chakula? Na mapato yenu kwa kitu kisichoshibisha?” (Isaya 55:2a) Ikiwa Wayahudi mateka wanatumainia mtu mwingine yeyote tofauti na Yehova, ‘wanatoa fedha kwa ajili ya kitu ambacho si chakula.’ Hakika hawatafunguliwa watoke Babiloni kwa sababu desturi ya huko hairuhusu mateka warudi nyumbani kwao. Kwa kweli, Babiloni haiwezi kamwe kuwafaidi Wayahudi wahamishwa kupitia utawala wake wa mabavu, biashara, na ibada ya uongo.
10. (a) Ikiwa Wayahudi wahamishwa watamsikiliza Yehova, yeye atawathawabishaje? (b) Ni agano gani ambalo Yehova alikuwa amefanya pamoja na Daudi?
10 Yehova anawasihi sana watu wake hivi: “Nisikilizeni mimi kwa makini, nanyi mtakula vilivyo bora, na kufurahia vinono. ‘Tegeni sikio enyi watu wangu, mje kwangu; nisikilizeni, ili mpate kuishi. Nami nitafanya nanyi agano la milele; nitawapeni fadhili nilizomwaminisha Daudi.’” (Isaya 55:2b, 3, “BHN”) Tumaini pekee kwa watu hawa wasiolishwa vizuri kiroho ni Yehova, ambaye sasa anamtumia Isaya kuongea nao kupitia unabii. Uhai wao wenyewe unategemea kusikiliza ujumbe wa Mungu, kwani anasema kwamba wakifanya hivyo, ‘wataishi.’ Ingawa hivyo, “agano la milele” ambalo Yehova atafanya na wale wanaomtii ni nini? Agano hilo linahusu “fadhili” za upendo alizomtendea Daudi. Karne kadhaa mapema, Yehova alimwahidi Daudi kwamba kiti chake cha ufalme ‘kingethibitishwa milele.’ (2 Samweli 7:16) Kwa hiyo, “agano la milele” linalotajwa hapa linahusu utawala.
Mrithi wa Kudumu wa Ufalme wa Milele
11. Kwa nini huenda wahamishwa walioko Babiloni wakaona kwamba ile ahadi ambayo Mungu alimpa Daudi ni kama dhana tupu?
11 Ni kweli kwamba huenda hao wahamishwa Wayahudi wakaona ni vigumu sana utawala upite katika ukoo wa Daudi. Ala, si wamepoteza nchi yao na hata wakaacha kuwa taifa! Lakini ni kwa muda tu. Yehova hajasahau agano lake na Daudi. Kusudi la Mungu kuhusu Ufalme wa milele katika ukoo wa Daudi litafanikiwa, hata kama linaonekana kuwa jambo gumu sana machoni pa wanadamu. Lakini vipi na lini? Mwaka wa 537 K.W.K., Yehova anawafungua watu wake kutoka utekwani Babiloni na kuwarudisha kwenye nchi yao. Je, hiyo inafanya ufalme wa kudumu milele uanzishwe? Sivyo, bali wanaendelea kutiishwa chini ya milki nyingine ya kipagani, Umedi-Uajemi. “Nyakati zilizowekwa rasmi” ili mataifa yatawale hazijakwisha bado. (Luka 21:24) Kwa kuwa hakuna mfalme katika Israeli, ahadi ambayo Yehova alimtolea Daudi itakaa bila kutimizwa muda wa karne kadhaa zinazokuja.
12. Yehova alichukua hatua gani kuelekea kutimiza agano la Ufalme alilofanya na Daudi?
12 Zaidi ya miaka 500 baada ya Israeli kuachiliwa kutoka utekwani Babiloni, Yehova alichukua hatua kubwa kuelekea kulitimiza agano la Ufalme. Alifanya hivyo alipohamisha uhai wa Mwana wake mzaliwa wa kwanza, ambaye ndiye mwanzo wa uumbaji wake, akautoa katika utukufu wa kimbingu, akauingiza katika tumbo la uzazi la Maria, bikira Myahudi. (Wakolosai 1:15-17) Akitangaza tukio hilo, malaika wa Yehova alimwambia Maria hivi: “Huyu atakuwa mkubwa na ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi Sana; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na hakutakuwa na mwisho wa ufalme wake.” (Luka 1:32, 33) Kwa hiyo Yesu alizaliwa katika ukoo wa kifalme wa Daudi, akarithi haki ya kuwa mfalme. Akiisha kutawazwa kuwa mfalme, Yesu angetawala “hata milele.” (Isaya 9:7; Danieli 7:14) Hivyo, sasa ikawa inawezekana kutimiza ahadi ya Yehova iliyosemwa karne nyingi zilizotangulia kwamba angempa Mfalme Daudi mrithi wa kudumu.
“Jemadari kwa Kabila za Watu”
13. Yesu alikuwaje “shahidi kwa kabila za watu” wakati wa huduma yake na pia baada ya kupaa kwake?
13 Mfalme huyu wa wakati ujao atafanya nini? Yehova anasema hivi: “Angalieni, nimemweka kuwa shahidi kwa kabila za watu; kuwa kiongozi na jemadari kwa kabila za watu.” (Isaya 55:4) Yesu alipokuwa mtu mzima, alikuwa mwakilishi wa Yehova duniani, shahidi wa Mungu kwa mataifa. Wakati wa maisha yake ya kibinadamu, huduma yake ilielekezwa kwa “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Lakini, muda mfupi kabla Yesu hajapaa mbinguni, aliwaambia wafuasi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote . . . Tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 10:5, 6; 15:24; 28:19, 20) Hivyo, baada ya muda, ujumbe wa Ufalme ulipelekwa kwa watu wasio Wayahudi, na wengine wao walishiriki katika utimizo wa agano lililofanywa pamoja na Daudi. (Matendo 13:46) Kwa njia hiyo, hata baada ya Yesu kufa, kufufuliwa, na kupaa mbinguni, aliendelea kuwa ‘shahidi wa Yehova kwa kabila za watu.’
14, 15. (a) Yesu alijithibitisha jinsi gani kwamba yeye ni “kiongozi na jemadari”? (b) Wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walikuwa na tazamio gani?
14 Pia Yesu alipaswa kuwa “kiongozi na jemadari.” Kulingana na maelezo hayo ya kiunabii, Yesu alikubali kabisa madaraka ya ukichwa wake alipokuwa duniani, akawapa watu mwongozo kwa kuwawekea mfano ufaao katika kila jambo. Alivutia vikundi vikubwa vya watu, akawafundisha maneno ya kweli, na kuwaonyesha faida zinazowajia wale wanaofuata uongozi wake. (Mathayo 4:24; 7:28, 29; 11:5) Aliwazoeza wanafunzi wake kwa njia yenye mafaa, akawatayarisha kufanya kazi kubwa ya kuhubiri iliyokuwa mbele yao. (Luka 10:1-12; Matendo 1:8; Wakolosai 1:23) Katika muda wa miaka mitatu na nusu tu, Yesu aliweka msingi wa kutaniko la kimataifa lenye umoja, lenye maelfu ya washirika waliotolewa kutoka makabila mengi! Ni “kiongozi na jemadari” wa kweli peke yake ambaye angaliweza kutimiza kazi kubwa hivyo.b
-