Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Rumania
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Kusanyiko la Kwanza la Kitaifa

      Mnamo Septemba 28 na 29, 1946, Mashahidi wa Yehova walifanya kusanyiko lao la kwanza la kitaifa nchini Rumania. Lilifanywa kwenye Uwanja wa Waroma jijini Bucharest. Kampuni ya reli ilikubali kupanga gari-moshi la pekee na hata kupunguza nauli kwa nusu! Gari-moshi hilo liliwasafirisha wahudhuriaji zaidi ya 1,000 kutoka sehemu za mbali zaidi za nchi hadi Bucharest. Wengi walibeba mabango yaliyowavutia watu njiani. Hata hivyo, safari hiyo haikuwa shwari kabisa.

      Makasisi walisikia kuhusu kusanyiko hilo nao wakajaribu kusimamisha gari-moshi hilo. Mashahidi walioishi Bucharest walianza kumiminika kwenye kituo cha gari-moshi mwendo wa saa 3.00 asubuhi ya Ijumaa iliyotangulia kusanyiko, wakitarajia kuwakaribisha ndugu zao kati ya saa 3:00 na saa 4:00 asubuhi hiyo. Walisubiri hadi mwendo wa saa 12:00 jioni, ndipo gari-moshi lilipofika hatimaye. Ni vigumu kueleza jinsi wageni na wale waliowakaribisha walivyosisimka walipokumbatiana. Polisi wenye silaha walikuwapo ili kudumisha amani, lakini hawakuwa na kazi.

      Haikuwa rahisi kupata mahali pa kulala kwa sababu sehemu kubwa ya Bucharest pamoja na nyumba 12,000 zilikuwa zimeharibiwa wakati wa vita. Lakini ndugu hawakushindwa la kufanya. Walinunua mabua mengi sana na kuyatandaza chini kwenye bustani ya ndugu aliyeishi katika kiunga kinachoitwa Berceni. Kwa sababu kulikuwa na joto isivyo kawaida katika mwezi wa Septemba, ndugu, dada, na watoto waliohudhuria kusanyiko walilala kwa starehe kwenye godoro la mabua, nyota zikimetameta angani. Leo kuna Jumba la Ufalme maridadi mahali hapo.

      Wale 3,400 waliohudhuria kusanyiko Jumamosi asubuhi walifurahi sana kusikia kwamba Mnara wa Mlinzi lilikuwa limeanza kuchapishwa tena mara mbili kwa mwezi katika Kirumania na Kihungaria. Asubuhi hiyo ndugu waligawiwa nakala 1,000 za toleo la kwanza la gazeti hilo. Kwa kipindi fulani, kila toleo lilikuwa na makala nne za funzo, ili wote wanufaike na habari walizokosa wakati wa vita.

      Jumapili asubuhi ilitengwa kwa ajili ya kazi ya kuhubiri. Wahubiri walitangaza hotuba ya watu wote kotekote. Mabango yao yalikuwa na picha ya nyundo, upanga, na chuma cha kufulia. Maandishi yalisema: “‘Panga Zinafuliwa Kuwa Majembe’—Mungu Aliongoza Maneno Hayo Yaandikwe. Manabii Wawili Waliyaandika. Lakini Ni Nani Watakaotenda Kupatana Nayo?” Wahubiri waliwapa watu karatasi za mwaliko na kuwatolea magazeti waliyoyabeba katika mifuko myeupe yenye maneno, “Mashahidi wa Yehova,” “Wahubiri wa Ufalme wa Mungu,” au “Wahubiri wa Utawala wa Mungu.”

      Martin Magyarosi alianza hotuba yake alasiri hiyo kwa kusema: “Leo, viongozi wa ulimwengu wanajadiliana kuhusu amani huko Paris. Hapa, kwenye kusanyiko letu kuna wahudhuriaji 15,000. Kama ungewapekua Mashahidi wa Yehova wote waliopo, hungepata upanga wala hata bunduki moja. Kwa nini? Kwa sababu sisi tumekwisha fua panga zetu kuwa majembe!” Hotuba hiyo ilikuwa yenye kuvutia na ya wakati unaofaa kwa sababu athari za vita zilionekana kila mahali.

      Mkuu wa sheria, katibu mmoja wa Wizara ya Mambo ya Ndani, polisi kadhaa, na kikundi cha makasisi wa Kanisa Othodoksi walihudhuria Jumapili. Ndugu na wale wenye mamlaka walifikiri kwamba makasisi wangesababisha mchafuko kama walivyotisha kufanya. Lakini mtu mmoja tu ndiye aliyejaribu kuvuruga mkutano huo. Ndugu walimzuia walipomwona akielekea kwenye jukwaa wakati wa hotuba ya watu wote, wakashika mikono yake kwa nguvu, na kumrudisha kitini. Walimnong’onezea hivi: “Hakuna haja kwa kasisi wa Kanisa Othodoksi kuwahutubia watu hawa, lakini umekaribishwa kwa moyo wote kuketi na kusikiliza.” Hakujaribu kusababisha mchafuko tena. Baadaye, yule mkuu wa sheria alisema kwamba alifurahia hotuba zilizotolewa na kwamba alivutiwa na utaratibu wa Mashahidi wa Yehova.

      Baadaye, ndugu mmoja aliandika hivi kuhusu kusanyiko hilo: “Njama ya maadui ilishindwa kabisa, na ndugu walirudi nyumbani wakiwa na shangwe nyingi.” Ndugu walikuwa na roho mpya ya amani na umoja, na hilo lilitia moyo sana kwa sababu wengi walikuja kusanyikoni wakiwa wamechanganyikiwa kwa sababu ya migawanyiko iliyotokea wakati wa vita.

  • Rumania
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 105]

      Bango linalotangaza kusanyiko la kitaifa la mwaka wa 1946

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki