Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Kuna Kiumbe Fulani Anayesababisha Uovu?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 1
    • Je, Kuna Kiumbe Fulani Anayesababisha Uovu?

      “NILIKUTANA uso kwa uso na Ibilisi.” Hivyo ndivyo kamanda wa majeshi ya Umoja wa Mataifa nchini Rwanda alivyosema akionyesha kushindwa kwa majeshi hayo kuchukua hatua yoyote ya kukomesha mauaji ya jamii nzima-nzima nchini humo mwaka wa 1994. Akizungumza kuhusu ukatili usio wa kawaida ambao ulifanywa wakati huo, mtu mwingine alisema: “Ikiwa kuna mtu anayetilia shaka kama kuna Shetani, basi tukutane kwenye kaburi la ujumla nchini Rwanda.” Je, ukatili kama huo ni kazi ya Ibilisi?

      Watu wengi hawafikiri kwamba jeuri na ukatili wa aina hiyo ni kazi ya kiumbe mwovu wa roho asiyeonekana. Wengi wanafikiri kwamba mambo kama hayo yanasababishwa na uovu tuliozaliwa nao na kwamba chanzo kikuu cha uovu ni mtazamo wetu wa ubinafsi. Watu wengine wanafikiri kwamba kundi fulani la watu matajiri na wenye nguvu, ambao wanafanyiza mtandao wa siri wa ulimwenguni pote, wamekuwa wakidanganya watu kwa miaka mingi ili waitawale dunia. Kisha, kuna wale wanaozilaumu serikali na watawala wa nchi zao kwa ukosefu wa haki na mateso wanayoona.

      Wewe una maoni gani? Kwa nini uovu, ukatili, jeuri, na kuteseka kumeenea sana ulimwenguni leo ingawa kuna jitihada za kukomesha mambo hayo? Kwa nini wanadamu wanakimbilia kufanya mambo maovu, huku wakipuuza maonyo yanayotolewa? Je, kuna kiumbe anayesababisha mambo yote hayo? Ni nani hasa anayeutawala ulimwengu? Huenda majibu ya maswali hayo yakakushangaza.

  • Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 1
    • Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?

      HUENDA hujawahi kamwe kukutana na kiongozi yeyote wa kikundi cha wahalifu. Je, hilo linamaanisha kwamba hakuna viongozi kama hao? Viongozi wa makundi ya wahalifu wana ujuzi wa kujificha ili wasijulikane au hata kuongoza makundi yao wakiwa gerezani. Hata hivyo, vichwa vikuu vya magazeti kuhusu mapambano kati ya makundi ya kuuza dawa za kulevya, makundi ya makahaba, na biashara ya kuuza watu, vinatukumbusha kuhusu uvutano na matokeo mabaya ya wahalifu kama hao. Tunajua kwamba kuna viongozi wa vikundi vya wahalifu kwa sababu tunaona mambo wanayowafanyia wanadamu.

      Neno la Mungu, Biblia, linaonyesha kwamba Shetani ni kiumbe halisi wa roho ambaye kama tu kiongozi mwenye nguvu wa kikundi cha wahalifu, anajaribu kutimiza makusudi yake kupitia “ishara za uwongo” na “udanganyifu usio wa uadilifu.” Kwa kweli, kama Biblia inavyosema, Shetani “huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wathesalonike 2:9, 10; 2 Wakorintho 11:14) Vivyo hivyo, tunaweza kujua kwamba Ibilisi ni kiumbe halisi kutokana na mambo anayotenda. Hata hivyo, ni vigumu kwa watu wengi kuamini kwamba kuna kiumbe mwovu wa roho asiyeonekana. Kabla hatujachunguza kwa undani Biblia inasema nini kuhusu Ibilisi, acheni tuone baadhi ya vizuizi na itikadi zenye makosa zinazowafanya wengi wakatae wazo la kwamba Ibilisi ni kiumbe halisi.

      ◼ “Kwa nini Mungu mwenye upendo alimuumba Ibilisi?” Kwa kuwa Biblia inasema kwamba Mungu ni mwema na ni mkamilifu, lingekuwa jambo lisilopatana na akili kufikiri kwamba angemuumba kiumbe mwovu, na mwenye chuki kama huyo. Ukweli ni kwamba Biblia haisemi Mungu aliumba kiumbe kama huyo. Kinyume cha hilo, inasema hivi kumhusu Mungu: “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.”—Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 5:4.

      Jambo tunalopaswa kufikiria ni ikiwa kiumbe mkamilifu aliyeumbwa na Mungu angeweza kufanya mambo yasiyo sawa. Badala ya kuwaumba viumbe wake kama mashine, Mungu aliwapa uhuru wa kuchagua, yaani, uwezo wa kufanya maamuzi yao wenyewe. Hivyo, kiumbe mkamilifu mwenye akili anaweza kuchagua kutenda mema au mabaya. Kwa kweli, mambo yanayofanywa tu na kiumbe mwenye akili, awe mwanadamu au kiumbe wa roho aliyepewa uhuru wa kuchagua, ndiyo yanayoweza kuwa makosa au sawa kimaadili.

      Kwa hiyo, Mungu hangewapa viumbe wake uhuru wa kuchagua na wakati huohuo awazuie kufanya mabaya ikiwa wangeamua kufanya hivyo. Yesu alizungumzia kuhusu matumizi mabaya ya uhuru wa kuchagua aliposema hivi kumhusu Ibilisi: “Hakusimama imara katika kweli.” (Yohana 8:44) Maneno hayo yanaonyesha waziwazi kwamba kiumbe wa roho ambaye mwanzoni alikuwa mkamilifu, alikuja kuwa Ibilisi, ingawa wakati fulani ‘alisimama imara katika kweli.’a Yehova Mungu aliwaumba viumbe wake wakiwa na uhuru wa kuchagua kwa sababu anawapenda na kuwaamini.—Ona sanduku “Je, Kiumbe Mkamilifu Angeweza Kupoteza Ukamilifu?” kwenye ukurasa wa 6.

      ◼ “Je, Ibilisi ni mtumishi wa Mungu?” Watu fulani wanaona ni kama Biblia inadokeza wazo hilo katika kitabu cha Ayubu. Kulingana na kitabu kimoja kinachofafanua Biblia, maneno Ibilisi alikuwa ‘akizurura huku na huku duniani’ yanarejelea jukumu la wapelelezi wa zamani wa Uajemi, ambao walienda huku na huku na kuleta ripoti kwa mfalme wao. (Ayubu 1:7) Hata hivyo, ikiwa kwa kweli Ibilisi alikuwa mpelelezi wa Mungu, kwa nini alipaswa kumweleza kwamba alikuwa ametoka ‘kuzurura huku na huku duniani’? Badala ya kumwita mtumishi wa Mungu, simulizi la kitabu cha Ayubu linamwita Ibilisi kwa jina Shetani, linalomaanisha “Mpinzani.” Jambo hilo linaonyesha kwamba yeye ndiye Adui mkuu wa Mungu. (Ayubu 1:6) Hivyo basi, wazo la kwamba Ibilisi anamtumikia Mungu linatoka wapi?

      Mapema katika karne ya kwanza W.K., vitabu vya apokrifa, kama vile “Kitabu cha Yubile” na “Sheria za Kawaida” vya madhehebu ya Qumran, vilimwonyesha Ibilisi akijadiliana na Mungu na bado akiwa anafanya mapenzi Yake. Katika kitabu chake Mephistopheles, mwanahistoria J. B. Russell anaeleza kwamba Mprotestanti Martin Luther, kiongozi wa Marekebisho Makubwa ya Kidini, alimwona Ibilisi kuwa kifaa cha Mungu, “kama jembe analotumia kupalilia bustani yake.” Russell anafafanua maoni hayo kwa kusema kwamba, “jembe linafurahia kuharibu magugu,” lakini bado linabaki katika mkono wenye nguvu wa Mungu likitimiza mapenzi Yake. Fundisho hilo la Luther—ambalo baadaye lilikubaliwa na mwanatheolojia Mfaransa John Calvin—liliwaudhi watu wengi kwa kuwa waliona si haki kufanya hivyo. Mungu mwenye upendo angewezaje kuruhusu uovu na hata kuusababisha? (Yakobo 1:13) Kwa sababu ya fundisho hilo, na pia ukatili uliotokea katika karne ya 20, watu wengi hawaamini kwamba kuna Mungu wala Ibilisi.

      ◼ “Ibilisi ni uovu tu” Kumwona Ibilisi kuwa uovu tu kunaweza kufanya iwe vigumu kuelewa masimulizi fulani katika Biblia. Kwa mfano, kama inavyoelezwa katika Ayubu 2:3-6, Mungu alikuwa akizungumza na nani? Je, inawezekana alikuwa akizungumza na uovu tu uliokuwa ndani ya Ayubu, au labda hata alikuwa akijizungumzia mwenyewe? Zaidi ya hayo, je, Mungu alikuwa akimsifu Ayubu kwa sifa zake nzuri, kisha kuruhusu Ayubu ajaribiwe na uovu fulani? Kumwazia Mungu kwa njia hiyo kungefanya aonekana kuwa mwovu badala ya kuonekana kuwa Mungu ambaye “ndani yake hamna ukosefu wowote wa uadilifu.” (Zaburi 92:15) Kinyume cha hilo, Mungu alikataa ‘kunyoosha mkono wake’ ili kumuumiza Ayubu. Kwa kweli, Ibilisi si uovu tu wala tabia fulani mbaya ambayo Mungu anayo, bali ni kiumbe wa roho ambaye alijifanya mwenyewe kuwa Adui wa Mungu.

      Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?

      Watu wengi leo wanahisi kwamba mtu anayeamini kuna Ibilisi amepitwa na wakati. Hata hivyo, maelezo ya kwamba Ibilisi ndiye chanzo cha uovu yanaridhisha sana kuliko ufafanuzi mwingine wowote. Kwa kweli, jitihada za kuonyesha kwamba hakuna Ibilisi zimefanya watu wamkatae Mungu na pia kukataa kufuata viwango vyovyote vya maadili.

      Charles-Pierre Baudelaire, mshairi wa karne ya 19, aliandika hivi: “Ujanja wa hali ya juu wa Ibilisi ni kutushawishi tuamini kwamba yeye hayuko.” Kwa kuficha utambulisho wake, Ibilisi amesababisha kuwe na shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu. Ikiwa hakuna Ibilisi, je, hilo halingefanya Mungu alaumiwe kuwa chanzo cha uovu? Je, si ni kweli kwamba Ibilisi angependa watu waamini hivyo?

      Kama vile kiongozi wa kikundi cha wahalifu anavyofanya, Ibilisi anaficha utambulisho wake ili atimize lengo lake. Lengo gani? Biblia inasema: “Mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini, ili nuru ya habari njema yenye utukufu juu ya Kristo, aliye mfano wa Mungu, isipenyeze mwangaza.”—2 Wakorintho 4:4.

      Swali moja muhimu linabaki. Mungu atamfanya nini Ibilisi ambaye ndiye chanzo kisichoonekana cha uovu na kuteseka kote? Hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ili kuelewa kwa nini Mungu hakukomesha uasi wa Ibilisi mara moja, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      Je, Ibilisi ni mtumishi wa Mungu au ni mpinzani wake?

      [Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 6]

      Je, Kiumbe Mkamilifu Angeweza Kupoteza Ukamilifu?

      Ukamilifu ambao Mungu amewapa viumbe wake wenye akili ni wa kadiri tu. Ingawa Adamu aliumbwa akiwa mkamilifu, alipaswa kuheshimu mipaka aliyowekewa na Muumba wake. Kwa mfano, hangeweza kula udongo, changarawe, au mbao bila kupata matatizo. Ikiwa angepuuza sheria ya uvutano na kuruka kutoka mahali palipoinuka sana, angeweza kufa au kuumia vibaya.

      Vivyo hivyo, hakuna kiumbe mkamilifu—binadamu au malaika—anayeweza kupuuza kanuni ambazo zimewekwa na Mungu kuhusu mwenendo mzuri na asipatwe na matatizo. Hivyo, wakati kiumbe mwenye akili anapotumia vibaya uhuru wake wa kuamua, anaanguka kwa urahisi katika kosa na dhambi.—Mwanzo 1:29; Mathayo 4:4.

  • Mtawala wa Ulimwengu Asiyeonekana Afunuliwa
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 1
    • Mtawala wa Ulimwengu Asiyeonekana Afunuliwa

      PINDI moja Yesu aliwaambia watu hivi: “Mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” Baadaye akaongeza kuwa ‘mtawala wa ulimwengu hana uwezo juu yake’ na kwamba “mtawala wa ulimwengu huu amehukumiwa.” (Yohana 12:31; 14:30; 16:11) Yesu alikuwa akizungumza kumhusu nani?

      Kwa kufikiria yale ambayo Yesu alikuwa akisema kuhusu “mtawala wa ulimwengu huu,” ni wazi kwamba hakuwa akimrejelea Baba yake, Yehova Mungu. Hivyo basi, “mtawala wa ulimwengu huu” ni nani? “Atatupwa nje” jinsi gani, na “amehukumiwa” jinsi gani?

      “Mtawala wa Ulimwengu Huu” Ajifunua Mwenyewe

      Kama vile mara nyingi kiongozi wa kikundi cha wahalifu anavyojisifu kuhusu nguvu zake, ndivyo Ibilisi alivyofanya alipokuwa akimjaribu Yesu, Mwana wa Mungu. Baada ya kumwonyesha Yesu “falme zote” za dunia, Shetani alimpa ahadi hii: “Hakika nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wake, kwa sababu nimepewa, na yeyote ninayetaka mimi humpa. Kwa hiyo, ukifanya tendo la ibada mbele yangu, yote itakuwa yako.”—Luka 4:5-7.

      Ikiwa Ibilisi ni uovu tu, kama ambavyo wengine wamedokeza, kishawishi hicho kingefafanuliwa jinsi gani? Je, Yesu alikuwa akishawishiwa na mawazo fulani maovu au hali ya kuvurugika ambayo huenda ilimpata baada ya kubatizwa? Ikiwa ndivyo, kwa nini isemwe kuwa “hakuna dhambi ndani yake”? (1 Yohana 3:5) Yesu hakupinga kwamba ibilisi ana nguvu juu ya wanadamu, badala yake, alikazia jambo hilo aliposema kwamba Ibilisi ni “mtawala wa ulimwengu huu” na pia ni “muuaji” na “mwongo.”—Yohana 14:30; 8:44.

      Miaka 60 hivi baada ya Kristo kukutana na Ibilisi, mtume Yohana aliwakumbusha Wakristo kuhusu uvutano wenye nguvu wa Ibilisi, akisema kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Yohana pia alisema kwamba Ibilisi ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (1 Yohana 5:19; Ufunuo 12:9) Kwa wazi, Biblia inamtaja kiumbe wa roho asiyeonekana kuwa ndiye “mtawala wa ulimwengu.” Hata hivyo, uvutano wake juu ya wanadamu ni mkubwa kadiri gani?

      Mtawala wa Ulimwengu Anawapa Washirika Wake Mamlaka

      Akiandika kuhusu vita vya imani vya Wakristo, mtume Paulo alitaja waziwazi maadui wao wakubwa. “Tuna kushindana mweleka,” akasema waziwazi, “si juu ya damu na mwili, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Hivyo, Wakristo hawapigani na wanadamu wenzao, kwa kuwa vita hivyo vinapiganwa, “si juu ya damu na mwili,” bali dhidi ya “majeshi ya roho waovu.”

      Kulingana na tafsiri nyingi za Biblia za kisasa, “majeshi ya roho waovu” hayarejelei uovu tu, bali viumbe waovu wa roho wenye nguvu. Katika Biblia fulani maneno hayo yametafsiriwa kuwa “majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho” (Union Version), “jeshi ovu la ulimwengu wa roho” (Biblia Habari Njema). Hivyo, Ibilisi amekuwa akitumia mamlaka yake kupitia malaika waasi ambao waliacha “makao yao wenyewe yanayofaa” huko mbinguni.—Yuda 6.

      Kitabu cha Biblia cha unabii wa Danieli kinafunua jinsi ambavyo ‘watawala hao wa dunia’ wamekuwa wakiongoza mambo ulimwenguni tangu zamani za kale. Akiwa anahangaishwa na hali ya Wayahudi wenzake ambao katika mwaka wa 537 K.W.K. walikuwa wamerudi Yerusalemu kutoka uhamishoni Babiloni, nabii Danieli alisali kwa niaba yao kwa majuma matatu. Malaika, aliyetumwa na Mungu kumtia moyo nabii huyo, alimweleza kwa nini alichelewa kufika. Alisema: “Mkuu wa ufalme wa Uajemi alikuwa amesimama katika upinzani juu yangu kwa siku 21.”—Danieli 10:2, 13.

      Huyo “mkuu wa ufalme wa Uajemi” alikuwa nani? Bila shaka, malaika yule hakuwa akimrejelea Mfalme Koreshi wa Uajemi, ambaye wakati huo alipendezwa na Danieli na watu wake. Zaidi ya hayo, mfalme wa kibinadamu angeweza jinsi gani kumzuia kiumbe wa roho kwa majuma matatu na inajulikana kwamba ilimchukua malaika mmoja usiku mmoja tu kuua wanajeshi hodari 185,000? (Isaya 37:36) ‘Mkuu huyo wa ufalme wa Uajemi’ mwenye uadui ni lazima alikuwa mwakilishi wa Ibilisi, yaani, roho mwovu ambaye alikuwa amepewa mamlaka juu ya serikali ya Milki ya Uajemi. Baadaye kwenye simulizi hilo, malaika wa Mungu alisema kwamba angepaswa kupigana tena na “mkuu wa ufalme wa Uajemi” na pia roho mwingine mwovu ambaye alikuwa “mkuu wa ufalme wa Ugiriki.”—Danieli 10:20.

      Tunaweza kukata kauli gani? Kwa kweli, kuna “watawala wa ulimwengu,” roho wakuu waovu ambao wanashirikiana kuiongoza dunia chini ya mamlaka ya kiongozi wao mkuu, Shetani Ibilisi. Lakini wamekuwa na lengo gani mpaka sasa?

      Mtawala wa Ulimwengu Aonyesha Utu Wake Halisi

      Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo, mtume Yohana anasimulia jinsi Yesu, akiwa Mikaeli, yule malaika mkuu, anavyomshinda Ibilisi na mashetani wake na anataja pia kuhusu matokeo mabaya ya kufukuzwa kwao kutoka mbinguni. Tunasoma hivi: ‘Ole wa dunia kwa sababu Ibilisi ameshuka kwako, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.’—Ufunuo 12:9, 12.

      Ibilisi ameonyesha jinsi gani hasira yake kali? Kama vile tu wahalifu wengi waliokata tamaa wanavyofuata azimio la ‘kutawala au kuangamiza,’ Ibilisi na mashetani wake wameazimia kwamba kufikia wakati watakapoangamizwa watakuwa wameangamiza dunia pamoja na wakaaji wake. Akijua kwamba wakati wake ni mfupi, Ibilisi amekuwa akitumia sehemu moja kuu iliyo chini ya mamlaka yake—biashara kubwa-kubwa—ili kuchochea tamaa ya kununua vitu vingi, jambo linalosababisha kupungua kwa maliasili na kuharibiwa kwa mazingira ulimwenguni, na hivyo kuhatarisha uhai wa wanadamu.—Ufunuo 11:18; 18:11-17.

      Tangu mwanzo wa historia ya mwanadamu, tamaa ya Ibilisi ya kutaka kutawala imeonekana pia katika siasa na dini. Kitabu cha Ufunuo kinafananisha mamlaka za kisiasa na wanyama ambao Ibilisi amewapa “mamlaka kubwa.” Pia kitabu hicho kinaonyesha kwamba ni jambo la aibu kwa dini kujihusisha na siasa na kinauita uhusiano huo uzinzi wa kiroho wenye kuchukiza. (Ufunuo 13:2; 17:1, 2) Fikiria ukandamizaji, utumwa, vita, na mizozo ya kikabila ya muda mrefu ambayo imesababisha vifo vya mamilioni ya watu. Je, kuna yeyote ambaye anaweza kusema kwa unyofu kwamba matukio yote hayo yenye kushtua ambayo yametokea katika historia yamesababishwa na wanadamu tu? Au yamesababishwa na majeshi ya roho waovu wasioonekana?

      Biblia inamtambulisha na kumfunua waziwazi kiumbe ambaye amekuwa akiwaongoza watawala wa kibinadamu na serikali kuu za ulimwengu. Wawe wanajua au hawajui, wanadamu wanaonyesha utu wa mtawala wa ulimwengu na azimio lake la ‘kutawala au kuangamiza.’ Hata hivyo, wanadamu wataendelea kuteseka chini ya utawala wa Ibilisi kwa muda gani?

      Kuangamizwa kwa Ibilisi

      Huduma ya Kristo hapa duniani katika karne ya kwanza ilionyesha kwamba Ibilisi na mashetani wake wataangamizwa hivi karibuni. Wanafunzi wa Yesu waliposimulia jinsi walivyowafukuza mashetani, Yesu aliwaambia: “Nilianza kumwona Shetani akiwa tayari ameanguka kama umeme kutoka mbinguni.” (Luka 10:18) Kwa maneno hayo, Yesu alikuwa akishangilia ushindi ambao angepata dhidi ya mtawala wa ulimwengu huu, baada ya Yesu kurudi mbinguni akiwa Mikaeli yule malaika mkuu. (Ufunuo 12:7-9) Uchunguzi wa kina wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba ushindi huo ulitokea mbinguni mwaka wa 1914 au muda mfupi baadaye.a

      Tangu wakati huo, Ibilisi anajua kwamba ni muda mfupi tu unaobaki kabla ya kuangamizwa. Ingawa ‘ulimwengu mzima unakaa katika nguvu zake,’ mamilioni ya watu leo hawajapotoshwa na jitihada zake za kujaribu kuwaongoza. Biblia imewasaidia kujua yeye ni nani na mbinu anazotumia. (2 Wakorintho 2:11) Wanafarijiwa na maneno haya ya Paulo kwa Wakristo wenzake: “Mungu anayetoa amani atamponda Shetani chini ya miguu yenu upesi.”b—Waroma 16:20.

      Hivi karibuni Ibilisi ataangamizwa! Chini ya uongozi wenye upendo wa Kristo, wanadamu waadilifu watakigeuza kiti cha mfano cha kuwekea miguu cha Mungu, yaani, dunia, kuwa paradiso. Hakutakuwa na jeuri, chuki, wala pupa milele. “Mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini,” inasema Biblia. (Isaya 65:17) Kitakuwa kitulizo kikubwa kama nini kwa wote wanaomkataa mtawala asiyeonekana wa ulimwengu huu na utawala wake!

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu mwaka huo, ona nyongeza katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ukurasa wa 215 hadi 218.

      b Maneno ya Paulo kwenye mstari huo yanarejelea unabii wa kwanza wa Biblia ulio katika Mwanzo 3:15 ambao unaeleza kuhusu kuangamizwa kwa Ibilisi. Ili kueleza tukio hilo, Paulo alitumia neno la Kigiriki linalomaanisha “kuvunja-vunja, kutikisa-tikisa, kuvunja vipande-vipande kwa kuponda.”—Vine’s Complete Expository Dictionary of Old and New Testament Words.

      [Blabu katika ukurasa wa 9]

      Chini ya uongozi wenye upendo wa Kristo, wanadamu waadilifu wataigeuza dunia kuwa paradiso

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki