Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuokolewa Wakati wa Maafa
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Agosti 15
    • Kuokolewa Wakati wa Maafa

      DUKA la orofa tano katika Seoul, Korea, liliporomoka ghafula, likinasa mamia kadhaa ya watu ndani! Wafanyakazi wa kuokoa walifanya kazi ngumu mchana na usiku ili kuokoa uhai wa watu wengi kadiri ilivyowezekana. Kadiri siku zilivyopita, ndivyo uwezekano wa kupata waokokaji zaidi waliozikwa chini ya rundo kubwa la vifusi ulivyozidi kudidimia.

      Kulipokuwa hakuna tena tumaini lolote la kupata waokokaji, ndipo jambo la kushangaza lilipotokea. Kilio dhaifu cha huzuni kilisikika kikitoka chini ya hivyo vifusi. Wakiwa na wasiwasi waokoaji walifukua kwa mikono yao mitupu ili kumwokoa mwanamke mwenye umri wa miaka 19 aliyekuwa amezikwa akiwa hai kwa siku 16 zilizoonekana kuwa ndefu. Shimo la lifti iliyoporomoka lilikuwa limefanyiza uvungu uliotoa himaya juu yake na ulikuwa umemkinga na tani nyingi za saruji iliyokuwa ikianguka. Ijapokuwa alikuwa amepoteza maji mengi sana mwilini na amekatwa, alikuwa ameponyoka kifo!

      Siku hizi, karibu kila mwezi kuna ripoti za msiba fulani, iwe ni tetemeko la dunia, dhoruba kali, mlipuko wa volkeno, aksidenti, au njaa kuu. Na hadithi za kustaajabisha za kuokoza na za uokokaji huvutia mamilioni ya watu, ambao husikiliza na kusoma habari. Hata hivyo, onyo la afa fulani linalokuja—moja ambalo ni kubwa zaidi kupita jinginelo katika historia ya kibinadamu—kwa ujumla limepuuzwa. (Mathayo 24:21) Biblia hulifafanua tukio hilo linalokuja katika maneno haya: “Tazama, uovu [“afa,” NW] utatokea toka taifa hata taifa, na tufani kuu itainuliwa toka pande za mwisho wa dunia. Na waliouawa na BWANA siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.”—Yeremia 25:32, 33.

      Maneno yenye kushtusha! Lakini tofauti na misiba na aksidenti za asili, afa hilo halitakuwa uchinjaji usiochagua. Kwa hakika, kuokolewa—kuokolewa kwako—kwawezekana!

      Wakati wa Uharaka

      Ili kuelewa jambo hili kabisa, lazima mtu aelewe kwa nini afa hili la tufeni pote litatokea. Kwa kweli, hilo ndilo suluhisho halisi pekee kwa matatizo ya mwanadamu. Ni watu wachache tu leo ambao huhisi wakiwa salama salimini. Licha ya jitihada za sayansi, maradhi yenye kuambukiza yanaendelea kuangamiza wakazi wa dunia. Vita vinavyotokana na tofauti za kidini, kikabila, na kisiasa vimeua maelfu ya watu. Njaa kuu huongezea taabu na kuteseka kwa wanaume, wanawake, na watoto wasio na hatia. Hali ya kudhoofika kiadili huharibu hasa ule msingi wa jamii; hata watoto wamepotoshwa wafanye mabaya.

      Kwa usahihi usio na kifani, unabii wa Biblia ulioandikwa miaka zaidi ya 1,900 iliyopita hufafanua hali yetu. Wasema hivi: “Ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.”—2 Timotheo 3:1, Union Version; linganisha Mathayo 24:3-22.

      Je, laonekana jambo lenye kupatana na kufikiri kuzuri kwamba Mungu mwenye upendo angekuwa asiyejali hali yetu iliyo mbaya? Biblia yasema hivi: “Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; . . . hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Ndiyo, badala ya kuruhusu sayari hii yenye kupendeza iangamizwe na wakazi wake wote waishe, Mungu ataingilia kati. Swali ni, Atafanyaje hivyo?

      Chagua Uhai!

      Biblia yajibu hivi kwenye Zaburi 92:7: “Wasio haki wakichipuka kama majani na wote watendao maovu wakistawi. Ni kwa kusudi waangamizwe milele.” Suluhisho la Mungu kwa matatizo ya dunia ni kuondoshwa kwa uovu wenyewe. Kwa kufurahisha, hili halimaanishi kwamba watu wote wahitaji kuondoshwa. Zaburi 37:34 yatuhakikishia hivi: “Wewe umngoje BWANA, uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi, wasio haki watakapoharibiwa utawaona.”

      Maneno hayo yaonyesha kwamba kuna uwezekano wa kuokolewa katika afa kubwa kupita yote litakalowapata wanadamu. Mungu ametupatia chaguo. Maneno ambayo kwayo Musa aliwahimiza sana Waisraeli walipokuwa wakijitayarisha kuingia Bara Lililoahidiwa yanatumika kwetu katika njia ileile: “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima [“uhai,” NW], ili uwe hai, wewe na uzao wako.” (Kumbukumbu la Torati 30:19) Lakini, mtu ‘huchaguaje uhai’ na kuokolewa? Je, wokovu wa kweli wamaanisha nini kwa kweli?

  • Wokovu—Inachomaanisha kwa Kweli
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Agosti 15
    • Wokovu—Inachomaanisha kwa Kweli

      ‘WEWE umeokoka?’ Mara nyingi, wanaouliza swali hili huhisi kwamba wameokoka kwa sababu ‘wamemkubali Yesu kuwa Mwokozi wao binafsi.’ Hata hivyo wengine huhisi kwamba kuna njia mbalimbali za kufikia wokovu na maadamu ‘Yesu yumo ndani ya moyo wako,’ haidhuru kile unachoamini au hata wewe ni wa kanisa gani.

      Biblia husema kwamba ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe.” (1 Timotheo 2:3, 4) Hivyo wokovu unapatikana kwa wote watakaoukubali. Lakini yamaanisha nini kuokolewa? Je, kwa kweli ni jambo linalotukia kwako tu kwa kufanya bidii kidogo au bila kufanya bidii yoyote?

      Neno “wokovu” lamaanisha “kukombolewa katika hatari au uharibifu.” Hivyo ni kweli wokovu wahusisha zaidi ya hali tulivu ya akilini. Wamaanisha kuokolewa katika uharibifu wa huu mfumo wa mambo wa sasa ulio mwovu na hatimaye katika kifo chenyewe! Lakini ni nani ambaye Mungu atamwokoa? Kwa kujibu, acheni tuchunguze yale aliyofunza Yesu Kristo juu ya habari hii. Huenda matokeo ya uchunguzi wetu yakakushangaza.

      Wokovu—Wapatikana Katika Dini Zote?

      Pindi moja, Yesu alikuwa na mazungumzo na mwanamke Msamaria. Ijapokuwa hakuwa Myahudi, aliamini kwa usahihi kabisa kwamba Mesiya angekuja “aitwaye Kristo.” (Yohana 4:25) Je, itikadi hiyo ilitosha ili aweze kuokolewa? La, kwa maana Yesu alimwambia huyo mwanamke kwa ujasiri hivi: “Nyinyi mwaabudu kile msichojua.” Yesu alijua kwamba ikiwa mwanamke huyo angepata wokovu, angepaswa kurekebisha njia yake ya kuabudu. Kwa hiyo Yesu alieleza hivi: “Hata hivyo, saa inakuja, nayo ipo sasa, wakati waabudu wa kweli watakapomwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta wa namna hiyo wamwabudu yeye.”—Yohana 4:22, 23.

      Pindi nyingine ambayo Yesu alifunua maoni yake juu ya wokovu ilihusisha Mafarisayo, farakano mashuhuri la Dini ya Kiyahudi. Mafarisayo walikuwa wamefanyiza mfumo wa ibada na waliamini kwamba ulikuwa na kibali cha Mungu. Lakini sikiliza maneno ya Yesu kwa hao Mafarisayo: “Nyinyi wanafiki! Isaya alisema kweli alipotabiri hivi juu yenu: ‘Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao iko mbali nami. Wao huniabudu bure; mafundisho yao yakiwa tu sheria zilizofundishwa na wanadamu.’”—Mathayo 15:7-9, New International Version.

      Lakini vipi juu ya vikundi vya kidini leo vinavyodai kumwamini Kristo? Je, Yesu angevikubali vyote kuwa njia halali za kupata wokovu? Kwa habari hiyo hatuhitaji kukisia, kwa maana Yesu alisema hivi: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbingu, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye katika mbingu ataingia. Wengi wataniambia katika siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya kazi nyingi zenye nguvu katika jina lako?’ Na bado ndipo hakika nitaungama kwao: Sikuwajua nyinyi kamwe! Ondokeni kwangu, nyinyi wafanyakazi wa uasi-sheria.”—Mathayo 7:21-23.

      Ujuzi Sahihi juu ya Yesu Ni wa Maana kwa Wokovu

      Maneno haya ya Yesu yana maana yenye kufanya mtu afikiri. Yaonyesha kwamba watu wengi walio wachaji wanashindwa ‘kufanya mapenzi ya Baba.’ Basi, mtu aweza kupataje wokovu wa kweli? Kitabu cha 1 Timotheo 2:3, 4 chajibu hivi: “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.”—Linganisha Wakolosai 1:9, 10.

      Ujuzi huo ni wa maana sana ili kupata wokovu. Mlinzi wa jela Mroma alipowauliza mtume Paulo na mwandamani wake, Sila, “Ni nini ambalo lazima nifanye ili nipate kuokolewa?” walimjibu hivi: “Amini juu ya Bwana Yesu nawe utapata kuokolewa, wewe na watu wa nyumbani mwako.” (Matendo 16:30, 31) Je, hilo lilimaanisha kwamba jambo tu ambalo mlinzi wa jela na familia yake walihitaji kufanya ni kuwa na hisia fulani mioyoni mwao? La, kwa sababu, hawangeweza kwa kweli “kuamini juu ya Bwana Yesu” bila kuwa na uelewevu fulani juu ya Yesu alikuwa nani, alifanya nini, na lile alilofunza.

      Kwa kielelezo, Yesu alifundisha kuanzishwa kwa serikali ya kimbingu—“ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Pia alieleza waziwazi kanuni juu ya adili na tabia za Kikristo. (Mathayo, sura ya 5-7) Alieleza kwa muhtasari msimamo ambao wanafunzi wake wangechukua ilipohusu mambo ya kisiasa. (Yohana 15:19) Alianzisha programu ya elimu ya tufeni pote na kuwaagiza wafuasi wake waishiriki. (Mathayo 24:14; Matendo 1:8) Ndiyo, ‘kuamini juu ya Yesu’ kulimaanisha kuelewa mambo mengi! Basi, si ajabu kwamba, Paulo na Sila ‘walimwambia [huyo mlinzi wa jela] neno la Yehova pamoja na wote wale walio katika nyumba yake’ kabla ya waamini hao kubatizwa.—Matendo 16:32, 33.

      Ujuzi Sahihi juu ya Mungu Ni Muhimu Pia

      Sehemu ya lazima katika kumwamini Yesu kikweli huhusisha kumwabudu Mungu ambaye Yesu mwenyewe humwabudu. Yesu alisali hivi: “Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

      Wakati wa huduma yake ya kidunia, Mwana wa Mungu alielekeza uangalifu sikuzote kwa Babake na si kwake mwenyewe. Hakudai kamwe kuwa Mungu Mweza-Yote. (Yohana 12:49, 50) Katika pindi nyingi Yesu alieleza wazi wadhifa wake katika mpango wa Mungu kwa kusema kwamba alikuwa chini ya Babake. (Luka 22:41, 42; Yohana 5:19) Kwani, Yesu alijulisha wazi hivi: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Je, kanisa lako limekufundisha huo uhusiano wa kweli kati ya Mungu na Kristo? Au umeongozwa kuamini kwamba Yesu mwenyewe ni Mungu Mweza-Yote? Wokovu wako wategemea kuwa na uelewevu sahihi.

      Katika Sala ya Bwana, Yesu aliwasihi sana wanafunzi wake wasali hivi: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Tafsiri zilizo nyingi zaidi za Biblia zimelificha jina la Mungu, wakilitafsiri “Bwana.” Lakini katika nakala za kale za “Agano la Kale” jina la Mungu lilionekana zaidi ya mara elfu sita! Hivyo andiko la Zaburi 83:18 lasomeka hivi: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Italiki ni zetu.) Je, umefundishwa kulitumia jina la Mungu, Yehova? Ikiwa sivyo, wokovu wako u hatarini, kwa maana “kila mtu aitiaye jina la Yehova ataokolewa”!—Matendo 2:21; linganisha Yoeli 2:32.

      Kwa Roho na Kweli

      Yesu Kristo pia alielekeza uangalifu kwenye Neno la Mungu, Biblia. Alipokuwa akifafanua maoni ya Mungu juu ya mambo fulani, nyakati nyingi alikuwa akisema hivi: “Imeandikwa.” (Mathayo 4:4, 7, 10; 11:10; 21:13) Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alisali kuhusu wanafunzi wake hivi: “Watakase kwa njia ya ile kweli; neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17.

      Hivyo, kuwa na uelewevu wa mafundisho ya Neno la Mungu, Biblia, ni takwa jingine la kutimiza ili kupata wokovu. (2 Timotheo 3:16) Biblia tu ndiyo hujibu maswali kama vile: Ni nini kusudi la uhai? Kwa nini Mungu ameruhusu uovu uendelee kwa muda mrefu sana? Inakuwaje kwa mtu anapokufa? Je, Mungu kwa kweli huwatesa watu motoni? Kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia ni nini?a Mtu hawezi kumwabudu Mungu ifaavyo bila uelewevu sahihi wa masuala hayo, kwa maana Yesu alisema hivi: ‘Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli.’—Yohana 4:23.

      Imani Huchochea Matendo

      Wokovu huhusisha mengi zaidi ya kupata habari tu. Katika moyo wenye kuitikia, ujuzi sahihi juu ya Mungu hutokeza imani. (Waroma 10:10, 17; Waebrania 11:6) Imani hiyo husukuma mtu atende. Kwa kielelezo, Biblia huonya kwa upole hivi: “Tubuni na mgeuke kabisa ili mpate kufutiwa dhambi zenu, ili majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa utu wa Yehova.”—Matendo 3:19.

      Ndiyo, wokovu pia huhusisha kujipatanisha mwenyewe na viwango vya Mungu vya mwenendo na vya adili. Chini ya uvutano wenye kugeuza umbo wa Neno la Mungu, ufuatiaji wa haki na ukweli huchukua mahali pa mazoea ya muda mrefu wa maisha wa kusema uwongo na kudanganya. (Tito 2:10) Mazoea yasiyo ya adili, kama vile ugoni-jinsia-moja, uzinzi, na uasherati, yanaachwa na mahali pake huchukuliwa na mwenendo safi kiadili. (1 Wakorintho 6:9-11) Huko si kujiepusha kwa muda ambako kwategemea hisia-moyo lakini ni badiliko la kudumu litokanalo na funzo na matumizi yenye uangalifu ya Neno la Mungu.—Waefeso 4:22-24.

      Baada ya muda, kumpenda na kumthamini Mungu humsukuma mtu mwenye moyo wa haki ajiweke wakfu kabisa kwa Mungu na kuuonyesha kwa ubatizo wa maji. (Mathayo 28:19, 20; Waroma 12:1) Wakristo waliobatizwa wameokolewa machoni pa Mungu. (1 Petro 3:21) Wakati wa uharibifu unaokuja wa ulimwengu huu mwovu, Mungu atawaokoa kabisa kwa kuwahifadhi hadi mwisho wa dhiki hiyo.—Ufunuo 7:9, 14.

      Kile Ambacho Wokovu Waweza Kumaanisha Kwako

      Ni wazi kutokana na mazungumzo haya mafupi kwamba kupata wokovu kwahusisha mengi zaidi ya ‘kuwa na Bwana Yesu moyoni.’ Kwamaanisha kuendelea kutwaa ujuzi sahihi juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo na kufanya mabadiliko yahitajiwayo maishani mwa mtu. Huenda kufanya hivyo kukasikika kuwa jambo gumu, lakini Mashahidi wa Yehova wako tayari kukusaidia katika jitihada hiyo. Kupitia funzo la Biblia nyumbani, wanaweza kukusaidia kuanza kutembea katika njia ya wokovu wa kweli.b

      Kwa sababu ya ukaribu wa siku ya Mungu ya hukumu inayokuja, kufanya hivyo ni jambo la uharaka zaidi kuliko wakati mwingine wowote uliotangulia! Sasa ndio wakati wa kuyatii maneno haya ya nabii: “Kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA. Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”—Sefania 2:2, 3.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki