-
Uzuri Mwingi Mno wa Kiti cha Ufalme cha Yehova cha KimbinguUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
27, 28. (a) Elezo la Yohana la njozi hii linapasa lituathirije? (b) Ni maswali gani huzuka kwa habari ya ambacho Yohana anafuata kuona na kusikia?
27 Ni nani anaweza kubaki bila kuchochewa hisia zake anaposoma simulizi la Yohana la njozi hii? Ni nzuri mno na tukufu! Lakini kitu halisi lazima kiweje? Fahari yenyewe ya Yehova lazima ihuishe yeyote aliye na moyo wenye uthamini ajiunge na wale viumbe hai wanne na wale wazee 24 katika kumsifu Yeye, katika sala na pia kwa kutangaza peupe jina Lake. Huyu ndiye Mungu ambaye kwa ajili yake Wakristo wana pendeleo la kuwa mashahidi leo. (Isaya 43:10) Kumbuka kwamba njozi ya Yohana inahusu ile siku ya Bwana, tulimo sisi sasa. “Zile roho saba” sikuzote ziko karibu kutuongoza na kututia imara. (Wagalatia 5:16-18) Neno la Mungu linapatikana leo kutusaidia tuwe watakatifu katika kutumikia Mungu mtakatifu. (1 Petro 1:14-16) Kwa hakika, sisi tu wenye furaha kusoma kwa sauti kubwa maneno ya unabii huu. (Ufunuo 1:3, NW) Yanaandaa kishawishi kama nini tuwe waaminifu kwa Yehova na tusiruhusu ulimwengu utukengeushe kutoka kuimba kwa utendaji sifa zake!—1 Yohana 2:15-17.
28 Kufikia hapo, Yohana ameeleza anachoona wakati anapoalikwa akaribie kupitia mlango huo uliofunguliwa katika mbingu. Kwa kutokeza zaidi sana, yeye anaripoti kwamba Yehova, akiwa katika uzuri wote wa fahari Yake na adhama, ameketi juu ya kiti cha ufalme Chake cha kimbingu. Yeye anazungukwa na tengenezo lenye nguvu zaidi ya matengenezo yote—liking’aa kwa umaridadi mwingi na ushikamanifu walo. Mahakama ya kimungu i kikaoni. (Danieli 7:9, 10, 18) Jukwaa limewekwa kwa ajili ya kitu kisicho cha kawaida kitukie. Ni nini, na kinatuathirije sisi leo? Acheni tutazame kadiri mandhari ifungukavyo!
-
-
“Ni Nani Ambaye Anastahili Kufungua Hati-Kunjo?”Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 15
“Ni Nani Ambaye Anastahili Kufungua Hati-Kunjo?”
1. Ni nini kinachotukia sasa katika ile njozi ya Yohana?
YA HALI YA JUU MNO! YENYE KUVUVIA HOFU MNO! Ndivyo ilivyo ile njozi yenye kuchochea ya kiti cha ufalme cha Yehova katika mazingira yacho katikati ya taa za moto, makerubi, wazee 24, na bahari ya kioo. Lakini Yohana, ni kitu gani unachofuata kuona? Yohana anakaza macho yake juu ya kitovu chenyewe cha mandhari hii ya kimbingu, akituambia hivi: “Na mimi nikaona katika mkono wa kulia wa Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme hati-kunjo iliyoandikwa ndani na kwenye upande-pindu, imefungwa kikiki kwa vifungo saba. Na mimi nikaona malaika kabambe akipiga mbiu kwa sauti kubwa: ‘Ni nani ambaye anastahili kufungua hati-kunjo na kulegeza vifungo vyayo?’ Lakini wala katika mbingu wala juu ya dunia wala chini ya dunia hakukupatikana hata mmoja anayeweza kufungua hati-kunjo hiyo au kutazama ndani yayo. Na mimi nikabubujisha machozi mengi kwa sababu hakuna mmoja aliyepatikana kuwa anastahili kufungua hati-kunjo hiyo au kutazama ndani yayo.”—Ufunuo 5:1-4, NW.
2, 3. (a) Ni kwa nini Yohana ana hamu nyingi kwamba mtu fulani apatikane wa kufungua hati-kunjo, lakini ni nini linaloonekana kuwa tazamio la jambo hilo? (b) Watu wa Mungu wamengojea nini kwa hamu nyingi katika wakati wetu?
2 Yehova mwenyewe, Bwana Mwenye Enzi Kuu wa uumbaji wote, ndiye anayetoa hati-kunjo hiyo. Ni lazima iwe imejaa habari za muhimu, kwa kuwa ina maandishi mbele na nyuma. Udadisi wetu unaamshwa. Hati-kunjo hiyo ina nini ndani? Tunakumbuka mwaliko wa Yehova kwa Yohana: “Njoo juu huku, na mimi nitakuonyesha wewe vitu ambavyo lazima vitukie.” (Ufunuo 4:1, NW) Tukiwa na taraja lenye kuwasha-washa, sisi tunatazama mbele ili tujifunze juu ya vitu hivyo. Lakini ole, hati-kunjo imeshindikwa ndi, ikafungwa kwa vifungo saba!
3 Je! yule malaika kabambe atapata mtu anayestahili kufungua hiyo hati-kunjo? Kulingana na Kingdom Interlinear, hati-kunjo iko “juu ya mkono wa kulia” wa Yehova. Hii hudokeza kwamba yeye anaitoa juu ya kiganja chake kilichofunguliwa. Lakini inaonekana kwamba hakuna mmoja katika mbingu au juu ya dunia anayestahili kupokea na kufungua hati-kunjo hiyo. Wala hata chini ya dunia, miongoni mwa watumishi wa Mungu ambao wamekufa, hakuna yeyote aliye na sifa zinazofaa kupokea heshima hii ya juu sana. Si ajabu kwamba Yohana anaonekana amefadhaika! Pengine yeye hatajifunza kamwe vile “vitu ambavyo lazima vitukie.” Vilevile katika siku yetu, watu wa Mungu waliopakwa mafuta wamengojea kwa hamu sana Yehova apeleke nuru yake na ukweli juu ya Ufunuo. Hili angefanya kwa mwendeleo katika wakati uliowekwa wa utimizo wa unabii huo, ili aongoze watu wake katika njia ya “wokovu mtukufu.”—Zaburi 43:3, 5, NW.
Mmoja Ambaye Anastahili
4. (a) Ni nani ambaye amepatikana anayestahili kufungua hati-kunjo na vifungo vyayo? (b) Wale wa jamii ya Yohana na waandamani wayo sasa wanashiriki katika thawabu na pendeleo gani?
4 Ndiyo kuna mtu fulani ambaye anaweza kufungua hati-kunjo! Yohana asimulia hivi: “Lakini mmoja wa wale wazee asema kwangu mimi: ‘Acha kutoa machozi. Tazama! Simba ambaye ni wa kabila la Yuda, mzizi wa Daudi, ameshinda ili kufungua hati-kunjo na vifungo saba vyayo.’” (Ufunuo 5:5, NW) Kwa hiyo Yohana, kausha machozi hayo! Ile jamii ya Yohana na waandamani wayo washikamanifu leo wamevumilia pia makumi ya miaka ya majaribu makali huku wakingojea kwa saburi nuru ya elimu. Lo! ni thawabu yenye kufariji kama nini tuliyo nayo sasa katika kuelewa ile njozi, na ni pendeleo kama nini kushiriki katika utimizo wayo kwa kupiga mbiu ya ujumbe wayo kwa wengine!
5. (a) Ni unabii gani uliosemwa kuhusu Yuda, na wazao wa Yuda walitawala wapi? (b) Shilo ni nani?
5 Aha, “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda”! Yohana anazoelea unabii ambao Yakobo, babu ya jamii ya Kiyahudi, alitangaza kuhusu mwana wake wa nne, Yuda: “Mwana-simba ni Yuda. Kutoka windo, mwana wangu, wewe utapanda hakika. Yeye aliinama, yeye alijinyoosha mwenyewe kama simba na, kama simba, ni nani ambaye huthubutu kuamsha yeye? Fimbo ya kifalme haitageuka kando kutoka Yuda, wala gongo la kamanda kutoka katikati ya nyayo zake, mpaka Shilo aje; na kwa yeye utii wa vikundi vya watu utakuwa.” (Mwanzo 49:9, 10, NW) Mstari wa kifalme wa watu wa Mungu ulikuwa na shina katika Yuda. Kuanzia na Daudi, wafalme wote waliotawala katika Yerusalemu mpaka wakati Wababuloni walipoharibu jiji hilo walikuwa wazao wa Yuda. Lakini hakuna mmoja wao aliyekuwa ndiye Shilo aliyetabiriwa na Yakobo. Shilo humaanisha “Yeye Ambaye [Haki] Ni Yake.” Kiunabii, jina hilo lilielekeza kwa Yesu, mmoja ambaye sasa Ufalme wa Kidaudi ni wake daima.—Ezekieli 21:25-27; Luka 1:32, 33; Ufunuo 19:16.
6. Ni katika njia gani Yesu alikuwa “kitawi” cha Yese na pia “mzizi wa Daudi”?
6 Kwa haraka Yohana anatambua lile rejezo kwa “mzizi wa Daudi.” Mesiya aliyeahidiwa anaitwa kiunabii “kitawi kutoka kisiki cha Yese [baba ya Mfalme Daudi] . . . chipukizi” na pia “mzizi wa Yese ambao utakuwa unasimama kuwa ishara kwa vikundi vya watu.” (Isaya 11:1, 10, NW) Yesu alikuwa kitawi cha Yese, akizaliwa katika mstari wa kifalme wa Daudi, mwana wa Yese. Na zaidi, akiwa mzizi wa Yese, ndiye yule Mmoja ambaye alifanya nasaba ya kifalme ya Kidaudi ichipuke tena, akiipa uhai na lisho milele.—2 Samweli 7:16.
7. Ni nini kinachomstahilisha Yesu kuchukua hati-kunjo kutoka mkono wa Mmoja anayeketi juu ya kiti cha ufalme?
7 Yesu ndiye mmoja ambaye kwa kutokeza sana, akiwa binadamu mkamilifu, alitumikia Yehova katika ukamilifu na chini ya majaribu yenye maumivu makali sana. Yeye alitoa jawabu kamili kwa dai la Shetani. (Mithali 27:11) Hivyo, yeye angeweza kusema kama alivyosema katika ule usiku kabla ya kifo chake cha dhabihu, “mimi nimeshinda ulimwengu.” (Yohana 16:33, NW) Kwa sababu hiyo, Yehova alimwaminisha Yesu aliyefufuliwa “mamlaka yote katika mbingu na juu ya dunia.” Yeye pekee kati ya watumishi wote wa Mungu ndiye aliye na sifa zinazofaa kupokea hati-kunjo, akitazamia kujulisha ujumbe wayo wenye maana kubwa.—Mathayo 28:18, NW.
8. (a) Kwa habari ya Ufalme, ni jambo gani linaloonyesha ustahili wa Yesu? (b) Ni kwa nini inafaa kwamba mmoja wa wale wazee 24 afunulie Yohana yule mtu ambaye anastahili kufungua hati-kunjo?
8 Inafaa kweli kweli kwamba yapasa Yesu afungue hati-kunjo. Tangu 1914 yeye ameketishwa juu ya kiti cha ufalme akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimesiya, na hati-kunjo inafunua mengi sana kuhusu ule Ufalme na utakachotimiza. Kwa uaminifu Yesu alitoa ushuhuda kwa ukweli wa Ufalme alipokuwa hapa duniani. (Yohana 18:36, 37) Yeye alifundisha wafuasi wake wasali juu ya kuja kwa Ufalme huo. (Mathayo 6:9, 10) Yeye alianzisha kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme mwanzoni mwa wakati wa Kikristo na akatoa unabii juu ya kukamilishwa kwa kazi hiyo ya kuhubiri katika pindi ya wakati wa mwisho. (Mathayo 4:23; Marko 13:10) Hali kadhalika, inafaa kwamba yapasa mmoja wa wazee 24 afunulie Yohana kwamba Yesu ndiye mmoja atakayefungua vile vifungo. Kwa nini? Kwa sababu wazee hawa wanakalia viti vya ufalme na huvaa mataji, wakiwa warithi washirika pamoja na Kristo katika Ufalme wake.—Warumi 8:17; Ufunuo 4:4.
‘Mwana-Kondoo Ambaye Alichinjwa’
9. Badala ya simba, Yohana anaona nini kikisimama “katikati ya kiti cha ufalme,” naye alielezaje habari zacho?
9 Yohana anatazama aone huyu “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda.” Lakini inashangaza kama nini! Umbo la ufananisho lililo tofauti kabisa latokea: “Na mimi nikaona akisimama katikati ya kiti cha ufalme na ya viumbe hai wanne na katikati ya wazee mwana-kondoo kana kwamba alikuwa amechinjwa, akiwa na pembe saba na macho saba, macho ambayo humaanisha roho saba za Mungu ambazo zimepelekwa katika dunia kwa ujumla.”—Ufunuo 5:6, NW.
10. Ni nani aliye “mwana-kondoo” ambaye Yohana aliona, na ni kwa nini jina hilo linafaa?
10 Katika kitovu kabisa, kando ya kile kiti cha ufalme, ndani ya duara zilizofanyizwa na wale viumbe hai wanne na wale wazee 24, kuna mwana-kondoo! Bila shaka Yohana anashirikisha kwa haraka huyu mwana-kondoo na “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda” na “mzizi wa Daudi.” Yeye anajua kwamba, zaidi ya miaka 60 mapema, Yohana Mbatizaji alimjulisha Yesu kwa Wayahudi watazamaji kuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29, NW) Wakati wote wa maisha yake duniani, Yesu alibaki bila kutiwa waa na ulimwengu—kama vile mwana-kondoo asiye na ila—ili aweze kutoa uhai wake usio na lawama uwe dhabihu kwa ajili ya aina ya binadamu.—1 Wakorintho 5:7; Waebrania 7:26.
11. Ni kwa nini si utovu wa adhama kumwakilisha Yesu aliyetukuzwa kuwa “mwana-kondoo kana kwamba alikuwa amechinjwa”?
11 Je! kwa vyovyote ni kumfanya mdogo au utovu wa adhama kuwakilisha Yesu aliyetukuzwa kuwa “mwana-kondoo kana kwamba alikuwa amechinjwa”? Sivyo kabisa! Ule uhakika wa kwamba Yesu alibaki akiwa mwaminifu mpaka kifo ulikuwa ushinde mkuu kwa Shetani na ushindi mkubwa wenye shangwe kwa Yehova Mungu. Kumwakilisha Yesu katika njia hii huonyesha waziwazi ushindi wake juu ya ulimwengu wa Shetani na ni kikumbusho cha ule upendo wenye kina walio nao Yehova na Yesu kwa aina ya binadamu. (Yohana 3:16; 15:13; linga Wakolosai 2:15.) Hivyo Yesu anaonyeshwa kuwa ile Mbegu iliyoahidiwa, akiwa na sifa zinazofaa zenye kutokeza kufungua ile hati-kunjo.—Mwanzo 3:15.
12. Zile pembe saba za Mwana-Kondoo hufananisha nini?
12 Ni kitu gani kingine kinachoongeza uthamini wetu kwa huyu “mwana-kondoo”? Ana pembe saba. Pembe katika Biblia mara nyingi huwa ni ufananisho wa nguvu au mamlaka, na saba ingeonyesha utimilifu. (Linga 1 Samweli 2:1, 10; Zaburi 112:9; 148:14.) Kwa sababu hiyo, zile pembe saba za Mwana-Kondoo zawakilisha utimilifu wa nguvu ambazo Yehova ameaminisha Yesu. Yeye yuko “juu sana juu ya kila serikali na mamlaka na nguvu na ubwana na kila jina linaloitwa jina, si katika huu mfumo wa mambo tu, bali pia katika ule unaopasa kuja.” (Waefeso 1:20-23; 1 Petro 3:22, NW) Hasa Yesu ametumia nguvu, nguvu za kiserikali, tangu 1914 wakati Yehova alipomketisha juu ya kiti cha ufalme akiwa Mfalme wa kimbingu.—Zaburi 2:6.
13. (a) Macho saba ya Mwana-Kondoo yanafananisha nini? (b) Mwana-Kondoo anaanza kufanya nini?
13 Zaidi ya hilo, Yesu amejazwa roho takatifu kwa utimilifu, kama inavyofananishwa na yale macho saba ya Mwana-Kondoo, ambayo “humaanisha roho saba za Mungu.” Yesu ni mfereji ambao kupitia huo utimilifu wa kani-tendaji ya Mungu hutiririkia watumishi Wake wa kidunia. (Tito 3:6) Kwa udhahiri, ni kupitia roho ii hii kwamba yeye huona kutoka mbinguni yanayotendeka hapa duniani. Kama Baba yake, Yesu ana utambuzi mkamilifu. Hakuna kitu kinachoponyoka asikione. (Linga Zaburi 11:4; Zekaria 4:10.) Kwa wazi, Mwana huyu—yule mshika ukamilifu aliyeshinda ulimwengu; yule Simba wa kabila la Yuda; ule mzizi wa Daudi; yule mmoja aliyetoa uhai wake kwa ajili ya aina ya binadamu; yule mmoja aliye na mamlaka kamili, utimilifu wa roho takatifu, na utambuzi mkamilifu kutoka kwa Yehova Mungu—ndiyo, huyu mmoja anastahili kwa kutokeza sana kutwaa hati-kunjo kutoka mkono wa Yehova. Je! yeye anasitasita kukubali utume huu wa utumishi katika tengenezo tukufu la Yehova? Hapana! Badala yake, “yeye alienda na mara hiyo akaitwaa [hati-kunjo] kutoka mkono wa kulia wa Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme.” (Ufunuo 5:7, NW) Ni kielelezo kilichoje cha utii wa moyo wa kupenda!
Nyimbo za Sifa
14. (a) Wale viumbe hai wanne na wazee 24 wanatendaje kwa kuitikia kutwaa kwa Yesu hati-kunjo? (b) Ile habari ambayo Yohana anapokea kuhusu wale wazee 24 inathibitishaje utambulisho na cheo chao?
14 Wale wengine mbele ya kiti cha ufalme cha Yehova wanatendaje kwa kuitikia? “Na wakati alipotwaa ile hati-kunjo, wale viumbe hai wanne na wale wazee ishirini na wanne walianguka chini mbele ya Mwana-Kondoo, kila mmoja akiwa na kinubi na mabakuli ya dhahabu yaliyokuwa yamejaa uvumba, na huo uvumba humaanisha sala za watakatifu.” (Ufunuo 5:8, NW) Kama wale viumbe hai wanne wa kikerubi mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu, wazee 24 wanainamia Yesu katika kukiri mamlaka yake. Lakini hao wazee wako peke yao katika kuwa na vinubi na mabakuli ya uvumba.a Na wao peke yao sasa waimba wimbo mpya. (Ufunuo 5:9) Hivyo wanafanana na wale 144,000 wa “Israeli wa Mungu” watakatifu, ambao pia wanabeba vinubi na kuimba wimbo mpya. (Wagalatia 6:16; Wakolosai 1:12; Ufunuo 7:3-8; 14:1-4) Na zaidi, wale wazee 24 wanaonyeshwa wakitimiza utendaji wa kikuhani wa kimbingu, uliofananishwa na ule wa makuhani katika Israeli wa kale ambao walimchomea Yehova uvumba katika ile tabenakulo—utendaji ambao ulikwisha wakati Yehova alipoioondolea mbali ile Sheria ya Musa, akiigongomelea penye nguzo ya mateso ya Yesu. (Wakolosai 2:14) Tunakata neno gani kutokana na haya yote? Kwamba hapa wale washindi wapakwa-mafuta wanaonekana wakiwa katika mgawo wao wa mwisho kabisa wakiwa ‘makuhani wa Mungu na wa Kristo, wakitawala wakiwa wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.’—Ufunuo 20:6, NW.
15. (a) Katika Israeli, ni nani pekee aliyependelewa kuingia ndani ya Patakatifu Zaidi Sana pa ile tabenakulo? (b) Ni kwa nini ilikuwa ni uhai au kifo kwamba kuhani mkuu achome uvumba mbele ya kuingia ndani ya Patakatifu Zaidi Sana?
15 Katika Israeli wa kale, kuhani mkuu pekee ndiye aliyeruhusiwa kuingia Patakatifu Zaidi Sana mbele za kuwapo kwa ufananisho kwa Yehova. Kwake yeye, kupeleka uvumba kulikuwa ni uhai au kifo. Sheria ya Yehova ilisema: “Ni lazima [Haruni] achukue kishika-moto kilichojaa makaa-mawe yenye kuwaka moto kutoka madhabahu mbele za Yehova, na mavungu mawili ya mikono yake yakiwa yamejaa uvumba mzuri uliotiwa manukato, na yeye lazima avilete ndani ya pazia. Ni lazima pia atie uvumba juu ya moto mbele za Yehova, na wingu la uvumba lazima litande juu ya funiko la Arka, lililo juu ya Agano, ili asije akafa.” (Walawi 16:12, 13, NW) Haikuwezekana kuhani mkuu apenye kwa kufaulu ndani ya Patakatifu Zaidi Sana isipokuwa yeye alichoma uvumba.
16. (a) Katika mfumo wa mambo wa Kikristo, ni nani wanaopenya ndani ya Patakatifu Zaidi Sana palipofananishwa? (b) Ni kwa nini Wakristo wapakwa-mafuta sharti ‘wachome uvumba’?
16 Katika mfumo wa mambo wa Kikristo, anayepata kuingia Patakatifu Zaidi Sana palipofananishwa, mahali pa kuwapo kwa Yehova katika mbingu, si Kuhani Mkuu tu aliyefananishwa, yaani, Yesu Kristo, bali hatimaye kila mmoja wa makuhani wa chini 144,000 pia hupata kupaingia. (Waebrania 10:19-23) Mwingio ndani wa hapa Patakatifu Zaidi Sana hauwezekani kwa makuhani hawa, kama wanavyowakilishwa hapa na wale wazee 24, isipokuwa wao ‘wachome uvumba,’ yaani, watoe sala na dua kwa Yehova kwa kuendelea.—Waebrania 5:7; Yuda 20, 21; linga Zaburi 141:2.
Wimbo Mpya
17. (a) Ni wimbo gani mpya wanaoimba wale wazee 24? (b) Usemi huo “wimbo mpya” hutumiwaje kwa kawaida katika Biblia?
17 Sasa wimbo wa kimelodia wasikika. Anaimbiwa Mwana-Kondoo na washiriki wenzake wa kikuhani, wale wazee 24: “Na wao huimba wimbo mpya, kusema: ‘Wewe wastahili kuchukua hati-kunjo na kufungua vifungo vyayo, kwa sababu wewe ulichinjwa na kwa damu yako wewe ulinunua watu kwa ajili ya Mungu kutoka kila kabila na ulimi na kikundi cha watu na taifa.’” (Ufunuo 5:9, NW) Usemi “wimbo mpya” huonekana mara kadhaa katika Biblia na kwa kawaida hurejezea kumsifu Yehova kwa ajili ya tendo fulani hodari la ukombozi. (Zaburi 96:1; 98:1; 144:9) Hivyo, wimbo ni mpya kwa sababu yule mwimbaji sasa anaweza kupiga mbiu za kazi zaidi za ajabu za Yehova na aonyeshe uthamini uliofanywa upya kwa ajili ya jina Lake tukufu.
18. Ni kwa ajili ya nini wazee 24 wanamsifu Yesu wakiwa na wimbo wao mpya?
18 Ingawa hivyo, hapa, wale wazee 24 wanaimba wimbo mpya mbele ya Yesu badala ya mbele za Yehova. Lakini kanuni ni ile ile. Wao wanamsifu Yesu kwa ajili ya vitu vipya ambavyo yeye, akiwa Mwana wa Mungu, amewafanyia. Kwa njia ya damu yake, yeye alipatanisha agano jipya na hivyo akafanya kuwezekane kule kutokezwa kwa taifa jipya likiwa miliki ya pekee ya Yehova. (Warumi 2:28, 29; 1 Wakorintho 11:25; Waebrania 7:18-25) Washiriki wa hili taifa jipya la kiroho walitoka kwa mataifa mengi ya kimnofu, lakini Yesu aliwaunganisha kuwa kundi moja wawe taifa moja.—Isaya 26:2; 1 Petro 2:9, 10.
19. (a) Ni baraka gani ambazo Israeli wa kimnofu walishindwa kupata kwa sababu ya kutoaminika kwao? (b) Taifa jipya la Yehova linapata kufurahia baraka gani?
19 Wakati Yehova alipofanyiza Waisraeli wa kale kuwa taifa huko nyuma katika siku za Musa, yeye alifanya agano pamoja nao na akaahidi kwamba ikiwa wao wangebaki wakiwa waaminifu kwa agano hilo, wao wangekuwa ufalme wa makuhani mbele zake. (Kutoka 19:5, 6) Waisraeli hawakuwa waaminifu na kwa hiyo hawakupata kamwe utimizo wa ahadi hiyo. Kwa upande mwingine, taifa jipya, lililofanyizwa kwa thamani ya agano jipya lenye kupatanishwa na Yesu, limebaki likiwa jaminifu. Basi washiriki walo wanapata kutawala juu ya dunia wakiwa wafalme na pia wanatumikia wakiwa makuhani, wakisaidia wale wenye mioyo inayofaa miongoni mwa aina ya binadamu wapatanishwe kwa Yehova. (Wakolosai 1:20) Ni kama vile ule wimbo mpya unavyoonyesha hilo: “Na wewe ulifanya wao kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao wanapaswa kutawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:10, NW) Hao wazee 24 wana shangwe kama nini katika kuimba huu wimbo mpya wa sifa kwa Yesu Kristo aliyetukuzwa!
Korasi ya Kimbingu
20. Ni wimbo gani wa kusifu Mwana-Kondoo unaovumishwa sasa?
20 Wale wengine wa lile jeshi kubwa mno la kimbingu la tengenezo la Yehova wanaitikiaje huu wimbo mpya: Yohana anasisimuka kuona upatani wao wa kuhisi moyoni: “Na mimi nikaona, na mimi nikasikia sauti ya malaika wengi kuzunguka kiti cha ufalme na viumbe hai na wazee, na nambari yao ilikuwa mamiriadi ya mamiriadi na maelfu ya maelfu, wakisema kwa sauti kubwa: ‘Mwana-Kondoo ambaye alichinjwa anastahili kupokea nguvu na utajiri na hekima na imara na heshima na utukufu na baraka.’” (Ufunuo 5:11, 12, NW) Ni wimbo wa sifa wenye kuvutia kama nini!
21. Je! kusifiwa kwa Mwana-Kondoo kunapunguza enzi kuu au cheo cha Yehova?
21 Je! hii inamaanisha kwamba sasa Yesu amechukua mahali pa Yehova Mungu na kwamba sasa uumbaji wote umegeuka ukaanza kumsifu yeye badala ya Baba yake? Mbali sana na hilo! Badala ya hivyo, huu wimbo wa sifa unapatana na yale aliyoandika mtume Paulo: “Mungu alikweza yeye [Yesu] kwenye cheo cha juu sana na kwa fadhili akampa yeye jina ambalo liko juu ya kila jina jingine, ili kwamba kwa jina la Yesu kila goti lipaswe kupigwa la wale walio katika mbingu na wale walio juu ya dunia na wale walio chinichini ya dunia, na kila ulimi upaswe kukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Wafilipi 2:9-11, NW) Yesu anasifiwa hapa kwa sababu ya sehemu yake katika kumaliza lile suala la msingi lililo mbele ya uumbaji wote—kutetewa kwa uhalali wa enzi kuu ya Yehova. Kweli kweli, ni utukufu ulioje hilo limeletea Baba yake!
Wimbo wa Utukuzo Unaokua
22. Sauti kutoka milki ya kidunia zinajiunga katika wimbo gani wa utukuzo?
22 Katika ile mandhari aliyoieleza Yohana, majeshi ya kimbingu yanamtolea Yesu kigelegele cha kimelodia katika ukiri wa uaminifu wake na mamlaka yake ya kimbingu. Katika hili, wanaungwa na sauti kutoka milki ya kidunia hizo nazo zinaposhiriki kusifu Baba na Mwana pia. Kama vile mambo aliyotimiza mwana wa kibinadamu yanavyoweza kuwaletea sifa wazazi, ndivyo na mwendo wa ushikamanifu wa Yesu unavyotokeza sifa miongoni mwa uumbaji wote “kwa utukufu wa Mungu Baba.” Hivyo, Yohana anaendelea kuripoti hivi: “Na kila kiumbe ambacho kimo katika mbingu na juu ya dunia na chini-chini ya dunia na juu ya bahari, na vitu vyote vilivyo ndani yavyo, mimi nilisikia vikisema: ‘Kwake yule Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme na kwa Mwana-Kondoo kuwe baraka na heshima na utukufu na uweza milele na milele.’”—Ufunuo 5:13, NW.
23, 24. (a) Ni nini kinachoonyesha ni wakati gani wimbo wa utukuzo ungeanza katika mbingu, na wakati gani juu ya dunia? (b) Wimbo wa utukuzo unazidije kukua kadiri miaka inavyopita?
23 Ni wakati gani huu wimbo wa utukuzo unaopita ubora wote unapovuma? Ulianza mapema katika ile siku ya Bwana. Baada ya Shetani na roho waovu wake kutupwa nje ya zile mbingu, “kila kiumbe ambacho kimo katika mbingu” kingeweza kuungana katika huu wimbo wa sifa. Na, kama vile maandishi yanavyoonyesha, tangu 1919 umayamaya unaoendelea kukua duniani umeunganisha sauti zao katika kusifu Yehova, ukiongezeka kutoka maelfu machache mpaka zaidi ya milioni sita kufikia mwaka wa 2005.b Baada ya mfumo wa Shetani wa kidunia kuangamizwa, “kila kiumbe . . . juu ya dunia” kitakuwa kikiimba juu ya sifa za Yehova na Mwana wake. Katika wakati wa Yehova mwenyewe, ufufuo wa yale mamilioni yasiyohesabika ya wafu utaanza, na ndipo “kila kiumbe . . . chinichini ya dunia” ambacho kimo katika kumbukumbu la Mungu kitakuwa na fursa ya kujiunga katika kuimba wimbo wa utukuzo.
24 Tayari, “kutoka miisho ya dunia . . . bahari na . . . visiwa,” mamilioni ya binadamu wanaimba wimbo mpya katika ushirika na tengenezo la Yehova la tufe lote. (Isaya 42:10, Zaburi 150:1-6, NW) Sifa hii yenye shangwe itafikia uvumo wenye sauti kubwa kwenye mwisho wa ile Mileani, wakati aina ya binadamu itakuwa imeinuliwa kufikia ukamilifu. Yule nyoka wa zamani, mdanganyaji mkuu, Shetani mwenyewe, ataangamizwa baada ya hapo katika utimizo kamili wa Mwanzo 3:15, na katika upeo wenye shangwe yenye ushindi, uumbaji wote ulio hai, wa kiroho na wa kibinadamu, utaimba kwa sauti moja: “Kwake yule Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme na kwa Mwana-Kondoo kuwe baraka na heshima na utukufu na uweza milele na milele.” Hakutakuwa na sauti yenye kukaidi katika ulimwengu wote mzima.
25. (a) Kusoma simulizi la Yohana kuhusu wimbo wa utukuzo wa ulimwengu wote mzima kunatuhimiza sisi tufanye nini? (b) Ni kielelezo gani kizuri sana tunachowekewa na viumbe hai wanne na wazee 24 wakati njozi inapoisha?
25 Huo utakuwa wakati wenye shangwe kama nini! Hakika, yale ambayo Yohana anaeleza hapa yanafanya mioyo yetu ifure kwa furaha na yanachochea sisi tujiunge na majeshi ya kimbingu katika kuimbia Yehova Mungu na Yesu Kristo sifa za kuhisi moyoni. Je! sisi hatuazimii zaidi ya wakati mwingine wowote kuvumilia katika kazi zinazofaa? Tukifanya hivyo, sisi tunaweza kutazamia kwamba, kwa msaada wa Yehova, sisi mmoja mmoja tutakuwapo kwenye huo upeo wenye furaha, tukiongeza sauti zetu kwenye korasi hiyo ya sifa ya ulimwengu wote mzima. Kwa hakika, wale viumbe hai wanne wa kikerubi na wale Wakristo wapakwa-mafuta waliofufuliwa wanapatana kabisa, kwa kuwa ile njozi inamalizia kwa maneno haya: “Na viumbe hai wanne wakaenda wakisema: ‘Ameni!’ na wazee wakaanguka chini na wakaabudu.”—Ufunuo 5:14, NW.
26. Inatupasa sisi tuzoee imani katika nini, naye Mwana-Kondoo anajitayarisha kufanya nini?
26 Wewe msomaji mpendwa, na uzoee imani katika dhabihu ya Mwana-Kondoo—‘mmoja anayestahili’—na ubarikiwe katika jitihada zako za unyenyekevu za kumwabudu na kumtumikia Yehova—“yule Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme.” Acha jamii ya Yohana ikusaidie leo iandaapo “kipimo cha ugavi wa chakula [cha kiroho kinachohitajiwa] kwenye wakati unaofaa.” (Luka 12:42, NW) Lakini tazama! Yule Mwana-Kondoo anajitayarisha kufungua vile vifungo saba. Kuna mafumbuo gani yenye kusisimua katika akiba sasa kwa ajili yetu?
[Maelezo ya Chini]
a Kusema kisarufi, usemi “kila mmoja akiwa na kinubi na mabakuli ya dhahabu yaliyokuwa yamejaa uvumba” ungeweza kurejezea wazee na viumbe hai wanne pia. Hata hivyo, muktadha hudhihirisha kwamba usemi huo unarejezea wazee 24 pekee.
b Ona chati kwenye ukurasa 64.
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 86]
-
-
Wana-Farasi Wanne Katika Mwendo!Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 16
Wana-Farasi Wanne Katika Mwendo!
Njozi ya 3—Ufunuo 6:1-17
Habari: Upandaji wa wana-farasi wanne, mashahidi wafia imani walio chinichini ya madhabahu, na siku kubwa ya hasira-jeuri
Wakati wa utimizo: Kuanzia 1914 kufikia uharibifu wa huu mfumo wa mambo
1. Yehova anaonyeshaje Yohana vilivyomo ndani ya hati-kunjo yenye kuvutia ambayo Yesu anafungua?
KATIKA siku hii yenye hatari, je! sisi hatupendezwi sana na “vitu ambavyo lazima vitukie karibuni”? Hakika tunapendezwa, kwa kuwa sisi wenyewe tunahusika! Basi acheni sisi tuandamane na Yohana wakati Yesu anapofungua hati-kunjo yenye kuvutia. Kwa kustaajabisha, Yohana halazimiki kusoma. Kwa nini sivyo? Kwa sababu vitu vilivyomo vinatolewa kwake “kwa ishara” kwa mfululizo wa mandhari zenye nguvu-msukumo, na zinazojaa matendo.—Ufunuo 1:1, 10, NW.
2. (a) Yohana anaona na kusikia nini, na kuonekana kwa kerubi kunadokeza nini? (b) Amri ya huyo kerubi wa kwanza inatolewa kwa nani, na sababu gani wewe unajibu hivyo?
2 Msikilize Yohana wakati Yesu anapofungua kifungo cha kwanza cha hati-kunjo: “Na mimi nikaona wakati Mwana-Kondoo alipofungua mmoja wa vile vifungo saba, na mimi nikasikia mmoja wa wale viumbe hai wanne akisema kwa sauti kama ya ngurumo: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:1, NW) Hii ni sauti ya kerubi wa kwanza. Kuonekana kwake kama simba kungemdokezea Yohana kwamba tengenezo la Yehova litatenda kwa ujasiri katika kutekeleza hukumu Zake za uadilifu. Nayo amri hiyo inatolewa kwa nani? Hangeweza kuwa Yohana, kwa kuwa Yohana alikuwa amekwisha kualikwa ashiriki mandhari hizi za kiunabii. (Ufunuo 4:1) Hiyo “sauti ya ngurumo” inawaita wajitokeze washiriki wengine katika wa kwanza wa ule mfululizo wa vituko vinne vyenye kuamsha.
Farasi Mweupe na Mpandaji Wake Mashuhuri
3. (a) Sasa Yohana anaeleza nini? (b) Kupatana na mifananisho ya Biblia, ni lazima huyo farasi mweupe atoe picha ya nini?
3 Yohana, na pamoja naye ile jamii ya Yohana na waandamani wayo leo, wanapendelewa kuona drama yenye mwendo wa kasi sana! Yohana anasema hivi: “Na mimi nikaona, na, tazama! farasi mweupe; na mmoja aliyeketi juu yake alikuwa na upinde; na taji lilipewa kwa yeye, na yeye akatoka kwenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufunuo 6:2, NW) Ndiyo, katika kujibu sauti yenye mngurumo “Njoo!” farasi mweupe atokea. Katika Biblia, mara nyingi farasi hufananisha vita. (Zaburi 20:7; Mithali 21:31; Isaya 31:1) Farasi huyu, yaelekea ni farasi dume mwenye sura nzuri, anameta kwa weupe unaoonyesha utakatifu usio na ila. (Linga Ufunuo 1:14; 4:4; 7:9; 20:11.) Hiyo inafaa kama nini, kwa kuwa inaonyesha vita iliyo safi na ya uadilifu machoni pa Yehova!—Ona pia Ufunuo 19:11, 14.
4. Ni nani aliye Mpandaji-farasi mweupe? Eleza.
4 Ni nani aliye Mpandaji-farasi huyu? Yeye ana upinde, silaha ya vita ya kushambulia, lakini anapewa pia taji. Wale waadilifu pekee wanaoonekana wakivaa taji katika pindi ya ile siku ya Bwana ni Yesu na ile jamii inayowakilishwa na wale wazee 24. (Danieli 7:13, 14, 27; Luka 1:31-33; Ufunuo 4:4, 10; 14:14)a Haielekei kwamba mshiriki wa kile kikundi cha wazee 24 angeonyeshwa kuwa akipokea taji kwa ustahili wake mwenyewe. Kwa sababu hiyo, huyu mpanda-farasi aliye pekee lazima awe Yesu Kristo na si mwingine. Yohana anamwona katika mbingu wakati ule wa kihistoria wenye maana kubwa katika 1914 wakati Yehova anapotangaza “Mimi, hata mimi, nimeweka mfalme wangu,” na kumwambia kwamba hili ni kwa kusudi la “kwamba mimi nipate kukupa mataifa yawe urithi wako.” (Zaburi 2:6-8, NW)b Hivyo, katika kufungua kile kifungo cha kwanza Yesu anafunua jinsi yeye mwenyewe, akiwa Mfalme ambaye amevikwa taji sasa hivi, anatoka kwenda kupiga vita katika wakati wa Mungu uliowekwa.
5. Mwandikaji wa zaburi anaelezaje habari ya Mpandaji katika njia inayofanana na Ufunuo 6:2?
5 Mandhari hii inapatana vizuri na Zaburi 45:4-7, NW, inayoelekezwa kwa Mfalme aliyeketishwa na Yehova juu ya kiti cha ufalme: “Na katika umaridadi wako songa mbele ukapate fanikio; panda kwa sababu ya ukweli na unyenyekevu na uadilifu, na mkono wa kulia wako utakufunza wewe katika vitu vyenye kuvuvia hofu. Mishale yako ni mikali—chini yako vikundi vya watu vinafuliza kuanguka—katika moyo wa maadui wa mfalme. Mungu ndiye kiti cha ufalme chako kwa wakati usio dhahiri, hata milele; fimbo ya umaliki wako ni fimbo ya unyoofu. Wewe umependa uadilifu na wewe wachukia uovu. Hiyo ndiyo sababu Mungu, Mungu wako, amepaka wewe mafuta ya mchachawo zaidi ya washirika wako.” Akiwa anazoelea elezo hili la kiunabii, Yohana anathamini kwamba linatumika kuhusu utendaji wa Yesu akiwa Mfalme.—Linga Waebrania 1:1, 2, 8, 9.
Kutoka Kwenda Akishinda
6. (a) Ni kwa nini lazima Mpandaji atoke aende akishinda? (b) Ni kupitia miaka ipi upandaji wa ushindi unaendelea?
6 Ingawa hivyo, ni kwa nini lazima huyo Mfalme mvikwa-taji sasa hivi apande hali akienda kwenye vita? Ni kwa sababu umaliki wake unasimamishwa kukiwa na upinzani mkali kutoka kwa yule hasimu mkuu wa Yehova, Shetani Ibilisi, na wale walio juu ya dunia ambao—wakijua au pasipo kujua—wanatumikia makusudi ya Shetani. Uzawa wa Ufalme wenyewe wataka kuwe vita kuu katika mbingu. Akipiga vita kwa jina Mikaeli (linalomaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”), Yesu anamshinda Shetani na roho waovu wake na kuwavurumisha chini kwenye dunia. (Ufunuo 12:7-12) Upandaji wenye ushindi wa Yesu unaendelea kupitia miongo ya kufungua ya siku ya Bwana wakati binadamu wenye mfano wa kondoo wanakusanywa. Ijapokuwa ulimwengu kwa ujumla ungali unalala “katika uwezo wa yule mwovu,” kwa upendo Yesu anaendelea kuchunga ndugu zake wapakwa-mafuta na waandamani wenzao, akisaidia kila mmoja apate ushindi wa imani.—1 Yohana 5:19, NW.
7. Ni ushindi gani ambao Yesu amepata katika miongo ya kwanza-kwanza ya siku ya Bwana, na azimio letu lapasa liwe nini?
7 Yesu amepata ushindi gani mwingine wakati wa miaka 90 na zaidi ya siku ya Bwana? Kuzunguka tufe lote, watu wa Yehova wakiwa mmoja mmoja na wakiwa kundi, wamepatwa na magumu mengi, mikazo, na minyanyaso, inayofanana na ile aliyoieleza mtume Paulo katika kutoa ithibati ya huduma yake. (2 Wakorintho 11:23-28) Mashahidi wa Yehova wamehitaji “nguvu zinazopita zilizo za kawaida,” ili wavumilie, hasa katika sehemu za vita na jeuri. (2 Wakorintho 4:7, NW) Lakini hata katika hali zenye kujaribu zaidi Mashahidi waaminifu wameweza kusema kama alivyosema Paulo: “Bwana alisimama karibu na mimi na akatia nguvu ndani ya mimi, kwamba kupitia mimi kuhubiri kupate kutimizwa kikamili.” (2 Timotheo 4:17, NW) Ndiyo, Yesu alishinda kwa niaba yao. Naye ataendelea kwenda akishinda kwa niaba yetu, maadamu sisi tunaazimia kukamilisha ushindi wetu wa imani.—1 Yohana 5:4.
8, 9. (a) Ni ushindi gani ambao kundi la Mashahidi wa Yehova la pote katika tufe limeshiriki? (b) Ni wapi ambako ukuzi wa Mashahidi wa Yehova umekuwa wenye kutokeza kweli kweli?
8 Kundi la Mashahidi wa Yehova la pote katika tufe limeshiriki ushindi mwingi chini ya mwongozo wa Mfalme walo mwenye kushinda. Kwa kutokeza sana, yeye aliwapa himaya hawa Wanafunzi wa Biblia wasipatwe na utowesho katika 1918, wakati wao wenyewe ‘waliposhindwa’ kwa muda na tengenezo la Shetani la kisiasa. Hata hivyo, katika 1919, alivunja mapingo ya gereza awaache huru, kisha akawahuisha ili wapige mbiu ya habari njema “mpaka kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Ufunuo 13:7; Matendo 1:8, NW.
9 Kabla na wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, yale Mataifa Mhimili ya kidikteta yalijaribu kufutilia mbali Mashahidi wa Yehova katika mabara mengi ambako viongozi wa kidini, hasa mapadri wa Roma Katoliki, walitoa uungaji-mkono wa waziwazi au usio wa waziwazi kwa madikteta waonezi. Lakini Mashahidi 71,509 waliokuwa wakihubiri wakati vita ilipoanza katika 1939 wakawa 141,606 kufikia mwisho wayo katika 1945, hata ingawa zaidi ya 10,000 walikuwa wametumia miaka mirefu katika magereza na kambi za mateso, na 2,000 hivi walikuwa wameuawa. Hesabu ya Mashahidi watendaji duniani pote imepanuka kuwa zaidi ya milioni sita leo. Ukuzi umekuwa wenye kutokeza katika mabara ya Kikatoliki na katika nchi ambako minyanyaso ilikuwa mikali zaidi sana—kama Ujeremani, Italia, na Japani, ambamo Mashahidi wanaripoti jumla ya wahudumu wa shamba watendaji zaidi ya 600,000.—Isaya 54:17; Yeremia 1:17-19.
10. Ni kwa ushindi gani yule Mfalme mwenye kushinda amebariki watu wake “katika kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema”?
10 Mfalme wetu mwenye kushinda amebariki pia watu wake wenye bidii kwa kuwaongoza kwenye ushindi mwingi “katika kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema” katika mahakama ya sheria na mbele ya watawala. (Wafilipi 1:7; Mathayo 10:18; 24:9, NW) Hiyo imekuwa katika mataifa yote—katika Australia, Ajentina, Kanada, Ugiriki, India, Swazilandi, Swizalandi, Uturuki na mabara mengineyo. Miongoni mwa ushindi mbalimbali 50 wa kisheria waliopata Mashahidi wa Yehova katika Mahakama Kuu Zaidi Sana ya United States umekuwa ule unaohakikishia haki ya kujulisha wazi habari njema “peupe na nyumba kwa nyumba” na kutofanya sherehe za kuabudu sanamu za kizalendo. (Matendo 5:42; 20:20, NW; 1 Wakorintho 10:14) Hivyo, njia imeachwa wazi kwa ajili ya kupanua kazi ya kutoa ushahidi katika tufe lote.
11. (a) Yule Mpandaji ‘anakamilishaje ushindi wake’? (b) Kufunguliwa kwa kifungo cha pili, cha tatu, na cha nne kwapasa kuwe na tokeo gani juu yetu?
11 Yesu ‘anakamilishaje ushindi wake’?c Yeye anafanya hivyo, kama tutakavyoona, kwa kukomesha dini bandia na kisha kuvurumisha kila kisehemu kinachobaki cha tengenezo linaloonekana la Shetani ndani ya “ziwa la moto” la ufananisho wa uharibifu, katika kutetea enzi kuu ya Yehova. Kwa uhakika, sasa sisi tunatazamia siku hiyo kwenye Har–Magedoni wakati “Mfalme wa wafalme” wetu atajipatia ushindi juu ya tengenezo la Shetani la kisiasa lenye uonevu! (Ufunuo 16:16; 17:14; 19:2, 14-21; Ezekieli 25:17) Kwa wakati uliopo, Mshindi huyo asiyeshindika akiwa juu ya farasi mweupe anaendelea kupanda akisonga mbele kadiri Yehova anavyoongeza watu wenye mioyo minyofu kwenye taifa Lake lenye uadilifu duniani. (Isaya 26:2; 60:22) Je! wewe unashiriki pamoja na jamii ya Yohana iliyopakwa mafuta katika upanuzi huo wa Ufalme wenye shangwe? Ikiwa ndivyo, anachoona Yohana wakati vile vifungo vitatu vinavyofuata vinapofunguliwa bila shaka kitakuchochea wewe kwenye ushiriki mkubwa hata zaidi katika kazi ya Yehova kwa ajili ya siku hii.
Ona, Farasi wa Rangi-Moto!
12. Yesu alisema ni nini kingetia alama kuwapo kwake kusikoonekana akiwa Mfalme?
12 Kuelekea mwisho wa huduma ya Yesu duniani, wanafunzi wake walimuuliza faraghani hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Katika kujibu, yeye alitabiri maafa ambayo yangekuwa “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu.” Akasema Yesu: “Taifa litainuka dhidi ya taifa, na ufalme dhidi ya ufalme; na kutakuwa na matetemeko ya dunia makubwa, na katika mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kipuku na upungufu wa chakula; na kutakuwa na maono ya kutia hofu na kutoka mbinguni ishara kubwa.” (Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:10, 11, NW) Vitu ambavyo Yohana anaona wakati vifungo vinavyobaki vya hati-kunjo vinapofunguliwa huandaa ulingano wa kustaajabisha wa unabii huo. Angalia sasa Yesu aliyetukuzwa afunguapo kifungo cha pili!
13. Ni tofauti gani inayokaribia kuwa wazi kwa Yohana?
13 “Na wakati yeye alipofungua kifungo cha pili, mimi nikasikia kiumbe hai wa pili akisema: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:3, NW) Ni yule kerubi wa pili, aliye na mwonekano wa fahali, anayetoa amri. Hapa nguvu ndiyo sifa inayofananishwa, lakini ni nguvu iliyotumiwa kwa uadilifu. Ingawa hivyo, kwa kutofautisha, sasa Yohana ataona wonyesho wenye kukirihisha sana wa nguvu, wenye kuleta kifo.
14. Ni farasi na mpandaji gani anayefuata kuonwa na Yohana, nayo njozi hii inatoa picha ya nini?
14 Basi, mwito huu “Njoo!” unajibiwaje? Katika njia hii: “Na mwingine akatokea, farasi wa rangi-moto; na yule mmoja aliyeketi juu yake alipewa ruhusa ya kuondolea mbali amani kutoka dunia ili wao wapaswe kuchinja mmoja na mwenzake; na upanga mkubwa akapewa yeye.” (Ufunuo 6:4, NW) Ni njozi ya kutia hofu kweli kweli! Na hakuna shaka juu ya inachotolea picha: vita! Si vita ya uadilifu, yenye ushindi wa Mfalme wa Yehova mwenye kushinda bali ni vita yenye ukatili ya kimataifa, yenye kufanyizwa na binadamu, yenye umwagaji-damu na maumivu ya bure. Inafaa kama nini kwamba mpandaji huyu anampanda farasi wa rangi-nyekundu kama moto!
15. Ni kwa nini haitupasi sisi tutake sehemu yoyote ya upandaji wa yule mwana-farasi wa pili?
15 Kwa hakika, Yohana hangetaka sehemu yoyote ya mwana-farasi na upandaji wake wenye haraka isiyo na akili, kwa kuwa unabii ulitolewa kuhusu watu wa Mungu hivi: “Wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Ingawa wangali “katika ulimwengu,” Yohana na, kwa upanuzi, ile jamii ya Yohana na umati mkubwa leo wao “si sehemu” ya huu mfumo wenye madoa ya damu. Silaha zetu ni za kiroho na “zinajaa nguvu kwa njia ya Mungu” kwa ajili ya kupiga mbiu ya ukweli kwa bidii, bila vita ya kimwili.—Yohana 17:11, 14; 2 Wakorintho 10:3, 4, NW.
16. Ni lini na jinsi gani mpandaji-farasi mwekundu alipewa “upanga mkubwa”?
16 Kulikuwa kumekuwa na vita vingi kabla ya 1914, ule mwaka Mpandaji-farasi mweupe alipopokea taji lake. Lakini sasa mpandaji-farasi mwekundu anapewa “upanga mkubwa.” Hiyo inadokeza nini? Kwa mlipuko wa Vita ya Ulimwengu 1, vita vya binadamu vimekuwa vyenye umwagaji-damu mwingi zaidi, vyenye uharibifu mwingi zaidi ya vilivyopata kuwa kabla ya hapo. Wakati wa mwosho-damu wa 1914-18, matanki, gesi zenye sumu, eropleni, sabmarini, mizinga mikubwa, na silaha za otomatiki zilitumiwa ama kwa mara ya kwanza ama kwa kadiri isiyotangulia kufanywa. Katika mataifa yapata 28, idadi ya watu wa nchi kwa ujumla, si wale tu ambao kazi yao ya maisha ni askari-jeshi, walisukumizwa kwenye jitihada za vita. Majeruhi walikuwa kadiri ya kuogopesha. Askari-jeshi zaidi ya milioni tisa walichinjwa, na majeruhi ya raia walikuwa wengi mno. Hata ilipokwisha vita, hakukuwa na kurudia amani halisi duniani. Zaidi ya miaka 50 baada ya vita, Konrad Adenauer waziri wa serikali Mjeremani alitoa elezo hili: “Usalama na utulivu vimetoweka katika maisha ya watu tangu 1914.” Kweli kweli yule mpandaji-farasi wa rangi-moto alipewa ruhusa aondolee mbali amani duniani!
17. Utumizi wa huo “upanga mkubwa” umeendeleaje, kufuata Vita ya Ulimwengu 1?
17 Halafu, kiu yake ya kutaka kuona damu ikimwagwa ikiwa imechochewa, yule mpandaji-farasi mwekundu alijitumbukiza ndani ya Vita ya Ulimwengu 2. Zana za uchinjaji zilizidi kuwa za kishetani zaidi, nayo majeruhi yakapanda juu kuwa mara nne ya yale ya Vita ya Ulimwengu 1. Katika 1945 bomu mbili za atomu zililipuka juu ya Japani, kila mojapo ilifutilia mbali—kwa dharuba moja—makumi ya maelfu ya majeruhi. Katika pindi ya vita ya pili ya ulimwengu, yule mpandaji-farasi mwekundu alivuna mavuno makubwa ya maisha zapata milioni 55, na hata wakati huo yeye hakutosheka. Imeripotiwa kwa njia yenye kuaminika kwamba nafsi zaidi ya milioni 20 zimeanguka chini ya ule “upanga mkubwa” tangu Vita ya Ulimwengu 2.
18, 19. (a) Badala ya huo kuwa ushindi wenye shangwe wa tekinolojia ya kivita, lile chinjo tangu Vita ya Ulimwengu 2 ni uhakika wa ushuhuda gani? (b) Ni hatari gani inayokabili aina ya binadamu, lakini yule Mpandaji-farasi mweupe atafanya nini kuisawazisha?
18 Je! sisi tungeweza kuita huu kuwa ushindi wenye shangwe wa tekinolojia ya kivita? Badala ya hivyo, huo ni ushuhuda wa kwamba yule farasi mwekundu asiye na rehema yuko katika mwendo. Na mwendo huo utaishia wapi? Baadhi ya wanasayansi wanasema kwamba kuna uwezekano wa vita ya nyukilia kutokea kiaksidenti—achia mbali mteketezo mkubwa wa kinyukilia uliopangwa! Lakini kwa furaha yule Mpandaji-farasi mweupe mwenye kushinda ana fikira tofauti juu ya jambo hili.
19 Maadamu msingi wa jamii ya watu ni kiburi cha kitaifa na chuki, lazima aina ya binadamu iendelee kukalia kipipa cha hatari ya nyukilia. Hata kama mataifa yangekwangulia mbali silaha zayo za nyukilia kwa kutamauka, yangebaki na huo ujuzi. Kwa muda mfupi sana, wangeunda tena vidude vyao vya nyukilia vya uuaji-makusudi; kwa sababu hiyo, vita yoyote ikitumia silaha za kadiri ingevuvumuka upesi kama uyoga na kuwa maangamizi makubwa. Kile kiburi na chuki inayofunika mataifa leo lazima viongoze kwenye ujiuaji wa binadamu, isipokuwa—aha, ndiyo, isipokuwa yule Mpandaji-farasi mweupe ageuzie mbali mwendo wa kichaa wa yule mpandwaji wa rangi-moto. Acheni sisi tuwe na uhakika kwamba Kristo Mfalme atapanda, ili akamilishe ushindi wake juu ya ulimwengu wenye kudhibitiwa na Shetani na pia ili asimamishe jamii mpya ya kidunia ambayo msingi wayo ni upendo—upendo kwa Mungu na kwa jirani—kani kwa ajili ya amani, iliyo ya juu zaidi ya ile yenye kutikisika ya mazuio ya vita ya nyakati zetu zenye kichaa.—Zaburi 37:9-11; Marko 12:29-31; Ufunuo 21:1-5.
Farasi Mweusi Aruka Kuja Mbele
20. Sisi tuna uhakikisho gani kwamba Mpandaji-farasi mweupe ataiweza hali yoyote yenye balaa?
20 Yesu anafungua sasa kifungo cha tatu! Yohana, unaona nini? “Na wakati yeye alipofungua kifungo cha tatu, mimi nikasikia kiumbe hai wa tatu akisema: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:5a, NW) Kwa furaha kerubi huyu wa tatu “ana uso kama wa binadamu,” kuonyesha sifa ya upendo. Upendo wenye kuongozwa na kanuni utakuwa mwingi sana katika ulimwengu mpya wa Mungu, hata kama vile sifa hiyo nzuri sana inavyoenea katika tengenezo lote la Yehova leo. (Ufunuo 4:7; 1 Yohana 4:16) Sisi tunaweza kuwa na hakika kwamba Mpandaji-farasi mweupe, ambaye “lazima atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka maadui wote chini ya nyayo zake,” kwa upendo ataondoa ile hali yenye maafa ambayo inafuata kuletwa kwenye uchunguzi wa Yohana.—1 Wakorintho 15:25, NW.
21. (a) Ni nini kinachotolewa picha na yule farasi mweusi na mpandaji wake? (b) Ni nini kinachothibitisha kwamba huyo farasi mweusi angali katika mwendo wake wenye ukali?
21 Basi, Yohana anaona nini, wakati ule mwito wa tatu “Njoo!” unapojibiwa? “Na mimi nikaona, na, tazama! farasi mweusi ti; na mmoja aliyeketi juu yake alikuwa na jozi ya mizani katika mkono wake.” (Ufunuo 6:5b, NW) Njaa tupu! Huo ndio ujumbe wa kutisha wa mandhari hii ya kiunabii. Unaelekeza mbele kwenye hali za mapema katika siku ya Bwana wakati lazima chakula kipimwe kwa mizani. Tangu 1914 njaa imekuwa tatizo la ulimwenguni pote lenye kuendelea. Vita vya ki-siku-hizi huleta njaa ikifuatana navyo, kwa kuwa rasilimali ambazo kwa kawaida hutumiwa kulisha watu wenye njaa mara nyingi hugeuzwa na kutumiwa kutoa ugavi wa silaha za vita. Wafanya kazi wa mashamba wanaingizwa jeshini kwa nguvu, nazo sera zinazokataza kulima nyanja zenye makovu ya vita na dunia iliyounguzwa hupunguza uzalishaji wa chakula. Hiyo ilikuwa kweli kama nini wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, mamilioni yalipotaabishwa na njaa na wakafa! Zaidi ya hilo, yule mpandaji-farasi mweusi wa njaa hakuacha ilipoisha vita. Wakati wa muda wa tangu 1930, milioni tano walipotea katika njaa moja tu katika Ukraine. Ile vita ya pili ya ulimwengu ilileta pamoja nayo upungufu zaidi wa chakula na njaa. Kadiri yule farasi mweusi alivyoendelea na mwendo wake, Baraza la Chakula Ulimwenguni liliripoti katikati ya 1987 kwamba binadamu milioni 512 walikuwa wakifa njaa na kwamba watoto 40,000 wanakufa kila siku kwa visababishi vinavyohusiana na njaa.
22. (a) Sauti inasema nini, ikionyesha uhitaji gani? (b) Ni jambo gani linalodokezwa na bei ya kwarti moja ya ngano na kwarti tatu za shayiri?
22 Je! Yohana ana zaidi ya kutuambia sisi: “Na mimi nilisikia sauti kana kwamba ni katikati ya viumbe hai wanne ikisema: ‘Kwarti moja ya ngano kwa dinari moja, na kwarti tatu za shayiri kwa dinari moja; na usidhuru mafuta ya zeituni na divai.’” (Ufunuo 6:6, NW) Makerubi wote wanne wana umoja katika kuonyesha uhitaji wa kulinda ugavi wa chakula kwa uangalifu—kama vile watu walikuwa hawana budi ‘kula chakula kwa uzani na katika ujalifu wenye wasiwasi’ kabla ya uharibifu wa Yerusalemu katika 607 K.W.K. (Ezekieli 4:16, NW) Katika wakati wa Yohana, kwarti ya ngano ilihesabiwa kuwa ndiyo posho ya kila siku ya askari-jeshi. Posho kama hiyo ingegharimu kiasi gani? Dinari moja—mshahara wa siku nzima! (Mathayo 20:2)d Namna gani kama mtu alikuwa na jamaa? Basi, badala ya hiyo yeye angeweza kununua kwarti tatu za shayiri isiyosafishwa. Hata hiyo ingeweza kulisha jamaa ndogo tu. Na shayiri haikuonwa kuwa chakula bora kama vile ngano.
23. Ni nini kinachodokezwa na taarifa, “Usidhuru mafuta ya zeituni na divai”?
23 Ni nini kinachodokezwa na taarifa, “Usidhuru mafuta ya zeituni na divai”? Wengine wameiona kuwa ikimaanisha kwamba ingawa wengi wangepungukiwa na chakula na hata wafe njaa, vitu vya anasa vya matajiri havingedhuriwa. Lakini katika Mashariki ya Kati, mafuta na divai si vitu vya anasa kwa kweli. Katika nyakati za Biblia, mkate, mafuta, na divai vilionwa kuwa chakula kikuu. (Linga Mwanzo 14:18; Zaburi 104:14, 15.) Sikuzote maji hayakuwa safi, kwa hiyo divai ilitumiwa sana kwa kunywa na nyakati nyingine kwa makusudi ya kitiba. (1 Timotheo 5:23) Kwa habari ya mafuta, katika siku ya Eliya mjane wa Sarepta, ajapokuwa maskini, bado alikuwa amebakiza mafuta kiasi fulani ya kupikia unga wake uliobaki. (1 Wafalme 17:12) Kwa hiyo, amri “usidhuru mafuta ya zeituni na divai” inaonekana kuwa shauri la kutotumia bidhaa hizo za msingi kwa uharaka mno lakini kuzitumia kwa kulimbika. La sivyo, ‘zitadhuriwa,’ yaani, zitakwisha kabla ya njaa kwisha.
24. Ni kwa nini farasi mweusi hataendelea na mwendo wake kwa muda zaidi ulio mrefu?
24 Jinsi tunavyoweza kuwa na furaha kwamba yule Mpandaji-farasi mweupe karibuni atazuia kwa hatamu mwendo wa farasi huyo mweusi! Kwa maana imeandikwa kuhusu uandalizi Wake wa upendo kwa ajili ya ulimwengu mpya hivi: “Katika siku zake mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi uwe haupo tena. . . . Kutakuja kuwa na utele wa nafaka juu ya dunia; juu ya kilele cha milima kutakuwa na mfuriko.”—Zaburi 72:7, 16, NW; ona pia Isaya 25:6-8.
Farasi Rangi Nyeupe-Nyeupe na Mpandaji Wake
25. Wakati Yesu anapofungua kifungo cha tatu, Yohana anasikia sauti ya nani, na hiyo inaonyesha nini?
25 Hadithi haijaisha kabisa kusimuliwa. Yesu anafungua kifungo cha nne, naye Yohana anatusimulia tokeo: “Na wakati yeye alipofungua kifungo cha nne, mimi nikasikia sauti ya kiumbe hai wa nne ikisema: ‘Njoo!’” (Ufunuo 6:7, NW) Hii ni sauti ya kerubi anayeshabihi tai arukaye. Hekima yenye kuona mbali ndiyo inayoonyeshwa hapa, na kweli kweli Yohana, jamii ya Yohana, na wengine wote wa watumishi wa Mungu duniani wamehitaji kuona na kutenda kwa muono-ndani kwa sababu ya kinachoonyeshwa na picha hapa. Kwa kufanya hivyo, sisi tunaweza kupata kadiri fulani ya himaya tusipatwe na mapigo yanayosumbua wenye hekima ya kilimwengu wa kizazi cha leo chenye kiburi na utovu wa maadili.—1 Wakorintho 1:20, 21.
26. (a) Mwana-farasi wa nne ni nani, na ni kwa nini rangi ya farasi wake inafaa? (b) Ni nani anayemfuata mwana-farasi wa nne, na ni nini kinachopata majeruhi wake?
26 Basi, ni hofu gani mpya zinazoachiliwa, wakati mwana-farasi wa nne anapoitikia mwito? Yohana anatusimulia hivi: “Na mimi nikaona, na, tazama! farasi rangi nyeupe-nyeupe; na mmoja aliyeketi juu yake alikuwa na jina Kifo. Na Hadesi alikuwa akifuata yeye karibu-karibu.” (Ufunuo 6:8a, NW) Mpandaji-farasi wa mwisho ana jina: Kifo. Ni yeye pekee kati ya hao wana-farasi wanne wa Apokalipsi ambaye amefunua jina lake hivyo moja kwa moja. Kwa kufaa, Kifo hupanda farasi ambaye ni rangi nyeupe-nyeupe, kwa kuwa neno -eupe-eupe (Kigiriki, khlo·rosʹ) hutumiwa katika fasihi za Kigiriki kueleza nyuso ambazo zimefanywa kuwa nyeupe, kana kwamba kwa kifo. Pia kwa kufaa, Kifo kinafuatwa karibu-karibu na Hadesi (kaburi kwa ujumla) kwa njia fulani isiyoelezwa, kwa kuwa Hadesi hupokea ndani yake idadi iliyo kubwa zaidi ya wale wanaokuwa majeruhi wa mikumbo ya huyo mwana-farasi wa nne. Kwa furaha, kwa hao kutakuwako ufufuo, wakati ‘kifo na Hadesi vinapotoa wafu walio ndani yavyo.’ (Ufunuo 20:13, NW) Lakini Kifo kinadaije hao majeruhi?
27. (a) Mpandaji Kifo anadaije majeruhi wake? (b) Ni nini kinachomaanishwa na “sehemu ya nne ya dunia” ambayo juu yayo Kifo ana mamlaka?
27 Njozi inataja baadhi ya njia hizo: “Na wao walipewa mamlaka juu ya sehemu ya nne ya dunia, kuua kwa upanga mrefu na kwa upungufu wa chakula na kwa tauni yenye kufisha na kwa hayawani-mwitu wa dunia.” (Ufunuo 6:8b, NW) La, hasha, si sehemu ya nne halisi ya idadi ya watu wa dunia lakini fungu kubwa la dunia, iwe inasongamana watu au inakaliwa na wachache, ingeathiriwa na upandaji huu. Mwana-farasi huyu anavuna majeruhi ya ule upanga mkubwa wa mwana-farasi wa pili na njaa na upungufu wa chakula wa yule wa tatu. Vilevile, anavuna vuno lake mwenyewe kutokana na tauni yenye kufisha na pia vuno kutokana na matetemeko ya dunia, kama inavyoelezwa kwenye Luka 21:10, 11, NW.
28. (a) Kumekuwaje na utimizo wa unabii kuhusu “tauni yenye kufisha”? (b) Watu wa Yehova wamepewaje himaya juu ya magonjwa mengi leo?
28 Lenye umaana wa kisasa hapa ni “tauni yenye kufisha.” Kufuata mikumbo ya Vita ya Ulimwengu 1, homa-mafua ya Hispania ilivuna maisha za binadamu milioni 20 katika miezi michache tu ya 1918-19. Eneo pekee duniani lililoepuka pigo hili ni kisiwa kidogo cha St. Helena. Katika mahali ambako idadi ya watu waliuawa sana na ugonjwa huu marundo ya kuni za maziko yaliwashwa ili kuchoma maiti chunguchungu. Na leo kuna tukio lenye kuogofya la ugonjwa wa moyo na kansa, na chenye kuyasababisha sana ni uchafuzi wa tumbako. Katika kile kilichoelezwa kuwa “mwongo wenye sura mbaya” wa miaka ya 1980, njia ya maisha ambayo ni ya uasi wa sheria kulingana na viwango vya Biblia iliongeza lile pigo la UKIMWI kwa ile “tauni yenye kufisha.” Katika mwaka wa 2,000, iliripotiwa kwamba daktari mkuu wa Marekani alisema kwamba “huenda [UKIMWI] ndio ugonjwa mbaya zaidi wenye kuambukiza uliopata kutokea ulimwenguni.” Alisema kwamba watu milioni 52 ulimwenguni pote walikuwa na virusi vya UKIMWI, na milioni 20 kati yao tayari walikuwa wamekufa. Jinsi watu wa Yehova walivyo wenye shukrani kwamba lile shauri la hekima la Neno lake linawaepusha na uasherati na tumizi baya la damu, ambalo kupitia kwalo magonjwa mengi sana yanapitishwa leo!—Matendo 15:28, 29, NW; linga 1 Wakorintho 6:9-11.
29, 30. (a) Kungekuwa na tumizi gani leo la yale ‘matendo manne yenye kudhuru’ ya Ezekieli 14:21? (b) Sisi tuelewe nini kwa usemi “hayawani-mwitu” wa Ufunuo 6:8? (c) Ni nini linaloonekana kuwa jambo kuu la mandhari hiyo ya kiunabii?
29 Njozi ya Yohana hutaja hayawani-mwitu kuwa kisababishi cha nne cha kifo cha mapema. Kweli kweli, hivyo vitu vinne vilivyoonyeshwa kwa kufunguliwa kwa kifungo cha nne—vita, njaa, ugonjwa, na hayawani-mwitu—vilionwa katika nyakati za kale kuwa visababishi vikuu vya kifo cha mapema. Hivyo vingetangulia kuweka kivuli cha visababishi vyote vya kifo cha mapema leo. Ni kama vile Yehova alivyoonya Israeli: “Ndivyo, vilevile, itakuwa wakati kutakuwa matendo yangu manne yenye kudhuru ya hukumu—upanga na njaa na hayawani-mwitu wenye kudhuru na ugonjwa wa kipuku—ambayo mimi hakika nitapeleka juu ya Yerusalemu ili kukatilia mbali kutoka hilo mwanadamu wa dunia na mnyama wa nyumbani.”—Ezekieli 14:21, NW.
30 Si mara nyingi ambapo vifo vinavyoletwa na hayawani-mwitu vimekuwa vichwa vikuu magazetini katika nyakati za ki-siku-hizi, ingawa katika nchi za kitropiki wanyama-mwitu wamezidi kudai majeruhi. Katika wakati ujao, huenda wakadai hata zaidi ikiwa mabara yanaachwa ukiwa kwa sababu ya vita au watu wanadhoofishwa mno na njaa wasiweze kufukuzia mbali wanyama wenye njaa. Kwa kuongezea, kuna binadamu wengi sana leo ambao, kama wanyama wasiofikiri, wanaonyesha mielekeo ya kihayawani tofauti kabisa na ile inayoelezwa kwenye Isaya 11:6-9. Watu hawa ndio sana sana walio na daraka la mweneo wa pote katika tufe wa uhalifu unaohusiana na ngono, uuaji-makusudi, uvamizi-haramu, na milipuko ya mabomu katika ulimwengu wa ki-siku-hizi. (Linga Ezekieli 21:31; Warumi 1:28-31; 2 Petro 2:12.) Yule mwana-farasi wa nne huvuna majeruhi wao vilevile. Kweli kweli, jambo kuu la mandhari hii ya kiunabii linaonekana kuwa kwamba yule mpandaji-farasi rangi nyeupe-nyeupe huvuna kwa njia nyingi kifo cha mapema cha aina ya binadamu.
31. Ijapokuwa mikumbo inayosababishwa na wale wapandaji-farasi mwekundu, mweusi, na mweupe-mweupe, ni kwa sababu gani sisi tunaweza kutiwa moyo?
31 Ile habari iliyofunuliwa kwa kufunguliwa vile vifungo vinne vya kwanza hutumainisha sisi kwa sababu inatufundisha kutotamaushwa na vita, njaa, magonjwa, na visababishi vingine vya kifo cha mapema ambavyo vinaenea sana leo; wala haitupasi kupoteza tumaini kwa sababu viongozi wa kibinadamu wameshindwa kutatua matatizo ya sasa. Ikiwa hali za ulimwengu zinaifanya iwe wazi kwamba wale wapandaji-farasi mwekundu, mweusi, na rangi nyeupe-nyeupe wako kotekote, usisahau kwamba Mpandaji-farasi mweupe alikuwa wa awali kuanza upandaji wake. Yesu amekuwa Mfalme, na tayari yeye ameshinda kwa kadiri ya kumtupa Shetani nje ya mbingu. Ushindi wake mwingine mbalimbali unatia ndani kukusanywa kwa mabaki ya wana wa Israeli wa kiroho na umati mkubwa wa kimataifa, unaofikia hesabu ya mamilioni, ili wakaokolewe kupitia ile dhiki kubwa. (Ufunuo 7:4, 9, 14) Upandaji wake lazima uendelee mpaka akamilishapo ushindi wake.
32. Ni nini kinachotofautisha kufunguliwa kwa kila kimoja cha vifungo vinne vya kwanza?
32 Kufunguliwa kwa kila kimoja cha hivyo vifungo vya kwanza kumefuatwa na ule mwito: “Njoo!” Kila wakati, farasi na mpandaji wake walitoka wakiwa katika mwendo. Kuanzia na kifungo cha tano, sisi hatusikii tena mwito kama huo. Lakini wana-farasi hao wangali wanapanda, nao wataendelea katika mwendo muda wote wa huu umalizio wa mfumo wa mambo. (Linga Mathayo 28:20.) Ni matukio gani mengine yenye maana kubwa ambayo Yesu anafunua anapofungua vifungo vitatu vinavyobaki? Baadhi ya matukio ni yasiyoonekana na macho ya kibinadamu. Mengine, ingawa ni yenye kuonekana, bado ni ya wakati ujao. Hata hivyo, utimizo wayo ni hakika. Acheni sisi tuone ni matukio gani hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Hata hivyo, angalia kwamba “mwanamke” wa Ufunuo 12:1 ana “taji la nyota kumi na mbili” la kitamathali.
b Kupata ithibati yenye maelezo mengi ya kwamba Yesu aliingia katika Ufalme wake katika 1914, ona ukurasa wa 215-218 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
c Ingawa tafsiri nyingi hufasiri fungu hili la maneno “kushinda” (Swahili Union Version, Revised Standard, The New English Bible, King James Version) “akiwa amenuia kupata ushindi” (Phillips, New International Version), tumizi hapa la namna ya kitenzi katika Kigiriki asilia bila kuonyesha kukamilika au muda wa tendo hutoa maana ya ukamilisho au mwisho kabisa. Kwa sababu hiyo, Word Pictures in the New Testament cha Roberts hutoa elezo hili: “Kitenzi-wakati hapa cha kutoonyesha kukamilika au muda wa tendo huelekeza kwenye ushindi wa mwisho kabisa.”
d Ona New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
[Picha katika ukurasa wa 92]
Yule Mfalme Apanda kwa Ushindi
Katika Miaka ya 1930 na 1940, maadui wenye kujikaza walijaribu kufanya ionekane kwamba huduma ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa haramu, yenye uhalifu, au hata yenye kufitini serikali. (Zaburi 94:20) Katika mwaka 1936 pekee, kulikuwako kutiwa mbaroni kulikorekodiwa 1,149 katika United States. Mashahidi walipiga vita ya kesi za kisheria mwendo wote kufikia ile Mahakama Kuu Zaidi Sana, na ufuatao ni baadhi ya ushindi wao mbalimbali wenye kutokeza.
Katika Mei 3, 1943, Mahakama Kuu Zaidi Sana katika kesi ya Murdock v. Pennsylvania iliamua kwamba Mashahidi hawakuhitaji leseni ili waangushe vitabu kwa pesa. Siku iyo hiyo, ule uamuzi katika kesi ya Martin v. City of Struthers ulishikilia kwamba si kinyume cha sheria kupiga kengele ya mlango wakati wa kushiriki kugawa karatasi na vitu vingine vya kuvumisha habari.
Katika Juni 14, 1943, Mahakama Kuu Zaidi Sana iliamua katika kesi ya Taylor v. Mississippi kwamba Mashahidi hawakutia moyo utovu wa ushikamanifu kwa serikali kwa kuhubiri kwao. Siku iyo hiyo, katika kesi ya West Virginia State Board of Education v. Barnette, Mahakama hiyo ilishikilia kwamba baraza la shule halikuwa na haki ya kufukuza kutoka shuleni watoto wa Mashahidi wa Yehova waliokataa kusalimu bendera. Kesho yake yenyewe, Mahakama Kuu ya Australia iliyojaa iliondoa marufuku ambayo nchi hiyo iliwekea Mashahidi wa Yehova, hiyo ikitangazwa kuwa “isiyo ya haki, bila sababu nzuri na yenye uonevu.”
[Picha katika ukurasa wa 94]
“Alipewa Ruhusa Kuondolea Mbali Amani Kutoka Dunia”
Tekinolojia inaongoza wapi? The Globe and Mail, Toronto, Kanada, Januari 22, 1987, iliripoti yafuatayo kutokana na hotuba ya Ivan L. Head, msimamizi wa International Development Research Centre:
“Inakadiriwa kwa njia yenye kutegemeka kwamba mmoja wa kila wanasayansi na wanatekinolojia wanne katika ulimwengu wanaofanya utafiti na usitawishi anafanya kazi ya kuunda silaha. . . . Kwa makadirio ya 1986, gharama ni zaidi ya dola milioni 1.5 kwa dakika. . . . Je! sisi sote ni wenye usalama zaidi kama tokeo la mkazo wa aina hii ya tekinolojia? Silaha za nyukilia yalizo nazo yale mataifa yenye nguvu zaidi zina kani ya baruti ya zana zote za vita zilizotumiwa na wapiganaji wote katika Vita ya Ulimwengu 2 yote—mara 6,000. Vita ya Ulimwengu 2 elfu sita. Tangu 1945, kumekuwa na [muda] ulio punde ya majuma saba wakati ulimwengu umekuwa bila utendaji wa kivita. Kumekuwako zaidi ya vita 150 vya asilia ya kimataifa au vya raia wenyewe kwa wenyewe, ambavyo vimekadiriwa kuwa vilidai maisha milioni 19.3, vingi vyavyo vikiwa ni tokeo la tekinolojia mpya zenye usahihi zaidi ambazo zimezuka katika wakati huu wa Umoja wa Mataifa.”
Kufikia 2005, utendaji wa kijeshi ulikuwa umesababisha vifo zaidi ya milioni 20.
[Picha katika ukurasa wa 98 99]
Muundo wa Kitabu cha Ufunuo
Tukiwa tumeendelea kufikia hapa katika mazungumzo yetu ya kitabu cha Ufunuo, tunaanza kuona kwa wazi zaidi muundo wa kitabu. Baada ya utangulizi wacho wenye kusisimua (Ufunuo 1:1-9), Ufunuo kinaweza kuonwa kuwa kimegawanywa katika njozi 16 kama ifuatavyo:
NJOZI YA 1 (1:10–3:22): Yohana kwa kuvuviwa anamwona Yesu Kristo aliyetukuzwa, ambaye anapeleka jumbe zenye uchangamshi za shauri kwa yale makundi saba.
NJOZI YA 2 (4:1–5:14): Mwono wenye uzuri mwingi mno wa kiti cha ufalme cha kimbingu cha Yehova Mungu. Huyu Mmoja anamkabidhi Mwana-Kondoo hati-kunjo.
NJOZI YA 3 (6:1-17): Akivunja na kufungua vile vifungo sita vya kwanza vya hati-kunjo, Mwana-Kondoo anafunua kwa mwendeleo njozi yenye matukio mengi ambayo hayana budi kuwa katika siku ya Bwana. Wale wana-farasi wanne wa Apokalipsi wanatoka wakiwa wamepanda, watumwa wa Mungu waliofia imani wanapokea majoho meupe, na siku ya hasira-jeuri inaelezwa.
NJOZI YA 4 (7:1-17): Malaika wanazuia zile pepo za uharibifu mpaka Waisraeli wa kiroho 144,000 watiwe kifungo. Umati mkubwa kutoka mataifa yote wanawahesabia Mungu na Kristo wokovu nao wanakusanywa kwa ajili ya wokovu kupitia dhiki kubwa.
NJOZI YA 5 (8:1–9:21): Wakati wa kufunguliwa kwa kifungo cha saba, kunakuwa na mipigo saba ya tarumbeta, sita ya kwanza ya hiyo inafanyiza njozi ya tano. Mipigo hii sita ya tarumbeta yatoa habari ya maonyesho ya hukumu ya Yehova juu ya aina ya binadamu. Zile tarumbeta za tano na sita pia zinajulisha ole wa kwanza na wa pili.
NJOZI YA 6 (10:1–11:19): Malaika kabambe anampa Yohana hati-kunjo ndogo, hekalu linapimwa, nasi tunajifunza habari ya yanayopata mashahidi wawili. Inafikia upeo kwa kupulizwa kwa tarumbeta ya saba, ambayo inatoa habari ya ole wa tatu kwa ajili ya maadui wa Mungu—Ufalme wa Yehova na wa Kristo unaokuja.
NJOZI YA 7 (12:1-17): Hii hueleza habari za uzawa wa Ufalme, matokeo yakiwa ni Mikaeli kuvurumisha chini duniani yule nyoka, Shetani.
NJOZI YA 8 (13:1-18): Hayawani-mwitu anayejaa nguvu anakuja kutoka bahari, na hayawani-mwitu mwenye pembe mbili kama mwana-kondoo ahimiza aina ya binadamu iabudu huyo.
NJOZI YA 9 (14:1-20): Mtazamo-tangulizi mzuri ajabu wa wale 144,000 juu ya Mlima Sayuni. Jumbe za kimalaika zasikiwa kuzunguka dunia yote, mzabibu wa dunia unavunwa, nalo shinikizo la divai la kasirani ya Mungu lakanyagwa.
NJOZI YA 10 (15:1–16:21): Mtazamo mwingine mfupi wa kitala cha kifalme cha kimbingu, ukifuatwa na kumiminwa kwa mabakuli saba ya kasirani ya Mungu ndani ya dunia. Sehemu hii, vilevile, inaisha kwa elezo la kiunabii la mwisho wa mfumo wa Shetani.
NJOZI YA 11 (17:1-18): Kahaba mkubwa, Babuloni Mkubwa, apanda hayawani-mwitu wa rangi nyekundu-angavu, ambaye anaingia kifupi ndani ya abiso lakini anatokea tena na kumwangamiza.
NJOZI YA 12 (18:1–19:10): Anguko na uharibifu wa mwisho wa Babuloni Mkubwa watangazwa. Baada ya kuuawa kwake, baadhi waomboleza, wengine wanasifu Yehova; ndoa ya Mwana-Kondoo yatangazwa.
NJOZI YA 13 (19:11-21): Yesu anaongoza majeshi ya mbingu kutekeleza hukumu za Mungu zenye kujaa hasira-jeuri juu ya mfumo wa Shetani, majeshi yao, na waunga-mkono wao; ndege-wala-nyama wafanya karamu ya kula mizoga yao.
NJOZI YA 14 (20:1-10): Kutiwa ndani ya abiso kwa Shetani Ibilisi, Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo na wafalme wenzake, mtihani wa mwisho kabisa wa aina ya binadamu, na kuharibiwa kwa Shetani na roho waovu wake.
NJOZI YA 15 (20:11–21:8): Ufufuo wa watu wote na Siku ya Hukumu iliyo kubwa; mbingu mpya na dunia mpya zatokea, zikiwa na baraka za milele kwa aina ya binadamu yenye uadilifu.
NJOZI YA 16 (21:9–22:5): Ufunuo unafikia upeo kwa njozi tukufu ya Yerusalemu Jipya, mke wa Mwana-Kondoo. Uandalizi wa Mungu wa kuponya na uhai kwa aina ya binadamu watiririka kutoka jiji hilo.
Ufunuo wamalizika kwa maneno machangamfu ya salamu na shauri kutoka kwa Yehova, Yesu, malaika, na Yohana mwenyewe. Mwaliko kwa kila mmoja ni “Njoo!”—Ufunuo 22:6-21.
-
-
‘Nafsi Zilizochinjwa’ ZathawabishwaUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 17
‘Nafsi Zilizochinjwa’ Zathawabishwa
1. Sisi tunaishi katika kipindi cha wakati gani, na kuna ithibati gani ya hili?
UFALME wa Mungu watawala! Yule Mpandaji-farasi mweupe anakaribia kukamilisha ushindi wake! Farasi mwekundu, farasi mweusi, na farasi rangi nyeupe-nyeupe wamo katika mwendo kotekote duniani! Pasipo kukanushika, unabii wa Yesu mwenyewe kuhusu kuwapo kwake kwa kifalme unatimizwa. (Mathayo, sura 24, 25; Marko, sura 13; Luka, sura 21) Ndiyo, sisi tunaishi katika siku za mwisho za huu mfumo wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa kuwa ndivyo, acheni sisi tutoe uangalifu wa makini wakati Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, anapovunja na kufungua kifungo cha tano cha hati-kunjo. Sasa ni ufunuo gani zaidi ambao sisi tutashiriki?
2. (a) Yohana aliona nini wakati kifungo cha tano kilipofunguliwa? (b) Ni kwa nini haitupasi kushangaa kusoma juu ya madhabahu ya ufananisho katika mbingu?
2 Yohana anaeleza habari ya mandhari yenye kutoza huruma: “Na wakati alipofungua kifungo cha tano, mimi nikaona chini-chini ya madhabahu nafsi za wale waliochinjwa kwa sababu ya Neno la Mungu na kwa sababu ya kazi ya ushuhuda ambayo walizoea kuwa nayo.” (Ufunuo 6:9, NW) Ni nini hiyo? Madhabahu ya kidhabihu juu mbinguni? Ndiyo! Ndio wakati wa kwanza ambapo Yohana anataja madhabahu. Ingawa hivyo, Yohana amekwisha eleza habari za Yehova akiwa ameketi juu ya kiti cha ufalme Chake, makerubi wanaozunguka, bahari ya kioo, taa, na wazee 24 wanaopeleka uvumba—vyote hivyo vikiwa mshabaha wa vitu vya tabenakulo ya kidunia, patakatifu pa Yehova katika Israeli. (Kutoka 25:17, 18; 40:24-27, 30-32; 1 Nyakati 24:4) Basi, je! itushangaze kuona pia madhabahu ya ufananisho katika mbingu?—Kutoka 40:29.
3. (a) Kwenye tabenakulo ya Kiyahudi ya kale, nafsi zilimwagwaje “penye msingi wa madhabahu”? (b) Ni kwa nini Yohana aliona nafsi za mashahidi waliochinjwa zikiwa chini-chini ya madhabahu ya ufananisho katika mbingu?
3 Chini-chini ya madhabahu hii ziko “nafsi za wale waliochinjwa kwa sababu ya Neno la Mungu na kwa sababu ya kazi ya ushuhuda ambayo walizoea kuwa nayo.” Hii humaanisha nini? Hizi hazingekuwa nafsi zilizoachanishwa na mwili—kama zile walizoamini Wagiriki wapagani. (Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4, ZSB) Badala ya hivyo, Yohana anajua kwamba nafsi, au uhai, hufananishwa na damu, na wakati makuhani kwenye tabenakulo ya kale ya Kiyahudi walipochinja mnyama wa dhabihu, wao walinyunyiza damu “kuzunguka pande zote juu ya madhabahu” au “penye msingi wa madhabahu ya toleo la kuteketezwa.” (Walawi 3:2, 8, 13; 4:7; 17:6, 11, 12, NW) Kwa sababu hiyo, nafsi ya mnyama ilishirikishwa karibu-karibu na madhabahu. Lakini ni kwa sababu gani nafsi, au damu, za hawa watumishi wa Mungu hasa zionwe chini-chini ya madhabahu ya ufananisho katika mbingu? Ni kwa sababu kifo chao huonwa kuwa cha kidhabihu.
4. Ni katika njia gani kifo cha Wakristo waliozaliwa kwa roho ni cha kidhabihu?
4 Kweli kweli, wale wote wanaozaliwa kuwa wana wa roho wa Mungu wanakufa kifo cha kidhabihu. Kwa sababu ya daraka wanalopaswa kushiriki katika Ufalme wa Yehova wa kimbingu, ni mapenzi ya Mungu kwamba wakane kabisa kabisa na wadhabihu tumaini lolote la uhai wa milele duniani. Katika njia hii, wao wanajitiisha kwenye kifo cha kidhabihu kwa ajili ya enzi kuu ya Yehova. (Wafilipi 3:8-11; linga 2:17.) Hiyo ni kweli katika maana halisi kabisa kwa habari ya wale ambao Yohana aliona chini ya madhabahu. Wao walikuwa wapakwa-mafuta ambao katika siku yao walifia imani kwa ajili ya huduma yao ya bidii katika kutegemeza Neno na enzi kuu ya Yehova. ‘Nafsi zao zilichinjwa kwa sababu ya Neno la Mungu na kwa sababu ya kazi ya ushuhuda [mar·ty·riʹan] ambayo walizoea kuwa nayo.’
5. Ni kwa jinsi gani nafsi za waaminifu, zijapokuwa zimekufa, zinalia kwa sauti kubwa ili kisasi kilipwe?
5 Ule mfululizo wa mandhari waendelea kufunguka: “Na hizo zikalia kwa sauti kubwa, zikisema: ‘Ni mpaka lini, Bwana Mwenye Enzi Kuu mtakatifu na wa kweli, wewe unajizuia usihukumu na kulipiza kisasi damu yetu juu ya wale ambao wanakaa juu ya dunia?’” (Ufunuo 6:10, NW) Nafsi zao, au damu, zingeweza kuliaje kwa kutaka kisasi, kwa kuwa Biblia inaonyesha kwamba wafu hawana fahamu? (Mhubiri 9:5) Basi, je! damu ya Abeli mwadilifu haikulia kwa sauti kubwa wakati Kaini alipomwua kimakusudi? Ndipo Yehova alipomwambia Kaini hivi: “Wewe umefanya nini? Sikiliza! Damu ya ndugu yako inanililia mimi kwa sauti kubwa kutoka ardhi.” (Mwanzo 4:10, 11, NW; Waebrania 12:24) Si kwamba damu ya Abeli ilikuwa ikitamka maneno kihalisi. Badala ya hivyo, Abeli alikuwa amekufa akiwa jeruhi asiye na hatia, nayo haki ililia kwa sauti kubwa ikitaka mwuaji kimakusudi wake aadhibiwe. Hali moja na hiyo, Wakristo hao wafia-imani hawana hatia, na kwa haki lazima walipiwe kisasi. (Luka 18:7, 8) Kilio cha kutaka kisasi kilipwe ni kikuu kwa sababu maelfu wengi wamekufa.—Linga Yeremia 15:15, 16.
6. Ni umwagaji-damu gani usio na hatia uliolipizwa kisasi katika 607 K.W.K.?
6 Hali hiyo ingeweza kufananishwa pia na ile iliyokuwa Yuda yenye kuasi imani wakati Mfalme Manase alipokuja kukalia kiti cha ufalme katika 716 K.W.K. Yeye alimwaga damu nyingi isiyo na hatia, pengine ‘akimpasua vipande vipande kwa msumeno’ nabii Isaya. (Waebrania 11:37, NW; 2 Wafalme 21:16) Ijapokuwa baadaye Manase alitubu na akabadilika, hiyo hatia ya damu ilibaki. Katika 607 K.W.K., wakati Wababuloni walipouacha ukiwa ufalme wa Yuda, “ilikuwa tu kwa amri ya Yehova kwamba hilo likatukia dhidi ya Yuda, kuiondoa machoni pake kwa ajili ya madhambi ya Manase, kulingana na yale yote ambayo yeye alikuwa amefanya; na pia kwa ajili ya damu isiyo na hatia ambayo yeye alikuwa amemwaga, hivi kwamba yeye alijaza Yerusalemu damu isiyo na hatia, na Yehova hakuidhini kutoa msamaha.”—2 Wafalme 24:3, 4, NW.
7. Ni nani hasa mwenye hatia ya ‘umwagaji-damu ya watakatifu’?
7 Kama vile katika nyakati za Biblia, ndivyo na leo, wengi wa wale watu mmoja mmoja walioua mashahidi wa Mungu huenda wamekufa kitambo. Lakini tengenezo lililosababisha ufia-imani wao lingali hai sana na ni lenye hatia ya damu. Ni tengenezo la Shetani la kidunia, mbegu yake ya kidunia. Sehemu yenye kutokeza katika hiyo ni Babuloni Mkubwa, ile milki ya ulimwengu ya dini bandia.a Yeye anaelezwa kuwa ‘amelewa kwa damu ya watakatifu na kwa damu ya mashahidi wa Yesu.’ Ndiyo, “katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wale wote ambao wamechinjwa juu ya dunia.” (Ufunuo 17:5, 6; 18:24; Waefeso 4:11; 1 Wakorintho 12:28, NW) Ni mzigo wa hatia ya damu kama nini! Maadamu Babuloni Mkubwa yupo, damu ya majeruhi wake italia kwa sauti kubwa kwa kutaka haki itekelezwe.—Ufunuo 19:1, 2.
8. (a) Ni mifano gani ya ufia-imani iliyokuwa imetukia wakati wa maisha ya Yohana? (b) Ni minyanyaso gani iliyochochewa na wamaliki Waroma?
8 Yohana mwenyewe alishuhudia ufia-imani katika karne ya kwanza wakati Nyoka mkatili na mbegu yake ya kidunia walipopiga vita juu ya kundi la Wakristo wapakwa-mafuta lililokuwa likikua. Yohana alikuwa ameona Bwana yetu akitundikwa juu ya nguzo na alikuwa ameishi kupitia vipindi vya kuuawa kwa Stefano, kwa ndugu yake mwenyewe Yakobo, na kwa Petro, kwa Paulo, na washiriki wengine wa karibu. (Yohana 19:26, 27; 21:15, 18, 19; Matendo 7:59, 60; 8:2; 12:2; 2 Timotheo 1:1; 4:6, 7) Katika 64 W.K., Nero, maliki Mroma alikuwa amelaumu bure Wakristo, akiwashtakia kuteketeza jiji, ili kukanusha uvumi wa kwamba ndiye aliyekuwa mwenye hatia. Mwanahistoria Takito anaripoti hivi: “Wao [Wakristo] walikufa kwa njia za dhihaka; baadhi yao walifunikwa ngozi za hayawani-mwitu kisha wakararuliwa na mbwa, baadhi yao [walitundikwa juu ya nguzo],b baadhi yao walichomwa kuwa mienge ya kunurisha usiku.” Wimbi zaidi la mnyanyaso chini ya Maliki Domitiano (81-96 W.K.) lilikuwa limetokeza kuhamishwa kwa Yohana kupelekwa kisiwa cha Patmosi. Kama Yesu alivyosema: “Ikiwa wao wamenyanyasa mimi, wao watanyanyasa nyinyi pia.”—Yohana 15:20; Mathayo 10:22, NW.
9. (a) Ni kipeo gani cha udanganyifu alichotokeza Shetani kufikia karne ya nne W.K., nacho ni sehemu kuu ya nini? (b) Baadhi ya watawala wa Jumuiya ya Wakristo waliwatendeaje Mashahidi wa Yehova wakati wa Vita ya Ulimwengu 1 na 2?
9 Kufikia karne ya nne W.K., yule nyoka wa zamani, Shetani Ibilisi, alikuwa ametokeza kipeo cha udanganyifu wake, ile dini yenye uasi-imani ya Jumuiya ya Wakristo—mfumo wa Kibabuloni uliofichwa chini ya kibandiko cha “Ukristo.” Ndiyo sehemu iliyo kuu ya mbegu ya yule Nyoka na imesitawi ikawa umati wa farakano zenye kuhitilafiana. Kama Yuda ya kale isiyo na imani, Jumuiya ya Wakristo inabeba hatia nzito ya damu, ikiwa imekwisha kujihusisha sana katika pande zote mbili za Vita ya Ulimwengu 1 na 2. Wengine wa watawala wa kisiasa wa Jumuiya ya Wakristo hata walitumia vita hivyo kuwa kisababu cha kuchinja watumishi wa Mungu. Likiripoti juu ya Hitla kunyanyasa Mashahidi wa Yehova, pitio la kitabu Kirchenkampf in Deutschland (Vita ya Makanisa Katika Ujeremani) lilitaarifu hivi: “Theluthi moja yao [Mashahidi] waliuawa, ama walifishwa kwa amri ya kiserikali, ama kwa matendo mengine ya jeuri, njaa, ugonjwa au kazi ngumu ya utumwa. Ukali wa utiisho huu ulikuwa bila kitangulizi na ulikuwa tokeo la imani thabiti ambayo haingeweza kupatanishwa na siasa ya Usoshalisti wa Kitaifa.” Kweli kweli, inaweza kusemwa juu ya Jumuiya ya Wakristo, kutia na upadri wayo: “Katika marinda yako zimepatikana alama za damu ya nafsi za maskini wasio na hatia.”—Yeremia 2:34, NW.c
10. Wanaume vijana wa ule umati mkubwa wamepatwa na minyanyaso gani katika mabara mengi?
10 Tangu 1935 wanaume vijana waaminifu wa ule umati mkubwa wamehimili ukali wa minyanyaso katika mabara mengi. (Ufunuo 7:9) Hata wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipokuwa ikiisha katika Ulaya, katika mji mmoja tu vijana Mashahidi wa Yehova 14 walifishwa kwa kunyongwa kwa amri ya kiserikali. Uhalifu wao? Kukataa ‘kujifunza vita tena.’ (Isaya 2:4) Karibuni zaidi, wanaume vijana katika Mashariki na katika Afrika wamepigwa mpaka kifo au wakauawa na kikosi cha wapiga risasi kwa amri ya kiserikali juu ya suala ilo hilo. Wafia-imani hawa vijana, wategemezaji wastahilifu wa ndugu za Yesu wapakwa-mafuta, hakika watapata ufufuo kuingia ndani ya ile dunia mpya iliyoahidiwa.—2 Petro 3:13; Linga Zaburi 110:3; Mathayo 25:34-40; Luka 20:37, 38.
Joho Jeupe
11. Ni katika maana gani Wakristo wapakwa-mafuta waliofia imani hupokea “joho jeupe”?
11 Baada ya kuthibiti kwa maandishi imani ya washika-ukamilifu wa nyakati za kale, mtume Paulo alisema: “Na hata hivyo wote hawa, ijapokuwa ushuhuda ulitolewa kwao kupitia imani yao, hawakupata utimizo wa ahadi, kwa kuwa Mungu alitangulia kuona kitu fulani kilicho bora kwa ajili yetu sisi, ili kwamba wao wasifanywe kuwa wakamilifu mbali na sisi.” (Waebrania 11:39, 40, NW) Ni nini hicho “kitu fulani kilicho bora” ambacho Paulo na Wakristo wengine wapakwa-mafuta walitarajia? Yohana anakiona hapa katika njozi: “Na joho jeupe lilipewa kwa kila mmoja wao; na wao waliambiwa wapumzike kwa kitambo kidogo zaidi, mpaka hesabu ilipokuwa imejazwa pia ya watumwa wenzao na ndugu zao ambao walikuwa karibu kuuawa kama wao pia walivyokuwa.” (Ufunuo 6:11, NW) Kupokea kwao “joho jeupe” kunahusiana na kufufuliwa kwao wakawe viumbe wa roho wasioweza kufa. Hawalali tena wakiwa nafsi zilizochinjwa chini-chini ya madhabahu, bali wanainuliwa wakawe sehemu ya kile kikundi cha wazee 24 ambao huabudu mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu. Huko, wao wenyewe wamepewa viti vya ufalme, kuonyesha kwamba wao wamekwisha ingia katika mapendeleo ya kifalme. Na “wamevalia mavazi ya nje meupe,” kuashiria kwamba wao wamekwisha hukumiwa kuwa waadilifu, wastahilio mahali pa heshima mbele za Yehova katika kitala cha kifalme. Hilo pia ni katika utimizo wa ahadi ya Yesu kwa Wakristo wapakwa-mafuta waaminifu katika kundi la Sardisi: “Yeye ambaye hushinda atapambwa hivyo kwa mavazi ya nje meupe.”—Ufunuo 3:5; 4:4; 1 Petro 1:4, NW.
12. Ni katika njia gani Wakristo waliofufuliwa ‘hupumzika kwa kitambo kidogo zaidi,’ na mpaka lini?
12 Ithibati yote huonyesha kwamba ufufuo huu wa kimbingu ulianza katika 1918, baada ya Yesu kuketishwa juu ya kiti cha ufalme katika 1914 na kutoka kwake aende akipanda farasi kuanza ushindi wake wa kifalme kwa kuzisafisha mbingu watoke Shetani na roho waovu wake. Hata hivyo, wapakwa-mafuta hao waliofufuliwa wanaambiwa kwamba lazima “wapumzike kwa kitambo kidogo zaidi, mpaka hesabu . . . pia ya watumwa wenzao” ijazwe. Wale wa jamii ya Yohana ambao wangali duniani lazima wathibitishe ukamilifu wao chini ya jaribu na mnyanyaso, na huenda baadhi ya hawa bado wakauawa. Hata hivyo, mwishowe, damu yote yenye uadilifu iliyomwagwa na Babuloni Mkubwa na hawara zake wa kisiasa italipiwa kisasi. Kwa wakati uliopo, pasipo shaka wale waliofufuliwa wana shughuli wakiwa na wajibu mwingi wa kimbingu. Wao wanapumzika, si kwa kustarehe katika raha ya kutotenda, bali katika njia ya kwamba wao wanangojea kwa subira siku ya kisasi cha Yehova. (Isaya 34:8; Warumi 12:19) Pumziko lao litakwisha wakati wao watashuhudia uharibifu wa dini bandia na, wakiwa ‘walioitwa na waliochaguliwa na waaminifu,’ wao wanaandamana na Bwana Yesu Kristo katika kutekeleza hukumu hapa duniani juu ya sehemu nyingine zote za mbegu mbovu ya Shetani.—Ufunuo 2:26, 27; 17:14; Warumi 16:20.
‘Wale Ambao Wamekufa Wainuka Kwanza’
13, 14. (a) Kulingana na mtume Paulo, ufufuo wa kimbingu huanza lini, na ni nani wanaofufuliwa? (b) Wale wapakwa-mafuta wanaoendelea kuishi kufikia siku ya Bwana wanafufuliwa lini waende mbinguni?
13 Ule muono-ndani unaotolewa kwa kufunguliwa kwa kifungo cha tano unakubaliana kabisa kabisa na maandiko mengine yanayohusiana na ufufuo wa kimbingu. Mathalani, mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa maana hili ndilo ambalo sisi tunaambia nyinyi kwa neno la Yehova, kwamba sisi tulio hai ambao twaishi kufikia kuwapo kwa Bwana hatutatangulia kwa vyovyote wale ambao wamelala usingizi katika kifo; kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wa kuamuru, na sauti ya malaika mkuu na tarumbeta ya Mungu, na wale ambao wamekufa katika muungano pamoja na Kristo watainuka kwanza. Baadaye sisi tulio hai ambao twaendelea kuishi, pamoja nao, tutadakwa mbali katika mawingu ili kumkuta Bwana katika hewa; na hivyo sisi tutakuwa na Bwana sikuzote.”—1 Wathesalonike 4:15-17, NW.
14 Ni hadithi yenye kusisimua kama nini ambayo mistari hii inasimulia! Wale wa ndugu za Yesu wapakwa-mafuta ambao huendelea kuishi kufikia kuwapo kwa Yesu, yaani, ambao wangali hai duniani wakati wa kuwapo kwake, wanatanguliwa kuingia ndani ya mbingu na wale ambao tayari wamekufa. Hao, ambao wamekufa katika muungano pamoja na Kristo, huinuka kwanza. Yesu hushuka, yaani, huelekeza uangalifu kwao, na kuwafufua kwenye uhai wa roho, akiwapa “joho jeupe.” Baadaye, wale ambao wangali hai wakiwa binadamu wanamaliza mwendo wao wa kidunia, wengi wao wakifa kijeuri mikononi mwa wapinzani. Hata hivyo, wao hawalali usingizi katika kifo kama watangulizi wao walivyofanya. Badala ya hivyo, wanapokufa, wao huinuliwa mara hiyo—“katika kufumba na kufumbua jicho”—wakidakwa mbali kwenda katika mbingu wakawe pamoja na Yesu na washiriki wenzi wa mwili wa Kristo. (1 Wakorintho 15:50-52, NW; linga Ufunuo 14:13.) Hivyo, kufufuliwa kwa Wakristo wapakwa-mafuta huanza upesi baada ya wale wapandaji-farasi wanne wa Apokalipsi kuanza upandaji wao.
15. (a) Kufunguliwa kwa kifungo cha tano kumeandaa habari njema gani? (b) Kupanda kwa Mshindi aliye juu ya farasi mweupe hufikia upeo gani?
15 Kule kufunguliwa kwa kifungo hiki cha tano cha hati-kunjo kumeandaa habari njema kuhusu washika ukamilifu wapakwa-mafuta ambao wameshinda, wakiwa waaminifu mpaka kifo. Lakini hakuandai habari njema kwa Shetani na mbegu yake. Upandaji wa yule Mshindi aliye juu ya farasi mweupe unaendelea bila kukinzwa na hufikia upeo katika wakati wa kutozwa hesabu kwa ulimwengu ambao “unalala katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Hili linadhihirishwa wakati Mwana-Kondoo anapofungua kifungo cha sita.
[Maelezo ya Chini]
a Utambulisho wa Babuloni Mkubwa huzungumzwa kirefu katika Sura ya 33.
b Linganisha New World Translation Reference Bible, ukurasa 1577, nyongeza 5C, “Nguzo ya Mateso.”
c Ithibati ya hatia-damu ya dini imetolewa kirefu katika Sura ya 36.
[Sanduku katika ukurasa wa 102]
‘Nafsi Zilizochinjwa’
Cyclopedia ya McClintock na Strong hunukuu John Jortin, Mprotestanti Mwingereza wa karne ya 18, aliyezaliwa na wazazi Wahuguenoti Wafaransa, kuwa akisema: “Mahali minyanyaso inapoanza, Ukristo hukoma . . . Ilikuwa baada ya Ukristo kuimarishwa kuwa dini ya milki ya [Kiroma], na baada ya wahudumu wayo kupewa utajiri na heshima, ndipo ovu lenye kuchukiza sana la mnyanyaso lilipata imara kubwa mno, nalo likatupa uvutano walo wenye kuvunja-vunja juu ya dini ya Gospeli.”
[Picha katika ukurasa wa 103]
“Na joho jeupe lilipewa kwa kila mmoja wao”
-
-
Matetemeko ya Dunia Katika Siku ya BwanaUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 18
Matetemeko ya Dunia Katika Siku ya Bwana
1, 2. (a) Ikoje kuishi kupitia tetemeko la dunia kali? (b) Yohana anaeleza habari ya nini wakati kifungo cha sita kinapofunguliwa?
JE! WEWE umewahi kuishi kupitia tetemeko la dunia kali? Si ono zuri. Mtetemeko mkubwa huenda ukaanza kwa msukosuko wenye kugonjwesha na kelele yenye mtutumo. Myumboyumbo huenda ukazidi kuwa mbaya vipindi kwa vipindi na huku wewe ukikimbilia usalama—pengine chini ya dawati. Au huenda likaja likiwa mshtuo wa ghafula, wenye kuvunjavunja, ukifuatwa na kuvunjikavunjika kwa vikombe na sahani, samani na hata majengo. Uharibifu huenda ukawa wenye kuleta hasara sana, kukiwa na mishtuo ya baadaye ikileta uharibifu zaidi na kuongezea janga.
2 Ukiwa na hayo akilini, fikiria yale ambayo Yohana anaeleza wakati wa kufunguliwa kwa kifungo cha sita: “Na mimi nikaona wakati yeye alipofungua kifungo cha sita, na tetemeko la dunia kubwa likatukia.” (Ufunuo 6:12a, NW) Lazima hili lianguke katika muda wa wakati ule ule wa kufunguliwa kwa vile vifungo vingine. Ni wakati gani hasa katika siku ya Bwana tetemeko la dunia hili linatukia, nalo ni tetemo la namna gani?—Ufunuo 1:10.
3. (a) Ni matukio gani aliyotabiri Yesu katika unabii juu ya ishara ya kuwapo kwake? (b) Matetemeko ya dunia halisi yahusianaje na tetemeko la dunia la ufananisho la Ufunuo 6:12?
3 Matetemeko ya dunia ya kihalisi na ya kitamathali yametajwa katika Biblia mara kadhaa. Katika unabii mkubwa juu ya ishara ya kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme, Yesu alitabiri “matetemeko ya dunia katika mahali pamoja baada ya pengine.” Hayo yangekuwa sehemu ya “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu.” Tangu 1914, idadi ya watu wa dunia ikiwa inaongezeka ghafula sana kuwa maelfu ya mamilioni, mitetemo hiyo imechangia kwa kutokeza sana taabu za nyakati zetu. (Mathayo 24:3, 7, 8, NW) Hata hivyo, hata ingawa yanatimiza unabii, matetemeko ya dunia hayo yamekuwa misiba asilia, yenye kuonekana. Hayo ni utangulizi wa lile tetemeko la dunia kubwa la ufananisho la Ufunuo 6:12. Kweli kweli, hili laja likiwa ndiyo tamati yenye kukumba ya mfululizo wa mitetemo yenye kutangulia inayotikisa mpaka misingi yenyewe mfumo wa mambo ya kibinadamu wa kidunia wa Shetani.a
Mitetemo Katika Jamii ya Kibinadamu
4. (a) Ni tangu lini watu wa Yehova walikuwa wamekuwa wakitaraji kwamba matukio yenye kuleta uharibifu yangeanza katika 1914? (b) 1914 ungetia alama ya mwisho wa kipindi gani cha wakati?
4 Kuanzia miaka ya katikati ya 1870 watu wa Yehova walikuwa wamekuwa wakitaraji kwamba matukio yenye kuleta uharibifu yangeanza katika 1914 nayo yangeonyesha mwisho wa Majira ya Mataifa. Hiki ndicho kipindi cha “nyakati saba” (miaka 2,520) kikianza na kupinduliwa kwa ufalme wa Kidaudi katika Yerusalemu katika 607 K.W.K. hadi kuketishwa kwa Yesu juu ya kiti cha ufalme katika Yerusalemu la kimbingu katika 1914 W.K.—Danieli 4:24, 25; Luka 21:24.b
5. (a) Ni tangazo gani alilofanya C. T. Russell katika Oktoba 2, 1914? (b) Ni mabadiliko makubwa gani ya kisiasa ambayo yametukia tangu 1914?
5 Hivyo, wakati C. T. Russell alipoonekana kwa ajili ya ibada ya asubuhi pamoja na jamaa ya Betheli ya Brooklyn, New York, asubuhi ya Oktoba 2, 1914, yeye alifanya tangazo hili lenye kusisimua: “Majira ya Mataifa yamekwisha; siku ya wafalme wayo imekwisha.” Kweli kweli, lile badiliko kubwa lililoanza katika 1914 lilikuwa na matokeo makubwa sana hivi kwamba falme nyingi zilizokuwa zimesimama kwa muda mrefu zilitoweka. Lile angusho la utawala wa zari katika pinduzi la Bolsheviki la 1917 liliongoza kwenye mkabiliano wa muda mrefu kati ya Umarksizimu na ukapitalisti (ubepari). Mitetemo ya badiliko la kisiasa yaendelea kusumbua jamii ya kibinadamu duniani pote. Leo, serikali nyingi zinashindwa kuendelea kwa muda unaozidi mwaka mmoja au miwili. Ukosefu wa imara katika ulimwengu wa kisiasa unatolewa kielezi na kisa cha Italia, ambayo ilikuwa na serikali mpya 47 katika muda wa miaka 42 tu kufuatia Vita ya Ulimwengu 2. Lakini mitetemo hiyo ni utangulizi tu wa badiliko kubwa la kiserikali lenye kufikia upeo mkuu. Tokeo litakuwa nini? Ufalme wa Mungu utachukua utawala kamili wa dunia.—Isaya 9:6, 7.
6. (a) H. G. Wells alielezaje habari ya muhula mpya wenye maana kubwa? (b) Mwanafalsafa mmoja na waziri wa serikali mmoja waliandika nini juu ya muhula wa tangu 1914?
6 Wanahistoria, wanafalsafa, na viongozi wa kisiasa wameelekeza kwenye mwaka 1914 kuwa mwanzo wa muhula mpya na wenye maana kubwa. Miaka 17 ya kuingia katika muhula huo, mwanahistoria H. G. Wells alitoa elezo hili: “Kwa mteremo nabii angetoa unabii wa vitu vizuri. Lakini wajibu wake ni kusimulia anachoona. Yeye anaona ulimwengu ambao ungali unadhibitiwa kiimara na askari-jeshi, wazalendo, wala-riba, na mabarakala wa kifedha; ulimwengu uliojikabidhi kwenye shuku na chuki, ukipoteza kwa haraka sana mauhuru ya faragha yaliyobaki, ukijongeza ki-upofu-upofu kuelekea mapambano makali ya kitabaka, na kutayarisha kwa ajili ya vita vipya.” Katika 1953 mwanafalsafa Bertrand Russell aliandika: “Tangu 1914, kila mtu anayejua maelekeo yaliyo katika ulimwengu amesumbuliwa sana na ule ambao umeonekana kuwa kama mwendo wenye tukio baya na uliokusudiwa kimbele kuelekea msiba unaozidi kuwa mkubwa. . . . Wao wanaona jamii ya kibinadamu, kama shujaa wa hadithi yenye misiba ya Kigiriki, akiendeshwa na miungu wenye kasirani na yeye siye bwana-mkubwa tena wa tukio baya.” Katika 1980 waziri wa serikali Harold Macmillan, akirudisha fikira nyuma kwenye mwanzo wenye amani wa karne ya 20, alisema: “Kila kitu kingezidi kuwa bora na bora. Huu ndio ulimwengu nilimozaliwa mimi. . . . Ghafula, asubuhi moja katika 1914 kitu kizima chote kilikuja kwenye mwisho.”
7-9. (a) Ni mabadiliko makubwa gani ambayo yametikisa jamii ya kibinadamu tangu 1914? (b) Mabadiliko makubwa katika jamii ya kibinadamu wakati wa kuwapo kwa Yesu hatimaye yangetia ndani hali gani miongoni mwa wanadamu?
7 Vita ya Ulimwengu 2 ilileta wimbi jingine la mabadiliko makubwa. Na vita vidogo zaidi pamoja na ugaidi wa kimataifa vinaendelea kutikisa dunia. Lile tisho la magaidi au mataifa yanayotumia silaha za maangamizi makubwa linafanya watu wengi wawe na wasiwasi.
8 Ingawa hivyo, mambo mengine licha ya vita yametikisa jamii ya kibinadamu mpaka kwenye misingi yayo tangu 1914. Mojapo mabadiliko makubwa ambalo lilikuwa lenye kuumiza zaidi sana lilianzishwa na anguko la soko la rasilimali la U.S. la Oktoba 29, 1929. Hilo lilileta Ule Mshuko Mkubwa wa Thamani ya Pesa, ambao uliathiri nchi zote za ukapitalisti. Mshuko huo ulifikia upeo wa chini zaidi kati ya 1932 na 1934, lakini sisi tungali tunahisi matokeo yao. Tangu 1929 ulimwengu mgonjwa kiuchumi umetiwa-tiwa viraka kwa kutumia mipango-badala. Serikali zinajitia katika madeni ya kifedha. Ile shida kubwa ya mafuta ya 1973 na mshuko-ghafula wa 1987 wa soko la rasilimali viliongezea mitikiso ya milki ya kifedha. Kwa wakati uliopo, mamilioni ya watu hununua vitu kwa mkopo. Idadi zisizohesabika huwa majeruhi ya madanganyo ya kifedha, mipango ya kipiramidi, na hila za michezo ya bahati-nasibu na kamari, mingi yayo ikiwa inadhaminiwa na serikali ambazo zapaswa kuwa zikiwapa himaya watu. Hata waevanjeli wa televisheni wa Jumuiya ya Wakristo hunyoosha mikono yao wapate hisa yao ya mamilioni ya dola!—Linga Yeremia 5:26-31.
9 Mapema zaidi, shida za kiuchumi zilikuwa zimefungulia njia Mussolini na Hitla wanyakue mamlaka. Babuloni Mkubwa hakupoteza wakati wowote akitafuta kupendwa nao, na Vatikani iliingia katika mapatano na Italia katika 1929 na Ujeremani katika 1933. (Ufunuo 17:5) Zile siku zenye huzuni zilizofuata hakika zilikuwa sehemu ya utimizo wa unabii wa Yesu kuhusu kuwapo kwake, ambao ungetia ndani “huzuni kuu ya mataifa, yasijue njia ya kutokea . . . huku watu wakizirai kwa woga na taraja la vitu vinavyokuja juu ya dunia inayokaliwa.” (Luka 21:7-9, 25-31, NW)c Ndiyo, yale matetemeko yaliyoanza kutikisa jamii ya kibinadamu katika 1914 yameendelea, kukiwa na mishtuo ya baadaye yenye nguvu.
Yehova Atikisa
10. (a) Ni kwa nini kuna mitetemo mingi sana katika mambo ya kibinadamu? (b) Yehova anafanya nini, kwa kutayarishia nini?
10 Mitetemo hiyo katika mambo ya kibinadamu ni matokeo ya kutoweza kwa binadamu kuelekeza hatua zake mwenyewe. (Yeremia 10:23) Zaidi ya hilo, Shetani, nyoka wa zamani, “ambaye anaongoza vibaya dunia nzima yote inayokaliwa,” analeta ole katika jaribio lake la mwisho la kukengeua aina ya binadamu kutoka ibada ya Yehova. Tekinolojia ya ki-siku-hizi imeifanya dunia iwe ndogo kama ujirani mmoja tu, ambapo chuki za kitaifa na za kijamii zinatikisa jamii ya kibinadamu mpaka misingi yayo, nao ule unaoitwa eti Umoja wa Mataifa, hauwezi kupata ponyo lenye kuleta matokeo. Kama isivyopata kuwa hapo zamani, mwanadamu anatawala mwanadamu kwa umizo lake. (Ufunuo 12:9, 12; Mhubiri 8:9, NW) Hata hivyo, Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu, Mfanyiza mbingu na dunia, amekuwa akifanya aina yake mwenyewe ya utikisaji kwa karibu miaka 90, katika kujitayarishia kutatua matatizo ya dunia mara moja na kwa wakati wote. Jinsi gani hivyo?
11. (a) Ni mtikiso gani unaoelezwa katika Hagai 2:6, 7? (b) Unabii wa Hagai unatimizwaje?
11 Kwenye Hagai 2:6, 7, NW, tunasoma hivi: “Kwa kuwa hivi ndivyo Yehova wa majeshi amesema, ‘Bado mara moja—ni kitambo kidogo—na mimi ninatikisa mbingu na dunia na bahari na nchi kavu. Na mimi nitatikisa mataifa yote, na vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote lazima vije ndani; na mimi nitajaza nyumba hii utukufu,’ Yehova wa majeshi amesema.” Tangu 1919 hasa, Yehova amefanya mashahidi wake wapige mbiu ya hukumu zake miongoni mwa elementi zote za jamii ya kibinadamu duniani. Mfumo wa ulimwengu wa Shetani umetahadharishwa kwa onyo la pote katika tufe.d Kadiri onyo hilo linavyopata nguvu, binadamu wenye kumhofu Mungu, vile “vitu vyenye kutamanika,” wamechochewa wajitenge na mataifa. Si kwamba wanatikiswa na kule kutetemeshwa katika tengenezo la Shetani. Lakini wanapotambua hali, wao wanafanya uamuzi wao wenyewe washiriki pamoja na jamii ya Yohana yenye kupakwa mafuta katika kuijaza utukufu nyumba ya Yehova ya ibada. Hilo linatimizwaje? Kwa kazi ya bidii ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. (Mathayo 24:14) Ufalme huu, ambao washiriki wao ni Yesu na wafuasi wake wapakwa-mafuta, utaendelea kusimama daima kwa utukufu wa Yehova ukiwa “ufalme usioweza kutikiswa.”—Waebrania 12:26-29, NW.
12. Ikiwa wewe umeanza kuitikia kazi ya kuhubiri iliyotabiriwa kwenye Mathayo 24:14, inakupasa wewe ufanye nini kabla halijatokea lile tetemeko la dunia kubwa la Ufunuo 6:12?
12 Je! wewe ni mmoja ambaye ameanza kuitikia kuhubiri huko? Je! pengine wewe ni mmoja wa wale mamilioni ambao katika miaka ya karibuni wamehudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu? Ikiwa ndivyo, zidi kufanya maendeleo katika funzo lako la ukweli wa Biblia. (2 Timotheo 2:15; 3:16, 17) Acha kabisa ule mtindo wa maisha wenye ufisadi wa jamii ya kidunia ya Shetani iliyohukumiwa maangamizi! Njoo na kuingia mpaka ndani ya jamii ya ulimwengu mpya ya Kikristo na ushiriki kikamili katika utendaji wayo kabla ya lile “tetemeko la dunia” la mwisho lenye kuleta uharibifu halijavunja vipande vipande ulimwengu wote wa Shetani. Lakini ni nini hilo tetemeko la dunia kubwa? Acheni tuone sasa.
Lile Tetemeko la Dunia Kubwa!
13. Ni kwa njia gani hilo tetemeko la dunia kubwa ni ono jipya kabisa kwa binadamu?
13 Ndiyo, hizi siku za mwisho zenye hatari zimekuwa wakati wa matetemeko ya dunia—halisi na ya kitamathali. (2 Timotheo 3:1) Lakini hapana mojapo matetemeko haya ambalo ndilo ule mtikiso mkubwa wa mwisho ambao Yohana anaona wakati wa kufunguliwa kwa kifungo cha sita. Wakati wa mitetemo ya utangulizi umekwisha. Linakuja sasa tetemeko la dunia kubwa ambalo ni jipya kabisa kuonwa na aina ya binadamu. Ni tetemeko kubwa sana hivi kwamba mitetemo na misukosuko linayosababisha haiwezi kupimwa kwa kipima-tetemeko cha Richter au kwa kipimo kinginecho cha kibinadamu. Hili si mshtuo wa mahali tu bali mtikiso wenye msiba mkubwa ambao unakumba “dunia” nzima yote, yaani, jamii yote ya kibinadamu iliyo fasiki.
14. (a) Ni unabii gani ambao hutabiri tetemeko la dunia kubwa na matokeo yalo? (b) Ni lazima unabii wa Yoeli na Ufunuo 6:12, 13 urejezee nini?
14 Wengine wa manabii wa Yehova walitabiri tetemeko la dunia kama hilo na matokeo yalo yenye kuleta uharibifu. Mathalani, yapata 820 K.W.K., Yoeli alisema juu ya “kuja kwa siku kuu na yenye kuvuvia hofu ya Yehova,” akitaarifu kwamba ndipo “jua lenyewe litageuzwa kuwa giza, na mwezi kuwa damu.” Baadaye, yeye anaongezea maneno haya: “Halaiki za watu, halaiki za watu zimo katika bonde la uamuzi, kwa kuwa siku ya Yehova i karibu katika uwanda-bonde wa uamuzi. Jua na mwezi vyenyewe kwa hakika vitakuwa vyenye giza, na nyota zenyewe hakika zitaondoa uangavu wazo. Na kutoka Sayuni Yehova mwenyewe atanguruma, na kutoka Yerusalemu yeye atatoa nje sauti yake. Na mbingu na dunia kwa hakika zitatikiswa; lakini Yehova atakuwa kimbilio kwa ajili ya watu wake, na ngome kwa ajili ya wana wa Israeli.” (Yoeli 2:31; 3:14-16, NW) Kutikiswa huku kungetumika kuhusu tu kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova wakati wa dhiki kubwa. (Mathayo 24:21) Kwa hiyo lile simulizi mlingano kwenye Ufunuo 6:12, 13 kimantiki lingetumika jinsi iyo hiyo.—Ona pia Yeremia 10:10; Sefania 1:14, 15.
15. Ni mtikiso gani wenye nguvu aliotabiri nabii Habakuki?
15 Yapata miaka 200 baada ya Yoeli, nabii Habakuki alisema na Mungu katika sala hivi: “O Yehova mimi nimesikia ripoti juu yako wewe. Mimi nimeogopa, O Yehova, utendaji wako. Katikati ya miaka O ulete kwenye uhai! Katikati ya miaka wewe na uufanye ujulikane. Wakati wa msukosuko, kuonyesha rehema wewe na ukumbuke.” Huo “msukosuko” ungekuwa nini? Habakuki anaendelea kutoa elezo dhahiri sana la dhiki kubwa, akisema kwa habari ya Yehova: “Yeye alisimama tuli, ili apate kutikisa dunia. Yeye aliona, na kisha akasababisha mataifa kuruka. . . . Pamoja na shutumu wewe ulienda ukipiga miguu kupitia dunia. Katika kasirani wewe ulienda ukiyapura mataifa. Hata hivyo, kwa habari yangu mimi, mimi nitachachawa katika Yehova mwenyewe; mimi nitakuwa mwenye shangwe katika Mungu wa wokovu wangu.” (Habakuki 3:1, 2, 6, 12, 18, NW) Lo! ni mtikiso wenye nguvu kama nini ambao Yehova atasababisha katika dunia yote wakati yeye atakapoyapura mataifa!
16. (a) Ni nini analotabiri nabii Ezekieli kwa ajili ya wakati ambao Shetani anafanya shambulio lake la mwisho juu ya watu wa Mungu? (b) Ni nini linalotokana na tetemeko la dunia kubwa la Ufunuo 6:12?
16 Ezekieli alitabiri kwamba wakati Gogu wa Magogu (Shetani aliyetwezwa) anapofanya shambulio la mwisho juu ya watu wa Mungu, Yehova atasababisha “tetemeko kubwa” litukie “katika udongo wa Israeli.” (Ezekieli 38:18, 19, NW) Ingawa huenda matetemeko ya dunia halisi yakahusika, inatupasa sisi kukumbuka kwamba Ufunuo umetolewa kwa ishara. Unabii huu pamoja na unabii mwingine uliotajwa ni wa ufananisho kabisa. Kwa sababu hiyo, kufunguliwa kwa kifungo cha sita inaelekea kunafunua ule upeo wa mitikiso yote ya huu mfumo wa mambo wa kidunia—lile tetemeko la dunia kubwa ambalo katika hilo binadamu wote wanaopinga enzi kuu ya Yehova Mungu wanaharibiwa.
Wakati wa Giza
17. Hilo tetemeko la dunia kubwa linaathirije jua, mwezi, na nyota?
17 Kama vile Yohana aendeleavyo kuonyesha, tetemeko la dunia kubwa linaandamana na matukio yenye kuogofya ambayo yanahusu hata mbingu. Yeye anasema: “Nalo jua likawa jeusi kama gunia la nywele, na mwezi mzima wote ukawa kama damu, na nyota zote za mbingu zikaanguka kwenye dunia, kama vile wakati mtini unapotikiswa na upepo mkali hurusha tini zao zisizoiva.” (Ufunuo 6:12b, 13, NW) Ni kituko chenye kugutusha kama nini! Je! wewe unaweza kuwazia giza lenye kuogopesha ambalo lingetokea kama unabii huo ungetimizwa kihalisi? Hakungekuwa tena na nuru ya jua yenye joto na yenye kufariji mchana! Hakungekuwa tena na nuru ya mwezi ya kirafiki na yenye rangi ya fedha usiku! Na zile miriadi za nyota hazingemetameta dhidi ya kisetiri-nyuma cha kimahameli cha anga. Badala ya hivyo, kungekuwa na weusi ti, wenye baridi, usiokoma.—Linga Mathayo 24:29.
18. Ni katika njia gani ‘mbingu zilipata kuwa zenye giza’ kwa ajili ya Yerusalemu katika 607 K.W.K.?
18 Katika maana ya kiroho, giza kama hilo lilitolewa unabii kwa Israeli wa kale. Yeremia alionya hivi: “Ukiwa mtupu ndivyo bara kwa ujumla litakuja kuwa, na je! mimi sitatimiza uharibifu kabisa? Kwa sababu hiyo bara litaomboleza, na mbingu zilizo juu zitakuwa giza.” (Yeremia 4:27, 28, NW) Katika 607 K.W.K. wakati unabii huo ulipotimizwa, mambo yalikuwa yenye giza kweli kweli kwa watu wa Yehova. Yerusalemu, jiji lao kuu, lilianguka kwa Wababuloni. Hekalu lao liliharibiwa, na bara lao likaachwa ukiwa. Kwa wao, hakukuwa na nuru yenye kufariji kutoka mbingu. Badala, ilikuwa kama vile Yeremia alivyoambia Yehova kwa kuomboleza: “Wewe umeua; wewe hukuonyesha huruma. Umefunga ufikio kwako wewe kwa tungamo la wingu, kwamba sala isipate kupenya.” (Maombolezo 3:43, 44, NW) Kwa Yerusalemu, giza hilo la kimbingu lilimaanisha kifo na uharibifu.
19. (a) Isaya, nabii wa Mungu anaelezaje habari ya giza katika mbingu juu ya Babuloni wa kale? (b) Ni wakati gani na jinsi gani unabii wa Isaya ulitimizwa?
19 Baadaye, giza linalofanana na hilo katika mbingu liliashiria uharibifu kwa Babuloni wa kale. Kwa habari ya hilo, nabii wa Mungu alivuviwa aandike hivi: “Tazama! Siku ya Yehova yenyewe inakuja, katili kwa kiruu na kasirani yenye kuwaka pia, ili kufanya bara liwe kitu cha mshangao, na kwamba iweze kutowesha wafanya dhambi wa bara kutoka kwayo. Kwa kuwa nyota zenyewe za zile mbingu na makundi ya Kesili yazo hazitameremesha nuru yazo; kwa hakika jua litakuwa giza wakati wa kutokea kwalo, na mwezi wenyewe hautafanya nuru yao kuangaza. Na mimi kwa hakika nitaonyesha wazi ubaya walo lenyewe juu ya bara lenye kuzaa, na kosa lao wenyewe juu ya waovu wenyewe.” (Isaya 13:9-11, NW) Unabii huu ulitimizwa katika 539 K.W.K. wakati Babuloni ilipoanguka kwa Wamedi na Waajemi. Unaeleza vizuri ule weusi ti, ule utotumaini, ule ukosefu wa nuru ya faraja kwa Babuloni ilipokuwa ikianguka milele kutoka cheo chayo cha kuwa serikali kuu ya ulimwengu.
20. Ni tokeo gani lenye kuhofisha linalongojea huu mfumo wa mambo wakati tetemeko la dunia kubwa linapopiga?
20 Kwa njia iyo hiyo, wakati tetemeko la dunia kubwa linapopiga, mfumo wote huu wa ulimwengu utagharikishwa katika tamausho la giza tititi. Vile vimeti viangavu, vyenye kung’aa vya mfumo wa kidunia wa Shetani havitatoa miale ya tumaini. Tayari leo, viongozi wa kisiasa wa dunia, hasa katika Jumuiya ya Wakristo, wana sifa mbaya sana kwa sababu ya ufisadi wao, kusema uwongo na mtindo wao wa maisha wa utovu wa adili. (Isaya 28:14-19) Hawawezi kuitibariwa tena. Nuru yao yenye kusinzia itapatwa na giza kabisa Yehova atekelezapo hukumu. Uvutano wao ulio kama mwezi juu ya mambo ya dunia utafunuliwa kuwa umetiwa damu, wenye kuleta kifo. Nyota zao mashuhuri za kilimwengu zitazimwa kama vimondo viangukavyo ghafula na zitatawanywa kama tini zisizoiva katika upepo-dhoruba wenye kuvuma. Tufe letu lote litatetemeka chini ya “dhiki kubwa kama ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21, NW) Lo! ni tazamio lenye kujaa hofu kama nini!
“Mbingu” Yaondoka
21. Katika njozi yake, Yohana anaona nini kuhusu “mbingu” na “kila mlima na kila kisiwa”?
21 Njozi ya Yohana inaendelea: “Na mbingu ikaondoka kama hati-kunjo inayokunjwa, na kila mlima na kila kisiwa viliondolewa mahali pavyo.” (Ufunuo 6:14, NW) Kwa wazi hizi si mbingu halisi au milima na visiwa halisi. Lakini hizo zinafananisha nini?
22. Katika Edomu ni aina gani za “mbingu” ‘zilizokunjwa, kama hati-kunjo’?
22 Kwa habari ya “mbingu,” sisi tunasaidiwa katika uelewevu wetu na unabii unaofanana na huo unaosema juu ya hasira kali ya Yehova dhidi ya mataifa: “Na wale wote wa lile jeshi la zile mbingu lazima waozee mbali. Na zile mbingu lazima zikunjwe kama hati-kunjo.” (Isaya 34:4, NW) Hasa Edomu lazima akione. Jinsi gani? Alishambuliwa na Wababuloni muda mfupi baada ya uharibifu wa Yerusalemu katika 607 K.W.K. Wakati huo, hakuna matukio yenye kutokeza yaliyorekodiwa kuwa yakitukia katika mbingu halisi. Lakini yalikuwako matukio yenye kuleta uharibifu katika “mbingu” za Edomu.e Mamlaka zake za serikali za kibinadamu zilishushwa kutoka cheo chazo kilichoinuliwa, mfano wa mbingu. (Isaya 34:5) ‘Zilikunjwa’ zikawa kana kwamba zimewekwa kando, kama hati-kunjo kuukuu ambayo haina matumizi yoyote tena kwa yeyote.
23. Ni “mbingu” gani ‘itakayoondoka kama hati-kunjo,’ nayo maneno ya Petro yanathibitishaje uelewevu huu?
23 Hivyo, “mbingu” inayopaswa ‘kuondoka kama hati-kunjo’ hurejeza kwenye serikali zinazopinga Mungu ambazo hutawala juu ya dunia hii. Hizo zitaondolewa kwa ukomo na yule Mpandaji-farasi mweupe. (Ufunuo 19:11-16, 19-21) Hilo linathibitishwa na aliyosema mtume Petro wakati alipotazama mbele kwenye matukio yaliyoashiriwa na kule kufunguliwa kwa kifungo cha sita: “Mbingu na dunia zilizopo sasa zimewekwa akiba kwa moto na zimehifadhiwa kwa ajili ya siku ya hukumu na ya uharibifu wa watu wasiohofu Mungu.” (2 Petro 3:7, NW) Lakini namna gani usemi huu, “kila mlima na kila kisiwa viliondolewa mahali pavyo”?
24. (a) Katika unabii wa Biblia, ni wakati gani inaposemwa kwamba milima na visiwa vinatikiswa au kuondolewa uimara? (b) ‘Milima ilitikisikaje’ wakati Ninawi ulipoanguka?
24 Katika unabii wa Biblia, milima na visiwa vinasemwa kuwa vinatikiswa au kuondolewa uimara wakati wa mabadiliko makubwa ya kisiasa. Mathalani, wakati wa kutabiri hukumu za Yehova dhidi ya Ninawi, nabii Nahumu aliandika: “Milima yenyewe imetikisika kwa ajili ya yeye, na vilima halisi vikajikuta vyenyewe vikiyeyuka. Nayo dunia itapinduliwa kwa sababu ya uso wake.” (Nahumu 1:5, NW) Hakuna maandishi yanayoonyesha kuvunjika kokote kwa milima halisi wakati Ninawi ulipoanguka kikweli katika 632 K.W.K. Lakini serikali kubwa ya ulimwengu ambayo hapo kwanza ilionekana kuwa kama mlima katika imara yayo ilianguka ghafula.—Linga Yeremia 4:24.
25. Kwenye ule mwisho unaokuja wa huu mfumo wa mambo, “kila mlima na kila kisiwa” vitaondolewaje mahali pavyo?
25 Kwa hiyo, kimantiki “kila mlima na kila kisiwa” kama inavyorejezewa mwanzoni mwa kufunguliwa kwa kifungo cha sita vingekuwa serikali za kisiasa na matengenezo yanayozitegemea ya ulimwengu huu ambazo zimeonekana kuwa imara sana kwa wengi wa aina ya binadamu. Zitatikiswa zitoke mahali pazo, kwa fadhaa na hofu ya wale ambao hapo kwanza waliziitibari. Kama vile unabii huo uendeleavyo kusimulia, hakutakuwa na shaka lolote kwamba ile siku kubwa ya hasira-kisasi ya Yehova na Mwana wake—lile tetemeko la mwisho kabisa ambalo linaondoa matengenezo yote ya Shetani—imekuja ikiwa na kisasi!
“Angukeni Juu ya Sisi na Kuficha Sisi”
26. Binadamu wanaopinga enzi kuu ya Mungu watatendaje katika hofu yao, na ni maneno gani ya hofu kuu watakayotamka?
26 Maneno ya Yohana yanaendelea: “Na wafalme wa dunia na wenye vyeo vya juu na makamanda wa kivita na matajiri na makamambe na kila mtumwa na kila mtu huru wakajificha wenyewe katika mapango na katika yale matungamo-miamba ya milima. Na wao walifuliza kusema kwa milima na kwa matungamo-miamba: ‘Angukeni juu ya sisi na kuficha sisi kutoka uso wa yule Mmoja aliyeketi juu ya kiti cha ufalme na kutoka hasira-kisasi ya Mwana-Kondoo, kwa sababu siku kubwa ya hasira-kisasi yao imekuja, na ni nani anaweza kusimama?’”—Ufunuo 6:15-17, NW.
27. Ni vilio gani vilivyotamkwa na Waisraeli wasio waaminifu wa Samaria, na maneno hayo yalitimizwaje?
27 Wakati Hosea alipokuwa akitamka hukumu ya Yehova juu ya Samaria, jiji kuu la ufalme wa kaskazini wa Israeli, yeye alisema hivi: “Sehemu za juu za Beth-aveni, dhambi ya Israeli, kwa kweli zitatoweshwa kabisa. Miiba na mibigili yenyewe itapanda juu ya madhabahu yao. Na kwa hakika watu watasema kwa milima yenyewe, ‘Funikeni sisi!’ na kwa vilima, ‘Angukeni juu ya sisi!’” (Hosea 10:8, NW) Maneno haya yalitimizwaje? Basi, wakati Samaria lilipoanguka kwa Waashuri wakatili katika 740 K.W.K. hapakuwa na mahali pa Waisraeli kukimbilia. Maneno ya Hosea huonyesha hisia ya utotumaini, hofu tupu, na kuachwa walikohisi watu hao walioshindwa. Wala vilima halisi wala matengenezo ya Samaria yaliyokuwa kama milima hayangeweza kuwapa himaya, hata ingawa yalikuwa yameonekana kuwa ya kudumu sana wakati uliopita.
28. (a) Ni onyo gani ambalo Yesu aliwapa wanawake wa Yerusalemu? (b) Onyo la Yesu lilitimizwaje?
28 Hali moja na hiyo, Yesu alipokuwa akipelekwa na askari-jeshi Waroma kwenye kifo, yeye alihutubia wanawake wa Yerusalemu na kusema: “Siku zinakuja ambazo katika hizo watu watasema, ‘Wenye furaha ni wale wanawake walio tasa, na matumbo-uzazi ambayo hayakuzaa na matiti ambayo hayakunyonyesha!’ Ndipo wataanza kusema kwa milima, ‘Angukeni juu ya sisi!’ na kwa vilima, ‘Funikeni sisi!’” (Luka 23:29, 30, NW) Ule uharibifu wa Yerusalemu ulioletwa na Waroma katika 70 W.K. umethibitishwa vizuri kimaandishi, na ni wazi kwamba maneno ya Yesu yana maana inayofanana na ile ya maneno ya Hosea. Wakati ule hapakuwa na mahali pa kujificha kwa Wayahudi ambao walikuwa wamebaki katika Yudea. Kokote walikojaribu kujificha katika Yerusalemu, au hata wakati walipokimbilia ngome ya Masada juu ya mlima, wao hawakuweza kuepuka wonyesho wenye jeuri wa hukumu ya Yehova.
29. (a) Wakati siku ya Yehova ya hasira-kisasi inapokuja, ni nini kitakachopata wale ambao wamejitoa kuunga mkono huu mfumo wa mambo? (b) Ni unabii gani wa Yesu utakaotimizwa wakati Yehova anapoonyesha hasira-kisasi Yake?
29 Sasa, kule kufunguliwa kwa kifungo cha sita kumeonyesha kwamba kitu fulani kama hicho kitatukia wakati wa siku inayokuja ya hasira-kisasi ya Yehova. Wakati wa kutikiswa kwa mwisho kabisa kwa huu mfumo wa mambo wa kidunia, wale waliojitoa kuuunga mkono watatafuta sana mahali pa kujificha, lakini hawatapata hata pamoja. Dini bandia, Babuloni Mkubwa, tayari imeshindwa vya kusikitisha sana kuwasaidia. Wala mapango katika milima halisi wala matengenezo ya kisiasa na ya kibiashara yaliyo mfano wa milima hayataandaa usalama wa kifedha au msaada mwingine wa aina yoyote. Hakuna kitu kitakachowakinga wasipatwe na hasira-kisasi ya Yehova. Hofu yao imeelezwa vizuri na Yesu: “Ndipo ishara ya Mwana wa binadamu itaonekana katika mbingu, na ndipo makabila yote ya dunia yatajipigapiga yenyewe kwa ombolezo, na yataona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbingu akiwa na nguvu na utukufu mkubwa.”—Mathayo 24:30, NW.
30. (a) Ni nini kinachodokezwa na swali hili: “Ni nani anaweza kusimama?” (b) Je! wowote wataweza kusimama wakati wa hukumu ya Yehova?
30 Ndiyo, wale ambao wamekataa kutambua mamlaka ya yule Mpandaji-farasi mweupe mwenye ushindi watalazimika kukubali kosa lao. Wanadamu ambao kwa kupenda wamekuwa mbegu ya yule nyoka wataelekeana na uharibifu wakati ulimwengu wa Shetani unapopitilia mbali. (Mwanzo 3:15; 1 Yohana 2:17) Hali ya ulimwengu kwenye wakati huo itakuwa ya aina ya kwamba, ni kana kwamba wengi watakuwa wakiuliza: “Ni nani anaweza kusimama?” Yaonekana kama watadhani hakuna yeyote kwa vyovyote ambaye anaweza kusimama akiwa anakubalika mbele za Mungu katika siku hiyo ya hukumu yake. Lakini watakuwa wenye kukosea, kama vile kitabu cha Ufunuo kinavyoendelea kuonyesha.
[Maelezo ya Chini]
a Matetemeko ya dunia halisi mara nyingi hutanguliwa na misukosuko yenye mtutumo ambayo husababisha mbwa kubweka au kutenda bila kutulia na hutaharakisha wanyama wengine na samaki, ingawa huenda wanadamu wasishuku mpaka tetemeko lenyewe linapopiga.—Ona Amkeni (Kiingereza), Julai 8, 1982, ukurasa 14.
b Ili kupata maelezo zaidi, ona kurasa 22, 24.
c Kwa zaidi ya miaka 35, kutoka 1895 mpaka 1931, maneno ya Luka 21:25, 28, 31 yalinukuliwa yakawekwa kwenye jalada la gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) dhidi ya kisetiri-nyuma cha mnara wa taa ukimulikia anga zenye dhoruba juu ya bahari yenye mchafuko.
d Mathalani, katika kampeni ya pekee katika 1931, Mashahidi wa Yehova binafsi walipelekea viongozi wa kidini, wanasiasa, na wafanya-biashara kotekote duniani, maelfu mengi ya kijitabu The Kingdom, the Hope of the World.
e Katika tumizi kama hilo la neno “mbingu,” unabii wa “mbingu mpya” katika Isaya 65:17, 18 ulikuwa na utimizo wao wa kwanza katika ule mfumo mpya wa kiserikali, uliohusu Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yeshua, uliosimamishwa katika Bara la Ahadi baada ya Waisraeli kurudi kutoka uhamisho wa Kibabuloni.—2 Nyakati 36:23; Ezra 5:1, 2; Isaya 44:28.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 105]
1914 Ulitangulia Kuonwa
“Ilikuwa katika K.K. 606, kwamba ufalme wa Mungu ulikwisha, taji liliondolewa, na dunia yote ikapewa Wasio Wayahudi. Miaka 2520 kutoka K.K. 606, itakwisha katika M.B. 1914.”f—The Three Worlds, kilichotangazwa 1877, ukurasa 83.
“Ithibati ya Biblia ni wazi na thabiti kwamba ‘Majira ya Mataifa’ ni kipindi cha miaka 2520, kutoka K.K. 606 kufika na kutia ndani M.B. 1914”—Studies in the Scriptures, Buku 2, kilichoandikwa na C. T. Russell na kikatangazwa 1889, ukurasa 79.
Charles Taze Russell na Wanafunzi wa Biblia wenzake waling’amua miongo kadhaa mapema zaidi kwamba 1914 ungeonyesha mwisho wa Majira ya Mataifa, au nyakati zilizowekwa za mataifa. (Luka 21:24) Ingawa katika siku hizo za mapema wao hawakuelewa kikamili hii ingemaanisha nini, wao walisadikishwa kwamba 1914 ingekuwa tarehe ya mabadiliko katika historia ya ulimwengu, nao walikuwa sahihi. Angalia dondoo hili linalofuata la nyusipepa:
“Ule mfyatuko wa vita wenye kuogopesha katika Ulaya umetimiza unabii usio wa kawaida. Kwa robo ya karne iliyopita, kupitia wahubiri na kupitia magazeti, wale ‘Wanafunzi wa Biblia,’ wanaojulikana vizuri zaidi kuwa ‘Wanamapambazuko wa Mileani,’ wamekuwa wakitangazia ulimwengu kwamba ile Siku ya Hasira-Kisasi iliyotolewa unabii na Biblia ingepambazuka katika 1914. ‘Lindeni kwa ajili ya 1914!’ kimekuwa ndicho kilio cha mamia ya waevanjeli wasafirio.”—The World, nyusipepa moja ya New York, Agosti 30, 1914.
[Maelezo ya Chini]
f Kwa uongozi wa kimungu, hao Wanafunzi wa Biblia hawakuwa wameng’amua kwamba hakukuwa na mwaka sufuri katikati ya “K.K.” na “M.B.” Baadaye, wakati utafiti ulipofanya ihitajiwe kabisa kurekebisha K.K. 606 kuwa 607 K.W.K., ule mwaka sufuri uliondolewa pia, hivi kwamba ule utabiri ukawa sahihi kwenye “M.B. 1914.”—Ona “The Truth Shall Make You Free,” kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1943, ukurasa 239.
[Picha katika ukurasa wa 106]
1914—Kigeukio cha Historia
Kile Kitabu Politikens Verdenshistorie—Historiens Magt og Mening kilichotangazwa 1987 katika Copenhagen, kinatoa oneleo hili kwenye ukurasa 40:
“Imani ya karne ya 19 katika mwendeleo ilipata pigo layo lenye kufisha katika 1914. Ule mwaka uliotangulia mfyatuko wa vita, mwanahistoria na mwanasiasa Mdanishi Peter Munch aliandika akiwa na matumaini mazuri hivi: ‘Ithibati yote iko dhidi ya uwezekano wa kutokea kwa vita kati ya serikali kubwa-kubwa za Ulaya. “Ile hatari ya vita” pia itatoweka katika wakati ujao, kama vile imefanya wakati kwa wakati tangu 1871.’
“Kwa kutofautisha, sisi tunasoma katika kumbukumbu zake za baadaye: ‘Ule mfyatuko wa vita katika 1914 ndio kigeukio kikubwa cha historia ya binadamu. Kutoka katika wakati maalumu ulio mwangavu wa maendeleo, ambao katika huo mambo yangefuatiliwa kwa usalama wenye kiasi, sisi tuliingia kizazi cha msiba, hofu kuu, na chuki, kukiwa na utosalama kila mahali. Hakuna yeyote angeweza kusema, na hata leo hakuna anayeweza kusema, kama giza lililoanguka juu yetu wakati huo litamaanisha uharibifu wenye kudumu wa muundo mzima wote wa kitamaduni ambao binadamu amejiumbia mwenyewe kwa mileani zilizopita.’”
[Picha katika ukurasa wa 110]
‘Kila mlima ukaondolewa mahali pao’
[Picha katika ukurasa wa 111]
Wakajificha wenyewe katika mapango
-
-
Kutia Muhuri Israeli wa MunguUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 19
Kutia Muhuri Israeli wa Mungu
Njozi ya 4—Ufunuo 7:1-17
Habari: Wale 144,000 watiwa muhuri, na umati mkubwa unaonwa umesimama mbele ya kiti cha ufalme cha Yehova na mbele ya Mwana-Kondoo
Wakati wa utimizo: Tangu kuketishwa katika kiti cha ufalme kwa Kristo Yesu katika 1914 na kuendelea kuingia Utawala wa Mileani wake
1. “Ni nani anaweza kusimama” wakati wa siku kubwa ya hasira-kisasi ya kimungu?
“NI NANI anaweza kusimama?” (Ufunuo 6:17, NW) Ndiyo, ni nani kweli kweli? Wakati siku kubwa ya hasira-kisasi ya kimungu inapokumba mfumo wa Shetani, watawala na watu wa ulimwengu huenda kwa kufaa wakauliza swali hilo. Itaonekana kwao kwamba kumbo hilo kubwa linalokuja litazima uhai wote wa kibinadamu. Lakini je! litafanya hivyo? Kwa furaha, nabii wa Mungu anatuhakikishia: “Kila mmoja ambaye anaita juu ya jina la Yehova ataponyoka akiwa salama.” (Yoeli 2:32, NW) Mitume Petro na Paulo wathibitisha uhakika huo. (Matendo 2:19-21; Warumi 10:13) Ndiyo, wale wanaoita juu ya jina la Yehova watakuwa waokokaji. Hao ni akina nani? Kadiri njozi inayofuata ikunjulikavyo, sisi tutaona.
2. Ni kwa nini ni jambo la kushangaza kwamba kutakuwa na waokokaji wa siku ya hukumu ya Yehova?
2 Kwa kweli ni jambo lenye kushangaza kwamba yapasa yeyote apitie siku ya Yehova ya hukumu akiwa hai, kwa kuwa mwingine wa manabii wa Mungu anaieleza kwa maneno haya: “Tazama! Upepo-dhoruba wa Yehova, hasira kali yenyewe, imetoka ikaenda nje, tufani yenye kwenda mbele ikifagia. Juu ya kichwa cha waovu itazunguka vuruvuru. Kasirani yenye kuwaka ya Yehova haitarudi nyuma mpaka yeye awe ameua na mpaka yeye awe ametekeleza mawazo ya moyo wake.” (Yeremia 30:23, 24, NW) Ni jambo la uharaka kwamba sisi tuchukue hatua za kusalimika katika dhoruba hiyo!—Mithali 2:22; Isaya 55:6, 7; Sefania 2:2, 3.
Zile Pepo Nne
3. (a) Ni utumishi gani wa pekee unaofanywa na malaika anaouona Yohana? (b) Ni nini kinachofananishwa na “pepo nne”?
3 Kabla ya Yehova kuachilia kiruu hiki, malaika wa kimbingu wanafanya utumishi wa pekee. Sasa Yohana anaona hilo katika njozi: “Baada ya hili mimi niliona malaika wanne wakisimama juu ya kona nne za dunia, wakishika sana pepo nne za dunia, kwamba upepo wowote usipate kupuliza juu ya dunia au juu ya bahari au juu ya mti wowote.” (Ufunuo 7:1, NW) Hili linamaanisha nini kwa sisi leo? Hizi “pepo nne” ni ufananisho halisi wa hukumu yenye kuharibu inayokaribia kuachiliwa juu ya jamii mbovu ya kidunia, juu ya “bahari” yenye kusukasuka ya binadamu waasi-sheria, na juu ya watawala walioinuka mfano wa miti ambao wanapata uungaji-mkono na utegemezo kutoka kwa watu wa dunia.—Isaya 57:20; Zaburi 37:35, 36.
4. (a) Malaika wanne wanawakilisha nini? (b) Tokeo linakuwa nini juu ya tengenezo la kidunia la Shetani wakati pepo nne zinapoachiliwa?
4 Hapana shaka, hawa malaika wanne wanawakilisha vikundi vinne vya kimalaika, ambavyo Yehova anatumia kuzuia utekelezo wa hukumu yake mpaka wakati uliowekwa. Malaika hao waachiliapo pepo nne za hasira-kisasi zizunguke vuruvuru wakati ule ule mmoja kutoka kaskazini, kusini, mashariki, na magharibi, kumbo hilo litakuwa kubwa mno. Litafanana, lakini kwa kadiri kubwa mno, na utumiaji wa Yehova wa pepo nne kutawanya Waelamu, akiwavunjavunja na kuwaulia mbali kabisa. (Yeremia 49:36-38) Itakuwa dhoruba ya upepo mkubwa mno yenye kukumba zaidi ya ile “tufani” ambayo kwayo Yehova alifutilia mbali taifa la Amoni. (Amosi 1:13-15, NW) Hakuna sehemu ya tengenezo la Shetani duniani ambayo itaweza kusimama katika siku ya kiruu cha Yehova, wakati yeye anapotetea enzi kuu yake kwa umilele wote utakaokuja.—Zaburi 83:15, 18; Isaya 29:5, 6.
5. Unabii wa Yeremia unatusaidiaje kuelewa kwamba hukumu za Mungu zitaenea dunia yote nzima?
5 Je! sisi tunaweza kuwa na hakika kwamba hukumu za Yehova zitakumba dunia nzima? Sikiliza tena nabii wake Yeremia: “Tazama! Afa moja linaenda kutoka taifa moja kwenda kwenye jingine, na tufani kubwa yenyewe itaamshwa juu kutoka sehemu za mbali zaidi sana za dunia. Na wale wenye kuuawa na Yehova kwa hakika watakuja kuwa katika siku hiyo kutoka mwisho mmoja wa dunia hadi kufika mwisho mwingine kabisa wa dunia.” (Yeremia 25:32, 33, NW) Ni wakati wa dhoruba hii yenye tufani kwamba giza litagharikisha ulimwengu huu. Mawakili wao wenye kutawala watatikiswa waingie ndani ya utowesho. (Ufunuo 6:12-14) Lakini wakati ujao hautakuwa wenye giza kwa kila mmoja. Basi, ni kwa ajili ya nani zile pepo nne zinazuiwa?
Kuwatia Muhuri Watumwa wa Mungu
6. Ni nani anayeambia malaika wazuie pepo nne, na hilo linaruhusu wakati kwa ajili ya nini?
6 Yohana anaendelea kueleza jinsi baadhi ya watu wanavyotiwa alama kwa ajili ya kuokoka, akisema: “Na mimi nikaona malaika mwingine akipanda juu kutoka kwenye zukio la jua, akiwa na muhuri wa Mungu anayeishi; na yeye alilia kwa sauti kubwa kwa wale malaika wanne ambao kwao ruhusa ilipewa ya kudhuru dunia na bahari, akisema: ‘Msidhuru dunia au bahari au miti, mpaka baada ya sisi tuwe tumetia muhuri watumwa wa Mungu wetu katika vipaji vya nyuso zao.’”—Ufunuo 7:2, 3, NW.
7. Ni nani hasa aliye malaika wa tano, na ni ithibati gani inayotusaidia tuthibitishe utambulisho wake?
7 Ingawa huyu malaika wa tano hatajwi jina, ithibati yote inaonyesha kwamba lazima awe Bwana Yesu aliyetukuzwa. Kupatana na kuwa kwa Yesu Malaika Mkuu, yeye anaonyeshwa hapa akiwa na mamlaka juu ya wale malaika wengine. (1 Wathesalonike 4:16; Yuda 9) Yeye anapanda juu kutoka mashariki, kama “wafalme kutoka zukio la jua”—Yehova na Kristo wake—ambao wanakuja kutekeleza hukumu, kama walivyofanya wafalme Dario na Sairasi wakati waliponyenyekeza Babuloni wa kale. (Ufunuo 16:12; Isaya 45:1; Yeremia 51:11; Danieli 5:31, NW) Malaika huyu anashabihi Yesu katika njia ya kwamba yeye ameaminishwa kazi ya kutia muhuri Wakristo wapakwa-mafuta. (Waefeso 1:13, 14) Na zaidi, wakati pepo zinapoachiliwa, ni Yesu anayeongoza majeshi ya kimbingu katika kutekeleza hukumu juu ya mataifa. (Ufunuo 19:11-16) Basi, kimantiki, Yesu angekuwa ndiye wa kuamuru kwamba uharibifu kwa tengenezo la kidunia la Shetani uzuiwe mpaka watumwa wa Mungu wawe wametiwa muhuri.
8. Kutia muhuri ni nini, nako kulianza wakati gani?
8 Huku kutia muhuri ni nini, na hawa watumwa wa Mungu ni nani? Kutia muhuri huku kulianza katika Pentekoste 33 W.K. wakati Wakristo Wayahudi wa kwanza walipopakwa mafuta kwa roho takatifu. Baadaye, Mungu aliendelea kuita na kupaka mafuta “watu wa mataifa.” (Warumi 3:29; Matendo 2:1-4, 14, 32, 33; 15:14, NW) Mtume Paulo aliandika juu ya Wakristo wapakwa-mafuta wakiwa na uhakikisho wa kwamba wao ‘ni wa Kristo’ na akaongeza kwamba Mungu “pia ametia muhuri wake juu yetu na ametupa sisi dalili ya kitu ambacho kitakuja, yaani, roho, katika mioyo yetu.” (2 Wakorintho 1:21, 22; linga Ufunuo 14:1, NW.) Hivyo, wakati watumwa hawa wanapolelewa kuwa wana wa kiroho wa Mungu, wanapokea dalili yenye kutangulia urithi wao wa kimbingu—muhuri au rehani. (2 Wakorintho 5:1, 5; Waefeso 1:10, 11) Ndipo wanapoweza kusema: “Roho yenyewe hutoa ushuhuda pamoja na roho yetu kwamba sisi tu watoto wa Mungu. Ikiwa, basi, sisi ni watoto, sisi ni warithi pia: warithi kweli kweli wa Mungu, lakini warithi washirika pamoja na Kristo, iwapo sisi tunateswa pamoja ili kwamba sisi tuweze pia kutukuzwa pamoja.”—Waroma 8:15-17, NW.
9. (a) Ni uvumilivu gani unaotakwa upande wa mabaki ya wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho? (b) Kutahiniwa kwa wale wapakwa-mafuta kutaendelea mpaka lini?
9 “Iwapo sisi tunateswa pamoja”—hiyo inamaanisha nini? Ili kupokea taji la uhai, Wakristo wapakwa-mafuta lazima wavumilie, wakiwa waaminifu mpaka kifo. (Ufunuo 2:10) Si shauri la ‘wakiisha okolewa, wanaokolewa daima.’ (Mathayo 10:22; Luka 13:24) Badala ya hivyo, wao wanapewa onyo hili la upole: “fanyeni yoteyote mwezayo mfanye kuitwa na kuchaguliwa kwa nyinyi kuwe hakika kwa ajili yenu wenyewe.” Kama vile mtume Paulo, mwishowe kabisa ni lazima wao waweze kusema: “Mimi nimepiga vita nzuri, mimi nimekimbia katika shindano mpaka mwisho, mimi nimeshika imani.” (2 Petro 1:10, 11; 2 Timotheo 4:7, 8, NW) Hivyo hapa duniani kule kutahiniwa na kupepetwa kwa yale mabaki ya wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho lazima kuendelee mpaka Yesu na malaika wanaoandamana naye wawe wamekwisha kuutia kikiki muhuri ‘katika kipaji cha uso’ wa hawa wote, kuwatambulisha kabisa kabisa, bila kutanguka, kuwa “watumwa wa Mungu wetu” waliojaribiwa na waaminifu. Ndipo muhuri unapokuwa alama ya daima. Kwa wazi, wakati pepo nne za dhiki zinapoachiliwa, Waisraeli wote wa kiroho watakuwa wamekwisha tiwa muhuri kabisa kabisa, hata ingawa wachache watakuwa wangali wanaishi katika mnofu. (Mathayo 24:13; Ufunuo 19:7) Hesabu nzima ya washiriki itakuwa imekamilika!—Warumi 11:25, 26.
Ni Wangapi Wanatiwa Muhuri
10. (a) Ni maandiko gani yanaonyesha kwamba hesabu ya watiwa muhuri ina kikomo? (b) Ni nini jumla ya hesabu iliyotiwa muhuri, na wao wanaorodheshwaje?
10 Yesu aliambia wale waliokuwa katika mstari wa huku kutiwa muhuri: “Msiwe na hofu, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu ametoa kibali cha kuwapa nyinyi ufalme.” (Luka 12:32, NW) Maandiko mengine, kama vile Ufunuo 6:11 na Warumi 11:25, huonyesha kwamba hesabu ya hili kundi dogo ina kikomo kweli kweli na, kwa hakika, ilikusudiwa kimbele. Maneno ya Yohana yanayofuata yanathibitisha hili: “Na mimi nikasikia hesabu ya wale ambao walitiwa muhuri, mia na arobaini na nne elfu, waliotiwa muhuri kutoka kila kabila la wana wa Israeli: Kutoka kabila la Yuda elfu kumi na mbili walitiwa muhuri; kutoka kabila la Reubeni elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Gadi elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Asheri elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Naftali elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Manase elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Simeoni elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Lawi elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Isakari elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Zebuloni elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Yosefu elfu kumi na mbili; kutoka kabila la Benyamini elfu kumi na mbili walitiwa muhuri.”—Ufunuo 7:4-8, NW.
11. (a) Ni kwa nini lile rejezo kwa makabila 12 halingeweza kutumika kuhusu Israeli halisi, wa mnofu? (b) Ni kwa nini Ufunuo huorodhesha makabila 12? (c) Ni kwa nini hakuna kabila ambalo hilo pekee ndilo la kifalme au la kikuhani katika Israeli wa Mungu?
11 Je! hii haingeweza kuwa inarejeza kwa Israeli halisi, wa mnofu? La, kwa kuwa Ufunuo 7:4-8 hutofautiana na ile orodha ya kawaida ya kikabila. (Hesabu 1:17, 47) Kwa wazi, orodha hii hapa si kwa kusudi la kutambulisha Wayahudi wa mnofu kwa makabila yao bali ni kuonyesha muundo wa kitengenezo kama huo kwa Israeli wa kiroho. Hili linasawazika. Wanapaswa waweko washiriki 144,000 wa hili taifa jipya—12,000 kutoka kila mojapo makabila 12. Hakuna kabila katika huyu Israeli wa Mungu ambalo hilo pekee ndilo la kifalme au la kikuhani. Taifa lote kwa ujumla litatawala likiwa wafalme, na taifa lote kwa ujumla litatawala likiwa makuhani.—Wagalatia 6:16; Ufunuo 20:4, 6.
12. Ni kwa nini inafaa kwamba wale wazee 24 wanaimba mbele ya Mwana-Kondoo maneno ya ule wimbo wa Ufunuo 5:9, 10?
12 Ijapokuwa Wayahudi asilia na waongofu wa Kiyahudi walipewa fursa ya kwanza ili wachaguliwe kwa ajili ya kuwa Israeli wa kiroho, ni wachache tu wa taifa hilo walioitikia. Kwa hiyo Yehova aliwatolea mwaliko wale wasio Wayahudi. (Yohana 1:10-13; Matendo 2:4, 7-11; Warumi 11:7) Kama vile kwa habari ya Waefeso, ambao hapo kwanza walikuwa “wametenganishwa na dola la Israeli,” sasa watu wasio Wayahudi wangeweza kutiwa muhuri kwa roho ya Mungu na kuwa sehemu ya kundi la Wakristo wapakwa-mafuta. (Waefeso 2:11-13; 3:5, 6; Matendo 15:14) Basi, inafaa wazee 24 kuimba mbele za Mwana-Kondoo: “Kwa damu yako wewe ulinunua watu kwa ajili ya Mungu kutoka kila kabila na ulimi na kikundi cha watu na taifa, na wewe ulifanya wao kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao wanapaswa kutawala wakiwa wafalme juu ya dunia.”—Ufunuo 5:9, 10, NW.
13. Ni kwa nini ilifaa Yakobo ndugu-nusu ya Yesu aandike barua yake “kwa makabila kumi na mawili yaliyotawanyika kotekote”?
13 Kundi la Kikristo ni “jamii teule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu.” (1 Petro 2:9, NW) Likichukua mahali pa Israeli asilia likiwa taifa la Mungu, linakuwa Israeli mpya ambaye ni “‘Israeli’ kikweli.” (Warumi 9:6-8; Mathayo 21:43, NW)a Kwa sababu hii, ilifaa kabisa Yakobo ndugu-nusu ya Yesu aandike barua yake ya kiuchungaji “kwa makabila kumi na mawili yaliyotawanyika kotekote,” yaani, kwa kundi la ulimwenguni pote la Wakristo wapakwa-mafuta ambalo baadaye hesabu yalo ingekuwa 144,000.—Yakobo 1:1, NW.
Israeli wa Mungu Leo
14. Ni nini linaloonyesha kwamba bila ugeugeu Mashahidi wa Yehova wameshikilia kwamba 144,000 ni hesabu halisi ya wale wanaojumlika kuwa Israeli wa kiroho?
14 Kwa kupendeza, Charles T. Russell, alitambua 144,000 kuwa hesabu halisi ya watu mmoja mmoja wanaojumlika kuwa Israeli wa kiroho. Katika The New Creation, Buku 6 la mfululizo wake wa Studies in the Scriptures, kilichotangazwa 1904, yeye aliandika: “Sisi tuna kila sababu kuitikadi kwamba ile hesabu dhahiri, iliyo imara ya wateule [wapakwa-mafuta waliochaguliwa] ni ile ambayo imetaarifiwa mara kadhaa katika Ufunuo (7:4; 14:1); yaani, 144,000 ‘waliokombolewa kutoka miongoni mwa wanadamu.’” Katika Light, Kitabu cha Kwanza, kilichotangazwa katika 1930 na Wanafunzi wa Biblia, ilitaarifiwa hali kadhalika hivi: “Hivyo washiriki 144,000 wa mwili wa Kristo wako katika kusanyiko wakionyeshwa kuwa wamechaguliwa na kupakwa mafuta, au kutiwa muhuri.” Bila ugeugeu Mashahidi wa Yehova wameshikilia oni la kwamba kihalisi Wakristo wapakwa-mafuta 144,000 wanajumlika kuwa Israeli wa kiroho.
15. Kabla tu ya siku ya Bwana, wanafunzi wa Biblia wenye mioyo myeupe walifikiri Wayahudi asilia wangefurahia nini baada ya Majira ya Mataifa kuisha?
15 Hata hivyo, je! Waisraeli asilia leo hawastahili kadiri fulani ya upendeleo wa pekee? Katika pindi iliyokuwa kabla tu ya siku ya Bwana, wakati wanafunzi wa Biblia wenye mioyo myeupe walipokuwa wakigundua tena nyingi za kweli za msingi za Neno la Mungu, ilidhaniwa kwamba Majira ya Mataifa yakiisha, Wayahudi wangefurahia tena msimamo wenye kibali mbele za Mungu. Hivyo, kitabu cha C. T. Russell The Time Is at Hand (Buku 2 la Studies in the Scriptures), kilichotangazwa 1889, kilitumia Yeremia 31:29-34 kuhusu Wayahudi asilia, na kueleza: “Ulimwengu ni shahidi wa uhakika wa kwamba adhabu ya Israeli chini ya utawala wa wasio Wayahudi imekuwa ikiendelea tangu K.K. [607], kwamba ingali inaendelea, na kwamba hakuna sababu ya kutazamia mtengenezo mpya wa kitaifa upesi zaidi ya M.B. 1914, kile kikomo cha ‘nyakati saba’ zao—miaka 2520.” Ilielekea kwamba wakati huo Wayahudi wangepata urudisho wa kitaifa, na kwa wazi tazamio hilo lilitiwa uangavu 1917, wakati Julisho-Wazi la Balfour lilipoahidi kuunga mkono Uingereza kwa kufanya Palestina kuwa kao la kitaifa kwa ajili ya Wayahudi.
16. Ni jitihada gani walizofanya Mashahidi wa Yehova kufikia Wayahudi asilia wakiwa na ule ujumbe wa Kikristo, na kukawa na tokeo gani?
16 Kufuata vita ya kwanza ya ulimwengu, Palestina ikawa eneo chini ya usimamizi wa Uingereza, na njia ikafunguka Wayahudi warudi kwenye bara hilo. Katika 1948 Dola la kisiasa la Israeli lilitokezwa. Je! hiyo haikuonyesha kwamba Wayahudi walikuwa katika mstari wa kupata baraka za kimungu? Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova waliitikadi kwamba ilikuwa hivyo. Hivyo, katika 1925 walitangaza kitabu chenye kurasa 128, Comfort for the Jews. Katika 1929 walitoa buku lenye kuvutia la kurasa 360, Life, ambalo lilikusudiwa livutie Wayahudi na pia lilishughulika na kitabu cha Biblia cha Ayubu. Jitihada kubwa zilifanywa, hasa katika Jiji la New York, kufikia Wayahudi kwa huu ujumbe wa Kimesiya. Kwa furaha, watu wachache mmoja mmoja waliitikia, lakini Wayahudi kwa ujumla, kama babu zao wa karne ya kwanza, waliikataa ithibati ya kuwapo kwa Mesiya.
17, 18. Watumwa wa Mungu walikuja kuelewa nini kuhusu agano jipya na unabii wa Biblia wa urudisho?
17 Ilikuwa wazi kwamba Wayahudi, wakiwa taifa, hawakuwa yule Israeli aliyeelezwa katika Ufunuo 7:4-8 au katika unabii mwingine wa Biblia unaohusu siku ya Bwana. Wakifuata pokeo, Wayahudi waliendelea kuepuka kutumia jina la kimungu. (Mathayo 15:1-3, 7-9) Kikizungumzia Yeremia 31:31-34, kitabu Jehovah, kilichotangazwa na Mashahidi wa Yehova katika 1934, kilitaarifu hivi kwa mkataa: “Lile agano jipya halihusiani kwa vyovyote na wazao asilia wa Israeli pamoja na aina ya binadamu kwa ujumla, bali . . . lina mpaka kwa Israeli wa kiroho tu.” Unabii wa Biblia juu ya urudisho hauhusu wala Wayahudi asilia wala Israeli ya kisiasa, ambayo ni mshiriki wa Umoja wa Mataifa na ni sehemu ya ulimwengu ambao Yesu alizungumzia kwenye Yohana 14:19, 30 na 18:36.
18 Katika 1931 watumwa wa Mungu duniani walikuwa wamepokea, kwa shangwe kubwa, jina Mashahidi wa Yehova. Wao waliweza kukubaliana kwa moyo wote na maneno ya Zaburi 97:11, NW: “Nuru yenyewe imemeta juu ya mwadilifu, na kushangilia hata kwa ajili ya wale walio wanyoofu katika moyo.” Wao wangeweza kufahamu kwamba Israeli wa kiroho pekee walikuwa wameletwa ndani ya agano jipya. (Waebrania 9:15; 12:22, 24) Waisraeli asilia wasioitikia hawakuwa na sehemu humo, wala aina ya binadamu kwa ujumla. Uelewevu huu ulifungulia njia mmeto mwangavu wa nuru ya kimungu, wenye kutokeza sana katika habari ya tarehe za historia ya kitheokrasi. Huo ungefunua jinsi Yehova atoavyo kwa wingi sana rehema, fadhili za upendo, na ukweli kwa wanadamu wote ambao wanamkaribia yeye. (Kutoka 34:6; Yakobo 4:8) Ndiyo, wengine mbali na Israeli wa Mungu wangenufaishwa na uzuifu wa malaika wa pepo nne za uharibifu. Hao wangekuwa nani? Je! wewe ungeweza kuwa mmoja wao? Acheni tuone sasa.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kufaa, jina Israeli humaanisha “Mungu Hushindana; Mwenye Kushindana (Mwendelevu) Pamoja na Mungu.”—Mwanzo 32:28, New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 114]
[Picha katika ukurasa wa 116, 117]
Uteuzi wa ujumla wa Israeli wa kweli wa Mungu uliendelea kuanzia siku ya Pentekoste 33 W.K. kufika 1935 wakati, kwenye mkusanyiko wenye kufanyiza historia wa Mashahidi wa Yehova katika Washington, D.C., mkazo uligeuzwa ukaelekezwa kwenye kukusanywa kwa umati mkubwa wenye matazamio ya uhai wa kidunia (Ufunuo 7:9)
-
-
Umati Mkubwa Wenye Watu Wengi SanaUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 20
Umati Mkubwa Wenye Watu Wengi Sana
1. Baada ya kueleza habari ya kutiwa muhuri kwa wale 144,000, Yohana anaona kikundi gani kingine?
AKIISHA kueleza habari ya kutiwa muhuri kwa 144,000, Yohana anaendelea kuripoti mmojapo mafunuo yenye kutaharakisha zaidi sana katika Andiko lote. Lazima moyo wake uwe uliruka-ruka kwa shangwe alipokuwa akiuripoti, akisema: “Baada ya vitu hivi mimi nikaona, na, tazama! umati mkubwa ambao hakuna binadamu aliyeweza kuhesabu kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na ndimi, wakisimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wamevalia majoho meupe; na kulikuwa na matawi ya mitende katika mikono yao.” (Ufunuo 7:9, NW) Ndiyo, kuzuiliwa kwa zile pepo nne kunaruhusu wakati kwa ajili ya wokovu wa kikundi kingine mbali na washiriki 144,000 wa Israeli wa kiroho: umati mkubwa wa lugha nyingi, wa kimataifa.a—Ufunuo 7:1.
2. Waelezaji wa kilimwengu wameelezaje umati mkubwa, na hata Wanafunzi wa Biblia zamani walionaje kikundi hiki?
2 Waelezaji wa kilimwengu wamefasiri huu umati mkubwa kuwa watu wa mnofu wasio Wayahudi ambao wameongolewa kwenye Ukristo au kuwa Wakristo wafia-imani wanaoelekea mbinguni. Zamani, hata Wanafunzi wa Biblia waliwaona kuwa jamii ya pili ya kimbingu, kama ilivyotajwa katika 1886 katika Buku I la Studies in the Scriptures, The Divine Plan of the Ages: “Wao wanapoteza zawadi ya kiti cha ufalme, na ile asili ya kimungu, lakini mwishowe watafikia uzawa wakiwa viumbe wa roho wa hali ya chini zaidi ya asili ya kimungu. Ingawa hawa ni wakfu kikweli, wao wanashindwa na roho ya ulimwengu kwa kadiri ya kwamba wao wanakosa kutoa maisha yao kuwa dhabihu.” Hata karibuni zaidi kama 1930, hilo wazo lilitolewa katika Light, Kitabu cha Kwanza: “Wale wanaojumlika kuwa huu umati mkubwa wanashindwa kuitikia mwaliko wa kuwa mashahidi wenye bidii kwa ajili ya Bwana.” Ilielezwa kuwahusu kuwa kikundi cha wenye uadilifu wa kujifanyia wenyewe waliokuwa na maarifa ya ukweli lakini walifanya kidogo sana kuuhubiri. Walipaswa kwenda mbinguni wakiwa jamii ya pili ambayo haingeshiriki kutawala pamoja na Kristo.
3. (a) Ni tumaini gani walilotolewa wengine wa wale wenye mioyo inayofaa ambao baadaye walikuwa wenye bidii katika kazi ya kuhubiri? (b) Katika 1923 Mnara wa Mlinzi ulielezaje mfano wa kondoo na mbuzi?
3 Hata hivyo, kulikuwako wengine walioshirikiana na Wakristo wapakwa-mafuta ambao baadaye walikuwa wenye bidii zaidi sana katika kazi ya kuhubiri. Wao hawakuwa na tamaa za kwenda mbinguni. Kweli kweli, tumaini lao lilipatana na kichwa cha hotuba iliyotolewa na Mashahidi wa Yehova kuanzia 1918 kufika 1922. Mwanzoni kabisa, hiyo ilikuwa “Ulimwengu Umekoma—Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.”b Upesi baada ya hapo gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1923, lilieleza mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi (Mathayo 25:31-46), likataarifu: “Kondoo huwakilisha vikundi vyote vya mataifa, si vilivyozaliwa kwa roho lakini vyenye mwelekeo wa uadilifu, ambavyo kiakili hukiri Yesu Kristo kuwa Bwana na ambavyo hutazamia na kutumaini wakati ulio bora chini ya utawala wake.”
4. Nuru kuhusu jamii ya kidunia ilipataje kuwa nyangavu zaidi katika 1931? katika 1932? katika 1934?
4 Miaka kadhaa baadaye, katika 1931, Vindication, Kitabu cha Kwanza, kilizungumzia Ezekieli sura ya 9 kikitambulisha wale watu wenye kutiwa alama juu ya kipaji cha uso kwa ajili ya kuhifadhiwa kwenye mwisho wa ulimwengu kuwa kondoo wa huo mfano wa juu. Vindication, Kitabu cha Tatu, kilichotolewa 1932, kilieleza habari ya unyoofu wa mwelekeo wa moyoni wa mtu asiye Mwisraeli, Yehonadabu, aliyejiunga na Mfalme mpakwa-mafuta, Yehu Mwisraeli katika gari lake akaenda naye akaone bidii ya Yehu katika kufisha wanadini bandia. (2 Wafalme 10:15-17) Kitabu hicho kilitoa elezo hili: “Yehonadabu aliwakilisha au akatangulia kuweka kivuli cha jamii ya watu ambao wako duniani leo katika wakati ambao kazi ya Yehu [ya kujulisha wazi hukumu za Yehova] inaendelea, ambao ni wa nia njema, hawapatani na tengenezo la Shetani, ambao wanachukua msimamo wao katika upande wa uadilifu, na ndio ambao Bwana atahifadhi hai wakati wa Har–Magedoni awachukue kupitia taabu hiyo, na kuwapa uhai wa milele duniani. Hao wanajumlika kuwa ‘jamii ya kondoo.’ Katika 1934 Mnara wa Mlinzi ulieleza wazi kwamba Wakristo hawa walio na matumaini ya kidunia wapaswa wajiweke wakfu kwa Yehova na wabatizwe. Nuru kuhusu hii jamii ya kidunia ilikuwa iking’aa kwa uangavu zaidi na zaidi.—Mithali 4:18.
5. (a) Ni utambulisho gani wa umati mkubwa uliofanywa katika 1935? (b) Wakati J. F. Rutherford katika 1935 alipouliza wanamkusanyiko waliokuwa na tumaini la kuishi milele duniani wasimame, kulitukia nini?
5 Ule uelewevu wa Ufunuo 7:9-17 ulikuwa sasa unakaribia kububujika pamoja na uangavu wao wote wenye kumeremeta! (Zaburi 97:11) Kwa kurudiarudia gazeti Mnara wa Mlinzi lilikuwa limeonyesha tumaini la kwamba mkusanyiko mmoja uliokuwa umeratibiwa Mei 30 kufika Juni 3, 1935, katika Washington D.C., U.S.A., ungekuwa “faraja halisi na manufaa” kwa wale waliotolewa picha na Yehonadabu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa! Katika hotuba yenye kusisimua juu ya “Mkutano Mkubwa” iliyotolewa kwa wanamkusanyiko wapatao 20,000, J. F. Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa akielekeza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, alitoa uthibitisho wa Kimaandiko kwamba kondoo wengine wa ki-siku-hizi ni jamii ile ile ya umati mkubwa wa Ufunuo 7:9. Kwenye upeo wa hotuba hii, msemaji huyo aliuliza: “Wale wote ambao wana tumaini la kuishi milele juu ya dunia tafadhali mnaweza kusimama?” Sehemu kubwa ya hadhirina ilipokuwa ikisimama, msemaji alitangaza: “Tazameni! Mkutano mkubwa!” Kukawa na kimya, kikifuatwa na vigelegele vyenye mngurumo. Ilifurahi kama nini jamii ya Yohana—na pia kikundi cha Yehonadabu! Keshoye, Mashahidi wapya 840 walibatizwa, walio wengi zaidi wa hawa wakidai kuwa wa huo umati mkubwa.
Kuthibitisha Utambulisho wa Umati Mkubwa
6. (a) Ni kwa nini sisi tunaweza kuelewa waziwazi kwamba umati mkubwa ni kikundi cha ki-siku-hizi cha Wakristo walio wakfu ambao wanatumaini kuishi milele duniani? (b) Yale majoho meupe ya huo umati mkubwa yanafananisha nini?
6 Sisi tunaweza kutaarifuje tukiwa na uhakika sana hivyo kwamba ule umati mkubwa ni kikundi hiki cha ki-siku-hizi cha Wakristo waliojiweka wakfu ambao wanatumaini kuishi milele juu ya dunia ya Mungu? Wakati uliotangulia, Yohana alikuwa ameona katika njozi kikundi cha kimbingu ‘ambacho kilinunuliwa kwa ajili ya Mungu kutoka kila kabila na ulimi na vikundi vya watu na taifa.’ (Ufunuo 5:9, 10, NW) Umati mkubwa una chanzo kinachofanana na hicho lakini wanakoenda ni tofauti. Tofauti na Israeli wa Mungu, hesabu yao haikukusudiwa kimbele. Hakuna mtu anayeweza kusema mapema watakuwa wangapi. Majoho yao meupe yameoshwa kwa damu ya yule Mwana-Kondoo, kufananisha kwamba wao wana msimamo wenye uadilifu mbele za Yehova kwa sababu ya imani yao katika dhabihu ya Yesu. (Ufunuo 7:14) Nao wanapungapunga matawi ya mitende, wakimshangilia Mesiya kuwa Mfalme wao.
7, 8. (a) Kule kupungwapungwa kwa matawi ya mitende bila shaka kulimkumbusha mtume Yohana juu ya matukio gani? (b) Ni nini maana ya uhakika wa kwamba hao wa umati mkubwa wanapungapunga matawi ya mitende?
7 Anapotazama katika njozi hii, mawazo ya Yohana lazima yawe yanamrudisha nyuma zaidi ya miaka 60 kwenye juma la mwisho la Yesu duniani katika Nisani 9, 33 W.K., wakati umati ulipokuja makundi makundi ili kumkaribisha Yesu ndani ya Yerusalemu, wao “walichukua matawi ya mitende wakatoka nje kumlaki. Na wao wakaanza kupaaza sauti: ‘Okoa, sisi twaomba wewe! Mbarikiwa ni yeye ambaye anakuja katika jina la Yehova, hata mfalme wa Israeli!’” (Yohana 12:12, 13, NW) Hali moja na hiyo, kule kupungapunga matawi ya mitende na kupaaza sauti upande wa umati mkubwa huonyesha shangwe yao isiyozuilika katika kumkubali Yesu kuwa Mfalme wa Yehova aliyewekwa rasmi.
8 Pasipo shaka, hayo matawi ya mitende na vilio vya kuchachawa pia vinamkumbusha Yohana ile Sikukuu ya Vibanda ya kale ya Israeli. Kwa ajili ya sikukuu hii Yehova aliamuru: “Na ni lazima nyinyi mjichukulie kwa ajili yenu wenyewe katika siku ya kwanza tunda la miti mizuri sana, na matagaa ya mitende na matanzu ya miti yenye matawi na mipopla ya bonde la mvo, na ni lazima nyinyi mshangilie mbele za Yehova Mungu wenu siku saba.” Matawi ya mitende yalitumiwa kuwa alama ya kushangilia. Vibanda vya muda vilikuwa kikumbusha kwamba Yehova alikuwa amewaokoa watu wake kutoka Misri, waishi katika mahema katika jangwa. “Mkazi mgeni na mvulana asiye na baba na mjane” walishiriki hii sikukuu. Waisraeli wote walipaswa ‘wawe si kitu ila wenye kujawa na shangwe.’—Walawi 23:40; Kumbukumbu 16:13-15, NW.
9. Umati mkubwa unajiunga katika kilio gani cha shangwe?
9 Basi, inafaa kwamba, umati mkubwa, ingawa si sehemu ya Israeli wa kiroho, upungepunge matawi ya mitende kwa kuwa wanaonyesha kwa shangwe na asante kwamba ushindi na wokovu hutoka kwa Mungu na Mwana-Kondoo kama Yohana anavyoona hapa: “Nao hufuliza kulia kwa sauti kubwa, kusema: ‘Wokovu wetu ni kwa Mungu wetu, ambaye ameketi juu ya kiti cha ufalme, na kwa Mwana-Kondoo.’” (Ufunuo 7:10, NW) Ijapokuwa wao wametengwa kutoka vikundi vyote vya kikabila, huo umati mkubwa unalia kwa hiyo “sauti kubwa” moja tu. Wao wanawezaje kufanya hivi, wajapokuwa ni wa mataifa na lugha mbalimbali?
10. Umati mkubwa unaweza kuliaje kwa umoja kwa “sauti kubwa” moja ijapokuwa ni wa mataifa na lugha mbalimbali?
10 Huu umati mkubwa ni sehemu ya tengenezo la mataifa mengi ambalo ndilo pekee lina umoja kweli kweli duniani leo. Wao hawana viwango tofauti-tofauti kwa nchi tofauti-tofauti bali wanatumia kwa ajili ya upatani kanuni za Biblia zinazofaa kokote wanakoishi. Wao hawajiingizi katika harakati za kitaifa, zenye kutaka mapinduzi bali wao ‘wamefua panga zao zikawa majembe ya plau.’ (Isaya 2:4, NW) Wao hawana mgawanyiko wa mafarakano au vikundi vya kidini, hivi kwamba wanapaaza sauti zilizovurugika au jumbe za pamoja zenye kupingana-pingana kama zinavyofanya dini za Jumuiya ya Wakristo; wala wao hawaachii jamii ya viongozi wa kidini wenye kulipwa mshahara wafanye kusifu kwa ajili yao. Wao hawapaazi sauti kwamba wokovu wao hutoka kwa roho takatifu kwa kuwa wao si watumishi wa kamungu ka utatu. Katika maeneo ya kijiografia 200 kuzunguka dunia, wao wana umoja katika kuita juu ya jina la Yehova wanaposema lugha safi ya ukweli. (Sefania 3:9) Kwa kufaa, wao wanakiri peupe kwamba wokovu wao unakuja kutoka kwa Yehova Mungu wa wokovu, kupitia Yesu Kristo, Wakili Mkuu Wake wa wokovu.—Zaburi 3:8; Waebrania 2:10.
11. Tekinolojia ya ki-siku-hizi imesaidiaje wale wa umati mkubwa kufanya sauti yao kubwa iwe kubwa hata zaidi?
11 Tekinolojia ya ki-siku-hizi imesaidia kufanya sauti kubwa ya umati mkubwa wenye umoja ivume kwa ukubwa hata zaidi. Hakuna kikundi kinginecho cha kidini duniani ambacho kina uhitaji wa kuchapisha misaada ya kujifunza Biblia katika lugha zaidi ya 400, kwa maana hakuna kikundi kinginecho ambacho kinapendezwa na kufikia vikundi vyote vya watu wa dunia kwa ujumbe mmoja wenye umoja. Kama msaada zaidi katika jambo hili, chini ya uangalizi wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lililopakwa mafuta mfumo uitwao, Multilanguage Electronic Phototypesetting System (MEPS) uliundwa. Kufikia wakati kitabu hiki kilipochapishwa, namna tofauti-tofauti za MEPS zinatumiwa katika maeneo zaidi ya 125 kuzunguka dunia, na jambo hili limesaidia kufanya iwezekane utangazaji sawia wa jarida la mara mbili kwa mwezi, Mnara wa Mlinzi, katika lugha zaidi ya 130. Pia watu wa Yehova wanatangaza kisawia, vitabu kama hiki, kwa lugha kadhaa. Hivyo, Mashahidi wa Yehova, ambao ule umati mkubwa ndio walio wengi sana, wanaweza kila mwaka kugawa mamia ya mamilioni ya vichapo katika lugha zote zinazojulikana vizuri zaidi, wakiwezesha misongamano mingi zaidi ya kutoka makabila yote na lugha wajifunze Neno la Mungu na kuunga sauti zao kwenye ile sauti kubwa ya umati mkubwa.—Isaya 42:10, 12.
Mbinguni au Duniani?
12, 13. Ni katika njia gani umati mkubwa ‘umesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo’?
12 Sisi tunajuaje kwamba ‘kusimama mbele ya kiti cha ufalme’ hakumaanishi kwamba umati mkubwa umo mbinguni? Kuna ithibati nyingi iliyo wazi juu ya jambo hili. Mathalani, neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “mbele” (e·noʹpi·on) humaanisha kihalisi “katika [mwono wa]” nalo linatumiwa mara kadhaa kuhusu wanadamu duniani ambao wako “mbele” au “katika mwono wa” Yehova. (1 Timotheo 5:21; 2 Timotheo 2:14; Warumi 14:22; Wagalatia 1:20, NW) Katika pindi moja wakati Waisraeli walipokuwa katika jangwa, Musa alimwambia Haruni hivi: “Sema kwa kusanyiko zima la wana wa Israeli, ‘Njooni karibu mbele za Yehova, kwa sababu yeye amesikia manung’uniko yenu.’” (Kutoka 16:9, NW) Waisraeli hao hawakulazimika kusafirishwa mpaka mbinguni ili wakasimame mbele za Yehova katika pindi hiyo. (Linga Walawi 24:8.) Badala ya hivyo, uko huko jangwani walisimama katika mtazamo wa Yehova, na uangalifu wake ukawa juu yao.
13 Kwa kuongezea, sisi tunasoma hivi: “Wakati Mwana wa binadamu anapowasili katika utukufu wake . . . mataifa yote yatakusanywa mbele ya yeye.”c Jamii ya kibinadamu kwa ujumla haitakuwamo katika mbingu wakati unabii huu unapotimizwa. Bila shaka, wale ambao ‘huondoka kwenda kuingia katika kukatiliwa mbali milele’ hawatakuwamo katika mbingu. (Mathayo 25:31-33, 41, 46, NW) Badala ya hivyo, aina ya binadamu husimama duniani katika mtazamo wa Yesu, naye hugeuza uangalifu wake awahukumu. Hali kadhalika, umati mkubwa uko “mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo” katika maana ya kwamba huo husimama katika mtazamo wa Yehova na Mfalme wake, Kristo Yesu, ambao kutoka kwao unapokea hukumu yenye kupendeleka.
14. (a) Ni nani wanaosimuliwa kuwa wako “kuzunguka kiti cha ufalme” na “juu ya Mlima Sayuni” wa kimbingu? (b) Ingawa umati mkubwa unatumikia Mungu “katika hekalu lake,” ni kwa sababu gani hilo haliwafanyi kuwa jamii ya kikuhani?
14 Wazee 24 na kikundi cha wapakwa-mafuta 144,000 wanasimuliwa kuwa wako ‘kuzunguka kiti cha ufalme cha Yehova pande zote’ na “juu ya Mlima Sayuni” wa kimbingu. (Ufunuo 4:4; 14:1, NW) Umati mkubwa si jamii ya kikuhani nao haufikii cheo hicho kilichokwezwa. Kweli, baadaye unasimuliwa katika Ufunuo 7:15 kuwa unatumikia Mungu “katika hekalu lake.” Lakini hekalu hili halirejezei patakatifu pa ndani zaidi, pale Patakatifu Zaidi Sana. Badala ya hivyo, ni ua wa kidunia wa hekalu la Mungu la kiroho. Neno la Kigiriki na·osʹ, linalotafsiriwa hapa “hekalu,” mara nyingi huwasilisha maana pana ya jengo zima lote lililojengwa kwa ajili ya ibada ya Yehova. Leo, hili ni jengo la kiroho ambalo hutia ndani mbingu na dunia pia.—Linga Mathayo 26:61; 27:5, 39, 40; Marko 15:29, 30; Yohana 2:19-21, New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
Vigelegele vya Sifa vya Ulimwengu Wote Mzima
15, 16. (a) Kunakuwa na tendo-itikio gani katika mbingu kwa kuonekana kwa umati mkubwa? (b) Uumbaji wa roho wa Yehova unatendaje kwa kuitikia kila ufunuo mpya wa kusudi lake? (c) Sisi tuliopo duniani tunaweza kujiungaje kuimba wimbo wa sifa?
15 Umati mkubwa unamsifu Yehova, lakini wengine pia wanaimba sifa zake. Yohana anaripoti: “Na malaika wote walikuwa wakisimama kuzunguka kiti cha ufalme na wazee na viumbe hai wanne, na wao walianguka nyuso zao chini mbele ya kiti cha ufalme na wakaabudu Mungu, kusema: ‘Ameni! Baraka na utukufu na hekima na utoaji-shukrani na heshima na nguvu na imara ziwe kwa Mungu wetu milele na milele. Ameni.’”—Ufunuo 7:11, 12, NW.
16 Wakati Yehova alipoumba dunia, malaika zake wote watakatifu ‘walipiga kilio kikuu kwa shangwe pamoja, na wana wote wa Mungu wakaanza kupaaza sauti kwa vifijo.’ (Ayubu 38:7, NW) Kila ufunuo mpya wa kusudi la Yehova lazima uwe ulitokeza mipaazo ya sifa ya kimalaika jinsi iyo hiyo. Wakati wazee 24—144,000 katika utukufu wao wa kimbingu—wanapolia kwa sauti kubwa katika kumtambua Mwana-Kondoo, wengine wote wa viumbe wa kimbingu huitikia kwa kusifu Yesu na Yehova Mungu. (Ufunuo 5:9-14) Tayari, viumbe hawa wamekuwa na shangwe mno kuona utimizo wa kusudi la Yehova katika kufufua kwake wanadamu wapakwa-mafuta waaminifu kwenye mahali penye utukufu katika milki ya kiroho. Sasa, viumbe wote waaminifu wa Yehova wa kimbingu wanabubujika kwa sifa za kimelodia wakati umati mkubwa unapoonekana. Kwa kweli, kwa watumishi wote wa Yehova, siku ya Bwana ni wakati wenye kusisimua kuishi humo. (Ufunuo 1:10) Hapa duniani, sisi ni wenye pendeleo kama nini kushiriki kuimba wimbo wa sifa kwa kuutolea Ufalme wa Yehova ushuhuda!
Umati Mkubwa Wajionyesha
17. (a) Ni swali gani linalozushwa na mmoja wa wazee 24, na uhakika wa kwamba mzee angeweza kupata mahali pa jibu unadokeza nini? (b) Swali la mzee lilijibiwa lini?
17 Tangu wakati wa mtume Yohana na kundelea mpaka ndani ya siku ya Bwana, Wakristo wapakwa-mafuta walitatizika wakitaka kujua utambulisho wa umati mkubwa. Basi, inafaa kwamba, mmoja wa wazee 24, akiwakilisha wapakwa-mafuta ambao tayari wako katika mbingu, achochee kufikiri kwa Yohana kwa kuzusha swali hususa: “Na katika kuitikia mmoja wa wazee akasema kwangu mimi: ‘Hawa ambao wamevalia majoho meupe, wao ni akina nani na wao walitoka wapi?’ Kwa hiyo mara hiyo mimi nikasema kwa yeye: ‘Bwana yangu, wewe ndiwe mmoja ambaye anajua.’” (Ufunuo 7:13, 14a, NW) Ndiyo, huyo mzee angeweza kupata mahali pa jibu na kumpa Yohana. Hiyo inadokeza kwamba waliofufuliwa wa kikundi cha wazee 24 huenda wakawa wanahusika katika kuwasilisha kweli za kimungu leo. Kwa upande wao, wale wa jamii ya Yohana waliomo duniani walipata kujua utambulisho wa umati mkubwa kwa kutazama kwa ukaribu sana alichokuwa akifanya Yehova katikati yao. Wao walikuwa wenye uharaka wa kuthamini mmeto wenye kutia kiwi wa nuru ya kimungu ambao ulipamba anga la kitheokrasi katika 1935, wakati barabara wa Yehova.
18, 19. (a) Ni tumaini gani lililokaziwa na jamii ya Yohana wakati wa miaka ya 1920 na 1930, lakini ni nani walioitikia ujumbe kwa hesabu yenye kuongezeka? (b) Ule utambulisho wa umati mkubwa katika 1935 ulionyesha nini kwa habari ya 144,000? (c) Takwimu za Ukumbusho zinafunua nini?
18 Wakati wa miaka ya 1920 na 1930, jamii ya Yohana ilikuwa imekazia tumaini la kimbingu, katika vichapo na katika kazi ya kuhubiri pia. Kwa wazi hesabu kamili ya 144,000 ilikuwa bado kutimia. Lakini hesabu iliyokuwa ikiongezeka ya wale waliotii ujumbe na wakaonyesha bidii katika kazi ya kutoa ushuhuda wakaja kudhihirisha kuwa wanapendezwa na kuishi milele katika dunia Paradiso. Wao hawakuwa na tamaa ya kwenda mbinguni. Huo haukuwa mwito wao. Wao hawakuwa sehemu ya kundi dogo bali ya kondoo wengine. (Luka 12:32; Yohana 10:16) Kutambulishwa kwao katika 1935 kuwa umati mkubwa wa wale kondoo wengine kilikuwa kionyeshi cha kwamba wakati huo kuchaguliwa kwa 144,000 kulikuwa karibu kumekamilika.
19 Je! takwimu zinaunga mkono mkataa huu? Ndiyo. Katika 1938, ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova 59,047 walishiriki katika huduma. Kati ya hao 36,732 walishiriki mifano kwenye mwadhimisho wa kila mwaka wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu, hivyo wakionyesha kwamba walikuwa na mwito wa kimbingu. Katika miaka iliyofuata tangu hapo, hesabu ya washiriki hao imeendelea kupungua, hasa kwa sababu Mashahidi waaminifu wa Yehova walimaliza mwendo wa maisha yao ya kidunia katika kifo. Katika 2005 ni 8,524 pekee walioshiriki mifano ya Ukumbusho—asilimia 0.05 tu ya wale 16,390,116 waliohudhuria mwadhimisho huo wa pote katika tufe.
20. (a) Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, ni elezo gani alilotoa faraghani J. F. Rutherford kwa habari ya umati mkubwa? (b) Ni uhakika gani sasa unaoonyesha kwamba umati mkubwa ni mkubwa kweli kweli?
20 Wakati vita ya pili ya ulimwengu ilipofyatuka, Shetani alitia jitihada kali azuie kuvunwa kwa umati mkubwa. Kazi ya Yehova ilizuiwa katika nchi nyingi. Siku hizo zilizokuwa ngumu, na muda mfupi kabla ya kifo chake katika Januari 1942, J. F. Rutherford alisikiwa akisema: “Basi . . . inaonekana kama umati mkubwa hautakuwa mkubwa sana hata hivyo.” Lakini baraka za kimungu zilielekeza vingine! Kufikia 1946 hesabu ya Mashahidi waliokuwa wakitumikia ulimwenguni pote ilikuwa imeruka kufikia 176,456—walio wengi wa hao wakiwa wa umati mkubwa. Katika 2005 walikuwako Mashahidi 6,390,022 waliokuwa wakitumikia Yehova kiaminifu katika mabara mbalimbali 235—UMATI MKUBWA kweli kweli! Na hesabu inazidi kuongezeka.
21. (a) Kuvunwa kwa watu wa Mungu wakati wa siku ya Bwana kumekuwaje katika upatani kamili na njozi ya Yohana? (b) Unabii fulani wa maana ulianza kutimizwaje?
21 Hivyo kuvunwa kwa watu wa Mungu wakati wa siku ya Bwana kumekuwa katika upatani kamili na njozi ya Yohana: kwanza kazi ya kukusanya mabaki ya 144,000; kisha kukusanywa kwa umati mkubwa. Kama Isaya alivyotoa unabii, sasa “katika sehemu ya mwisho kabisa ya siku,” watu wa mataifa yote wanamiminika kushiriki ibada safi ya Yehova. Na, kweli kweli, sisi tunachachawa katika uthamini wa uumbaji wa Yehova wa “mbingu mpya na dunia mpya.” (Isaya 2:2-4; 65:17, 18, NW) Mungu anakusanya “tena vitu vyote pamoja katika Kristo, vitu katika mbingu na vitu juu ya dunia.” (Waefeso 1:10, NW) Warithi wapakwa-mafuta wa Ufalme wa kimbingu—waliochaguliwa katika muda wa karne zilizopita tangu siku ya Yesu—ndio “vitu katika mbingu.” Na sasa, umati mkubwa wa kondoo wengine wanatokea wakiwa wa kwanza wa “vitu juu ya dunia.” Kutumikia kwako kupatana na mpango huo kunaweza kumaanisha furaha ya milele kwa ajili ya wewe.
Baraka za Umati Mkubwa
22. Ni habari gani zaidi anayopokea Yohana kuhusu umati mkubwa?
22 Kupitia mfereji wa kimungu Yohana anapokea habari zaidi kuhusu huu umati mkubwa: “Na yeye [mzee] akasema kwangu mimi: ‘Hawa ndio wale ambao huja kutoka dhiki kubwa, na wamefua majoho yao na wameyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Hiyo ndiyo sababu wao wako mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu; na wao wanatolea yeye utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake; na Mmoja anayeketi juu ya kiti cha ufalme atatanda hema yake juu yao.’”—Ufunuo 7:14b, 15, NW.
23. Ni nini iliyo dhiki kubwa ambayo umati mkubwa “huja kutoka” hiyo?
23 Katika pindi ya mapema zaidi, Yesu alikuwa amesema kwamba kuwapo kwake katika utukufu wa Ufalme kungefikia upeo katika “dhiki kubwa kama ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21, 22, NW) Katika utimizo wa unabii huo, wale malaika wataachilia pepo nne za dunia zikumbe mfumo wa ulimwengu wa Shetani. Cha kwanza kwenda kitakuwa ni Babuloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini bandia. Kisha, kwenye upeo wa dhiki hiyo, Yesu ataokoa mabaki duniani ya 144,000, pamoja na umati mkubwa wenye watu wengi sana.—Ufunuo 7:1; 18:2.
24. Watu mmoja mmoja wa umati mkubwa wanastahilije kwa ajili ya kuokoka?
24 Watu mmoja mmoja wa umati mkubwa wanastahilije kwa ajili ya kuokoka? Yule mzee anamwambia Yohana kwamba “wamefua majoho yao na wameyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Kwa maneno mengine, wao wamezoea imani katika Yesu akiwa Mkombozi wao, wamejiweka wakfu kwa Yehova, nao wameonyesha wakfu wao kwa ubatizo wa maji, na ‘wanashika dhamiri njema’ kwa mwenendo wao mnyoofu. (1 Petro 3:16, 21; Mathayo 20:28, NW) Hivyo, wao ni safi na waadilifu katika macho ya Yehova. Na wanajiweka wenyewe “bila doa kutoka ulimwengu.”—Yakobo 1:27, NW.
25. (a) Umati mkubwa unamtoleaje Yehova “utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake”? (b) Yehova ‘anatandaje hema lake’ juu ya umati mkubwa?
25 Na zaidi, wao wamekuwa Mashahidi wenye bidii wa Yehova—“wanatolea yeye utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” Je! wewe ni mmoja wa huu umati mkubwa ulio wakfu? Ikiwa ndivyo, ni pendeleo lako kutumikia Yehova bila kuacha katika ua wake wa kidunia wa hekalu lake kubwa la kiroho. Leo, chini ya mwelekezo wa wapakwa-mafuta, umati mkubwa unafanya sehemu iliyo kubwa zaidi ya kazi ya kutoa ushuhuda. Wajapokuwa na madaraka ya kimwili, mamia ya maelfu wanautafutia nafasi ule utumishi wa wakati wote wakiwa mapainia. Lakini uwe wewe ni wa kikundi hicho au la, ukiwa mshiriki aliye wakfu wa umati mkubwa, wewe unaweza kushangilia ukiwa rafiki ya Mungu na mgeni anayekaribishwa katika hema yake. (Zaburi 15:1-5; Yakobo 2:21-26) Hivyo Yehova ‘anatanda hema yake’ juu ya wale ambao wanampenda yeye na, akiwa mkaribishaji-wageni mwema, anawapa himaya.—Mithali 18:10.
26. Ni baraka gani nyingine utakazofurahia umati mkubwa?
26 Yule mzee anaendelea: “Wao hawataona njaa tena wala kuona kiu tena, wala jua halitapiga juu yao tena wala joto lolote lenye kuunguza, kwa sababu Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kiti cha ufalme, atachunga wao, na ataelekeza wao kwenye vibubujiko vya maji ya uhai. Na Mungu atapangusa kabisa kila chozi kutoka macho yao.” (Ufunuo 7:16, 17, NW) Ndiyo, Yehova ni mkaribishaji-wageni kikweli! Lakini kuna maana gani yenye kina kirefu katika maneno haya?
27. (a) Isaya alitoaje unabii wa jambo linalofanana na maneno ya mzee? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba unabii wa Isaya ulianza kutimizwa juu ya kundi la Kikristo katika siku ya Paulo?
27 Acheni sisi tufikirie unabii ulio na maneno yanayofanana na hayo: “Hivi ndivyo Yehova amesema: ‘Katika wakati wa nia njema mimi nilijibu wewe, na katika siku ya wokovu mimi nimekusaidia wewe . . . Wao hawataenda njaa, wala hawataenda kiu, wala joto lenye kukausha au jua halitapiga wao. Kwa kuwa Mmoja ambaye ana sikitikio juu yao ataendesha wao, na kando ya chemchemi za maji yeye ataongoza wao.’” (Isaya 49:8, 10, NW; ona pia Zaburi 121:5, 6.) Mtume Paulo alinukuu sehemu ya unabii huu na akautumia kuhusu “siku ya wokovu” iliyoanza Pentekoste 33 W.K. Yeye aliandika: “Kwa maana yeye [Yehova] asema: ‘Katika wakati uliokubalika mimi nilisikia wewe, na katika siku ya wokovu mimi nilisaidia wewe.’ Tazama! Sasa ndio hasa wakati uliokubalika. Tazama! Sasa ndiyo siku ya wokovu.”—2 Wakorintho 6:2, NW.
28, 29. (a) Maneno ya Isaya yalitimizwaje katika karne ya kwanza? (b) Maneno ya Ufunuo 7:16 yanatimizwaje kwa habari ya umati mkubwa? (c) Ni nini litakalokuwa tokeo la kuelekezwa kwa umati mkubwa kwenye “vibubujiko vya maji ya uhai”? (d) Ni kwa nini umati mkubwa utakuwa usio na kifani miongoni mwa aina ya binadamu?
28 Ile ahadi ya kutoona njaa au kiu au kutaabishwa na joto lenye kukausha ilitumikaje wakati huo huko nyuma? Hakika, Wakristo katika karne ya kwanza walitaabishwa na njaa na kiu halisi nyakati nyingine. (2 Wakorintho 11:23-27) Ingawa hivyo, katika maana ya kiroho, wao walikuwa na chakula tele. Wao waliandaliwa kwa wingi hivi kwamba wao hawakwenda njaa au kiu kwa vitu vya kiroho. Zaidi ya hilo, Yehova hakuruhusu joto la kasirani yake liwake dhidi yao wakati yeye alipoharibu mfumo wa mambo wa Kiyahudi katika 70 W.K. Maneno ya Ufunuo 7:16 yana utimizo wa kiroho unaofanana na huo kwa ajili ya umati mkubwa leo. Pamoja na Wakristo wapakwa-mafuta, wao wanafurahia wingi wa maandalizi ya kiroho.—Isaya 65:13; Nahumu 1:6, 7.
29 Ikiwa wewe ni mmoja wa ule umati mkubwa, hali yako njema ya moyo itakufanya wewe “upige kilio kikuu kwa shangwe,” si kitu ulazimike kuvumilia nini kwa habari ya manyimo na mikazo wakati wa miaka hii ya gizagiza ya mfumo wa Shetani. (Isaya 65:14, NW) Katika maana hiyo, hata sasa, Yehova anaweza ‘kupangusa kabisa kila chozi kutoka macho yako.’ “Jua” lenye joto jingi la Mungu au hukumu mbaya halikutishi wewe tena, na pepo nne za uharibifu ziachiliwapo, huenda wewe ukakingwa na “joto lenye kuunguza” la kutopendezwa kwa Yehova. Baada ya uharibifu huo kwisha, yule Mwana-Kondoo atakuelekeza wewe unufaishwe kikamili na “vibubujiko vya maji ya uhai” vyenye kutia uhai mpya, hivyo vikiwa vinawakilisha maandalizi yote ambayo Yehova anakufanyia wewe upate uhai wa milele. Imani yako katika damu ya Mwana-Kondoo itatetewa katika maana ya kwamba wewe utainuliwa polepole ufikie ukamilifu wa kibinadamu. Nyinyi wa umati mkubwa mtakuwa bila kifani miongoni mwa aina ya binadamu mkiwa yale “mamilioni” ambayo hayakulazimika hata kufa! Katika maana iliyo kamili zaidi, kila chozi litakuwa limekwisha panguswa kabisa kutoka macho yenu.—Ufunuo 21:4.
Kufanya Ule Mwito Uwe Hakika
30. Ni mandhari gani nzuri mno inayofunguka kwetu katika njozi ya Yohana, na ni nani ambaye ataweza “kusimama”?
30 Lo! maneno haya yanatufungulia mandhari nzuri mno kama nini! Yehova mwenyewe yu katika kiti cha ufalme chake, na watumishi wake wote, wa kimbingu na wa kidunia, wanaungana katika kumsifu yeye. Watumishi wake wa kidunia wanathamini ni pendeleo lenye kutia hofu kama nini walilo nalo kushiriki katika hii korasi ya sifa inayoongezeka. Karibuni sana, Yehova na Kristo Yesu watatekeleza hukumu, nacho kilio hiki kitasikika: “Siku kubwa ya hasira-kisasi yao imekuja, na ni nani anaweza kusimama?” (Ufunuo 6:17, NW) Na jibu? Ni sehemu ndogo tu ya aina ya binadamu, kutia na wowote kati ya 144,000 waliotiwa muhuri ambao huenda wangali wanabaki katika mnofu na umati mkubwa wa kondoo wengine ndio ‘watasimama,’ yaani, wataokoka pamoja nao.—Yeremia 35:19; 1 Wakorintho 16:13.
31. Utimizo wa njozi ya Yohana wapasa uathirije Wakristo, wa wapakwa-mafuta na wa ule umati mkubwa pia?
31 Kwa sababu ya uhakika huu, Wakristo wapakwa-mafuta wa jamii ya Yohana hujipinda wenyewe kisulubu katika ‘kufuatilia kuteremka kuelekea mradi kwa ajili ya tuzo la mwito wa kuelekea juu wa Mungu kwa njia ya Kristo Yesu.’ (Wafilipi 3:14, NW) Wao wanafahamu kabisa kwamba matukio wakati wa siku hizi hutaka uvumilivu wa pekee upande wao. (Ufunuo 13:10) Baada ya kutumikia Yehova kishikamanifu kwa miaka mingi, wao wanashikilia sana imani, wakishangilia kwamba majina yao “yamechorwa katika mbingu.” (Luka 10:20; Ufunuo 3:5, NW) Wale wa umati mkubwa vilevile wanajua kwamba ni “yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye ambaye ataokolewa.” (Mathayo 24:13, NW) Ingawa umati mkubwa ukiwa kikundi umetiwa alama utoke katika dhiki kubwa, watu mmoja mmoja wa huo lazima wajipinde wenyewe wabaki wakiwa safi na wenye kutenda.
32. Ni hali gani yenye umuhimu inayokaziwa na uhakika wa kwamba ni vikundi viwili tu ndivyo vitaweza “kusimama” katika siku ya hasira-kisasi ya Yehova?
32 Hakuna ithibati kwamba yeyote kando na hivi vikundi viwili ‘atasimama’ katika siku ya hasira-kisasi ya Yehova. Hii humaanisha nini kwa yale mamilioni ambayo kila mwaka huonyesha staha fulani kwa dhabihu ya Yesu kwa kuhudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho wa kifo chake lakini ambao bado hawajajizoeza imani katika dhabihu ya Yesu kufikia hatua ya kuwa watumishi wa Yehova walio wakfu na waliobatizwa, wenye kutenda katika utumishi wake? Na zaidi, namna gani wale ambao hapo zamani walikuwa watendaji lakini ambao wameruhusu mioyo yao ‘ilemewe na mahangaikio ya maisha?’ Wote hao na waamke, na wakae wakiwa macho, ili ‘wafaulu katika kuponyoka mambo hayo yote ambayo yamekusudiwa yatukie na katika kusimama mbele ya Mwana wa binadamu’—Yesu Kristo. Wakati ni mfupi!—Luka 21:34-36, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Ona New World Translation Reference Bible, kielezi cha chini.
b The Watch Tower, Aprili 1, 1918, ukurasa 98.
c Kihalisi, “katika mbele ya yeye,” The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures.
[Picha katika ukurasa wa 119]
Fasiri ni za Mungu
Kwa miongo mingi jamii ya Yohana iliulizia-ulizia utambulisho wa umati mkubwa lakini bila kupata elezo lenye kuridhisha. Kwa nini? Sisi tunapata jibu katika maneno ya Yusufu mwaminifu, wakati yeye aliposema: “Je! fasiri si za Mungu?” (Mwanzo 40:8, NW) Ni lini na jinsi gani Mungu anapofasiri utimizo wa unabii wake? Kwa kawaida, ni wakati unapokaribia kutimizwa au wakati unapoendelea kutimizwa ili ujumbe wao uweze kufahamiwa na watumishi wake wenye kutafuta-tafuta. Uelewevu huu unatolewa “kwa ajili ya agizo letu, ili kwamba kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutoka Maandiko sisi tupate kuwa na tumaini.”—Waroma 15:4, NW.
[Picha katika ukurasa wa 124]
Washiriki wa umati mkubwa
▪ huja kutoka mataifa na makabila na vikundi vya watu na ndimi zote
▪ husimama mbele ya kiti cha ufalme cha Yehova
▪ wamefua majoho yao yakawa meupe katika damu ya Mwana-Kondoo
▪ husema wokovu hutoka kwa Yehova na Yesu
▪ huja kutoka ile dhiki kubwa
▪ hutumikia Yehova katika hekalu lake mchana na usiku
▪ hupokea himaya yenye upendo na uangalizi wa Yehova
▪ huchungwa na Yesu kwenye vibubujiko vya maji ya uhai
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 121]
[Picha katika ukurasa wa 127]
Umati mkubwa hutegemea wokovu wao kutoka kwa Mungu na Mwana-Kondoo
[Picha katika ukurasa wa 128]
Yule Mwana-Kondoo ataelekeza umati mkubwa kwenye vibubujiko vya maji ya uhai
-
-
Tauni za Yehova juu ya Jumuiya ya WakristoUfunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
-
-
Sura ya 21
Tauni za Yehova juu ya Jumuiya ya Wakristo
Njozi ya 5—Ufunuo 8:1–9:21
Habari: Kuvumishwa kwa sita kati ya zile tarumbeta saba
Wakati wa utimizo: Kutoka kuketishwa kwa Kristo Yesu katika kiti cha ufalme katika 1914 hadi dhiki kubwa
1. Kunakuwa nini wakati Mwana-Kondoo anapofungua kifungo cha saba?
“PEPO nne” zimezuiwa mpaka 144,000 wa Israeli wa kiroho wawe wametiwa muhuri na ule “umati mkubwa” uwe umekubaliwa kwa ajili ya kuokoka. (Ufunuo 7:1, 9, NW) Hata hivyo, kabla hiyo dhoruba yenye tufani haijafyatukia dunia, hukumu mbaya za Yehova dhidi ya ulimwengu wa Shetani lazima pia zijulishwe! Mwana-Kondoo aendeleapo kufungua kifungo cha saba na cha mwisho kabisa, lazima Yohana awe anatazama kwa makini aone ni kitu gani kitakunjulika. Sasa yeye anashiriki pamoja na sisi ono lake: “Na wakati yeye [Mwana-Kondoo] alipofungua kifungo cha saba, kukawa kimya katika mbingu kwa muda wapata nusu saa. Na mimi nikaona malaika saba ambao husimama mbele za Mungu, na tarumbeta saba wakapewa wao.”—Ufunuo 8:1, 2, NW.
Wakati wa Sala ya Bidii
2. Kunatukia nini wakati wa nusu saa ya kimya katika mbingu?
2 Hiki ni kimya chenye kutokeza sana! Nusu saa yaweza kuonekana kuwa wakati mrefu unapongojea jambo fulani liwe. Sasa, hata korasi daima ya kimbingu yenye sifa haisikiki tena. (Ufunuo 4:8) Kwa nini? Yohana anaona sababu katika njozi: “Na malaika mwingine akawasili na akasimama kwenye madhabahu, akiwa na chombo cha dhahabu cha uvumba; na kiasi kikubwa cha uvumba akapewa yeye akitoe pamoja na sala za watakatifu wote juu ya madhabahu ya dhahabu ambayo ilikuwa mbele ya kiti cha ufalme. Na moshi wa uvumba ukapaa kutoka mkono wa malaika pamoja na sala za watakatifu mbele za Mungu.”—Ufunuo 8:3, 4, NW.
3. (a) Kuchomwa kwa uvumba hutukumbusha juu ya nini? (b) Ni nini kusudi la nusu saa ya kimya katika mbingu?
3 Hii inatukumbusha kwamba chini ya mfumo wa mambo wa Kiyahudi, uvumba ulichomwa kila siku kwenye tabenakulo na, katika miaka ya baadaye, kwenye hekalu katika Yerusalemu. (Kutoka 30:1-8) Wakati wa kuchoma uvumba hivyo, Waisraeli wasio wa kikuhani walingojea nje ya eneo takatifu, wakisali—pasipo shaka kwa kimya katika mioyo yao—kwa Mmoja ambaye kwake moshi wa uvumba ulikuwa ukipaa. (Luka 1:10) Yohana sasa anaona kitu fulani kama hicho kikitukia katika mbingu. Uvumba unaotolewa na malaika unashirikishwa na “sala za watakatifu.” Kwa kweli, katika njozi ya mapema zaidi, uvumba unasemwa kuwa ukiwakilisha sala hizo. (Ufunuo 5:8; Zaburi 141:1, 2) Kwa wazi, basi, kimya cha ufananisho katika mbingu ni kuruhusu “sala za wale watakatifu” walio duniani zisikike.
4, 5. Ni matukio gani ya kihistoria yanayotusaidia kujua kipindi cha wakati kinacholingana na nusu saa ya ufananisho yenye kimya?
4 Je! sisi tunaweza kujua wakati hili linapokuwa? Ndiyo, tunaweza, kwa kuchunguza muktadha pamoja na matukio ya kihistoria ya mapema katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10, NW) Wakati wa 1918 na 1919, matukio duniani yalipatana katika njia yenye kutokeza sana na mandhari-mfululizo inayoelezwa kwenye Ufunuo 8:1-4. Kwa miaka 40 kabla ya 1914, Wanafunzi wa Biblia—kama walivyokuwa wakiitwa Mashahidi wa Yehova wakati huo—walikuwa wakitangaza kwa ujasiri kwamba “majira ya Mataifa” yangekwisha wakati huo. Yale matukio yenye kujaa taabu ya 1914 yaliwathibitisha kuwa sahihi. (Luka 21:24; Mathayo 24:3, 7, 8) Lakini wengi wao waliitikadi pia kwamba katika 1914 wao wangechukuliwa kutoka dunia hii wapelekwe kwenye urithi wao wa kimbingu. Hilo halikuwa hivyo. Badala ya hivyo, wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, walivumilia wakati wa mnyanyaso mkali. Katika Oktoba 31, 1916, Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, akafa. Kisha, katika Julai 4, 1918, msimamizi mpya, Joseph F. Rutherford, na wawakilishi wengine saba wa Sosaiti wakasafirishwa kupelekwa kwenye gereza katika Atlanta, Georgia, wakihukumiwa kimakosa miaka mirefu katika jela.
5 Wakristo wenye mioyo myeupe wa jamii ya Yohana walitatizika. Mungu alitaka wao wafanye nini kufuata hapo? Ni lini wangechukuliwa juu mbinguni? Makala moja iliyokuwa na kichwa “Mavuno Yamekwisha—Ni Nini Kitafuata?” Ilitokea katika toleo la Mei 1, 1919, la Mnara wa Mlinzi. Hiyo ilionyesha hali hii ya kutokuwa na hakika na ikatia moyo waaminifu waendelee kuvumilia, ikiongeza: “Sisi tunaitikadi ni usemi wa kweli sasa kwamba mavuno ya jamii ya ufalme ni uhakika uliokamilishwa, kwamba wote hao wamekwisha tiwa muhuri na kwamba mlango umefungwa.” Katika pindi hii ngumu, sala za bidii za jamii ya Yohana zilikuwa zikipaa, kana kwamba katika moshi wa kiasi kikubwa cha uvumba. Na sala zao zilikuwa zikisikiwa!
Kuvurumisha Moto Kwenye Dunia
6. Kunakuwa na nini baada ya hicho kimya katika mbingu, na ni katika kuitikia nini?
6 Yohana anatuambia: “Lakini mara hiyo malaika akachukua chombo cha uvumba, na kukijaza baadhi ya moto wa madhabahu na kuuvurumisha kwenye dunia. Na ngurumo zikatukia na sauti na meme na tetemeko la dunia.” (Ufunuo 8:5, NW) Baada ya kimya, kuna utendaji wa ghafula wenye kutazamisha! Kwa wazi huo ni katika kuitikia “sala za watakatifu,” kwa kuwa huo unaanzishwa na moto uliochukuliwa kutoka madhabahu ya uvumba. Huko nyuma katika 1513 K.W.K. kwenye Mlima Sinai, ngurumo na meme, kelele kubwa, moto, na kutetemeka kwa mlima viliashiria kugeuzwa kwa uangalifu wa Yehova kuelekea watu wake. (Kutoka 19:16-20) Madhihirisho kama hayo yanayoripotiwa na Yohana hali kadhalika huonyesha uangalifu wa Yehova ukitolewa kwa watumishi wake duniani. Lakini anachoona Yohana kinatolewa kwa ishara. (Ufunuo 1:1, NW) Kwa hiyo moto, ngurumo, sauti, meme, na tetemeko la dunia vya ufananisho vitafasiriwaje leo?
7. (a) Ni moto gani wa ufananisho ambao Yesu aliwasha duniani wakati wa huduma yake? (b) Ndugu za kiroho za Yesu waliwashaje moto katika Jumuiya ya Wakristo?
7 Pindi moja, Yesu aliambia wanafunzi wake: “Mimi nilikuja kuanzisha moto juu ya dunia.” (Luka 12:49, NW) Kwa kweli, yeye aliwasha moto. Kwa kuhubiri kwake kwa bidii, Yesu alifanya Ufalme wa Mungu uwe ndio suala kubwa mbele ya watu wa Kiyahudi, na huo ulitokeza ubishani mkubwa kotekote katika taifa hilo. (Mathayo 4:17, 25; 10:5-7, 17, 18) Katika 1919 ndugu za kiroho za Yesu waliokuwako duniani, kile kikosi kidogo cha Wakristo wapakwa-mafuta ambao walikuwa wameokoka siku zenye kujaribu za Vita ya Ulimwengu 1, waliwasha moto kama huo katika Jumuiya ya Wakristo. Katika Septemba wa mwaka huo, roho ya Yehova ilionekana wazi kwa njia yenye kutokeza sana wakati Mashahidi wake washikamanifu walipokusanyika katika Sida Pointi, Ohaiyo, U.S.A. kutoka karibu na mbali. Joseph F. Rutherford, aliyekuwa ameachiliwa hivi majuzi kutoka jela na ambaye karibuni angeondolewa kabisa mashtaka yote, alihutubia mkusanyiko huo kwa ujasiri, akisema: “Kwa kutii amri ya Bwana-Mkubwa wetu, na tukitambua pendeleo na wajibu wetu wa kufanya vita dhidi ya ngome za kosa ambazo zimeshika watu katika utumwa kwa muda mrefu sana, shughuli yetu ilikuwa na ni kutangaza ufalme mtukufu unaokuja wa Mesiya.” Hilo ndilo suala kuu—Ufalme wa Mungu!
8, 9. (a) J. F. Rutherford alielezaje habari ya mwelekeo na tamaa ya watu wa Mungu wakati wa miaka migumu ya vita? (b) Ilikuwaje kwamba moto ulivurumishwa kwenye dunia? (c) Ngurumo, sauti, meme, na tetemeko la dunia vimetukiaje?
8 Akirejezea magumu ya karibuni ya watu wa Mungu, mhutubu huyo alisema: “Shambulio la adui lilikuwa lisilo na sikitikio sana hivi kwamba wengi wa kundi lenye kupendwa la Bwana waliduwaa wakasimama tuli kwa mshangao, wakisali na kungojea Bwana aonyeshe penzi lake. . . . Lakini ijapokuwa kivunja-moyo cha kitambo, kulikuwako tamaa yenye kuwaka ya kutangaza ujumbe wa ufalme.”—Ona toleo la Septemba 15, 1919 la The Watch Tower ukurasa 280.
9 Katika 1919 tamaa hiyo ilitoshelezwa. Hiki kikundi kidogo lakini chenye kutenda cha Wakristo kiliwashwa moto, kusema kiroho, waanze kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote. (Linga 1 Wathesalonike 5:19.) Moto ulivurumishwa duniani katika njia ya kwamba Ufalme wa Mungu ukawa ndilo suala lenye kuwaka, na ndivyo unaendelea kuwa! Sauti zenye nguvu zilichukua mahali pa kimya, zikivumisha ujumbe wa Ufalme kwa uwazi. Maonyo ya dhoruba yenye kunguruma kutoka Biblia yalitoa sauti. Kama mimeto ya umeme, miale miangavu ya ukweli iliangaza kutoka Neno la Yehova la kiunabii, na tetemeko la dunia lenye nguvu likaanza kutikisa milki ya kidini mpaka misingi yayo. Jamii ya Yohana iliona kwamba kulikuwako kazi ya kufanywa. Na kufikia leo hii, kazi hiyo huendelea kupanuka kwa njia tukufu kotekote katika dunia inayokaliwa!—Warumi 10:18.
-