Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Historia ya Kisasa ya Serbia

      Nchi ya Serbia ambayo iko katikati ya eneo la Balkani, ina watu wa mataifa na tamaduni mbalimbali. Ofisi ya tawi ilianzishwa katika mji wa Belgrade, nchini Serbia, mwaka wa 1935 ili kushughulikia maeneo ya nchi iliyokuwa ikiitwa Yugoslavia, kukawa na ongezeko kubwa la kitheokrasi. Katika nyakati za karibuni, ndugu katika nchi ya Serbia wamesaidia jinsi gani nchi mpya zilizoundwa katika eneo hilo?

      Mipaka ya nchi hizo ilipokuwa ikifungwa na chuki ya kidini na ya kijamii kuenea, ndugu wa mataifa mbalimbali walikuwa wakifanya kazi pamoja kwa amani katika ofisi ya tawi huko Zagreb, Kroatia. Mwishowe, ndugu zetu Waserbia walilazimika kuondoka kwa sababu chuki ya kijamii na ya kitaifa ilikuwa imepamba moto katika maeneo yaliyozunguka Betheli. Mwaka wa 1992, vichapo vya Kiserbia vilianza tena kutafsiriwa huko Belgrade, Serbia, kama ilivyokuwa miaka 50 hivi iliyopita. Hatua hiyo ilithibitika kuwa ya hekima na ya wakati unaofaa.

      Watu wengi sana walihitaji misaada huko Bosnia, ambako vita vikali vilikuwa vikiendelea. Kwa upendo, ofisi ya tawi ya Austria ilikuwa imepanga kupeleka misaada, na ndugu wa Serbia wangeweza kupeleka kwa urahisi misaada hiyo katika maeneo ya Bosnia yaliyotawaliwa na Waserbia.

      Ingawa vita havikufika Serbia, nchi hiyo ilipatwa na matokeo ya vita hivyo. Vikwazo vya kiuchumi vilifanya iwe vigumu kupata vichapo kutoka Ujerumani ambako vilichapishiwa. Makutaniko yalipokosa magazeti mapya, ndugu zetu walijifunza magazeti ya zamani mpaka magazeti mapya yalipofika. Hata hivyo, mwishowe ndugu zetu hawakukosa kamwe gazeti lolote.

      ‘MSAADA WENYE KUTIA NGUVU’

      Daniel Nizan, aliyehitimu Shule ya Gileadi alisema hivi: “Tulipofika Serbia mwaka wa 1991, nchi hiyo ilikuwa na msukosuko mkubwa wa kisiasa. Tulivutiwa na bidii ambayo ndugu walionyesha hata ingawa waliishi katika hali ngumu sana. Ninakumbuka jinsi tulivyoshangaa kuona watu wapya 50 wakisimama ili wabatizwe katika kusanyiko la kwanza la pekee ambalo mimi na mke wangu tulihudhuria. Hilo lilitutia moyo sana.”

      Ndugu na Dada Nizan walisaidia sana kupanga kazi katika ofisi mpya huko Belgrade. Ofisi ya kwanza, ambayo ilitoshea watu kumi, ilikuwa kwenye Barabara ya Milorada Mitrovića. Pia, Jumba la Ufalme lilikuwa sehemu ya chini ya jengo hilo. Nafasi zaidi zilihitajiwa kwa ajili ya watafsiri waliokuwa wakiongezeka. Mwishowe, uwanja ulipatikana na ujenzi ukaanza. Mwishoni mwa mwaka wa 1995, familia ya Betheli ilihamia makao mapya.

      Matatizo yaliyokuwa yakiongezeka yaliwachochea watu zaidi wakubali kweli, na kadiri hesabu ya wahubiri ilivyoongezeka ndivyo kulivyokuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa waangalizi wenye upendo. Mapainia wa pekee kutoka Italia walikuja kusaidia—watumishi wa wakati wote wenye bidii na wenye kujidhabihu ambao walijitolea kwa kupenda. Ingawa haikuwa rahisi kujifunza lugha mpya na kuzoea utamaduni mpya wakati wa vita, mapainia hao walikuwa ‘msaada wenye kuwatia nguvu’ ndugu zetu huko Serbia.—Kol. 4:11.

      Mapainia kutoka nchi nyingine walisaidia katika njia nyingi, lakini njia ya maana zaidi ni kwamba “walikuwa na uzoefu wa mambo ya kitengenezo,” akasema Rainer Scholz, mratibu wa Halmashauri ya Nchi huko Serbia. Leo, kuna makutaniko 55 nchini Serbia ambayo yanasaidiwa na mapainia wa pekee 70.

      HALI MBAYA SANA YA KUONGEZEKA KWA BEI KUPITA KIASI

      Serbia ilikumbwa na hali mbaya sana ya kiuchumi iliyosababishwa na vita, hasa kuongezeka kwa bei kupita kiasi. Gazeti moja linaripoti hivi: “Katika muda wa siku 116 kati ya Oktoba 1993 na Januari 24, 1994, bei za vitu ziliongezeka kwa asilimia trilioni 500.” Mira Blagojević, ambaye amefanya kazi Betheli tangu 1982, anakumbuka kwamba alihitaji kubeba gunia lililojaa pesa ili kwenda kununua mboga chache sokoni.

      Dada mwingine, Gordana Siriški, anasema kwamba mama yake alipoenda kuchukua malipo yake ya uzeeni ya mwezi mmoja, angeweza kununua karatasi moja tu ya chooni. Gordana alisema: “Ni vigumu sana kuelewa jinsi watu walivyoishi kwa kuwa kila kitu walichokuwa nacho kilipoteza thamani kwa ghafula. Ndugu zetu wa ulimwenguni pote walituletea misaada. Kadiri watu walivyokatishwa tamaa na benki na serikali, ndivyo wengi walivyoanza kumwamini Mungu, na akina ndugu walisitawisha uhusiano wa karibu zaidi.”

      KUTAFSIRI BIBLIA

      Kwa miaka mingi vikundi vya kutafsiri nchini Yugoslavia vilifanya kazi mahali pamoja huko Zagreb, Kroatia. Baada ya vita, kila kikundi cha kutafsiri kilihamia nchi yao lakini, bado waliendelea kuwasiliana na kikundi cha kutafsiri kilichokuwa Zagreb. Hatua hiyo ilisaidia sana hasa wakati kikundi cha Kiserbia kilipoanza kutafsiri Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Walikusudia itolewe kwenye kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova la 1999.

      Hata hivyo, watafsiri walipokuwa wakimalizia kazi ya kutafsiri Biblia, nchi ilikuwa ikijitayarisha kwa ajili ya vita. Kwa kuwa mabomu yangeangushwa, na mawasiliano ya simu kukatizwa, ingekuwa vigumu kwa watafsiri kutuma habari kutoka Belgrade mpaka kwenye kiwanda cha uchapishaji nchini Ujerumani. Mnamo Jumanne, Machi 23, huku mashambulizi ya hewani yakitarajiwa, akina ndugu walifanya kazi usiku wote na wakafaulu kutuma faili za elektroniki mpaka Ujerumani mapema asubuhi. Saa chache baadaye, mabomu yalianza kuangushwa na watafsiri wakakimbilia mahali salama, huku wakishangilia! Walishangilia hata zaidi wakati Biblia iliyochapishwa ilipotolewa miezi minne baadaye kwenye kusanyiko lililofanyiwa Belgrade. Akina ndugu waliendelea kutafsiri vichapo vingine ijapokuwa walikabili mashambulizi hayo na ukosefu wa umeme. Lakini mara nyingi iliwabidi waache kazi na kukimbilia mahali salama. Kwa kweli, ulikuwa wakati mgumu, lakini wote walifurahia kushiriki kutayarisha chakula cha kiroho kilichohitajiwa sana.

      Kupitia kazi nyingi ngumu na baraka za Yehova, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa katika Kiserbia mnamo Julai 1999. Wajumbe walithamini na kushangilia sana kwa sababu ya kupata tafsiri hiyo katika lugha yao wenyewe. Mwishowe, kwenye makusanyiko ya 2006, Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa katika maandishi ya Kisiriliki na Kilatini.

      UPINZANI WA KIDINI UNAONGEZEKA

      Kwa kuwa Kanisa Othodoksi la Kiserbia ndiyo dini kuu nchini, watu wengi wanafikiri Waserbia wote ni Waothodoksi. Wanahisi kwamba mtu ambaye si mfuasi wa Kanisa Othodoksi si Mserbia. Hata hivyo, ujumbe wetu wa tumaini kutoka katika Biblia ulikubaliwa na watu wengi katika miaka ya 1990. Vita vilipokuwa vikikaribia kwisha mwaka wa 1999, hesabu ya wahubiri ilikuwa imeongezeka karibu mara mbili, na kufikia kilele cha wahubiri 4,026.

      Kanisa Othodoksi liliwakasirikia watu wa Yehova kwa sababu ya ufanisi wao wa kiroho. Kwa kuwachochea watu wawe wazalendo, kanisa hilo lilijaribu kukomesha kazi yetu ya Kikristo ya kuhubiri. Wapinzani walijaribu kuwavunja moyo ndugu zetu kwa kuwatesa na kwa kutumia sheria vibaya. Kwa mfano, ndugu zetu 21 walifungwa gerezani kwa sababu ya kutounga mkono vita. Wengi wao waliachiliwa huru muda mfupi baada ya vita, na walifurahi kwamba Yehova alitia nguvu imani yao wakati huo mgumu.

      Kwa ghafula, mnamo Aprili 9, 2001, Wizara ya Mambo ya Ndani ilipiga marufuku kuleta vichapo vyetu nchini. Kwa nini? Walidai kwamba vichapo vyetu vingewapotosha vijana wa nchi hiyo. Orodha ya vichapo vilivyopigwa marufuku ilitia ndani Biblia!

      Televisheni na magazeti yalieneza ripoti za uwongo kuhusu kazi yetu, na nyakati nyingine ripoti hizo ziliwafanya wenye nyumba fulani watutendee kwa jeuri. Painia mmoja wa pekee alisema hivi: “Walitupiga ngumi au makofi tulipohubiri nyumba kwa nyumba, na nyakati nyingine waliturushia mawe.” Kwa kuongezea, Majumba fulani ya Ufalme yaliporwa na kuharibiwa. Leo, ndugu zetu nchini Serbia wanaruhusiwa kisheria kukutana pamoja ingawa wanahitaji kufanya hivyo kwa busara.

      Ndugu wanaendelea kuhubiri kwa bidii. Wanaonyesha kwamba watu wa Yehova hawana maoni yasiyofaa kuelekea watu na kwamba wana upendo wa kweli kama wa Kristo. Kampeni zenye mafanikio za kuhubiri zimepangwa katika miaka ya karibuni, na akina ndugu kutoka katika nchi nyingine za Ulaya wametumia likizo yao kusaidia kuhubiri maeneo ambayo hayajahubiriwa nchini Serbia na Montenegro. Hata hivyo, bado wana kazi nyingi ya kuwahubiria watu karibu milioni tatu wanaoishi katika maeneo hayo.

      Leo Betheli ya Belgrade ina majengo matatu yaliyo katika bustani yenye kuvutia. Washiriki watatu wa Halmashauri ya Nchi wanasimamia kazi nchini Serbia na pia Montenegro. Yehova amewabariki watu wake katika eneo hilo lililokuwa na vita hivi kwamba jina Serbia sasa linatukumbusha bidii na azimio la Mashahidi wa Yehova.

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 232]

      ‘Walinihudumia kwa Njia Bora Kabisa’

      ŠANDOR PALFI

      ALIZALIWA 1933

      ALIBATIZWA 1964

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Wazazi wake walijifunza kweli katika kambi iliyoanzishwa na kikundi cha Wakomunisti muda mfupi baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Alikuwa mwangalizi anayesafiri mwishoni mwa juma na sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Nchi ya Serbia.

      KWA sababu familia yangu ilizaliwa Hungaria, tulipelekwa kwa muda mfupi katika kambi iliyoanzishwa na kikundi cha Wakomunisti. Hatua hiyo ilituletea baraka, kwa sababu wazazi wangu walijifunza kweli katika kambi hiyo. Nikiwa kijana, sikupendezwa sana na kweli. Lakini Ndugu Franz Brand aliyeishi katika nyumba yetu kwa miaka kadhaa alinisaidia sana kubadili maoni yangu. Nilidhani kwamba nilikuwa nikimsaidia tu nilipokubali ombi lake la kutafsiri kichapo cha Kihungaria katika Kiserbia. Baadaye niligundua kwamba hakikuhitaji kutafsiriwa; alitaka tu kuhakikisha kwamba nimesoma kichapo hicho. Mbinu yake ilifanya kazi, na punde si punde, nikabatizwa mwaka wa 1964.

      Jambo moja lililoniletea shangwe kubwa sana lilikuwa kutumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri. Haikuwa rahisi sikuzote kwa sababu akina ndugu walikuwa maskini. Mara nyingi nililala pamoja na familia nzima katika chumba kimoja. Kujidhabihu kwa njia hizo zote kulileta faida. Nilifurahi sana kuona shangwe ya akina ndugu, ambao walikuwa wakingojea kwa hamu ziara yangu. Walijitahidi kadiri wawezavyo kunihudumia kwa njia bora kabisa. Sikuwa na sababu yoyote ya kulalamika.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki