-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Historia ya Kisasa ya Slovenia
Kabla ya Slovenia kupata uhuru mwaka wa 1991, ilikuwa sehemu ya kaskazini-magharibi ya Yugoslavia. Baada ya Slovenia kupata uhuru, uchumi wake ulisitawi sana, ikajiunga na Muungano wa Ulaya mwaka wa 2004. Ingawa Slovenia ni nchi ndogo, ina mandhari mbalimbali zenye kuvutia. Ina milima mirefu iliyochongoka, maziwa yaliyo milimani, misitu mikubwa, mapango makubwa sana ya chokaa, na eneo maridadi sana la kitalii la pwani. Kwa muda wa saa moja hivi, unaweza kushuka kwenye miteremko yenye kuvutia sana ya milima na kufika kwenye mashamba yanayonukia vizuri ya mizeituni na mizabibu kwenye Pwani ya Adriatiki. Zaidi ya hayo, unaweza kujifunza mengi sana katika maeneo ya kitamaduni na ya kihistoria ya Slovenia. Hata hivyo, nchi hiyo ndogo ina uzuri mwingine zaidi ya uzuri wa mbuga za kitaifa na miji ya kihistoria. Slovenia ina utajiri mwingi sana wa kiroho.
MAJUMBA YA UFALME NA MAPAINIA
Bila shaka, unakumbuka kwamba Maribor ndio mji ambamo wale “vinyozi wanaoamini Biblia” walihubiri kuhusu imani yao mpya. Mkahawa fulani, ambao baadaye uliitwa kwa kufaa Novi Svet (Ulimwengu Mpya), ulikuwa mahali pazuri sana pa kukutania pa kikundi kidogo kilichoanzishwa huko. Leo, Mashahidi wa Slovenia wanamshukuru Yehova kwa sababu ya Majumba maridadi ya Ufalme ambamo wanakutania ili kuabudu na kufundishwa. Kwa sababu ya kuongezeka kwa idadi ya wahubiri, na kuboreka kwa hali katika miaka ya 1990, Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa ilianzishwa. Kwa msaada wa wajitoleaji zaidi ya 100 na michango kutoka nchi nyingine, makutaniko yamejenga au kurekebisha Majumba ya Ufalme 14 tangu 1995.
Hesabu ya wahubiri iliongezeka na pia hesabu ya mapainia wa kawaida, kutoka mapainia 10 mwaka wa 1990 mpaka 107 mwaka wa 2000. Anica Kristan alikuwa mmoja wa mapainia hao wenye bidii, na kabla ya kukubali kweli alijihusisha sana na siasa.
Ndugu na dada waliokuja kutumika nchini Slovenia kutoka katika nchi nyingine wamechangia sana ukuzi wa kazi ya kuhubiri. Mwaka wa 1992, wamishonari wa kwanza walifika Slovenia, Franco na Debbie Dagostini. Franco na Debbie walipopewa mgawo wa kwenda Afrika, wamishonari wawili wapya, Daniel na Karin Friedl kutoka Austria walitumwa Slovenia. Na hivi karibuni zaidi, wamishonari wa Gileadi, Geoffrey na Tonia Powell na Jochen na Michaela Fischer walitumwa Slovenia. Wamishonari hao pamoja na mapainia wa pekee kutoka Austria, Italia, na Poland, ambao wanampenda sana Yehova, wanatamani sana kuwasaidia watu.
HALMASHAURI ZA UHUSIANO NA HOSPITALI
Mnamo mwaka wa 1994, Dawati la Habari za Hospitali lilifunguliwa Betheli, na Halmashauri mbili za Uhusiano na Hospitali zikaanzishwa. Ndugu fulani waliowekwa rasmi katika halmashauri hizo walikutana na waziri wa afya, ambaye alipanga mkutano pamoja na wakurugenzi wa hospitali zote nchini Slovenia. Ndugu hao walieleza kazi ya Halmashauri za Uhusiano na Hospitali na kwa nini Mashahidi wa Yehova wanakataa kutiwa damu mishipani. Mkutano huo umesaidia madaktari kushirikiana vizuri na wagonjwa wanaokataa kutiwa damu mishipani, na zaidi ya hilo, makala zinazoeleza kuhusu matibabu bila damu zimechapishwa katika magazeti ya kitiba.
Mwaka wa 1995, madaktari wa Slovenia walifanya upasuaji wa kwanza wa moyo bila kutumia damu. Vyombo vya habari viliripoti kwamba upasuaji huo ulifanikiwa, na daktari na mtaalamu wa unusukaputi waliohusika wakaandika makala ya pekee kuhusu upasuaji huo. Hivyo, wagonjwa wanaweza kutibiwa bila kutiwa damu, na madaktari wengi zaidi wako tayari kuheshimu uamuzi wa Mashahidi wa Yehova wa matibabu yasiyohusisha damu.
KUTOSHELEZA MAHITAJI YA HESABU INAYOONGEZEKA YA WAHUBIRI
Baada ya mabadiliko ya kisiasa mwaka wa 1991, Baraza Linaloongoza liliamua kwamba ofisi inapaswa kufunguliwa huko Slovenia ili isimamie vizuri kazi ya Ufalme. Jengo la ghorofa moja lilinunuliwa katikati ya mji mkuu wa Slovenia, Ljubljana. Jengo hilo lilirekebishwa, na mnamo Julai 1, 1993 lilimalizika na Wanabetheli wakajitayarisha kuhamia humo. Mwanzoni, familia ya Betheli ilikuwa na washiriki 10, lakini katika muda wa miaka 10 hesabu yao iliongezeka kufikia 35. Kwa hiyo, jengo la karibu lilikodiwa, nalo lilikuwa na mahali pa kupikia, pa kulia vyakula, na pa kufulia nguo. Wakati huohuo, Wanabetheli walihamia nyumba nyingine za karibu ili kuwe na nafasi zaidi ya ofisi. Mwaka wa 1997, ofisi ya Slovenia ilianza kufanya kazi ikiwa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova.
Baraza Linaloongoza lilipotoa idhini ya kujenga ofisi mpya ya tawi nchini Slovenia, akina ndugu walianza kutafuta uwanja unaofaa. Baada ya kuchunguza viwanja karibu 40, ndugu walichagua uwanja ulio karibu na mji wa Kamnik, kilomita 20 kutoka kwenye mji mkuu, chini ya safu yenye kuvutia ya milima. Muda si muda, walitimiza matakwa yote ya ujenzi, wakapata vibali vya ujenzi, uwanja ukanunuliwa, wakafanya makubaliano pamoja na kampuni ya ujenzi, kisha watumishi wa kimataifa wakaitwa ili washiriki katika ujenzi huo. Walikuwa tayari kabisa kuanza ujenzi.
Hata hivyo, habari kuhusu mradi huo zilipoenea, majirani waliandamana haraka ili kupinga ujenzi huo. Siku ya kuanza ujenzi ilipofika, watu waliandamana na kufunga njia ya kuingia kwenye uwanja huo. Kisha wakabeba mabango ya kupinga mradi huo. Siku sita baadaye, karibu saa sita mchana, polisi 30 hivi walikuja kuwalinda wafanyakazi wa baraza la jiji waliotumwa kuondoa vizuizi vya waandamanaji; waandamanaji hao waliwatukana polisi. Kazi ya ujenzi ilikuwa imeahirishwa, basi hakuna ndugu wala mfanyakazi yeyote wa kampuni ya ujenzi aliyefika mahali pa ujenzi siku hiyo. Upinzani ulianza kupungua baada ya ujenzi kuahirishwa, na ndugu zetu walijaribu kusuluhisha tatizo hilo kwa amani.
Ua wa uwanja huo ulikuwa umebomolewa mara tatu na wapinzani, lakini mwishowe kazi ya ujenzi ilianza tena baada ya mwezi na kuendelea bila kuvurugwa. Kwa kweli, hatua hiyo ya kuwashambulia watu wa Yehova mwishowe ilileta baraka kwa sababu ilitangazwa sana na vyombo vya habari. Ripoti zaidi ya 150 kuhusu ujenzi huo zilitangazwa kwenye televisheni na redio na katika magazeti. Ujenzi ulikamilika baada ya miezi 11, na mnamo Agosti 2005, familia ya Betheli ilihamia majengo hayo mapya.
Tangu wakati huo, uhusiano kati ya ndugu na majirani wao umebadilika kabisa. Majirani wengi wametembelea ofisi ya tawi. Mtu mmoja aliyekuwa mpinzani baadaye alipendezwa sana na ujenzi huo. Alituuliza sisi ni nani na ni kazi gani itakayofanywa katika ofisi hiyo. Alipotembelea ofisi ya tawi, alivutiwa sana kuona akikaribishwa kwa urafiki na alivutiwa pia na usafi wa jengo hilo. Aliwaambia hivi akina ndugu: “Majirani wananiuliza ikiwa sasa nimejiunga nanyi. Nami ninawajibu hivi: ‘Hata ingawa niliwapinga vikali Mashahidi wa Yehova mwanzoni, sasa ninawaunga mkono kwa sababu ni watu wazuri.’”
Agosti 12, 2006 ilikuwa siku yenye furaha kwa sababu Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya wakfu iliyosikilizwa na watu 144 kutoka katika nchi 20 hivi. Katika mkutano wa pekee huko Ljubljana, aliwahutubia wasikilizaji 3,097 kutoka sehemu mbalimbali za Slovenia, na pia kutoka Kroatia na Bosnia na Herzegovina.
WAKATI UJAO MZURI
Mashahidi wa Yehova nchini Slovenia wana tumaini zuri la wakati ujao wakiwa na uhakika kwamba Baba yao wa mbinguni atawaongoza na kuwabariki. Katika kusanyiko la wilaya la 2004, walifurahi sana kupata Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kislovenia. Sasa, kwa kuwa wana ofisi mpya ya tawi yenye vifaa na wengi wao wanajitahidi wakiwa mapainia, wameazimia kutimiza mgawo wao wa kuhubiri na kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.
Nchi ya Slovenia ina Wakatoliki wengi, lakini enzi ya Ukomunisti iliwafanya watu wengi waamini kwamba hakuna Mungu. Kwa kuongezea, watu wengi wanalemewa na mahangaiko ya maisha au wanavutiwa na tamaa ya vitu vya kimwili. Wengine wanapendezwa zaidi na michezo au burudani. Hata hivyo, bado kuna watu wenye mioyo minyoofu wanaovutiwa na ahadi za Mungu zilizo katika Biblia.
Kazi imeendelea kusitawi. Slovenia ilifikia kilele cha wahubiri 1,935 katika mwezi wa Agosti 2008, na karibu robo ya wahubiri walishiriki katika utumishi mbalimbali wa upainia. Maeneo ya lugha za kigeni yanatia ndani maeneo yanayotumia Kialbania, Kichina, Kikroatia, Kiingereza, na Kiserbia, vilevile Lugha ya Ishara ya Slovenia. Tofauti na mwanzo mdogo wa kazi ya kuhubiri katika Slovenia, kulipokuwa na vinyozi wawili tu waliohubiri habari njema, sasa kuna umati mkubwa wa wahubiri wenye bidii kutoka katika mataifa mbalimbali wanaowatafuta watu wanaostahili ambao wanataka kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.—Mt. 10:11.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 249, 259]
“Ni Kana Kwamba Yehova Aliwafumba Macho”
JANEZ NOVAK
ALIZALIWA 1964
ALIBATIZWA 1983
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikaa gerezani kwa miaka mitatu kwa sababu ya imani yake na sasa yeye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Slovenia.
MNAMO Desemba 1984, wakuu wa jeshi waliniagiza tena na tena nijiunge na jeshi. Walipobandika kwenye mlango wangu taarifa ya kuniita katika jeshi na kutisha kwamba askari-jeshi wangekuja kunichukua, niliamua kwenda kwenye kambi ya jeshi ili nieleze msimamo wangu. Sikufaulu, hivyo wakaamua kufanya yote wanayoweza ili kunilazimisha kuwa mwanajeshi. Walininyoa kichwa, wakachukua nguo zangu za raia, na kunipa nguo za wanajeshi. Nilipokataa nguo hizo, walinivisha kwa nguvu, kisha wakajaribu kunilazimisha kushika kalamu na kutia sahihi ya kukubali kujiunga na jeshi. Nilikataa.
Pia nilikataa kufanya mazoezi ya asubuhi na kuisalimu bendera. Wanajeshi wanne waliponipeleka uwanjani na kuniamuru nifanye mazoezi, nilikataa kuinua mikono yangu. Walijaribu kuinua mikono yangu lakini wakaona kwamba ni jambo la kipumbavu sana kujaribu kuniinua mikono. Walinielekezea bunduki na kutisha kuniua. Nyakati nyingine walijaribu kunihonga kwa kunipa kahawa na keki.
Wanajeshi wengine walilia walipoona azimio langu. Wengine walikasirika nilipokataa kuitemea mate picha ya Jemadari Tito ambayo waliiweka mbele ya uso wangu. Baada ya siku kadhaa, walijaribu kunilazimisha kubeba silaha, nikakataa pia. Hilo lilionwa kuwa kosa la kijeshi, hivyo nikafungiwa kambini kwa mwezi mmoja. Halafu nilikaa gerezani huko Zagreb, Kroatia, kwa majuma kadhaa, nikingojea uamuzi. Taa nyekundu iliwashwa kwenye chumba changu cha gereza usiku mzima, na niliruhusiwa kwenda chooni ikiwa tu askari aliyekuwa kwenye zamu alikuwa na furaha siku hiyo.
Mwishowe, nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu gerezani kwenye kisiwa cha Adriatiki kinachoitwa Goli Otok, ambako wafungwa hatari sana walipelekwa. Walinipeleka kwenye gereza hilo ambalo lilikuwa na wafungwa wakatili sana. Walinifunga mikono kwa minyororo kwa sababu nilikataa kupigana vita. Katika gereza hilo nilikutana na Mashahidi wengine wanne ambao walifungwa kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono vita.
Hatukuruhusiwa kuwa na Biblia au kitabu kingine chochote. Hata hivyo, tayari kulikuwa na Biblia moja gerezani. Watu wangu wa ukoo walinitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi ndani ya sanduku lenye sehemu iliyojificha. Walinzi hawakupata kamwe vichapo vyetu wala hawakugundua kamwe kwamba tulikuwa tukifanya mikutano ya Kikristo. Nyakati nyingine, walinzi walipokuja, vichapo vilivyosahauliwa vilikuwa mbele yao tu, lakini ni kana kwamba Yehova aliwafumba macho kwa sababu hawakuviona hata kidogo.
Baada ya mwaka mmoja, nilipelekwa Slovenia ili nimalizie kifungo changu huko. Nilimwoa Rahela nilipokuwa gerezani. Nilipoachiliwa huru, nilianza kufanya upainia pamoja na mke wangu, na tangu 1993 tumekuwa tukitumikia katika Betheli ya Slovenia.
-