Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ibada ya Kweli Yapanuka Ulimwenguni Pote
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Sura Ya Ishirini Na Moja

      Ibada ya Kweli Yapanuka Ulimwenguni Pote

      Isaya 60:1-22

      1. Isaya sura ya 60 ina ujumbe gani wa kutia moyo?

      SURA ya 60 ya Isaya imeandikwa kama drama yenye kuchochea kweli kweli. Katika mistari ya kwanza, fikira zetu zinanaswa na tamasha yenye kusisimua moyo. Matukio yanafuatana mbio-mbio, yakituongoza kwenye upeo wa kuvutia. Sura hiyo inatumia maneno maridadi kuhusu kurudishwa kwa ibada ya kweli katika Yerusalemu la kale na kupanuka kwa ibada ya kweli ulimwenguni pote leo. Tena, inaelekeza kwenye baraka za milele zinazowangoja wale wanaomwabudu Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu. Kila mmoja wetu anaweza kushiriki katika utimizo wa sehemu hii ya kusisimua ya unabii wa Isaya. Basi acheni tuichunguze kwa uangalifu.

      Nuru Yang’aa Gizani

      2. Mwanamke fulani aliyelala gizani anapewa amri gani, na kwa nini anapaswa kutii haraka?

      2 Maneno ya kwanza ya sura hii ya Isaya yameelekezwa kwa mwanamke mwenye hali za huzuni. Ni wazi kwamba mwanamke huyo amelala kifudifudi gizani. Kwa ghafula, nuru yapenya ule weusi, huku Yehova akimtumia Isaya kupaaza sauti hivi: “Ondoka, [“inuka, Ee mwanamke,” “NW”] uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja; na utukufu wa BWANA umekuzukia.” (Isaya 60:1) Ndiyo, “mwanamke” huyo anapaswa kusimama ili yeye naye aangaze utukufu wa Mungu! Kwa nini afanye hivyo haraka? Unabii unaendelea kusema hivi: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu; bali BWANA atakuzukia wewe, na utukufu wake utaonekana juu yako.” (Isaya 60:2) Ni lazima “mwanamke” huyo ‘aangaze’ kwa faida ya wale wanaomzunguka, ambao wangali wanapapasa-papasa gizani. Kutakuwa na matokeo gani? “Mataifa wataijilia nuru yako, na wafalme kuujia mwanga wa kuzuka kwako.” (Isaya 60:3) Maneno haya ya kwanza yanaandaa maana hasa ya kile kitakachoelezwa kwa urefu katika mistari inayofuata. Yaani, ni lazima ibada ya kweli ipanuke ulimwenguni pote!

      3. (a) “Mwanamke” huyo ni nani? (b) Kwa nini “mwanamke” huyo amekuwa akilala gizani?

      3 Ingawa Yehova anaongea juu ya matukio ya wakati ujao, anamwambia yule “mwanamke” kwamba nuru yake “imekuja.” Hiyo inakazia uhakika wa kwamba unabii huo utatimizwa.

  • Ibada ya Kweli Yapanuka Ulimwenguni Pote
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Utimizo Mkubwa Zaidi

      4. Ni akina nani leo duniani wanaowakilisha yule “mwanamke,” na matumizi mapana ya unabii huo yanahusu nani?

      4 Licha ya kupendezwa na utimizo wa unabii huu kuhusiana na Yerusalemu la kale, tunapendezwa pia na utimizo wake wa baadaye. Leo “mwanamke” wa kimbingu wa Yehova anawakilishwa duniani na “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Katika muda ambao taifa hili la kiroho limekuwako, tangu Pentekoste 33 W.K. mpaka sasa, limekuja kuwa na jumla ya washirika watiwa-mafuta 144,000, “ambao wamenunuliwa kutoka katika dunia” wakitazamia kutawala pamoja na Kristo mbinguni. (Ufunuo 14:1, 3) Utimizo wa kisasa wa Isaya sura ya 60 unawahusu hasa wale 144,000 walio hai duniani wakati wa “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Unabii huu unawahusu pia waandamani wa Wakristo hao watiwa-mafuta, yaani “umati mkubwa” wa “kondoo wengine.”—Ufunuo 7:9; Yohana 10:11, 16.

      5. Washiriki waliobaki wa Israeli wa Mungu walijikuta wakiwa wamelala gizani lini, na nuru ya Yehova iliwaangazia lini?

      5 Kwa muda mfupi katika miaka ya mapema ya 1900, washirika wa Israeli wa Mungu ambao wangali duniani walikuwa wakisujudu gizani, kwa usemi wa mfano. Vita ya kwanza ya ulimwengu ilipokuwa ikikaribia kumalizika, walikuwa katika hali inayoelezwa kwa njia ya mfano katika kitabu cha Ufunuo, yaani, maiti zao zilikuwa zimelala “juu ya njia pana ya jiji kubwa ambalo katika maana ya kiroho laitwa Sodoma na Misri.” (Ufunuo 11:8) Hata hivyo, mwaka wa 1919 Yehova akawaangazia nuru yake. Nao wakaitikia kwa kusimama na kuangazia wengine nuru hiyo, wakitangaza habari njema za Ufalme wa Mungu bila hofu.—Mathayo 5:14-16; 24:14.

      6. Ulimwengu kwa ujumla umeitikiaje tangazo la kuwapo kwa Yesu akiwa mfalme, lakini ni nani ambao wamevutiwa na nuru ya Yehova?

      6 Wanadamu kwa ujumla wameshawishiwa na Shetani, mkuu wa “watawala wa ulimwengu wa giza hili,” kulikataa tangazo linalotolewa kuhusu kuwapo kwa Yesu Kristo, aliye “nuru ya ulimwengu.” Tangazo hilo linasema kwamba sasa Yesu ni mfalme. (Waefeso 6:12; Yohana 8:12; 2 Wakorintho 4:3, 4) Hata hivyo, mamilioni ya watu wamevutiwa na nuru ya Yehova. Watu hao ni kutia ndani “wafalme” (wale ambao wamekuwa warithi watiwa-mafuta wa Ufalme wa kimbingu) na “mataifa” (ule umati mkubwa wa kondoo wengine).

      Mpanuko Waleta Shangwe ya Moyoni

      7. Yule “mwanamke” anaona jambo gani la kuchangamsha moyo?

      7 Akiendeleza habari iliyotajwa katika Isaya 60:3, Yehova anampa yule “mwanamke” amri nyingine: “Inua macho yako, utazame pande zote”! “Mwanamke” huyo anapotii, anaona jambo la kuchangamsha moyo—loo, watoto wake ndio hawa wakija nyumbani! “Wote wanakusanyana; wanakujia wewe; wana wako watakuja kutoka mbali. Na binti zako watabebwa nyongani.” (Isaya 60:4) Matokeo ya kutangazwa kwa Ufalme katika mataifa yote kuanzia mwaka wa 1919 ni kwamba maelfu ya “wana” na “binti” watiwa-mafuta wanaunganishwa na Israeli wa Mungu. Kwa njia hiyo, Yehova alichukua hatua za kukamilisha idadi iliyotabiriwa ya wale 144,000, ambao watatawala pamoja na Kristo.—Ufunuo 5:9, 10.

      8. Israeli wa Mungu wamekuwa na sababu gani ya kufurahi tangu mwaka wa 1919?

      8 Ongezeko hilo lilileta shangwe. “Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, utajiri wa mataifa utakuwasilia.” (Isaya 60:5) Israeli wa Mungu alifurahi sana kwa sababu ya kukusanywa kwa watiwa-mafuta miaka ya 1920 na ya 1930. Hata hivyo, wamekuwa na sababu nyingine ya shangwe. Hasa tangu miaka ya katikati ya 1930, watu ambao hapo kwanza walikuwa sehemu ya “bahari” ya wanadamu waliotenganishwa na Mungu wametoka katika mataifa yote ili kuabudu pamoja na Israeli wa Mungu. (Isaya 57:20; Hagai 2:7) Watu hawa hawaendi zao kumtumikia Mungu, kila mtu kivyake. Bali, wanamjia “mwanamke” wa Mungu na kuwa sehemu ya kundi la Mungu lenye umoja. Matokeo ni kwamba, watumishi wote wa Mungu wanashiriki kuipanua ibada ya kweli.

      Mataifa Yatoka Pande Zote Kuja Kukutanikia Yerusalemu

      9, 10. Ni nani wanaoonekana wakitoka pande mbalimbali kuja kukutanikia Yerusalemu, na Yehova anawapokeaje?

      9 Yehova anaeleza jinsi mpanuko utakavyofanyika, akitumia mifano inayofahamika na watu wa wakati wa Isaya. “Mwanamke” huyo anatazama akiwa pale alipo juu ya Mlima Sayuni na kuangaza-angaza macho yake kwenye upeo wa mashariki. Anaona nini? “Wingi wa ngamia utakufunika, ngamia vijana wa Midiani na Efa; wote watakuja kutoka Sheba; wataleta dhahabu na uvumba; na kuzitangaza sifa za BWANA.” (Isaya 60:6) Misafara ya ngamia inayotumiwa na wafanya-biashara wa makabila mbalimbali inashika njia kwenda Yerusalemu ikipita katika barabara zinazoelekea huko. (Mwanzo 37:25, 28; Waamuzi 6:1, 5; 1 Wafalme 10:1, 2) Ngamia wako kila mahali, kama mafuriko yanayoifunika nchi! Misafara hiyo inaleta zawadi za thamani kubwa, kuonyesha kwamba wafanya-biashara hao wanakuja wakiwa na makusudio ya amani. Wanataka kumwabudu Yehova na kumpa kilicho bora.

      10 Si wafanya-biashara hawa tu walio mwendoni. “Makundi yote ya Kedari yatakusanyika kwako, kondoo waume wa Nebayothi watakutumikia.” Ndiyo, hata makabila yaliyo na desturi ya kuchunga mifugo yanasafiri kwenda Yerusalemu. Yanakuja na zawadi za mali zao zenye thamani kubwa zaidi, yaani makundi ya kondoo, kisha wanajitoa wawe wahudumu. Yehova atawapokeaje? Yeye anasema: “Watapanda juu ya madhabahu yangu kwa kibali, nami nitaitukuza nyumba ya utukufu wangu.” (Isaya 60:7) Yehova anazikubali zawadi zao, nazo zitatumiwa katika ibada safi.—Isaya 56:7; Yeremia 49:28, 29.

      11, 12. (a) Yule “mwanamke” anaona nini anapokaza macho magharibi? (b) Kwa nini watu wengi sana wanafanya haraka kwenda Yerusalemu?

      11 Sasa Yehova anamwagiza yule “mwanamke” atazame kwenye upeo wa magharibi. Halafu Yehova anauliza: “Ni nani hawa warukao kama wingu, na kama njiwa waendao madirishani kwao?” Yehova mwenyewe anajibu hivi: “Hakika yake visiwa vitaningojea, na merikebu za Tarshishi kwanza, ili kuleta wana wako kutoka mbali, na fedha yao na dhahabu yao pamoja nao, kwa ajili ya jina la BWANA, Mungu wako, kwa ajili yake Mtakatifu wa Israeli, kwa kuwa amekutukuza wewe.”—Isaya 60:8, 9.

      12 Wazia kwamba umesimama pamoja na “mwanamke” huyo, ukikaza macho magharibi ng’ambo ya Bahari Kuu. Unaona nini? Wingu la mbali la madoa meupe yakielea juu ya maji. Wanaonekana kama ndege. Lakini wanapokaribia zaidi, unaona kwamba kumbe ni merikebu zenye matanga yaliyotwekwa. ‘Zimekuja kutoka mbali.’a (Isaya 49:12) Mashua zinazoenda kasi kuelekea Sayuni ni nyingi sana hivi kwamba zinaonekana kama kundi la njiwa wanaoelekea nyumbani. Haraka yote hiyo ya nini? Kikosi hicho kina hamu nyingi ya kuwafikisha pwani waabudu wa Yehova waliomo, ambao wametoka bandari za mbali. Kwa kweli, wote wale wanaowasili sasa hivi—Waisraeli na wageni pia, kutoka mashariki au magharibi na kutoka nchi za karibu au za mbali—wanafanya haraka kwenda Yerusalemu wakafanye vitu vyote walivyo navyo viwe wakfu kwa jina la Yehova, Mungu wao.—Isaya 55:5.

      13. Nyakati za kisasa, “wana” na “binti” ni akina nani, na “utajiri wa mataifa” ni akina nani?

      13 Lo, andiko la Isaya 60:4-9 linatoa ufafanuzi ulio wazi kama nini kuhusu mpanuko ambao umetukia ulimwenguni pote tangu “mwanamke” wa Yehova aanze kuangaza nuru katikati ya giza la ulimwengu huu! Kwanza wakafika “wana” na “binti” za Sayuni wa kimbingu, wale waliokuja kuwa Wakristo watiwa-mafuta. Mwaka wa 1931, walijitambulisha peupe kuwa Mashahidi wa Yehova. Halafu wingu la watu watiifu, ambao ndio “utajiri wa mataifa” na “wingi wa bahari,” likafanya haraka kujiunga na ndugu za Kristo waliobaki.b Leo watumishi wote hawa wa Yehova wanaotoka pembe nne za dunia na kutoka hali zote za maisha wanajiunga na Israeli wa Mungu kumsifu Bwana wao Mwenye Enzi Kuu, Yehova, na kukweza jina lake kuwa ndilo tukufu zaidi katika ulimwengu mzima.

      14. Wale wanaowasili sasa hivi ‘wanapandaje juu ya madhabahu ya Mungu’?

      14 Ingawa hivyo, inamaanisha nini kwamba watu hawa wanaowasili sasa hivi kutoka kwenye mataifa “watapanda juu ya madhabahu [ya Mungu]”? Dhabihu huwekwa juu ya madhabahu. Mtume Paulo alitumia usemi unaohusisha dhabihu alipoandika hivi: “Nawasihi sana nyinyi . . . mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri.” (Waroma 12:1) Wakristo wa kweli wana moyo wa kujitoa. (Luka 9:23, 24) Wanatoa wakati wao, nguvu zao, na stadi zao kuendeleza ibada safi. (Waroma 6:13) Kwa kufanya hivyo, wanatoa dhabihu zinazokubalika za kumsifu Mungu. (Waebrania 13:15) Jambo la kwamba mamilioni ya waabudu wa Yehova leo, vijana kwa wazee, wameweka tamaa zao za kibinafsi nyuma ya masilahi ya Ufalme wa Mungu, linachangamsha moyo kama nini! Wanaonyesha roho ya kweli ya kujidhabihu.—Mathayo 6:33; 2 Wakorintho 5:15.

      Wale Wanaowasili Sasa Hivi Wanashiriki Katika Mpanuko

      15. (a) Nyakati za kale, rehema ya Yehova ilionyeshwaje kuhusiana na wageni? (b) Nyakati za kisasa, “wageni” wameshiriki jinsi gani kuijenga ibada ya kweli?

      15 Wale wanaowasili sasa hivi wanatoa mali zao na hata huduma zao binafsi kumtegemeza “mwanamke” wa Yehova. “Wageni watajenga kuta zako, na wafalme wao watakuhudumu; maana katika ghadhabu yangu nalikupiga, lakini katika upendeleo wangu nimekurehemu.” (Isaya 60:10) Rehema ya Yehova ilionyeshwa karne ya sita K.W.K. wakati wageni waliposaidia kazi ya ujenzi Yerusalemu. (Ezra 3:7; Nehemia 3:26) Katika utimizo mkubwa wa leo, “wageni,” yaani umati mkubwa, wanaunga mkono mabaki watiwa-mafuta kujenga ibada ya kweli. Wanasaidia kujenga sifa za Kikristo katika wanafunzi wao wa Biblia, na hivyo wanajenga makutaniko ya Kikristo na kuimarisha “kuta” za tengenezo la Yehova. (1 Wakorintho 3:10-15) Pia wanajenga kwa njia halisi, wakijibidiisha kujenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya Betheli. Hivyo wanajiunga na ndugu zao watiwa-mafuta kutunza mahitaji ya tengenezo la Yehova linalopanuka.—Isaya 61:5.

      16, 17. (a) “Malango” ya tengenezo la Mungu yamewekwaje wazi? (b) “Wafalme” wamemhudumiaje Sayuni? (c) Itakuwaje kwa wale wanaojaribu kuyafunga “malango” ambayo Yehova anataka yaachwe wazi?

      16 Matokeo ya programu ya ujenzi wa kiroho ni kwamba, kila mwaka mamia ya maelfu ya “wageni” huanza kushirikiana na tengenezo la Yehova, na njia huwa wazi ili wengi hata zaidi waingie. Yehova anasema hivi: “Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; hayatafungwa mchana wala usiku; ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa, na wafalme wao wakiongozwa pamoja nao.” (Isaya 60:11) Ingawa hivyo, ni akina nani wale “wafalme” wanaoongoza kuuletea Sayuni utajiri wa mataifa?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki