-
Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya AjabuSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
“UTASIMAMA”
18, 19. (a) Malaika alimaanisha nini alipomwambia Danieli kwamba ‘angesimama’ wakati ujao? (b) Danieli angewezaje kujua juu ya tumaini la ufufuo?
18 Kitabu cha Danieli chamalizika kwa mojawapo ya ahadi nzuri sana ambazo Mungu amepata kumwahidi mwanadamu. Malaika wa Yehova alimwambia Danieli hivi: “Nawe utasimama katika kura yako mwisho wa siku hizo.” Malaika huyo alimaanisha nini? Basi, kwa kuwa ‘starehe’ aliyokuwa ametoka tu kurejezea ilikuwa kifo, ahadi ya kwamba Danieli ‘angesimama’ wakati fulani ujao, ingeweza kumaanisha kitu kimoja tu—ufufuo!b Hata wasomi fulani wamesisitiza kwamba Danieli sura ya 12 ina rejezo la kwanza lililo wazi kabisa juu ya ufufuo liwezalo kupatikana katika Maandiko ya Kiebrania. (Danieli 12:2) Hata hivyo, wamekosea. Danieli alijua vema juu ya tumaini la ufufuo.
19 Kwa kielelezo, haikosi Danieli alijua maneno haya ambayo Isaya alikuwa amerekodi karne mbili mapema: “Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, ninyi mnaokaa mavumbini, kwa maana . . . ardhi itawatoa waliokufa.” (Isaya 26:19) Muda mrefu kabla ya hapo, Eliya na Elisha waliwezeshwa na Yehova kufufua watu kihalisi. (1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37) Hata mapema zaidi, Hana, mama ya nabii Samweli, alikiri kwamba Yehova aweza kuleta watu juu kutoka kuzimu, kaburini. (1 Samweli 2:6) Isitoshe, hata mapema zaidi, Yobu mwaminifu alionyesha tumaini lake mwenyewe katika maneno haya: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu, hata kufunguliwa kwangu kunifikilie. Wewe ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.”—Ayubu 14:14, 15.
20, 21. (a) Kwa hakika Danieli atapata ufufuo gani? (b) Yamkini ufufuo katika Paradiso utafanywaje?
20 Kama Yobu, Danieli alikuwa na sababu za kuwa na uhakika kwamba Yehova kwa kweli angetamani sana kumrudisha kwenye uhai siku fulani wakati ujao. Hata hivyo, bado lazima alitiwa moyo sana kusikia kiumbe-roho chenye nguvu kikimhakikishia tumaini hilo. Ndiyo, Danieli atasimama katika “ufufuo wa walio waadilifu,” utakaofanywa wakati wa Utawala wa Mileani wa Kristo. (Luka 14:14) Hilo litakuwaje kwa Danieli? Neno la Mungu hutuambia mengi zaidi juu yake.
21 Yehova ni “Mungu, si wa kukosa utaratibu, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Basi ni dhahiri kwamba ufufuo katika Paradiso utafanywa kwa utaratibu. Huenda wakati fulani utakuwa umepita tangu Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Mfumo wa mambo wa kale utakuwa umeondolewa kabisa, na bila shaka matayarisho ya kuwakaribisha wafu yatakuwa yamefanywa. Kwa habari ya utaratibu ambao wafu watafufuliwa, Biblia yatoa utaratibu huu: “Kila mmoja katika daraja lake mwenyewe.” (1 Wakorintho 15:23) Yaonekana kwamba wakati wa “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu,” waadilifu watafufuliwa kwanza. (Matendo 24:15) Kwa hiyo, watu waaminifu wa kale, kama vile Danieli, wataweza kusaidia katika kusimamia mambo ya kidunia, kutia ndani kufundisha mabilioni ya “wasio waadilifu” watakaofufuliwa.—Zaburi 45:16.
22. Huenda Danieli atakuwa na hamu ya kujibiwa maswali gani?
22 Kabla Danieli hajawa tayari kutwaa madaraka hayo, huenda atakuwa na maswali ya kuuliza. Kwani, alisema hivi kuhusu unabii mbalimbali mgumu aliokabidhiwa: “Nami nikasikia, lakini sikuelewa.” (Danieli 12:8) Atasisimuka kama nini kuweza kuelewa mafumbo hayo ya Mungu hatimaye! Huenda atataka kusikia yote juu ya Mesiya. Danieli atapata kujua na kustaajabia mfuatano wa serikali za ulimwengu tangu siku yake mwenyewe hadi leo, atajua ni nani “watakatifu wa Aliye juu”—waliovumilia licha ya minyanyaso katika “wakati wa mwisho”—na juu ya ule uharibifu wa mwisho wa falme zote utakaoletwa na Ufalme wa Kimesiya wa Mungu.—Danieli 2:44; 7:22; 12:4.
KURA YA DANIELI NA YAKO KATIKA PARADISO!
23, 24. (a) Ulimwengu ambao Danieli atajikuta ndani yake utakuwaje tofauti na ulimwengu alioujua? (b) Je, Danieli atakuwa na mahali katika Paradiso, nasi twajuaje?
23 Danieli atataka kujua juu ya ulimwengu atakaojikuta ndani yake wakati huo—ulimwengu ulio tofauti sana na ule alioishi. Hakutakuwa na vita vyovyote wala uonezi wowote ambao uliharibu ulimwengu alioujua. Hakutakuwa majonzi yoyote, ugonjwa wowote, wala kifo chochote. (Isaya 25:8; 33:24) Lakini kutakuwa na wingi wa chakula, nyumba nyingi, na kazi yenye kuridhisha kwa watu wote. (Zaburi 72:16; Isaya 65:21, 22) Wanadamu watakuwa familia moja iliyoungana na yenye furaha.
24 Ni dhahiri kwamba Danieli atakuwa na mahali katika ulimwengu huo. “Utasimama katika kura yako,” malaika alimwambia. (Italiki ni zetu.) Neno la Kiebrania ambalo latafsiriwa “kura” hapa ndilo lilelile ambalo hutumiwa kurejezea viwanja halisi vya shamba.c Huenda Danieli aliujua unabii wa Ezekieli juu ya kugawa nchi iliyorudishwa ya Israeli. (Ezekieli 47:13–48:35) Katika utimizo wake kwenye Paradiso, unabii wa Ezekieli wadokeza nini? Kwamba watu wote wa Mungu watakuwa na mahali katika Paradiso, hata nchi itagawanywa kwa utaratibu na kwa haki. Bila shaka, kura ya Danieli katika Paradiso itahusisha mengi zaidi ya nchi tu. Itatia ndani fungu lake katika kusudi la Mungu huko. Hakika Danieli atapata thawabu aliyoahidiwa.
25. (a) Ni matazamio gani ya maisha katika Paradiso yanayokupendeza? (b) Kwa nini twaweza kusema kwamba Paradiso ni makao ya wanadamu?
25 Hata hivyo, vipi juu ya kura yako? Wewe vilevile waweza kupata ahadi hizo. Yehova anataka wanadamu watiifu ‘wasimame’ kwa ajili ya kura zao, wawe na mahali katika Paradiso. Hebu wazia! Kwa kweli, lingekuwa jambo lenye kusisimua kwelikweli kukutana na Danieli ana kwa ana, pamoja na wanaume na wanawake wengine waaminifu wa nyakati za Biblia. Kisha kutakuwa na wengine wengi watakaofufuliwa, watakaohitaji kufundishwa ili wapate kumjua na kumpenda Yehova Mungu. Jiwazie ukitunza makao yetu ya kidunia na kusaidia kuyafanya yawe paradiso yenye unamna-namna mwingi na uzuri wenye kudumu. Wazia kufundishwa na Yehova, kujifunza kuishi alivyokusudia wanadamu waishi. (Isaya 11:9; Yohana 6:45) Naam, una mahali katika Paradiso. Ingawa huenda wengine wakaiona Paradiso kuwa kitu kipya, kumbuka kwamba mwanzoni Yehova alikusudia wanadamu waishi mahali pa aina hiyo. (Mwanzo 2:7-9) Katika maana hiyo, Paradiso ndiyo makao ya asili ya mabilioni ya wakazi wa dunia. Huko ndiko kwao. Kufikia Paradiso kutakuwa sawa na kurudi nyumbani.
-
-
Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya AjabuSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
b Kulingana na The Brown-Driver-Briggs Hebrew and English Lexicon, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-simama” ambalo latumiwa hapa larejezea “kuhuishwa baada ya kifo.”
-
-
Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya AjabuSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
c Neno hilo la Kiebrania lahusiana na neno “kijiwe cha mviringo,” kwa kuwa vijiwe vidogo vilitumiwa kupiga kura. Nyakati nyingine nchi iligawanywa hivyo. (Hesabu 26:55, 56) Kichapo A Handbook on the Book of Daniel chasema kwamba hapa neno hilo lamaanisha “kilichowekwa kando (na Mungu) kwa ajili ya mtu.”
-