Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mfadhaiko Hatari Kubwa kwa Afya
    Amkeni!—2010 | Juni
    • Mfadhaiko Hatari Kubwa kwa Afya

      “Ninafanya kazi kwa muda mrefu, usiku na mchana. Mara nyingi ninapomaliza upasuaji katika hospitali moja, ninakuwa na dakika chache tu za kwenda kwenye hospitali nyingine kupitia barabara yenye msongamano mwingi ili nikashughulikie upasuaji mwingine.”—Dakt. Peter Stuart, Afrika Kusini.

      HUENDA unaelewa hisia za Dakt. Stuart, hata ikiwa hali zinazokuletea mfadhaiko ni tofauti na zake. Hata mfadhaiko wako uwe unasababishwa na jambo gani—iwe ni kuendesha gari katika barabara zenye msongamano mkubwa, hali ya kutoelewana nyumbani au kazini, au iwe ni jambo tofauti—ni kawaida kwa wanadamu kukabiliana na mfadhaiko.

      Zaidi ya karne 30 zilizopita, mwanajeshi mwenye uzoefu alikiri hivi waziwazi: “Kutetemeka kunaingia ndani yangu, na mtetemeko unanifunika.” (Zaburi 55:5) Mwanamume huyo alielewa mfadhaiko ni nini. Alipokuwa kijana mchungaji, alikabiliana na simba, dubu, na shujaa aliyekusudia kumwua.—1 Samweli 17:4-10, 23, 24, 34-36, 41-51.

      Kwa kweli, si vibaya kupatwa na mkazo. Mkazo unaweza kutusaidia tukabiliane na kipingamizi. Watu wanapokabiliwa na hali zinazohatarisha maisha, mkazo umewawezesha kufanya mambo ambayo hawakufikiria wanaweza kufanya. Ulipokuwa na mgawo muhimu, huenda mkazo ulitokeza adrenalini ndani yako na hilo likakuchochea umalize mgawo huo kwa wakati.a

      Hata hivyo, mkazo unapozidi sana mwili wetu hushindwa kutulia kisha tunafadhaika. Mtafiti mmoja anasema kwamba “mfadhaiko ndio unaotokeza hatari kubwa zaidi kwa afya yetu.” Ikiwa unahisi kwamba huwezi kuvumilia mfadhaiko wako au ikiwa ungependa kuepuka kupatwa na mfadhaiko mkali, huenda ukajiuliza, “Je, kuna jambo lolote ninaloweza kufanya ili nipunguze mfadhaiko?”

      Ndiyo kunalo! Wote wanaweza kupata msaada ambao umewasaidia watu wengi kukabiliana na mfadhaiko. Msaada huo unatoka katika chanzo ambacho hungetazamia, yaani, Neno la Mungu, Biblia. Ingawa Biblia si kitabu cha kutoa msaada wa kitiba, kina hekima inayoweza kutusaidia. Kinaeleza kwa nini watu wanafadhaika sana leo na kinaonyesha mambo yanayosababisha au kuchangia mfadhaiko. Pia kina mapendekezo ya kutusaidia kupunguza na kukabiliana na mfadhaiko.

      [Maelezo ya Chini]

      a Adrenalini ni homoni inayotokezwa na tezi za adrenali na inakusaidia kukabiliana na hali za dharura.

  • Jinsi Mfadhaiko Unavyotuathiri
    Amkeni!—2010 | Juni
    • Jinsi Mfadhaiko Unavyotuathiri

      Ni nini hutukia unapokimbia ili usiachwe na basi au treni? Bila shaka, unahisi jinsi shinikizo la damu mwilini hupanda na kufanya moyo wako upige kwa kasi zaidi. Hata ukiachwa na basi hilo, moyo wako utaacha kupiga kwa kasi na utapumua kwa njia ya kawaida.

      HATA hivyo, mambo yanaweza kuwa tofauti unaposhughulika na hali yenye kufadhaisha inayoendelea kwa muda mrefu. Inaweza kuchukua muda mrefu zaidi kabla ya wasiwasi, kukazika kwa misuli, kupanda kwa shinikizo la damu, na mfumo wako wa umeng’enyaji kurudia hali ya kawaida. Watu wanazidi kutambua kwamba si rahisi kuacha kuwa na wasiwasi. Kwa mfano, wengi huhisi kana kwamba wao ni wafungwa katika kazi ambayo haiwaletei faida yoyote. Mfadhaiko unaathiri mwili na afya yako kwa njia gani?

      Jinsi Mwili Wako Unavyotenda Unapofadhaika

      Dakt. Arien van der Merwe, mtaalamu anayeshughulikia mfadhaiko, anaeleza jinsi ambavyo mwili wako hutenda unapofadhaika. Mara moja mwili unaanza kutenda na “kemikali nyingi za mfumo wa neva na homoni huenea mwilini na kutayarisha viungo na mifumo yote iwe tayari kukabiliana na mfadhaiko unaokuja.”

      Uko tayari kuchukua hatua upesi. Hisi zako zote zinatendeshwa, iwe ni ile ya kuona, kusikia, au kugusa. Ubongo wako hutenda kwa kasi na tezi zako za adrenali hutoa homoni zenye nguvu, na kutendesha misuli yako kutia ndani moyo, mapafu, na viungo vingine ili viweze kukabiliana na hali yoyote yenye kufadhaisha.

      Kwa hiyo, hali ya dharura inapotokea uhai wako unaweza kuokolewa kwa sababu ya jinsi mwili wako unavyotenda unapofadhaika, kama vile kukufanya uruke kando na kuhepa gari linalokaribia. Hata hivyo, hali huwa tofauti kabisa mfadhaiko unapoendelea.

      Mfadhaiko Unapokuwa Wenye Kudhuru

      Namna gani ikiwa kila wakati mwili wako unatendeshwa kwa kasi hivyo? Misuli yako itaendelea kukazika, moyo wako utaendelea kupiga kwa kasi, shinikizo la damu litaendelea kuwa juu, na damu itaendelea kuwa na viwango vya juu vya kolesteroli, mafuta, sukari, homoni, na kemikali nyingine. Kemikali kama hizo—ambazo zimekusudiwa kutokea kwa wakati mfupi tu kunapokuwa na mkazo—zinaweza kuharibu viungo muhimu vya mwili iwapo zitaendelea kutokezwa kwa wingi. Kukiwa na madhara gani?

      Unaweza kuanza kupatwa na maumivu ya mgongo, kichwa, mshtuko wa ghafula wa misuli ya shingo, na kukazika kwa misuli. Madaktari wanasema kwamba mara nyingi dalili kama hizo zinahusiana na mfadhaiko wa kuendelea. Mfadhaiko kama huo unaweza kumfanya mtu asiwe na matokeo kazini, na hata unaweza kumfanya asiwe mchangamfu na asiwe na uhusiano mzuri na wengine. Unaweza pia kumfanya awe na ugonjwa wa kuhara, kukazika kwa misuli ya umio. Huenda mfadhaiko unaoendelea ukatokeza madhara makubwa hata zaidi. Magonjwa kama vile kiharusi, mshtuko wa moyo, figo kuacha kufanya kazi, matatizo ya kupumua, na kisukari yanaweza kusababishwa au kuzidishwa na mfadhaiko unaoendelea.

      Van der Merwe anaandika hivi: “Kwa sababu ya kutokezwa kwa homoni inayoitwa cortisol mtu anapokuwa na mfadhaiko wa muda mrefu, mafuta hujikusanya tumboni na mgongoni.” Matatizo ya ngozi kama vile ukurutu na kubambuka kwa ngozi yanasababishwa au kuzidishwa na mfadhaiko. Mfadhaiko mkali umehusianishwa pia na kushuka moyo, mtu kuwa mkali sana, na uchovu wa kupindukia. Kumbukumbu na pia uwezo wa kukaza fikira unaweza kuathiriwa sana na mfadhaiko unaoendelea. Mfumo wa kinga wa mtu aliye na mfadhaiko wa muda mrefu unaweza kuathiriwa sana hivi kwamba anaweza kupatwa kwa urahisi na mafua na hata kansa na magonjwa yanayotokea kwa sababu ya mfumo wake wa kinga kushambulia chembe fulani za mwili.

      Kwa kuwa mfadhaiko ni tisho kubwa kwa afya yetu ya kiakili, kimwili, kihisia, na kiroho, tunahitaji kujua jinsi tunavyoweza kuudhibiti. Hata hivyo, hatutaki kuondoa kabisa uwezo wa mwili wetu wa kukabiliana na mfadhaiko. Kwa nini?

      Tunaweza kulinganisha mfadhaiko na farasi aliye na msisimuko. Farasi huyo anapotubeba, tunaweza kufurahia safari na kusisimka. Hata hivyo, farasi huyo akienda mbio bila kudhibitiwa, anaweza kuhatarisha uhai wetu. Vivyo hivyo, kuwa na mkazo fulani mwilini mwetu kunaweza kufanya maisha yafurahishe na kusisimua, na kutuchochea tuwe wabunifu, tufanye kazi kwa bidii, tuwe wachangamfu, na wenye afya.

      Hata hivyo, tunaweza kudhibiti mfadhaiko kwa njia gani ili tufurahie maisha? Habari inayofuata inazungumzia njia zinazofaa za kudhibiti mfadhaiko na jinsi ambavyo tunatenda tunapofadhaika.

      [Sanduku katika ukurasa wa 5]

      ‘TUMEUMBWA KWA NJIA YA AJABU’ NA MUUMBA MWENYE UPENDO NA HEKIMA

      Jinsi miili yetu inavyokabiliana na mfadhaiko si jambo tulilorithi kutoka kwa watu wa kale kama watu wengine wanavyodhania. Badala yake, mifumo tata ya mwili wetu imeundwa kwa ustadi na Muumba mwenye hekima. Kwa mfano, uwezo wa damu kuganda ambao huuwezesha mwili kujikinga dhidi ya maambukizo na kuponesha vidonda, na pia uwezo wa mwili kukabiliana na mfadhaiko ni uthibitisho wa kwamba miili yetu iliumbwa na Mbuni mwenye hekima na upendo.

      Mifumo hiyo ya mwili inathibitisha kwamba ‘tumeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.’ (Zaburi 139:13-16) Maandalizi ya kiroho na ya kimwili ambayo Mungu anatoa kwa upendo, na pia jinsi alivyowaumba wanadamu kwa njia ya ajabu ili wafurahie maisha, inatuhakikishia kwamba hakutakuwa na maumivu, maombolezo, au kifo katika Paradiso duniani.—Ufunuo 21:3-5.

      [Mchoro/Picha katika ukurasa wa 5]

      (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

      MADHARA YA MFADHAIKO WA MUDA MREFU

      Maumivu ya kichwa

      Kusaga meno

      Maumivu ya shingo

      Ugonjwa wa moyo

      Vidonda vya tumbo

      Maumivu ya mgongo

      Mshtuko wa ghafula wa misuli

  • Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko
    Amkeni!—2010 | Juni
    • Jinsi ya Kudhibiti Mfadhaiko

      Biblia inazungumza kuhusu “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Bila shaka, utakubali kwamba leo tunaishi katika nyakati zilizo na mfadhaiko mkubwa.—2 Timotheo 3:1.

      KAMA unavyojua, ni rahisi kuzima moto mdogo kuliko moto mkubwa. Vivyo hivyo, ni rahisi kudhibiti mfadhaiko mdogo mara tu unapotokea kuliko kudhibiti mfadhaiko mkubwa ambao umekuwapo kwa muda mrefu. Daktari mmoja alisema kwamba “licha ya maisha yetu yenye shughuli nyingi, ni muhimu tuwe na zoea la kupunguza mfadhaiko kila siku.”a

      Kuna faida mbili za kuwa na zoea la kupunguza mfadhaiko kila siku. Kwanza, hilo litasaidia kupunguza mambo yanayosababisha mfadhaiko maishani. Na pili, litasaidia kudhibiti jinsi tunavyotenda tunapopata mfadhaiko usioweza kuepukwa.

      Je, Biblia inatoa mwongozo ambao unaweza kutusaidia kukabiliana na mfadhaiko?

      Kweli za Biblia Ni Muhimu

      Kwa kufyonza kweli zilizo katika Biblia, tunaweza kupata mawazo ya Muumba wetu yenye kuburudisha na kuridhisha. Neno la Mungu ni chanzo cha mwongozo wenye thamani. Kwa kweli, Biblia ina kweli nyingi za kiroho zinazoweza kutupa kitulizo kutokana na mfadhaiko! Kweli hizo zinaweza kutusaidia ‘tusitetemeke wala kuwa na hofu’ na tufanikiwe kukabiliana na mfadhaiko kila siku.—Yoshua 1:7-9.

      Biblia inatusaidia kupunguza mfadhaiko kwa njia yenye kupendeza kwa kutuhakikishia kwamba Baba yetu wa kimbingu, Yehova, “ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) “Jambo moja ambalo limenisaidia sana,” anasema Patricia, aliyekuwa profesa katika chuo kikuu kimoja huko California, “ni kufikiria kuhusu mapenzi ya Mungu na mambo ya ajabu anayotimiza.”

      Fikiria jinsi matendo na maneno ya Yesu Kristo yenye fadhili yalivyowaburudisha wasikilizaji wake waliokuwa wamekandamizwa na kufadhaika. Alisihi hivi: “Njoni kwangu nyinyi nyote mnaofanyishwa kazi kupita kiasi na kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha [yaani, nitawaburudisha kiroho].”—Mathayo 11:28-30, The New Testament—An Understandable Version; mabano ni yao.

      Kwa kweli, Yesu hakuwa mkali. Badala yake, alifikiria mahitaji ya kihisia na ya kimwili ya wanafunzi wake, hata akafanya mipango ili waweze kupumzika kutokana na shughuli zao nyingi za kuhubiri. (Marko 6:30-32) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu, ambaye sasa ni Mfalme mbinguni anaelewa hisia zetu tunapopatwa na mfadhaiko wenye kulemea. Kwa rehema, yeye anatusaidia kwa kutupa “msaada kwa wakati unaofaa.”—Waebrania 2:17, 18; 4:16.

      Umuhimu wa Mawasiliano Mazuri

      Mawasiliano mazuri ni mojawapo ya njia zenye matokeo za kudhibiti mfadhaiko. Biblia inafundisha: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” (Methali 15:22) Kwa hiyo, watu wengi wamegundua kwamba kuzungumza na mwenzi wao wa ndoa, rafiki, au mfanyakazi mwenzao husaidia sana kupunguza mfadhaiko.

      Njia muhimu sana na yenye kufaa ya kuwa na “mazungumzo ya siri” ni kusali kwa Mungu. Kusali kwa ukawaida kunaweza kukusaidia ‘usihangaike juu ya kitu chochote.’ Wengi wameona kwamba kutegemea sala kumewasaidia kupata “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” Na kulingana na ahadi ya Biblia, ‘mioyo na nguvu zao za kufikiri’ hulindwa.—Wafilipi 4:6, 7; Methali 14:30.

      Kitabu kimoja kuhusu mfadhaiko kinasema kwamba “watu walio na marafiki wa kuwategemeza hukabiliana vizuri zaidi na mfadhaiko na wana afya nzuri ya akili kuliko wale wanaojaribu kufanya kila kitu bila kuhusisha wengine.” Marafiki bora zaidi wanaoweza kututegemeza ni wale wanaomwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Kwa kutii agizo la Biblia, wao hukutanika pamoja kwa ukawaida na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Mtu mmoja ambaye huhudhuria mikutano hiyo alisema hivi: “Nyakati nyingine mimi hufanya kazi kwa saa nyingi, na ninapatwa na mfadhaiko mkubwa. Hata hivyo, ninapoenda kwenye mikutano, kufikia wakati wa sala ya mwisho, mfadhaiko wangu huwa umekwisha nami huhisi nimeburudishwa.”

      Jambo lingine muhimu ambalo halipaswi kupuuzwa tunapokabiliana na mfadhaiko ni ucheshi. Mhubiri 3:4 inasema kwamba kuna “wakati wa kulia na wakati wa kucheka.” Kucheka huburudisha na pia hutokeza manufaa za kiafya kwa kuwa kama daktari mmoja alivyoeleza, “tunapocheka, mwili hutokeza kemikali inayoitwa endorphin na kuzuia kutokezwa kwa adrenalini.” Mwanamke mmoja aliyeolewa alisema hivi: “Tukiwa chini ya hali yenye mfadhaiko sana, mume wangu husema au kufanya jambo lenye kuchekesha na hilo husaidia sana.”

      Sifa Zinazopunguza Mfadhaiko

      Biblia inatutia moyo tukuze sifa zinazopunguza mfadhaiko. Sifa hizo ambazo zinaitwa “matunda ya roho” ya Mungu zinatia ndani “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, [na] kujizuia.” Pia Biblia inatuhimiza tuepuke “uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano.” Kisha inaongezea hivi: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”—Wagalatia 5:22, 23; Waefeso 4:31, 32.

      Daktari mmoja alieleza manufaa ya kufuata mafundisho hayo ya Biblia, hasa katika ulimwengu wa leo. Alisema: “Kuwatendea watu kwa heshima husaidia kupunguza mfadhaiko.” Biblia inatusaidia pia kuwa na kiasi, yaani, kujua mipaka ya uwezo wetu.—Mika 6:8.

      Mungu anatarajia tukubali kwa unyenyekevu mipaka ya uwezo wetu wa kimwili, kiakili, na kihisia na kwamba hatuwezi kufanya kila jambo tunalotaka kufanya. Huenda tukahitaji kujifunza wakati wa kukataa kufanya mambo yanayopita uwezo wetu hata ingawa ikawa vigumu kufanya hivyo.

      Hilo halimaanishi kwamba tukifuata mashauri yote yanayotegemea Biblia yaliyotolewa katika habari hii, hatutapatwa na mfadhaiko wowote. Ukweli wa mambo ni kwamba Shetani Ibilisi anawalenga wale wanaomwabudu Mungu ili kuthibitisha kwamba wataacha ibada ya kweli wakipatwa na mfadhaiko mwingi. (Ufunuo 12:17) Lakini, kama vile tumeona, Mungu hutoa msaada kwa wakati wake katika njia mbalimbali ili kutusaidia kupunguza na kukabiliana na mfadhaiko.b

      [Maelezo ya Chini]

      a Unapokabili mfadhaiko mkali au unaoendelea kwa muda mrefu, inapendekezwa umwone mtaalamu ili upate matibabu.

      b Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na mfadhaiko, tafadhali soma mfululizo wa makala “Kukabiliana na Mfadhaiko” katika toleo la Amkeni! la Februari 8, 2005 (8/2/2005), na “Kukabiliana na Hekaheka za Leo,” katika toleo la Februari 8, 2001.

      [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      NJIA FULANI ZA KUPUNGUZA MFADHAIKO

      ● Usitarajie ukamilifu kutoka kwako au kwa wengine.—Mhubiri 7:16.

      ● Panga mambo yanayofaa kutangulizwa.—Wafilipi 1:10, 11.

      ● Fanya mazoezi kwa ukawaida.—1 Timotheo 4:8.

      ● Furahia uumbaji wa Yehova.—Zaburi 92:4, 5.

      ● Tenga wakati wa kuwa peke yako mahali patulivu.—Mathayo 14:23.

      ● Pumzika na upate usingizi wa kutosha.—Mhubiri 4:6.

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Kuwasiliana ni muhimu ili kupunguza mfadhaiko

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Kusitawisha sifa za kimungu husaidia kupunguza mfadhaiko

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki