Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Mungu, Kwa Nini Uliruhusu Msiba Huu Utokee?’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 1
    • ‘Mungu, Kwa Nini Uliruhusu Msiba Huu Utokee?’

      RICARDO bado anakumbuka wakati alipoketi na mke wake Maria katika chumba cha wanaosubiri daktari.a Wote wawili hawakuwa na ujasiri wa kusoma matokeo ya uchunguzi wa kitiba ambao Maria alikuwa amefanyiwa karibuni. Baadaye, Ricardo alifungua bahasha iliyokuwa na ripoti ya daktari na wote wakaipitia haraka-haraka. Waliona neno “kansa,” kisha wakaanza kulia kwa kuwa walielewa kabisa kilichomaanishwa na neno hilo.

      Ricardo anasema hivi: “Daktari alikuwa mwenye fadhili sana, lakini yaonekana alielewa hiyo ilikuwa hali ngumu kwa sababu alituambia tena na tena kwamba tunapaswa kumtumaini Mungu.”

      Kabla ya Maria kuanza kutibiwa kwa kutumia mionzi, daktari wake aliona kwamba mguu wake wa kulia ulikuwa unatetemeka. Alipopimwa tena, iligunduliwa kwamba kansa hiyo ilikuwa imesambaa hadi kwenye ubongo wake. Baada ya juma moja tu, matibabu hayo ya mionzi yalisimamishwa. Maria alipoteza fahamu na akafa miezi miwili baadaye. “Nilifurahi kwamba mateso yake yalikoma,” aeleza Ricardo, “lakini nilimkosa sana hivi kwamba nilianza kutamani kufa pia. Mara kwa mara nilimlilia Mungu: ‘Kwa nini uliruhusu msiba huu utokee?’”

      Watu Huuliza Maswali Mengi Wanapopatwa na Msiba

      Kama Ricardo, watu wengi duniani hulazimika kukabiliana na hali ya kuteseka. Mara nyingi watu wasio na hatia ndio huteseka. Fikiria huzuni kubwa inayosababishwa na vita vya wanadamu visivyokoma. Au fikiria maumivu wanayopata watu ambao walibakwa, wakatendewa vibaya wakiwa watoto, wakatendewa kikatili nyumbani, na mambo mengine maovu. Inaonekana kwamba katika historia yote wanadamu wameendelea kutendeana mambo yasiyo ya haki na yenye kuumiza. (Mhubiri 4:1-3) Kuna wengine ambao wamekumbwa na misiba ya asili au magonjwa ya kihisia-moyo, kiakili, na kimwili. Si ajabu kwamba wengi huuliza, “Kwa nini Mungu huruhusu mateso hayo?”

      Si rahisi hata kwa wale walio na imani kukabiliana na kuteseka. Huenda hata wewe ukashangaa ni kwa sababu gani Mungu mwenye upendo na nguvu zote huruhusu wanadamu wateseke. Kupata jibu lenye kuridhisha na la kweli kwa swali hilo lenye kutatanisha ni muhimu ili tudumishe amani ya akili na uhusiano wetu pamoja na Mungu. Biblia hujibu swali hilo. Tafadhali chunguza vile inavyosema katika makala ifuatayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Majina yamebadilishwa.

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Daktari alituambia tena na tena kwamba tunapaswa kumtumaini Mungu

  • Faraja kwa Wanaoteseka
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 1
    • Faraja kwa Wanaoteseka

      KWA karne nyingi, wanafalsafa na wanatheolojia wengi wamekosa kuelewa ni kwa nini Mungu huruhusu wanadamu wateseke. Baadhi yao wamedai kwamba lazima Mungu awe ndiye husababisha kuteseka kwa kuwa yeye ni mwenye nguvu zote. Mwandikaji wa kitabu The Clementine Homilies, kichapo cha karne ya pili ambacho ukweli wake haujathibitishwa, alidai kwamba Mungu hutawala ulimwengu kwa mikono miwili. Kwa “mkono wake wa kushoto,” yaani, Ibilisi, yeye husababisha kuteseka na matatizo, na kwa “mkono wake wa kulia,” yaani, Yesu, yeye huokoa na kubariki.

      Wengine wameamua kutokubali kwamba kuna kuteseka kwa kuwa wanashindwa kuamini kwamba Mungu anaweza kuruhusu hali hiyo hata kama haisababishi. “Uovu ni hali ya kuwaziwa tu, si halisi,” akaandika Mary Baker Eddy. “Dhambi, ugonjwa, na kifo zingetoweka kama zingechukuliwa tu kuwa mambo yasiyo halisi.”—Science and Health With Key to the Scriptures.

      Kutokana na misiba ambayo imetokea katika historia, hasa tangu vita ya kwanza ya ulimwengu hadi leo, wengi wamefikia mkataa kwamba Mungu hawezi kuzuia kuteseka. Msomi mmoja Myahudi aitwaye David Wolf Silverman aliandika hivi: “Naona yale Maangamizi Makubwa yameondolea mbali maoni kwamba Mungu ni mwenye nguvu zote.” Aliongeza kusema, ‘Iwapo Mungu ataeleweka, basi ni lazima wema wake upatane na kuwepo kwa uovu, na hilo linawezekana tu ikiwa Yeye si mwenye nguvu zote.’

      Lakini, madai kwamba Mungu huunga mkono kuteseka kwa njia fulani, kwamba hawezi kuzuia hali hiyo, au kwamba kuteseka ni jambo la kuwaziwa tu, hayafariji wanaoteseka. Na jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba maoni hayo hayapatani kabisa na Biblia inayomfafanua Mungu kuwa mwenye haki, mwenye nguvu, na mwenye kujali. (Ayubu 34:10, 12; Yeremia 32:17; 1 Yohana 4:8) Hivyo basi, Biblia inasema ni kwa nini kuteseka kumeruhusiwa?

      Kuteseka Kulianzaje?

      Mungu hakuwaumba wanadamu wateseke. Badala yake, aliwapa wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, akili na miili mikamilifu, akawatayarishia shamba lenye kupendeza liwe makao yao, na akawapa kazi muhimu na yenye kuridhisha. (Mwanzo 1:27, 28, 31; 2:8) Hata hivyo, wangeendelea kuwa wenye furaha tu iwapo wangetambua utawala wa Mungu na kwamba ana haki ya kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya. Amri hiyo ya Mungu iliwakilishwa na mti ulioitwa “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwanzo 2:17) Adamu na Hawa wangeonyesha ujitiisho wao kwa Mungu kama wangalitii amri yake ya kutokula matunda ya mti huo.a

      Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa walishindwa kumtii Mungu. Kiumbe wa roho aliyeasi ambaye baadaye alitambuliwa kuwa Shetani Ibilisi, alifanya Hawa aamini kwamba hangenufaika kwa kumtii Mungu. Ni kana kwamba Mungu alikuwa anamnyima kitu kinachotamanika sana: uhuru, yaani, haki ya kujiamulia yaliyo mema na yaliyo mabaya. Shetani alidai kwamba kama Hawa angekula matunda ya mti huo, ‘macho yake yangefumbuliwa, naye angekuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ (Mwanzo 3:1-6; Ufunuo 12:9) Hawa alishawishiwa na taraja la kuwa huru, hivyo akala katika matunda ya mti uliokatazwa, naye Adamu akala pia.

      Siku hiyohiyo, Adamu na Hawa walianza kupatwa na matokeo ya uasi wao. Walipokataa utawala wa Mungu, walikosa ulinzi na baraka ambazo zilitokana na kujitiisha kwa Mungu. Mungu aliwafukuza katika Paradiso naye akamwambia Adamu hivi: “Ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako. Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi.” (Mwanzo 3:17, 19) Adamu na Hawa walianza kupatwa na magonjwa, maumivu, uzee, na kifo. Hivyo wanadamu wakaanza kuteseka.—Mwanzo 5:29.

      Kujibu Suala

      Huenda mtu akauliza, ‘Si Mungu angeipuuza tu dhambi ya Adamu na Hawa?’ La, hangefanya hivyo, kwa kuwa jambo hilo lingezidi kuivunjia mamlaka yake heshima na huenda baadaye lingechochea maasi na kuteseka zaidi. (Mhubiri 8:11) Zaidi ya hayo, Mungu angekuwa anaunga mkono kosa kwa kuachilia dhambi hiyo ya kutotii. Mwandikaji wa Biblia Musa anatukumbusha hivi: ‘Kazi ya Mungu ni kamilifu; maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki na adili.’ (Kumbukumbu la Torati 32:4) Ili atende kulingana na viwango vyake, ilimbidi Mungu awaruhusu Adamu na Hawa wapatwe na matokeo ya dhambi yao ya kutotii.

      Kwa nini Mungu hakuwaharibu mara moja wenzi hao wawili wa kwanza pamoja na Shetani, mchochezi asiyeonekana wa uasi huo? Alikuwa na uwezo wa kufanya hivyo na kama angalifanya hivyo, Adamu na Hawa hawangalizaa watoto waliorithi kuteseka na kifo. Hata hivyo, wonyesho huo wa nguvu zake haungalithibitisha kwamba Mungu ana haki ya kutawala viumbe wake wenye akili—wanadamu na malaika. Isitoshe, kama Adamu na Hawa wangalikufa bila kupata watoto, hiyo ingalimaanisha kushindwa kwa kusudi la Mungu la kuijaza dunia watoto wao wakamilifu. (Mwanzo 1:28) Naye “Mungu si mtu aseme uongo, . . . je, ataahidi kitu na asikifanye, au kusema kitu asikitimize?”—Hesabu 23:19, Biblia Habari Njema.

      Kupatana na hekima yake kamilifu, Yehova Mungu aliamua kuacha uasi huo uendelee kwa muda fulani. Waasi hao wangekuwa na fursa ya kutosha kujionea matokeo ya kujitawala bila kumtegemea Mungu. Historia ingethibitisha pasipo shaka yoyote kwamba mwanadamu anahitaji mwongozo wa Mungu na kwamba utawala wa Mungu ni bora kuliko wa wanadamu au wa Shetani. Wakati huohuo Mungu alichukua hatua ya kuhakikisha kwamba kusudi lake la awali kuhusu dunia lingetimizwa. Aliahidi kwamba “mbegu,” au “uzao” ungekuja ambao ‘ungemponda Shetani kichwa,’ na kuondoa kabisa uasi pamoja na madhara yake.—Mwanzo 3:15.

      Yesu Kristo ndiye Mbegu hiyo iliyoahidiwa. Kwenye 1 Yohana 3:8, tunasoma kwamba “Mwana wa Mungu alifanywa dhahiri, . . . ili avunje-vunje kazi za Ibilisi.” Alifanya hivyo kwa kudhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu na kulipa fidia iliyohitajiwa ili kukomboa watoto wa Adamu kutoka kwa dhambi na kifo walichorithi. (Yohana 1:29; 1 Timotheo 2:5, 6) Wale wanaoonyesha imani ya kweli katika dhabihu ya Yesu wanaahidiwa kwamba kuteseka kutaondolewa kabisa. (Yohana 3:16; Ufunuo 7:17) Wakati gani?

      Mwisho wa Kuteseka

      Kukataa mamlaka ya Mungu kumesababisha mateso mengi sana. Kwa hiyo inafaa Mungu atumie mamlaka yake kwa njia ya pekee ili kukomesha kuteseka na kutimiza kusudi lake la awali kuhusu dunia. Yesu alitaja mpango huo wa Mungu alipowafunza wafuasi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye katika mbingu, . . . acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.

      Muda ambao Mungu ameruhusu wanadamu wajitawale umekaribia kwisha. Kupatana na unabii wa Biblia, Ufalme wake ulisimamishwa mbinguni mwaka wa 1914 Yesu Kristo akiwa Mfalme.b Hivi karibuni, Ufalme huo utavunja-vunja na kukomesha serikali zote za wanadamu.—Danieli 2:44.

      Wakati wa huduma yake fupi duniani, Yesu alionyesha kimbele baraka ambazo wanadamu watapata baada ya utawala wa Mungu kurudishwa. Vitabu vya Injili vinathibitisha kwamba Yesu aliwahurumia watu waliokuwa maskini na waliobaguliwa. Aliponya wagonjwa, akalisha wenye njaa, na kufufua wafu. Hata nguvu za asili zilimtii. (Mathayo 11:5; Marko 4:37-39; Luka 9:11-16) Hebu wazia mambo ambayo Yesu atatimiza atakapotumia dhabihu yake ya fidia yenye kutakasa ili kuwanufaisha wanadamu wote watiifu! Biblia inaahidi kwamba kupitia utawala wa Kristo, Mungu “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho [ya wanadamu], na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.”—Ufunuo 21:4.

      Faraja kwa Wale Wanaoteseka

      Inatia moyo kama nini kujua kwamba Yehova, Mungu wetu mwenye upendo na nguvu zote, anatujali na kwamba karibuni atawaletea wanadamu kitulizo! Kwa kawaida, mtu aliye mgonjwa sana hukubali bila kusita matibabu ambayo yatamponya hata yawe yenye uchungu sana. Vivyo hivyo, iwapo tunajua kwamba njia ya Mungu ya kushughulikia mambo italeta baraka za milele, ujuzi huo unaweza kututegemeza hata tukipatwa na matatizo ya muda.

      Ricardo aliyetajwa katika makala iliyotangulia, hufarijiwa na ahadi za Biblia. “Baada ya mke wangu kufa, nilitaka sana kujitenga, lakini upesi nikatambua kwamba mke wangu hangefufuka kwa kufanya hivyo bali hali ingekuwa mbaya hata zaidi,” akasema. Badala ya kujitenga, Ricardo aliendelea kuhudhuria mikutano ya Kikristo kama kawaida na kuhubiria wengine ujumbe wa Biblia. “Nilipohisi utegemezo wa Yehova wenye upendo na kuona jinsi alivyojibu sala zangu kuhusu mambo niliyoyaona kuwa madogo, nilimkaribia zaidi,” Ricardo anasema. “Kujua kwamba Mungu ananipenda kuliniwezesha kuvumilia jaribu baya zaidi lililowahi kunipata.” Ricardo anakiri hivi: “Bado ninamkosa mke wangu sana, lakini sasa ninaamini kabisa kwamba hakuna chochote ambacho Yehova huruhusu kitokee kinachoweza kuwa na madhara ya kudumu.”

      Je, wewe kama Ricardo unatamani wakati ambapo kuteseka kwa wanadamu ‘hakutakumbukwa, wala kuingia moyoni’? (Isaya 65:17) Uwe na hakika kwamba unaweza kupata baraka za Ufalme wa Mungu ukifuata ushauri huu wa Biblia: “Mtafuteni BWANA, maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu.”—Isaya 55:6.

      Ili upate msaada wa kufanya hivyo, zingatia sana kusoma na kujifunza kwa makini Neno la Mungu maishani mwako. Pata kumjua Mungu na yule aliyemtuma, Yesu Kristo. Jitahidi kuishi kupatana na viwango vya Mungu na hivyo kuonyesha kwamba uko tayari kujitiisha kwa utawala wake. Kufanya hivyo kutakuletea furaha nyingi sasa licha ya majaribu ambayo huenda yakakupata. Na wakati ujao, utaweza kufurahia maisha katika ulimwengu ambamo wanadamu hawatateseka.—Yohana 17:3.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kielezi-chini kwenye Mwanzo 2:17 katika tafsiri ya The Jerusalem Bible kinaeleza “ujuzi wa mema na mabaya” kuwa “uwezo wa kuamua . . . yaliyo mema na yaliyo mabaya kisha kutenda kulingana na uamuzi huo, yaani, dai la kuwa huru kabisa kujiamulia yaliyo mema na yaliyo mabaya na hivyo kukataa kutambua kwamba uliumbwa.” Kinaongeza kusema: “Dhambi ya kwanza ilikuwa ni shambulio dhidi ya haki ya Mungu ya kutawala.”

      b Ili kupata maelezo zaidi juu ya unabii wa Biblia kuhusu mwaka wa 1914, ona sura ya 10 na 11 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki