Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutumia Biblia Kujibu Maswali
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 18

      Kutumia Biblia Kujibu Maswali

      Unahitaji kufanya nini?

      Unahitaji kutumia vizuri Biblia kujibu maswali kuliko kutumia maoni yako.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Tumeagizwa ‘kuhubiri neno.’ Yesu alituwekea mfano, akisema: “Sisemi kwa ubuni wangu mwenyewe.”—2 Tim. 4:2; Yn. 14:10.

      TUNAPOULIZWA maswali yanayohusu imani yetu, maisha yetu, maoni yetu juu ya matukio ya nyakati zetu, na tumaini letu la wakati ujao, sisi hujitahidi kutumia Biblia kujibu. Kwa nini? Kwa sababu Biblia ni Neno la Mungu. Imani yetu inategemea Biblia. Maisha yetu yanategemea Biblia. Maoni yetu kuhusu matukio ya ulimwengu yanategemea Biblia. Tumaini letu la wakati ujao linategemea kabisa ahadi za Biblia zilizopuliziwa.—2 Tim. 3:16, 17.

      Tunafahamu sana uzito wa jina letu. Sisi ni Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:12) Kwa hiyo, tunapojibu maswali, tunayajibu kulingana na maoni ya Yehova tunayopata katika Neno lake lililopuliziwa wala hatujibu kulingana na falsafa za wanadamu. Ingawa ni kweli kwamba kila mmoja wetu ana maoni yake kuhusu mambo mbalimbali, sisi huacha Neno la Mungu lirekebishe maoni yetu kwa sababu tunasadiki kabisa kwamba Neno hilo ndilo kweli. Bila shaka, Biblia inaturuhusu kuwa na maoni tofauti-tofauti katika masuala mengi. Badala ya kushurutisha wengine wafuate maoni yetu, sisi tunapenda kufundisha watu kanuni za Maandiko, na hivyo tunawaruhusu wawe na uhuru wa kuchagua kama sisi. Kama mtume Paulo, sisi hujaribu “kukuza utii kwa njia ya imani.”—Rom. 16:26.

      Andiko la Ufunuo 3:14 linasema kwamba Yesu Kristo ni “shahidi mwaminifu na wa kweli.” Alijibu maswali na kukabiliana na hali kwa njia gani? Nyakati nyingine alitumia mifano iliyofanya watu wafikiri. Nyakati nyingine aliuliza yule mwenye kuuliza swali jinsi anavyofahamu andiko fulani. Mara nyingi alinukuu maandiko, alitaja jinsi maandiko yanavyosema, au aliyarejelea. (Mt. 4:3-10; 12:1-8; Luka 10:25-28; 17:32) Katika karne ya kwanza, kwa kawaida vitabu vya kukunjwa vya Maandiko vilihifadhiwa katika masinagogi. Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Yesu alikuwa na vitabu vyake mwenyewe vya kukunjwa, lakini alijua sana Maandiko na aliyarejelea mara nyingi alipokuwa akifundisha wengine. (Luka 24:27, 44-47) Kwa kweli angeweza kusema kwamba yale aliyofundisha hayakutokana na ubuni wake. Alisema mambo aliyosikia kutoka kwa Baba yake.—Yn. 8:26.

      Tunataka kuiga mfano wa Yesu. Hakuna mmoja wetu ambaye amewahi kumsikia Mungu akisema, kama alivyomsikia Yesu. Lakini Biblia ni Neno la Mungu. Tukiitumia kujibu maswali, tunaepuka kujielekezea fikira. Tunaonyesha tumeazimia kabisa kufuata maoni ya Mungu kuhusu kweli badala ya kutoa maoni ya wanadamu wasiokamilika.—Yn. 7:18; Rom. 3:4.

      Bila shaka, tamaa yetu si kutumia tu Biblia bali ni kuitumia kwa njia inayomfaidi zaidi msikilizaji. Tunataka asikilize bila kuwa na maoni yenye ubaguzi. Kwa kutegemea maoni yake, unaweza kutaja mambo yanayotokana na Biblia kwa kusema: “Je, hukubali kwamba maneno ya Mungu ndiyo muhimu zaidi?” Au unaweza kusema: “Je, unajua kwamba Biblia inazungumzia swali hili hasa?” Ikiwa unazungumza na mtu ambaye haamini Biblia, unaweza kutumia utangulizi tofauti kidogo. Unaweza kusema: “Ebu nikueleze unabii huu wa kale.” Au unaweza kusema: “Kitabu ambacho kimeenezwa zaidi katika historia kinasema hivi . . . ”

      Nyakati nyingine, unaweza kutaja tu jinsi andiko fulani linavyosema. Lakini, ikiwezekana ni afadhali zaidi kufungua Biblia na kuisoma. Mwonyeshe mtu huyo andiko hilo katika Biblia yake hali ikiruhusu. Kutumia Biblia moja kwa moja kwa njia hiyo mara nyingi hugusa sana mioyo ya watu.—Ebr. 4:12.

      Wazee Wakristo wana wajibu wa kipekee wa kutumia Biblia wanapojibu maswali. Mojawapo ya sifa za kumstahilisha mtu awe mzee ni “kushika kwa imara lile neno la uaminifu kwa habari ya usanifu wa kufundisha kwake.” (Tito 1:9) Mshiriki wa kutaniko anaweza kufanya maamuzi mazito maishani baada ya kushauriwa na mzee. Ni muhimu shauri litegemee Maandiko. Mfano ambao mzee anaweka unaweza kuwa na uvutano sana juu ya jinsi wengine wanavyofundisha.

      JINSI YA KUFAULU

      • Soma Biblia kila siku. Uwe na programu nzuri ya kujifunza kibinafsi.

      • Uwe na zoea la kutaja maandiko unapotoa maelezo katika mikutano ya kutaniko.

      • Unapokabili maswali au hali mbalimbali, kabla ya kujibu au kufanya maamuzi, siku zote jiulize, ‘Biblia inasema nini?’

      • Ikiwa hujui Biblia inasema nini juu ya jambo fulani, usijaribu kukisia-kisia au kutoa maoni yako mwenyewe. Fanya utafiti.

      MAZOEZI: Orodhesha swali moja au maswali mawili ambayo umeulizwa (1) katika utumishi wa shambani, (2) juu ya jambo fulani ambalo limesemwa katika habari hivi karibuni, na (3) juu ya kushiriki katika utendaji fulani ambao watu wanapenda sana. Chagua angalau andiko moja linalofaa ambalo utatumia kujibu kila mojawapo ya maswali hayo.

  • Kuwasaidia Wasikilizaji Kutumia Biblia
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 19

      Kuwasaidia Wasikilizaji Kutumia Biblia

      Unahitaji kufanya nini?

      Unahitaji kuwasaidia wasikilizaji wafuatane na wewe unaposoma maandiko ya Biblia.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Jambo ambalo mtu anaona kwa macho yake, hasa katika Biblia yake mwenyewe, humgusa moyo zaidi.

      KUSUDI letu ni kuelekeza fikira za kila mtu kwenye Neno la Mungu, Biblia. Kitabu hicho kitakatifu ndicho msingi wa ujumbe tunaohubiri, na tunataka watu watambue kwamba yale tunayosema yanatokana na Mungu wala hatusemi mambo yetu wenyewe. Watu wanahitaji kuitumaini Biblia.

      Katika Huduma ya Shambani. Unapojitayarisha kwa ajili ya huduma ya shambani, sikuzote chagua andiko moja au zaidi ambalo utawaonyesha wale walio tayari kusikiliza. Hata kama unapanga kutoa kichapo fulani cha Biblia kwa muda mfupi tu, kwa kawaida ni vizuri kusoma andiko linalofaa la Biblia. Biblia ina uwezo mkubwa wa kuelekeza wenye mfano wa kondoo kuliko jambo jingine lolote ambalo tunaweza kusema. Ikiwa hali hazikuruhusu kusoma Biblia, unaweza kuinukuu. Katika karne ya kwanza, vitabu vya kukunjwa vya Maandiko havikupatikana sana. Hata hivyo, Yesu na mitume wake walinukuu sana Maandiko. Hata sisi tunapaswa kujitahidi kushika Maandiko na kuyatumia vizuri katika huduma yetu, nyakati nyingine tukiyanukuu tu.

      Ikiwa hali zinakuruhusu kusoma Biblia, uishike vizuri ili mwenye nyumba aweze kufuatana nawe unaposoma. Ikiwa mwenye nyumba anafuatana nawe akisoma Biblia yake mwenyewe, yale anayosoma yanaweza kumfanya aitikie kwa njia nzuri zaidi.

      Hata hivyo, ni lazima utambue kwamba baadhi ya watafsiri wa Biblia wamebadili Neno la Mungu. Huenda tafsiri zao hazipatani kwa kila hali na mambo yaliyokuwa katika lugha za awali za Biblia. Tafsiri kadhaa za kisasa zimeondoa jina la Mungu, hazisemi wazi kile ambacho maandishi ya lugha za awali yalisema kuhusu wafu, na zinaficha mafundisho ya Biblia kuhusu kusudi la Mungu kwa dunia. Ili kuonyesha mtu badiliko ambalo limefanywa, mnaweza kuchunguza maandiko hayo katika Biblia tofauti-tofauti au kuchunguza tafsiri za awali za Biblia za lugha iyo hiyo. Kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinalinganisha jinsi tafsiri kadhaa zinavyotafsiri maneno makuu ya maandiko ambayo hutumiwa mara nyingi. Mtu yeyote anayependa kweli atafurahi kujua mambo hayo.

      Katika Mikutano ya Kutaniko. Wote wasaidiwe kutumia Biblia katika mikutano ya kutaniko. Kuna faida nyingi za kufanya hivyo. Kunawasaidia wasikilizaji wakazie fikira mambo yanayozungumzwa. Kunakazia maneno ya msemaji kwa sababu wasikilizaji wenyewe wanayasoma maneno hayo. Na kufanya hivyo kunawasadikisha wale wanaopendezwa kwamba kwa kweli Biblia ndiyo msingi wa imani yetu.

      Wasikilizaji watafuatana nawe unaposoma Maandiko katika Biblia ikiwa tu utawasaidia kufanya hivyo. Mojawapo ya njia bora ya kuwatia moyo kutumia Biblia ni kuwaomba wafuatane nawe unaposoma andiko fulani.

      Ni daraka la msemaji kuamua maandiko anayotaka kukazia anapowaomba wasikilizaji wafuatane naye. Inafaa kusoma maandiko yanayokusaidia kufafanua mambo makuu. Kisha kadiri wakati unavyoruhusu, ongezea maandiko mengine machache yanayotegemeza jambo unalozungumzia.

      Kwa kawaida, haitoshi tu kutaja andiko fulani wala haitoshi kuwaomba wasikilizaji wafuatane nawe unapolisoma. Ukisoma andiko moja kisha usome jingine mbiombio hata kabla ya wasikilizaji kupata wakati wa kufungua lile la kwanza, upesi watachoka na wataacha kujaribu kufuatana nawe unaposoma Biblia. Uwe na utambuzi. Soma andiko wakati wengi wamelipata.

      Fikiria kimbele. Taja vizuri andiko hilo mapema kabla ya kulisoma. Jambo hilo litapunguza wakati unaopotea unapongojea wasikilizaji wafungue Biblia zao. Ingawa hutaweza kuzungumzia mambo mengi sana ukiwapa wasikilizaji wakati wa kufungua Biblia, utawafaidi sana.

      JINSI YA KUFAULU

      • Onyesha mwenye nyumba andiko unalosoma katika Biblia, au umwombe atumie Biblia yake kufuatana nawe unaposoma.

      • Unapotoa hotuba kutanikoni, waombe wasikilizaji wafungue maandiko makuu, kisha uwape nafasi ya kufungua Biblia.

      MAZOEZI: Katika ziara za kurudia, jaribu kutumia njia zinazofuata: (1) Mpe mwenye nyumba Biblia yako, mwulize kama angependa kusoma andiko ambalo umechagua. (2) Mwulize kama angependa kuleta Biblia yake mwenyewe na kusoma andiko fulani kuu.

  • Kutoa Utangulizi Mzuri wa Maandiko
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 20

      Kutoa Utangulizi Mzuri wa Maandiko

      Unahitaji kufanya nini?

      Tayarisha akili za wasikilizaji kabla ya kusoma andiko.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Kutoa utangulizi mzuri wa andiko kunaweza kuwasaidia wasikilizaji kuelewa vizuri maana yake.

      MAANDIKO ndiyo msingi wa mafundisho yetu katika mikutano ya kutaniko. Pia, maandiko ya Biblia ndiyo msingi wa mahubiri yetu katika huduma ya shambani. Lakini, mafanikio yetu ya kutumia maandiko katika mazungumzo yanategemea kwa kiasi fulani utangulizi tunaotoa kabla ya kuyasoma.

      Usirejelee tu andiko na kumwomba mtu afuatane nawe unapolisoma. Unapotaka kutaja andiko, jaribu kutimiza mambo haya mawili: (1) Chochea hamu ya kusoma andiko hilo, na (2) onyesha kusudi la kulisoma. Kuna njia mbalimbali za kutimiza mambo hayo mawili.

      Uliza Swali. Njia hii ni bora ikiwa wasikilizaji bado hawajui vizuri jibu la swali unalouliza. Jaribu kuuliza swali kwa njia inayofanya watu wafikiri. Yesu alifanya hivyo. Mafarisayo walipomwendea hekaluni na kujaribu hadharani ujuzi wake wa Maandiko, Yesu aliwauliza: “Nyinyi mwafikiri nini juu ya Kristo? Yeye ni mwana wa nani?” Wakamjibu: “Wa Daudi.” Yesu akawauliza: “Basi, ni jinsi gani, kwamba Daudi kwa upulizio amwita yeye ‘Bwana’?” Kisha akanukuu Zaburi 110:1. Mafarisayo wakanyamazishwa. Lakini, umati ukamsikiliza Yesu kwa furaha.—Mt. 22:41-46.

      Unaweza kutumia maswali kama haya kwenye utangulizi wako katika utumishi wa shambani: “Mimi nina jina na wewe una jina. Je, Mungu pia ana jina? Ebu tupate jibu katika Zaburi 83:18.” “Je, kweli itawezekana kuwe na serikali moja inayotawala wanadamu wote? Ebu ona jinsi Danieli 2:44 linavyojibu.” “Je, kweli Biblia inazungumzia hali za siku zetu? Ebu linganisha hali unazoona leo na hali zinazotajwa katika 2 Timotheo 3:1-5.” “Je, kweli kuna wakati ambapo kifo na kuteseka hakutakuwapo tena? Biblia inajibu swali hilo katika Ufunuo 21:4, 5.”

      Kutumia maswali vizuri katika hotuba ili kutoa utangulizi mzuri wa maandiko kunaweza kuchochea wasikilizaji kuona maandiko kwa njia tofauti, hata kama ni maandiko wanayofahamu vizuri. Lakini, watafanya hivyo ikiwa tu maswali unayouliza kwa kweli yanawahusu. Hata kama wasikilizaji wanapendezwa na habari unayozungumza, akili zao zinaweza kutangatanga unaposoma maandiko ambayo wamesikia mara nyingi. Ili akili zao zisitangetange, fikiria sana jinsi ya kufanya hotuba yako ivutie.

      Taja Tatizo Fulani. Unaweza kutaja tatizo fulani kisha uonyeshe andiko linalotaja suluhisho. Usiwafanye wasikilizaji watarajie suluhisho kubwa kuliko lile watakalopata katika andiko. Mara nyingi andiko huonyesha suluhisho la kadiri fulani tu. Lakini unaposoma andiko, unaweza kuuliza wasikilizaji wafikirie mwongozo unaopatikana katika andiko hilo unaosaidia kukabili tatizo mnalozungumzia.

      Vilevile, unaweza kutaja kanuni fulani inayohusu mwenendo mzuri kisha utumie tukio fulani katika Biblia linaloonyesha hekima ya kufuata kanuni hiyo. Ikiwa andiko ambalo wasemaji wengine wanasoma lina mambo mawili hususa (au labda zaidi) ambayo yanahusiana na jambo wanalozungumzia, wao huwaomba wasikilizaji wawe makini kuyaona. Ikiwa inaonekana wasikilizaji fulani hawaelewi jambo unalozungumzia, unaweza kuchochea fikira zao kwa kutaja mambo yanayoweza kufanywa ili kulisuluhisha kisha utumie andiko kuonyesha suluhisho.

      Rejelea Biblia. Ikiwa tayari umeamsha upendezi wa wasikilizaji katika habari unayozungumzia na tayari umetaja jambo moja au mambo mawili kuihusu, unaweza kusema hivi kabla ya kusoma andiko: “Ona jinsi Neno la Mungu linavyosema kuhusu jambo hili.” Ukifanya hivyo unaonyesha kwamba jambo unalotaka kusoma linategemea Neno la Mungu.

      Yehova alitumia wanaume kama Luka, Paulo, Petro, na Yohana kuandika sehemu fulani za Biblia. Lakini wao ni waandishi tu; Yehova ndiye Mtungaji. Ikiwa unazungumza na watu ambao hawasomi Maandiko Matakatifu, huenda ikafaa zaidi kusema “Neno la Mungu” linasema kuliko kusema “Petro aliandika” au “Paulo alisema” kabla ya kusoma andiko. Ona kwamba nyakati nyingine Yehova alimwamuru Yeremia aseme maneno haya kabla ya kutangaza ujumbe wake: “Sikilizeni neno la BWANA.” (Yer. 7:2; 17:20; 19:3; 22:2) Iwe tunatumia jina la Yehova tunapotaka kusoma andiko au la, kabla ya kumalizia mazungumzo yetu, tujaribu kuonyesha kwamba yaliyomo katika Biblia ni neno lake.

      Fikiria Muktadha. Unapaswa kuelewa muktadha unapofikiria utakavyotoa utangulizi wa andiko. Nyakati nyingine unaweza kutaja muktadha, lakini kwa njia nyinginezo ni muktadha unaoweza kuamua maneno utakayotumia. Kwa mfano, je, unaweza kutoa utangulizi wa maneno ya Yobu aliyemcha Mungu kwa njia ile ambayo ungetoa utangulizi wa maneno ya mmojawapo wa wafariji wake bandia? Luka aliandika kitabu cha Matendo, lakini pia ananukuu Yakobo, Petro, Paulo, Filipo, Stefano, na malaika, na vilevile ananukuu Gamalieli na Wayahudi wengine ambao hawakuwa Wakristo. Utasema ni nani aliyesema maneno unayonukuu? Kwa mfano, kumbuka kwamba Daudi hakutunga zaburi zote wala Solomoni hakuandika kitabu chote cha Mithali. Pia ni vizuri kujua mwandishi wa Biblia anazungumza na nani na kwa ujumla anazungumza habari gani.

      Tumia Habari za Ziada. Hii ni njia bora ikiwa unaweza kuonyesha kwamba hali zinazohusu simulizi la Biblia unalosoma zinalingana na hali unazozungumzia. Nyakati nyingine unahitaji kutumia habari za ziada ili watu waelewe andiko fulani vizuri. Tuseme unataka kutumia andiko la Waebrania 9:12, 24 katika hotuba inayohusu fidia. Kabla ya kusoma andiko hilo unaweza kufafanua kifupi chumba cha ndani kabisa cha tabenakulo, ambacho maandiko yanaonyesha kinafananisha mahali ambapo Yesu aliingia alipoenda mbinguni. Lakini usitumie habari nyingi sana kiasi cha kufunika andiko ambalo unataka kusoma.

      Ili utoe utangulizi wa maandiko kwa njia bora, chunguza jinsi wasemaji wenye ujuzi wanavyofanya. Tazama njia tofauti-tofauti wanazotumia. Ona matokeo ya njia hizo. Unapotayarisha hotuba zako, tambua maandiko makuu na ufikirie kwa makini jambo unalotaka kutimiza unaposoma kila andiko. Panga kwa uangalifu jinsi ambavyo utatoa utangulizi wa kila andiko ili liwe na matokeo bora zaidi. Baadaye, fanya vivyo hivyo na maandiko yote unayotumia. Unapoendelea kuboresha sehemu hii katika hotuba zako, utakuwa ukielekeza fikira zaidi kwenye Neno la Mungu.

      JINSI YA KUFAULU

      • Unapochagua utangulizi wa maandiko ambao utaamsha upendezi wa wasikilizaji, kumbuka mambo ambayo tayari wasikilizaji wanafahamu na ufikirie jinsi wanavyoona habari hiyo.

      • Hakikisha unajua kusudi lako unaposoma kila andiko, na utangulizi wako wa maandiko hayo uonyeshe kusudi hilo.

      MAZOEZI: Chagua andiko ambalo unaona unaweza kutumia vizuri katika eneo lenu. Fikiria (1) swali au jambo linalotatiza ambalo utazungumzia ili kuamsha upendezi wa mwenye nyumba na (2) jinsi utakavyoonyesha kusudi lako la kusoma andiko unalopangia kusoma.

  • Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 21

      Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa

      Unahitaji kufanya nini?

      Kazia maneno makuu ya habari unayozungumzia. Soma kwa hisia inayofaa.

      Kwa Nini Ni Muhimu?

      Uzito wa maandiko yanayosomwa hudhihirishwa kwa mkazo unaofaa.

      UNAPOZUNGUMZA na wengine kuhusu mambo ambayo Mungu amekusudia, iwe unamhubiria mtu au unahutubu jukwaani, unapaswa kutegemea Neno la Mungu. Mara nyingi mazungumzo hayo hutia ndani kusoma Biblia, na tunapaswa kuisoma vizuri.

      Mkazo Unaofaa Unatia Ndani Hisia. Tusome maandiko kwa hisia. Ebu ona mifano michache. Unaposoma kwa sauti Zaburi 37:11, sauti yako inapasa kuonyesha furaha ya kutazamia amani ambayo imeahidiwa katika andiko hilo. Unaposoma Ufunuo 21:4 kuhusu mwisho wa kuteseka na kifo, sauti yako ionyeshe shukrani za moyoni kwa sababu ya faraja hiyo nzuri ajabu ambayo imetabiriwa hapo. Soma Ufunuo 18:2, 4, 5 kwa sauti ya dharura kwa sababu linatuhimiza tutoke kwenye “Babiloni Mkubwa” mwenye dhambi tele. Hisia tunayoonyesha itoke moyoni lakini isipite kiasi. Kadiri nzuri ya hisia inategemea andiko unalosoma na jinsi unavyolitumia.

      Kazia Maneno Yanayofaa. Kama unazungumzia sehemu fulani tu ya andiko, kazia sehemu hiyo unaposoma. Kwa mfano, ikiwa unataka kuelezea maana ya “kutafuta kwanza ufalme” unaposoma Mathayo 6:33, usikazie “uadilifu wake” wala “vitu vingine vyote.”

      Tuseme umepanga kusoma Mathayo 28:19 katika hotuba utakayotoa katika Mkutano wa Utumishi. Utakazia maneno gani? Ikiwa unataka kutia watu moyo wawe na bidii kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani, kazia ‘kufanya wanafunzi.’ Na kama unataka kuzungumzia daraka la Mkristo la kuwajulisha kweli za Biblia watu wa nchi za kigeni au kama unataka kuwatia moyo wahubiri wengine watumikie katika sehemu zenye uhitaji zaidi, unaweza kukazia “watu wa mataifa yote.”

      Mara nyingi tunasoma andiko kujibu swali au kuunga mkono jambo fulani ambalo wengine hubisha. Ikiwa unakazia kila wazo katika andiko hilo kwa kadiri ileile, wasikilizaji wanaweza kukosa kuelewa kusudi lako la kusoma andiko hilo. Wewe unaweza kufahamu wazi kusudi lako la kulisoma lakini huenda wao wasilifahamu.

      Kwa mfano, unaposoma Zaburi 83:18 katika Biblia ambayo ina jina la Mungu, mwenye nyumba anaweza kukosa kufahamu jambo linaloonekana kuwa wazi la kwamba Mungu ana jina ikiwa unakazia sana ile sehemu inayosema “Uliye juu.” Kazia jina “Yehova.” Lakini, unapotumia andiko hilo kuonyesha kwamba Yehova ni mwenye enzi kuu, kazia maneno “Uliye juu.” Vilevile unapotumia Yakobo 2:24 kuonyesha kwamba imani inapaswa kuonyeshwa kwa matendo, kukazia ‘kutangazwa kuwa mwadilifu’ badala ya kukazia “kazi” kunaweza kufanya wengine wasipate maana.

      Tunaweza kupata mfano mwingine mzuri katika Waroma 15:7-13. Hii ni sehemu ya barua ambayo mtume Paulo aliandikia kutaniko lenye mchanganyiko wa watu wa Mataifa na Wayahudi wa asili. Anasema hapo kwamba huduma ya Kristo haiwafaidi tu Wayahudi waliotahiriwa bali inawafaidi pia watu wa mataifa ili “mataifa yapate kumtukuza Mungu kwa ajili ya rehema yake.” Kisha ananukuu maandiko manne kuthibitisha jambo hilo. Unapaswa kusoma manukuu hayo kwa njia gani ili kukazia jambo ambalo Paulo alimaanisha? Ikiwa unatia alama maneno ya kukazia, unaweza kutia alama “mataifa” katika mstari wa 9, “nyinyi mataifa” katika mstari wa 10, “mataifa yote” na “vikundi vyote vya watu” katika mstari wa 11, na “mataifa” katika mstari wa 12. Ebu jaribu kusoma Waroma 15:7-13 kwa mkazo huo. Unapofanya hivyo, hoja ya Paulo itakuwa wazi na kueleweka kwa urahisi.

      Njia za Kutia Mkazo. Unaweza kutumia njia kadhaa kukazia maneno muhimu ambayo unataka yawe wazi. Njia unayotumia kutia mkazo ilingane na andiko unalosoma na muktadha wa hotuba yako. Hapa pana madokezo machache.

      Kutia mkazo kupitia sauti. Njia hii inahusisha kubadili sauti kwa njia yoyote inayofanya maneno yenye maana yawe wazi kuliko maneno mengine katika sentensi. Unaweza kutia mkazo kwa kuinua sauti au kuipunguza. Katika lugha nyingi, kuinua sauti kunaweza kuongeza mkazo. Lakini katika lugha nyinginezo, kuinua sauti kunaweza kubadili maana ya jambo unalosema. Ukipunguza mwendo wako na kuongea polepole unapofikia maneno makuu, maneno hayo hutokea kwa uzito zaidi. Katika lugha ambazo huwezi kukazia maneno fulani kwa kubadili sauti, unaweza kufuata desturi za kukazia maneno katika lugha hizo.

      Kutua kifupi. Unaweza kutua kifupi kabla ya kusoma sehemu kuu ya andiko au baada ya kuisoma, au kabla na baada ya kuisoma. Kutua kifupi kabla tu ya kusoma wazo kuu hufanya watu wawe na hamu ya kujua jambo linalofuata na kutua baada tu ya kulisoma hufanya jambo hilo lieleweke zaidi. Lakini ukitua-tua sana, hakuna jambo litakalokuwa wazi.

      Kurudia jambo kuu. Unaweza kukazia jambo fulani kwa kutua na kulisoma tena. Njia nzuri ya kutua inayotumiwa mara nyingi ni kumaliza kusoma andiko lote kisha urudie kusoma wazo kuu unalotaka kukazia.

      Ishara. Mara nyingi ishara za mwili na za uso zinaweza kuongezea hisia jambo unalosema.

      Hali ya sauti. Katika lugha fulani, nyakati nyingine maneno yanaweza kusomwa kwa sauti inayotokeza maana fulani na kuyatia mkazo. Pia unahitaji kutumia busara kuhusu jambo hili hasa unapotumia maneno ya dhihaka.

      Wengine Wanaposoma Maandiko. Mwenye nyumba anaposoma andiko, anaweza kukazia maneno yasiyostahili kukaziwa au labda asikazie neno lolote. Ufanye nini basi? Kwa ujumla ni vizuri ufafanue maana unapomwonyesha jinsi maandiko hayo yanavyotumika. Baada ya kufanya hivyo, unaweza kukazia hasa maneno yanayotokeza maana katika Biblia.

      KUJUA JINSI YA KUTUMIA MKAZO

      • Jiulize hivi kuhusu andiko lolote ambalo utasoma: ‘Maneno haya yanaonyesha hisia gani? Nionyeshe hisia hizo kwa njia gani?’

      • Chunguza maandiko unayopanga kutumia. Jiulize hivi kuhusu kila mojawapo ya maandiko hayo: ‘Andiko hili litatimiza kusudi gani? Nahitaji kukazia maneno gani kutimiza kusudi hilo?’

      MAZOEZI: (1) Chunguza andiko ambalo unataka kutumia katika utumishi wa shambani. Fanya mazoezi ya kulisoma kwa hisia inayofaa. Ukikumbuka jinsi unavyotaka kulitumia, lisome kwa sauti ukikazia neno au maneno yanayofaa. (2) Katika kichapo kinachotumiwa wakati huu kwenye funzo, chagua fungu moja ambalo lina manukuu ya maandiko. Chunguza jinsi ambavyo maandiko yametumiwa hapo. Tia alama maneno yanayotokeza maana. Soma fungu lote kwa sauti kwa njia inayokazia vizuri maandiko.

  • Kutumia Maandiko Vizuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • SOMO LA 22

      Kutumia Maandiko Vizuri

      Unahitaji kufanya nini?

      Hakikisha unatumia andiko kulingana na muktadha wake na kulingana na Biblia yote kwa ujumla. Pia tumia andiko kulingana na maelezo ambayo yamechapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”

      KWA NINI NI MUHIMU?

      Kufundisha wengine Neno la Mungu ni jambo zito sana. Mungu anataka watu wapate “ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Kwa hiyo tuna wajibu wa kufundisha Neno la Mungu kwa usahihi.

      KUFUNDISHA wengine si kusoma tu maandiko ya Biblia. Mtume Paulo alimwandikia hivi mshiriki wake Timotheo: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.”—2 Tim. 2:15.

      Ili tufanye hivyo, ni lazima tufafanue maandiko kulingana na mafundisho ya Biblia. Hiyo inamaanisha tufikirie muktadha badala ya kuchagua tu maneno yanayotupendeza na kutoa maoni yetu wenyewe. Kupitia nabii Yeremia, Yehova aliwaonya watu wasiwasikilize manabii waliodai kusema maneno yake lakini kumbe walisema “maono ya mioyo yao wenyewe.” (Yer. 23:16) Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wasichafue Neno la Mungu kwa falsafa za wanadamu alipoandika: “Tumeyakataa kabisa mambo ya kichinichini yaliyo ya kuaibikia, si kutembea kwa ujanja, wala tukilighushi neno la Mungu.” Siku hizo, wauzaji wa divai wenye pupa walikuwa wakitia divai maji ili iwe nyingi wapate pesa zaidi. Sisi hatughushi Neno la Mungu kwa kulichanganya na falsafa za wanadamu. Paulo alitangaza kwamba “sisi si wachuuzi wa neno la Mungu kama watu wengi walivyo, bali tunasema kwa weupe wa moyo, ndiyo, tukiwa waliotumwa kutoka kwa Mungu, mbele ya Mungu, kwa ushirika na Kristo.”—2 Kor. 2:17; 4:2.

      Nyakati nyingine unaweza kunukuu andiko ili kukazia kanuni fulani. Biblia imejaa kanuni zenye mwongozo bora zinazotusaidia kushughulika na hali mbalimbali za maisha. (2 Tim. 3:16, 17) Lakini hakikisha kwamba unatumia kwa usahihi kanuni hizo na usitumie andiko vibaya, ukifanya andiko lionekane kana kwamba linasema jambo ambalo wewe unataka liseme. (Zab. 91:11, 12; Mt. 4:5, 6) Ni lazima utumie andiko kulingana na kusudi la Yehova, kupatana na Neno lote la Mungu.

      ‘Kulitumia sawasawa neno la ile kweli’ pia kunatia ndani kufahamu vile Biblia inavyosema. Biblia si “rungu” la kutwangia watu wengine. Walimu wa kidini waliompinga Yesu Kristo walinukuu Maandiko, lakini walipuuza mambo mazito ambayo Mungu alitaka yaonyeshwe kama vile haki, rehema, na uaminifu. (Mt. 22:23, 24; 23:23, 24) Yesu alionyesha utu wa Baba yake alipofundisha Neno la Mungu. Bidii ya Yesu kwa ajili ya ile kweli iliambatana na upendo mwingi aliowaonyesha watu aliofundisha. Tujaribu kuiga mfano wake.—Mt. 11:28.

      Tunawezaje kuwa na hakika kwamba tunatumia maandiko vizuri? Kusoma Biblia kwa ukawaida kunasaidia. Pia tunahitaji kutambua kwamba Yehova ametuandalia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” jamii ya Wakristo watiwa-mafuta ambayo Yehova anatumia kuandalia nyumba ya waamini chakula cha kiroho. (Mt. 24:45) Funzo la binafsi na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida na kuishiriki kutatusaidia kufaidika na mafunzo yanayoandaliwa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.

      Ikiwa kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinapatikana katika lugha yenu, jifunze kukitumia vizuri na kitakusaidia sana kuelewa kwa urahisi jinsi ya kupata mwongozo unaohitaji ili kutumia vizuri mamia ya maandiko ambayo hutumiwa mara nyingi katika huduma ya shambani. Ikiwa unataka kutumia andiko ambalo hulifahamu, kwa unyenyekevu fanya utafiti ili ulitumie sawasawa neno la ile kweli.—Mit. 11:2.

      Onyesha Vizuri Jinsi Andiko Linavyohusika. Unapowafundisha wengine, hakikisha wanaelewa vizuri uhusiano ulioko kati ya habari unayozungumzia na maandiko unayotumia. Ukiuliza swali kabla ya kusoma andiko, waonyeshe wasikilizaji jinsi andiko hilo linavyojibu swali lile. Ikiwa unatumia andiko kuunga mkono jambo fulani unalosema, hakikisha mwanafunzi anaona wazi jinsi andiko hilo linavyothibitisha jambo hilo.

      Mara nyingi haitoshi tu kusoma andiko, hata kama unalisoma kwa mkazo. Kumbuka kwamba mtu wa kawaida hafahamu vizuri Biblia na ukisoma andiko mara moja tu labda hatakuelewa. Kazia sehemu ya andiko inayohusu jambo unalozungumzia.

      Kwa kawaida unaweza kukazia jambo kwa kutenga maneno makuu, yaani maneno ambayo yanahusiana na jambo unalozungumzia. Njia rahisi zaidi ni kurudia kutaja maneno yenye mambo unayotaka kukazia. Ikiwa unazungumza na mtu fulani, unaweza kuuliza maswali ambayo yanaweza kumsaidia kutambua maneno makuu. Wasemaji wengine wanapohutubu, wao hupendelea kukazia maneno makuu kwa kutumia maneno mengine yenye maana sawa au kwa kurudia kutaja wazo kuu. Na ukiamua kufanya hivyo, hakikisha wasikilizaji wanaona jinsi jambo unalozungumzia linavyohusiana na andiko unalosoma.

      Ikiwa umetenga maneno makuu, basi umeweka msingi mzuri. Sasa jenga kwenye msingi huo. Kabla ya kusoma andiko, je, umeonyesha wazi sababu ya kulisoma? Ikiwa ndivyo, onyesha jinsi maneno ambayo umekazia yanavyohusiana na matarajio ya wasikilizaji kuhusu andiko hilo. Onyesha vizuri uhusiano ulioko. Hata kama utangulizi wa andiko hilo haukuwa dhahiri sana, onyesha sababu ya kulisoma.

      Mafarisayo walimwuliza Yesu swali ambalo walifikiri ni gumu, yaani: “Je, yaruhusika kisheria mtu kutaliki mke wake kwa kila namna ya sababu?” Yesu alitumia Mwanzo 2:24 kujibu. Ebu ona kwamba Yesu alitaja sehemu tu ya andiko hilo, kisha akaonyesha jinsi sehemu hiyo inavyohusika. Baada ya Yesu kutaja kwamba mwanamume na mke wake watakuwa “mwili mmoja,” alimalizia kusema: “Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mt. 19:3-6.

      Unapaswa kufafanua andiko kwa kadiri gani ili liwe wazi? Hiyo inategemea wasikilizaji na umuhimu wa jambo unalozungumza. Kusudi lako liwe kufafanua andiko kwa njia rahisi na ya moja kwa moja.

      Tumia Maandiko Kutoa Sababu. Matendo 17:2, 3 linapozungumzia huduma ya mtume Paulo huko Thesalonike, linatuambia kwamba ‘alitoa sababu kutokana na Maandiko.’ Kila mtumishi wa Yehova anapaswa kujaribu kukuza uwezo huu. Kwa mfano, Paulo alisimulia mambo yaliyohusu maisha ya Yesu na huduma yake, akaonyesha kwamba mambo hayo yalitabiriwa katika Maandiko ya Kiebrania, kisha akamalizia kwa nguvu akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia nyinyi.”

      Paulo alinukuu Maandiko ya Kiebrania mara nyingi alipowaandikia Waebrania. Mara nyingi alitenga neno au maneno fulani kisha akaonyesha umuhimu wake ili kukazia jambo au kulifafanua vizuri. (Ebr. 12:26, 27) Katika masimulizi ya Waebrania sura ya 3, Paulo alinukuu Zaburi 95:7-11. Ona kwamba alifafanua sehemu tatu za maandiko hayo: (1) alitaja moyo (Ebr. 3:8-12), (2) umuhimu wa neno “Leo” (Ebr. 3:7, 13-15; 4:6-11), na (3) maana ya maneno haya: “Hawataingia katika pumziko langu.” (Ebr. 3:11, 18, 19; 4:1-11) Jaribu kuiga mfano huo unapoonyesha jinsi kila andiko linavyohusika na jambo unalozungumzia.

      Ona jinsi Yesu alivyotoa sababu vizuri akitumia Maandiko katika Luka 10:25-37. Mtaalamu mmoja wa Sheria alimwuliza: “Mwalimu, ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Kwanza, Yesu akamwuliza mtu huyo maoni yake juu ya swali hilo, kisha Yesu akakazia kwamba ni muhimu kufanya kile ambacho Neno la Mungu linasema. Ilipokuwa wazi kwamba mtu huyo haelewi, Yesu alifafanua kabisa neno moja tu katika andiko hilo, “jirani.” Na badala ya kulifafanua tu neno hilo, Yesu alitumia mfano uliomwezesha mtu huyo afikie jibu linalofaa.

      Yesu alipokuwa akijibu maswali, hakunukuu tu maandiko na kutoa majibu rahisi na ya wazi. Alifafanua maandiko hayo na kuonyesha jinsi yanavyojibu swali aliloulizwa.

      Masadukayo walipopinga tumaini la ufufuo, Yesu alikazia sehemu fulani tu ya Kutoka 3:6. Lakini hakuachia hapo tu. Alisababu juu ya andiko hilo na kuonyesha wazi kwamba ufufuo ni sehemu ya kusudi la Mungu.—Mk. 12:24-27.

      Ili kuwa mwalimu bora ni muhimu kukuza uwezo wa kutumia Maandiko kutoa sababu vizuri na kwa matokeo mazuri.

      JINSI YA KUKUZA UWEZO HUO

      • Soma Biblia kwa ukawaida. Jifunze kwa makini Mnara wa Mlinzi, na utayarishe vizuri mikutano ya kutaniko.

      • Hakikisha unajua maana ya maneno unayotumia katika andiko lolote unalotaka kutumia. Soma andiko hilo kwa makini ili uelewe vizuri jambo linalosema.

      • Uwe na mazoea ya kutumia vichapo vyetu vya Kikristo kufanya utafiti.

      MAZOEZI: Fikiria 2 Petro 3:7. Je, linathibitisha dunia itaharibiwa kwa moto? (Unapofafanua maana ya neno “dunia,” pia fikiria maana ya “mbingu.” Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba “dunia” inaweza kuwa na maana ya mfano? Kulingana na mstari wa 7 ni nani, au ni nini kinachoharibiwa? Jambo hilo linalinganaje na tukio la wakati wa Noa linalotajwa katika mstari wa 5 na 6?)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki