-
Daima Kaza Uangalifu kwa Kufundisha KwakoMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 15
-
-
Daima Kaza Uangalifu kwa Kufundisha Kwako
“Daima kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.”—1 TIMOTHEO 4:16.
1, 2. Kwa nini walimu wenye bidii wanahitajiwa kwa haraka leo?
“NENDENI mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . [na] kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kwa kuzingatia amri hiyo ya Yesu Kristo, ni lazima Wakristo wote wajitahidi kuwa walimu. Walimu wenye bidii wanahitajiwa ili wawasaidie watu wenye mioyo ya haki wapate ujuzi juu ya Mungu kabla hawajachelewa mno. (Waroma 13:11) Mtume Paulo alihimiza hivi: “Lihubiri neno, lifanye kwa hima katika majira yenye kufaa, katika majira yenye taabu.” (2 Timotheo 4:2) Hilo lahitaji kufundisha ndani na pia nje ya kutaniko. Kwa kweli, utume wenyewe wa kuhubiri wahusisha mengi kuliko tu kutangaza ujumbe wa Mungu. Ufundishaji wenye matokeo wahitajika ili wanaopendezwa wawe wanafunzi.
2 Twaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Watu wamepotoshwa na falsafa za kilimwengu na mafundisho ya uwongo. Wengi ‘wako katika giza kiakili’ na ‘wameishiwa na hisia zote za adili.’ (Waefeso 4:18, 19) Baadhi yao wana majeraha ya kihisia-moyo yenye maumivu. Naam, kwa kweli watu “[wanachunwa] ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Hata hivyo, kwa kutumia usanifu wa kufundisha, twaweza kuwasaidia wenye mioyo ya haki wafanye mabadiliko yanayohitajiwa.
Walimu Ndani ya Kutaniko
3. (a) Utume wa Yesu wa kufundisha hutia ndani nini? (b) Ni nani walio na daraka la msingi la kufundisha ndani ya kutaniko?
3 Kupitia mpango wa funzo la Biblia nyumbani, mamilioni ya watu wanapata mafunzo ya kibinafsi. Hata hivyo, baada ya kubatizwa, wapya wahitaji msaada zaidi ili wapate “kutia mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi.” (Waefeso 3:17) Tuendeleapo kutimiza utume wa Yesu uliorekodiwa kwenye Mathayo 28:19, 20 na kuwaelekeza wapya kwenye tengenezo la Yehova, wao hunufaika kutokana na kufundishwa ndani ya kutaniko lenyewe. Kulingana na Waefeso 4:11-13, wanaume wamechaguliwa ili watumikie wakiwa “wachungaji na walimu, kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo.” Nyakati nyingine, usanifu wao wa kufundisha wahusisha uhitaji wa ‘kukaripia, kukemea, kuhimiza kwa bidii, kwa ustahimilivu wote.’ (2 Timotheo 4:2) Kazi ya walimu ilikuwa muhimu sana hivi kwamba, alipowaandikia Wakorintho, Paulo aliwaorodhesha walimu punde tu baada ya mitume na manabii.—1 Wakorintho 12:28.
4. Uwezo wa kufundisha unatusaidiaje kutii himizo la Paulo lililorekodiwa kwenye Waebrania 10:24, 25?
4 Ni kweli kwamba si Wakristo wote hutumikia wakiwa wazee au waangalizi. Hata hivyo, wote wanatiwa moyo kuchocheana “kwenye upendo na kazi zilizo bora.” (Waebrania 10:24, 25) Kufanya hivyo kwenye mikutano kwahusisha maelezo yaliyotayarishwa vizuri, ya kuhisiwa moyoni ambayo yaweza kujenga na kutia wengine moyo. Wahubiri wa Ufalme wenye uzoevu huenda pia ‘wakachochea kwa kazi zilizo bora’ kwa kushiriki na wahubiri wapya ujuzi na uzoevu wao wanapohubiri nao shambani. Agizo lenye thamani laweza kutolewa nyakati kama hizo na katika hali za kivivi hivi. Kwa mfano, wanawake wakomavu wanahimizwa wawe “walimu wa lililo jema.”—Tito 2:3.
Wanashawishwa Kuamini
5, 6. (a) Ukristo wa kweli watofautianaje na ibada isiyo ya kweli? (b) Wazee huwasaidiaje wapya wafanye maamuzi yenye hekima?
5 Hivyo, Ukristo wa kweli hutofautiana sana na dini za uwongo zilizo nyingi ambazo hutafuta kudhibiti fikira za washiriki wao. Yesu alipokuwa duniani, viongozi wa kidini walitafuta kudhibiti karibu kila jambo katika maisha ya watu kupitia mapokeo ya kibinadamu yenye uonevu. (Luka 11:46) Mara nyingi makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wamefanya vivyo hivyo.
6 Hata hivyo, ibada ya kweli ni “utumishi mtakatifu” ambao twautoa pamoja na ‘nguvu zetu za kufikiri kuzuri.’ (Waroma 12:1) Watumishi wa Yehova ‘wanashawishwa kuamini.’ (2 Timotheo 3:14) Nyakati fulani, wale wanaoongoza huenda wakahitaji kuanzisha miongozo na taratibu fulani ili kutaniko litende kazi kwa njia inayofaa. Hata hivyo, badala ya wazee kutafuta kuwafanyia Wakristo wenzao maamuzi, wao huwafundisha “kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.” (Waebrania 5:14) Kimsingi, wazee hufanya hivyo kwa kulilisha kutaniko “maneno ya imani na fundisho bora.”—1 Timotheo 4:6.
Kukaza Uangalifu kwa Kufundisha Kwako
7, 8. (a) Watu wenye uwezo mbalimbali wa kiasi wanawezaje kutumikia wakiwa walimu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba wahitaji jitihada ya kibinafsi ili kuwa mwalimu mwenye matokeo?
7 Ingawa hivyo, acheni tugeukie tena ule utume wetu wa ujumla wa kufundisha. Je, utume huo wahitaji stadi zozote hususa, elimu, au uwezo mbalimbali ili kuushiriki? Si lazima. Sehemu kubwa ya ufundishaji huu wa ulimwenguni pote inafanywa na watu mmoja-mmoja wa kawaida walio na uwezo mbalimbali wa kiasi. (1 Wakorintho 1:26-29) Paulo aeleza: “Sisi tuna hazina hii [yaani, huduma] katika vyombo vya udongo [miili isiyokamilika], ili nguvu ipitayo iliyo ya kawaida ipate kuwa ya Mungu na si ile ya kutoka katika sisi wenyewe.” (2 Wakorintho 4:7) Mafanikio makubwa mno ambayo kazi ya kuhubiri Ufalme tufeni pote imepata yanathibitisha nguvu za roho ya Yehova!
8 Hata hivyo, wahitaji kujitahidi sana ili uwe “mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.” (2 Timotheo 2:15) Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Daima kaza uangalifu kwako mwenyewe na kwa kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivi utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.” (1 Timotheo 4:16) Ni jinsi gani hasa mtu hukaza uangalifu kwa kufundisha kwake, iwe ndani au nje ya kutaniko? Je, kufanya hivyo kwahitaji mtu awe na ustadi mkubwa au mbinu fulani za kufundisha?
9. Ni jambo gani muhimu zaidi kuliko uwezo mbalimbali wa kiasili?
9 Kwa hakika Yesu alionyesha ufahamu usio wa kawaida wa njia za kufundisha katika Mahubiri ya Mlimani ambayo ni maarufu sana. Alipomaliza kusema, “umati ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 7:28) Bila shaka, hakuna mmoja wetu awezaye kufundisha sawasawa na vile Yesu alivyofanya. Ingawa hivyo, hatuhitaji kuwa wasemaji wenye ufasaha ili tuwe walimu wenye matokeo. Kwani, kulingana na Ayubu 12:7, hata “wanyama” na “nyuni” waweza kufundisha kimya-kimya! Jambo muhimu zaidi kwa kuongezea uwezo au stadi mbalimbali ambazo huenda tukawa nazo ni kwamba sisi ni “watu wa namna gani”—aina ya sifa tulizo nazo na aina ya mazoea ambayo tumesitawisha yanayoweza kuigwa na wanafunzi.—2 Petro 3:11; Luka 6:40.
Wanafunzi wa Neno la Mungu
10. Yesu aliwekaje kielelezo kizuri akiwa mwanafunzi wa Neno la Mungu?
10 Ni lazima mwalimu wa kweli za Kimaandiko mwenye matokeo awe mwanafunzi wa Neno la Mungu. (Waroma 2:21) Yesu Kristo aliweka kielelezo kisicho cha kawaida kuhusiana na hilo. Wakati wa huduma yake, Yesu alirejezea au kutoa mawazo yaliyolingana na vifungu vilivyo karibu katika nusu ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania.a Ujuzi wake juu ya Neno la Mungu ulikuwa wazi alipokuwa mwenye umri wa miaka 12, alipokutwa “ameketi katikati ya walimu na akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” (Luka 2:46) Akiwa mtu mzima, Yesu alikuwa na zoea la kwenda katika sinagogi, ambapo Neno la Mungu lilisomwa.—Luka 4:16.
11. Ni mazoea gani mazuri ya kujifunza ambayo mwalimu apaswa kusitawisha?
11 Je, wewe ni msomaji mwenye bidii wa Neno la Mungu? Ukilisoma kwa bidii ndipo “utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu.” (Mithali 2:4, 5) Kwa hiyo, sitawisha mazoea mazuri ya kusoma. Jaribu kusoma sehemu ya Neno la Mungu kila siku. (Zaburi 1:2) Fanya liwe zoea kusoma kila toleo la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! punde ulipatapo. Kaza uangalifu kwenye mikutano ya kutaniko. Jifunze kufanya utafiti kwa makini. Ukijifunza ‘kufuatisha mambo yote kwa uangalifu,’ unaweza kuepuka kutia chumvi na kusema mambo yasiyo sahihi unapofundisha.—Luka 1:3.
Upendo na Staha kwa Wale Wanaofundishwa
12. Mtazamo wa Yesu kuelekea wanafunzi wake ulikuwa nini?
12 Sifa nyingine muhimu ni mtazamo unaofaa kuelekea wale unaofundisha. Mafarisayo waliwadharau wale waliomsikiliza Yesu. “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa,” wakasema. (Yohana 7:49) Lakini Yesu alikuwa na upendo wenye kina kirefu na pia staha kwa wanafunzi wake. Yeye alisema: “Siwaiti nyinyi tena watumwa, kwa sababu mtumwa hayajui yale afanyayo bwana-mkubwa wake. Lakini nimewaita nyinyi marafiki, kwa sababu mambo yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu nimewajulisha nyinyi.” (Yohana 15:15) Hilo lilionyesha namna ambavyo wanafunzi wa Yesu wanapaswa kuendesha utendaji wao wa kufundisha.
13. Paulo alihisije juu ya wale aliofundisha?
13 Kwa mfano, Paulo hakudumisha uhusiano usio wa kirafiki, ulio kama wa kikazi, baina yake na wanafunzi wake. Aliwaambia Wakorintho hivi: “Ingawa huenda mkawa mna wafunzi elfu kumi katika Kristo, hakika si baba wengi mlio nao; kwa maana katika Kristo Yesu mimi nimekuwa baba yenu kupitia habari njema.” (1 Wakorintho 4:15) Nyakati nyingine, Paulo alitoa machozi huku akiwaonya kwa upole wale aliofundisha! (Matendo 20:31) Alionyesha pia saburi na fadhili isiyo ya kawaida. Kwa hiyo angeweza kuwaambia Wathesalonike hivi: “Tulipata kuwa waanana katikati yenu, kama wakati mama mwenye kunyonyesha atunzavyo sana watoto wake mwenyewe.”—1 Wathesalonike 2:7.
14. Kwa nini ni jambo muhimu sana kupendezwa kibinafsi na wanafunzi wetu? Toa kielezi.
14 Je, wewe unawaiga Yesu na Paulo? Upendo wa kweli kwa wanafunzi wetu unaweza kujazia upungufu wowote katika uwezo mbalimbali wa kiasili ambao huenda tukawa nao. Je, wanafunzi wetu wa Biblia wanahisi kwamba kweli tunapendezwa nao kibinafsi? Je, tunatumia wakati ili tupate kuwajua? Mwanamke mmoja Mkristo alipokuwa na tatizo la kumsaidia mwanafunzi afanye maendeleo ya kiroho, aliuliza kwa fadhili hivi: “Je, kuna jambo fulani linalokuhangaisha?” Huyo mwanamke akaanza kufunua yaliyokuwa moyoni mwake, akasimulia mahangaiko yake mengi sana. Mazungumzo hayo yenye upendo yakawa mwanzo wa mabadiliko makubwa kwa huyo mwanamke. Katika visa kama hivyo, mawazo na maneno ya Kimaandiko yenye kufariji na kutia moyo yafaa. (Waroma 15:4) Ingawa hivyo, kuna neno la tahadhari: Huenda mwanafunzi wa Biblia anafanya maendeleo ya haraka lakini huenda bado anahitaji kushinda mazoea fulani yasiyo ya Kikristo. Kwa hiyo huenda lisiwe jambo la hekima kuwa na uhusiano wa karibu sana na mtu huyo. Mipaka ya Kikristo inayofaa yapasa kudumishwa.—1 Wakorintho 15:33.
15. Twaweza kuonyeshaje staha kwa wanafunzi wetu wa Biblia?
15 Staha kwa wanafunzi wetu yahusisha kuepuka kujaribu kudhibiti maisha yao ya kibinafsi. (1 Wathesalonike 4:11) Kwa mfano, twaweza kuwa tunajifunza na mwanamke ambaye anaishi na mwanamume ambaye hajafunga ndoa naye. Labda wamezaa watoto pamoja. Mwanamke huyo ataka kurekebisha mambo ili ajipatanishe na viwango vya Yehova kwa kuwa amepata ujuzi sahihi juu ya Mungu. (Waebrania 13:4) Je, apaswa kuolewa na mwanamume huyo au kutengana naye? Labda twahisi kwa dhati kwamba kuolewa na mwanamume ambaye hapendezwi sana na mambo ya kiroho kungezuia maendeleo yake ya baadaye. Kwa upande mwingine, huenda tukahofia hali njema ya watoto wake na kufikiria kwamba ingekuwa afadhali aolewe na huyo mwanamume. Kwa vyovyote vile, itakuwa kukosa kuonyesha staha na upendo kuingilia maisha ya mwanafunzi na kujaribu kumlazimisha akubali maoni yetu katika mambo kama hayo. Kwani, ni huyo mwanamke ambaye ni lazima aishi na matokeo ya uamuzi wake. Basi, je, haingekuwa bora kumzoeza mwanafunzi wa aina hiyo kutumia ‘nguvu zake mwenyewe za ufahamu’ na kujiamulia yale anayopaswa kufanya?—Waebrania 5:14.
16. Wazee waweza kuonyeshaje upendo na staha kwa kundi la Mungu?
16 Ni jambo la muhimu hasa kwa wazee wa kutaniko kulitendea kundi kwa njia ya upendo na staha. Akimwandikia Filemoni, Paulo alisema hivi: “Ingawa nina uhuru mkubwa wa usemi kwa kuhusiana na Kristo kukuagiza ufanye ambalo ni lenye kufaa, badala ya hivyo ninakuhimiza kwa bidii juu ya msingi wa upendo.” (Filemoni 8, 9) Nyakati nyingine, hali zenye kuvunja moyo zaweza kutokea kutanikoni. Huenda ikawa lazima kuwa imara. Paulo alimhimiza Tito “[afulize] kuwakaripia [wenye kukosea] kwa ukali, ili wapate kuwa wenye afya katika imani.” (Tito 1:13) Hata hivyo, lazima waangalizi wajihadhari kutosema na kutaniko kamwe kwa njia isiyo ya fadhili. “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana,” Paulo akaandika, “bali ahitaji kuwa mwanana kuelekea wote, mwenye sifa za ustahili kufundisha, akifuliza kujizuia mwenyewe chini ya uovu.”—2 Timotheo 2:24; Zaburi 141:3.
17. Musa alifanya kosa gani, na wazee wanaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
17 Waangalizi wapaswa kujikumbusha sikuzote kwamba wanashughulika na “kundi la Mungu.” (1 Petro 5:2) Ingawa Musa alikuwa mnyenyekevu, alipoteza maoni hayo kwa muda mfupi. Waisraeli “waliiasi roho yake, akasema yasiyofaa kwa midomo yake.” (Zaburi 106:33) Mungu alikasirishwa sana na huko kutendwa vibaya kwa kundi Lake, hata ingawa wao pia walikuwa na lawama. (Hesabu 20:2-12) Wazee wanapokabili magumu kama hayo leo, wapaswa kujitahidi kufundisha na kuagiza kwa ufahamu wenye kina na fadhili. Ndugu zetu huitikia kwa njia bora zaidi wanapotendewa kwa ufikirio na kama watu mmoja-mmoja wanaohitaji msaada, bali si kama wakosaji wasioweza kurekebishwa. Wazee wanahitaji kudumisha mtazamo mzuri ambao Paulo alikuwa nao aliposema hivi: “Tuna uhakika katika Bwana kuhusu nyinyi, kwamba mnafanya na mtaendelea kufanya mambo tuagizayo.”—2 Wathesalonike 3:4.
Kuitikia Mahitaji Yao
18, 19. (a) Twapaswa kuitikiaje mahitaji ya wanafunzi wa Biblia walio na upungufu mbalimbali? (b) Huenda tukawasaidiaje wanafunzi walio na tatizo la mambo hususa?
18 Mwalimu mwenye matokeo huwa tayari kubadilikana ili afae uwezo na upungufu mbalimbali wa wanafunzi wake. (Linganisha Yohana 16:12.) Katika kielezi cha Yesu kuhusu talanta, bwana-mkubwa alimpa mapendeleo “kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.” (Mathayo 25:15) Twaweza kufuata kiolezo kama hicho tunapoongoza mafunzo ya Biblia. Kwa kawaida, ni vizuri kumaliza kichapo kinachotegemea Biblia kwa muda mfupi ifaavyo. Hata hivyo, ni lazima ikubaliwe kwamba si wote walio na stadi nzuri za kusoma au uwezo wa kuelewa mawazo mapya haraka. Kwa hiyo, ufahamu wahitajika ili kuamua ni wakati gani tunapopaswa kusonga kutoka kwenye hoja moja hadi nyingine kwenye funzo ikiwa watu mmoja-mmoja wanaoitikia vizuri wanakabili tatizo la kufanya maendeleo haraka. Jambo muhimu zaidi ni kuwasaidia wanafunzi wapate maana ya yale wanayojifunza kuliko tu kumaliza habari kwa mwendo uliowekwa.—Mathayo 13:51.
19 Jambo hilohilo laweza kusemwa kuhusu wanafunzi wa Biblia ambao wana tatizo la mambo hususa, kama vile Utatu au sikukuu za kidini. Ingawa kwa kawaida si lazima kutia ndani habari za utafiti unaotegemea Biblia tunapokuwa kwenye mafunzo yetu, twaweza kufanya hivyo mara kwa mara ikiwa hilo litakuwa na manufaa iliyo wazi. Uamuzi mzuri wapasa kutumiwa ili tusipunguze maendeleo ya mwanafunzi isivyo lazima.
Uwe na Shauku!
20. Paulo aliwekaje kielelezo katika kuonyesha shauku na usadikisho katika kufundisha kwake?
20 “Iweni wenye kuwaka roho,” asema Paulo. (Waroma 12:11) Ndiyo, iwe tunaongoza funzo la Biblia nyumbani au tunashiriki sehemu fulani katika mikutano ya kutaniko, twapaswa kufanya hivyo kwa bidii na kwa shauku. Paulo aliwaambia Wathesalonike hivi: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu.” (1 Wathesalonike 1:5) Kwa njia hiyo Paulo na waandamani wake waliwapa “si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi [zao] wenyewe.”—1 Wathesalonike 2:8.
21. Twaweza kudumishaje mtazamo wenye shauku kuelekea migawo yetu ya kufundisha?
21 Shauku ya kweli hutokana na usadikisho imara kwamba wanafunzi wetu wa Biblia wahitaji kusikia yale tunayotaka kusema. Acheni tusiuone kamwe mgawo wowote wa kufundisha kana kwamba ni jambo la kawaida tu. Kwa hakika mwandishi Ezra alikaza uangalifu kwa kufundisha kwake kuhusiana na hili. Yeye ‘aliuelekeza [“aliutayarisha,” NW] moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda, na kufundisha . . . katika Israeli.’ (Ezra 7:10) Twapaswa kufanya vivyo hivyo kwa kutayarisha kikamili na kutafakari juu ya umuhimu wa habari hizo. Acheni tusali kwa Yehova atujaze imani na usadikisho. (Luka 17:5) Shauku yetu yaweza kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia kusitawisha upendo halisi kwa ile kweli. Bila shaka, kukaza uangalifu kwa kufundisha kwetu kwaweza kutia ndani pia kutumia mbinu hususa za kufundisha. Makala yetu inayofuata itazungumzia baadhi ya mbinu hizo.
-
-
Fundisha kwa Ufahamu Wenye Kina na UshawishiMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 15
-
-
Fundisha kwa Ufahamu Wenye Kina na Ushawishi
“Moyo wa mwenye hekima husababisha kinywa chake kuonyesha ufahamu wenye kina, na kwa midomo yake huongeza ushawishi.”—MITHALI 16:23, NW.
1. Ni kwa nini kufundisha Neno la Mungu kwahusisha mengi kuliko tu kuwasilisha habari?
MRADI wetu tukiwa walimu wa Neno la Mungu ni kuelimisha, si akili tu za wanafunzi wetu, bali pia mioyo yao. (Waefeso 1:18) Kwa hiyo, kufundisha kwahusisha mengi kuliko tu kuwasilisha habari. Mithali 16:23, NW, yasema: “Moyo wa mwenye hekima husababisha kinywa chake kuonyesha ufahamu wenye kina, na kwa midomo yake huongeza ushawishi.”
2. (a) Inamaanisha nini kushawishi? (b) Inawezekanaje kwa Wakristo wote kuwa walimu wenye kushawishi?
2 Kwa hakika, mtume Paulo alitumia kanuni hiyo katika kazi yake ya kufundisha. Alipokuwa Korintho, “yeye alikuwa akitoa hotuba katika sinagogi kila sabato na alikuwa akishawishi Wayahudi na Wagiriki.” (Matendo 18:4) Kulingana na chanzo kimoja chenye mamlaka, neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “kushawishi” lamaanisha “kusababisha badiliko la maoni kupitia uvutano wa kusababu au ufikirio wa kiadili.” Kwa njia ya majadiliano yenye kusadikisha, Paulo aliweza kuwafanya watu wabadilishe hasa njia yao ya kufikiri. Uwezo wake wa kushawishi ulikuwa wa ajabu sana hivi kwamba maadui wake walimwogopa. (Matendo 19:24-27) Hata hivyo, ufundishaji wa Paulo haukuwa wonyesho wa uwezo wa mwanadamu. Aliwaambia Wakorintho hivi: “Usemi wangu na lile nililohubiri halikuwa kwa maneno yenye ushawishi ya hekima bali kwa wonyesho wa roho na nguvu, ili imani yenu ipate kuwa, si katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:4, 5) Kwa kuwa Wakristo wote wana msaada wa roho ya Yehova Mungu, wote wanaweza kuwa walimu wenye kushawishi. Lakini jinsi gani? Acheni tuchunguze mbinu kadhaa za ufundishaji wenye matokeo.
Uwe Msikilizaji Mzuri
3. Kwa nini ufahamu wenye kina wahitajika tunapowafundisha wengine, na twawezaje kuufikia moyo wa mwanafunzi wa Biblia?
3 Mbinu ya kwanza ya kufundisha yahusisha kusikiliza, bali si kusema. Kama inavyoonyeshwa kwenye Mithali 16:23, ili tuwe wenye kushawishi ni lazima tuwe na ufahamu wenye kina. Kwa hakika Yesu alikuwa na ufahamu wenye kina kuhusu watu aliofundisha. Yohana 2:25 lasema: “Yeye mwenyewe alijua kile kilichokuwa katika binadamu.” Lakini twaweza kujuaje yale yaliyo mioyoni mwa wale tunaofundisha? Njia moja ni kuwa msikilizaji mzuri. Yakobo 1:19 lasema: “Kila mtu lazima awe mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema.” Ni kweli, si watu wote hueleza fikira zao kwa urahisi. Wanafunzi wetu wa Biblia wanapoendelea kusadikishwa juu ya upendezi wetu wa kweli kwao, huenda wakawa na mwelekeo zaidi wa kueleza hisia zao za kweli. Maswali yenye fadhili lakini yenye utambuzi huenda mara kwa mara yakatusaidia kufikia moyo na ‘kuteka’ maelezo kama hayo.—Mithali 20:5.
4. Kwa nini ni lazima wazee Wakristo wawe wasikilizaji wazuri?
4 Ni muhimu hasa kwa wazee Wakristo kuwa wasikilizaji wazuri. Ni kwa kufanya hivyo tu ndipo kwa kweli wanaweza “kujua jinsi [wapaswavyo] kumpa jibu kila mmoja.” (Wakolosai 4:6) Mithali 18:13 yaonya hivi: “Yeye ajibuye kabla hajasikia, ni upumbavu na aibu kwake.” Wakati mmoja ndugu wawili waliokuwa na nia nzuri walimpa dada shauri kuhusu mambo ya kilimwengu kwa kuwa alikosa mikutano kadhaa. Dada huyo aliumizwa sana kwa sababu hawakumwuliza kwa nini hakuwepo. Alikuwa akipata nafuu kutokana na upasuaji uliofanywa karibuni. Basi, ni muhimu jinsi gani kwamba tusikilize kabla ya kutoa shauri!
5. Wazee wanaweza kushughulikiaje mabishano ambayo huzuka miongoni mwa akina ndugu?
5 Kwa wazee, kufundisha mara nyingi huhusisha kuwashauri wengine. Hapa, pia, ni muhimu kuwa msikilizaji mzuri. Kusikiliza ni kwa lazima mabishano yanapozuka miongoni mwa Wakristo wenzi. Ni baada tu ya kusikiliza ndipo wazee wawezapo kumwiga “Baba ambaye huhukumu bila ubaguzi wowote.” (1 Petro 1:17) Mara nyingi hisia-moyo huwa kali sana katika hali kama hizo, na mzee apaswa kukumbuka shauri la Mithali 18:17: “Ajiteteaye kwanza huonekana kuwa na haki; lakini juani yake huja na kumchunguza.” Mwalimu mwenye matokeo atasikiliza pande zote mbili. Kwa kutoa sala, yeye husaidia kuleta hali ya utulivu. (Yakobo 3:18) Ikiwa hisia-moyo zawa kali sana, huenda akadokeza kwamba kila ndugu amweleze mahangaiko yake moja kwa moja, badala ya hao wawili kuzozana. Kwa kutumia maswali yanayofaa, huenda mzee akabainisha masuala yanayochunguzwa. Katika visa vingi, mawasiliano mabaya, wala si nia ya kudhuru, ndiyo hubainika kuwa kisababishi cha mabishano. Lakini ikiwa kanuni za Biblia zimevunjwa, mwalimu mwenye upendo aweza sasa kufundisha akitumia ufahamu wenye kina, baada ya kusikiliza pande zote mbili.
Ubora wa Usahili
6. Paulo na Yesu waliwekaje kielelezo katika kufundisha kwa usahili?
6 Ustadi mwingine bora wa kufundisha ni kufanya mambo yawe sahili. Ni kweli, twataka wanafunzi wa Biblia wapate kwa “ukamili kuweza kufahamu kiakili pamoja na watakatifu wote ni nini ulio upana na urefu na kimo na kina” cha ile kweli. (Waefeso 3:18) Yapo mambo fulani ya mafundisho ya Biblia ambayo yanavutia sana na mara nyingi yanakuwa magumu. (Waroma 11:33) Hata hivyo, Paulo alipowahubiria Wagiriki, alikazia fikira habari sahili juu ya ‘Kristo akiwa ametundikwa.’ (1 Wakorintho 2:1, 2) Vivyo hivyo, Yesu alihubiri kwa njia iliyo wazi na yenye kuvutia. Alitumia maneno sahili katika Mahubiri ya Mlimani. Na bado, hayo mahubiri yana baadhi ya kweli zenye kina sana ambazo zimewahi kutamkwa.—Mathayo, sura ya 5 hadi 7.
7. Twaweza kuwekaje mambo yakiwa sahili tunapoongoza mafunzo ya Biblia?
7 Vivyo hivyo, sisi tunaweza kuweka mambo yakiwa sahili tunapofundisha kwenye mafunzo ya Biblia. Kwa njia gani? Kwa kukaza fikira juu ya “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Tunapoeleza mambo magumu kueleweka, twapaswa kujaribu kujieleza kwa maneno yaliyo sahili. Twapaswa kukazia fikira maandiko muhimu badala ya kujaribu kusoma na kuzungumzia kila andiko la Biblia ambalo limetajwa katika kichapo. Hilo lahitaji tutayarishe vizuri. Twahitaji kuepuka kumlemea mwanafunzi kwa kumpa mambo mengi, tukiepuka kukengeushwa fikira na masuala yenye umuhimu mdogo. Ikiwa mwanafunzi ana swali ambalo halihusu somo moja kwa moja, twaweza kudokeza kwa busara kwamba lizungumziwe baada ya somo kwisha.
Kutumia Maswali kwa Njia Yenye Matokeo
8. Yesu alitumiaje maswali kwa njia yenye matokeo?
8 Ustadi mwingine wa kufundisha wenye mafaa wahusisha kuuliza maswali yenye matokeo. Yesu Kristo alitumia maswali kwa wingi sana katika ufundishaji wake. Kwa mfano, Yesu alimwuliza Petro: “‘Wewe wafikiri nini, Simoni? Ni kutoka kwa nani wafalme wa dunia hupokea ushuru wa forodhani au kodi ya kichwa? Ni kutoka kwa wana wao au ni kutoka kwa wageni?’ Aliposema: ‘Kutoka kwa wageni,’ Yesu akamwambia: ‘Basi, kwa kweli hao wana hawalipi kodi.’” (Mathayo 17:24-26) Akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Yule aliyeabudiwa kwenye hekalu, kwa kweli Yesu hakuhitajika kulipa kodi ya hekalu. Lakini Yesu aliwasilisha kweli hiyo kwa kutumia maswali kwa njia yenye matokeo. Hivyo, Yesu alimsaidia Petro kufikia mkataa unaofaa uliotegemea habari ambazo tayari alikuwa nazo.
9. Twaweza kutumiaje maswali tunapokuwa kwenye mafunzo ya Biblia?
9 Twaweza kutumia maswali kwa njia nzuri tunapokuwa kwenye mafunzo ya Biblia. Ikiwa mwanafunzi atoa jibu lisilo sahihi, huenda ikashawishi kumweleza jibu sahihi, lakini je, kweli atashika habari hizo? Mara nyingi ni vizuri kumwelekeza mwanafunzi afikie mkataa unaofaa kwa kuuliza maswali. Kwa mfano, ikiwa anapata ugumu wa kuelewa ni kwa nini apaswa kulitumia jina la Mungu, huenda tukauliza, ‘Je, jina lako ni muhimu kwako? . . . Kwa nini? . . . Ungehisije ikiwa mtu fulani angekataa kulitumia jina lako? . . . Je, si jambo lenye sababu nzuri kwa Mungu kututaka tulitumie jina lake la kibinafsi?’
10. Huenda wazee wakatumiaje maswali wanapowasaidia watu mmoja-mmoja ambao wamejeruhiwa kihisia-moyo?
10 Wazee pia wanaweza kutumia maswali kwa njia nzuri wanapolichunga kundi. Wengi katika kutaniko wamechubuliwa kihisia-moyo na kuumizwa na ulimwengu wa Shetani na huenda wakahisi kwamba wao ni wachafu na wasioweza kupendwa. Huenda mzee akasababu na mtu kama huyo kwa kusema hivi: ‘Ingawa unasema kwamba unahisi wewe ni mchafu, Yehova anahisije kukuhusu? Ikiwa Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo alimruhusu Mwana wake afe na kuandaa fidia kwa ajili yako, je, hilo halimaanishi kwamba Mungu anakupenda?’—Yohana 3:16.
11. Maswali yasiyodai majibu hutimiza kusudi gani, nayo yaweza kutumiwaje katika kusema mbele ya watu wote?
11 Mbinu nyingine yenye mafaa ni utumizi wa maswali yasiyodai majibu. Wasikilizaji hawatarajiwi kujibu maswali hayo kwa sauti, lakini kwa njia hiyo wao husaidiwa kusababu juu ya masuala. Mara nyingi manabii wa zamani waliuliza maswali kama hayo ili kuwafanya wasikilizaji wafikirie kwa uzito. (Yeremia 18:14, 15) Yesu alitumia maswali yasiyodai majibu kwa njia yenye matokeo. (Mathayo 11:7-11) Maswali ya aina hiyo ni yenye matokeo hasa katika kusema mbele ya watu. Badala tu ya kuwaambia wasikilizaji kwamba ni lazima wawe wenye nafsi yote ili wampendeze Yehova, huenda ikawa na matokeo zaidi kuuliza, ‘Ikiwa kwa kweli sisi si wenye nafsi yote katika utumishi wetu, je, Yehova atapendezwa?’
12. Kuna faida gani kuuliza maswali ya maoni?
12 Maswali ya maoni ni yenye mafaa katika kutambua ikiwa kweli mwanafunzi wa Biblia anaamini yale anayojifunza. (Mathayo 16:13-16) Huenda mwanafunzi akajibu kwa usahihi kwamba uasherati ni mbaya. Lakini kwa nini usifuatilie hilo kwa maswali kama vile, Wewe binafsi wahisije juu ya kiwango cha Mungu cha adili? Je, unahisi kwamba ni chenye kuzuia mno? Je, ungeweza kusema kwamba haidhuru ikiwa unafuata viwango vya Mungu au huvifuati?
Vielezi Vinavyoufikia Moyo
13, 14. (a) Inamaanisha nini kutoa kielezi cha kitu fulani? (b) Ni kwa nini vielezi vizuri ni vyenye matokeo?
13 Njia nyingine ya kufikia mioyo ya wasikilizaji na wanafunzi wa Biblia ni kupitia utumizi wenye matokeo wa vielezi. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kielezi” humaanisha kihalisi “kuweka kando ya au pamoja.” Unapotoa kielezi, unaeleza kitu kwa ‘kukiweka kando ya’ kitu kingine kinachofanana nacho. Kwa mfano, Yesu aliuliza: “Tutaufananisha ufalme wa Mungu na nini, au tutauweka katika kielezi gani?” Kwa kujibu, Yesu alitaja punje ya haradali ambayo watu waliifahamu vizuri.—Marko 4:30-32.
14 Manabii wa Mungu walitumia vielezi vingi vyenye nguvu. Waashuri, waliokuwa wametumikia wakiwa chombo cha Mungu cha kuwaadhibu Waisraeli, walipotumia ukatili wa kinyama, Isaya alifunua kiburi chao kupitia kielezi hiki: “Je! shoka lijisifu juu yake alitumiaye? je! msumeno ujitukuze juu yake auvutaye?” (Isaya 10:15) Alipokuwa akiwafundisha wengine, Yesu pia alitumia vielezi kwa wingi. Imeripotiwa kwamba “bila kielezi hakuwa akisema nao.” (Marko 4:34) Vielezi vizuri ni vyenye matokeo kwa sababu vinahusisha akili na moyo. Hivyo huwaruhusu wasikilizaji washike habari mpya kwa utayari kwa kuilinganisha na kitu ambacho tayari wanakifahamu.
15, 16. Ni nini kitakachofanya vielezi viwe na matokeo zaidi? Toa mifano.
15 Twaweza kutumiaje vielezi ambavyo kwa kweli vinaufikia moyo? Kwanza kabisa, lazima kielezi kifanane ifaavyo na kitu kinachoelezwa. Ikiwa kwa kweli ulinganisho haufai, kielezi kitakengeusha badala ya kuelimisha wasikilizaji. Wakati mmoja msemaji mwenye nia nzuri alijaribu kuwasilisha ujitiisho wa mabaki watiwa-mafuta kwa Yesu Kristo kwa kuwalinganisha na mbwa mwaminifu wa nyumbani. Lakini je, ulinganisho huo wenye kutweza unafaa kweli? Biblia huwasilisha wazo sawa na hilo kwa njia yenye kuvutia zaidi na yenye heshima. Inawalinganisha wafuasi watiwa-mafuta 144,000 wa Yesu na “bibi-arusi aliyerembwa kwa ajili ya mume wake.”—Ufunuo 21:2.
16 Vielezi vinakuwa na matokeo zaidi vinapohusu maisha ya watu. Kielezi cha Nathani cha mwana-kondoo aliyechinjwa kilimgusa Mfalme Daudi kwa sababu aliwapenda kondoo, kwa kuwa ujanani mwake alitumikia akiwa mchungaji. (1 Samweli 16:11-13; 2 Samweli 12:1-7) Ikiwa kielezi hicho kingehusisha fahali, huenda hakingekuwa na matokeo sawa na hayo. Kwa njia hiyohiyo, vielezi vinavyotegemea matukio ya kisayansi au matukio ya kihistoria yasiyoeleweka vizuri huenda visiwe na umuhimu mkubwa kwa wasikilizaji wetu. Yesu alitumia vielezi vilivyohusu maisha ya kila siku. Alisema juu ya vitu vya kawaida kama vile taa, ndege wa angani na yungiyungi wa kondeni. (Mathayo 5:15, 16; 6:26, 28) Wasikilizaji wa Yesu wangeweza kuvielewa vitu hivyo kwa urahisi.
17. (a) Twaweza kutegemeza vielezi vyetu juu ya nini? (b) Twaweza kufanyaje ili vielezi vilivyotumiwa katika vichapo vyetu vibadilikane ili kufaa hali za wanafunzi wetu?
17 Katika huduma yetu, tuna fursa nyingi za kutumia vielezi sahili lakini vyenye matokeo. Uwe mwenye utambuzi. (Matendo 17:22, 23) Labda kielezi chaweza kutegemea watoto wa msikilizaji, nyumba yake, kazi yake, au hobi yake. Au twaweza kutumia ujuzi wetu wa kibinafsi juu ya mwanafunzi wa Biblia ili kuboresha vielezi ambavyo tayari tumeandaliwa katika habari za funzo. Kwa mfano, chukua kielezi chenye matokeo kilichotumiwa katika fungu la 14 la sura ya 8 katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kinahusu mzazi mwenye upendo ambaye anachongewa na jirani. Twaweza kufikiria jinsi tunavyoweza kukibadilisha kielezi hicho ili kifae hali za mwanafunzi wa Biblia ambaye ni mzazi vilevile.
Kusoma Maandiko kwa Ustadi
18. Kwa nini twapaswa kujitahidi kuwa wasomaji wenye ufasaha?
18 Paulo alimhimiza sana Timotheo hivi: “Endelea kujitahidi mwenyewe kusoma mbele ya watu wote, kuhimiza kwa bidii, kufundisha.” (1 Timotheo 4:13) Kwa kuwa Biblia ndiyo msingi wa ufundishaji wetu, inanufaisha kuweza kuisoma kwa ufasaha. Walawi walikuwa na pendeleo la kusomea watu wa Mungu Sheria ya Kimusa. Je, walibabaika walipokuwa wakisoma au walisoma kwa sauti isiyosisimua? La, Biblia yasema hivi kwenye Nehemia 8:8: “Wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, hata wakayafahamu yaliyosomwa.”
19. Twaweza kuboreshaje usomaji wetu wa Maandiko?
19 Baadhi ya wanaume Wakristo ambao ni wasemaji wenye ufasaha hushindwa inapofika wakati wa kusoma. Wanaweza kufanyaje maendeleo? Kwa kujizoeza. Naam, kwa kusoma kwa sauti kubwa tena na tena mpaka waweze kufanya hivyo kwa ufasaha. Ikiwa kaseti za usomaji wa Biblia zapatikana katika lugha yako, ni jambo la hekima kusikiliza namna msomaji anavyokazia maana na kubadilisha sauti na kusikiliza jinsi ambavyo majina na maneno yasiyo ya kawaida yanavyotamkwa. Kwa kufanya mazoezi, hata majina kama vile Maher-shalal-hash-bazi yaweza kusomwa kwa utulivu wenye kiasi.—Isaya 8:1.
20. Twawezaje ‘kukaza uangalifu kwa kufundisha kwetu’?
20 Tukiwa watu wa Yehova, tuna pendeleo lililoje kutumiwa tukiwa walimu! Basi, acheni kila mmoja wetu achukue daraka hilo kwa uzito. Acheni ‘daima tukaze uangalifu kwetu wenyewe na kwa kufundisha kwetu.’ (1 Timotheo 4:16) Twaweza kuwa walimu wazuri tukiwa wasikilizaji wazuri, kwa kuweka mambo yakiwa sahili, kwa kuuliza maswali ya ufahamu wenye kina, kwa kutumia vielezi vyenye matokeo, na kwa kusoma maandiko kwa ustadi. Sisi sote na tupate faida kutokana na mazoezi yanayoandaliwa na Yehova kupitia tengenezo lake, kwa kuwa hayo yaweza kutusaidia kuwa na ‘ulimi wa hao waliofundishwa.’ (Isaya 50:4) Tukitumia kikamili vifaa vyote ambavyo tumeandaliwa kwa ajili ya huduma yetu, kutia ndani broshua, kaseti za usomaji wa Biblia na kaseti za video, twaweza kujifunza kufundisha kwa ufahamu wenye kina na ushawishi.
-