-
‘Weka Moyoni Mwako’ Hekalu la Mungu!Mnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
-
-
15. (a) Hekalu la kiroho la Yehova lilianza kutenda lini? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba ono la Ezekieli halikutimizwa wakati wa maisha ya Kristo duniani?
15 Kwa wazi, lazima tutafute utimizo mkubwa wa ono la Ezekieli katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova, ambalo mtume Paulo azungumzia kwa urefu katika kitabu cha Waebrania. Hekalu hilo lilianza kutenda wakati Yesu Kristo alipotiwa mafuta awe Kuhani wa Cheo cha Juu wake mwaka wa 29 W.K. Lakini je, ono la Ezekieli lilitimizwa katika siku ya Yesu? Yaonekana sivyo. Yesu, akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu, alitimiza maana ya kiunabii ya Siku ya Kufunika kupitia ubatizo wake, kifo chake cha kidhabihu, na kuingia kwake ndani ya Patakatifu Zaidi Sana, mbinguni kwenyewe. (Waebrania 9:24) Hata hivyo, kwa kupendeza, ono la Ezekieli halitaji kamwe lolote kuhusu kuhani wa cheo cha juu au Siku ya Kufunika. Hivyo, haielekei kuwa ono hilo lilikuwa likielekeza kwenye karne ya kwanza W.K. Basi, ono hilo linahusu kipindi kipi cha wakati?
16. Mandhari ya ono la Ezekieli yatukumbusha juu ya unabii gani mwingine, na hilo latusaidiaje kuutambua wakati wa utimizo mkubwa wa ono la Ezekieli?
16 Ili kupata jibu, acheni tulirudie ono lenyewe. Ezekieli aliandika: “Katika maono ya Mungu alinileta mpaka nchi ya Israeli, akaniweka juu ya mlima mrefu sana, ambao juu yake palikuwapo kana kwamba ni umbo la mji upande wa kusini.” (Ezekieli 40:2) Mandhari ya ono hilo, ambayo ni “mlima mrefu sana,” hutukumbusha juu ya Mika 4:1: “Itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi.” Unabii huo waanza kutimizwa wakati gani? Mika 4:5 huonyesha kwamba huo waanza kutimizwa mataifa yakiwa yangali yanaabudu miungu isiyo ya kweli. Kwa kweli, imetimizwa wakati wetu wenyewe, “siku za mwisho,” ambapo ibada safi imeinuliwa juu, imerudishwa mahali pake panapofaa maishani mwa watumishi wa Mungu.
17. Unabii wa Malaki 3:1-5 watusaidiaje kutambua wakati hekalu la ono la Ezekieli liliposafishwa?
17 Ni nini kilichofanya hali hiyo ya kurudishwa iwezekane? Kumbuka, katika tukio muhimu zaidi katika ono la Ezekieli, Yehova aja kwenye hekalu na kusisitiza kwamba nyumba yake isafishwe kwa kuondolewa ibada ya sanamu. Hekalu la Mungu la kiroho lilisafishwa lini? Kwenye Malaki 3:1-5, Yehova atabiri juu ya wakati ambapo “atalijilia hekalu lake” akiandamana na “mjumbe [wake] wa agano,” Yesu Kristo. Kwa kusudi gani? ‘Yeye atakuwa mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, na kama mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo.’ Kusafishwa huko kulianza wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza. Tokeo lilikuwa nini? Yehova amekaa katika nyumba yake na kubariki nchi ya kiroho ya watu wake kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea. (Isaya 66:8) Basi, twaweza kukata kauli kwamba unabii wa hekalu wa Ezekieli unapata utimizo muhimu wakati wa siku za mwisho.
-
-
‘Weka Moyoni Mwako’ Hekalu la Mungu!Mnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
-
-
Ono Hilo Hukazia Siku Yetu Wenyewe
19, 20. Kwa nini ni lazima utimizo mkuu wa ono hilo utukie leo, wala si katika Paradiso?
19 Ezekieli aliona hekalu lililohitaji kusafishwa liondolewe ibada ya sanamu na uasherati wa kiroho. (Ezekieli 43:7-9) Hilo kwa kweli halingeweza kutumika kuhusu ibada ya Yehova katika Paradiso. Na zaidi, makuhani katika ono hilo hufananisha jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta wakiwa wangali duniani, wala si baada ya ufufuo wao wa kimbingu au wakati wa kipindi cha Milenia. Kwa nini? Ona kwamba makuhani hao wanaonyeshwa wakitumikia katika ua wa ndani. Makala katika Mnara wa Mlinzi yameonyesha kwamba ua huo hufananisha ule msimamo wa kipekee ambao makuhani wa cheo cha chini wa Kristo wanao wakiwa wangali duniani.c Pia ona kwamba ono hilo hukazia kutokamilika kwa makuhani hao. Wanaambiwa watoe dhabihu kwa ajili ya dhambi zao wenyewe. Wanaonywa juu ya hatari ya kuwa wachafu—kiroho na kiadili. Kwa hivyo, hawafananishi wale watiwa-mafuta waliofufuliwa, ambao mtume Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Tarumbeta itavuma, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioharibika.” (1 Wakorintho 15:52; Ezekieli 44:21, 22, 25, 27) Makuhani katika ono hilo huchangamana na kutumikia watu moja kwa moja. Haitakuwa hivyo katika Paradiso, wakati jamii ya kikuhani itakuwa mbinguni. Kwa hiyo, ono hilo hutoa mfano bora kabisa wa jinsi ambavyo watiwa-mafuta hufanya kazi kwa ukaribu na “umati mkubwa” ulio duniani leo.—Ufunuo 7:9; Ezekieli 42:14.
20 Hivyo, ono la Ezekieli la hekalu huashiria matokeo yenye mafaa yanayoletwa na usafishaji wa kiroho unaotimizwa leo. Lakini hilo lamaanisha nini kwako? Hilo sio fumbo tu la kitheolojia lisilokuhusu. Ono hilo lina mengi zaidi yanayohusu ibada yako ya siku kwa siku ya kumwabudu Mungu wa pekee wa kweli, Yehova. Tutaona jinsi jambo hilo lilivyo katika makala yetu inayofuata.
-
-
Lile “Hekalu” na Yule “Mkuu” LeoMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
-
-
Lile “Hekalu” na Yule “Mkuu” Leo
“Na mukubwa [“mkuu,” “Union Version”], wakati wanapoingia, ataingia katikati yao; na wakati wanapotoka, watatoka pamoja.” —EZEKIELI 46:10, Zaire Swahili Bible.
1, 2. Ni ukweli gani muhimu unaotuwezesha kuelewa maana nyingi ya ono la Ezekieli la hekalu?
MARABI fulani wa zamani hawakuridhika kabisa na kitabu cha Ezekieli. Kulingana na Talmud, baadhi yao hata walifikiria juu ya kukiondoa kabisa kutoka kwa orodha ya Maandiko Matakatifu yaliyokubalika. Ilikuwa vigumu kwao kueleza maana ya hilo ono la hekalu na wakatangaza kwamba hakuna mwanadamu angeweza kulielewa. Wasomi wengine wa Biblia wametatanishwa na ono hilo la Ezekieli la hekalu la Yehova. Vipi sisi?
2 Tangu kurudishwa kwa ibada safi, Yehova amewabariki watu wake kwa mimweko mingi ya ufahamu wa kiroho, kutia ndani kutambua maana ya hekalu la Mungu la kiroho ni nini—mpango wa kihekalu wa Yehova kwa ajili ya ibada safi.a Ukweli huu muhimu hutuwezesha kuelewa kwa kadiri kubwa maana ya ono la Ezekieli la hekalu. Acheni tuchunguze kwa makini sehemu nne za ono hilo—hekalu, ukuhani, mkuu, na nchi. Hizo zamaanisha nini leo?
Lile Hekalu na Wewe
3. Twajifunza nini kutokana na dari refu na michoro iliyo ukutani katika vijia vya kuingia hekaluni?
3 Wazia kwamba tunazuru hekalu hilo la kimaono. Twakaribia na kupanda vipandio saba hadi kwenye moja la hayo malango makubwa mno. Tukiwa ndani ya kijia hicho cha kuingilia, twatazama juu kwa kuduwaa. Dari lake lina urefu wa meta 30 kwenda juu! Hivyo, twakumbushwa kwamba viwango vya kuingia katika mpango wa Yehova wa ibada ni vya juu sana. Miali ya nuru inayopenyeza kutoka madirishani yamulika michoro ya mitende iliyo ukutani, ambayo hutumiwa katika Maandiko kufananisha unyofu. (Zaburi 92:12; Ezekieli 40:14, 16, 22) Mahali hapo patakatifu ni pa wale walio wanyofu kiadili na kiroho. Kwa kupatana na hilo, twataka kubaki tukiwa wanyofu ili ibada yetu ikubalike kwa Yehova.—Zaburi 11:7.
4. Ni nani wanaozuiwa kuingia hekaluni, na hilo latufunza nini?
4 Kando-kando ya pande zote za kijia hicho, pana vyumba vitatu vya walinzi. Je, hao walinzi wataturuhusu tuingie ndani ya hekalu? Yehova amwambia Ezekieli kwamba hapana mgeni ambaye “moyo wake haukutahiriwa” awezaye kuingia. (Ezekieli 40:10; 44:9) Hilo lamaanisha nini? Lamaanisha kwamba Mungu hukubali tu wale wanaopenda sheria zake na kuishi kulingana nazo wamwabudu. (Yeremia 4:4; Waroma 2:29) Yeye huwakaribisha watu wa aina hiyo katika hema lake la kiroho, nyumba yake ya ibada. (Zaburi 15:1-5) Tangu ibada safi irudishwe mwaka wa 1919, tengenezo la kidunia la Yehova limetegemeza na kufafanua sheria zake za adili hatua kwa hatua. Wale wanaokataa kutii kimakusudi hawakubaliwi tena kushirikiana na watu wake. Leo, lile zoea linalotegemea Biblia la kutenga na ushirika wakosaji wasiotubu limesaidia kudumisha ibada yetu ikiwa safi na yenye utakato.—1 Wakorintho 5:13.
5. (a) Ni ufanano gani uliopo kati ya ono la Ezekieli na ono la Yohana ambalo limerekodiwa kwenye Ufunuo 7:9-15? (b) Katika ono la Ezekieli, makabila 12 yanayoabudia kwenye ua wa nje yafananisha nani?
5 Kijia hicho chaelekeza kwenye ua wa nje ambapo watu wamwabudu na kumsifu Yehova. Hilo latukumbusha juu ya ono la mtume Yohana la “umati mkubwa” ukimwabudu Yehova “mchana na usiku katika hekalu lake.” Mitende yaonyeshwa katika maono yote mawili. Katika ono la Ezekieli hiyo yapamba kuta za kijia cha kuingilia. Katika ono la Yohana waabudu wana matawi ya mitende mikononi mwao, ikionyesha shangwe yao katika kumsifu Yehova na kumkaribisha Yesu akiwa Mfalme wao. (Ufunuo 7:9-15) Katika muktadha wa ono la Ezekieli, yale makabila 12 ya Israeli yafananisha “kondoo wengine.” (Yohana 10:16; linganisha Luka 22:28-30.) Je, wewe ni mmoja wa wale wanaopata shangwe katika kumsifu Yehova kwa kutangaza Ufalme wake?
6. Kusudi la vyumba vya kulia vilivyo katika ua wa nje lilikuwa nini, na hilo laweza kuwakumbusha wale wa kondoo wengine kuhusu pendeleo jipi?
6 Tunapozuru ua wa nje, twaona vyumba vya kulia 30 ambamo watu wanashiriki kula matoleo yao ya hiari. (Ezekieli 40:17) Leo, wale walio miongoni mwa kondoo wengine hawatoi dhabihu za wanyama, lakini hawaji kwenye hekalu la kiroho mikono mitupu. (Linganisha Kutoka 23:15.) Mtume Paulo aliandika: “Kupitia [Yesu] acheni sikuzote tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani. Zaidi ya hayo, msisahau kule kutenda mema na kule kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana kwa dhabihu za namna hiyo Mungu hupendezwa vema.” (Waebrania 13:15, 16; Hosea 14:2) Ni pendeleo kubwa kumtolea Yehova dhabihu kama hizo.—Mithali 3:9, 27.
7. Kupimwa kwa hekalu hutupa uhakikisho juu ya nini?
7 Ezekieli atazama malaika alipimapo hekalu hilo la kimaono. (Ezekieli 40:3) Vivyo hivyo, mtume Yohana aliambiwa: “Inuka upime patakatifu pa hekalu la Mungu na madhabahu na wale wanaoabudu ndani yalo.” (Ufunuo 11:1) Kupima huko kwamaanisha nini? Katika visa vyote viwili yaonekana hilo lilikuwa uhakikisho kamili, ishara kwamba hapana chochote kiwezacho kumzuia Yehova asitimize makusudi yake yanayohusu ibada safi. Vivyo hivyo leo, twaweza kuhakikishiwa kwamba hakuna chochote—hata upinzani mkali kutoka kwa serikali zenye nguvu—kiwezacho kuzuia kurudishwa kwa ibada safi.
8. Ni nani waingiao malango yanayoelekea kwenye ua wa ndani, na malango hayo yatukumbusha nini?
8 Tunapotembea kuvuka ua wa nje, huenda tukaona kwamba kuna malango matatu ya kuingia kwenye ua wa ndani; malango ya ndani yako kwenye mpangilio mmoja na malango ya nje, nayo ni yenye kipimo kimoja na hayo ya nje. (Ezekieli 40:6, 20, 23, 24, 27) Ni makuhani tu wanaoweza kuingia katika ua wa ndani. Malango ya ndani yatukumbusha kwamba ni lazima watiwa-mafuta wafikie viwango na sheria za kimungu, viwango na sheria hizohizo huwaongoza Wakristo wote wa kweli. Lakini kazi ya makuhani ni nini, nayo yamaanisha nini leo?
Ukuhani Mwaminifu
9, 10. “Ukuhani wa kifalme,” kama ulivyotangulia kuonyeshwa na jamii ya kikuhani katika ono la Ezekieli, umetoa ufundishaji wa kiroho jinsi gani?
9 Katika nyakati za kabla ya Ukristo, makuhani walifanya kazi ngumu hekaluni. Kazi ya kuchinja wanyama wa dhabihu, kuwatoa kwenye madhabahu, na kuwatumikia makuhani wenzao na watu ilikuwa yenye kuchosha sana. Lakini walikuwa na kazi nyingine muhimu. Yehova aliamuru hivi kuhusu makuhani hao: “Watawafundisha watu wangu tofauti iliyopo kati ya vitu vitakatifu na vitu vya sikuzote [“vichafu,” NW], na kuwafundisha kupambanua kati ya yaliyo machafu na yaliyo safi.”—Ezekieli 44:23; Malaki 2:7.
10 Je, unathamini kazi ngumu na utumishi mnyenyekevu ambao watiwa-mafuta wakiwa kikundi, “ukuhani wa kifalme,” wamefanya kwa ajili ya ibada safi? (1 Petro 2:9) Kama ukuhani wa Kilawi wa zamani, wameongoza katika kutoa mafundisho ya kiroho, wakisaidia watu kuelewa kile ambacho ni safi na chenye kukubalika machoni pa Mungu na kile ambacho si safi na kisichokubalika. (Mathayo 24:45) Mafundisho hayo, yanayotolewa kupitia vichapo vinavyotegemea Biblia na mikutano ya Kikristo na mikusanyiko, yamewasaidia mamilioni ya watu kupatanishwa na Mungu.—2 Wakorintho 5:20.
11. (a) Ono la Ezekieli lilikaziaje umuhimu wa usafi kwa makuhani? (b) Katika siku za mwisho, watiwa-mafuta wamesafishwaje katika maana ya kiroho?
11 Hata hivyo, ni lazima makuhani wafanye mengi zaidi ya kufundisha wengine wawe safi; ni lazima wao wenyewe wawe safi. Hivyo basi, Ezekieli aliona kimbele hatua ya kusafishwa kwa ukuhani wa Israeli. (Ezekieli 44:10-16) Vivyo hivyo, historia yaonyesha kwamba mwaka wa 1918, Yehova aliketi “kama asafishaye” katika hekalu lake la kiroho, akiichunguza jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta. (Malaki 3:1-5) Wale walioonwa kuwa safi kiroho au waliotubu kuhusu ibada yao ya sanamu ya hapo awali, waliruhusiwa kuendelea na pendeleo la utumishi katika hekalu lake la kiroho. Na bado, sawa na watu wale wengine wote, watiwa-mafuta wakiwa mtu mmoja-mmoja wanaweza kuwa wachafu—kiroho na kiadili. (Ezekieli 44:22, 25-27) Imewalazimu kujitahidi sana ili kubaki “bila doa kutokana na ulimwengu.”—Yakobo 1:27; linganisha Marko 7:20-23.
12. Kwa nini twapaswa kuthamini kazi ya watiwa-mafuta?
12 Kila mmoja wetu aweza kujiuliza, ‘Je, ninathamini kielelezo kilichowekwa na watiwa-mafuta kwa miaka mingi ya utumishi wao mwaminifu? Je, ninaiga imani yao?’ Ni vizuri kwa wale wa umati mkubwa kukumbuka kwamba hawatakuwa na watiwa-mafuta sikuzote hapa duniani. Yehova alisema hivi kuhusu makuhani katika ono la Ezekieli: “Wala hamtawapa milki [ya nchi] iwayo yote katika Israeli; mimi ni milki yao.” (Ezekieli 44:28) Vivyo hivyo, watiwa-mafuta hawana sehemu yoyote yenye kudumu milele hapa duniani. Wao wana urithi wa kimbingu, na wale wa umati mkubwa huliona kuwa pendeleo kuwaunga mkono na kuwatia moyo wakiwa wangali hapa duniani.—Mathayo 25:34-40; 1 Petro 1:3, 4.
Yule Mkuu—Yeye Ni Nani?
13, 14. (a) Ni kwa nini yule mkuu lazima awe mmoja wa kondoo wengine? (b) Mkuu hufananisha nani?
13 Sasa swali lenye kuamsha udadisi lazuka. Basi, mkuu huyo anawakilisha nani? Kwa kuwa yeye huzungumziwa akiwa kama mtu mmoja na vilevile kama kikundi, twaweza kukata kauli kwamba anawakilisha jamii ya watu. (Ezekieli 44:3; 45:8, 9) Lakini watu gani? Kwa hakika si watiwa-mafuta. Katika ono hilo, yeye anafanya kazi kwa kushirikiana na ukuhani, lakini yeye si mmoja wao. Tofauti na jamii ya kikuhani, yeye apewa urithi katika nchi hiyo na kwa hiyo wakati wake ujao upo hapa duniani, wala si mbinguni. (Ezekieli 48:21) Na zaidi, Ezekieli 46:10 (ZSB), lasema: “Na mukubwa [“mkuu,” UV], wakati wanapoingia [yale makabila yasiyo ya kikuhani yanapoingia kwenye ua wa nje wa hekalu], ataingia katikati yao; na wakati wanapotoka, watatoka pamoja.” Yeye haingii katika ua wa ndani bali huabudia katika ua wa nje, akiingia na kutoka hekaluni pamoja na hao watu. Kwa wazi mambo hayo ya hakika humweka mkuu huyo miongoni mwa umati mkubwa wa kondoo wengine.
14 Kwa wazi, mkuu huyo ana daraka fulani miongoni mwa watu wa Mungu. Katika ua wa nje, yeye aketi katika ukumbi wa Lango la Mashariki. (Ezekieli 44:2, 3) Hilo lingeonyesha cheo cha uangalizi, kinachofanana na kile cha wanaume wazee katika Israeli walioketi kwenye lango la jiji na kutoa hukumu. (Ruthu 4:1-12; Mithali 22:22) Ni nani miongoni mwa kondoo wengine walio na vyeo vya uangalizi leo? Ni wazee walio na tumaini la kidunia ambao wamewekwa rasmi na roho takatifu. (Matendo 20:28) Hivyo, jamii ya mkuu sasa inatayarishwa kwa tazamio la kutumikia baadaye katika cheo cha usimamizi katika ulimwengu mpya.
15. (a) Ono la Ezekieli hutufafanuliaje uhusiano uliopo baina ya wazee ambao ni wa umati mkubwa na jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta? (b) Wazee watiwa-mafuta wamechukua uongozi upi katika tengenezo la Mungu la kidunia?
15 Lakini je, ni uhusiano gani uliopo baina ya jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta na wanaume wazee hao ambao, wakiwa sehemu ya umati mkubwa, wanatumikia katika vyeo vya usimamizi? Ono la Ezekieli ladokeza kwamba fungu la wazee hao walio washiriki wa umati mkubwa ni la chini na la kuunga mkono, huku watiwa-mafuta wakichukua uongozi wa kiroho. Jinsi gani? Kumbuka, makuhani katika ono hilo walipewa daraka la kufundisha watu mambo ya kiroho. Pia waliambiwa watumikie wakiwa mahakimu katika kesi za kisheria. Kwa kuongezea, Walawi walipewa kazi ya kuwa “wasimamizi” katika malango ya hekalu. (Ezekieli 44:11, 23, 24) Kwa wazi, mkuu huyo alipaswa kujitiisha kwa utumishi wa kiroho na uongozi wa hao makuhani. Basi, inafaa kwamba katika nyakati za kisasa watiwa-mafuta wamechukua uongozi katika ibada safi. Kwa mfano, washiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova wamechaguliwa kutoka miongoni mwao. Wazee hao waaminifu, watiwa-mafuta, wamekuwa wakiizoeza kwa makumi ya miaka jamii ya mkuu huyo inayokua. Washiriki hao wa Baraza Linaloongoza wanawatayarisha wale wanaotazamia kuwa washiriki wa jamii hii kwa ajili ya siku watakapoachiwa mamlaka kamili ya madaraka yao katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja.
16. Kulingana na Isaya 32:1, 2, ni lazima wazee wote watendeje?
16 Je, hawa wanaotazamia kuwa washiriki, ambao wako katika mstari wa kupata madaraka yaliyoongezeka wakiwa kama jamii ya mkuu, ni waangalizi wa aina gani? Unabii ulio kwenye Isaya 32:1, 2 wasema hivi: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu [“wana-wafalme,” NW] watatawala kwa hukumu. Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” Unabii huo unatimizwa sasa, wazee Wakristo—watiwa-mafuta na kondoo wengine—wanapofanya kazi ili kulinda kundi dhidi ya “dhoruba” kama vile mnyanyaso na kuvunjika moyo.
17. Wachungaji Wakristo wapaswa kujionaje, na kundi lapaswa kuwaonaje?
17 Maneno “mwana-mfalme” na “mkuu,” ambayo yana maana sawa katika lugha ya Kiebrania, hayatumiwi kama majina ya vyeo vinavyokusudiwa kuwatukuza wanadamu. Badala yake, yanafafanua daraka ambalo wanaume hawa wanalo katika kutunza kondoo za Mungu. Yehova aonya kwa ukali hivi: “Na iwatoshe ninyi, enyi wakuu wa Israeli; ondoeni dhuluma na unyang’anyi; fanyeni hukumu na haki.” (Ezekieli 45:9) Yafaa wazee wote leo wazingatie shauri hilo. (1 Petro 5:2, 3) Kwa upande mwingine, kundi hutambua kwamba Yesu ameandaa wachungaji, ambao ni “zawadi zikiwa wanadamu.” (Waebrania 4:8) Sifa zao za ustahili zimeandikwa katika Neno la Mungu mwenyewe lililopuliziwa. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Hivyo basi, Wakristo hufuata mwongozo wa wazee.—Waebrania 13:7.
18. Ni nini baadhi ya madaraka ya wale wanaotazamia kuwa jamii ya mkuu sasa, na wakati ujao daraka lake litakuwa nini?
18 Katika nyakati za Biblia wakuu fulani walikuwa na uwezo mkubwa, na wengine uwezo mdogo. Leo, wazee wa ule umati mkubwa wana madaraka mengi mbalimbali. Baadhi yao hutumikia kutaniko moja; wengine hutumikia makutaniko mengi wakiwa waangalizi wasafirio; wengine hutumikia nchi nzimanzima wakiwa washiriki wa Halmashauri ya Tawi; wengine husaidia moja kwa moja halmashauri mbalimbali za Baraza Linaloongoza. Katika ulimwengu mpya, Yesu ataweka rasmi “wakuu katika nchi zote” ili waongoze miongoni mwa waabudu wa Yehova duniani. (Zaburi 45:16) Yaelekea atateua wengi wao kutoka miongoni mwa wazee waaminifu wa siku hizi. Kwa kuwa hawa wanaume wanajithibitisha wenyewe sasa, ataamua kuwakabidhi wengi mapendeleo makubwa zaidi wakati ujao anapofunua daraka la jamii ya mkuu katika ulimwengu mpya.
Nchi ya Watu wa Mungu Leo
19. Nchi iliyo kwenye ono la Ezekieli huwakilisha nini?
19 Pia, ono la Ezekieli laonyesha nchi iliyorudishwa ya Israeli. Sehemu hii ya ono huwakilisha nini? Unabii mwingine mbalimbali wa urudisho ulitabiri kwamba nchi hiyo, Israeli, ingekuwa paradiso kama Edeni. (Ezekieli 36:34, 35) Leo, twafurahia “nchi” iliyorudishwa, na hii pia ni ya Kiedeni kwa njia fulani. Vivyo hivyo, mara nyingi sisi husema juu ya paradiso yetu ya kiroho. Gazeti la Mnara wa Mlinzi limefafanua “nchi” yetu kuwa “eneo la utendaji” la watu wa Mungu waliochaguliwa.b Kokote ambako huenda mtumishi wa Yehova yuko, yeye yumo katika nchi hiyo iliyorudishwa maadamu anajitahidi kutegemeza ibada ya kweli kwa kutembea katika hatua za Kristo Yesu.—1 Petro 2:21.
20. Twaweza kujifunza kanuni ipi kutokana na “toleo takatifu” kwenye ono la Ezekieli, nasi huenda tukaitumiaje kanuni hii?
20 Vipi juu ya sehemu ya nchi iitwayo “toleo takatifu”? Hiyo ilikuwa toleo la watu ili kutegemeza ukuhani na jiji. Vivyo hivyo, “watu wote wa nchi” wangepaswa kutoa sehemu ya nchi kwa ajili ya mkuu. Hilo lamaanisha nini leo? Bila shaka, halimaanishi kwamba watu wa Mungu watwikwe mzigo wa kulipa jamii ya makasisi mshahara. (2 Wathesalonike 3:8) Badala yake, utegemezo unaotolewa kwa wazee hasa ni wa kiroho. Unatia ndani kusaidia katika kazi iliyopo na kuonyesha roho ya ushirikiano, na ya kujitiisha. Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika siku ya Ezekieli, toleo hili hutolewa “kwa BWANA [“Yehova,” NW], wala si kwa mwanadamu yeyote.—Ezekieli 45:1, 7, 16.
21. Huenda tukajifunza nini kutokana na kugawanywa kwa nchi katika ono la Ezekieli?
21 Si mkuu na makuhani pekee waliogawiwa mahali katika nchi hiyo iliyorudishwa. Kugawanywa kwa nchi kwaonyesha kwamba kila moja la yale makabila 12 lina urithi ulio salama. (Ezekieli 47:13, 22, 23) Hivyo, wale wa umati mkubwa wana sehemu katika paradiso ya kiroho iliyopo sasa na pia watagawiwa nchi watakaporithi sehemu katika eneo la kidunia la Ufalme wa Mungu.
22. (a) Jiji kwenye ono la Ezekieli huwakilisha nini? (b) Ni nini tunachoweza kujifunza kutokana na jiji kuwa na malango pande zote?
22 Hatimaye, jiji kwenye ono hilo huwakilisha nini? Hilo si jiji la kimbingu, kwa kuwa limo katikati mwa sehemu ya nchi “chafu” (isiyo takatifu). (Ezekieli 48:15-17, NW) Hivyo, ni lazima liwe la kidunia. Naam, jiji ni nini? Je, hilo halitoi wazo la watu kuja pamoja wakiwa kikundi na kufanyiza kitu fulani kilichoundwa na kilichopangwa kitengenezo? Ndiyo. Hivyo, yaonekana jiji hilo hufananisha usimamizi wa kidunia unaowafaidi wote watakaofanyiza jamii yenye uadilifu ya kidunia. Jiji hilo litatenda kikamilifu katika “dunia mpya” itakayokuja. (2 Petro 3:13) Malango yaliyo pande zote za jiji hilo, moja kwa kila kabila, yaonyesha vizuri uwazi wa mambo. Leo, watu wa Mungu hawako chini ya usimamizi fulani wa kisiri na wa kichinichini. Ndugu walio na madaraka lazima wawe wenye kufikika; wote wanajua vizuri kanuni zinazowaongoza. Uhakika wa kwamba watu kutoka makabila yote hulima shamba linalotegemeza jiji hilo hutukumbusha kwamba kondoo wengine huunga mkono, hata kwa njia ya kimwili, mipango ya usimamizi ambayo imefanywa kwa ajili ya watu wa Mungu ulimwenguni pote.—Ezekieli 48:19, 30-34.
23. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?
23 Lakini, vipi juu ya mto unaotiririka kutoka patakatifu pa hekalu? Kile ambacho huo huwakilisha leo na wakati ujao ndilo litakalokuwa jambo kuu la makala ya tatu na ya mwisho katika mfululizo huu.
-
-
Baraka ya Yehova Juu ya “Nchi” YetuMnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
-
-
Baraka ya Yehova Juu ya “Nchi” Yetu
“Kila kitu kitaishi po pote utakapofikilia mto huo.”—EZEKIELI 47:9.
1, 2. (a) Maji yana umuhimu gani? (b) Maji kwenye mto wa kimaono wa Ezekieli hufananisha nini?
MAJI ni kitu cha ajabu. Uhai wote duniani huyategemea. Hakuna yeyote kati yetu awezaye kuishi kwa muda mrefu bila maji. Pia twayatumia kwa kusafisha, kwa kuwa maji yaweza kufyonza na kuondolea mbali uchafu. Hivyo, sisi hutumia maji kuogea, kufulia nguo, na hata kuoshea vyakula. Kufanya hivyo kwaweza kuokoa uhai wetu.
2 Biblia hutumia maji kufananisha maandalizi ya Yehova ya kiroho kwa ajili ya uhai. (Yeremia 2:13; Yohana 4:7-15) Maandalizi haya yatia ndani kusafishwa kwa watu wake kupitia fidia ya dhabihu ya Kristo na ujuzi juu ya Mungu ulio katika Neno lake. (Waefeso 5:25-27) Katika ono la Ezekieli la hekalu, mto wa kimwujiza unaotiririka kutoka kwenye hekalu hufananisha baraka hizo zinazotokeza uhai. Lakini mto huo hutiririka lini, nao wamaanisha nini kwetu leo?
Mto Watiririka Katika Nchi Iliyorudishwa
3. Ezekieli aliona nini, kama ilivyoripotiwa kwenye Ezekieli 47:2-12?
3 Wakiwa mateka huko Babiloni, watu wa Ezekieli walihitaji sana maandalizi ya Yehova. Basi ilimtia Ezekieli moyo kama nini kuona mchuruziko wa maji ukitokea mahali patakatifu na kutiririka kutoka ndani ya hekalu la kimaono! Malaika fulani akipima kijito hicho baada ya kila dhiraa 1,000. Kina chake chaongezeka kutoka kifundo cha mguu hadi kufikia magotini, kutoka magotini hadi kiunoni, halafu unakuwa mto ambao mtu ahitaji kuogelea. Mto huo hutokeza uhai na mazao. (Ezekieli 47:2-11) Ezekieli aambiwa: “Na karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa chakula.” (Ezekieli 47:12a) Mto huo unapoingia Bahari ya Chumvi—maji yasiyo na uhai—uhai waanza! Samaki watokea kwa wingi. Biashara ya uvuvi yasitawi.
4, 5. Ni jinsi gani unabii wa Yoeli unaohusu mto unafanana na ule wa Ezekieli, na kwa nini hilo ni muhimu?
4 Huenda unabii huo mzuri uliwakumbusha Wayahudi wahamishwa unabii mwingine uliorekodiwa zaidi ya karne mbili mapema: “Chemchemi itatokea katika nyumba ya BWANA, na kulinywesha bonde la Shitimu.”a (Yoeli 3:18) Unabii wa Yoeli, kama ulivyo wa Ezekieli, unatabiri kwamba mto ungetiririka kutoka kwenye nyumba ya Mungu, lile hekalu, na kutokeza uhai katika eneo la ukame.
5 Kwa muda mrefu gazeti Mnara wa Mlinzi limeeleza kwamba unabii wa Yoeli unatimizwa siku zetu.b Kwa hakika basi, iko vivyo hivyo kwa habari ya ono la Ezekieli linalofanana na unabii huo. Katika nchi iliyorudishwa ya watu wa Mungu leo, kama tu katika Israeli la kale, baraka za Yehova zimetiririka kwelikweli.
Mtiririko Mkubwa wa Baraka
6. Kunyunyizwa kwa damu katika madhabahu ya kimaono kulipaswa kuwakumbusha Wayahudi juu ya nini?
6 Ni nini chanzo cha baraka ambazo watu wa Mungu waliorudishwa wanazo? Naam, ona kwamba maji hayo hutiririka kutoka hekalu la Mungu. Vivyo hivyo leo, baraka hizo huja kutoka kwa Yehova kupitia hekalu lake kubwa la kiroho—mpango kwa ajili ya ibada safi. Ono la Ezekieli laongezea jambo fulani muhimu. Katika ua wa ndani, kijito hicho chatiririka kupitia kusini mwa madhabahu. (Ezekieli 47:1) Madhabahu imo katikati hasa mwa hekalu hilo la kimaono. Yehova amfafanulia Ezekieli kwa makini kuihusu na aamuru kwamba damu ya dhabihu inyunyizwe juu yake. (Ezekieli 43:13-18, 20) Madhabahu hiyo ilikuwa na maana kubwa sana kwa Waisraeli wote. Agano lao na Yehova lilikuwa limehalalishwa muda mrefu mapema wakati Musa aliponyunyiza damu juu ya madhabahu iliyokuwa chini ya Mlima Sinai. (Kutoka 24:4-8) Kunyunyizwa kwa damu juu ya madhabahu hiyo ya kimaono kulipaswa kuwakumbusha kwamba mara warudipo kwenye nchi yao iliyorudishwa, baraka za Yehova zingetiririka maadamu wangeishi kulingana na agano lao naye.—Kumbukumbu la Torati 28:1-14.
7. Wakristo leo wanapata maana gani katika madhabahu ya ufananisho?
7 Hali kadhalika, watu wa Mungu leo wanabarikiwa kupitia agano—lililo bora, agano jipya. (Yeremia 31:31-34) Hilo pia lilihalalishwa muda mrefu uliopita kwa damu ya Yesu Kristo. (Waebrania 9:15-20) Leo, tuwe miongoni mwa watiwa-mafuta, ambao ni washiriki wa agano hilo, au miongoni mwa “kondoo wengine,” ambao wanafaidika kutokana nalo, twapata maana kubwa katika madhabahu hiyo ya mfano. Hiyo hufananisha mapenzi ya Mungu kuhusiana na dhabihu ya Kristo. (Yohana 10:16; Waebrania 10:10) Kama tu vile madhabahu hiyo ya ufananisho imo katikati hasa mwa hekalu la kiroho, dhabihu ya fidia ya Kristo ni ya umuhimu mkubwa katika ibada safi. Hiyo ndiyo msingi wa msamaha wa dhambi zetu na kwa sababu hiyo, dhabihu hiyo inakuwa pia msingi wa matumaini yetu yote ya wakati ujao. (1 Yohana 2:2) Hivyo, twajitahidi kuishi kulingana na sheria inayohusishwa na hilo agano jipya, “sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Maadamu twafanya hivyo, tutafaidika kutokana na maandalizi ya Yehova ya uhai.
8. (a) Ni nini ambacho ua wa ndani wa hekalu la kimaono ulikosa? (b) Makuhani kwenye hekalu la kimaono wangejisafisha kwa njia gani?
8 Faida moja ya aina hiyo ni msimamo safi mbele za Yehova. Katika hekalu hilo la kimaono, ua wa ndani unakosa kitu fulani ambacho kilitokeza sana katika ua wa tabenakulo na katika hekalu la Solomoni—beseni kubwa, ambayo baadaye iliitwa bahari, kwa ajili ya makuhani kuogea ndani. (Kutoka 30:18-21; 2 Mambo ya Nyakati 4:2-6) Je, makuhani katika hekalu la kimaono la Ezekieli wangetumia nini kusafishia? Naam, kijito kile cha kimwujiza kinachotiririka kupitia ua wa ndani! Ndiyo, Yehova angewabariki kwa kuwawezesha kufurahia msimamo safi, au mtakatifu.
9. Ni jinsi gani watiwa-mafuta na umati mkubwa waweza kuwa na msimamo safi leo?
9 Vivyo hivyo leo, watiwa-mafuta wamebarikiwa kwa kupewa msimamo safi mbele za Yehova. Yehova huwaona kuwa watakatifu, akiwatangaza kuwa waadilifu. (Waroma 5:1, 2) Vipi juu ya “umati mkubwa,” unaofananishwa na yale makabila yasiyo ya kikuhani? Wao wanaabudia katika ua wa nje, na kijito kile kile hupitia ndani ya sehemu hiyo ya hekalu la kimaono. Basi, yafaa kama nini, kwamba mtume Yohana aliona umati mkubwa ukiwa umevaa kanzu safi nyeupe wanapoabudia katika ua wa hekalu la kiroho! (Ufunuo 7:9-14) Haidhuru wametendewa vipi katika ulimwengu huu ulioshuka kiadili, wanaweza kuwa na uhakika kwamba maadamu wanazoea imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo, Yehova awaona kuwa safi na wenye kutakata. Wanajizoezaje imani? Kwa kufuata hatua za Yesu, wakiwa na uhakika kamili katika dhabihu ya fidia.—1 Petro 2:21.
10, 11. Ni ipi iliyo sehemu moja muhimu ya maji ya ufananisho, na hiyo yahusuje mpanuko wa ajabu wa mto huo?
10 Kama ilivyotangulia kutajwa, kuna sehemu nyingine muhimu ya maji haya ya ufananisho—ujuzi. Katika Israeli lililorudishwa, Yehova aliwabariki watu wake kwa mafundisho ya Kimaandiko kupitia ukuhani. (Ezekieli 44:23) Kwa njia kama hiyo, Yehova amewabariki watu wake leo kwa mafundisho tele juu ya Neno lake la kweli, kupitia ule “ukuhani wa kifalme.” (1 Petro 2:9) Ujuzi juu ya Yehova Mungu, juu ya makusudi yake kwa wanadamu, na hasa juu ya Yesu Kristo na Ufalme wa Kimesiya umetiririka kwa wingi unaozidi kuongezeka daima wakati huu wa siku za mwisho. Burudisho la mbubujiko wa kiroho tunaopata na ambao unazidi kuongezeka ni tukufu jinsi gani!—Danieli 12:4.
11 Kama vile ule mto ambao malaika aliupima ulivyoendelea kuongezeka kina hatua kwa hatua, ndivyo mtiririko wa baraka zinazotokeza uhai kutoka kwa Yehova umeongezeka sana ili kutosheleza mmiminiko wa watu wanaoingia katika nchi yetu ya kiroho iliyobarikiwa. Unabii mwingine wa urudisho ulitabiri hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Maneno hayo yametimia—mamilioni ya watu wamemiminika makundi makundi na kujiunga nasi katika ibada safi! Yehova amefanya “maji” mengi sana yapatikane kwa wote wanaomjia. (Ufunuo 22:17) Yeye huhakikisha kwamba tengenezo lake la kidunia hugawa Biblia na fasihi za Biblia ulimwenguni pote, katika mamia ya lugha. Vivyo hivyo, mikutano ya Kikristo na mikusanyiko imepangwa ulimwenguni pote ili wote waweze kupewa maji safi kabisa ya kweli. Maandalizi hayo huwaathirije watu?
Maji Yatokeza Uhai!
12. (a) Ni kwa nini miti iliyo katika ono la Ezekieli yaweza kuzaa kama ifanyavyo? (b) Miti hiyo yenye kuzaa sana huwakilisha nini katika siku za mwisho?
12 Mto katika ono la Ezekieli watokeza uhai na afya. Ezekieli anapopata kujua juu ya miti ambayo ingekua kando-kando ya mto huo, aambiwa: “Majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe; . . . na matunda yake yatakuwa chakula; na majani yake yatakuwa ni dawa.” Kwa nini miti hiyo huzaa kwa njia hii yenye kustaajabisha? “Kwa sababu maji yake yanatoka mahali patakatifu.” (Ezekieli 47:12b) Miti hiyo ya mfano hufananisha kimbele maandalizi yote ya Mungu kwa ajili ya kurudisha wanadamu kwenye ukamilifu kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Hapa duniani wakati huu, baki la watiwa-mafuta huongoza katika kuandaa lishe na ponyo la kiroho. Baada ya wale 144,000 wote kupokea thawabu yao ya kimbingu, faida zinazotokana na utumishi wao wa kikuhani wakiwa watawala-wenzi pamoja na Kristo zitaenea hadi wakati ujao, hatimaye zikiongoza kwenye kushindwa kabisa kwa kifo cha Kiadamu.—Ufunuo 5:9, 10; 21:2-4.
13. Ni ponyo gani limetimizwa wakati wetu?
13 Mto huo wa kimaono unaingia katika Bahari ya Chumvi isiyo na uhai na kuponya chochote ambacho hukifikia. Bahari hiyo hufananisha mazingira yaliyokufa kiroho. Lakini uhai watokea kwa wingi ‘kila mahali ufikapo mto huo.’ (Ezekieli 47:9) Vivyo hivyo, katika siku za mwisho, watu wamefanywa hai kiroho kokote ambako maji ya uhai yamepenyeza. Watu wa kwanza kutiwa uhai mpya jinsi hiyo ni baki la watiwa-mafuta mwaka wa 1919. Walirudishwa kighafula kwenye uhai wa kiroho kutoka hali iliyo kama kifo, ya kutotenda. (Ezekieli 37:1-14; Ufunuo 11:3, 7-12) Tangu wakati huo maji hayo ya uhai yamewafikia watu wengine walio wafu kiroho, nao wamekuwa hai na kufanyiza umati mkubwa wa kondoo wengine unaozidi kuongezeka daima, wanaompenda na kumtumikia Yehova. Hivi karibuni, uandalizi huu utafikia halaiki ya watu watakaofufuliwa.
14. Biashara ya uvuvi inayositawi sehemu fulani ya ufuo wa Bahari ya Chumvi yaonyesha vizuri jambo gani leo?
14 Uhai wa kiroho hutokeza uzalishaji. Hilo laonyeshwa kwa biashara ya uvuvi inayositawi kwenye fuo za bahari ambayo hapo kwanza ilikuwa imekufa. Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Nitawafanya nyinyi kuwa wavuvi wa watu.” (Mathayo 4:19) Katika siku za mwisho, kazi ya uvuvi ilianza kwa kukusanywa kwa mabaki ya watiwa-mafuta, lakini haijakomea hapo. Maji yenye kutokeza uhai yatokayo katika hekalu la kiroho la Yehova, kutia ndani baraka ya ujuzi sahihi, yaathiri watu wa mataifa yote. Kokote ambako mto huo umefikia, uhai wa kiroho umetokezwa.
15. Ni nini kionyeshacho kwamba si kila mtu atakayekubali maandalizi ya Mungu ya uhai, nalo tokeo la mwisho ni nini kwa watu kama hao?
15 Bila shaka, si wote huitikia ujumbe wa uhai ifaavyo sasa; wala si wote watakaofufuliwa wakati wa Utawala wa Milenia wa Kristo wataitikia ifaavyo. (Isaya 65:20; Ufunuo 21:8) Malaika atangaza kwamba sehemu fulani za bahari haziponywi. Sehemu hizo zenye matope, zisizo na uhai ‘zaachwa ziwe za chumvi.’ (Ezekieli 47:11) Kwa habari ya watu wa siku yetu, si wote huyakubali maji ya Yehova yenye kutokeza uhai wanayopewa. (Isaya 6:10) Kwenye Har–Magedoni, wale wote ambao wamechagua kubaki katika hali isiyo na uhai na yenye ugonjwa kiroho wataachiwa chumvi, yaani, wataharibiwa milele. (Ufunuo 19:11-21) Hata hivyo, wale ambao wamekuwa wakinywa maji hayo kwa uaminifu wanaweza kutumaini kuokoka na kuona utimizo wa mwisho wa unabii huu.
-