Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mbinu Mpya za Ugaidi
    Amkeni!—2001 | Mei 22
    • Mbinu Mpya za Ugaidi

      Mara ya mwisho tulipozungumzia ugaidi katika gazeti la “Amkeni!” tulitumia picha inayofahamika kwenye jalada —picha ya wauaji wenye bunduki waliofunika nyuso zao huku kukiwa na mlipuko mkubwa nyuma yao. Lakini siku hizi hali imebadilika.

      MSAFARA wa malori yasiyopambwa wapita taratibu kwenye maeneo ya makazi katika mwanga hafifu wa machweo. Malori hayo yasimama karibu na shule moja. Punde si punde, kikosi maalumu cha wanaume waliovalia vinyago vya kujikinga gesi na mavazi ya kujikinga dhidi ya kemikali, chaibuka na kuingia vichakani. Wanajua tu kwamba kombora dogo lililipuka wakati wa tamasha ya michezo shuleni humo. Gesi kali ya kombora hilo ilisambaa na kuwadhuru watazamaji wengi. Wanaume wanne wanakagua eneo hilo kwa uangalifu huku wakishirikiana na kikosi cha hali ya dharura cha mji huo ili kujua kilichotukia. Kombora hilo lilikuwa na gesi gani? Je, ni gesi yenye viini vya maradhi ya wanyama (anthrax) yanayoambukiza wanadamu? Je, ni gesi inayodhuru neva?

      Wanaume hao wanatembea taratibu kuelekea uwanjani, huku wakiwa wamebeba vifaa mbalimbali vya kuchunguza kemikali. Wanaingia kwenye chumba kidogo wanamopata vipande vya kombora hilo. Wanahitaji kuwa waangalifu sana, kwa kuwa wanatumia vifaa vidogo vya kupimia na pia wanahitaji kusogeza vitu vizito.

      Muda si muda jasho lawatiririka. Kazi hiyo inachosha sana, hata kwa watu waliozoezwa. Wanagundua gesi hiyo baada ya muda usiozidi dakika 10. Mtaalamu wa kemikali anayeambatana nao asema hivi: “Bila shaka ni gesi yenye viini vya maradhi ya wanyama yanayoambukiza wanadamu.”

      Mbinu Mpya za Ugaidi

      Tukio hilo halikuwa halisi. Hayo yalikuwa mazoezi ya kujaribu itikio la kikosi hicho kwa shambulizi bandia la gesi ya sumu. Mazoezi hayo yalifanywa katika jimbo moja kaskazini mwa New York. Kikosi hicho ni mojawapo ya Vikosi vya Kulinda Umma Kutokana na Silaha Hatari (Weapons of Mass Destruction Civil Support Teams). Vikosi hivyo vinachunguza uwezo na athari ya mbinu mpya zinazotumiwa na magaidi. Vinapima viini hatari, kemikali, au vifaa vyenye mnururisho.

      Kikosi hicho ni mojawapo ya vikosi vingi ambavyo vimebuniwa ulimwenguni pote ili kupambana na mbinu mpya na matatizo mapya ya ugaidi.a Visa vilivyotukia miaka ya majuzi vyaonyesha kwamba matendo ya kigaidi yanayofanywa na vikundi mbalimbali au na watu wenye siasa kali yanaongezeka. Ijapokuwa magaidi wengi bado hushambulia vituo vya kijeshi na makao ya kibalozi, baadhi yao wameanza pia kushambulia zile zinazoitwa eti shabaha rahisi, kama vile mifumo ya usafiri wa umma, tamasha za michezo, sehemu za miji zenye watu wengi, mahoteli, na vituo vya watalii.

      Porter Goss, mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi ya Bunge la Wawakilishi la Marekani, alikiri magaidi wanatumia mbinu mpya aliposema hivi: “Ni lazima tubadili maoni yetu ya kale kuhusu magaidi wanaodhaminiwa na serikali na kutambua mbinu mpya za ugaidi. Matendo ya kigaidi yanayoongezeka sasa ni yale yanayofanywa na magaidi wenye lengo hususa.”

      Mbinu mpya za ugaidi zatia ndani matendo na harakati ambazo haziwezi kuzuiwa au kukomeshwa kwa urahisi. Magaidi wengi zaidi wanatumia tekinolojia mpya na wanajitafutia msaada wa kifedha. Gazeti la USA Today laripoti hivi: “Ni vigumu sana kukomesha ugaidi kwa sababu magaidi wanatumia tekinolojia mpya ya kompyuta na ya mawasiliano na wanashirikiana na makundi ya siri ya ujambazi.” Siku hizi magaidi wana shabaha mpya. Jambo hilo limewafanya waandishi na wachanganuzi wa habari wabuni semi mpya kama vile “ugaidi wa Internet,” “ugaidi wa viini hatari,” na “ugaidi wa kimazingira.”

      Mbinu hizo mpya za ugaidi ni hatari kadiri gani? Je, uhai wako umo hatarini? Je, tatizo la kuenea kwa ugaidi ulimwenguni pote laweza kutatuliwa? Makala zifuatazo zitajibu maswali hayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Watu wana maoni mbalimbali kuhusu ugaidi. Kwa mfano, katika nchi zilizoharibiwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe, matendo ya kijeuri kati ya vikundi vinavyozozana yanaweza kuonwa kuwa matendo halali ya kivita au kama ugaidi, ikitegemea yule anayehojiwa. Katika mfululizo huu wa makala, neno “ugaidi” kwa ujumla linamaanisha kuwashurutisha watu kwa kutumia jeuri.

      [Sanduku/Ramani katika ukurasa wa 4, 5]

      (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

      Mwongo wa UGAIDI

      1. Buenos Aires, Argentina

      Machi 17, 1992

      Bomu lililotegwa katika gari lalipua Ubalozi wa Israeli. Waliouawa: 29. Waliojeruhiwa: 242

      2. Algiers, Algeria

      Agosti 26, 1992

      Bomu lalipuka kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa. Waliouawa: 12. Waliojeruhiwa: angalau 128

      3. New York City, Marekani

      Februari 26, 1993

      Wanadini wenye siasa kali walipua bomu lenye nguvu sana chini ya jengo la World Trade Center. Waliouawa: 6. Waliojeruhiwa: 1,000 hivi

      4. Matsumoto, Japani

      Juni 27, 1994

      Wafuasi wa madhehebu ya Aum Shinrikyo wasambaza gesi ya sarin kwenye eneo la makazi. Waliouawa: 7. Waliojeruhiwa: 270

      5. Tokyo, Japani

      Machi 20, 1995

      Wafuasi wa madhehebu ya Aum Shinrikyo waweka makopo sita ya gesi ya sarin kwenye magari ya moshi ya chini ya ardhi huko Tokyo. Makopo hayo yaeneza gesi yenye sumu ya sarin. Waliouawa: 12. Waliojeruhiwa: zaidi ya 5,000

      6. Oklahoma City, Marekani

      Aprili 19, 1995

      Bomu lililotegwa katika lori lalipuka karibu na jengo la serikali. Magaidi wenye siasa kali walaumiwa. Waliouawa: 168. Waliojeruhiwa: zaidi ya 500

      7. Colombo, Sri Lanka

      Januari 31, 1996

      Magaidi wa kikabila wagongesha lori lililojaa makombora kwenye benki. Waliouawa: 90. Waliojeruhiwa: zaidi ya 1,400

      8. London, Uingereza

      Februari 9, 1996

      Magaidi wa kutoka Ireland walipua bomu kwenye maegesho. Waliouawa: 2. Waliojeruhiwa: zaidi ya 100

      9. Jerusalem, Israel

      Februari 25, 1996

      Mpiganaji wa kujitolea kufa alipua basi kwa bomu. Yasemekana kwamba wanadini wenye siasa kali ndio waliofanya hivyo. Waliouawa: 26. Waliojeruhiwa: 80

      10. Dhahran, Saudi Arabia

      Juni 25, 1996

      Lori la mafuta lenye bomu lalipuka nje ya makazi ya kijeshi ya Marekani. Waliouawa: 19. Waliojeruhiwa: 515

      11. Phnom Penh, Kambodia

      Machi 30, 1997

      Magaidi warushia waandamanaji makombora manne. Waliouawa: 16 hivi. Waliojeruhiwa: zaidi ya 100

      12. Coimbatore, India

      Februari 14, 1998

      Mabomu kadhaa yalipuliwa na wapiganaji wa kidini wenye siasa kali. Waliouawa: 43. Waliojeruhiwa: 200

      13. Nairobi, Kenya, na Dar es Salaam, Tanzania

      Agosti 7, 1998

      Majengo ya Ubalozi wa Marekani yalipuliwa kwa bomu. Waliouawa: 250. Waliojeruhiwa: zaidi ya 5,500

      14. Kolombia

      Oktoba 18 na Novemba 3, 1998

      Shambulizi moja la mabomu na jingine la makombora. Bomba la mafuta lalipuliwa kwa mabomu. Waliouawa: 209. Waliojeruhiwa: zaidi ya 130

      15. Moscow, Urusi

      Septemba 9 na 13, 1999

      Milipuko miwili mikubwa yabomoa majengo mawili ya makazi. Waliouawa: 212. Waliojeruhiwa: zaidi ya 300

      [Hisani]

      Chanzo cha habari: The Interdisciplinary Center, Herzliya, Israel

      Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

      Victor Grubicy/Sipa Press

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

      Kompyuta Zavamiwa

      Machi 1999: Ripoti zaonyesha kwamba kompyuta za Makao Makuu ya Wizara ya Ulinzi ya Marekani (Pentagon) zimekuwa zikivamiwa “kisirisiri, na kwa mpango” na watu wasiojulikana. Wataalamu wa kompyuta huvamia mifumo ya kompyuta ya Wizara ya Ulinzi ya Marekani mara 60 hadi 80 kila siku.

      Katikati ya Mwaka wa 1999: Katika kipindi cha miezi mitatu tu, wataalamu wa kompyuta wanaopinga serikali walivamia vituo vya Internet vya Bunge la Marekani, Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI), Jeshi la Marekani, Ikulu ya White House, na wizara kadhaa za serikali ya Marekani.

      Januari 2000: Inaripotiwa kwamba biashara ulimwenguni pote zilitumia dola bilioni 12.1 za Marekani katika kupambana na “ugaidi wa kiuchumi” uliosababishwa na programu hatari zinazoharibu mifumo ya kompyuta.

      Agosti 2000: Mtaalamu wa kompyuta avamia vituo vya Internet vya shirika la serikali na vya halmashauri ya mitaa katika Muungano wa Uingereza na Ireland.

  • Kukabiliana na Tisho la Ugaidi
    Amkeni!—2001 | Mei 22
    • Kukabiliana na Tisho la Ugaidi

      MWISHONI mwa miaka ya 1980, ilionekana kana kwamba ugaidi ulikuwa ukididimia. Hata hivyo, mbinu mpya za ugaidi zimeibuka. Tatizo lililopo la ugaidi linasababishwa hasa na watu wenye siasa kali ambao wanapata pesa kutokana na ulanguzi wa dawa za kulevya, biashara za kibinafsi, matajiri, misaada, na wadhamini wengine. Magaidi wangali wakatili.

      Kumekuwa na visa chungu nzima vya ugaidi vyenye kusikitisha katika miaka ya karibuni. Jengo la World Trade Center huko New York City lililipuliwa kwa bomu, watu 6 wakauawa na 1,000 kujeruhiwa. Washiriki wa madhehebu fulani walisambaza gesi ya sarin inayodhuru neva kwenye magari ya moshi ya chini ya ardhi huko Tokyo, watu 12 waliuawa na zaidi ya 5,000 kujeruhiwa. Jengo la serikali huko Oklahoma City liliporomoka baada ya kulipuliwa kwa bomu lililotegwa katika lori na gaidi mmoja. Watu 168 waliuawa na mamia kujeruhiwa. Kama chati iliyo kwenye ukurasa wa 4 na 5 inavyoonyesha, visa vya kigaidi vya kila namna vimeendelea kutukia hadi leo.

      Kwa ujumla, yaonekana siku hizi magaidi wanatenda kwa ukatili zaidi kuliko awali. Gaidi aliyeshtakiwa kwa kulipua jengo la serikali la Oklahoma City mnamo mwaka wa 1995, alinukuliwa akisema kwamba alihitaji kuua watu wengi zaidi ili madai yake yatimizwe. Kiongozi wa kikundi kilichohusika na ulipuaji wa jengo la World Trade Center huko New York City mwaka wa 1993, alitaka kulipua majengo yote mawili na kuua kila mtu aliyekuwamo.

      Leo magaidi wanaweza kupata silaha mbalimbali pia. Louis R. Mizell, Jr., mpelelezi stadi wa ugaidi, alisema hivi: “Twaishi katika enzi iliyo na silaha nyingi hatari zinazoweza kuangamiza watu wengi sana: silaha za nyuklia, kemikali, na zenye viini.” Watu wenye siasa kali wanaotaka kushtua ulimwengu wanatumia silaha hatari zaidi za kisasa.

      Mashambulizi ya Kigaidi Kupitia kwa Kompyuta

      Ugaidi wa Internet (cyber-terrorism) hutumia teknolojia ya kisasa kama vile kompyuta. Mojawapo ya vitu wanavyotumia ni programu hatari za kompyuta (computer virus) ambazo zinaharibu habari zilizohifadhiwa au kutatanisha mifumo ya kompyuta. Pia kuna programu nyingine hatari zinazoitwa kwa Kiingereza “logic bombs” ambazo huvuruga kompyuta. Kompyuta hujaribu kufanya kazi isiyowezekana halafu inakwama. Watu wengi wanahisi kwamba umma unakabili hatari ya ugaidi wa aina hiyo kwa sababu uchumi na usalama wa nchi nyingi unategemea sana mifumo ya kompyuta. Na ijapokuwa majeshi mengi yana mifumo ya mawasiliano inayoweza kustahimili vita ya nyuklia, huduma za umma kama vile usambazaji wa umeme, usafiri, na masoko ya fedha yanaweza kuvamiwa kwa urahisi sana.

      Miaka michache iliyopita, gaidi angeweza kukata umeme, tuseme katika jiji la Berlin, labda kwa kuomba kazi kwenye kampuni ya umeme akiwa na kusudi la kuharibu mfumo wa umeme. Lakini sasa, watu fulani wanasema kwamba mtaalamu wa kompyuta anaweza kukata umeme jijini akiwa nyumbani mwake katika kijiji kilicho upande mwingine wa dunia.

      Hivi majuzi mtaalamu mmoja wa kompyuta wa Sweden alivamia mfumo wa kompyuta huko Florida na kuvuruga huduma za dharura kwa muda wa saa moja. Polisi, wazima-moto, na magari ya wagonjwa hayangeweza kuitikia mwito wa dharura.

      “Ni kana kwamba tumetokeza jumuiya ya ulimwenguni pote isiyo na idara ya polisi,” akasema Frank J. Cilluffo, mkurugenzi wa Kikundi Kinachopambana na Ugaidi wa Kompyuta kilicho kwenye kituo cha Center for Strategic and International Studies (CSIS). Naye Robert Kupperman, mshauri mkuu wa kituo cha CSIS, alisema mnamo mwaka wa 1997 kwamba “hakuna shirika lolote la serikali linaloweza kukabiliana na mashambulizi ya magaidi” endapo magaidi wataamua kutumia teknolojia ya kisasa.

      Wachunguzi fulani wanaamini kwamba magaidi wanaotumia kompyuta wana ustadi wa kitekinolojia unaoweza kuwasaidia kuepuka kunaswa na vifaa vyovyote vinavyobuniwa na vikosi vya ulinzi. George Tenet, mkurugenzi wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA), alisema kwamba “adui mwenye ujuzi wa kuweka programu hatari kwenye mfumo wa kompyuta au anayeweza kufikia kompyuta ifaayo kwenye mtandao anaweza kusababisha hasara kubwa sana.”

      Magaidi Wanaotumia Kemikali au Viini

      Wengi wanahofia pia matumizi ya silaha za kemikali na zenye viini hatari. Watu wengi ulimwenguni walishtuka mapema mwaka wa 1995 waliposikia kwamba magaidi walishambulia magari ya moshi ya chini ya ardhi huko Tokyo kwa kutumia gesi ya sumu. Madhehebu yanayotabiri mwisho wa ulimwengu ndiyo yaliyolaumiwa kwa tukio hilo.

      “Kuna mbinu mpya za ugaidi,” asema Brad Roberts wa Institute for Defense Analyses. “Magaidi wa kale walitaka mikataba ya kisiasa. Lakini sasa makundi fulani ya kigaidi yanasema kwamba lengo lao kuu ni kuua watu wengi. Ndiyo sababu magaidi wanapendelea silaha zenye viini hatari.” Je, ni vigumu kupata silaha hizo? Gazeti Scientific American lasema hivi: “Mtu anaweza kukuza matrilioni ya bakteria kwa kutumia kifaa sahili cha kuchachusha pombe na mkorogo maalumu wa protini. Aweza kujikinga pia kutokana na gesi na viini kwa kuvalia kinyago usoni, na vazi refu la plastiki.” Baada tu ya kukuza viini hivyo, vinaweza kusafirishwa kwa urahisi sana. Watu hugundua siku moja au mbili baadaye kwamba wameshambuliwa kwa silaha ya viini. Na huwa tayari wameathiriwa mno.

      Yasemekana kwamba silaha yenye viini vya maradhi ya wanyama yanayoambukiza wanadamu (anthrax) hupendwa sana. Jina la maradhi hayo latokana na neno la Kigiriki la makaa ya mawe. Jina hilo larejezea upele mweusi unaoibuka kwenye ngozi ya wale wanaogusa wanyama wenye maradhi hayo. Wataalamu wa vikosi vya ulinzi wanahofia zaidi maambukizo ya mapafu yanayotokana na kupumua viini vya maradhi hayo. Wanadamu wengi wanaoambukizwa maradhi hayo hufa.

      Kwa nini silaha yenye viini vya maradhi ya wanyama yanayoambukiza wanadamu huwa hatari? Viini hivyo hukuzwa kwa urahisi na hustahimili hali mbalimbali. Siku chache baada ya kuambukizwa, mtu hupata dalili za kwanza za maradhi hayo. Yeye hujihisi akiwa mchovu kana kwamba ana mafua. Kisha hukohoa na kuhisi maumivu kifuani. Muda si muda yeye hushindwa kabisa kupumua, anakuwa mahututi, halafu anakufa baada ya saa chache tu.

      Je, Magaidi Wana Silaha za Nyuklia?

      Baada ya kuporomoka kwa Muungano wa Sovieti, baadhi ya watu walihofu kwamba huenda silaha ya nyuklia ikaibiwa na kuuzwa kwa njia haramu. Hata hivyo, wataalamu wengi hawadhani jambo hilo litapata kutukia. Robert Kupperman, aliyenukuliwa awali, asema kwamba “hakuna ushuhuda unaoonyesha kwamba kikundi chochote cha magaidi kimejaribu kununua silaha za nyuklia.”

      Silaha inayohofiwa zaidi ni silaha ya mnururisho ambayo ni hatari kama bomu ya nyuklia. Silaha hiyo haijulikani sana. Hailipuki. Haina sauti wala moto. Badala yake, inatokeza mnururisho unaoangamiza chembe mwilini. Chembe zinazoangamizwa zaidi ni chembe za uboho wa mifupa. Chembe hizo zinapokufa matatizo mbalimbali yanatokea, kutia ndani kuvuja damu na kuharibika kwa mfumo wa kinga. Tofauti na silaha za kemikali, ambazo hufifia mara tu zinapochanganyika na oksijeni na unyevu, mnururisho huendelea kudhuru kwa miaka mingi.

      Msiba uliotokea Goiânia, jiji lililo kusini ya kati ya Brazili, waonyesha hatari ya mnururisho. Mnamo mwaka wa 1987 mwanamume fulani alifunua pasipo kujua mkebe wa madini ya risasi uliokuwa kwenye mashine ya kitiba iliyotupwa. Mkebe huo ulikuwa na madini ya cesium-137. Alivutiwa mno na madini hayo yenye mng’ao mwangavu wa buluu kiasi cha kwamba alienda kuwaonyesha rafiki zake. Baada ya juma moja kupita, watu walioathiriwa na mnururisho walianza kumiminika kwenye hospitali moja ya karibu. Maelfu walichunguzwa ili kuona iwapo waliathiriwa na mnururisho huo. Wakazi wapatao 100 wakawa wagonjwa. Wakazi 50 wakalazwa hospitalini, na wanne wakafa. Wataalamu wanaopambana na ugaidi hushtuka sana wafikiripo kile kinachoweza kutukia iwapo kemikali hiyo ya cesium itasambazwa kimakusudi.

      Matokeo Mabaya ya Ugaidi

      Matokeo yaliyo wazi ya ugaidi ni vifo vya kusikitisha vya wanadamu. Lakini kuna matokeo zaidi. Ugaidi unaweza kuharibu au kuzorotesha jitihada za kuleta amani katika maeneo yenye vita duniani. Ugaidi huzidisha mapambano na jeuri.

      Ugaidi unaweza pia kuathiri uchumi wa nchi. Serikali nyingi zimelazimika kutumia wakati mwingi na mali ili kukabiliana nao. Kwa mfano, nchi ya Marekani peke yake ilitenga zaidi ya dola bilioni kumi katika mwaka wa 2000 ili kukabiliana na ugaidi.

      Ugaidi hutuathiri sote iwe twajua hivyo au la. Huathiri jinsi tunavyosafiri na maamuzi tunayofanya tunaposafiri. Nchi nyingi ulimwenguni hulazimika kutumia kiasi kikubwa cha fedha za kodi ili kulinda watu mashuhuri, vifaa au majengo muhimu, na kulinda raia kutokana na ugaidi.

      Basi swali linalobaki ni hili, Je, tatizo la ugaidi litatatuliwa kabisa? Makala ifuatayo itazungumzia swali hilo.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      Magaidi Wanaodai Wanahifadhi Mazingira

      Gazeti la Oregonian laripoti kwamba kuna magaidi wapya “wanaochoma mali kimakusudi, kulipua mabomu na kujeruhi watu wakidai eti wanahifadhi mazingira na viumbe.” Matendo hayo ya kihuni yameitwa ugaidi wa kimazingira (ecoterrorism). Angalau visa vibaya 100 vya aina hiyo vimetukia magharibi mwa Marekani tangu mwaka wa 1980. Vimesababisha hasara ya jumla ya dola milioni 42.8 za Marekani. Kwa kawaida uhalifu huo unakusudiwa kuzuia ukataji wa miti, kuwazuia watu kufanyia tafrija mbugani, au kuzuia watu kutumia wanyama kwa utafiti, kula nyama yao, au kutumia manyoya yao.

      Matukio hayo huonwa kuwa vitendo vya kigaidi kwa kuwa ujeuri hutumiwa ili kuwalazimisha watu na mashirika kubadili mtazamo, au kubadili sera za kijamii. Magaidi wa kimazingira huwavunja moyo wachunguzi wa mazingira kwa kushambulia vifaa muhimu. Kwa kawaida wanashambulia vifaa hivyo na kuviharibu kabisa wakati wa usiku. Ni hivi karibuni tu ndipo uhalifu unaofanywa kwa madai ya kuhifadhi mazingira ulipoanza kuenea na kushtua watu wengi. Lakini kuna vifaa vingi vinavyoweza kushambuliwa na magaidi siku hizi. Mpelelezi maalumu James N. Damitio, ambaye amekuwa mtafiti wa Idara ya Misitu ya Marekani kwa muda mrefu, alisema hivi: “Kusudi lao ni kuwafanya watu watambue harakati zao za kuleta mabadiliko. Wanapoona kwamba watu hawajali maoni yao, wanajaribu mbinu nyingine.”

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

      Ugaidi na Vyombo vya Habari

      “Magaidi wanaowadhulumu watu wasio na hatia hupenda sana kutangazwa kote ili kutimiza malengo yao ya kisiasa au kubabaisha watu tu,” asema Terry Anderson, mwandishi wa habari ambaye alitekwa na magaidi nchini Lebanon kwa miaka saba hivi. “Magaidi huhisi wamefaulu hasa inapotangazwa kwamba mtu ametekwa nyara kwa sababu za kisiasa, au ameuawa au watu wamelipuliwa kwa bomu. Habari hizo zisiposambazwa ulimwenguni pote, magaidi wanahisi kwamba matendo yao ya kikatili hayakuwa na maana yoyote.”

      [Picha katika ukurasa wa 8, 9]

      1. Bomu lalipuliwa na gaidi aliyejitolea kufa, huko Jerusalem, Israel

      2. Magaidi wa kikabila walipua benki kwa bomu huko Colombo, Sri Lanka

      3. Bomu lililotegwa katika gari lalipuka Nairobi, Kenya

      4. Familia za watu waliouawa kwa mlipuko wa bomu huko Moscow, Urusi

      [Hisani]

      Heidi Levine/Sipa Press

      A. Lokuhapuarachchi/Sipa Press

      AP Photo/Sayyid Azim

      Izvestia/Sipa Press

  • Ugaidi Utakoma Karibuni!
    Amkeni!—2001 | Mei 22
    • Ugaidi Utakoma Karibuni!

      MAGAIDI wanaweza kushambulia basi huko Jerusalem, jengo la serikali huko Oklahoma City, au jengo la makazi huko Moscow. Ijapokuwa magaidi hukusudia kuwasilisha ujumbe muhimu kwa wanasiasa, wakuu wa kijeshi, au wasimamizi wa mambo ya kiuchumi, mara nyingi wanashambulia watu wasiohusika. Katika visa vingi wao hushambulia watu wa kawaida—watu ambao hawahusiki hata kidogo na makusudi ya magaidi hao. Basi, mbona watu wenye siasa kali hutenda matendo ya kigaidi?

      Mbona Kuna Ugaidi?

      Matendo ya kigaidi huwa yamepangwa kimbele na kudhamiriwa. Lengo kuu si kuua na kujeruhi watu wengi. Mauaji hayo huwasaidia kutimiza lengo lao. Magaidi huzusha hali ya wasiwasi na hofu ili kudunisha wenye mamlaka. Wao hutaka kusikilizwa na kutimiziwa mahitaji yao hususa. Fikiria baadhi ya sababu zinazofanya magaidi watende kwa ujeuri.

      Chuki. “Ugaidi . . . huchochewa na chuki,” asema Louis J. Freeh, mkurugenzi wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI). “Wale walio na chuki hiyo huchochewa na watu wenye chuki, hila, na ujinga.”

      Uonevu. “Hatuna budi kukubali kwamba viongozi wa makundi na wa nchi fulani wana kusudi ovu la kuangamiza watu wa tamaduni nyingine,” aandika Stephen Bowman katika kitabu chake When the Eagle Screams. “Lakini ni wazi pia kwamba visa vingi vya kigaidi hufanywa na watu waliokata tamaa.”

      Kukata tamaa. “Mara nyingi . . . magaidi wengi hutenda hivyo kwa sababu ya kukatishwa tamaa na hali ngumu za kisiasa, kijamii, na kiuchumi,” asema mhariri wa kitabu Urban Terrorism.

      Ukosefu wa haki. “Ugaidi husababishwa na tatizo jingine,” asema Michael Shimoff katika makala yake yenye kichwa “Sera ya Ugaidi.” Aendelea kusema hivi: “Mradi wetu wapasa kuwa kukomesha hali za kijamii na za kisiasa zinazosababisha ugaidi. . . . Mbali na kupambana na ugaidi, ni sharti tujitahidi kwa udi na uvumba kudumisha uhuru, staha, haki, na heshima ya binadamu. Hatutaweza kukomesha ugaidi tusipojitahidi kudumisha mambo hayo.”

      Visababishi na historia ya ugaidi imethibitisha ukweli huu wa Biblia: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989) Biblia ilitabiri pia sifa ambazo zimesitawisha ugaidi. Yasema hivi: “Katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi.”—2 Timotheo 3:1-4.

      Ukweli ni kwamba jitihada za wanadamu za kukomesha ugaidi, hata ziwe za moyo mweupe jinsi gani, haziwezi kutatua matatizo yanayosababisha ugaidi. Biblia yasema hivi waziwazi: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Hata hivyo, Mungu anaweza kutatua tatizo la ugaidi, yeye si kama wanadamu wasiokuwa na uwezo.

      Utatuzi

      Wale ambao wamekata tamaa sana kwa sababu ya kudhulumiwa au kuonewa wanaweza kufarijiwa na ahadi hii hakika ya Biblia: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:21, 22.

      Ahadi hiyo ya Mungu itatimizwa hivi karibuni. Mtawala Wake, Mfalme Yesu Kristo anayemiliki atahakikisha imetimizwa. Unabii wa Biblia wasema hivi kumhusu Kristo: “Hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili.”—Isaya 11:3, 4.

      Naam, hivi karibuni Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, atakomesha ukosefu wote wa haki pamoja na wote wanaousababisha. Katika mfumo mpya wa Mungu wa uadilifu, ugaidi na jeuri ya kila namna zitatokomea kabisa. Halafu kila mtu duniani ataishi kwa usalama, hatahofu madhara yoyote.—Ufunuo 21:3, 4.

      [Picha katika ukurasa wa 12]

      Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni Mungu atakomesha uonevu wote na ukosefu wa haki

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki