Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Huu Ndio Wakati Muhimu Zaidi wa Kukaa Macho!
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 1
    • Huu Ndio Wakati Muhimu Zaidi wa Kukaa Macho!

      “Acheni tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali acheni tukae macho na kutunza hisi zetu.”—1 WATHESALONIKE 5:6.

      1, 2. (a) Pompeii na Herculaneum yalikuwa majiji ya aina gani? (b) Wakazi wa jiji la Pompeii na Herculaneum walipuuza onyo gani, nao wakapatwa na nini?

      KATIKA karne ya kwanza Wakati wa Kawaida, kulikuweko majiji mawili ya Roma yenye ufanisi yaliyoitwa Pompeii na Herculaneum yaliyokuwa karibu na Mlima Vesuvius. Matajiri wa Roma walipenda kwenda likizo kwenye majiji hayo. Viwanja vya maonyesho vya majiji hayo vilitoshea watu zaidi ya elfu moja, na katika jiji la Pompeii kulikuwa na uwanja mkubwa sana ambao ungeweza kutoshea karibu watu wote wa mji huo. Watu wanaochimbua vitu vya kale walipata baa 118 zilizokuwa katika jiji la Pompeii. Baadhi ya baa hizo zilitumiwa kuchezea kamari au kufanyia ukahaba. Ukosefu wa maadili na ufuatiaji wa vitu vya kimwili ulienea sana, kama inavyoonyeshwa na michoro ya ukutani na vitu vya kale.

      2 Siku ya Agosti 24, 79 W.K., Mlima Vesuvius ulianza kulipuka. Wataalamu wa volkeno wanaamini kwamba mlipuko wa kwanza uliorusha jivu na mawe ya volkeno kwenye majiji hayo mawili, labda usingaliwazuia wakazi kutoroka. Kwa kweli, yaonekana wengi walitoroka. Hata hivyo, wengine hawakuchukua kwa uzito hatari hiyo, au walipuuza tu dalili za onyo na wakaamua kubaki katika majiji hayo. Kisha, mwendo wa saa sita usiku, maporomoko ya gesi moto sana na mawe ya volkeno yalifunika jiji la Herculaneum, na kuangamiza wakazi wote waliosalia jijini humo. Asubuhi na mapema siku iliyofuata, maporomoko kama hayo yaliua wakazi wote waliokuwa katika jiji la Pompeii. Walipatwa na msiba ulioje kwa sababu ya kupuuza dalili za onyo!

      Mwisho wa Mfumo wa Mambo wa Kiyahudi

      3. Uharibifu wa Yerusalemu unafananaje na wa majiji ya Pompeii na Herculaneum?

      3 Uharibifu wenye kuogopesha wa jiji la Pompeii na Herculaneum haukuwa mkubwa kama ule wa Yerusalemu uliotukia miaka tisa mapema, na ambao ulisababishwa na watu. Uharibifu huo unaotajwa kuwa “mazingiwa mabaya zaidi katika historia,” ulisababisha vifo vya Wayahudi zaidi ya milioni moja. Hata hivyo, msiba uliopata jiji la Pompeii na Herculaneum ulitanguliwa na onyo na ndivyo na uharibifu uliopata jiji la Yerusalemu.

      4. Yesu alitoa ishara gani ya unabii ili kuonya wafuasi wake kwamba mwisho wa mfumo wa mambo ulikuwa umekaribia, na ishara hiyo ilitimizwaje mara ya kwanza katika karne ya kwanza?

      4 Yesu Kristo alikuwa ametabiri kwamba jiji hilo lingeharibiwa na kutaja matukio ambayo yangetangulia uharibifu huo—mambo ya kuogopesha kama vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, na uvunjaji wa sheria. Kungekuwa na manabii wasio wa kweli, lakini habari njema ya Ufalme wa Mungu ingehubiriwa ulimwenguni pote. (Mathayo 24:4-7, 11-14) Ingawa maneno ya Yesu yanatimizwa kwa kiwango kikubwa leo, yalitimizwa kwa kiwango kidogo wakati huo. Historia inaonyesha kwamba kulikuwa na njaa kali huko Yudea. (Matendo 11:28) Mwanahistoria Myahudi Josephus anaripoti kwamba kulikuwa na tetemeko la ardhi huko Yerusalemu kabla tu ya jiji hilo kuharibiwa. Uharibifu wa Yerusalemu ulipokaribia, mara nyingi kulikuwa na maasi yasiyokoma, vita ya wenyewe kwa wenyewe kati ya vikundi vya kisiasa vya Wayahudi, na mauaji katika majiji kadhaa ambayo wakazi wake walikuwa Wayahudi na watu wasio Wayahudi. Licha ya hayo, habari njema ya Ufalme ilikuwa ikihubiriwa “katika viumbe vyote chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.

      5, 6. (a) Ni unabii gani wa Yesu uliotimizwa mwaka wa 66 W.K.? (b) Kwa nini watu wengi sana walikufa Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 70 W.K.?

      5 Hatimaye, mnamo mwaka wa 66 W.K., Wayahudi waliasi dhidi ya Roma. Wakati Cestius Gallus alipoongoza majeshi yake yazingire Yerusalemu, wafuasi wa Yesu walikumbuka maneno haya ya Yesu: “Wakati mwonapo Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwalo kumekaribia. Ndipo waacheni wale walio katika Yudea waanze kukimbia hadi kwenye milima, na waacheni wale walio katikati yalo waondoke, na waacheni wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani yalo.” (Luka 21:20, 21) Wakati wa kuondoka Yerusalemu ulikuwa umefika. Lakini wangeondokaje? Gallus na majeshi yake yaliondoka kwa ghafula, hivyo Wakristo huko Yerusalemu na Yudea wakapata fursa ya kutii maneno ya Yesu na kukimbilia milimani.—Mathayo 24:15, 16.

      6 Miaka minne baadaye, yapata wakati wa Sikukuu ya Kupitwa, jeshi la Roma lilirudi likiongozwa na Jenerali Titus, aliyekuwa ameazimia kukomesha kabisa uasi wa Wayahudi. Majeshi yake yalizingira Yerusalemu na kujenga “boma lenye miti iliyochongoka,” na hivyo kuzuia mtu yeyote asiweze kutoroka. (Luka 19:43, 44) Licha ya tisho la vita, Wayahudi kutoka Milki yote ya Roma walikuwa wamekuja Yerusalemu kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa. Sasa wakawa wamenaswa. Kulingana na Josephus, idadi kubwa ya waliokufa wakati Roma lilipozingirwa ni wageni hao wa kusikitikiwa.a Wakati Yerusalemu lilipoharibiwa, karibu Myahudi mmoja kati ya kila Wayahudi saba alikufa katika Milki ya Roma. Kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu lake kulimaanisha kukomeshwa kwa taifa la Kiyahudi na mfumo wake wa kidini uliotegemea Sheria ya Musa.b—Marko 13:1, 2.

      7. Kwa nini Wakristo waaminifu waliokoka uharibifu wa Yerusalemu?

      7 Mnamo mwaka wa 70 W.K., Wakristo Wayahudi wangaliuawa au kupelekwa utumwani pamoja na watu wote waliokuwa Yerusalemu. Hata hivyo, historia inathibitisha kwamba walitii onyo la Yesu lililokuwa limetolewa miaka 37 mapema. Walikuwa wameondoka jijini na hawakuwa wamerudi.

      Maonyo ya Mitume ya Wakati Unaofaa

      8. Petro alitambua uhitaji gani, na yaelekea alikumbuka maneno gani ya Yesu?

      8 Leo, uharibifu mkubwa sana unakaribia, yaani, kuharibiwa kwa mfumo wote wa mambo. Miaka sita kabla Yerusalemu halijaharibiwa, mtume Petro alitoa shauri muhimu na la wakati unaofaa ambalo linahusu hasa Wakristo wa leo: Kaeni chonjo! Petro aliona kwamba Wakristo wanahitaji kuchochea ‘uwezo wao mwangavu wa kufikiri’ ili wasipuuze “amri ya Bwana,” Yesu Kristo. (2 Petro 3:1, 2) Akiwahimiza Wakristo wawe chonjo, yaelekea Petro alikumbuka maneno ambayo Yesu aliwaambia mitume Wake siku chache kabla hajafa: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho, kwa maana hamjui ni lini ulio wakati uliowekwa rasmi.”—Marko 13:33.

      9. (a) Watu fulani wangesitawisha mtazamo gani hatari? (b) Kwa nini ni hatari hasa kuwa na shaka?

      9 Leo, wengine husema hivi kwa dhihaka: “Kuko wapi kuwapo kwake huku kulikoahidiwa?” (2 Petro 3:3, 4) Bila shaka, watu hao huhisi kwamba mambo hayabadiliki hata kidogo bali yanaendelea kama kawaida tangu dunia iumbwe. Ni hatari kuwa na shaka kama hiyo. Shaka inaweza kufanya tusitambue umuhimu wa nyakati tunamoishi, na kutuchochea tuzingatie mno kutimiza tamaa za kimwili. (Luka 21:34) Mbali na hayo, Petro anasema kwamba wadhihaki hao wanasahau Furiko la siku za Noa lililoharibu mfumo wote wa mambo. Kwa kweli, mambo yalibadilika wakati huo!—Mwanzo 6:13, 17; 2 Petro 3:5, 6.

      10. Petro anawatia moyo kwa maneno gani wale ambao huenda wakakosa subira?

      10 Petro anawasaidia wasomaji wake wasitawishe subira kwa kuwakumbusha sababu ambayo mara nyingi hufanya Mungu asichukue hatua mara moja. Kwanza, Petro anasema: “Siku moja kwa Yehova ni kama miaka elfu na miaka elfu kama siku moja.” (2 Petro 3:8) Kwa kuwa Yehova huishi milele, anaweza kufikiria mambo yote yanayohusika na kuamua wakati unaofaa kabisa kuchukua hatua. Kisha, Petro anataja kwamba Yehova anatamani watu kila mahali watubu. Subira ya Mungu itafanya wengi waokoke ambao wangeangamia kama angechukua hatua haraka. (1 Timotheo 2:3, 4; 2 Petro 3:9) Hata hivyo, subira ya Yehova haimaanishi kwamba hatachukua hatua kamwe. “Siku ya Yehova itakuja kama mwizi,” asema Petro.—2 Petro 3:10.

      11. Ni nini kitakachotusaidia tukae macho kiroho, na kufanya hivyo ‘kutaharakishaje’ kwa njia ya mfano siku ya Yehova?

      11 Ulinganisho wa Petro unafaa. Si rahisi kuwakamata wezi, lakini mlinzi aliye macho usiku kucha anaweza kumwona mwizi kwa urahisi kuliko yule anayesinzia-sinzia. Mlinzi anawezaje kukaa macho? Ni rahisi mlinzi kuwa chonjo anapotembea-tembea kuliko anapoketi usiku kucha. Vivyo hivyo, kwa kuendelea kuwa na bidii katika mambo ya kiroho kutatusaidia kukaa macho tukiwa Wakristo. Kwa hiyo, Petro anatuhimiza tujishughulishe na “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (2 Petro 3:11) Utendaji huo utatusaidia tuendelee “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kuweka karibu akilini” linaweza kutafsiriwa kihalisi kuwa “kuharakisha.” (2 Petro 3:12) Ni kweli kwamba hatuwezi kubadili ratiba ya Yehova. Siku yake itakuja wakati wake barabara. Lakini tutaona kana kwamba wakati uliobaki unapita haraka iwapo tuna mengi ya kufanya katika utumishi wake.—1 Wakorintho 15:58.

      12. Tunawezaje kunufaika na subira ya Yehova?

      12 Kwa hiyo, mtu yeyote anayehisi kwamba siku ya Yehova inachelewa anatiwa moyo kutii shauri la Petro la kungojea kwa subira wakati uliowekwa wa Yehova. Kwa kweli, tunaweza kutumia kwa hekima wakati huu ambao Mungu ameruhusu kwa sababu ya subira yake. Kwa mfano, tunaweza kuendelea kusitawisha sifa muhimu za Kikristo na vilevile kuhubiri habari njema kwa watu wengi zaidi. Hatungeweza kufanya hivyo iwapo Yehova hangeonyesha subira. Tukikaa macho, Yehova atatupata tukiwa “bila doa na bila waa na katika amani” mwishoni mwa mfumo huu wa mambo. (2 Petro 3:14, 15) Hiyo itakuwa thawabu iliyoje!

      13. Paulo aliwaandikia Wakristo wa Thesalonike maneno gani yanayofaa sana leo?

      13 Pia Paulo anazungumzia uhitaji wa kukaa macho katika barua yake ya kwanza kwa Wakristo wa Thesalonike. Anashauri hivi: “Acheni tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali acheni tukae macho na kutunza hisi zetu.” (1 Wathesalonike 5:2, 6) Leo, ni muhimu sana kukaa macho kwa kuwa mwisho wa mfumo wote wa mambo unakaribia. Watumishi wa Yehova wanaishi katika ulimwengu usiojali mambo ya kiroho, na hilo linaweza kuwaathiri. Kwa hiyo, Paulo anashauri hivi: “Acheni tutunze hisi zetu na kuwa tumevaa bamba la kifuani la imani na upendo na kama kofia ya chuma lile tumaini la wokovu.” (1 Wathesalonike 5:8) Kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kushirikiana na ndugu zetu mikutanoni kutatusaidia kutii shauri la Paulo na kutambua umuhimu wa nyakati hizi.—Mathayo 16:1-3.

      Mamilioni Wanafuliza Kulinda

      14. Ni takwimu gani zinazoonyesha kwamba wengi leo wanatii shauri la Petro la kukaa macho?

      14 Je, leo wengi wanatii shauri hilo lililoongozwa na roho ya Mungu la kukaa macho? Ndiyo. Katika mwaka wa utumishi wa 2002, kilele cha wahubiri 6,304,645—ongezeko la asilimia 3.1 kuliko mwaka wa 2001—walithibitisha kwamba walikuwa chonjo kiroho kwa kutumia saa 1,202,381,302 wakizungumza na watu kuhusu Ufalme wa Mungu. Wahubiri hao walifurahia kazi hiyo. Ilikuwa kazi muhimu maishani mwao. Mtazamo wa wengi wao ni kama ule wa Eduardo na Noemi wanaoishi nchini El Salvador.

      15. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha kwamba wengi wanaendelea kukaa chonjo kiroho nchini El Salvador?

      15 Miaka kadhaa iliyopita, Eduardo na Noemi walizingatia maneno haya ya Paulo: “Mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Wakorintho 7:31) Walifanya maisha yao kuwa sahili na kuanza kazi ya upainia, yaani, utumishi wa wakati wote. Muda uliposonga walibarikiwa katika njia mbalimbali hata wakawa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya. Licha ya kupatwa na matatizo magumu, Eduardo na Noemi wanaamini kwamba walifanya uamuzi unaofaa walipoacha vitu vya kimwili na kuanza huduma ya wakati wote. Wengi wa wahubiri 29,269—kutia ndani mapainia 2,454—nchini El Salvador wameonyesha roho hiyo ya kujidhabihu. Kwa sababu hiyo, nchi hiyo ilikuwa na ongezeko la wahubiri la asilimia 2 mwaka jana.

      16. Ndugu fulani mchanga alionyesha mtazamo gani nchini Côte d’Ivoire?

      16 Nchini Côte d’Ivoire, Mkristo mchanga alionyesha mtazamo kama huo alipoandikia ofisi ya tawi hivi: “Mimi ni mtumishi wa huduma. Lakini siwezi kuwaambia akina ndugu wawe mapainia kwa sababu sijawawekea kielelezo kizuri. Kwa hiyo nimeacha kazi yenye mshahara mzuri na sasa nimejiajiri, na ninapata wakati zaidi wa kuhubiri.” Kijana huyo alikuwa miongoni mwa mapainia 983 wanaotumikia katika nchi ya Côte d’Ivoire, ambayo iliripoti wahubiri 6,701 mwaka jana, ongezeko la asilimia 5.

      17. Shahidi mchanga nchini Ubelgiji alionyeshaje kwamba hakuogopeshwa na ubaguzi?

      17 Hali ya kutovumiliana, upendeleo na ubaguzi unazidi kusababisha matatizo kwa wahubiri wa Ufalme 24,961 nchini Ubelgiji. Hata hivyo, wahubiri hao ni wenye bidii na hawana woga. Wakati Shahidi mwenye umri wa miaka 16 aliposikia Mashahidi wa Yehova wakiitwa madhehebu wakati wa somo la maadili shuleni, aliomba ruhusa ya kueleza maoni ya Mashahidi wa Yehova. Akitumia video Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name na broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Akina Nani?, aliweza kueleza ukweli kuhusu Mashahidi. Wanafunzi walifurahia sana habari hiyo na juma lililofuata wanafunzi wakapewa mtihani ambao walipaswa kujibu maswali kuhusu dini ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova.

      18. Kuna uthibitisho gani kwamba wahubiri nchini Argentina na Msumbiji hawakuacha kumtumikia Yehova kwa sababu ya magumu ya kiuchumi?

      18 Wakristo wengi wanalazimika kukabili matatizo magumu katika siku hizi za mwisho. Hata hivyo, wanajitahidi wasiache utumishi wao. Licha ya magumu ya kiuchumi, Argentina iliripoti kilele kipya cha Mashahidi 126,709 mwaka jana. Bado kuna umaskini mwingi nchini Msumbiji. Hata hivyo, kulikuwa na ongezeko la asilimia 4 na wahubiri 37,563 walishiriki kazi ya kuhubiri. Maisha ni magumu kwa watu wengi nchini Albania, hata hivyo, nchi hiyo iliripoti ongezeko la asilimia 12, na kufikia kilele cha wahubiri 2,708. Ni wazi kwamba roho ya Yehova haizuiwi na hali ngumu wakati watumishi wake wanapotanguliza Ufalme.—Mathayo 6:33.

      19. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba bado kuna watu wenye mfano wa kondoo ambao wanatamani kweli ya Biblia? (b) Ni mambo gani mengine katika ripoti ya kila mwaka yanayoonyesha kwamba watumishi wa Yehova wanaendelea kukaa macho kiroho? (Ona chati kwenye ukurasa wa 12-15.)

      19 Wastani wa mafunzo ya Biblia 5,309,289 ulimwenguni pote yaliyoripotiwa mwaka jana unaonyesha kwamba bado kuna watu wengi wenye mfano wa kondoo wanaotamani kweli ya Biblia. Miongoni mwa kilele kipya cha watu 15,597,746 waliohudhuria Ukumbusho, wengi wao hawamtumikii Yehova. Na waendelee kuzidisha ujuzi na upendo kwa Yehova na kwa ndugu zao. Inafurahisha kuona kwamba “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” unaendelea kupata matokeo mazuri huku wakimtumikia Muumba “mchana na usiku katika hekalu lake” pamoja na ndugu zao waliotiwa mafuta kwa roho.—Ufunuo 7:9, 15; Yohana 10:16.

      Tunayojifunza Kutoka kwa Loti

      20. Mfano wa Loti na mke wake unatufunza nini?

      20 Bila shaka, hata watumishi waaminifu wa Mungu wanaweza kusahau kwa muda umuhimu wa nyakati wanamoishi. Mfikirie Loti, mtoto wa ndugu ya Abrahamu. Alijulishwa na malaika wawili kwamba Mungu alikuwa karibu kuharibu Sodoma na Gomora. Loti hakushangazwa na habari hizo kwa sababu ‘alitaabishwa sana na kujitia mno kwa watu wanaokaidi sheria katika mwenendo mlegevu.’ (2 Petro 2:7) Hata hivyo, malaika wawili walipokuja kumtoa Sodoma, ‘alikawia-kawia.’ Karibu malaika wamkokote yeye na familia yake kutoka katika jiji hilo. Baadaye, mke wa Loti alipuuza onyo la malaika kwamba wasitazame nyuma. Alipoteza maisha yake kwa sababu ya mtazamo wake wa kutojali. (Mwanzo 19:14-17, 26) “Mkumbukeni mke wa Loti,” Yesu akaonya.—Luka 17:32.

      21. Kwa nini huu ndio wakati muhimu zaidi wa kukaa macho?

      21 Msiba uliopata jiji la Pompeii na Herculaneum, mambo yaliyotukia wakati Yerusalemu lilipoharibiwa, na vilevile wakati wa Furiko la Noa na siku za Loti yanaonyesha umuhimu wa kuchukua maonyo kwa uzito. Tukiwa watumishi wa Yehova, tunatambua ishara ya wakati wa mwisho. (Mathayo 24:3) Tumejitenga na dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 18:4) Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tunahitaji “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” (2 Petro 3:12) Naam, huu ndio wakati muhimu zaidi wa kukaa macho! Tunaweza kuchukua hatua gani, na tunaweza kusitawisha sifa gani ili tukae macho? Makala inayofuata itazungumzia mambo hayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Haielekei kwamba Yerusalemu lilikuwa na wakazi zaidi ya 120,000 katika karne ya kwanza. Eusebius anakadiria kwamba wakazi 300,000 kutoka mkoa wa Yudea walisafiri hadi Yerusalemu kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 70 W.K. Bila shaka, wengine waliokufa walitoka sehemu nyingine za milki hiyo.

      b Bila shaka, kulingana na maoni ya Yehova, agano jipya lilichukua mahali pa Sheria ya Musa mwaka wa 33 W.K.—Waefeso 2:15.

  • “Fulizeni Kulinda”!
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 1
    • “Fulizeni Kulinda”!

      “Lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.”—MARKO 13:37.

      1, 2. (a) Mtu mmoja alijifunza nini kuhusu kulinda mali zake? (b) Kielezi cha Yesu kuhusu mwizi kinatufunza nini kuhusu kukaa macho?

      JUAN aliweka vitu vyake vyenye thamani nyumbani. Aliviweka mahali alipodhani ni salama zaidi, yaani, mvunguni mwa kitanda chake. Hata hivyo, usiku mmoja alipokuwa amelala usingizi pamoja na mke wake, mwizi aliingia kwenye chumba cha kulala. Ni wazi kwamba mwizi huyo alijua kabisa mahali ambapo angepata kutafuta vitu hivyo. Alichukua kila kitu chenye thamani kutoka mvunguni mwa kitanda pamoja na pesa ambazo Juan alikuwa ameziweka kwenye droo ya meza iliyokuwa kando ya kitanda. Aligundua asubuhi iliyofuata kwamba pesa na vitu vyake vyenye thamani vimeibwa. Atakumbuka kwa muda mrefu jambo lenye kuhuzunisha alilojifunza: Mtu ambaye amelala usingizi hawezi kulinda mali zake.

      2 Ndivyo ilivyo katika maana ya kiroho. Hatuwezi kulinda tumaini na imani yetu iwapo tumelala. Kwa hiyo, Paulo anatuhimiza hivi: “Acheni tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali acheni tukae macho na kutunza hisi zetu.” (1 Wathesalonike 5:6) Ili kuonyesha umuhimu wa kukaa macho, Yesu alitumia kielezi cha mwizi. Alitaja matukio ambayo yangetangulia kuja kwake akiwa Hakimu, kisha akaonya hivi: “Kwa hiyo, fulizeni kulinda kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja. Lakini jueni jambo moja, kwamba ikiwa mwenye nyumba angalijua ni katika lindo gani mwizi anakuja, angalifuliza kuwa macho na hangaliruhusu nyumba yake ivunjwe na kuingiwa. Kwa sababu hiyo nyinyi pia jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.” (Mathayo 24:42-44) Mwizi hasemi wakati atakapokuja. Yeye angependa kuja wakati asipotarajiwa. Vivyo hivyo, kama Yesu alivyosema, mwisho wa mfumo huu utakuja kwenye ‘saa tusiyoifikiri kuwa hiyo.’

      “Kaeni Macho, Simameni Imara Katika Imani”

      3. Yesu alionyeshaje umuhimu wa kukaa macho kwa kutumia kielezi cha watumwa wanaomsubiri bwana wao arudi kutoka kwenye arusi?

      3 Katika maneno ya Injili ya Luka, Yesu aliwafananisha Wakristo na watumwa wanaomsubiri bwana wao arudi kutoka kwenye arusi. Wanahitaji kuwa chonjo ili ajapo wawe macho, tayari kumpokea. Kwa njia hiyohiyo, Yesu alisema: “Kwenye saa msiyofikiri yaelekea kuwa, Mwana wa binadamu anakuja.” (Luka 12:40) Huenda wengine ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi wakakosa kutambua umuhimu wa nyakati tunamoishi. Huenda hata wakakata kauli kwamba mwisho uko mbali sana. Lakini kufikiri kwa njia hiyo kunaweza kufanya tupuuze mambo ya kiroho na kuzingatia miradi ya kimwili, mambo yanayoweza kutufanya tusinzie kiroho.—Luka 8:14; 21:34, 35.

      4. Ni nini kitakachotusadikisha na kutuchochea tuendelee kulinda, na Yesu alionyeshaje jambo hilo?

      4 Kielezi cha Yesu kinaweza kutufunza jambo jingine. Ijapokuwa watumwa hao hawakujua saa ambayo bwana wao angewasili, yaonekana walijua usiku ambao angewasili. Haingekuwa rahisi kukaa macho usiku kucha ikiwa wangefahamu kwamba bwana wao hangewasili usiku huo. Lakini sivyo, walijua usiku ambao angewasili, na jambo hilo likawachochea kukaa macho. Kwa njia kama hiyo, unabii wa Biblia huonyesha waziwazi kwamba tunaishi wakati wa mwisho; lakini hautuambii siku au saa ya mwisho. (Mathayo 24:36) Tukiamini kwamba mwisho unakuja tutakaa macho, lakini tukiwa na uhakika kwamba siku ya Yehova imekaribia kweli, tutachochewa hata zaidi kuendelea kulinda.—Sefania 1:14.

      5. Tunaweza kuitikiaje himizo la Paulo la ‘kukaa macho’?

      5 Paulo aliwaandikia Wakorintho na kuwahimiza hivi: “Kaeni macho, simameni imara katika imani.” (1 Wakorintho 16:13) Naam, kukaa macho kunahusiana na kuwa na msimamo imara katika imani ya Kikristo. Tunawezaje kukaa macho? Kwa kujifunza Neno la Mungu kwa kina zaidi. (2 Timotheo 3:14, 15) Mazoea mazuri ya kujifunza na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida hutusaidia kuimarisha imani yetu na kuiweka akilini siku ya Yehova na hilo ni jambo muhimu kuhusiana na imani yetu. Tukisoma mara kwa mara uthibitisho wa kimaandiko kwamba mfumo huu unakaribia kwisha, hatutasahau kweli muhimu kuhusu mwisho huo.a Pia ni vizuri kufikiria matukio ya ulimwengu yanayotimiza unabii wa Biblia. Ndugu mmoja nchini Ujerumani aliandika hivi: “Kila wakati ninapotazama habari—vita, matetemeko ya ardhi, jeuri, na kuchafuliwa kwa sayari yetu—mambo hayo hukazia kwamba mwisho umekaribia.”

      6. Yesu alionyeshaje kwamba tunaweza kushindwa kuendelea kukaa macho kiroho kadiri muda unavyosonga?

      6 Katika Marko sura ya 13, tunaona simulizi lingine la Yesu akiwasihi wafuasi wake wakae macho. Kulingana na sura hiyo, Yesu analinganisha hali yao na ya mtunza-mlango anayesubiri bwana wake arudi kutoka safari ya ng’ambo. Mtunza-mlango hakujua saa ambayo bwana wake angerudi. Alipaswa kufuliza kulinda. Yesu alitaja malindo manne ambayo bwana angeweza kuwasili. Lindo la nne lilianza mwendo wa saa tisa za usiku hadi jua linapochomoza. Kwenye lindo hilo la nne, ni rahisi mtunza-mlango aanze kusinzia. Inasemekana kwamba, askari wanaona kuwa wakati unaofaa kumkamata adui ni kabla ya mapambazuko. Vivyo hivyo, wakati huu wa mwisho, ambapo ulimwengu umelala kabisa kiroho, huenda ikatubidi tujitahidi hata zaidi kukaa macho. (Waroma 13:11, 12) Kwa hiyo, katika kielezi chake, Yesu anatusihi hivi mara kadhaa: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho . . . Kwa hiyo fulizeni kulinda . . . Lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.”—Marko 13:32-37.

      7. Tunakabili hatari gani, na kwa kufikiria hatari hiyo, tunapata kitia-moyo gani mara kwa mara tunaposoma Biblia?

      7 Katika huduma yake, na baada ya kufufuliwa, mara nyingi Yesu alikazia umuhimu wa kukaa macho. Kwa kweli, karibu kila mara Maandiko yanapotaja mwisho wa mfumo huu wa mambo, tunaona onyo la kukaa macho au kufuliza kulinda.b (Luka 12:38, 40; Ufunuo 3:2; 16:14-16) Ni wazi kwamba, kuna hatari kubwa ya kusinzia kiroho. Sisi sote tunahitaji maonyo hayo!—1 Wakorintho 10:12; 1 Wathesalonike 5:2, 6.

      Mitume Watatu Walioshindwa Kukaa Macho

      8. Katika bustani ya Gethsemane, mitume watatu wa Yesu waliitikiaje ombi lake kwamba wafulize kulinda?

      8 Kukaa macho kunahitaji mengi zaidi ya kuwa na nia njema, kama vile kielelezo cha Petro, Yakobo, na Yohana kinavyoonyesha. Wanaume hao watatu walikuwa watu wa kiroho waliomfuata Yesu kwa uaminifu na waliompenda sana. Hata hivyo, usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., walishindwa kukaa macho. Walipoondoka kwenye chumba cha juu ambapo walikuwa wakisherehekea Sikukuu ya Kupitwa, mitume hao watatu waliambatana na Yesu hadi kwenye bustani ya Gethsemane. Wakiwa huko, Yesu aliwaambia hivi: “Nafsi yangu ina kihoro sana, hata kufikia kifo. Kaeni hapa na kufuliza kulinda pamoja nami.” (Mathayo 26:38) Yesu alisali kwa bidii mara tatu kwa Baba yake wa mbinguni, naye alirudi mara tatu mahali rafiki zake walipokuwa na kukuta wamelala.—Mathayo 26:40, 43, 45.

      9. Yaelekea ni nini kilichofanya mitume wasinzie?

      9 Kwa nini wanaume hao wenye imani walimkatisha Yesu tamaa usiku huo? Walikuwa wamechoka. Ilikuwa usiku sana, labda baada ya saa sita usiku, na “macho yao yalikuwa mazito” kwa usingizi. (Mathayo 26:43) Hata hivyo, Yesu alisema: “Fulizeni kulinda na kusali kwa kuendelea, ili msipate kuingia ndani ya jaribu. Bila shaka, roho ni yenye hamu, lakini mwili ni dhaifu.”—Mathayo 26:41.

      10, 11. (a) Licha ya uchovu, ni nini kilichomsaidia Yesu kufuliza kulinda katika bustani ya Gethsemane? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo lililowapata mitume watatu Yesu alipowaomba wafulize kulinda?

      10 Bila shaka, Yesu pia alikuwa amechoka usiku huo muhimu. Hata hivyo, badala ya kulala, Yesu alitumia wakati huo muhimu wa mwisho akiwa huru kusali kwa bidii. Siku chache zilizotangulia, alikuwa amewahimiza wafuasi wake wasali hivi: “Basi, fulizeni kuwa macho wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:36; Waefeso 6:18) Tukitii onyo la Yesu na kuiga kielelezo chake kizuri kuhusiana na sala, sala zetu za kutoka moyoni tunazomtolea Yehova zitatusaidia kukaa macho kiroho.

      11 Bila shaka, Yesu alielewa—ingawa wakati huo wafuasi wake hawakuelewa jambo hilo—kwamba baada ya muda mfupi angekamatwa na kuuawa. Angejaribiwa na hatimaye kufa kifo chenye maumivu makali kwenye mti wa mateso. Yesu alikuwa amewaonya mitume wake kuhusu mambo hayo, lakini hawakuelewa. Kwa hiyo, walilala alipokuwa macho akisali. (Marko 14:27-31; Luka 22:15-18) Kama vile mitume, mwili wetu pia ni dhaifu na kuna mambo ambayo bado hatuyajui. Hata hivyo, tusipotambua kwamba tunaishi nyakati muhimu, tunaweza kulala usingizi wa kiroho. Tunaweza kukaa macho tu kwa kuwa chonjo.

      Sifa Tatu Muhimu

      12. Ni sifa gani tatu ambazo Paulo anahusianisha na kutunza hisi zetu?

      12 Tunawezaje kutambua umuhimu wa nyakati tunamoishi? Tayari tumeona umuhimu wa sala na uhitaji wa kuweka akilini siku ya Yehova. Kwa kuongezea, Paulo anataja sifa tatu muhimu tunazopaswa kusitawisha. Anasema: “Kwa habari yetu sisi tulio wa mchana, acheni tutunze hisi zetu na kuwa tumevaa bamba la kifuani la imani na upendo na kama kofia ya chuma lile tumaini la wokovu.” (1 Wathesalonike 5:8) Na tuchunguze kifupi jinsi ambavyo imani, tumaini, na upendo hutusaidia kuendelea kukaa macho kiroho.

      13. Imani hutusaidiaje tuendelee kukaa chonjo?

      13 Lazima tuwe na imani isiyotikisika kwamba Yehova yuko na kwamba “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Kutimizwa kwa mara ya kwanza kwa unabii wa Yesu unaohusu mwisho katika karne ya kwanza kunaimarisha imani yetu kwamba unabii huo utatimizwa kwa kiwango kikubwa wakati wetu. Nayo imani yetu hufanya tutazamie kwa hamu siku ya Yehova, tukiwa na uhakika kwamba “[njozi ya kiunabii] haina budi kuja, haitakawia.”—Habakuki 2:3.

      14. Kuwa na tumaini kunawezaje kutusaidia sana kukaa macho?

      14 Tumaini letu ni kama “nanga ya nafsi” ambayo hutusaidia tuvumilie magumu hata kama itatubidi kungojea kutimizwa kwa ahadi hakika za Mungu. (Waebrania 6:18, 19) Margaret, dada aliyetiwa mafuta kwa roho ambaye ana umri wa miaka 90 na kitu na ambaye alibatizwa miaka 70 iliyopita, asema hivi: “Mume wangu alipokuwa mahututi kwa ugonjwa wa kansa mwaka wa 1963, nilitamani mwisho ufike upesi. Lakini sasa ninaona kwamba nilikuwa nikijifikiria tu. Wakati huo hatukujua kazi ingeenea hadi sehemu gani za dunia. Hata sasa, kuna maeneo mengi ambapo kazi imeanza kufanywa hivi karibuni tu. Kwa hiyo ninafurahi kwamba Yehova ameonyesha subira.” Mtume Paulo anatuhakikishia hivi: “Uvumilivu, [hutokeza] hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini, nalo tumaini haliongozi kwenye kukata tamaa.”—Waroma 5:3-5.

      15. Upendo utatuchocheaje hata ikionekana kana kwamba tumengoja kwa muda mrefu?

      15 Upendo wa Kikristo ni sifa ya pekee kwa sababu ndiyo msingi wa mambo yote tunayofanya. Tunamtumikia Yehova kwa sababu tunampenda, si kwa kufikiria tu ratiba yake. Upendo kwa jirani hutuchochea tuhubiri habari njema ya Ufalme, hata kama Mungu atataka tufanye hivyo muda mrefu kadiri gani au turudi kwa nyumba zilezile mara ngapi. Kama Paulo alivyoandika, “kwabaki imani, tumaini, upendo, matatu haya; lakini lililo kubwa zaidi sana kati ya haya ni upendo.” (1 Wakorintho 13:13) Upendo hutusaidia kuvumilia na kukaa macho. “[Upendo] hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:7, 8.

      “Fuliza Kushika Sana Lile Ulilo Nalo”

      16. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani badala ya kupunguza bidii?

      16 Tunaishi nyakati muhimu ambapo matukio ya ulimwengu hutukumbusha daima kwamba tuko kwenye umalizio wa siku za mwisho. (2 Timotheo 3:1-5) Sasa si wakati wa kupunguza bidii yetu bali ‘kufuliza kushika sana lile tulilo nalo.’ (Ufunuo 3:11) Kwa “kukesha katika sala” na kusitawisha imani, tumaini, na upendo, tutakuwa tayari kuvumilia majaribu. (1 Petro 4:7) Tuna mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. Kwa kujihusisha na matendo ya ujitoaji-kimungu tutakuwa macho kabisa.—2 Petro 3:11.

      17. (a) Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo tunapotamauka mara kwa mara? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 21.) (b) Tunawezaje kumwiga Yehova, na wale wanaomwiga watapata baraka gani?

      17 Yeremia aliandika, “BWANA ndiye fungu langu, kwa hiyo nitamtumaini yeye. BWANA ni mwema kwa hao wamngojeao, kwa hiyo nafsi imtafutayo. Ni vema mtu autarajie wokovu wa BWANA.” (Maombolezo 3:24-26) Baadhi yetu tumengoja kwa muda mfupi tu. Wengine wamengoja kwa miaka mingi kuona wokovu wa Yehova. Hata hivyo, muda huo wa kungoja ni mfupi kama nini unapolinganishwa na umilele! (2 Wakorintho 4:16-18) Na tunapongoja wakati wa Yehova unaofaa, tunaweza kusitawisha sifa muhimu za Kikristo na kuwasaidia wengine wanufaike na subira ya Yehova na kukubali kweli. Kwa hiyo, sote na tufulize kulinda. Na tumwige Yehova kwa kuwa wenye subira, na kushukuru kwa tumaini ambalo ametupatia. Na tuendeleapo kwa uaminifu kukaa macho, na tushike kabisa tumaini la uhai udumuo milele. Kisha, ahadi hizi za kiunabii zitatimia kwetu: “[Yehova] atakutukuza uirithi nchi, wasio haki watakapoharibiwa utawaona.”—Zaburi 37:34.

      [Maelezo ya Chini]

      a Huenda ikafaa kupitia mambo sita yanayothibitisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” ambayo yameonyeshwa kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi, Januari 15, 2000 ukurasa wa 12-13.—2 Timotheo 3:1.

      b Akizungumzia kitenzi cha Kigiriki kilichotafsiriwa “kaa macho,” mtaalamu wa kuandika kamusi W. E. Vine asema kwamba kitenzi hicho kihalisi kinamaanisha ‘kuondoa usingizi,’ na pia ‘kinakazia jinsi ambavyo watu wanaokusudia kufanya jambo fulani hukaa macho na kulinda.’

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki