-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Waangalizi Wasafirio Waimarisha Makutaniko
Vifungo vya kitengenezo viliimarishwa zaidi likiwa tokeo la utumishi wa waangalizi wasafirio. Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alishiriki kwa kutokeza sana katika utendaji huo. Nyakati nyingine, wanaume kama vile Barnaba, Timotheo, na Tito waliushiriki pia. (Mdo. 15:36; Flp. 2:19, 20; Tito 1:4, 5) Wote walikuwa waeneza-evanjeli wenye bidii. Kwa kuongezea, walitia moyo makutaniko kwa hotuba zao. Masuala yalipozuka ambayo yangeweza kuathiri umoja wa makutaniko, yalipelekwa kwenye baraza kuu lenye kuongoza. Halafu, “walipoendelea kusafiri kuyapitia majiji,” wale waliokabidhiwa madaraka walikuwa “wakiwakabidhi wale wa huko maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu ili yashikwe.” Matokeo yakawa nini? “Makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”—Mdo. 15:1–16:5; 2 Kor. 11:28, NW.
Tayari katika miaka ya 1870, Ndugu Russell alikuwa akizuru vile vikundi vya Wanafunzi wa Biblia—vya watu wawili na vya watatu pamoja na vikundi vikubwa zaidi—ili kuwajenga kiroho. Ndugu wengine wachache walishiriki katika miaka ya 1880. Halafu, katika 1894, mipango ilifanywa kwa Sosaiti ili wasemaji waliostahili vizuri wasafiri kwa ukawaida zaidi ili kusaidia Wanafunzi wa Biblia wakue katika ujuzi na uthamini kwa ajili ya kweli na kuwavuta karibukaribu zaidi.
Ikiwezekana, msemaji alikuwa akitumia siku moja au labda siku kadhaa pamoja na kikundi, akitoa hotuba moja au mbili za watu wote na kisha, kuzuru vile vikundi vidogo zaidi na watu mmoja-mmoja ili kuzungumza mambo yenye kina zaidi ya Neno la Mungu. Jitihada ilifanywa ili kila kikundi katika Marekani na Kanada kitembelewe mara mbili kwa mwaka, ingawa kwa kawaida si ndugu yuleyule alifanya hivyo. Katika kuteua wasemaji hao wasafirio, mkazo uliwekwa juu ya upole, unyenyekevu, na uelewevu mzuri wa kweli pamoja na ushikamano kwayo wa uaminifu-mshikamanifu na uwezo wa kuifundisha kwa uwazi. Wao hawakuwa jamii ya wahudumu wenye kulipwa. Waliandaliwa tu chakula na mahali pa kulala na ndugu wenyeji, na kwa kadiri ilivyohitajiwa, Sosaiti iliwasaidia kwa gharama za usafiri. Wakaja kujulikana kuwa “mapilgrimu” (wasafiri).
Wengi kati ya wawakilishi hao wa Sosaiti wasafirio walipendwa sana na wale waliotumikia. A. H. Macmillan, Mkanada, anakumbukwa kuwa ndugu ambaye kwake Neno la Mungu lilithibitika kuwa “kama moto uwakao.” (Yer. 20:9) Alilazimika kuongea juu yalo, naye aliongea, akisema kwa wasikilizaji katika Kanada na pia katika sehemu nyingi za Marekani na nchi nyinginezo. William Hersee, pilgrimu mwingine, hukumbukwa kwa shauku nyingi kwa sababu ya uangalifu wa pekee aliowapa vijana. Sala zake pia ziliacha uvutano wenye kudumu akilini mwao kwa sababu zilionyesha hali ya kiroho yenye kina iliyovuta sana mioyo ya wote vijana kwa wazee.
Usafiri haukuwa rahisi kwa mapilgrimu katika siku hizo za mapema. Kwa kielelezo, ili kutumikia kikundi karibu na Klamath Falls, Oregon, Edward Brenisen alisafiri kwanza kwa garimoshi, kisha usiku kwa gari la kukokotwa na farasi, na hatimaye kwa kigari chenye kutikisatikisa wasafiri kilipokuwa kikisafiri milimani kuelekea kwenye shamba ambako wangekutana. Mapema asubuhi, siku baada ya mkutano wao, ndugu mmoja alimpa farasi amwendeshe kilometa zipatazo 100 kwenda kwenye kituo cha garimoshi kilichokuwa karibu zaidi ili aweze kusafiri kwenda kwenye mgawo wake uliofuata. Yalikuwa maisha magumu, lakini jitihada za mapilgrimu zilikuwa na matokeo mazuri. Watu wa Yehova waliimarishwa, wakaunganishwa pamoja katika uelewevu wao wa Neno la Mungu, na wakavutwa pamoja karibu zaidi hata ingawa walitawanyika sana kijiografia.
Katika 1926, Ndugu Rutherford alianza kutumia mipango iliyobadili kazi ya mapilgrimu kutoka ile ya wasemaji wasafirio tu kuwa ile ya wasimamizi na waendelezaji wasafirio wa utumishi wa shambani wa makutaniko. Ili kukazia madaraka yao mapya, katika 1928 waliitwa waelekezi wa utumishi wa kimkoa. Walifanya kazi pamoja na ndugu wenyeji, wakiwapa maagizo ya kibinafsi katika utumishi wa shambani. Wakati huo iliwezekana kwao kufikia kila kutaniko katika Marekani na katika baadhi ya nchi nyinginezo mara moja hivi kwa mwaka, huku wakizuru pia watu mmoja-mmoja na vikundi vidogo ambavyo havikuwa vimepangwa kitengenezo kwa ajili ya utumishi.
Wakati wa miaka iliyofuata, kazi ya waangalizi wasafirio ilipata marekebisho mbalimbali.a Ilizidishwa sana katika 1938 watumishi wote katika makutaniko walipowekwa rasmi kwa njia ya kitheokrasi. Ziara kwenye makutaniko kwa vipindi vya ukawaida wakati wa miaka michache iliyofuata zilitoa fursa ya kuandaa mazoezi ya kibinafsi kwa kila mmoja wa watumishi waliowekwa rasmi na kuongeza msaada katika utumishi wa shambani kwa kila mmoja. Katika 1942, kabla ya waangalizi wasafirio kupelekwa tena kwenye makutaniko, walipewa mafunzo mengi sana; likiwa tokeo, kazi yao ilitekelezwa kwa upatani mkubwa zaidi. Ziara zao zilikuwa fupi sana (siku moja hadi tatu, ikitegemea ukubwa wa kutaniko). Katika pindi hiyo walichunguza rekodi za kutaniko, wakakutana na watumishi wote ili kutoa shauri lolote lililohitajiwa, wakatoa hotuba moja au zaidi kwa kutaniko, na kuongoza katika utumishi wa shambani. Katika 1946 ziara zilirefushwa kuwa juma moja kwa kila kutaniko.
Katika 1938 mpango huo wa kuzuru makutaniko uliongezewa utumishi wa mtumishi wa kimkoa akiwa na daraka jipya. Alisafiri eneo kubwa zaidi, akitumia juma moja pindi kwa pindi pamoja na ndugu waliokuwa wakisafiri katika kanda ya dunia (mzunguko) kuzuru makutaniko. Wakati wa ziara yake alitumikia katika programu ya kusanyiko lililohudhuriwa na makutaniko yote katika kanda hiyo ya dunia.b Mpango huo ulikuwa kichocheo kikubwa kwa akina ndugu na uliandaa fursa ya ukawaida kwa ajili ya ubatizo wa wanafunzi wapya.
“Mtu Apendaye Utumishi”
John Booth alikuwa miongoni mwa wale walioshiriki katika utumishi huo kuanzia 1936 na ambaye, katika 1974, alipata kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Alipokuwa akihojiwa akiwa mmoja awezaye kuwa msimamizi asafiriye, aliambiwa: “Wasemaji wenye ufasaha sio wanaohitajiwa, ni mtu apendaye utumishi tu na ambaye ataongoza katika huo na kuongea juu yao kwenye mikutano.” Ndugu Booth alikuwa na upendo huo kwa ajili ya utumishi wa Yehova, kama ithibitishwavyo na utumishi wake wa bidii wa painia tangu 1928, naye alichochea bidii ya kueneza evanjeli katika wengine kwa kielelezo na maneno ya kitia-moyo pia.
Kutaniko la kwanza alilozuru, katika Machi 1936, lilikuwa katika Easton, Pennsylvania. Baadaye aliandika: “Kwa kawaida nilikuwa nikiwasili mahali ili niwahi utumishi wa shambani asubuhi, nifanye mkutano na watumishi wa kampuni mapema jioni na baadaye mwingine na kampuni nzima. Kwa kawaida nilikuwa nikitumia siku mbili tu pamoja na kampuni na siku moja tu na kikundi kidogo zaidi, nyakati nyingine nikizuru vikundi sita kama hivyo kila juma. Nilikuwa nikisafiri daima.”
Miaka miwili baadaye, katika 1938, alipewa mgawo, akiwa mtumishi wa kimkoa, asimamie kusanyiko la kanda ya dunia (sasa lajulikana kuwa kusanyiko la mzunguko) kila juma. Hilo lilisaidia kuimarisha akina ndugu wakati ambapo mnyanyaso ulikuwa ukizidi kuwa mkali katika baadhi ya maeneo. Akikumbuka siku hizo na madaraka yake tofauti-tofauti, Ndugu Booth alisema hivi: “Katika juma lilelile [ambalo nilikuwa shahidi katika kesi ya mahakama iliyohusu Mashahidi wapatao 60 katika Indianapolis, Indiana] nilikuwa mshtakiwa katika kesi nyingine katika Joliet, Illinois, na wakili wa ndugu mmoja katika [kesi] nyingine katika Madison, Indiana, na, kwa kuongezea, nilisimamia kusanyiko la kanda ya dunia kila mwisho-juma.”
Miaka miwili baada ya makusanyiko haya ya kanda ya dunia kurudishwa katika 1946 (sasa yakiwa makusanyiko ya mzunguko), Carey Barber alikuwa miongoni mwa wale waliopewa migawo wakiwa watumishi wa wilaya. Tayari alikuwa amekuwa mshiriki wa familia ya Betheli katika Brooklyn, New York, kwa miaka 25. Wilaya yake ya kwanza ilienea sehemu yote ya magharibi mwa Marekani. Mwanzoni, safari kati ya makusanyiko ilikuwa kilometa kama 1,600 kila juma. Kadiri wingi na ukubwa wa makutaniko ulivyoongezeka, umbali huo ulipungua, na makusanyiko mengi ya mzunguko yalifanywa mara nyingi katika kanda moja ya jiji. Baada ya uzoefu wa miaka 29 akiwa mwangalizi asafiriye, Ndugu Barber alialikwa arudi kwenye makao makuu ya ulimwengu katika 1977 akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza.
Katika nyakati za vita na mnyanyaso mkali, waangalizi wasafirio mara nyingi walihatarisha uhuru na maisha zao ili kutosheleza hali-njema ya kiroho ya ndugu zao. Katika wakati wa kukaliwa kwa Ubelgiji na Wanazi, André Wozniak aliendelea kuzuru makutaniko na kusaidia kuyapelekea ugavi wa fasihi. Mara nyingi Gestapo walikuwa karibu sana kumkamata lakini hawakufaulu kumnasa.
Katika Rhodesia (sasa hujulikana kuwa Zimbabwe) katika miaka ya mwisho-mwisho ya 1970, watu waliishi kwa hofu, na usafiri ulipungua wakati wa pindi ya vita ya wenyewe kwa wenyewe. Lakini waangalizi wasafirio wa Mashahidi wa Yehova, wakiwa wachungaji na waangalizi wenye upendo, walithibitika kuwa kama “mahali pa kujificha na upepo” kwa ndugu zao. (Isa. 32:2) Baadhi yao walikuwa wakitembea kwa siku kadhaa kupitia vichaka, wakisafiri kupanda na kushuka milima, wakivuka mito yenye hatari, wakilala nje usiku—yote hayo ili kufikia makutaniko na wahubiri walio peke yao, kuwatia moyo wadumu imara katika imani. Miongoni mwao alikuwa Isaiah Makore, aliyeponea chupuchupu risasi zilipokuwa zikipita juu ya kichwa chake wakati wa pigano kati ya jeshi la serikali na “wapigania uhuru.”
Waangalizi wengine wasafirio wametumikia tengenezo kimataifa kwa miaka mingi. Wasimamizi wa Watch Tower Society wamesafiri mara nyingi kwenda nchi nyinginezo kushughulikia mahitaji ya kitengenezo na kuhutubia mikusanyiko. Ziara hizo zimesaidia kuwafahamisha sana Mashahidi wa Yehova kila mahali kuhusu udugu wao wa kimataifa. Hasa Ndugu Knorr alifuatia utendaji huo kwa ukawaida, akizuru kila tawi na makao ya mishonari. Kadiri tengenezo lilivyokua, ulimwengu uligawanywa kuwa kanda kumi za dunia za kimataifa, na kuanzia Januari 1, 1956, ndugu wenye kustahili, chini ya mwelekezo wa msimamizi, walianza kusaidia kutoa utumishi huo ili uweze kushughulikiwa kwa ukawaida. Zile ziara za kanda za dunia, zifanywazo sasa chini ya mwelekezo wa Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza, huendelea kuchangia umoja wa duniani pote na mwendo wa kusonga mbele wa tengenezo zima.
-
-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 224, 225]
Waangalizi Wasafirio Wachache Kati ya Maelfu Ambao Wametumikia
Kanada, 1905-1933
Uingereza, 1920-1932
Finland, 1921-1926, 1947-1970
Marekani, 1907-1915
Kusafiri kati ya makutaniko—
Greenland
Venezuela
Lesotho
Mexico
Peru
Sierra Leone
Makao ya kuhamishwa katika Namibia
Kushiriki pamoja na Mashahidi wenyeji katika utumishi wa shambani katika Japani
Kukutana na wazee wenyeji katika Ujerumani
Kutoa shauri litumikalo kwa mapainia katika Hawaii
Kufunza kutaniko katika Ufaransa
-