-
Tuna Furaha kwa Sababu Yehova Hutuonyesha Njia YakeMnara wa Mlinzi—1999 | Mei 15
-
-
Tuna Furaha kwa Sababu Yehova Hutuonyesha Njia Yake
“Mungu njia yake ni kamilifu; ahadi ya BWANA imehakikishwa.”—2 SAMWELI 22:31.
1, 2. (a) Wanadamu wote wana uhitaji wa msingi wa kupata nini? (b) Itakuwa vema tufuate kielelezo cha nani?
WANADAMU wote wana uhitaji wa msingi wa kupata mwongozo. Kwa kweli, tunahitaji msaada wa kutuongoza maishani. Ni kweli kwamba Yehova ametupa kiasi fulani cha akili na dhamiri inayotusaidia kufahamu lililo jema na lililo baya. Lakini dhamiri yetu yahitaji kuzoezwa ikiwa itatuongoza kwa njia yenye kutegemeka. (Waebrania 5:14) Nayo akili yetu yahitaji habari sahihi—na vilevile mazoezi ya kuichanganua habari hiyo—ikiwa tutafanya maamuzi mazuri. (Mithali 2:1-5) Lakini hata baada ya kufanya hivyo, huenda maamuzi yetu yakakosa kuwa vile tunavyotaka kwa sababu ya ukosefu wa uhakika maishani. (Mhubiri 9:11) Tukijitegemea, sisi hatuna njia inayotegemeka ya kujua mambo ya wakati ujao.
2 Kwa sababu hizo na nyingine nyingi, nabii Yeremia aliandika hivi: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Yesu Kristo, yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, alikubali mwelekezo. Alisema hivi: “Mwana hawezi kufanya hata kitu kimoja kwa uanzisho wake mwenyewe, ila tu kile atazamacho Baba akifanya. Kwa maana mambo yoyote yale Huyo hufanya, mambo hayo Mwana pia hufanya kwa namna kama hiyo.” (Yohana 5:19) Basi, ni jambo la hekima kama nini kumwiga Yesu na kumtegemea Yehova atupe msaada wa kuzielekeza hatua zetu! Mfalme Daudi aliimba hivi: “Mungu njia yake ni kamilifu; ahadi ya BWANA imehakikishwa; yeye ndiye ngao yao wote wanaomkimbilia.” (2 Samweli 22:31) Tukijitahidi kutembea katika njia ya Yehova badala ya kufuata hekima yetu wenyewe, tutapata mwongozo mkamilifu. Kuikataa njia ya Mungu husababisha msiba.
Yehova Aonyesha Njia
3. Yehova aliwaongozaje Adamu na Hawa, naye aliwatolea matazamio gani?
3 Fikiria kisa cha Adamu na Hawa. Walihitaji mwelekezo hata ingawa hawakuwa na dhambi. Yehova hakuacha Adamu ajipangie kila jambo katika bustani maridadi ya Edeni. Badala yake, Mungu alimpa kazi ya kufanya. Kwanza, Adamu alipaswa kuwapa wanyama majina. Kisha, Yehova akawapa Adamu na Hawa miradi ya muda mrefu. Walipaswa kuitiisha dunia, kuijaza kwa uzao wao, na kuwatunza wanyama wa dunia. (Mwanzo 1:28) Hiyo ingekuwa kazi kubwa mno, lakini matokeo ya mwisho yangekuwa paradiso ya ulimwenguni pote iliyojaa jamii kamilifu ya kibinadamu inayoishi kwa upatano na wanyama walioumbwa. Lilikuwa tazamio zuri kama nini! Na zaidi, maadamu Adamu na Hawa wangeendelea kutembea kwa uaminifu katika njia ya Yehova, wangewasiliana naye. (Linganisha Mwanzo 3:8.) Lilikuwa pendeleo la kustaajabisha kama nini—kuwa na uhusiano wenye kuendelea na wa kibinafsi pamoja na Muumba!
4. Adamu na Hawa walionyeshaje ukosefu wa tumaini na uaminifu-mshikamanifu, na matokeo yenye msiba yalikuwa gani?
4 Yehova aliwakataza wanadamu wawili wa kwanza kula kutokana na mti wa ujuzi wa mema na mabaya uliokuwa katika Edeni, na hilo liliwapa fursa ya papohapo ya kuonyesha utii wao—tamaa yao ya kutembea katika njia ya Yehova. (Mwanzo 2:17) Hata hivyo, baada ya muda mfupi, utii huo ulijaribiwa. Shetani alipokuja na maneno yake ya udanganyifu, Adamu na Hawa walihitaji kuonyesha uaminifu-mshikamanifu wao kwa Yehova na kuzitumaini ahadi Zake ikiwa wangedumisha utii. Kwa kusikitisha, walikosa uaminifu-mshikamanifu na tumaini. Shetani alipomtolea Hawa uhuru wa kujitegemea na kumshtaki Yehova isivyo kweli kwamba anasema uwongo, Hawa alidanganyika, akakataa kumtii Mungu. Naye Adamu akajiunga naye katika dhambi. (Mwanzo 3:1-6; 1 Timotheo 2:14) Walipata hasara kubwa mno kutokana na jambo hilo. Kutembea katika njia ya Yehova kungewapa shangwe yenye kuongezeka daima huku wakitimiza mapenzi yake hatua kwa hatua. Badala yake, maisha yao yakajawa na kukata tamaa na maumivu hadi kifo.—Mwanzo 3:16-19; 5:1-5.
5. Kusudi la Yehova la muda mrefu ni nini, naye huwasaidiaje wanadamu waaminifu kuona utimizo wake?
5 Hata hivyo, Yehova hakubadili kusudi lake kwamba siku moja dunia itakuwa makao ya paradiso kwa wanadamu wakamilifu, wasio na dhambi. (Zaburi 37:11, 29) Naye hajawahi kamwe kukosa kutoa mwongozo mkamilifu kwa wale wanaotembea katika njia yake na kutumaini kuona utimizo wa ahadi hiyo. Kwetu sisi tulio na masikio ya kusikia, sauti ya Yehova iko nyuma yetu, ikisema hivi: “Njia ni hii, ifuateni.”—Isaya 30:21.
Wengine Walitembea Katika Njia ya Yehova
6. Ni wanaume gani wa kale wawili waliotembea katika njia ya Yehova, na matokeo yakawa nini?
6 Kulingana na rekodi ya Biblia, ni watu wachache tu kati ya uzao wa Adamu na Hawa waliotembea katika njia ya Yehova. Wa kwanza kati yao ni Abeli. Ingawa alikufa kifo cha mapema, alikufa akiwa katika upendeleo wa Yehova na hivyo ana tazamio hakika la kufufuliwa katika “ufufuo wa waadilifu,” katika wakati alioweka Mungu. (Matendo 24:15) Yeye ataona utimizo wa mwisho wa kusudi kubwa la Yehova kwa dunia na wanadamu. (Waebrania 11:4) Mwingine aliyetembea katika njia ya Yehova ni Enoki, ambaye unabii wake kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo umehifadhiwa katika kitabu cha Yuda. (Yuda 14, 15) Enoki pia alikufa kifo cha mapema. (Mwanzo 5:21-24) Ingawa hivyo, “alikuwa na ushahidi kwamba alikuwa amempendeza Mungu vema.” (Waebrania 11:5) Alipokufa, yeye, sawa na Abeli, alikuwa na tazamio hakika la ufufuo, naye atakuwa miongoni mwa wale watakaoona makusudi ya Yehova yakitimizwa.
7. Noa na familia yake walionyeshaje uaminifu-mshikamanifu na tumaini kwa Yehova?
7 Ulimwengu wa kabla ya Furiko ulipozidi kujaa uovu, utii kwa Yehova ukaendelea zaidi na zaidi kuwa jaribu la uaminifu-mshikamanifu. Kufikia mwisho wa ulimwengu huo, ni kikundi kidogo tu kilichopatikana kikitembea katika njia ya Yehova. Noa na familia yake walimsikiliza Mungu na kutumaini yale aliyosema. Walitimiza kwa uaminifu kazi walizopewa nao wakakataa kuingizwa katika mazoea yenye uovu ya ulimwengu wa siku hizo. (Mwanzo 6:5-7, 13-16; Waebrania 11:7; 2 Petro 2:5) Tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa sababu ya utii wao wenye uaminifu-mshikamanifu na tumaini. Kwa sababu ya utii huo, waliokoka Furiko, wakawa mababu wetu.—Mwanzo 6:22; 1 Petro 3:20.
8. Kutembea katika njia ya Mungu kulitia ndani nini kwa taifa la Israeli?
8 Baadaye, Yehova alifanya agano na wazao wa Yakobo mwaminifu, nao wakawa taifa la pekee kwake. (Kutoka 19:5, 6) Yehova aliwaelekeza watu wake wa agano kupitia Sheria iliyoandikwa, ukuhani, na mwongozo wenye kuendelea wa kiunabii. Lakini lilikuwa daraka la Waisraeli kufuata mwelekezo huo. Yehova alimwagiza nabii wake awaambie Waisraeli hivi: “Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana; baraka ni hapo mtakapoyasikia maagizo ya BWANA, Mungu wenu, niwaagizayo leo; na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya BWANA, Mungu wenu, mkikengeuka katika njia niwaagizayo leo, kwa kuandama miungu mingine msiyoijua.”—Kumbukumbu la Torati 11:26-28.
Kwa Nini Wengine Waliiacha Njia ya Yehova
9, 10. Ni kwa sababu ya hali gani Waisraeli walihitaji kumtumaini Yehova na kusitawisha uaminifu-mshikamanifu kwake?
9 Waisraeli, sawa tu na Adamu na Hawa, walihitaji kumtumaini Yehova na kuwa waaminifu-washikamanifu kwake ikiwa wangedumu wakiwa watiifu. Israeli lilikuwa taifa dogo lililozungukwa na jirani wagomvi. Misri na Ethiopia zilikuwa upande wa kusini-magharibi. Siria na Ashuru zilikuwa kaskazini-mashariki. Filistia, Amoni, Moabu, na Edomu zilikuwa katika ujirani wa karibu. Hizi nchi zote zilithibitika kuwa adui za Israeli nyakati mbalimbali. Na zaidi, zote zilifuata dini isiyo ya kweli, iliyojulikana kwa ibada ya sanamu, unajimu, na katika visa vingine, sherehe za kingono zilizopotoka kabisa na kudhabihu watoto kikatili. Jirani za Israeli walitegemea miungu yao iwape familia kubwa, mavuno mengi, na ushindi vitani.
10 Taifa la Israeli pekee ndilo lililomwabudu Mungu mmoja, Yehova. Aliwaahidi baraka za familia kubwa, mavuno mengi, na usalama dhidi ya adui ikiwa wangezitii sheria zake. (Kumbukumbu la Torati 28:1-14) Kwa kusikitisha, wengi katika Israeli hawakufanya hivyo. Wengi waliotembea katika njia ya Yehova waliteswa kwa sababu ya uaminifu-mshikamanifu wao. Hata baadhi yao waliteswa vikali, wakadhihakiwa, wakapigwa mijeledi, wakafungwa gerezani, wakapigwa mawe, na kuuawa na Waisraeli wenzao. (Matendo 7:51, 52; Waebrania 11:35-38) Hayo yalikuwa majaribu makali kama nini kwa waaminifu hao! Hata hivyo, kwa nini wengi walitoka katika njia ya Yehova? Vielelezo viwili kutoka katika historia ya Israeli vinatusaidia kuona kufikiri kwao kusikofaa.
Kielelezo Kibaya cha Ahazi
11, 12. (a) Siria lilipomtisha Ahazi, yeye alikataa kufanya nini? (b) Ahazi alitafuta usalama kutoka vyanzo gani viwili?
11 Ahazi alitawala ufalme wa kusini wa Yuda katika karne ya nane K.W.K. Utawala wake haukuwa wa amani. Wakati mmoja, Siria na ufalme wa kaskazini wa Israeli waliungana vitani dhidi yake, na “moyo wake ukataharuki, na moyo wa watu wake.” (Isaya 7:1, 2) Hata hivyo, Yehova alipotaka kumsaidia na kumwalika Ahazi amjaribu, Ahazi alikataa katakata! (Isaya 7:10-12) Matokeo yakawa kwamba, Yuda lilishindwa vitani na watu wake wengi wakauawa.—2 Mambo ya Nyakati 28:1-8.
12 Ingawa Ahazi alikataa kumjaribu Yehova, alinyenyekea, akamwomba mfalme wa Ashuru msaada. Na bado, Yuda liliendelea kuteseka mikononi mwa jirani zake. Ashuru pia lilipomgeuka Ahazi na ‘kumfadhaisha,’ mfalme “akaitolea dhabihu miungu ya Dameski iliyompiga, akasema, Kwa sababu miungu ya Wafalme wa Shamu [“Siria,” NW] imewasaidia wao, mimi nitaitolea dhabihu, ili inisaidie mimi.”—2 Mambo ya Nyakati 28:20, 23, Union Version, Chapa ya 1989.
13. Ahazi alionyesha nini kwa kuigeukia miungu ya Siria?
13 Baadaye, Yehova aliliambia Israeli hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye katika njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:17, 18) Hatua ya Ahazi ya kuigeukia miungu ya Siria ilionyesha tu vile alivyokuwa amepotoka sana kutoka ‘katika njia impasayo kuifuata.’ Kufikiri kwa mataifa kulimpotosha kabisa, naye akategemea vyanzo bandia vya usalama badala ya kumtegemea Yehova.
14. Ni kwa nini Ahazi hakuwa na sababu ya kuigeukia miungu bandia?
14 Kwa muda mrefu miungu ya mataifa, kutia ndani ile ya Siria, ilikuwa imethibitishwa kwa muda mrefu kuwa “vinyago vya miungu.” (Isaya 2:8, BHN) Mapema, wakati wa utawala wa Mfalme Daudi, ukuu wa Yehova juu ya miungu ya Siria ulionekana waziwazi wakati Wasiria walipofanywa watumishi wa Daudi. (1 Mambo ya Nyakati 18:5, 6) Ni Yehova pekee, aliye “Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye kuogofya” awezaye kutoa usalama wa kweli. (Kumbukumbu la Torati 10:17) Ingawa hivyo, Ahazi alimkataa Yehova na kuitegemea miungu ya mataifa ili kupata usalama. Matokeo yalikuwa msiba kwa Yuda.—2 Mambo ya Nyakati 28:24, 25.
Wayahudi Wakiwa na Yeremia Misri
15. Wayahudi walifanyaje dhambi huko Misri katika siku ya Yeremia?
15 Yehova aliwaruhusu Wababiloni waliharibu Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 607 K.W.K., kwa sababu watu wake walikuwa na ukosefu mbaya sana wa uaminifu-mshikamanifu. Wengi katika taifa hilo walihamishiwa Babiloni. Hata hivyo, watu kadhaa walibaki, nabii Yeremia akiwa miongoni mwao. Liwali Gedalia alipouawa kihila, kikundi hicho kilikimbilia Misri na kumchukua Yeremia pamoja nao. (2 Wafalme 25:22-26; Yeremia 43:5-7) Wakaanza kuitolea miungu bandia dhabihu wakiwa huko. Yeremia alisababu kwa bidii na Wayahudi hao wasio waaminifu, lakini wakawa wakaidi. Walikataa kumgeukia Yehova na kusisitiza kwamba wangeendelea kumtolea “malkia wa mbinguni” uvumba. Kwa nini? Kwa sababu wao na baba zao wa zamani walikuwa wakifanya hivyo ‘katika miji ya Yuda, na katika njia kuu za Yerusalemu; walipokuwa na chakula tele, na kufanikiwa, wala hawakuona mabaya.’ (Yeremia 44:16, 17) Pia, Wayahudi walibisha hivi: “Tulipoacha kumfukizia uvumba malkia wa mbinguni, na kummiminia sadaka za kinywaji, tumepungukiwa na vitu vyote; na kuangamizwa kwa upanga, na kwa njaa.”—Yeremia 44:18.
16. Ni kwa nini Wayahudi waliokuwa Misri walikosea kabisa katika kusababu kwao?
16 Kwa kweli kumbukumbu yaweza kuhifadhi tu yale yanayotupendeza! Ukweli ulikuwa nini? Ni kweli kwamba Wayahudi waliitolea miungu bandia dhabihu katika nchi aliyowapa Yehova. Nyakati nyingine, kama katika siku za Ahazi, waliteseka kwa sababu ya uasi-imani. Hata hivyo, Yehova hakuwa “mwepesi wa hasira” kwa watu wake wa agano. (Kutoka 34:6; Zaburi 86:15) Aliwatuma manabii wake ili wawasihi watubu. Mara kwa mara, mfalme alipokuwa mwaminifu, Yehova alimbariki, nao watu wakafaidika kutokana na baraka hiyo hata ingawa wengi wao hawakuwa waaminifu. (2 Mambo ya Nyakati 20:29-33; 27:1-6) Wayahudi hao huko Misri walikosea kama nini kwa kudai kuwa ufanisi wowote walioufurahia wakiwa nchini mwao ulikuwa umetoka kwa miungu yao bandia!
17. Kwa nini Yuda lilipoteza nchi na hekalu lake?
17 Kabla ya mwaka wa 607 K.W.K., Yehova alikuwa amewasihi watu wa Yuda hivi: “Sikilizeni sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu nanyi mtakuwa watu wangu; mkaende katika njia ile yote nitakayowaamuru mpate kufanikiwa.” (Yeremia 7:23) Wayahudi walipoteza hekalu na nchi yao hasa kwa sababu walikataa kutembea ‘katika njia ile yote ambayo Yehova alikuwa amewaamuru.’ Acheni tuepuke kabisa kufanya kosa lenye kuangamiza kama hilo.
Yehova Huwabariki Wale Wanaotembea Katika Njia Yake
18. Ni lazima wale wanaotembea katika njia ya Yehova wafanye nini?
18 Leo, sawa na zamani, yahitaji uaminifu-mshikamanifu ili kutembea katika njia ya Yehova—azimio la kumtumikia yeye pekee. Inahitaji tumaini—imani kamili kwamba ahadi za Yehova zinategemeka na zitatimia. Yahitaji utii ili kutembea katika njia ya Yehova—tukifuata sheria zake bila kukengeuka na kushika viwango vyake vya juu. “BWANA ndiye mwenye haki, apenda matendo ya haki.”—Zaburi 11:7.
19. Watu wengi leo huabudu miungu ipi, na matokeo ni nini?
19 Ahazi aliitegemea miungu ya Siria ili apate usalama. Waisraeli huko Misri walitumaini kwamba “malkia wa mbinguni,” mungu wa kike aliyeabudiwa sana katika Mashariki ya kale ya Kati, angewapa ufanisi wa mali. Miungu mingi leo si sanamu halisi. Yesu alionya dhidi ya kutumikia “Utajiri” badala ya Yehova. (Mathayo 6:24) Mtume Paulo alisema kuhusu “tamaa, amba[y]o ni ibada ya sanamu.” (Wakolosai 3:5) Alisema pia kuhusu wale ambao “mungu wao ni tumbo lao.” (Wafilipi 3:19) Naam, baadhi ya miungu mikuu inayoabudiwa leo ni pesa na vitu vya kimwili. Kwa kweli, wengi zaidi—kutia ndani watu wengi wa dini—‘wanaweka tumaini lao juu ya mali zisizo hakika.’ (1 Timotheo 6:17) Wengi hufanya bidii sana kuitumikia miungu hiyo, na baadhi yao hupata thawabu—kuishi katika makao bora, kuwa na vitu vya bei ghali, na kula milo ya anasa. Hata hivyo, sio wote wanaofurahia utajiri kama huo. Na hata wale walio na utajiri wanagundua hatimaye kwamba huo wenyewe hauridhishi. Huo hauna uhakika, ni wa muda mfupi, na hautoshelezi mahitaji ya kiroho.—Mathayo 5:3.
20. Twahitaji kudumisha usawaziko gani?
20 Ni kweli kwamba tunapaswa kuwa wenye busara tuendeleapo kuishi katika siku za mwisho za huu mfumo wa mambo. Tunahitaji kuchukua hatua zifaazo ili kuandalia familia zetu mahitaji ya kimwili. Lakini tukikazia sana kiwango cha juu cha maisha, kufuatia pesa, au vitu kama hivyo badala ya kumtumikia Mungu, tutakuwa tumeingia katika namna fulani ya ibada ya sanamu nasi tutakuwa hatuendelei tena kutembea katika njia ya Yehova. (1 Timotheo 6:9, 10) Ingawa hivyo, itakuwaje tukikabiliwa na matatizo ya afya, ya kifedha, au mengineyo? Acheni tusiwe kama Wayahudi huko Misri waliosema kuwa kumtumikia Mungu ndiko kulikosababisha matatizo yao. Badala yake, acheni tumjaribu Yehova, jambo ambalo Ahazi alikataa kufanya. Mgeukie Yehova Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu ili akuongoze. Fuata mwongozo wake kwa kumtumaini, na kusali ili upate nguvu na hekima ya kushughulikia hali yoyote. Kisha, ngojea kwa uhakika baraka ya Yehova.
21. Wale wanaotembea katika njia ya Yehova wanapata baraka zipi?
21 Yehova aliwabariki sana wale waliotembea katika njia yake kwa historia yote ya Israeli. Mfalme Daudi aliimba hivi: “BWANA, uniongoze kwa haki yako, kwa sababu yao wanaoniotea.” (Zaburi 5:8) Yehova alimpa ushindi wa kivita dhidi ya mataifa jirani ambayo baadaye yalimsumbua Ahazi. Chini ya utawala wa Solomoni, Waisraeli walibarikiwa kwa kupewa amani na ufanisi ambao Wayahudi huko Misri walitamani sana baadaye. Hata Yehova alimpa Hezekia mwana wa Ahazi ushindi dhidi ya Ashuru lenye nguvu. (Isaya 59:1) Naam, mkono wa Yehova haukuwa mfupi kuelekea waaminifu-washikamanifu wake, ambao hawakusimama “katika njia ya wakosaji” bali walipendezwa na sheria ya Mungu. (Zaburi 1:1, 2) Hali ingali hivyo leo. Hata hivyo, tunaweza kuwaje na uhakika kwamba tunatembea katika njia ya Yehova? Jambo hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.
-
-
Endelea Kutembea Katika Njia ya YehovaMnara wa Mlinzi—1999 | Mei 15
-
-
Endelea Kutembea Katika Njia ya Yehova
“Wewe umngoje BWANA, uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi.”—ZABURI 37:34.
1, 2. Kutembea katika njia ya Yehova kulihusisha nini kwa Mfalme Daudi, nako kunahitaji nini kutoka kwetu leo?
“UNIJULISHE njia nitakayoiendea, kwa maana nakuinulia nafsi yangu.” (Zaburi 143:8) Wakristo leo wanayarudia maneno hayo ya Mfalme Daudi kwa moyo wote. Wao wanatamani kwa unyofu kumpendeza Yehova na kutembea katika njia yake. Jambo hilo lahusisha nini? Kwa Daudi, lilimaanisha kushika sheria ya Mungu. Lilihusisha kumtumaini Yehova badala ya kufanya miungano na mataifa. Naam, na pia ilimaanisha kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu, wala sio miungu ya majirani. Kwa Wakristo, kutembea katika njia ya Yehova kunahusisha mambo mengi zaidi.
2 Sababu moja ni kwamba kutembea katika njia ya Yehova leo humaanisha kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, tukimkubali yeye kuwa “ndiyo njia na kweli na uhai.” (Yohana 3:16; 14:6; Waebrania 5:9) Yamaanisha pia kutimiza “sheria ya Kristo,” ambayo hutia ndani kuonyeshana upendo, na hasa kuelekea ndugu watiwa-mafuta wa Yesu. (Wagalatia 6:2; Mathayo 25:34-40) Wale wanaotembea katika njia ya Yehova hupenda kanuni na amri zake. (Zaburi 119:97; Mithali 4:5, 6) Wao huhazini pendeleo lao lenye thamani la kushiriki katika huduma ya Kikristo. (Wakolosai 4:17; 2 Timotheo 4:5) Sala ni jambo la kawaida katika maisha yao. (Waroma 12:12) Nao ‘hufuliza kuangalia sana kwamba jinsi wanavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima.’ (Waefeso 5:15) Kwa hakika wao hawaachilii mbali utajiri wa kiroho ili kufuatilia masilahi ya mali au raha haramu za kimwili ambazo ni za muda mfupi. (Mathayo 6:19, 20; 1 Yohana 2:15-17) Isitoshe, uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova na kumtumaini ni mambo muhimu sana. (2 Wakorintho 1:9; 10:5; Waefeso 4:24) Kwa nini? Kwa sababu hali yetu inafanana sana na ile ya Israeli la kale.
Uhitaji wa Tumaini na Uaminifu-Mshikamanifu
3. Kwa nini uaminifu-mshikamanifu, imani na tumaini vitatusaidia tuendelee kutembea katika njia ya Yehova?
3 Israeli lilikuwa taifa dogo lililozungukwa na majirani wenye uhasama ambao walishiriki sherehe za utovu wa kingono katika kuiabudu miungu ya sanamu. (1 Mambo ya Nyakati 16:26) Ni Israeli pekee lililomtumikia Mungu mmoja wa kweli na asiyeonekana, Yehova, naye alitaka wadumishe viwango vya juu vya adili. (Kumbukumbu la Torati 6:4) Vivyo hivyo, leo ni watu milioni chache tu wanaomwabudu Yehova, nao wanaishi katika ulimwengu ulio na watu karibu bilioni sita ambao viwango vyao na mitazamo yao ya kidini ni tofauti sana na vile vya hao wachache. Ikiwa sisi tumo miongoni mwa hao milioni chache, ni lazima tujilinde dhidi ya kuvutiwa kwa njia mbaya. Jinsi gani? Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu, imani katika yeye, na tumaini thabiti kwamba atatimiza ahadi zake vitatusaidia. (Waebrania 11:6) Kufanya hivyo kutatuzuia tusiweke tumaini letu katika mambo ambayo ulimwengu unayatumaini.—Mithali 20:22; 1 Timotheo 6:17.
4. Kwa nini mataifa yako “katika giza kiakili”?
4 Mtume Paulo alionyesha jinsi Wakristo wanavyopaswa kuwa tofauti na ulimwengu alipoandika hivi: “Kwa hiyo, nasema hili na kutoa ushahidi katika Bwana, kwamba nyinyi msiendelee tena kutembea kama vile mataifa watembeavyo pia katika ukosefu wa faida wa akili zao, huku wao wakiwa katika giza kiakili, na kufanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutokuwa na ujuzi ambako kumo ndani yao, kwa sababu ya ukosefu wa hisi wa mioyo yao.” (Waefeso 4:17, 18) Yesu ndiye “nuru ya kweli.” (Yohana 1:9) Wowote wanaomkataa au wanaodai kuwa wanamwamini lakini hawaitii “sheria ya Kristo” wako “katika giza kiakili.” Hawatembei hata kidogo katika njia ya Yehova, bali “[wame]fanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu.” Hata wafikiri kuwa wana hekima kadiri gani katika mambo ya kilimwengu, wao ‘hawana ujuzi ndani yao’ kuhusiana na ujuzi pekee unaoongoza kwenye uhai, ujuzi wa Yehova Mungu na Yesu Kristo.—Yohana 17:3; 1 Wakorintho 3:19.
5. Ingawa nuru ya ile kweli inang’aa katika ulimwengu, ni kwa nini mioyo mingi haiitikii?
5 Na bado, nuru ya ile kweli inang’aa katika ulimwengu! (Zaburi 43:3; Wafilipi 2:15) “Hekima hupaza sauti yake katika njia kuu.” (Mithali 1:20) Mwaka jana, Mashahidi wa Yehova walitumia zaidi ya saa bilioni moja wakizungumza na jirani zao kuhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo. Mamia ya maelfu waliitikia. Je, tushangae kwa sababu wengine wengi hawakuitikia? La. Paulo alisema kuhusu “ukosefu wa hisi wa mioyo yao.” Wengine wana mioyo isiyoitikia kwa sababu ya ubinafsi au kupenda pesa. Wengine huvutiwa na dini isiyo ya kweli au mtazamo wa kilimwengu ambao umeenea sana leo. Hali ngumu maishani zimewafanya wengi wamkatae Mungu. Wengine hukataa kutimiza viwango vya juu vya adili vya Yehova. (Yohana 3:20) Je, moyo wa mtu anayetembea katika njia ya Yehova ungeweza kukosa hisi kuhusiana na hayo?
6, 7. Ingawa walikuwa waabudu wa Yehova Mungu, Waisraeli walianguka katika pindi zipi, na kwa nini?
6 Jambo hilo lilipata taifa la Israeli la kale, kama Paulo alivyoonyesha. Yeye aliandika hivi: “Mambo hayo yalipata kuwa vielelezo vyetu sisi, ili tusiwe watu wanaotamani mambo mabaya, kama vile wao walivyoyatamani. Wala tusiwe waabudu-sanamu, kama baadhi yao walivyokuwa; kama vile imeandikwa: ‘Watu waliketi kula na kunywa, nao wakainuka wapate kujitumbuiza.’ Wala tusiwe tukifanya uasherati, kama vile baadhi yao walivyofanya uasherati, ila kuanguka, ishirini na tatu elfu kati yao katika siku moja.”—1 Wakorintho 10:6-8.
7 Kwanza, Paulo anarejezea ile pindi ambapo Israeli liliabudu ndama wa dhahabu chini ya Mlima Sinai. (Kutoka 32:5, 6) Hiyo ilikuwa hatua ya moja kwa moja ya kutotii amri ya kimungu ambayo walikuwa wamekubali kuitii majuma machache tu mapema. (Kutoka 20:4-6; 24:3) Kisha, Paulo anaurejezea wakati Israeli lilipoinamia Baali likiwa pamoja na binti za Moabu. (Hesabu 25:1-9) Ibada ya ndama ilijulikana kwa kutimiza tamaa mbaya sana za kibinafsi, ‘kujitumbuiza.’a Ibada ya Baali iliandamana na ukosefu ulio wazi wa adili katika ngono. (Ufunuo 2:14) Ni kwa nini Waisraeli walifanya dhambi hizo? Kwa sababu waliiruhusu mioyo yao ‘itamani mambo mabaya’—iwe ni ibada ya sanamu au mazoea ya utovu wa kingono ambayo yaliandamana nayo.
8. Twaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyopata Israeli?
8 Paulo alionyesha kuwa tunapaswa kujifunza kutokana na matukio hayo. Kujifunza nini? Ni jambo lisilowazika kwa Mkristo kuinamia ndama wa dhahabu au mungu wa kale wa Moabu. Lakini vipi kuhusu ukosefu wa adili au kujiingiza mno katika anasa za kibinafsi? Mambo hayo ni ya kawaida leo, nasi tukiruhusu tamaa yake isitawi katika mioyo yetu, yatatutenganisha na Yehova. Matokeo yatakuwa ni kana kwamba tumeabudu sanamu—kutenganishwa na Mungu. (Linganisha Wakolosai 3:5; Wafilipi 3:19.) Kwa kweli, Paulo amalizia mazungumzo yake kuhusu matukio hayo kwa kuwasihi waamini wenzake hivi: “Ikimbieni ibada ya sanamu.”—1 Wakorintho 10:14.
Msaada wa Kutembea Katika Njia ya Mungu
9. (a) Ni msaada gani tunaopokea ili kutusaidia tuendelee kutembea katika njia ya Yehova? (b) Tunasikia ‘neno nyuma yetu’ kwa njia gani moja?
9 Ikiwa tumeazimia kuendelea kutembea katika njia ya Yehova, hatujaachwa bila msaada. Isaya alitabiri hivi: “Masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.” (Isaya 30:21) ‘Masikio yetu’ husikiaje lile ‘neno nyuma yetu’? Naam, hakuna yeyote leo anayesikia sauti halisi au kupokea ujumbe wa kibinafsi kutoka kwa Mungu. “Neno” linalosikiwa hutujia sisi sote kwa njia ileile. Kwanza kabisa, hilo huja kupitia Maandiko yaliyopuliziwa, Biblia, ambayo ina mawazo ya Mungu na rekodi ya jinsi alivyoshughulika na wanadamu. Kwa kuwa tunakabiliwa na propaganda kutoka kwa watu ‘waliofanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu,’ tunahitaji kuisoma Biblia na kuitafakari kwa ukawaida ili tuwe na afya njema ya kiroho. Hatua hiyo itatusaidia kuepuka ‘mambo ya bure’ na kuwa ‘hodari, tulioandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (Matendo 14:14, 15; 2 Timotheo 3:16, 17) Hiyo itatuimarisha, kututia nguvu, na kutusaidia ‘kuifanikisha njia yetu.’ (Yoshua 1:7, 8) Kwa sababu hiyo, Neno la Yehova husihi hivi: “Basi, wanangu, nisikilizeni sasa; maana heri wao wazishikao amri zangu. Sikieni mafundisho, mpate hekima, wala msiikatae.”—Mithali 8:32, 33.
10. Njia ya pili ambayo kupitia hiyo tunasikia ‘neno nyuma yetu’ ni gani?
10 ‘Neno lililo nyuma yetu’ pia huja kwa njia ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” anayeandaa “chakula . . . kwa wakati ufaao.” (Mathayo 24:45-47) Njia moja ya kuandaa chakula hiki ni kupitia vichapo vilivyochapwa, vinavyotegemea Biblia, na katika miaka ya hivi karibuni chakula hiki kimekuwa kingi. Kwa mfano, kupitia gazeti la Mnara wa Mlinzi, uelewevu wetu wa unabii umeboreshwa. Kupitia jarida hili, tumetiwa moyo kuvumilia katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi licha ya hali ya kutojali inayoongezeka, tumesaidiwa kuepuka mitego, nasi tumesihiwa tusitawishe sifa nzuri za Kikristo. Tunakithamini kama nini chakula hicho cha wakati ufaao!
11. Eleza njia ya tatu ambayo kupitia hiyo tunaweza kusikia ‘neno nyuma yetu.’
11 Pia, mtumwa mwaminifu na mwenye busara huandaa chakula kupitia mikutano yetu ya kawaida. Hiyo ni pamoja na mikutano ya kutaniko, mikutano inayofanywa mara mbili kila mwaka katika mzunguko, na mikusanyiko mikubwa zaidi ya kila mwaka. Ni Mkristo gani mwaminifu asiyeyathamini makusanyiko hayo? Hiyo ni misaada muhimu sana inayotutegemeza tunapotembea katika njia ya Yehova. Kwa kuwa wengi hulazimika kutumia wakati mwingi kazini au shuleni wakishirikiana na watu wasiofuata imani yao, ushirika wa Kikristo wa kawaida unaokoa uhai kihalisi. Mikutano hutupa fursa nzuri ya “kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora.” (Waebrania 10:24) Tunawapenda ndugu zetu, nasi tunapenda kushirikiana nao.—Zaburi 133:1.
12. Mashahidi wa Yehova wameazimia kufanya nini, nao walionyeshaje hilo hivi karibuni?
12 Wakiwa wametiwa nguvu na chakula hicho cha kiroho, karibu watu milioni sita leo wanatembea katika njia ya Yehova, na mamilioni ya wengine wanajifunza Biblia ili kujua namna wanavyoweza kufanya hivyo. Je, wao wamevunjika moyo na kudhoofishwa na ule uhakika wa kwamba idadi yao ni ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya watu duniani? Kwa hakika la! Wao wameazimia kuendelea kulitii ‘neno nyuma yao,’ wakifanya mapenzi ya Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Ukiwa wonyesho wa hadharani wa azimio hilo, katika “Njia ya Mungu ya Maisha” Mikusanyiko ya Wilaya na ya Kimataifa ya mwaka wa 1998 na 1999, wajumbe walikubali azimio linaloonyesha msimamo wao wa dhati. Yafuatayo ni maandishi ya azimio hilo.
Azimio
13, 14. Mashahidi wa Yehova wana maoni gani halisi kuhusu hali ya ulimwengu?
13 “Sisi, Mashahidi wa Yehova tuliokusanyika kwenye Mkusanyiko huu wa “Njia ya Mungu ya Maisha” twakubali kwa moyo wote kwamba njia ya Mungu ndiyo njia bora ya maisha. Hata hivyo, sisi twatambua kwamba leo wanadamu walio wengi wanahisi tofauti. Wanadamu wamejaribu dhana nyingi, falsafa nyingi, na mawazo mengi ya kidini juu ya njia bora zaidi ya maisha. Kuitazama kikweli historia ya kibinadamu na hali za ulimwengu leo kwathibitisha ukweli wa maneno ya Mungu yaliyorekodiwa kwenye Yeremia 10:23: ‘Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.’
14 “Kila siku twaona ushuhuda zaidi wa kuthibitisha ukweli wa maneno hayo. Sehemu kubwa ya jamii ya kibinadamu hupuuza njia ya Mungu ya maisha. Watu hufuatia kinachoonekana kuwa sawa machoni pao. Kufanya hivyo kumetokeza msiba—kuvunjika kwa maisha ya familia, watoto wakiachwa bila mwongozo; kufuatia sana vitu vya kimwili, kukitokeza utupu na hali ya kukata tumaini; uhalifu na ujeuri wa kipumbavu, ukiua idadi kubwa ya watu; mizozo na vita vya kikabila, vikiua watu wengi; ukosefu wa adili wenye kuenea, ukieneza maradhi yenye kupitishwa kingono. Haya ni baadhi tu ya matatizo mengi magumu ambayo hutatiza ufuatiaji wa furaha, amani, na usalama.
15, 16. Ni uamuzi gani ulioonyeshwa katika azimio hilo kuhusu njia ya Mungu ya maisha?
15 “Kwa sababu ya hali ya wanadamu yenye kusikitisha na kukaribia kwa ‘vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,’ Har–Magedoni (Ufunuo 16:14, 16), sisi tukiwa Mashahidi wa Yehova twaazimia kwamba:
16 “Kwanza: Twajiona wenyewe kuwa mali ya Yehova Mungu, tukiwa tumejiweka wakfu kwake sisi wenyewe bila masharti, nasi tutadumisha imani isiyotikisika katika uandalizi wa Yehova wa fidia kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. Tumeazimia kutembea katika njia ya Mungu ya maisha, tukitumikia tukiwa Mashahidi wake na kujitiisha chini ya enzi kuu kama ionyeshwavyo kupitia utawala wa Yesu Kristo.
17, 18. Mashahidi wa Yehova wataendelea kudumisha msimamo gani kuhusiana na viwango vya adili na udugu wa Kikristo?
17 “Pili: Tutaendelea kushikamana na viwango vya juu vya kiadili na vya kiroho vya Biblia. Tumeazimia kutotembea kama mataifa watembeavyo katika ukosefu wa faida wa akili zao. (Waefeso 4:17-19) Tumeazimia kubaki safi mbele za Yehova na bila doa kutokana na ulimwengu huu.—Yakobo 1:27.
18 “Tatu: Tutashikilia sana msimamo wetu wa Kimaandiko tukiwa udugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote. Tutadumisha kutokuwamo kwa Kikristo miongoni mwa mataifa, bila kujiruhusu wenyewe tunaswe katika chuki au mgawanyiko wa kitaifa, au wa kikabila.
19, 20. (a) Wazazi Wakristo watafanya nini? (b) Wakristo wote wa kweli wataendelea kujitambulishaje kuwa wanafunzi wa Kristo?
19 “Nne: Sisi tulio wazazi tutakaza kikiki njia ya Mungu katika watoto wetu. Tutaweka kielelezo kwa kuishi maisha ya Kikristo, kutia ndani kusoma Biblia kwa ukawaida, funzo la familia, na kushiriki kwa nafsi yote katika kutaniko la Kikristo na katika huduma ya shambani.
20 “Tano: Sisi sote tutajitahidi kusitawisha sifa za kimungu zinazoonyeshwa na Muumba wetu, nasi tutajitahidi kuiga utu wake na njia zake, kama alivyofanya Yesu. (Waefeso 5:1) Tumeazimia kuacha mambo yetu yote yatendeke kwa upendo, hivyo kujitambulisha wenyewe kuwa wanafunzi wa Kristo.—Yohana 13:35.
21-23. Mashahidi wa Yehova wataendelea kufanya nini, nao wamesadikishwa kuhusu nini?
21 “Sita: Tutaendelea bila kuacha kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, kufanya wanafunzi, nasi tutawaagiza katika njia ya Mungu ya maisha na kuwatia moyo wapokee mazoezi zaidi kwenye mikutano ya kutaniko.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Waebrania 10:24, 25.
22 “Saba: Tukiwa watu mmoja-mmoja na tukiwa tengenezo la kidini, tutaendelea kutanguliza mapenzi ya Mungu maishani mwetu. Tukitumia Neno lake, Biblia, kuwa mwongozo wetu, hatutageuka kulia wala kushoto, hivyo kuthibitisha kwamba njia ya Mungu ni bora zaidi kuliko njia za ulimwengu. Tumeazimia kufuata njia ya Mungu ya maisha—kwa uthabiti, na kwa uaminifu-mshikamanifu, sasa na milele!
23 “Twafanya azimio hili kwa sababu tuna uhakika kabisa katika ahadi yenye upendo ya Yehova kwamba yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu adumu milele. Twafanya azimio hili kwa sababu twasadiki kwamba kuishi kwa kanuni, shauri, na onyo la upole la Kimaandiko kwatokeza njia bora ya maisha leo na huweka msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili tupate kushika imara uhai ulio halisi. (1 Timotheo 6:19; 2 Timotheo 4:7b, 8) Zaidi ya yote, twafanya azimio hili kwa sababu sisi twampenda Yehova Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, akili yetu yote, na nguvu zetu zote!
24, 25. Ni nini lililokuwa itikio kwa azimio lililopendekezwa, na wale wanaotembea katika njia ya Yehova wameazimia kufanya nini?
24 “Wote wanaohudhuria mkusanyiko huu wanaokubali azimio hili, tafadhali semeni NDIYO!”
25 Mamia ya nyanja na stediamu ulimwenguni pote zilivuma huku wahudhuriaji wote wakijibu “NDIYO!” kwa ngurumo. Mashahidi wa Yehova hawana shaka kwamba wataendelea kutembea katika njia ya Yehova. Wao wana tumaini kamili katika Yehova na imani kuwa atatimiza ahadi zake. Wao wanadumu wakiwa waaminifu-washikamanifu kwake, haidhuru jambo gani litokee. Nao wameazimia kufanya mapenzi yake.
“Mungu Yuko Upande Wetu”
26. Wale wanaotembea katika njia ya Yehova wako katika hali gani yenye furaha?
26 Mashahidi wa Yehova hukumbuka himizo la mtunga-zaburi: “Wewe umngoje BWANA, uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi.” (Zaburi 37:34) Wao hawayasahau maneno ya Paulo yenye kutia moyo: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu? Yeye ambaye hakumwachilia hata Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, kwa nini pia yeye pamoja naye hatatupa sisi kwa fadhili vitu vingine vyote?” (Waroma 8:31, 32) Ndiyo, tukiendelea kutembea katika njia ya Yehova, atatuandalia “vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.” (1 Timotheo 6:17) Kuna mahali gani pengine panapoweza kuwa bora kuliko pale tulipo—kutembea katika njia ya Yehova, tukiwa pamoja na ndugu na dada zetu wapendwa. Yehova akiwa upande wetu, na tuazimie kudumu hapo na kuvumilia hadi mwisho, tukiwa na uhakika kamili kwamba katika wakati wake alioweka, tutaona akitimiza ahadi zake zote.—Tito 1:2.
-