Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 5/15 kur. 15-20
  • Endelea Kutembea Katika Njia ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Endelea Kutembea Katika Njia ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uhitaji wa Tumaini na Uaminifu-Mshikamanifu
  • Msaada wa Kutembea Katika Njia ya Mungu
  • Azimio
  • “Mungu Yuko Upande Wetu”
  • Je, Utatembea Pamoja na Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kutembea Pamoja na Mungu—Hatua za Mwanzo-Mwanzo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Enenda kwa Imani!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Je! Wewe Unatembea katika Jina la Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 5/15 kur. 15-20

Endelea Kutembea Katika Njia ya Yehova

“Wewe umngoje BWANA, uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi.”—ZABURI 37:34.

1, 2. Kutembea katika njia ya Yehova kulihusisha nini kwa Mfalme Daudi, nako kunahitaji nini kutoka kwetu leo?

“UNIJULISHE njia nitakayoiendea, kwa maana nakuinulia nafsi yangu.” (Zaburi 143:8) Wakristo leo wanayarudia maneno hayo ya Mfalme Daudi kwa moyo wote. Wao wanatamani kwa unyofu kumpendeza Yehova na kutembea katika njia yake. Jambo hilo lahusisha nini? Kwa Daudi, lilimaanisha kushika sheria ya Mungu. Lilihusisha kumtumaini Yehova badala ya kufanya miungano na mataifa. Naam, na pia ilimaanisha kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu, wala sio miungu ya majirani. Kwa Wakristo, kutembea katika njia ya Yehova kunahusisha mambo mengi zaidi.

2 Sababu moja ni kwamba kutembea katika njia ya Yehova leo humaanisha kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, tukimkubali yeye kuwa “ndiyo njia na kweli na uhai.” (Yohana 3:16; 14:6; Waebrania 5:9) Yamaanisha pia kutimiza “sheria ya Kristo,” ambayo hutia ndani kuonyeshana upendo, na hasa kuelekea ndugu watiwa-mafuta wa Yesu. (Wagalatia 6:2; Mathayo 25:34-40) Wale wanaotembea katika njia ya Yehova hupenda kanuni na amri zake. (Zaburi 119:97; Mithali 4:5, 6) Wao huhazini pendeleo lao lenye thamani la kushiriki katika huduma ya Kikristo. (Wakolosai 4:17; 2 Timotheo 4:5) Sala ni jambo la kawaida katika maisha yao. (Waroma 12:12) Nao ‘hufuliza kuangalia sana kwamba jinsi wanavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima.’ (Waefeso 5:15) Kwa hakika wao hawaachilii mbali utajiri wa kiroho ili kufuatilia masilahi ya mali au raha haramu za kimwili ambazo ni za muda mfupi. (Mathayo 6:19, 20; 1 Yohana 2:15-17) Isitoshe, uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova na kumtumaini ni mambo muhimu sana. (2 Wakorintho 1:9; 10:5; Waefeso 4:24) Kwa nini? Kwa sababu hali yetu inafanana sana na ile ya Israeli la kale.

Uhitaji wa Tumaini na Uaminifu-Mshikamanifu

3. Kwa nini uaminifu-mshikamanifu, imani na tumaini vitatusaidia tuendelee kutembea katika njia ya Yehova?

3 Israeli lilikuwa taifa dogo lililozungukwa na majirani wenye uhasama ambao walishiriki sherehe za utovu wa kingono katika kuiabudu miungu ya sanamu. (1 Mambo ya Nyakati 16:26) Ni Israeli pekee lililomtumikia Mungu mmoja wa kweli na asiyeonekana, Yehova, naye alitaka wadumishe viwango vya juu vya adili. (Kumbukumbu la Torati 6:4) Vivyo hivyo, leo ni watu milioni chache tu wanaomwabudu Yehova, nao wanaishi katika ulimwengu ulio na watu karibu bilioni sita ambao viwango vyao na mitazamo yao ya kidini ni tofauti sana na vile vya hao wachache. Ikiwa sisi tumo miongoni mwa hao milioni chache, ni lazima tujilinde dhidi ya kuvutiwa kwa njia mbaya. Jinsi gani? Uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu, imani katika yeye, na tumaini thabiti kwamba atatimiza ahadi zake vitatusaidia. (Waebrania 11:6) Kufanya hivyo kutatuzuia tusiweke tumaini letu katika mambo ambayo ulimwengu unayatumaini.—Mithali 20:22; 1 Timotheo 6:17.

4. Kwa nini mataifa yako “katika giza kiakili”?

4 Mtume Paulo alionyesha jinsi Wakristo wanavyopaswa kuwa tofauti na ulimwengu alipoandika hivi: “Kwa hiyo, nasema hili na kutoa ushahidi katika Bwana, kwamba nyinyi msiendelee tena kutembea kama vile mataifa watembeavyo pia katika ukosefu wa faida wa akili zao, huku wao wakiwa katika giza kiakili, na kufanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutokuwa na ujuzi ambako kumo ndani yao, kwa sababu ya ukosefu wa hisi wa mioyo yao.” (Waefeso 4:17, 18) Yesu ndiye “nuru ya kweli.” (Yohana 1:9) Wowote wanaomkataa au wanaodai kuwa wanamwamini lakini hawaitii “sheria ya Kristo” wako “katika giza kiakili.” Hawatembei hata kidogo katika njia ya Yehova, bali “[wame]fanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu.” Hata wafikiri kuwa wana hekima kadiri gani katika mambo ya kilimwengu, wao ‘hawana ujuzi ndani yao’ kuhusiana na ujuzi pekee unaoongoza kwenye uhai, ujuzi wa Yehova Mungu na Yesu Kristo.—Yohana 17:3; 1 Wakorintho 3:19.

5. Ingawa nuru ya ile kweli inang’aa katika ulimwengu, ni kwa nini mioyo mingi haiitikii?

5 Na bado, nuru ya ile kweli inang’aa katika ulimwengu! (Zaburi 43:3; Wafilipi 2:15) “Hekima hupaza sauti yake katika njia kuu.” (Mithali 1:20) Mwaka jana, Mashahidi wa Yehova walitumia zaidi ya saa bilioni moja wakizungumza na jirani zao kuhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo. Mamia ya maelfu waliitikia. Je, tushangae kwa sababu wengine wengi hawakuitikia? La. Paulo alisema kuhusu “ukosefu wa hisi wa mioyo yao.” Wengine wana mioyo isiyoitikia kwa sababu ya ubinafsi au kupenda pesa. Wengine huvutiwa na dini isiyo ya kweli au mtazamo wa kilimwengu ambao umeenea sana leo. Hali ngumu maishani zimewafanya wengi wamkatae Mungu. Wengine hukataa kutimiza viwango vya juu vya adili vya Yehova. (Yohana 3:20) Je, moyo wa mtu anayetembea katika njia ya Yehova ungeweza kukosa hisi kuhusiana na hayo?

6, 7. Ingawa walikuwa waabudu wa Yehova Mungu, Waisraeli walianguka katika pindi zipi, na kwa nini?

6 Jambo hilo lilipata taifa la Israeli la kale, kama Paulo alivyoonyesha. Yeye aliandika hivi: “Mambo hayo yalipata kuwa vielelezo vyetu sisi, ili tusiwe watu wanaotamani mambo mabaya, kama vile wao walivyoyatamani. Wala tusiwe waabudu-sanamu, kama baadhi yao walivyokuwa; kama vile imeandikwa: ‘Watu waliketi kula na kunywa, nao wakainuka wapate kujitumbuiza.’ Wala tusiwe tukifanya uasherati, kama vile baadhi yao walivyofanya uasherati, ila kuanguka, ishirini na tatu elfu kati yao katika siku moja.”—1 Wakorintho 10:6-8.

7 Kwanza, Paulo anarejezea ile pindi ambapo Israeli liliabudu ndama wa dhahabu chini ya Mlima Sinai. (Kutoka 32:5, 6) Hiyo ilikuwa hatua ya moja kwa moja ya kutotii amri ya kimungu ambayo walikuwa wamekubali kuitii majuma machache tu mapema. (Kutoka 20:4-6; 24:3) Kisha, Paulo anaurejezea wakati Israeli lilipoinamia Baali likiwa pamoja na binti za Moabu. (Hesabu 25:1-9) Ibada ya ndama ilijulikana kwa kutimiza tamaa mbaya sana za kibinafsi, ‘kujitumbuiza.’a Ibada ya Baali iliandamana na ukosefu ulio wazi wa adili katika ngono. (Ufunuo 2:14) Ni kwa nini Waisraeli walifanya dhambi hizo? Kwa sababu waliiruhusu mioyo yao ‘itamani mambo mabaya’—iwe ni ibada ya sanamu au mazoea ya utovu wa kingono ambayo yaliandamana nayo.

8. Twaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyopata Israeli?

8 Paulo alionyesha kuwa tunapaswa kujifunza kutokana na matukio hayo. Kujifunza nini? Ni jambo lisilowazika kwa Mkristo kuinamia ndama wa dhahabu au mungu wa kale wa Moabu. Lakini vipi kuhusu ukosefu wa adili au kujiingiza mno katika anasa za kibinafsi? Mambo hayo ni ya kawaida leo, nasi tukiruhusu tamaa yake isitawi katika mioyo yetu, yatatutenganisha na Yehova. Matokeo yatakuwa ni kana kwamba tumeabudu sanamu—kutenganishwa na Mungu. (Linganisha Wakolosai 3:5; Wafilipi 3:19.) Kwa kweli, Paulo amalizia mazungumzo yake kuhusu matukio hayo kwa kuwasihi waamini wenzake hivi: “Ikimbieni ibada ya sanamu.”—1 Wakorintho 10:14.

Msaada wa Kutembea Katika Njia ya Mungu

9. (a) Ni msaada gani tunaopokea ili kutusaidia tuendelee kutembea katika njia ya Yehova? (b) Tunasikia ‘neno nyuma yetu’ kwa njia gani moja?

9 Ikiwa tumeazimia kuendelea kutembea katika njia ya Yehova, hatujaachwa bila msaada. Isaya alitabiri hivi: “Masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema, Njia ni hii, ifuateni; mgeukapo kwenda mkono wa kulia, na mgeukapo kwenda mkono wa kushoto.” (Isaya 30:21) ‘Masikio yetu’ husikiaje lile ‘neno nyuma yetu’? Naam, hakuna yeyote leo anayesikia sauti halisi au kupokea ujumbe wa kibinafsi kutoka kwa Mungu. “Neno” linalosikiwa hutujia sisi sote kwa njia ileile. Kwanza kabisa, hilo huja kupitia Maandiko yaliyopuliziwa, Biblia, ambayo ina mawazo ya Mungu na rekodi ya jinsi alivyoshughulika na wanadamu. Kwa kuwa tunakabiliwa na propaganda kutoka kwa watu ‘waliofanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu,’ tunahitaji kuisoma Biblia na kuitafakari kwa ukawaida ili tuwe na afya njema ya kiroho. Hatua hiyo itatusaidia kuepuka ‘mambo ya bure’ na kuwa ‘hodari, tulioandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (Matendo 14:14, 15; 2 Timotheo 3:16, 17) Hiyo itatuimarisha, kututia nguvu, na kutusaidia ‘kuifanikisha njia yetu.’ (Yoshua 1:7, 8) Kwa sababu hiyo, Neno la Yehova husihi hivi: “Basi, wanangu, nisikilizeni sasa; maana heri wao wazishikao amri zangu. Sikieni mafundisho, mpate hekima, wala msiikatae.”—Mithali 8:32, 33.

10. Njia ya pili ambayo kupitia hiyo tunasikia ‘neno nyuma yetu’ ni gani?

10 ‘Neno lililo nyuma yetu’ pia huja kwa njia ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” anayeandaa “chakula . . . kwa wakati ufaao.” (Mathayo 24:45-47) Njia moja ya kuandaa chakula hiki ni kupitia vichapo vilivyochapwa, vinavyotegemea Biblia, na katika miaka ya hivi karibuni chakula hiki kimekuwa kingi. Kwa mfano, kupitia gazeti la Mnara wa Mlinzi, uelewevu wetu wa unabii umeboreshwa. Kupitia jarida hili, tumetiwa moyo kuvumilia katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi licha ya hali ya kutojali inayoongezeka, tumesaidiwa kuepuka mitego, nasi tumesihiwa tusitawishe sifa nzuri za Kikristo. Tunakithamini kama nini chakula hicho cha wakati ufaao!

11. Eleza njia ya tatu ambayo kupitia hiyo tunaweza kusikia ‘neno nyuma yetu.’

11 Pia, mtumwa mwaminifu na mwenye busara huandaa chakula kupitia mikutano yetu ya kawaida. Hiyo ni pamoja na mikutano ya kutaniko, mikutano inayofanywa mara mbili kila mwaka katika mzunguko, na mikusanyiko mikubwa zaidi ya kila mwaka. Ni Mkristo gani mwaminifu asiyeyathamini makusanyiko hayo? Hiyo ni misaada muhimu sana inayotutegemeza tunapotembea katika njia ya Yehova. Kwa kuwa wengi hulazimika kutumia wakati mwingi kazini au shuleni wakishirikiana na watu wasiofuata imani yao, ushirika wa Kikristo wa kawaida unaokoa uhai kihalisi. Mikutano hutupa fursa nzuri ya “kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora.” (Waebrania 10:24) Tunawapenda ndugu zetu, nasi tunapenda kushirikiana nao.—Zaburi 133:1.

12. Mashahidi wa Yehova wameazimia kufanya nini, nao walionyeshaje hilo hivi karibuni?

12 Wakiwa wametiwa nguvu na chakula hicho cha kiroho, karibu watu milioni sita leo wanatembea katika njia ya Yehova, na mamilioni ya wengine wanajifunza Biblia ili kujua namna wanavyoweza kufanya hivyo. Je, wao wamevunjika moyo na kudhoofishwa na ule uhakika wa kwamba idadi yao ni ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya watu duniani? Kwa hakika la! Wao wameazimia kuendelea kulitii ‘neno nyuma yao,’ wakifanya mapenzi ya Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Ukiwa wonyesho wa hadharani wa azimio hilo, katika “Njia ya Mungu ya Maisha” Mikusanyiko ya Wilaya na ya Kimataifa ya mwaka wa 1998 na 1999, wajumbe walikubali azimio linaloonyesha msimamo wao wa dhati. Yafuatayo ni maandishi ya azimio hilo.

Azimio

13, 14. Mashahidi wa Yehova wana maoni gani halisi kuhusu hali ya ulimwengu?

13 “Sisi, Mashahidi wa Yehova tuliokusanyika kwenye Mkusanyiko huu wa “Njia ya Mungu ya Maisha” twakubali kwa moyo wote kwamba njia ya Mungu ndiyo njia bora ya maisha. Hata hivyo, sisi twatambua kwamba leo wanadamu walio wengi wanahisi tofauti. Wanadamu wamejaribu dhana nyingi, falsafa nyingi, na mawazo mengi ya kidini juu ya njia bora zaidi ya maisha. Kuitazama kikweli historia ya kibinadamu na hali za ulimwengu leo kwathibitisha ukweli wa maneno ya Mungu yaliyorekodiwa kwenye Yeremia 10:23: ‘Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.’

14 “Kila siku twaona ushuhuda zaidi wa kuthibitisha ukweli wa maneno hayo. Sehemu kubwa ya jamii ya kibinadamu hupuuza njia ya Mungu ya maisha. Watu hufuatia kinachoonekana kuwa sawa machoni pao. Kufanya hivyo kumetokeza msiba—kuvunjika kwa maisha ya familia, watoto wakiachwa bila mwongozo; kufuatia sana vitu vya kimwili, kukitokeza utupu na hali ya kukata tumaini; uhalifu na ujeuri wa kipumbavu, ukiua idadi kubwa ya watu; mizozo na vita vya kikabila, vikiua watu wengi; ukosefu wa adili wenye kuenea, ukieneza maradhi yenye kupitishwa kingono. Haya ni baadhi tu ya matatizo mengi magumu ambayo hutatiza ufuatiaji wa furaha, amani, na usalama.

15, 16. Ni uamuzi gani ulioonyeshwa katika azimio hilo kuhusu njia ya Mungu ya maisha?

15 “Kwa sababu ya hali ya wanadamu yenye kusikitisha na kukaribia kwa ‘vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,’ Har–Magedoni (Ufunuo 16:14, 16), sisi tukiwa Mashahidi wa Yehova twaazimia kwamba:

16 “Kwanza: Twajiona wenyewe kuwa mali ya Yehova Mungu, tukiwa tumejiweka wakfu kwake sisi wenyewe bila masharti, nasi tutadumisha imani isiyotikisika katika uandalizi wa Yehova wa fidia kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. Tumeazimia kutembea katika njia ya Mungu ya maisha, tukitumikia tukiwa Mashahidi wake na kujitiisha chini ya enzi kuu kama ionyeshwavyo kupitia utawala wa Yesu Kristo.

17, 18. Mashahidi wa Yehova wataendelea kudumisha msimamo gani kuhusiana na viwango vya adili na udugu wa Kikristo?

17 “Pili: Tutaendelea kushikamana na viwango vya juu vya kiadili na vya kiroho vya Biblia. Tumeazimia kutotembea kama mataifa watembeavyo katika ukosefu wa faida wa akili zao. (Waefeso 4:17-19) Tumeazimia kubaki safi mbele za Yehova na bila doa kutokana na ulimwengu huu.—Yakobo 1:27.

18 “Tatu: Tutashikilia sana msimamo wetu wa Kimaandiko tukiwa udugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote. Tutadumisha kutokuwamo kwa Kikristo miongoni mwa mataifa, bila kujiruhusu wenyewe tunaswe katika chuki au mgawanyiko wa kitaifa, au wa kikabila.

19, 20. (a) Wazazi Wakristo watafanya nini? (b) Wakristo wote wa kweli wataendelea kujitambulishaje kuwa wanafunzi wa Kristo?

19 “Nne: Sisi tulio wazazi tutakaza kikiki njia ya Mungu katika watoto wetu. Tutaweka kielelezo kwa kuishi maisha ya Kikristo, kutia ndani kusoma Biblia kwa ukawaida, funzo la familia, na kushiriki kwa nafsi yote katika kutaniko la Kikristo na katika huduma ya shambani.

20 “Tano: Sisi sote tutajitahidi kusitawisha sifa za kimungu zinazoonyeshwa na Muumba wetu, nasi tutajitahidi kuiga utu wake na njia zake, kama alivyofanya Yesu. (Waefeso 5:1) Tumeazimia kuacha mambo yetu yote yatendeke kwa upendo, hivyo kujitambulisha wenyewe kuwa wanafunzi wa Kristo.—Yohana 13:35.

21-23. Mashahidi wa Yehova wataendelea kufanya nini, nao wamesadikishwa kuhusu nini?

21 “Sita: Tutaendelea bila kuacha kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, kufanya wanafunzi, nasi tutawaagiza katika njia ya Mungu ya maisha na kuwatia moyo wapokee mazoezi zaidi kwenye mikutano ya kutaniko.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Waebrania 10:24, 25.

22 “Saba: Tukiwa watu mmoja-mmoja na tukiwa tengenezo la kidini, tutaendelea kutanguliza mapenzi ya Mungu maishani mwetu. Tukitumia Neno lake, Biblia, kuwa mwongozo wetu, hatutageuka kulia wala kushoto, hivyo kuthibitisha kwamba njia ya Mungu ni bora zaidi kuliko njia za ulimwengu. Tumeazimia kufuata njia ya Mungu ya maisha—kwa uthabiti, na kwa uaminifu-mshikamanifu, sasa na milele!

23 “Twafanya azimio hili kwa sababu tuna uhakika kabisa katika ahadi yenye upendo ya Yehova kwamba yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu adumu milele. Twafanya azimio hili kwa sababu twasadiki kwamba kuishi kwa kanuni, shauri, na onyo la upole la Kimaandiko kwatokeza njia bora ya maisha leo na huweka msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili tupate kushika imara uhai ulio halisi. (1 Timotheo 6:19; 2 Timotheo 4:7b, 8) Zaidi ya yote, twafanya azimio hili kwa sababu sisi twampenda Yehova Mungu kwa moyo wetu wote, nafsi yetu yote, akili yetu yote, na nguvu zetu zote!

24, 25. Ni nini lililokuwa itikio kwa azimio lililopendekezwa, na wale wanaotembea katika njia ya Yehova wameazimia kufanya nini?

24 “Wote wanaohudhuria mkusanyiko huu wanaokubali azimio hili, tafadhali semeni NDIYO!”

25 Mamia ya nyanja na stediamu ulimwenguni pote zilivuma huku wahudhuriaji wote wakijibu “NDIYO!” kwa ngurumo. Mashahidi wa Yehova hawana shaka kwamba wataendelea kutembea katika njia ya Yehova. Wao wana tumaini kamili katika Yehova na imani kuwa atatimiza ahadi zake. Wao wanadumu wakiwa waaminifu-washikamanifu kwake, haidhuru jambo gani litokee. Nao wameazimia kufanya mapenzi yake.

“Mungu Yuko Upande Wetu”

26. Wale wanaotembea katika njia ya Yehova wako katika hali gani yenye furaha?

26 Mashahidi wa Yehova hukumbuka himizo la mtunga-zaburi: “Wewe umngoje BWANA, uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi.” (Zaburi 37:34) Wao hawayasahau maneno ya Paulo yenye kutia moyo: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu? Yeye ambaye hakumwachilia hata Mwana wake mwenyewe bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, kwa nini pia yeye pamoja naye hatatupa sisi kwa fadhili vitu vingine vyote?” (Waroma 8:31, 32) Ndiyo, tukiendelea kutembea katika njia ya Yehova, atatuandalia “vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.” (1 Timotheo 6:17) Kuna mahali gani pengine panapoweza kuwa bora kuliko pale tulipo—kutembea katika njia ya Yehova, tukiwa pamoja na ndugu na dada zetu wapendwa. Yehova akiwa upande wetu, na tuazimie kudumu hapo na kuvumilia hadi mwisho, tukiwa na uhakika kamili kwamba katika wakati wake alioweka, tutaona akitimiza ahadi zake zote.—Tito 1:2.

[Maelezo ya Chini]

a Akilirejezea neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa “wapate kujitumbuiza,” mwelezaji mmoja asema kuwa linarejezea dansi zilizofanywa kwenye sherehe za kipagani na kuongezea hivi: “Hizi dansi nyingi, kama inavyojulikana sana, zilikusudiwa kuamsha uchu wenye utovu mkubwa sana wa kingono.”

Je, Wakumbuka?

◻ Ni jambo gani linalohitajiwa ili Mkristo atembee katika njia ya Yehova?

◻ Ni kwa nini tunahitaji kusitawisha tumaini katika Yehova na uaminifu-mshikamanifu kwake?

◻ Ni msaada gani uliopo tuendeleapo kutembea katika njia ya Yehova?

◻ Taja baadhi ya mambo makuu ya azimio lililokubaliwa kwenye Mikusanyiko ya “Njia ya Mungu ya Maisha.”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Azimio muhimu lilikubaliwa kwenye “Njia ya Mungu ya Maisha” Mikusanyiko ya Wilaya na ya Kimataifa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki