Enenda kwa Imani!
“Sikuzote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa, wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. Maana twaenenda kwa imani, si kwa kuona.”—2 WAKORINTHO 5:6, 7.
(Makala ya Funzo la Kitabu)
1. Ni baadhi ya baraka gani tunazofurahia kwa sababu ya jicho la kibinadamu?
MOJA la maajabu ya mwili wa kibinadamu ni jicho. Kwa msaada wa kiungo hiki chenye kustaajabisha kinachopiga picha, si kwamba tu tunaepuka vikwazo bali pia tunaona vitu vingi sana, vingi kati yavyo vikiwa na matokeo juu ya uhusiano wetu na wengine. Ni wazi kwamba Mbuni wa jicho hakukusudia tupapase-papase katika makao yetu ya sayari tukiwa gizani. Zaidi ya hayo, lilikuwa kusudi lake kwamba tuone na kufurahia viumbe vyake vizuri ajabu—wanadamu na wanyama, milima na mito, maziwa ya maji na bahari, maua na mimea mingine, anga na uzuri wenye fahari wa jua likishuka. Watazamaji wenye kuthamini wanaweza kutamka hivi pamoja na mtunga-zaburi: “Jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.”—Zaburi 104:24.
2. Kwa sababu gani haitoshi kuenenda kwa kuona, na Paulo alisema nini katika habari hiyo?
2 Lakini, ingawa kuona vitu vya halisi ni kuzuri ajabu, kutembea kwa kuona halisi peke yake kunaambatana na hatari kubwa. Ikiwa tutafurahia kibali ya kimungu, ni lazima tutembee kwa imani katika Mbuni wa jicho la kibinadamu. Ni lazima tutafute mwelekezo wake ili tuzoee yaliyo mema. Akiandikia Wakristo wenzake waliopakwa mafuta, mtume Paulo kwa kufaa alisema: “Sikuzote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa, wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. Maana twaenenda kwa imani, si kwa kuona. Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana [kwa kufa na kufufuliwa kwenye uzima wa kimbingu]. Kwa hiyo, tena, ikiwa tupo hapa, imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyotenda, kwamba ni mema au mabaya.”—2 Wakorintho 5:6-10.
3. Tamaa ya watumishi wote wa Yehova walio wakfu yapasa kuwa nini, na ni maswali gani yanayostahili kuchunguzwa na sisi?
3 Watumishi wote wa Yehova walio wakfu—wawe ni mabaki waliopakwa mafuta au “mkutano mkubwa” wenye kuongezeka wenye matumaini ya kidunia—wanataka kuzoea yaliyo mema. (Ufunuo 7:9) Lakini ni kwa sababu gani inaweza kusemwa kuna hatari kubwa katika ‘kuenenda kwa kuona’? Na maana yake ni nini ‘kuenenda kwa imani’?
Hatari za ‘Kuenenda kwa Kuona’
4. (a) Kwa sababu gani tusilichukue kila jambo kwa maelekeo yake ya nje? (b) Muundaji wa jicho anayaonaje mambo?
4 Tukilichukua kila jambo kijuu-juu na kutegemea linavyoonekana nje, kuna hatari ya kudanganywa tuumie. Kwa mfano, mtu anaweza kuwa akitembea kwenye uwanja wenye nyasi na kujikuta ghafula ametumbukia ndani ya shimo. Au mtu huenda akaacha kujihadhari kwa sababu ya maelekeo ya kirafiki ya mtu ambaye kumbe ni ‘mbwamwitu aliyevaa mavazi ya kondoo.’ (Mathayo 7:15) Kwa hiyo ni lazima tukeshe. Muundaji wa jicho haongozwi na sura za nje. Alimwambia nabii Samweli hivi: “[Yehova] haangalii kama binadamu aangaliavyo, maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali [Yehova] huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Kweli kweli, aliyeunda jicho anatambua mawazo na sikuzote ni sahihi. (Linganisha Waebrania 4:12.) Kwa sababu ya kuona kwake kukamilifu na ufahamu wake mkamilifu, kwa kweli yeye Ndiye anayeona yote.
5. Kwa sababu gani ni jambo la maana sana tutangulie kuonywa juu ya hatari za ‘kuenenda kwa kuona’?
5 Lakini, kwa kuwa sisi ni wanadamu tu, hatuwezi kutambua vizuri yaliyo katika moyo wa mtu mwingine. Hata tukiwa na akili zetu tulizopewa na Mungu, sisi hatujakamilika na mara nyingi tunaweza kudanganywa. Kwa kweli, huenda moyo wetu wenyewe ukatudanganya, kwa maana “huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha.” (Yeremia 17:9) Kwa hiyo ni jambo la maana sana kwamba tutangulie kuonywa juu ya hatari za ‘kuenenda kwa kuona.’ Je! Yehova ametoa uandalizi wa uhitaji huo wa maana sana? Hakika amefanya hivyo! Ili kutuagiza, ameandikisha maandishi ya matukio mengine yenye kutokeza yanayoonyesha hatari za kuenenda kwa kuona tu.—Warumi 15:4.
6. ‘Kuenenda kwa kuona’ kulikuwa na matokeo gani juu ya Waisraeli?
6 Yaliyowapata watu wa kale wa Mungu, Waisraeli, yanaonyesha hilo sana. Hata ingawa mwelekezo usiokosea wa Yehova ulikuwa unapatikana kwa taifa hilo lililopendelewa sana, umati wa watu walo wasio na imani wakiwa wenye shingo ngumu walienenda “katika mashauri yao.” (Zaburi 81:12) ‘Wakienenda kwa kuona,’ waligeukia ibada ya sanamu au miungu yenye kuonekana kwa macho ya asili. Wakiwa wanaongozwa na sura za nje, walitetemeka kwa kuogopa hesabu kubwa sana za maadui wao. Zaidi ya hayo, kwa sababu ya ‘kuenenda kwa kuona, wala si kwa imani,’ Waisraeli pia walikaidi uongozi wa Musa aliopewa na Mungu na kulalamika juu ya fungu lao maishani. (Linganisha Yuda 16.) Ndiyo, na inaelekea wengi wao waliangalia kwa kijicho ule ulioonekana kuwa uhuru na fanaka katika mataifa jirani, wakapuuza uhakika wa kwamba watu hao walikuwa na maadili yaliyoshuka sana na walikuwa chini ya uongozi wa kishetani.—Mambo ya Walawi 18:1-3, 30.
7. Ilikuwaje kwa Waisraeli waliokataa uongozi wa kimungu?
7 Ilikuwaje kwa Waisraeli ambao waling’ang’ania kwenda ki-vyao, wakakataa uongozi wa kimungu? Yehova aliacha kupendezwa nao, akaacha kuwalinda hata wakashindwa na maadui wao! Hata katika Nchi ya Ahadi, mara nyingi Waisraeli walikuwa watumwa wa maadui wao wasio na huruma. (Waamuzi 2:17-23) Tofauti na Musa, aliyekataa kufurahia raha za jamii yenye kutawala ya Misri, watu wa Israeli walitafuta “kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo” nao hawakuendelea kuenenda ‘kama wamwonaye yeye asiyeonekana.’ Walikosa imani. Na kumbuka, “pasipo imani haiwezekani kumpendeza [Mungu].”—Waebrania 3:16-19; 11:6, 24-27.
8. Ni kwa sababu gani watumishi wa kisasa wa Yehova wanapaswa kuonywa na yaliyowapata Waisraeli wa kale?
8 Watumishi wa Yehova wa kisasa wanaweza kuonyeka kwa matukio ya wakati uliopita. Sisi, pia, tumo katika hatari ya kuwa dhaifu katika imani au hata kupoteza imani yetu. Je! si kweli kwamba tunaweza kuvutwa isivyofaa na maelekeo ya nje ya mambo na hivyo tuanze tena ‘kuenenda kwa kuona’? Ndiyo, na ndiyo sababu Yehova alitoa kwa fadhili uongozi kwa ajili ya wale ambao wangemtumikia katika imani. Alitumia Waisraeli na shughuli zake ziwe masomo kwa ajili ya vizazi vya baadaye, kutia kizazi chetu. (1 Wakorintho 10:11) Hivyo tunaimarishwa na maarifa sahihi, na tumaini lenye nguvu, na uvumilivu.
9. Kama ‘tungeenda kwa kuona,’ tungeweza kuwa na maoni gani juu ya mambo fulani fulani na juu ya mipango ya kitheokrasi?
9 Pasipo mwelekezo huo hakika, kutoka kwa Muumba wetu mwenye upendo, tungekuwa katika hatari ya kumtilia shaka Musa Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, tukisahau kwamba Mungu na Kristo wanaelekeza Wakristo wa kweli leo. (Linganisha 1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:24.) Huenda tukawa na maoni kwamba tengenezo la Mashahidi wa Yehova limetokana na wanadamu na kwa hiyo huenda tukajiona huru kufanya ambayo yanaonekana ni sawa machoni petu wenyewe. (Linganisha Waamuzi 21:25.) Kuongezea hayo, tunaweza kuanguka katika kosa la wengine ambao inaonekana wanafikiri kwamba maadamu mwendo fulani wa kutenda hausumbui dhamiri yao, hakuna ubaya. Huenda wengine wakaanza kufikiri kwamba tengenezo la kitheokrasi liko ili liwafae na kuwafaidi na kwamba matakwa yalo yote yanapasa kurahisishwa, wasitakiwe wajinyime. Hatari nyingine yaweza kuwa ni wazo la kwamba mipango ya tengenezo yapasa kupatanishwa na mapenzi yetu badala ya kuwa imepatanishwa na mapenzi ya Mungu. Lakini, aliye Mfano wetu, Yesu Kristo, sikuzote alifanya mapenzi ya Babaye wa kimbingu akiwa na furaha.—Zaburi 40:8; Waebrania 10:5-10.
10. Kungeweza kuwa na matokeo gani juu ya maoni yetu kuelekea huduma ya shambani na utendaji mwingine wa kitheokrasi kama tukipuuza au kudharau mwelekezo wa kimungu?
10 Kwa sababu ya kutoangalia uongozi wa kimungu au kwa sababu ya kuudharau, huenda wengine wakafikiri mikutano yetu yapasa kufanywa iwe mifupi zaidi, mahali pa kufanyia kusanyiko hapapasi kuwa mbali sana, na vitabu vya kujifunza vyapasa kuwa rahisi sikuzote, kwamba visiwe kamwe na “chakula kigumu.” (Waebrania 5:12) Katika nchi ambako Wakristo wanafurahia amani na utulivu, huenda wengine wakaziona baraka za Ufalme vivi hivi, wakiwa na maoni kwamba hakupasi kuwa jitihada katika utumishi mtakatifu. Tukisitawisha maoni hayo, huenda hata sisi tukawa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” Labda tuwe tunaweka kando karibu kila mwisho-juma kwa ajili ya tafrija badala ya kutumia wakati huo katika huduma ya shambani na utendaji mwingine wa kitheokrasi unaoonyesha kujitoa kwa moyo wote kwa Yehova. (2 Timotheo 3:1, 4) Ikiwa hivyo, je, tungeweza kusema kwamba kweli kweli ‘tunaenenda kwa imani, si kwa kuona’?
11. Kujibembeleza kunaweza kuwa na matokeo gani, lakini kuna uhitaji wa sisi kufanya nini?
11 Pia kuna hatari ya kujibembeleza. Ni rahisi kujifanya tufikiri kwamba kuumwa kidogo na kichwa au tatizo jingine kama hilo ni kubwa kuliko lilivyo kikweli. Mwili wetu usiokamilika huenda ukatusukuma tutumie jambo hilo kama udhuru wa kutotimiza daraka fulani, kama vile kutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Lakini je, yaweza ikawa kwamba hatungeruhusu nia iyo hiyo ituzuie tusishiriki katika tafrija ya namna fulani? Bila shaka, tunapaswa kutumia akili timamu na kutopunguza uzito wa dalili za magonjwa makubwa. Hata hivyo, tunahitaji kujikaza kwa bidii. (Luka 13:24) Na kwa hakika imani yapasa kushiriki sehemu kubwa katika maamuzi yetu ili ‘tusienende kwa kuona’ tu, kwa kupatana na mashauri yetu yasiyofaa.—Warumi 12:1-3.
12. Tunajikuta katika vita ya aina gani, na inataka maoni gani upande wetu?
12 Usisahau kamwe kwamba tumo katika vita dhidi ya majeshi maovu ya roho. (Waefeso 6:11-18) Adui yetu mkuu, Shetani Ibilisi, anaweza kuwa na uvutano mkubwa sana juu yetu kwa kutumia silaha zake zilizokusudiwa ziharibu imani yetu katika Yehova. Shetani atavutia maelekeo yetu ya kichoyo yaliyorithiwa katika wanadamu wala hatakosa kutumia ushawishi wo wote unaoweza kuvuta kando kufikiri kwetu. Ikiwa tunashirikiana na “waliosalia” wa “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu, au tengenezo la kimbingu, tumo katika vita. Ni vita ambayo hatuwezi kupumzika mpaka Yehova, ambaye anatutia nguvu tusimame dhidi ya mashambulio ya kishetani, atakapokomesha tengenezo lote la Ibilisi. (Ufunuo 12:16, 17; 1 Petro 5:6-11) Kwa hiyo, je, sasa si tunapaswa kuwa wenye uhodari na kuona mambo yanayotaka hatua ya haraka? Kwa hakika ndivyo!—Zaburi 31:24.
Maana ya ‘Kuenenda Katika Imani’
13. Maana yake nini ‘kuenenda kwa imani’?
13 ‘Kuenenda katika imani’ kunamaanisha kusonga mbele kupitia hali ngumu tukiwa na imani katika Mungu, katika uwezo wake wa kuongoza hatua zetu, na katika nia yake ya kuhakikisha tuko salama. (Zaburi 22:3-5; Waebrania 11:6) Kunamaanisha kukataa kuongozwa na maelekeo ya nje tu ya mambo au kwa kufikiri kwa kibinadamu kusikofaa. Imani itatusukuma tutembee kuelekea upande ambao Yehova anatuonyesha, hata njia hiyo iwe ngumu kama nini. ‘Tukienenda kwa imani,’ tutakuwa kama Daudi, aliyesema hivi juu ya Mungu: “Utanijulisha njia ya uzima; mbele za uso wako ziko furaha tele; na katika mkono wako wa kuume mna mema ya milele.” (Zaburi 16:11) Kuongezea hayo, tukimruhusu Yehova aelekeze hatua zetu, atatupa amani ya akili naye atatusaidia tushinde, hata upinzani uwe mkubwa kama nini. (Yohana 16:33; Wafilipi 4:6, 7) Kati ya mambo mengine, ‘kuenenda kwa imani’ kutatupeleka kwa ukawaida katika ushirikiano na ndugu na dada zetu wa kiroho kwa ajili ya funzo la Biblia na sala ya umoja.—Waebrania 10:24, 25.
14, 15. (a) Maoni ya Yesu kuelekea utajiri, cheo, na kujiingiza katika siasa yalikuwa nini? (b) Kama inavyoonyeshwa katika Maandiko, Yesu alikuwa na maoni gani juu ya uongozi wa Mungu?
14 Kama ilivyo, ‘kuenenda kwa imani’ pia kunatufanya tuwe wenzi wa watumishi waaminifu wa Yehova wa wakati uliopita. Aliyekuwa mkuu kati yao alikuwa Yesu Kristo, “mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu.” Tunapojitahidi ‘kufuata nyayo zake,’ tunaonaje?—Waebrania 12:1-3; 1 Petro 2:21.
15 Yesu aliepuka kujiingiza katika siasa za kilimwengu wala hakutafuta kamwe utajiri na cheo ambacho wengi walikuwa wakifuatia. Badala yake, alitaja kwamba Ufalme wake haukuwa “sehemu ya ulimwengu huu,” na kinyume kabisa cha kuwa mwenye kutafuta mali, ‘hakuwa na mahali pa kulaza kichwa chake.’ (Yohana 6:14, 15; 18:36, NW; Luka 9:57, 58) Ingawa Yesu alikuwa na akili kamilifu, hakutenda kwa kujitegemea bali alitafuta uongozi wa Babaye wa kimbingu.—Yohana 8:28, 29.
16. Kwa sababu ya mfano wa Yesu, ingeweza kusemwa nini juu ya maoni ya Mashahidi wa Yehova?
16 Kwa sababu ya mfano wa Yesu, inaweza kusemwa nini juu ya Mashahidi wa Yehova leo? Tukiwa wateteaji wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu, tunaheshimu ‘mamlaka kuu’ za kiserikali lakini tunadumisha kutokuwamo katika mambo ya kisiasa. (Warumi 13:1-7; Mathayo 6:9, 10; Yohana 17:16) Badala ya kutafuta utajiri na cheo katika ulimwengu huu, ‘tunatafuta kwanza Ufalme,’ tukiwa na uhakika kwamba Yehova atatoa mambo tunayohitaji maishani. (Mathayo 6:24-34; Zaburi 37:25) Na kama Yesu, sisi ‘hatutegemei akili zetu wenyewe’ bali kwa shukrani tunakubali uongozi wa Mungu wetu wa upendo. (Mithali 3:5, 6) Hakika, yote hayo yanatusaidia ‘tuenende kwa imani.’
Majaribu na Baraka
17. Watu wa Yehova wanapaswa kuvumilia nini ‘wanapoenenda kwa imani’? Tafadhali onyesha jinsi ilivyo hivyo.
17 Katika nchi nyingi mashahidi wenzetu wa Yehova wanalazimika kuvumilia shida na dhiki zisizo za kawaida, hata mateso ya ukatili, ‘wanapoenenda kwa imani.’ Bila shaka, majaribu ya imani yanatokea kwa namna mbalimbali. Kwa mfano, fikiria magumu na utumishi wa uaminifu wa ndugu mmoja mzee-mzee wa Ecuador. Aliupata ukweli akiwa na miaka 80, halafu akajifunza kusoma na kuandika. Alibatizwa miaka miwili baadaye. Kwa kuwa alikuwa akiishi porini, alilazimika kutembea kwa muda wa saa tatu ili afike kwenye Jumba la Ufalme. Mkeye mwenye kupinga alikuwa akificha nguo na pesa zake ili amvunje moyo asihudhurie mikutano ya Kikristo. Lakini matatizo hayo yote hayakumzuia ndugu huyu mwaminifu. Alitumikia akiwa painia wa muda, au msaidizi, kila mwezi kwa miaka kumi na alihubiri katika vijiji vingi, mara nyingi akitendwa vibaya na wanavijiji. Hata hivyo, mapainia na wamisionari walipotoa ushuhuda baadaye kwenye sehemu hizo, watu wengi waliwafikia na kuomba mafunzo ya Biblia. Kwa hiyo, mambo mema yalitokezwa na kazi ya bidii ya ndugu huyo mwenye juhudi. Aliuawa na ugonjwa wa kansa akiwa mwenye miaka 92 lakini alitumia saa 40 katika huduma mwezi ule ule aliokufa.
18. (a) Tunapaswa kufanya nini ili tufurahie kibali ya kimungu? (b) Tutakuwa na thawabu gani tukiendelea ‘kuenenda kwa imani, wala si kwa kuona’?
18 Sisi, pia, tunapaswa kuendelea yajapokuwa matatizo na magumu. (Mathayo 24:13) Iwapo tutafurahia kibali ya kimungu, ni jambo la maana sana kwamba tufuate mashauri ya Mungu, tumtegemee, na tubaki tukiwa tumejitenga na ulimwengu, maoni yake, na njia zake. (Zaburi 37:5; 1 Wakorintho 2:12; Yakobo 1:27) Basi na tujitahidi kufuata aliye Mfano wetu, Yesu Kristo. Na tuwe wenye kujinyima na wenye nia ya kujikaza katika utumishi wenye utukufu wa Yehova. Tunapofanya hivyo, tunaweza kutazamia kwa uhakika utimizo wa ahadi nzuri sana za Baba yetu wa kimbingu ambazo ametolea waabudu wake washikamanifu. Na hilo litaongoza kwenye Utaratibu Mpya wake! Zaidi ya yote, ‘kuenenda kwa imani, si kwa kuona’ kutatuletea thawabu ya kushiriki katika kutetea enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote.
[Picha katika ukurasa wa 29]
Wakati mashahidi wenzako wa Yehova wanaposhiriki shughuli za kitheokrasi, je, wewe na jamaa yako mara nyingi mnafunga safari ya kwenda mahali fulani pa tafrija?
[Picha katika ukurasa wa 31]
Yesu Kristo alituwekea mfano mzuri sana. Kama yeye,je, wewe ‘unaenenda kwa imani’?