Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?
    Endeleeni Kukesha!
    • Ulimwengu Huu Unaelekea Wapi?

      Matatizo makubwa na matukio yenye kushtua hutukia kila siku ulimwenguni pote! Yana maana gani?

      USALAMA: Mabomu yalipuliwa sokoni. Walimu na wanafunzi wapigwa risasi shuleni. Watoto wachanga watekwa nyara wazazi wakiwa wameangalia kwingineko. Wanawake na wanaume wazee wavamiwa na kuibiwa vitu wakati wa mchana.

      HALI YA DINI: Makanisa yaunga mkono majeshi yanayopigana. Viongozi wa kidini washtakiwa kwa kushiriki mauaji ya umati. Makasisi wafanya ngono na watoto; makanisa yaficha. Watu wanaoenda kanisani wapungua; makanisa yauzwa.

      MAZINGIRA: Misitu yakatwa kwa ajili ya miradi ya kibiashara. Maskini waharibu misitu wakitafuta kuni. Visima vyachafuliwa, maji yaharibiwa. Takataka za viwandani na baadhi ya njia za kisasa za uvuvi zawaangamiza samaki. Uchafuzi mbaya sana wa hewa.

      MAPATO: Inasemekana kwamba katika nchi zilizo kusini ya jangwa la Sahara, mshahara wa wastani wa mtu mmoja ni dola 480 hivi za Marekani kwa mwaka. Makampuni yafilisika na maelfu wapoteza kazi kwa sababu ya wakurugenzi wenye pupa. Wanabiashara wadanganywa na kupoteza pesa zao zote.

      UPUNGUFU WA CHAKULA: Watu wapatao 800,000,000 ulimwenguni pote hulala njaa kwa ukawaida.

      VITA: Katika karne ya 20, vita vilisababisha vifo vya watu zaidi ya 100,000,000. Silaha za nyuklia zilizopo zinatosha kuwaangamiza kabisa wanadamu wote. Vita vya wenyewe kwa wenyewe. Ugaidi waenea ulimwenguni pote.

      TAUNI NA MAGONJWA MENGINE: Kuanzia mwaka wa 1918, homa ya Kihispania iliwaua watu 21,000,000. Sasa UKIMWI ndio “ugonjwa hatari zaidi wa kuambukiza kuwahi kutokea.” Kansa na ugonjwa wa moyo unawaua watu ulimwenguni pote.

      Angalia matukio hayo yote kwa ujumla. Je, ni matukio yasiyohusiana? Au ni matukio yenye maana sana yanayotukia wakati uleule ulimwenguni pote?

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

      Je, Kweli Mungu Anajali?

      Wanapofadhaishwa na matukio yenye kushtua au msiba, watu wengi hushangaa ni kwa nini Mungu hakomeshi mambo hayo.

  • Matukio Hayo Yote Yanamaanisha Nini?
    Endeleeni Kukesha!
    • Matukio Hayo Yote Yanamaanisha Nini?

      YESU KRISTO alisema: “Umalizio wa mfumo wa mambo” ungekuwa na vita, upungufu wa chakula, tauni, na matetemeko ya nchi.—Mathayo 24:1-8; Luka 21:10, 11.

      Tangu mwaka wa 1914 maisha ya watu yameharibiwa na mashambulizi ya kigaidi ambayo yameenea kotekote na vita kati ya mataifa na kati ya makabila mbalimbali. Vita hivyo vimesababishwa na viongozi wa kidini wanaoingilia siasa.

      Ijapokuwa kuna maendeleo ya kisayansi katika uzalishaji wa chakula, bado mamia ya mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanakumbwa na upungufu mkubwa wa chakula. Kila mwaka, mamilioni ya watu hufa njaa.

      Tauni, yaani kuenea kwa magonjwa ya kuambukiza ni sehemu ya ishara aliyotoa Yesu. Baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, homa ya Kihispania iliwaua watu zaidi ya 21,000,000. Tofauti na tauni za kale zilizotukia mahali pamoja tu, homa hiyo iliathiri mataifa yote ulimwenguni kutia ndani visiwa vya mbali. Sasa UKIMWI unawaathiri watu wengi duniani pote, na tauni kama vile kifua kikuu, malaria, upofu wa mtoni, na ugonjwa wa malale zinaendelea kuwaathiri watu katika nchi zinazositawi.

      Inasemekana kwamba makumi ya maelfu ya matetemeko ya nchi yenye vipimo mbalimbali hutokea kila mwaka. Ingawa kuna vifaa na mbinu bora za kutoa habari kuhusu matetemeko ya nchi, misiba inayosababishwa na matetemeko ya nchi katika maeneo yenye watu wengi huripotiwa kwa ukawaida.

      Biblia ilitabiri hivi pia: “Ujue jambo hili, ya kwamba katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake; nawe geukia mbali kutoka kwa hao.”—2 Timotheo 3:1-5.

      Je, wewe hukubali kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo”?

      Je, umeona kwamba kwa kadiri kubwa watu hujipenda wenyewe, hupenda pesa, na wana kiburi?

      Ni nani anayeweza kubisha kwamba watu wengi ulimwenguni hujifikiria tu, hawana shukrani, hawataki kufanya makubaliano, na si washikamanifu?

      Je, unajua kwamba idadi ya watoto wasiotii wazazi inazidi kuongezeka na kuna ukosefu mkubwa sana wa upendo ulimwenguni pote?

      Bila shaka unatambua kwamba tunaishi katika ulimwengu ambao unapenda raha kupindukia lakini haupendi wema. Hivyo ndivyo Biblia inavyoeleza mitazamo ya watu katika “siku za mwisho.”

      Je, tunahitaji uthibitisho zaidi ili kutambua nyakati tunamoishi? Yesu pia alitabiri kwamba katika nyakati hizi, habari njema ya Ufalme wa Mungu ingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Je, inahubiriwa?

      Gazeti Mnara wa Mlinzi linalozungumzia Biblia na linalotangaza habari njema ya Ufalme wa Yehova huchapishwa kwa ukawaida katika lugha nyingi kuliko gazeti lingine lolote.

      Kila mwaka, Mashahidi wa Yehova hutumia mabilioni ya saa wakiwahubiria wengine kuhusu Ufalme wa Mungu.

      Hivi sasa, vichapo vya Mashahidi wa Yehova vinavyozungumzia Biblia huchapishwa katika lugha 400 hivi, kutia ndani lugha zinazozungumzwa na watu wachache katika maeneo ya mbali. Mashahidi wa Yehova wamehubiri habari njema katika mataifa yote; wamehubiri pia katika visiwa vingi na maeneo madogo sana ambayo yanapuuzwa na wanasiasa. Katika nchi nyingi, wanaendesha programu ya kawaida ya elimu ya Biblia.

      Kwa kweli, habari njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa, si ili kuugeuza ulimwengu, bali kutoa ushahidi. Watu kila mahali wanapewa nafasi ya kuonyesha ikiwa watamjali yule aliyeumba mbingu na dunia na ikiwa wataheshimu sheria zake na kuwapenda wanadamu wenzao.—Luka 10:25-27; Ufunuo 4:11.

      Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu utawaharibu waovu wote na kuifanya dunia kuwa paradiso.—Luka 23:43.

      [Sanduku katika ukurasa wa 6]

      Ni Siku za Mwisho za Nini?

      Si siku za mwisho za wanadamu. Biblia inaahidi kwamba wale wanaofanya mapenzi ya Mungu wataishi milele.—Yohana 3:16, 36; 1 Yohana 2:17.

      Si siku za mwisho za dunia. Neno la Mungu linaahidi kwamba dunia inayokaliwa itadumu milele.—Zaburi 37:29; 104:5; Isaya 45:18.

      Badala yake, hizi ni siku za mwisho za mfumo huu wa mambo wenye jeuri, usio na upendo na za wale wanaoshikilia njia zake.—Methali 2:21, 22.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      Je, Kweli Biblia Ni Neno la Mungu?

      Manabii wa Biblia waliandika hivi tena na tena: ‘Yehova amesema hivi.’ (Isaya 43:14; Yeremia 2:2) Hata Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alikazia kwamba ‘hakusema kwa kujitungia mwenyewe.’ (Yohana 14:10) Biblia yenyewe inasema hivi waziwazi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.”—2 Timotheo 3:16.

      Shirika la Muungano wa Vyama vya Biblia lilisema kwamba hakuna kitabu kingine kimechapishwa katika lugha nyingi kama Biblia—lugha zaidi ya 2,200. Hakuna kitabu kingine kimesambazwa kwa kadiri kubwa hivyo—kwa sasa zaidi ya nakala bilioni nne zimesambazwa. Je, hutarajii ujumbe wa Mungu kwa wanadamu wote uenee hivyo?

      Ili kupata uthibitisho zaidi kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu, soma kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      Utafaidika sana ukisoma Biblia na kutambua kwamba kwa kweli ni Neno la Mungu.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

      Ufalme wa Mungu Ni Nini?

      Ni serikali ya pekee iliyoanzishwa na Mungu wa kweli, Yehova, Muumba wa mbingu na dunia.—Yeremia 10:10, 12.

      Biblia inasema kwamba Yesu Kristo ndiye aliyepewa na Mungu mamlaka ya kutawala. (Ufunuo 11:15) Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwamba alikuwa amepewa mamlaka kubwa na Mungu. Alitumia mamlaka yake kudhibiti nguvu za asili, kuponya magonjwa, na hata kuwafufua wafu. (Mathayo 9:2-8; Marko 4:37-41; Yohana 11:11-44) Unabii wa Biblia ulioongozwa na roho takatifu ulitabiri kwamba Mungu angempa pia “utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.” (Danieli 7:13, 14) Serikali hiyo inaitwa Ufalme wa mbinguni kwa sababu Yesu Kristo anatawala sasa akiwa mbinguni.

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Habari njema inahubiriwa duniani pote

  • Maisha Yako Yanaelekea Wapi?
    Endeleeni Kukesha!
    • Maisha Yako Yanaelekea Wapi?

      • Watu wengi hujishughulisha mno na maisha ya kila siku hivi kwamba hawafikirii wanakoelekea.

      • Biblia inatujulisha matukio mazuri yaliyo mbele. Pia inatuonya kuhusu mabadiliko makubwa yatakayokumba mashirika ya wanadamu ulimwenguni pote. Ili tupate faida na kuepuka msiba, tunahitaji kuchukua hatua inayofaa haraka.

      • Watu fulani wanajua yale ambayo Biblia inasema na wanajaribu kuyafuata lakini wanaacha mahangaiko ya maisha yawakengeushe.

      • Je, wewe unaridhika na mwelekeo wa maisha yako? Unapopanga mambo, je, wewe hufikiria jinsi mambo hayo yanavyoweza kuathiri miradi yako ya wakati ujao?

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      Ni Nini Kilicho Muhimu Sana Kwako?

      Mambo yafuatayo ni muhimu kwako kadiri gani? Yaorodheshe ukianza na lililo muhimu zaidi.

      Mengi ya mambo haya ni muhimu maishani, lakini inapokuwa lazima uchague, utaweka jambo gani kwanza? pili? na kadhalika.

      ․․․ Vitumbuizo/tafrija

      ․․․ Kazi yangu

      ․․․ Afya yangu

      ․․․ Furaha yangu

      ․․․ Mwenzi wangu wa ndoa

      ․․․ Wazazi wangu

      ․․․ Watoto wangu

      ․․․ Nyumba nzuri, nguo nzuri

      ․․․ Kufanikiwa kabisa katika lolote nifanyalo

      ․․․ Kumwabudu Mungu

      [Sanduku katika ukurasa wa 10, 11]

      Je, Maamuzi Yako Yanakuelekeza Unakotaka Kwenda?

      FIKIRIA MASWALI HAYA

      VITUMBUIZO/TAFRIJA: Je, tafrija ninayochagua huniburudisha? Je, ninashiriki michezo inayosisimua ambayo inaweza kuhatarisha uhai wangu au hata kunilemaza kabisa? Je, ni “raha” inayosisimua kwa saa chache tu lakini inayoweza kuleta madhara ya kudumu? Hata kama vitumbuizo ninavyochagua vinafaa, je, vinachukua wakati mwingi hivi kwamba sipati wakati wa kufanya mambo yaliyo muhimu zaidi?

      KAZI YANGU: Je, inanisaidia kupata mahitaji ya lazima, au nimekuwa mtumwa wake? Je, inahitaji nguvu na wakati mwingi hivi kwamba inahatarisha afya yangu? Je, mimi huchagua kufanya kazi saa za ziada badala ya kuwa pamoja na mwenzi wangu au watoto wangu? Mwajiri wangu akitaka nifanye kazi ambayo inasumbua dhamiri yangu au ambayo mara nyingi huchukua wakati wa shughuli za kiroho, je, nitaifanya ili nisifutwe?

      AFYA YANGU: Je, mimi hupuuza afya yangu au huitunza kwa uangalifu sikuzote? Je, mimi huongea juu ya afya yangu kila wakati? Je, ninaitunza afya yangu kwa njia inayoonyesha kwamba ninaijali familia yangu?

      FURAHA YANGU: Je, furaha yangu ndilo jambo la kwanza maishani? Je, ninatanguliza furaha yangu badala ya furaha ya mwenzi wangu au ya familia yangu? Je, ninatafuta furaha kwa njia inayoonyesha kwamba mimi ni mwabudu wa Mungu wa kweli?

      MWENZI WANGU WA NDOA: Je, mimi humwona mwenzi wangu kuwa rafiki yangu wakati tu kufanya hivyo kunanifurahisha? Je, mimi humheshimu mwenzi wangu na kuona kuwa anastahili heshima? Je, imani yangu katika Mungu inaongoza jinsi ninavyomwona mwenzi wangu?

      WAZAZI WANGU: Ikiwa mimi ni mtoto, je, ninawatii wazazi wangu—ninawajibu kwa heshima, ninafanya kazi za nyumbani wanazonipa, ninarudi nyumbani saa walizoweka, ninaepuka mashirika na mambo wanayokataza? Ikiwa mimi ni mtu mzima, je, mimi huwasikiliza wazazi wangu kwa heshima na kuwapa msaada unaofaa wanapouhitaji? Je, ninashughulika nao nitakavyo au ninaongozwa na shauri la Neno la Mungu?

      WATOTO WANGU: Je, ninahisi kwamba nina daraka la kuwafundisha watoto wangu maadili yanayofaa au ninawaachia walimu daraka hilo? Je, mimi hutumia wakati pamoja na watoto wangu au huwaacha watumie wakati mwingi wakicheza na vitu vya kuchezea, wakitazama televisheni au kutumia kompyuta? Je, mimi huwatia nidhamu watoto wangu kila mara wanapopuuza vikumbusho vya Mungu, au mimi huwatia nidhamu wanaponikasirisha tu?

      NYUMBA NZURI, NGUO NZURI: Ni nini kinachoamua jinsi ninavyovaa na kujipamba na vitu ninavyonunua? Je, ni kutaka kuwavutia jirani zangu? Je, ni mahitaji ya familia yangu? Je, ni kwa sababu mimi ni mwabudu wa Mungu?

      KUFANIKIWA KABISA KATIKA LOLOTE NIFANYALO: Je, ninaona ni muhimu kufanya mambo vyema kabisa? Je, ninajitahidi kufanya mambo kwa njia bora kuliko mtu mwingine yeyote? Je, ninafadhaika mtu mwingine akifanya jambo kwa njia bora kuliko mimi?

      IBADA YA MUNGU: Je, kupata kibali cha Mungu ni muhimu kwangu kuliko kupata kibali cha mwenzi wangu, watoto wangu, wazazi wangu, au mwajiri wangu? Je, ningeacha maisha ya raha yachukue mahali pa utumishi wangu kwa Mungu?

      FIKIRIA KWA MAKINI SHAURI LA BIBLIA

      Ibada ya Mungu ni muhimu kwako kadiri gani?

      Mhubiri 12:13: “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”

      JIULIZE: Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba ninafuata andiko hilo? Je, ninatii amri za Mungu kwa kutekeleza madaraka yangu nyumbani, kazini, au shuleni? Au je, mambo mengine au mikazo ya maisha huamua ikiwa nitapata wakati wa kumtumikia Mungu?

      Una uhusiano gani na Mungu?

      Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”

      Mathayo 4:10: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”

      JIULIZE: Je, ninahisi hivyo kumhusu Mungu? Je, shughuli zangu za kila siku na jinsi ninavyokabiliana na matatizo kunaonyesha kwamba nimejitoa kwa Mungu na ninamtumaini?

      Kusoma na kujifunza Biblia ni muhimu kwako kadiri gani?

      Yohana 17:3: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”

      JIULIZE: Je, ninaonyesha kwamba ninaamini maneno hayo kwa kusoma Neno la Mungu na kulitafakari kwa bidii?

      Kuhudhuria mikutano ya Kikristo ya kutaniko ni muhimu kwako kadiri gani?

      Waebrania 10:24, 25: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, . . . na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.”

      Zaburi 122:1: “Nilishangilia walipokuwa wakiniambia: ‘Na twende katika nyumba ya Yehova.’”

      JIULIZE: Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba ninathamini mwongozo huo unaopatikana katika Neno la Mungu? Je, nilikosa kuhudhuria mkutano wowote wa Kikristo mwezi uliopita kwa sababu ya kutanguliza mambo mengine?

      Je, unawahubiria wengine kwa bidii kumhusu Mungu na kusudi lake?

      Mathayo 24:14: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi . . . , na ndipo ule mwisho utakapokuja.”

      Mathayo 28:19, 20: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”

      Zaburi 96:2: “Mwimbieni Yehova, libarikini jina lake. Tangazeni habari njema za wokovu wake siku baada ya siku.”

      JIULIZE: Je, utendaji huu ni muhimu maishani mwangu? Je, jitihada zangu katika utendaji huu zinaonyesha kwamba ninasadiki kuwa tunaishi nyakati za hatari?

  • “Saa Ya Hukumu” Imefika
    Endeleeni Kukesha!
    • “Saa Ya Hukumu” Imefika

      UFUNUO, kitabu cha mwisho cha Biblia kinatuarifu kwamba malaika anayeruka katikati ya mbingu ana “habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha.” Anasema hivi kwa sauti kubwa: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.” (Ufunuo 14:6, 7) ‘Saa hiyo ya hukumu’ inatia ndani kutangazwa na kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu. “Saa” ni kipindi kifupi cha wakati. Kutekelezwa kwa hukumu ndio upeo wa “siku za mwisho” tunamoishi leo.—2 Timotheo 3:1.

      “Saa ya hukumu” ni habari njema kwa wale wanaopenda uadilifu. Ni wakati ambapo Mungu atawaletea kitulizo watumishi wake ambao wameteseka mikononi mwa ulimwengu huu wenye jeuri na usio na upendo.

      Sasa, kabla “saa ya hukumu” kufikia upeo kwenye uharibifu wa ulimwengu huu mwovu, tunahimizwa hivi: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu.” Je, unafanya hivyo? Kufanya hivyo kunahusisha mengi zaidi ya kusema tu “ninamwamini Mungu.” (Mathayo 7:21-23; Yakobo 2:19, 20) Woga unaofaa wa Mungu unapaswa kutufanya tumheshimu. Unapaswa kutufanya tuepuke mabaya. (Methali 8:13) Unapaswa kutusaidia tupende mema na kuchukia mabaya. (Amosi 5:14, 15) Ikiwa tunamheshimu Mungu, tutamsikiliza kwa makini. Hatutaruhusu shughuli nyingine zitufanye tupuuze kusoma Neno lake, Biblia, kwa ukawaida. Tutamtegemea kwa moyo wetu wote nyakati zote. (Zaburi 62:8; Methali 3:5, 6) Wale wanaomheshimu kikweli humtambua kuwa Muumba wa mbingu na dunia, Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, nao hujitiisha kwake kwa upendo akiwa Mtawala wao. Tukitambua kwamba tunahitaji kuzingatia zaidi mambo haya, tunapaswa kufanya hivyo bila kukawia.

      Kipindi cha kutekeleza hukumu iliyotajwa na malaika huitwa pia “siku ya Yehova.” “Siku” kama hiyo ilikuja juu ya Yerusalemu la kale mwaka wa 607 K.W.K. kwa sababu wakazi wake hawakutii maonyo ambayo Yehova alitoa kupitia manabii wake. Walihatarisha uhai wao hata zaidi kwa kufikiria kwamba siku ya Yehova ilikuwa mbali. Yehova alikuwa amewaonya hivi: “Iko karibu, nayo inaharakisha sana.” (Sefania 1:14) ‘Siku nyingine ya Yehova’ ilikuja juu ya Babiloni la kale mwaka wa 539 K.W.K. (Isaya 13:1, 6) Wababiloni walitegemea ngome zao na miungu yao na hivyo wakapuuza maonyo yaliyotolewa na manabii wa Yehova. Lakini katika usiku mmoja, jiji kuu la Babiloni lilitekwa na Wamedi na Waajemi.

      Tunakabili nini leo? Tunakabili ‘siku nyingine ya Yehova’ iliyo kubwa zaidi. (2 Petro 3:11-14) Hukumu ya Mungu imetangazwa juu ya “Babiloni Mkubwa.” Kulingana na Ufunuo 14:8, malaika anatangaza hivi: “Babiloni Mkubwa ameanguka.” Tayari ameanguka. Hawezi tena kuwazuia waabudu wa Yehova. Ufisadi wake na kujihusisha kwake katika vita kumefunuliwa wazi. Sasa uharibifu wake wa mwisho umekaribia. Kwa sababu hiyo, Biblia inawahimiza watu wote hivi: “Tokeni kwake [Babiloni Mkubwa] . . . ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimekusanyika pamoja mpaka mbinguni, naye Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.”—Ufunuo 18:4, 5.

      Babiloni Mkubwa Ni Nini? Ni mfumo wa ulimwenguni pote wa dini zenye mazoea kama ya Babiloni la kale. (Ufunuo, sura ya 17, 18) Hebu ona baadhi ya mazoea hayo:

      • Makuhani wa Babiloni la kale walijihusisha sana na siasa za taifa hilo. Ndivyo ilivyo na dini nyingi leo.

      • Mara nyingi, makuhani wa Babiloni waliwatia watu moyo kwenda vitani. Mara nyingi dini za leo huwa mstari wa mbele katika kuwabariki wanajeshi wakati mataifa yanapoenda vitani.

      • Mafundisho na mazoea ya Babiloni la kale yaliongoza taifa hilo katika ukosefu mbaya sana wa maadili. Viongozi wa dini leo wanapopuuza viwango vya maadili vya Biblia, ukosefu wa maadili huenea sana kati ya viongozi wa dini na pia waumini. Yafaa kuzingatia kwamba Ufunuo humtaja Babiloni Mkubwa kuwa kahaba kwa sababu anafanya uasherati na ulimwengu na mifumo yake ya kisiasa.

      • Biblia pia inasema kwamba Babiloni Mkubwa anaishi “katika anasa isiyo na aibu.” Katika Babiloni la kale, wasimamizi wa hekalu walimiliki mashamba makubwa na makuhani wakawa wanabiashara mashuhuri. Leo, mbali na kumiliki makanisa mengi, Babiloni Mkubwa ana mali na biashara chungu nzima. Mafundisho yake na sikukuu zake humletea yeye pamoja na wengine katika ulimwengu wa biashara utajiri mkubwa.

      • Matumizi ya sanamu, mizungu, na ulozi yalikuwa ya kawaida katika Babiloni la kale, na ndivyo ilivyo katika sehemu nyingi leo. Kifo kilionwa kuwa njia ya kuingia katika maisha mengine. Jiji la Babiloni lilijaa mahekalu na majengo yaliyotumiwa kuabudu miungu yake, lakini Wababiloni waliwapinga waabudu wa Yehova. Babiloni Mkubwa hufuata mafundisho na mazoea hayohayo.

      Katika nyakati za kale, Yehova aliyatumia mataifa yenye nguvu kisiasa na kijeshi kuwaadhibu wale walioendelea kumpuuza yeye na mapenzi yake. Basi Samaria liliharibiwa na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K. Yerusalemu liliharibiwa kabisa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. na pia na Waroma mwaka wa 70 W.K. Nalo Babiloni lilitekwa na Wamedi na Waajemi mwaka wa 539 K.W.K. Biblia inatabiri kwamba katika nyakati zetu serikali za kisiasa, kama mnyama-mwitu, zitamshambulia “yule kahaba” na kumwacha uchi na hivyo kumfunua alivyo kikweli. Zitamwangamiza kabisa.—Ufunuo 17:16.

      Je, kweli serikali za ulimwengu zitafanya hivyo? Biblia inasema kwamba ‘Mungu atalitia hilo ndani ya mioyo yao.’ (Ufunuo 17:17) Shambulizi hilo litafanywa ghafula, litashangaza na kushtua na litatukia bila kutarajiwa.

      Unapaswa kuchukua hatua gani? Jiulize: ‘Je, bado mimi ni mfuasi wa dini ambayo imechafuliwa na mafundisho na mazoea yanayoifanya kuwa sehemu ya Babiloni Mkubwa?’ Hata kama wewe si mfuasi wa dini kama hiyo, huenda ukajiuliza: ‘Je, nimeruhusu roho yake iniathiri?’ Roho gani? Roho ya kukubali maadili mapotovu, kupenda mali na raha badala ya kumpenda Mungu, au kupuuza kimakusudi Neno la Yehova (hata katika mambo yanayoonekana kuwa madogo). Fikiria kwa uzito jibu lako.

      Ili tupate kibali cha Yehova ni muhimu tuonyeshe kwa matendo na kutoka moyoni kwamba kwa kweli sisi si sehemu ya Babiloni Mkubwa. Huu si wakati wa kukawia-kawia. Ikituonya kwamba mwisho utakuja ghafula, Biblia inasema: ‘Babiloni lile jiji kubwa litatupwa chini kwa mtupo wa kasi sana, naye hatapatikana tena.’—Ufunuo 18:21.

      Lakini kuna matukio mengine. Katika “saa ya hukumu,” Yehova atahukumu pia mfumo wa kisiasa wa ulimwengu, watawala wake, na wote wanaopuuza utawala wake kupitia Ufalme wake wa kimbingu ulio mikononi mwa Yesu Kristo. (Ufunuo 13:1, 2; 19:19-21) Maono ya kinabii yaliyoandikwa katika Danieli 2:20-45 yanaonyesha serikali za kisiasa tangu wakati wa Babiloni la kale hadi leo zikiwa kama sanamu kubwa iliyotengenezwa kwa dhahabu, fedha, shaba, chuma, na udongo. Unabii huo ulitabiri hivi kuhusu nyakati zetu: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe.” Na kuhusu yale yatakayotimizwa na Ufalme huo wakati wa “saa ya hukumu” ya Yehova, Biblia inatangaza hivi: “Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za kibinadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.

      Biblia inawaonya waabudu wa kweli wasipende “vitu vilivyo katika ulimwengu,” yaani, mtindo wa maisha unaoendelezwa na ulimwengu huu ambao umejitenga na Mungu wa kweli. (1 Yohana 2:15-17) Je, maamuzi na matendo yako yanaonyesha kwamba unaunga mkono kabisa Ufalme wa Mungu? Je, kweli wewe huutanguliza maishani mwako?—Mathayo 6:33; Yohana 17:16, 17.

      [Sanduku katika ukurasa wa 14]

      Mwisho Utakuja Lini?

      “Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.”—Mathayo 24:44.

      “Endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”—Mathayo 25:13.

      ‘Haitachelewa.’—Habakuki 2:3.

      [Sanduku katika ukurasa wa 14]

      Je, Maisha Yako Yatabadilika Ukijua Mwisho Utakuja Lini?

      Ukijua kwa uhakika kwamba siku ya kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu itakawia kwa miaka kadhaa, je, utabadili jinsi unavyoishi? Je, umepunguza bidii yako katika utumishi wa Yehova kwa sababu mwisho wa mfumo huu wa kale unaonekana umekawia?—Waebrania 10:36-38.

      Kutojua mwisho utakuja lini hutupa nafasi ya kuonyesha kwamba tunamtumikia Mungu kwa nia nzuri. Wale wanaomjua Yehova wanatambua kwamba hatapendezwa na bidii inayoonyeshwa dakika ya mwisho kwa kuwa yeye huona kilicho moyoni.—Yeremia 17:10; Waebrania 4:13.

      Wale ambao wanampenda Yehova kikweli hutanguliza mapenzi yake sikuzote. Wakristo wa kweli hufanya kazi ya kimwili kama watu wengine. Hata hivyo, kusudi lao si kutajirika, bali ni kupata mahitaji ya lazima na kuwa na kitu cha kuwagawia wengine. (Waefeso 4:28; 1 Timotheo 6:7-12) Wao pia hufurahia tafrija zenye kujenga na starehe, lakini kusudi lao si kufanya kama kila mtu anavyofanya bali ni kuburudika. (Marko 6:31; Waroma 12:2) Kama Yesu Kristo, wao hufurahia kufanya mapenzi ya Mungu.—Zaburi 37:4; 40:8.

      Wakristo wa kweli wanataka kuishi na kumtumikia Yehova milele. Tumaini hilo halipotezi maana hata kama wanalazimika kungoja baraka kwa muda mrefu kuliko wengine walivyotarajia.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

      Suala la Enzi Kuu

      Ili tuelewe ni kwa nini Mungu ameruhusu wanadamu wateseke sana, lazima tuelewe suala la enzi kuu. Enzi kuu ni nini? Ni mamlaka iliyo kuu zaidi.

      Yehova ndiye Muumba, kwa hiyo ana haki ya kuitawala dunia na wote wanaoishi humo. Hata hivyo, Biblia inaeleza kwamba mwanzoni mwa historia ya wanadamu, enzi kuu ya Yehova ilipingwa. Shetani Ibilisi alidai kwamba Yehova alikuwa amewawekea wazazi wetu wa kwanza vizuizi vingi, na alikuwa amewadanganya kuhusu matokeo ya kujitegemea na kupuuza sheria ya Mungu. Alidai kwamba ingekuwa afadhali kama wangejitawala pasipo msaada wa Mungu.—Mwanzo, sura ya 2 na 3.

      Ikiwa Mungu angewaharibu waasi hao mara moja, angethibitisha kwamba ana nguvu, lakini hangekuwa ametatua masuala yaliyozushwa. Badala ya kuwaharibu waasi hao papo hapo, Yehova amewaacha malaika na wanadamu waone matokeo ya uasi. Ingawa jambo hilo limesababisha mateso mengi, limetokeza nafasi ya sisi kuzaliwa.

      Isitoshe, Yehova alijidhabihu sana na kwa upendo akafanya mipango ili wanadamu wanaomtii na kuwa na imani katika dhabihu ya fidia ya Mwanaye wawekwe huru kutokana na dhambi na matokeo yake, kisha waishi katika Paradiso. Ikiwa lazima, jambo hilo litatimizwa kupitia ufufuo wa wafu.

      Kwa kuruhusu wakati upite ili suala hilo litatuliwe, Mungu amewapa watumishi wake nafasi ya kuonyesha kwamba wanaweza kuitikia upendo wake na kuthibitisha utimilifu wao kwa Yehova chini ya hali zozote zile. Kutatuliwa kwa suala la enzi kuu ya Mungu, pamoja na suala la utimilifu wa wanadamu ni muhimu ili watu waheshimu ifaavyo sheria katika ulimwengu wote. Hakuwezi kuwa na amani ya kweli watu wasipoheshimu sheria.a

      [Maelezo ya Chini]

      a Masuala hayo na mambo yote yanayohusiana nayo yameelezwa kwa urefu katika kitabu Mkaribie Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Picha]

      Mfumo wa serikali za kisiasa ulimwenguni pote utaharibiwa

  • Ulimwengu Mpya Ulioahidiwa Na Mungu
    Endeleeni Kukesha!
    • Ulimwengu Mpya Ulioahidiwa Na Mungu

      BIBLIA, Neno la Mungu lililoandikwa, hutupa tumaini linaposema hivi: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

      “Mbingu mpya” ni nini? Biblia inahusianisha mbingu na utawala. (Matendo 7:49) “Mbingu mpya” ni serikali mpya ambayo itatawala dunia. Ni mpya kwa sababu itachukua mahali pa mfumo wa utawala uliopo sasa; ni hatua mpya katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Huo ndio Ufalme ambao Yesu alitufundisha kusali juu yake. (Mathayo 6:10) Kwa kuwa Mungu ndiye Mwanzilishi wake na anaishi mbinguni, Ufalme huo unaitwa “ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 7:21.

      “Dunia mpya” ni nini? Si sayari mpya, kwa kuwa Biblia inasema waziwazi kwamba dunia itakaliwa milele. “Dunia mpya” ni jamii mpya ya wanadamu. Itakuwa mpya kwa sababu waovu watakuwa wamekatiliwa mbali. (Methali 2:21, 22) Wote watakaoishi wakati huo watamheshimu na kumtii Muumba na wataishi kupatana na matakwa yake. (Zaburi 22:27) Watu wa mataifa yote wanaalikwa wajifunze na kuishi kupatana na matakwa hayo sasa. Je, wewe unafanya hivyo?

      Katika ulimwengu mpya wa Mungu, kila mtu ataheshimu utawala Wake. Je, upendo wako kwa Mungu unakuchochea kumtii? (1 Yohana 5:3) Je, unaonyesha hivyo nyumbani? kazini au shuleni? na katika maisha yako?

      Katika ulimwengu mpya, wanadamu wote watamwabudu Mungu wa kweli kwa umoja. Je, unamwabudu Muumba wa mbingu na dunia? Je, kweli ibada yako inakuunganisha na waabudu wenzako kutoka mataifa, kabila, na lugha zote?—Zaburi 86:9, 10; Isaya 2:2-4; Sefania 3:9.

      [Sanduku katika ukurasa wa 17]

      Mungu Anayeahidi Mambo Hayo

      Yeye ndiye Muumba wa mbingu halisi na Dunia. Yesu Kristo alimtaja kuwa “Mungu wa pekee wa kweli.”—Yohana 17:3.

      Wanadamu wengi huiheshimu miungu waliyojitengenezea. Mamilioni huinamia sanamu zisizo na uhai. Wengine hutukuza mashirika ya kibinadamu, falsafa, au tamaa zao wenyewe. Hata baadhi ya watu wanaodai wanatumia Biblia hawaliheshimu jina la yule ambaye Biblia inamtaja kuwa “Mungu wa kweli.”—Kumbukumbu la Torati 4:35.

      Muumba anasema hivi kujihusu: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” (Isaya 42:5, 8) Jina hilo linapatikana zaidi ya mara 7,000 kwenye Biblia katika lugha za awali. Yesu Kristo aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”—Mathayo 6:9.

      Mungu wa kweli ana sifa gani? Anasema yeye ni “mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli” na hakosi kamwe kuwaadhibu wale wanaovunja sheria zake kimakusudi. (Kutoka 34:6, 7) Jinsi ambavyo ameshughulika na wanadamu kwa miaka mingi kumethibitisha ukweli wa maneno hayo.

      Jina na mwenye jina hilo anapaswa kutakaswa, au kuonwa kuwa mtakatifu. Anastahili utii na ibada yetu yote kwa kuwa yeye ndiye Muumba na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Je, wewe unamtii na kumwabudu?

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

      Ni Mabadiliko Gani Yatakayoletwa na “Mbingu Mpya na Dunia Mpya”?

      Dunia itageuzwa kuwa Paradiso Luka 23:43

      Jamii ya ulimwenguni pote ya Yohana 13:35;

      watu wa mataifa yote, kabila zote Ufunuo 7:9, 10

      na lugha zote wanaunganishwa na upendo

      Amani ya ulimwenguni pote, Zaburi 37:10, 11;

      usalama wa kweli kwa wote Mika 4:3, 4

      Kazi yenye kuridhisha, chakula tele Isaya 25:6; 65:17, 21-23

      Magonjwa, huzuni, na kifo Isaya 25:8;

      vitaondolewa Ufunuo 21:1, 4

      Ulimwengu uliounganishwa katika Ufunuo 15:3, 4

      ibada ya Mungu wa kweli

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

      Je, Utafaidika?

      Mungu hawezi kusema uwongo!—Tito 1:2.

      Yehova anatangaza hivi: “Neno langu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:11.

      Tayari Yehova anaumba “mbingu mpya na dunia mpya.” Serikali ya kimbingu tayari inatawala. Msingi wa “dunia mpya” tayari umewekwa.

      Baada ya kueleza baadhi ya mambo yenye kupendeza ambayo “mbingu mpya na dunia mpya” zitawaletea wanadamu, kitabu cha Ufunuo kinamnukuu Mungu mwenyewe, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, akisema hivi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Pia anasema: “Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.”—Ufunuo 21:1, 5.

      Swali muhimu ni, Je, tunafanya marekebisho yanayofaa ili tustahili kuwa sehemu ya “dunia mpya” chini ya utawala wa “mbingu mpya”?

  • Kutii Kuliokoa Uhai Wao
    Endeleeni Kukesha!
    • Kutii Kuliokoa Uhai Wao

      YESU KRISTO alionya kimbele kuhusu mwisho wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi ambao kitovu chake kilikuwa hekalu la Yerusalemu. Hakutaja tarehe ambayo mwisho huo ungekuja. Lakini alieleza matukio ambayo yangetangulia uharibifu huo. Aliwahimiza wanafunzi wake wakeshe na kuondoka katika eneo la hatari.

      Yesu alitabiri hivi: “Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia.” Pia alisema: “Mtakapoona lile chukizo linalosababisha ukiwa . . . likiwa limesimama katika mahali patakatifu, . . . ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani.” Yesu aliwasihi wanafunzi wake wasirudi kuchukua mali zao. Walipaswa kukimbia haraka ili kuokoa uhai wao.—Luka 21:20, 21; Mathayo 24:15, 16.

      Ili kukomesha uasi uliokuwa ukiendelea kwa muda mrefu, Cestius Gallus, aliyaongoza majeshi ya Roma kushambulia Yerusalemu mwaka wa 66 W.K. Hata aliingia jijini na kulizingira hekalu. Ghasia zilizuka jijini. Wale waliokuwa wakikesha wangeweza kuona kwamba msiba ulikuwa karibu. Lakini, je, wangeweza kukimbia? Bila kutarajia, Cestius Gallus aliyaondoa majeshi yake. Wayahudi waasi waliwatimua mbio. Huo ulikuwa wakati wa kukimbia kutoka Yerusalemu na Yudea yote!

      Mwaka uliofuata, majeshi ya Roma yalirudi yakiongozwa na Vespasian na mwanaye Titus. Nchi nzima ilikumbwa na vita. Mwanzoni mwa mwaka wa 70 W.K., Waroma walijenga ngome ya miti iliyochongoka kuzunguka Yerusalemu. Hakukuwa na njia ya kutorokea. (Luka 19:43, 44) Vikundi mbalimbali vilichinjana jijini humo. Watu waliobaki waliuawa na Waroma au kuchukuliwa mateka. Jiji hilo pamoja na hekalu lake liliharibiwa kabisa. Kulingana na Josephus, mwanahistoria Myahudi wa karne ya kwanza, zaidi ya Wayahudi milioni moja waliteseka na kufa. Hekalu hilo halijawahi kujengwa tena.

      Kama Wakristo wangekuwa bado Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., wangeuawa au kuchukuliwa mateka kama watu wengine. Hata hivyo wanahistoria wa kale wanaripoti kwamba Wakristo walitii onyo la Mungu, wakakimbia kutoka Yerusalemu na Yudea yote hadi milima iliyo mashariki mwa Mto Yordani. Baadhi yao walikaa Pela, katika jimbo la Perea. Walikuwa wameondoka Yudea na hawakuwa wamerudi. Kutii onyo la Yesu kuliokoa uhai wao.

      Je, Wewe Hutii Maonyo Kutoka Vyanzo Vyenye Kutegemeka?

      Watu wengi hupuuza maonyo yote kwa sababu wamesikia maonyo mengi sana yasiyo ya kweli. Hata hivyo, kutii maonyo kwaweza kuokoa uhai wako.

      Katika mwaka wa 1975, maonyo kuhusu tetemeko la nchi yalitolewa nchini China. Wenye mamlaka walichukua hatua. Watu walitii na maelfu waliokoka.

      Mnamo Aprili 1991, wanakijiji walioishi kwenye miteremko ya Mlima Pinatubo, nchini Ufilipino, waliripoti kwamba mvuke na majivu yalikuwa yakifoka kutoka mlimani. Baada ya kuchunguza hali hiyo kwa miezi miwili, Taasisi ya Ufilipino ya Elimu ya Volkeno na Matetemeko ya Nchi ilionya kwamba eneo hilo lilikuwa hatarini. Makumi ya maelfu ya watu walihamishwa mara moja. Mapema mnamo Juni 15, kulitokea mlipuko mkubwa uliovurumisha majivu angani umbali wa kilometa nane na kuyasambaza katika eneo lote. Maelfu ya watu waliokoka kwa sababu walitii onyo.

      Biblia inaonya kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo. Tunaishi katika siku za mwisho. Je, unakesha mwisho unapokaribia? Je, unachukua hatua ya kuondoka kwenye eneo la hatari? Je, unawaonya wengine wafanye hivyo huku ukizingatia hatari inayotukabili?

      [Picha katika ukurasa wa 20]

      Kutii maonyo kuliokoa watu wengi wakati Mlima Pinatubo ulipofoka majivu ya volkeno

      [Picha katika ukurasa wa 21]

      Wakristo waliotii onyo la Yesu waliokoka uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.

  • “Hawakujali”
    Endeleeni Kukesha!
    • “Hawakujali”

      KUPUUZA maonyo kunaweza kusababisha msiba.

      Mnamo mwaka wa 1974, wakazi wa Darwin, nchini Australia, walikuwa wakijitayarisha kusherehekea sikukuu, waliposikia milio ya ving’ora ikiwaonya kuhusu kimbunga kilichokuwa kikikaribia. Lakini miaka 30 hivi ilikuwa imepita tangu jiji la Darwin liharibiwe na kimbunga. Mbona liharibiwe wakati huu? Wakazi wengi walipuuza hatari hiyo hadi upepo mkali ulipoanza kung’oa paa na kubomoa kuta za nyumba ambamo watu walisongamana. Kufikia asubuhi jiji hilo lilikuwa magofu.

      Mnamo Novemba 1985, mlima mmoja wa volkeno ulilipuka huko Kolombia. Theluji na barafu ziliyeyuka na kuporomosha matope yaliyozika zaidi ya wakazi 20,000 wa mji wa Armero. Je, kulikuwa na maonyo yoyote ya mapema? Mlima huo ulitetemeka kwa miezi mingi. Hata hivyo, wakazi wengi wa Armero hawakujali kwa sababu hilo lilikuwa jambo la kawaida. Wenye mamlaka walionywa kwamba kungekuwa na msiba karibuni, lakini hawakujishughulisha kuwaonya watu. Matangazo ya redio yalitolewa ili kujaribu kuwatuliza watu. Kipaza-sauti cha kanisa kilitumiwa kuwasihi watu watulie. Kulikuwa na milipuko miwili mikubwa sana wakati wa jioni. Je, wewe ungeacha mali yako na kukimbia? Ni watu wachache tu waliofanya hivyo, lakini kwa wengi ilikuwa kuchelewa mno.

      Mara nyingi wataalamu wa miamba hutabiri kwa usahihi sana mahali ambapo matetemeko ya nchi yatatokea. Lakini ni mara chache sana wanapotabiri kwa usahihi yatatokea lini. Katika mwaka wa 1999, matetemeko ya nchi yaliwaua watu wapatao 20,000 ulimwenguni pote. Wengi wa waliokufa hawakudhani jambo hilo lingeweza kuwapata.

      Wewe Huitikiaje Maonyo Yanayotolewa na Mungu Mwenyewe?

      Biblia ilieleza waziwazi mapema mambo ambayo yangetukia siku za mwisho. Inapofafanua mambo hayo, Biblia inatuhimiza tufikirie “siku za Noa.” “Katika siku hizo kabla ya gharika,” watu walikuwa wakijishughulisha sana na mambo ya kawaida ya maisha hata ingawa walifadhaishwa na jeuri iliyokuwa imeenea. Mungu aliwaonya kupitia mtumishi wake Noa, lakini “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.” (Mathayo 24:37-39) Je, wewe ungetii onyo hilo? Je, unafanya hivyo sasa?

      Vipi kama ungeishi Sodoma, karibu na Bahari ya Chumvi, katika siku za Loti, mpwa wa Abrahamu? Sehemu za mashambani zilikuwa kama paradiso. Jiji hilo lilikuwa lenye ufanisi. Watu waliishi raha mustarehe. Katika siku za Loti, “walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, walikuwa wakinunua, walikuwa wakiuza, walikuwa wakipanda, walikuwa wakijenga.” Watu hao pia walikuwa na maadili mapotovu sana. Je, ungetii onyo la Loti aliposhutumu mazoea hayo maovu? Je, ungemsikiliza ikiwa angekwambia kwamba Mungu ameazimia kuliharibu jiji la Sodoma? Au ungedhani ni mzaha, kama walivyodhani wana-wakwe za Loti? Je, labda ungeanza kukimbia kisha kutazama nyuma kama alivyofanya mke wa Loti? Ingawa wengine hawakuchukua onyo hilo kwa uzito, siku ambayo Loti alitoka Sodoma, “kulinyesha moto na kiberiti kutoka mbinguni na kuwaangamiza wote.”—Luka 17:28, 29.

      Katika nyakati zetu, watu wengi hawajali. Lakini mifano hiyo imeandikwa katika Neno la Mungu ili kutuonya sisi na kututia moyo TUENDELEE KUKESHA!

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

      Je, Kweli Kulikuwa na Gharika ya Ulimwenguni Pote?

      Wachambuzi wengi wanasema Hapana. Lakini Biblia inasema Ndiyo.

      Yesu Kristo mwenyewe alizungumzia gharika hiyo, naye alikuwa hai mbinguni na aliiona ilipotukia.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

      Je, Kweli Majiji ya Sodoma na Gomora Yaliharibiwa?

      Vitu vya kale vilivyochimbuliwa vinathibitisha tukio hilo.

      Vitabu vya historia vinataja tukio hilo.

      Yesu Kristo alithibitisha tukio hilo, na limetajwa na vitabu 14 vya Biblia.

  • “Ili Msiingie Katika Jaribu”
    Endeleeni Kukesha!
    • “Ili Msiingie Katika Jaribu”

      “Endeleeni kukesha na kusali sikuzote, ili msiingie katika jaribu.”—MATHAYO 26:41.

      YESU KRISTO alipata mkazo mkali sana kupita mikazo yote aliyowahi kupata. Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alikuwa amekaribia mwisho wa maisha yake duniani. Yesu alijua kwamba muda si muda angekamatwa, kuhukumiwa kifo, na kutundikwa kwenye mti wa mateso. Alijua kwamba matendo na maamuzi yake yote yangeliletea jina la Baba yake suto au sifa. Yesu alijua pia kwamba tumaini la wakati ujao la wanadamu lilimtegemea. Alifanya nini chini ya mkazo huo wote?

      2 Yesu alienda kwenye bustani ya Gethsemane pamoja na wanafunzi wake. Yesu alipenda sana kwenda huko. Walipofika huko aliwaacha wanafunzi wake, akaenda mbali kidogo. Akiwa peke yake, alisali kwa Baba yake wa mbinguni kwa bidii mara tatu, akimweleza hisia zake za ndani na kumwomba amtie nguvu. Ingawa alikuwa mkamilifu, Yesu hakuhisi kwamba angeweza kukabili mkazo huo kwa nguvu zake mwenyewe.—Mathayo 26:36-44.

      3 Sisi pia tuko chini ya mkazo leo. Mwanzoni mwa broshua hii, tulichunguza uthibitisho unaoonyesha tunaishi siku za mwisho za mfumo huu mwovu. Majaribu na mikazo ya ulimwengu wa Shetani inazidi kuongezeka. Maamuzi na matendo ya kila mmoja wetu anayedai kumtumikia Mungu wa kweli huliletea jina lake sifa au suto, na yanaweza kuathiri sana tumaini letu la kuishi katika ulimwengu wake mpya. Tunampenda Yehova. Tunataka ‘kuvumilia mpaka mwisho’—iwe ni mwisho wa maisha yetu au mwisho wa mfumo huu. (Mathayo 24:13) Lakini tunawezaje kutambua umuhimu wa nyakati tunamoishi na kuendelea kukesha?

      4 Akijua kwamba wanafunzi wake wa karne ya kwanza na wa leo wangepatwa na mkazo, Yesu aliwahimiza hivi: “Endeleeni kukesha na kusali sikuzote, ili msiingie katika jaribu.” (Mathayo 26:41) Maneno hayo yanamaanisha nini kwetu leo? Unakabili majaribu gani? Na unawezaje ‘kuendelea kukesha’?

      Ni Majaribu Gani Tunayokabili?

      5 Kila siku, sote hukabili jaribu la kuingia katika “mtego wa Ibilisi.” (2 Timotheo 2:26) Biblia inatuonya kwamba waabudu wa Yehova ni shabaha kuu ya Shetani. (1 Petro 5:8; Ufunuo 12:12, 17) Ana kusudi gani? Kusudi lake hasa si kutuua. Shetani hafaidiki kwa vyovyote tukifa tukiwa waaminifu kwa Mungu. Shetani anajua kwamba Yehova, kwa wakati Wake, atabatilisha kifo kupitia ufufuo.—Luka 20:37, 38.

      6 Shetani anataka kuharibu kitu chenye thamani hata zaidi kuliko uhai wetu wa sasa, yaani, utimilifu wetu kwa Mungu. Shetani anataka sana kuthibitisha kwamba anaweza kutufanya tuache kumwabudu Yehova. Kwa hiyo, tukishawishiwa kuasi kwa kuacha kuhubiri habari njema au kuacha kanuni za Kikristo, huo utakuwa ushindi kwa Shetani! (Waefeso 6:11-13) Ndiyo sababu yule “Mjaribu” hutuletea majaribu.—Mathayo 4:3.

      7 Shetani hutumia “hila” mbalimbali. (Waefeso 6:11) Anaweza kutujaribu akitumia mali, woga, shaka, au kupenda raha. Lakini njia moja yenye matokeo sana anayotumia ni kuvunjika moyo. Shetani ni mjanja sana na anajua kwamba tukivunjika moyo tunaweza kudhoofika kiroho na kunaswa na jaribu kwa urahisi. (Methali 24:10) Kwa hiyo, yeye hujaribu kutuvunja moyo hasa ‘tunapopondeka’ kihisia.—Zaburi 38:8.

      8 Inaonekana kwamba kadiri siku za mwisho zinavyozidi kusonga ndivyo mambo yanayovunja moyo yanavyoongezeka, na hatuwezi kuyaepuka. (Ona sanduku “Baadhi ya Mambo Yanayovunja Moyo.”) Kuvunjika moyo kunaweza kutufanya tuwe dhaifu hata kisababishi kiwe nini. Ikiwa umechoka kimwili, kiakili na kihisia, itakuwa vigumu “kununua wakati unaofaa” ili kutimiza wajibu wa kiroho kama vile kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kuhubiri. (Waefeso 5:15, 16) Kumbuka kwamba Mjaribu anataka uache kumtumikia Mungu. Lakini huu si wakati wa kupunguza bidii yako au kupuuza umuhimu wa nyakati tunamoishi! (Luka 21:34-36) Unawezaje kupinga majaribu na kuendelea kukesha? Fikiria madokezo haya manne ambayo yanaweza kukusaidia.

      ‘Sali Sikuzote’

      9 Mtegemee Yehova kupitia sala. Mkumbuke Yesu alipokuwa katika bustani ya Gethsemane. Alifanya nini alipokuwa na mkazo mkali wa kihisia? Alimwomba Yehova msaada, akisali kwa bidii sana hivi kwamba “jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka chini.” (Luka 22:44) Hebu fikiria. Yesu alimjua Shetani vizuri sana. Akiwa mbinguni, Yesu aliona majaribu yote ambayo Shetani hutumia kuwanasa watumishi wa Mungu. Hata hivyo,Yesu hakuhisi kwamba anaweza kushinda kwa urahisi jaribu lolote kutoka kwa Shetani. Ikiwa Mwana mkamilifu wa Mungu aliona kwamba anahitaji kusali ili Mungu amsaidie na kumtia nguvu, vipi sisi?—1 Petro 2:21.

      10 Kumbuka pia kwamba baada ya Yesu kuwahimiza wanafunzi wake ‘wasali sikuzote,’ alisema hivi: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” (Mathayo 26:41) Yesu alimaanisha mwili wa nani? Si mwili wake; mwili wake wa kibinadamu ulikuwa mkamilifu na haukuwa na udhaifu wowote. (1 Petro 2:22) Lakini wanafunzi wake walikuwa tofauti. Kwa sababu ya kurithi kutokamilika na mwelekeo wa dhambi, wangehitaji sana msaada ili kupinga majaribu. (Waroma 7:21-24) Ndiyo sababu aliwahimiza wanafunzi wake, pamoja na Wakristo wote wa kweli, wasali ili wapate msaada wa kushinda majaribu. (Mathayo 6:13) Yehova hujibu sala hizo. (Zaburi 65:2) Jinsi gani? Angalau katika njia mbili.

      11 Kwanza, Mungu hutusaidia kutambua majaribu. Majaribu ya Shetani ni kama mitego iliyotapakaa katika njia yenye giza. Usipoiona, unaweza kunaswa. Kupitia Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia, Yehova humulika mitego ya Shetani na hivyo kutusaidia tusishindwe na majaribu. Kwa miaka mingi, vichapo na programu za makusanyiko zimetuonya tena na tena kuhusu hatari za mwenendo mchafu kingono, utafutaji wa mali, kuwaogopa wanadamu, na majaribu mengine ya Shetani. (Methali 29:25; 1 Wakorintho 10:8-11; 1 Timotheo 6:9, 10) Je, humshukuru Yehova kwa kutuonya kuhusu mbinu za Shetani? (2 Wakorintho 2:11) Maonyo hayo yote ni jibu kwa sala zako za kuomba msaada wa kushinda majaribu.

      12 Pili, Yehova hujibu sala zetu kwa kutupatia nguvu za kuvumilia majaribu. Neno lake linasema: “Mungu . . . hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea.” (1 Wakorintho 10:13) Tukiendelea kumtegemea Mungu, hataruhusu kamwe tulemewe na jaribu hata tukose nguvu za kiroho za kulipinga. ‘Anatufanyiaje njia ya kutokea’? Yeye ‘huwapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ (Luka 11:13) Roho hiyo inaweza kutusaidia kukumbuka kanuni za Biblia ambazo zinaweza kuimarisha azimio letu la kufanya mema na kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima. (Yohana 14:26; Yakobo 1:5, 6) Inaweza kutusaidia kuwa na sifa tunazohitaji ili kushinda mwelekeo usiofaa. (Wagalatia 5:22, 23) Roho ya Mungu hata inaweza kuwachochea waamini wenzetu ‘wawe msaada wenye kututia nguvu.’ (Wakolosai 4:11) Je, hushukuru kwamba Yehova hujibu kwa njia hizo zenye upendo sala zako za kuomba msaada?

      Uwe na Matarajio Yanayofaa

      13 Tunahitaji kuwa na matarajio yanayofaa ili kuendelea kukesha. Nyakati nyingine sote huchoka kwa sababu ya mikazo ya maisha. Lakini ni lazima tukumbuke kwamba Mungu hakuahidi kamwe kwamba hatutapatwa na matatizo katika mfumo huu wa kale. Hata watumishi wa Mungu katika nyakati za Biblia walikabili magumu kama vile mateso, umaskini, kushuka moyo, na magonjwa.—Matendo 8:1; 2 Wakorintho 8:1, 2; 1 Wathesalonike 5:14; 1 Timotheo 5:23.

      14 Sisi pia tunakumbwa na matatizo leo. Huenda tukapatwa na mateso, mahangaiko ya kiuchumi, tukapambana na mshuko wa moyo, tukawa wagonjwa, na kuteseka katika njia nyingine. Ikiwa Yehova angetulinda kimuujiza tusipatwe na madhara yoyote, basi Shetani angepata sababu ya kumdhihaki Yehova, sivyo? (Methali 27:11) Yehova huwaruhusu watumishi wake wajaribiwe na hata nyakati nyingine wauawe mikononi mwa wapinzani wao.—Yohana 16:2.

      15 Basi, Yehova ameahidi nini? Kama tulivyoona mapema, ameahidi kwamba atatuwezesha kupinga jaribu lolote ambalo huenda tukakabili, maadamu tunamtegemea kwa moyo wetu wote. (Methali 3:5, 6) Kupitia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake, anatulinda kiroho na kutusaidia kudumisha uhusiano wetu pamoja naye. Hata tukifa, tunakuwa washindi maadamu uhusiano huo ni imara. Hakuna kitu chochote, hata kifo, kinachoweza kumzuia Mungu kuwathawabisha watumishi wake waaminifu. (Waebrania 11:6) Na katika ulimwengu mpya ulio karibu, Yehova atatimiza ahadi zake zote nzuri na kuwabariki wale wanaompenda.—Zaburi 145:16.

      Kumbuka Yale Masuala

      16 Ili kuvumilia mpaka mwisho, ni lazima tukumbuke masuala muhimu yanayomfanya Mungu aruhusu uovu. Ikiwa nyakati nyingine matatizo yetu yanatulemea sana hivi kwamba tunashawishiwa kuacha kumtumikia Yehova, tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani alipinga haki ya Yehova ya kuwa mwenye enzi kuu. Mdanganyifu huyo pia ametilia shaka ujitoaji-kimungu na utimilifu wa waabudu wa Mungu. (Ayubu 1:8-11; 2:3, 4) Masuala hayo na jinsi ambavyo Yehova ameamua kuyatatua ni muhimu kuliko uhai wa kila mmoja wetu. Jinsi gani?

      17 Muda ambao Mungu ameruhusu magumu yaendelee umewapa wengine nafasi ya kukubali kweli. Hebu fikiria: Yesu aliteseka ili tupate uzima. (Yohana 3:16) Je, hatushukuru kwa jambo hilo? Lakini je, tuko tayari kuvumilia magumu kwa muda ili watu zaidi wapate uzima? Ili tuvumilie mpaka mwisho, ni lazima tutambue kwamba hekima ya Yehova ni kubwa zaidi kuliko hekima yetu. (Isaya 55:9) Atakomesha uovu wakati ufaao wa kutatua masuala hayo kabisa ufikapo, nasi tutafaidika milele. Kwa kweli, hiyo ndiyo njia bora kabisa ya kutatua masuala hayo. Mungu hana ukosefu wa haki!—Waroma 9:14-24.

      ‘Mkaribie Mungu’

      18 Ili tuendelee kutambua umuhimu wa nyakati zetu, tunahitaji kumkaribia Yehova. Tusisahau kamwe kwamba Shetani anafanya yote awezayo ili kuharibu uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova. Shetani anataka tuamini kwamba mwisho hautakuja kamwe na kwamba hakuna haja ya kuhubiri habari njema au kuishi kupatana na viwango vya Biblia. Lakini yeye “ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Ni lazima tuazimie ‘kumpinga Ibilisi.’ Hatupaswi kamwe kuuona uhusiano wetu na Yehova kuwa kitu kisicho na thamani. Biblia inatusihi hivi kwa upendo: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:7, 8) Unawezaje kumkaribia Yehova zaidi?

      19 Ni muhimu kusali na kutafakari. Mikazo ya maisha inapokulemea, mwambie Yehova yaliyo moyoni mwako. Ukimweleza mambo waziwazi, itakuwa rahisi kuona akijibu maombi yako. Huenda asijibu sala zako kama ulivyotarajia, lakini ikiwa unataka kumheshimu na kudumisha utimilifu wako, atakusaidia ufanikiwe kuvumilia. (1 Yohana 5:14) Utamkaribia zaidi unapoona jinsi anavyokuongoza maishani. Pia ni muhimu kusoma na kutafakari sifa na njia za Yehova zilizofunuliwa katika Biblia. Kutafakari huko kunakusaidia kumjua vizuri zaidi; kunachochea moyo wako na kuzidisha upendo wako kwake. (Zaburi 19:14) Zaidi ya jambo lingine lolote, upendo huo utakusaidia kupinga majaribu na kuendelea kukesha.—1 Yohana 5:3.

      20 Pia, ili tuendelee kumkaribia Yehova, ni muhimu tuwe karibu na waamini wenzetu. Jambo hilo litazungumziwa katika sehemu ya mwisho ya broshua hii.

      MASWALI YA FUNZO

      • Yesu alifanya nini alipokabili mkazo mkali alipokuwa akikaribia mwisho wa maisha yake hapa duniani, naye aliwahimiza wanafunzi wake wafanye nini? (Fu. 1-4)

      • Kwa nini waabudu wa Yehova ni shabaha ya Shetani, naye hutujaribu katika njia gani? (Fu. 5-8)

      • Ili tupinge majaribu, kwa nini ni lazima tusali sikuzote (Fu. 9-12), tuwe na matarajio yanayofaa (Fu. 13-15), tukumbuke yale masuala (Fu. 16-17), na ‘tumkaribie Mungu’ (Fu. 18-20)?

      [Sanduku katika ukurasa wa 25]

      Baadhi ya Mambo Yanayovunja Moyo

      Afya au uzee. Tunaweza kushuka moyo ikiwa ugonjwa usiopona au uzee unatuzuia kufanya mengi katika utumishi wa Mungu.—Waebrania 6:10.

      Kukata tamaa. Tunaweza kuvunjika moyo tukiona kwamba wengi hawaitikii tunapojitahidi kuwahubiria Neno la Mungu.—Methali 13:12.

      Kujihisi hufai. Huenda mtu aliyetendewa vibaya kwa miaka mingi akaamini kwamba hapendwi na yeyote, hata na Yehova.—1 Yohana 3:19, 20.

      Kuumizwa kihisia. Mtu aliyekosewa sana na mwamini mwenzake anaweza kufadhaika sana kufikia hatua ya kutaka kuacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo au kushiriki huduma ya shambani.—Luka 17:1.

      Mateso. Huenda ukapingwa, kuteswa, au kudhihakiwa na watu wenye imani tofauti na yako.—2 Timotheo 3:12; 2 Petro 3:3, 4.

      [Picha katika ukurasa wa 26]

      Yesu alituhimiza ‘tusali sikuzote’ ili tupate msaada wa kupambana na majaribu

  • “Zaidi Ya Mambo Yote, Iweni Na Upendo Mkubwa”
    Endeleeni Kukesha!
    • “Zaidi Ya Mambo Yote, Iweni Na Upendo Mkubwa”

      “Mwisho wa mambo yote umekaribia. . . . Zaidi ya mambo yote, iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi.”—1 PETRO 4:7, 8.

      YESU alijua kwamba saa chache za mwisho pamoja na mitume wake zilikuwa muhimu. Alijua mambo ambayo wangekabili. Walikuwa na kazi nyingi ya kufanya, lakini wangechukiwa na kuteswa kama yeye. (Yohana 15:18-20) Alipokuwa nao usiku wa mwisho, aliwakumbusha tena na tena kwamba wanapaswa ‘kupendana.’—Yohana 13:34, 35; 15:12, 13, 17.

      2 Mtume Petro ambaye alikuwapo usiku huo alielewa umuhimu wa kikumbusho cha Yesu. Miaka mingi baadaye, muda mfupi tu kabla ya Yerusalemu kuharibiwa, Petro aliandika na kukazia umuhimu wa upendo. Aliwashauri Wakristo hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia. . . . Zaidi ya mambo yote, iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi.” (1 Petro 4:7, 8) Maneno ya Petro ni yenye maana sana kwa wale wanaoishi “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. (2 Timotheo 3:1) “Upendo mkubwa” ni nini? Kwa nini ni muhimu tuwaonyeshe wengine upendo huo? Na tunawezaje kuonyesha upendo huo?

      “Upendo Mkubwa” Ni Nini?

      3 Watu wengi hufikiri upendo ni hisia inayojitokeza yenyewe. Lakini Petro hakuwa akizungumzia upendo wa aina yoyote tu; alikuwa akizungumzia upendo wa hali ya juu sana. Neno “upendo” kwenye 1 Petro 4:8 ni tafsiri ya neno la Kigiriki a·gaʹpe. Neno hilo linamaanisha upendo usio na ubinafsi ambao unaongozwa na kanuni. Kitabu kimoja kinasema: “Mtu anaweza kuamriwa kuonyesha upendo wa agape kwa sababu upendo huo si hisia tu bali ni azimio linalomwongoza kutenda.” Kwa kuwa tumerithi mwelekeo wa kuwa na ubinafsi, tunahitaji kukumbushwa mara kwa mara tupendane kulingana na kanuni za Mungu.—Mwanzo 8:21; Waroma 5:12.

      4 Lakini hiyo haimaanishi kwamba tupendane kwa sababu tu tumeamriwa kufanya hivyo. A·gaʹpe si upendo usio na hisia. Petro alisema ni lazima tuwe na ‘upendo mkubwa [kihalisi, “unaopanuka”] sisi kwa sisi.’a (Kingdom Interlinear) Hata hivyo, upendo huo unahitaji jitihada. Msomi mmoja alisema hivi kuhusu neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mkubwa”: “Linatoa wazo la mwanariadha anayekaza misuli yake na kujikakamua kwa nguvu zake zote kumaliza mbio.”

      5 Basi hatupaswi kuonyesha upendo wetu kwa watu wachache tu au inapokuwa rahisi kufanya hivyo. Tunahitaji ‘kuupanua’ moyo wetu na kuonyesha upendo wa Kikristo hata katika hali ngumu. (2 Wakorintho 6:11-13) Ni wazi kwamba tunahitaji kusitawisha upendo huo na kujitahidi kuukuza kama vile mwanariadha anavyohitaji kufanya mazoezi na kujitahidi kuboresha stadi zake. Ni muhimu kuwa na upendo huo sisi kwa sisi. Kwa nini? Angalau kwa sababu tatu.

      Kwa Nini Tunapaswa Kupendana?

      6 Kwanza, “kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu.” (1 Yohana 4:7) Yehova, ambaye ndiye Chanzo cha sifa hii yenye kuvutia, alitupenda sisi kwanza. Mtume Yohana anasema hivi: “Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye.” (1 Yohana 4:9) Mwana wa Mungu ‘alitumwa’ awe mwanadamu, atimize huduma yake, na kufa kwenye mti wa mateso—yote hayo yalifanywa ili “tupate uzima.” Tunapaswa kuitikiaje upendo huo mkubwa sana tulioonyeshwa na Mungu? Yohana anasema: “Ikiwa Mungu alitupenda hivi, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu wa kupendana.” (1 Yohana 4:11) Ona kwamba Yohana anaandika, “Ikiwa Mungu alitupenda hivi”—si alikupenda wewe tu, bali alitupenda sisi. Basi funzo ni wazi: Ikiwa Mungu anawapenda waabudu wenzetu, sisi pia tunapaswa kuwapenda.

      7 Pili, ni muhimu sana tupendane zaidi wakati huu ili tuweze kuwasaidia ndugu zetu wenye uhitaji kwa sababu “mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Petro 4:7) Tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Hali za ulimwengu, misiba ya asili, na upinzani hutuletea magumu. Tunahitaji kuwa na uhusiano wa karibu hata zaidi na wenzetu hali zinapokuwa ngumu. Upendo mkubwa utatuunganisha kabisa na kutuchochea ‘tutunzane.’—1 Wakorintho 12:25, 26.

      8 Tatu, tunahitaji kupendana kwa sababu hatutaki ‘kumpa Ibilisi nafasi’ ya kututumia vibaya. (Waefeso 4:27) Shetani yuko macho kutumia kutokamilika kwa waamini wenzetu, iwe ni udhaifu wao, kasoro zao, na makosa yao ili kutukwaza. Je, tutaacha kutaniko kwa sababu mwamini mwenzetu alisema bila kufikiri au alitutendea vibaya? (Methali 12:18) Hatutafanya hivyo ikiwa tuna upendo mkubwa sisi kwa sisi! Upendo huo hutusaidia kudumisha amani na kumtumikia Mungu kwa umoja na “bega kwa bega.”—Sefania 3:9.

      Jinsi ya Kuonyesha Kwamba Unawapenda Wengine

      9 Ni lazima upendo uanze nyumbani. Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kweli wangetambuliwa kwa upendo kati yao wenyewe. (Yohana 13:34, 35) Ni lazima upendo uonyeshwe kutanikoni na pia katika familia—kati ya wenzi wa ndoa na kati ya wazazi na watoto. Haitoshi tu kuwapenda washiriki wa familia; tunahitaji kuwaonyesha upendo kwa njia zinazofaa.

      10 Wenzi wa ndoa wanawezaje kuonyeshana upendo? Mume anayempenda mke wake kikweli humwonyesha kwa maneno na matendo kwamba anamthamini, hadharani na hata faraghani. Yeye humheshimu na kuzingatia mawazo, maoni, na hisia zake. (1 Petro 3:7) Anatanguliza masilahi yake na kufanya yote awezayo kumtunza kimwili, kiroho, na kihisia. (Waefeso 5:25, 28) Mke anayempenda mume wake kikweli “humheshimu sana,” hata ingawa nyakati nyingine mume wake anapungukiwa. (Waefeso 5:22, 33) Yeye humuunga mkono mume wake na kujitiisha kwake, naye si mwenye kudai mno, bali anashirikiana na mumewe kutanguliza mambo ya kiroho.—Mwanzo 2:18; Mathayo 6:33.

      11 Wazazi, mnawezaje kuwaonyesha watoto wenu upendo? Mnaonyesha kwamba mnawapenda mnapojitahidi kuwaandalia mahitaji ya kimwili. (1 Timotheo 5:8) Lakini watoto hawahitaji tu chakula, mavazi, na makao. Wanahitaji mazoezi ya kiroho ili wampende na kumtumikia Mungu wa kweli maishani. (Methali 22:6) Kwa hiyo ni lazima familia itenge wakati wa kujifunza Biblia, kuhubiri, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja. (Kumbukumbu la Torati 6:4-7) Ili kufanya mambo hayo kwa ukawaida, unahitaji kujidhabihu sana, hasa katika nyakati hizi za hatari. Unapowajali na kujitahidi kuwatunza watoto wako kiroho, unaonyesha kwamba unawapenda na unafikiria masilahi yao ya milele.—Yohana 17:3.

      12 Ni muhimu pia wazazi waonyeshe kwamba wanawapenda watoto wao kwa kushughulikia mahitaji yao ya kihisia. Watoto ni dhaifu; mioyo yao michanga inahitaji kuhakikishiwa kwamba unawapenda. Waambie kwamba unawapenda, waonyeshe kabisa unawapenda, ukifanya hivyo unawahakikishia kwamba wanapendwa na kuthaminiwa. Wapongeze kwa uchangamfu na kutoka moyoni, unapofanya hivyo, wanatambua kwamba unaona na kuthamini jitihada zao. Watie nidhamu kwa upendo, unapofanya hivyo unawaonyesha kwamba unajali sifa ambazo wanakuza. (Waefeso 6:4) Wonyesho huo wote wa upendo husaidia kujenga familia yenye furaha na umoja ambayo inaweza kupinga mikazo ya siku hizi za mwisho.

      13 Upendo hutusukuma kutokazia fikira kasoro za wengine. Kumbuka kwamba Petro alipowashauri wasomaji wake ‘wawe na upendo mkubwa wao kwa wao,’ alisema ni muhimu sana kufanya hivyo, “kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.” (1 Petro 4:8) ‘Kufunika’ dhambi hakumaanishi kuficha dhambi nzito. Wale walio na madaraka kutanikoni wanapaswa kujulishwa dhambi hizo ili wazishughulikie. (Mambo ya Walawi 5:1; Methali 29:24) Si jambo la upendo hata kidogo na ni kinyume cha Maandiko kuwaruhusu wale wanaotenda dhambi nzito waendelee kuwaumiza au kuwadhulumu watu wasio na hatia.—1 Wakorintho 5:9-13.

      14 Mara nyingi, makosa na kasoro za waamini wenzetu huwa ndogo sana. Nyakati nyingine sote hujikwaa kwa maneno au matendo na kuwavunja moyo au hata kuwaumiza wenzetu. (Yakobo 3:2) Je, tunapaswa kutangaza kasoro za wengine? Kufanya hivyo kutasababisha tu migogoro kutanikoni. (Waefeso 4:1-3) Ikiwa tunaongozwa na upendo, ‘hatutafichua kosa’ la mwabudu mwenzetu. (Zaburi 50:20) Kama vile simiti na rangi zinavyofunika mianya iliyo ukutani, ndivyo upendo unavyofunika kasoro za wengine.—Methali 17:9.

      15 Upendo utatufanya tuwasaidie wale walio na uhitaji mkubwa. Hali zinapozidi kuzorota katika siku hizi za mwisho, huenda nyakati nyingine waamini wenzetu wakahitaji msaada wa kimwili. (1 Yohana 3:17, 18) Kwa mfano, je, kuna mshiriki wa kutaniko letu ambaye amepatwa na matatizo ya kiuchumi au amepoteza kazi? Basi pengine tunaweza kumsaidia kimwili hali zetu zikiruhusu. (Methali 3:27, 28; Yakobo 2:14-17) Je, nyumba ya mjane mzee inahitaji kurekebishwa? Basi pengine tunaweza kujitolea kusaidia kuirekebisha.—Yakobo 1:27.

      16 Hatupaswi kuwapenda tu wale wanaoishi karibu nasi. Nyakati nyingine, huenda tukapata habari za watumishi wa Mungu katika nchi nyingine ambao wamekumbwa na dhoruba kali, matetemeko ya nchi, au vita. Huenda wakahitaji sana chakula, mavazi, na vitu vingine. Haidhuru wao ni wa taifa au kabila gani. ‘Tunaupenda ushirika mzima wa akina ndugu.’ (1 Petro 2:17) Kwa hiyo, kama makutaniko ya karne ya kwanza, tuko tayari kuunga mkono mipango ya kutoa misaada. (Matendo 11:27-30; Waroma 15:26) Tunapoonyesha upendo katika njia hizo zote, tunaimarisha vifungo vinavyotuunganisha katika siku hizi za mwisho.—Wakolosai 3:14.

      17 Upendo hutusukuma kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Fikiria mfano wa Yesu. Kwa nini alihubiri na kufundisha? ‘Aliwasikitikia’ umati kwa sababu ya hali yao mbaya ya kiroho. (Marko 6:34) Walipuuzwa na kudanganywa na wachungaji wa dini za uwongo, ambao walipaswa kuwafundisha kweli za kiroho na kuwapa tumaini. Kwa hiyo, akichochewa na upendo na huruma nyingi ya kutoka moyoni, Yesu aliwafariji watu kwa “habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Luka 4:16-21, 43.

      18 Leo pia, watu wengi wamepuuzwa kiroho na kudanganywa na hawana tumaini. Ikiwa, kama Yesu, sisi tunajali mahitaji ya kiroho ya wale wasiomjua Mungu wa kweli, basi upendo na huruma zitatusukuma kuwahubiria habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 6:9, 10; 24:14) Kwa sababu muda unaobaki ni mfupi, huu ndio wakati wa kuhubiri himahima ujumbe huu unaookoa uhai.—1 Timotheo 4:16.

      “Mwisho wa Mambo Yote Umekaribia”

      19 Kumbuka, Petro alipotushauri tuwe na upendo sisi kwa sisi, alianza shauri lake kwa maneno haya: “Mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Petro 4:7) Hivi karibuni ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu utachukua mahali pa ulimwengu huu mwovu. (2 Petro 3:13) Sasa si wakati wa kuwa na mtazamo wa kutojali. Yesu alituonya hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.

      20 Basi na tujitahidi kabisa ‘kuendelea kukesha,’ tukitambua umuhimu wa nyakati tunamoishi. (Mathayo 24:42) Na tuwe macho kuepuka majaribu yoyote ya Shetani ambayo yanaweza kutukengeusha. Tusiruhusu kamwe ulimwengu huu usio na upendo utuzuie kuwaonyesha wengine upendo. Zaidi ya yote, na tuzidi kumkaribia Yehova, Mungu wa kweli ambaye hivi karibuni Ufalme wake wa Kimasihi utatimiza kusudi lake tukufu kwa dunia.—Ufunuo 21:4, 5.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki