Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 15
    • UINGEREZA NA MAREKANI ZAPATA MAMLAKA

      3. Yule mnyama anayetisha mwenye pembe kumi anafananisha nini, na pembe kumi zinafananisha nini?

      3 Tunaweza kutambua kichwa cha saba cha yule mnyama-mwitu wa kitabu cha Ufunuo sura ya 13 kwa kulinganisha maono ya Yohana na maono ya Danieli kuhusu yule mnyama anayetisha mwenye pembe kumi.a (Soma Danieli 7:7, 8, 23, 24.) Mnyama huyo ambaye Danieli aliona anafananisha Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Roma. (Tazama chati kwenye ukurasa wa 12-13.) Katika karne ya tano W.K., Milki ya Roma ilianza kusambaratika. Pembe kumi zinazoota kwenye kichwa cha mnyama huyo mwenye kuogopesha zinafananisha falme zilizotokana na milki hiyo.

      4, 5. (a) Pembe ndogo ilifanya nini? (b) Kichwa cha saba cha yule mnyama-mwitu kinafananisha nini?

      4 Ni pembe nne, au falme nne tu kati ya falme zilizoota kwenye kichwa cha mnyama huyo mkali ndizo zinazozungumziwa kwa njia ya pekee. Pembe tatu zinang’olewa na pembe nyingine “ndogo.” Unabii huo ulitimia wakati Uingereza, ambayo zamani ilikuwa nchi ndogo chini ya Milki ya Roma, ilipoibuka na kuwa maarufu. Kufikia karne ya 17, Uingereza ilikuwa serikali isiyo na nguvu sana. Nchi nyingine tatu katika Milki ya kale ya Roma, yaani, Hispania, Uholanzi, na Ufaransa, zilikuwa na uvutano zaidi. Uingereza iling’oa serikali hizo moja baada ya nyingine, ikaziondoa kwenye vyeo hivyo vya kifahari. Kufikia katikati ya karne ya 18, Uingereza ilikuwa ikielekea kuwa serikali kuu ya ulimwengu. Lakini bado haikuwa kichwa cha saba cha yule mnyama-mwitu.

      5 Ingawa Uingereza ilipata mamlaka, nchi zilizokuwa chini ya ukoloni wake huko Amerika Kaskazini zilijitenga. Hata hivyo, Uingereza haikuizuia Marekani kuendelea kupata nguvu, na Marekani ililindwa na jeshi la wanamaji la Uingereza. Siku ya Bwana ilipoanza mwaka wa 1914, Uingereza ilikuwa imejenga milki kubwa zaidi katika historia na Marekani ilikuwa sasa nchi iliyositawi zaidi kiviwanda duniani.b Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Marekani ilikuwa imesitawisha uhusiano wa pekee na Uingereza. Kichwa cha saba cha yule mnyama sasa kilikuwa kimeibuka kikiwa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Kichwa hicho kiliutendeaje uzao wa mwanamke?

      6. Kichwa cha saba kimewatendeaje watu wa Mungu?

      6 Muda mfupi baada ya kuanza kwa siku ya Bwana, kichwa cha saba kiliwashambulia watu wa Mungu, ndugu za Kristo waliobaki duniani. (Mt. 25:40) Yesu alisema kwamba wakati wa kuwapo kwake, washiriki waliobaki wa ule uzao wangekuwa wakifanya kazi kwa bidii duniani. (Mt. 24:45-47; Gal. 3:26-29) Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ilipigana vita na watakatifu hao. (Ufu. 13:3, 7) Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, serikali hiyo iliwakandamiza watu wa Mungu, ikapiga marufuku baadhi ya machapisho yao, na kuwatupa gerezani wawakilishi wa jamii ya mtumwa mwaminifu. Ni kana kwamba kichwa cha saba cha mnyama-mwitu kilikomesha kazi ya kuhubiri kwa kipindi fulani. Yehova aliona mapema tukio hilo la ajabu na kumfunulia Yohana. Pia, Mungu alimwambia Yohana kwamba sehemu ya pili ya ule uzao ingepewa uhai tena na kushiriki kwa bidii zaidi katika utendaji wa kiroho. (Ufu. 11:3, 7-11) Historia ya kisasa ya watumishi wa Yehova inathibitisha kwamba mambo hayo yalitukia kama ilivyotabiriwa.

      SERIKALI KUU YA ULIMWENGU YA UINGEREZA NA MAREKANI NA MIGUU YA CHUMA NA UDONGO

      7. Kuna uhusiano gani kati ya kichwa cha saba cha mnyama-mwitu na ile sanamu kubwa sana?

      7 Kuna uhusiano gani kati ya kichwa cha saba cha mnyama-mwitu na ile sanamu kubwa sana? Uingereza, kutia ndani na Marekani, zilitokana na Milki ya Roma. Hata hivyo, namna gani miguu ya hiyo sanamu? Biblia inasema kwamba miguu hiyo ni mchanganyiko wa chuma na udongo. (Soma Danieli 2:41-43.) Maelezo hayo kuhusu miguu yanatimia kipindi kilekile ambacho kichwa cha saba, yaani, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani inapoibuka na kupata umaarufu. Kama vile ambavyo kitu kilichotengenezwa kwa mchanganyiko wa chuma na udongo kilivyo dhaifu kuliko kitu kilichotengenezwa kwa chuma tu, vivyo hivyo pia Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ni dhaifu kuliko serikali ambayo ilitokana nayo. Hilo lilitukia jinsi gani?

      8, 9. (a) Serikali kuu ya saba ya ulimwengu ilionyesha jinsi gani nguvu kama za chuma? (b) Udongo ulio katika miguu ya ile sanamu unafananisha nini?

      8 Nyakati nyingine, kichwa cha saba cha mnyama huyo kimeonyesha nguvu kama za chuma. Kwa mfano, kilithibitisha kwamba kina nguvu kiliposhinda Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, kichwa cha saba kilionyesha pia nguvu kama za chuma.c Hata baada ya vita hivyo, mara kwa mara kichwa cha saba kilionyesha nguvu kama za chuma. Hata hivyo, tangu mwanzoni, chuma hicho kimechanganyika na udongo.

      9 Kwa muda mrefu watumishi wa Yehova wamekuwa wakijitahidi kuelewa kile ambacho miguu ya sanamu hiyo inafananisha. Andiko la Danieli 2:41 linasema kwamba mchanganyiko wa chuma na udongo ni “ufalme,” mmoja, si falme nyingi. Kwa hiyo, udongo unafananisha vitu fulani katika utawala wa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, ambavyo vinaifanya iwe dhaifu zaidi kuliko Milki ya Roma iliyokuwa na nguvu kama chuma ambacho hakijachanganywa na kitu kingine chochote. Udongo unafananisha “uzao wa wanadamu,” au watu wa kawaida. (Dan. 2:43) Katika Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, watu wameinuka na kudai haki zao kupitia kampeni za kupigania haki za raia, vyama vya wafanyakazi, na harakati za kutafuta uhuru. Watu wa kawaida wanafanya iwe vigumu kwa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani kutenda kwa nguvu kama za chuma. Pia, maoni ya kisiasa yanayopingana na matokeo ya uchaguzi yanayokaribiana na ambayo hayaonyeshi wazi mshindi yamedhoofisha uwezo wa hata viongozi maarufu, hivi kwamba hawana mamlaka ya kutekeleza sera zao. Danieli alitabiri hivi: “Sehemu moja ya ufalme huo itakuwa yenye nguvu na nyingine itakuwa dhaifu.”—Dan. 2:42; 2 Tim. 3:1-3.

      10, 11. (a) Ni nini kitakachoipata “miguu” ya ile sanamu? (b) Tunaweza kukata kauli gani kuhusu idadi ya vidole vya miguu?

      10 Katika karne ya 21, serikali ya Uingereza na ya Marekani zimeendelea kuwa na uhusiano wa pekee, na mara nyingi zinashirikiana katika kushughulikia masuala ya ulimwengu. Unabii mbalimbali kuhusu ile sanamu kubwa sana na yule mnyama-mwitu unathibitisha kwamba wakati ujao hapatakuwa na serikali nyingine kuu ya ulimwengu ambayo itachukua mahali pa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Huenda serikali hiyo kuu ya mwisho ya ulimwengu ya Uingereza na Marekani ikawa dhaifu zaidi kuliko serikali inayofananishwa na ile miguu ya chuma, lakini serikali hiyo haitavunjika yenyewe.

      11 Je, idadi ya vidole vya miguu vya sanamu hiyo vina maana ya pekee? Fikiria jambo hili: Katika maono mengine, Danieli anataja idadi hususa, kwa mfano, idadi ya pembe zilizo kwenye vichwa vya wanyama mbalimbali. Idadi hizo zina maana. Hata hivyo, anapoeleza kuhusu ile sanamu, Danieli hataji idadi ya vidole vya miguu. Kwa hiyo, inaonekana kwamba idadi hiyo si muhimu sana kama vile ambavyo idadi ya mikono, vidole, miguu, na nyayo za sanamu hiyo si muhimu. Danieli anataja kihususa kwamba vidole vya miguu vingekuwa mchanganyiko wa chuma na udongo. Kutokana na maelezo yake, tunaweza kukata kauli kwamba Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ndiyo itakayokuwa ikitawala wakati ambapo “jiwe” linalofananisha Ufalme wa Mungu litakapoipiga miguu ya sanamu hiyo.—Dan. 2:45.

      SERIKALI YA UINGEREZA NA MAREKANI NA MNYAMA-MWITU MWENYE PEMBE MBILI

      12, 13. Mnyama-mwitu mwenye pembe mbili anafananisha nini, naye anafanya nini?

      12 Ingawa Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ni mchanganyiko wa chuma na udongo, maono ambayo Yesu alimpa Yohana yanaonyesha kwamba serikali hiyo ingeendelea kutimiza sehemu kubwa katika siku za mwisho. Jinsi gani? Yohana aliona maono ya mnyama-mwitu mwenye pembe mbili ambaye alisema kama joka mkubwa. Mnyama huyo wa ajabu anafananisha nini? Ana pembe mbili, kwa hiyo ni serikali pacha. Yohana anaona tena Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani lakini sasa ikitimiza daraka fulani la pekee.—Soma Ufunuo 13:11-15.

  • Yehova Anafunua Mambo Ambayo “Lazima Yatendeke Upesi”
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 15
    • 19. Tunaweza kuwa na uhakika gani, na huu ndio wakati wa kufanya nini?

      19 Tunaishi katika siku ambazo kile kichwa cha saba kinatawala. Hakuna vichwa vingine vitakavyoibuka juu ya mnyama huyo kabla hajaharibiwa. Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani ndiyo itakayokuwa ikiutawala ulimwengu wakati dini ya uwongo itakapoharibiwa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki