Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ibada Ambayo Mungu Anakubali
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
    • SURA YA KUMI NA TANO

      Ibada Ambayo Mungu Anakubali

      • Je, dini zote zinampendeza Mungu?

      • Tunaweza kuitambuaje dini ya kweli?

      • Ni nani walio waabudu wa kweli wa Mungu duniani leo?

      1. Tutapata faida gani tukimwabudu Mungu kwa njia inayofaa?

      YEHOVA MUNGU anatujali sana na anataka tufaidike na mwongozo wake wenye upendo. Tukimwabudu kwa njia inayofaa, tutakuwa wenye furaha na tutaepuka matatizo mengi maishani. Pia tutapata baraka na msaada wake. (Isaya 48:17) Hata hivyo, kuna mamia ya dini ambazo hudai kwamba zinafundisha kweli kumhusu Mungu. Lakini zinatofautiana katika mafundisho yao kumhusu Mungu na mapenzi yake.

      2. Tunawezaje kujua njia inayofaa ya kumwabudu Yehova, na ni mfano gani unaotusaidia kuelewa jambo hilo?

      2 Unawezaje kujua njia inayofaa ya kumwabudu Yehova? Si lazima ujifunze na kulinganisha mafundisho ya dini zote. Unahitaji tu kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha hasa kuhusu dini ya kweli. Kwa mfano: Katika nchi nyingi kuna tatizo la pesa bandia. Unawezaje kutofautisha pesa halali na pesa bandia? Je, unahitaji kuchunguza pesa zote bandia? Hapana. Ingekuwa afadhali kama ungechunguza na kujua pesa halali. Baada ya kujua jinsi pesa halali zinavyoonekana, unaweza kutambua pesa bandia. Vivyo hivyo, tunaweza kutambua dini za uwongo kwa kujifunza kutambua dini ya kweli.

      3. Yesu alisema tunapaswa kufanya nini ili tupate kibali cha Mungu?

      3 Ni muhimu tumwabudu Yehova katika njia anayokubali. Watu wengi huamini kwamba dini zote zinampendeza Mungu, lakini Biblia haifundishi hivyo. Hata haitoshi tu kudai kuwa Mkristo. Yesu alisema: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.” Kwa hiyo, ili tuwe na kibali cha Mungu, lazima tujifunze mapenzi ya Mungu na kuyafanya. Yesu aliwaita wale wasiofanya mapenzi ya Mungu “wenye matendo ya uasi-sheria.” (Mathayo 7:21-23) Dini ya uwongo haina thamani yoyote kama vile pesa bandia zisivyo na thamani. Isitoshe, dini hizo ni hatari.

      4. Yesu alimaanisha nini alipozungumzia zile barabara mbili, na kila moja inaelekea wapi?

      4 Yehova anampa kila mtu duniani nafasi ya kupata uzima wa milele. Hata hivyo, ili tuishi milele katika Paradiso, ni lazima tumwabudu Mungu kwa njia inayofaa na tuishi maisha yanayompendeza. Inasikitisha kwamba wengi hukataa kufanya hivyo. Ndiyo sababu Yesu alisema: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu barabara inayoongoza kwenye uharibifu ni pana na kubwa, na wengi ndio wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Dini ya kweli inaongoza kwenye uzima wa milele. Dini ya uwongo inaongoza kwenye uharibifu. Yehova hataki mwanadamu yeyote aharibiwe na ndiyo sababu anawapa watu wote nafasi ya kujifunza kumhusu. (2 Petro 3:9) Hivyo basi, uhai wetu unategemea jinsi tunavyomwabudu Mungu.

      JINSI YA KUITAMBUA DINI YA KWELI

      5. Tunawezaje kuwatambua wafuasi wa dini ya kweli?

      5 “Barabara inayoongoza kwenye uzima” inaweza kupatikanaje? Yesu alisema kwamba dini ya kweli ingetambuliwa kwa matendo ya wafuasi wake. Alisema: ‘Kwa matunda yao mtawatambua. Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri.’ (Mathayo 7:16, 17) Yaani, wale wanaofuata dini ya kweli wangetambuliwa kwa mafundisho na matendo yao. Waabudu wa kweli hujitahidi kufanya mapenzi ya Mungu wakiwa kikundi ingawa hawajakamilika na wanakosea. Hebu tuzungumzie mambo sita yanayowatambulisha wafuasi wa dini ya kweli.

      6, 7. Watumishi wa Mungu huionaje Biblia, na Yesu aliwekaje mfano mzuri kuhusiana na jambo hilo?

      6 Watumishi wa Mungu hutumia Biblia kama msingi wa mafundisho yao. Biblia yenyewe inasema hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Hivyo, mafundisho na matendo ya wafuasi wa dini ya kweli hayategemei maoni au desturi za wanadamu. Yanategemea Neno la Mungu, Biblia, lililoongozwa na roho.

      7 Yesu Kristo aliweka mfano mzuri kwa kutumia Neno la Mungu kama msingi wa mafundisho yake. Katika sala kwa Baba yake wa mbinguni alisema: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Yesu aliamini Neno la Mungu, na mambo yote aliyofundisha yalipatana na Maandiko. Mara nyingi Yesu alisema: “Imeandikwa.” (Mathayo 4:4, 7, 10) Kisha Yesu alinukuu andiko. Vivyo hivyo, watu wa Mungu leo hawafundishi maoni yao wenyewe. Wanaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu, nao hutegemeza kwa uthabiti mafundisho yao katika yale inayosema.

      8. Kumwabudu Yehova kunatia ndani nini?

      8 Wafuasi wa dini ya kweli humwabudu Yehova peke yake na kulijulisha jina lake. Yesu alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:10) Kwa hiyo, watumishi wa Mungu humwabudu Yehova peke yake. Ibada hiyo inatia ndani kuwajulisha watu jina la Mungu wa kweli na sifa zake. Zaburi 83:18 inasema: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Yesu aliweka mfano kwa kuwasaidia wengine wamjue Mungu, kama alivyosali: “Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni.” (Yohana 17:6) Vivyo hivyo, waabudu wa kweli leo huwafundisha wengine kuhusu jina la Mungu, makusudi yake, na sifa zake.

      9, 10. Wakristo wa kweli huonyeshana upendo katika njia zipi?

      9 Watu wa Mungu wanapendana kikweli bila ubinafsi. Yesu alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Wakristo wa zamani walipendana kama Yesu alivyosema. Upendo huo unaotegemea kanuni za Biblia, hauzuiwi na tofauti za kikabila, kijamii, na kitaifa nao huwavuta watu pamoja katika kifungo cha kudumu cha undugu wa kweli. (Wakolosai 3:14) Wafuasi wa dini za uwongo hawana undugu kama huo wenye upendo. Tunajuaje? Wanauana kwa sababu ya tofauti za kitaifa au kikabila. Wakristo wa kweli hawatumii silaha wala kuwaua ndugu zao Wakristo au mtu mwingine yeyote. Biblia inasema: “Watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi ni wazi kwa jambo hili: Kila mtu ambaye haendelei kufanya uadilifu hatokani na Mungu, wala yeye ambaye hampendi ndugu yake. . . . Tunapaswa kupendana; si kama Kaini, aliyetokana na yule mwovu akamuua ndugu yake.”—1 Yohana 3:10-12; 4:20, 21.

      10 Bila shaka, kuwa na upendo wa kweli hakumaanishi tu kutowaua wengine. Wakristo wa kweli hutumia wakati, nguvu, na mali zao kusaidiana na kutiana moyo bila ubinafsi. (Waebrania 10:24, 25) Wanasaidiana wakati wa taabu na hawadhulumiani. Wao huishi kulingana na kanuni ya Biblia inayosema “tuwatendee wote mema.”—Wagalatia 6:10.

      11. Kwa nini ni muhimu kukubali kwamba Mungu anamtumia Yesu Kristo kutuokoa?

      11 Wakristo wa kweli hukubali kwamba Mungu anamtumia Yesu Kristo kutuokoa. Biblia inasema: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo lazima sisi tupate kuokolewa.” (Matendo 4:12) Kama tulivyoona katika Sura ya 5, Yesu alitoa uhai wake kuwa fidia kwa wanadamu watiifu. (Mathayo 20:28) Isitoshe, Yesu ni Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu katika Ufalme wa mbinguni ambao utatawala dunia yote. Na Mungu anataka tumtii Yesu na kufuata mafundisho yake ikiwa tunataka kuishi milele. Ndiyo sababu Biblia inasema: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima.”—Yohana 3:36.

      12. Kutokuwa sehemu ya ulimwengu kunahusisha nini?

      12 Waabudu wa kweli si sehemu ya ulimwengu. Alipokuwa ameshtakiwa mbele ya Pilato, mtawala Mroma, Yesu alisema: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Katika nchi yoyote ile wanamoishi, wafuasi wa kweli wa Yesu ni raia wa Ufalme wake wa mbinguni na hivyo hawajihusishi kamwe na siasa za ulimwengu huu. Hawaungi mkono upande wowote. Hata hivyo, waabudu wa Yehova hawawazuii wengine kujiunga na chama cha kisiasa, kugombea kiti cha kisiasa au kupiga kura. Waabudu wa kweli wa Mungu wanatii sheria hata ingawa hawajihusishi na siasa. Kwa nini? Kwa sababu Neno la Mungu linawaamuru ‘wajitiishe’ kwa “mamlaka zilizo kubwa” za kiserikali. (Waroma 13:1) Matakwa ya kisiasa yanapopingana na matakwa ya Mungu, waabudu wa kweli huiga mfano wa mitume ambao walisema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29; Marko 12:17.

      13. Wafuasi wa kweli wa Yesu wana maoni gani kuhusu Ufalme wa Mungu, na hivyo wanachukua hatua gani?

      13 Wafuasi wa kweli wa Yesu wanahubiri kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu. Yesu alitabiri: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo hutangaza Ufalme wa mbinguni wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu badala ya kuwatia watu moyo wategemee utawala wa kibinadamu kusuluhisha matatizo yao. (Zaburi 146:3) Yesu alitufundisha kusali kwa ajili ya serikali hiyo kamilifu aliposema: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Neno la Mungu lilitabiri kwamba Ufalme huo wa mbinguni “utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [zilizopo leo], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.

      14. Ni dini gani inayotimiza matakwa ya ibada ya kweli?

      14 Kulingana na mambo ambayo tayari tumezungumzia, jiulize: ‘Ni dini gani inayotumia Biblia kama msingi wa mafundisho yake yote na kuwajulisha watu jina la Yehova? Ni dini gani huonyesha upendo jinsi Yehova anavyotuagiza, ina imani katika Yesu, si sehemu ya ulimwengu, na hutangaza Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu? Kati ya dini zote duniani, ni dini gani inayotimiza matakwa hayo?’ Uthibitisho unaonyesha wazi kwamba ni Mashahidi wa Yehova.—Isaya 43:10-12.

      UTAFANYA NINI?

      15. Mungu anataka tufanye nini mbali na kuamini tu kwamba yeye yuko?

      15 Huwezi kumpendeza Mungu kwa kudai tu kwamba unamwamini. Kwani, Biblia inasema kwamba hata roho waovu wanaamini kwamba Mungu yuko. (Yakobo 2:19) Hata hivyo, ni wazi kwamba hawafanyi mapenzi ya Mungu na hawana kibali chake. Ili tukubaliwe na Mungu, haitoshi tu kuamini kwamba yeye yuko, ni lazima tufanye mapenzi yake. Ni lazima pia tujitenge kabisa na dini za uwongo na kukubali ibada ya kweli.

      16. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kushirikiana na dini za uwongo?

      16 Mtume Paulo alisema kwamba hatupaswi kushiriki katika ibada ya uwongo. Aliandika: “‘Tokeni katikati yao, na mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kilicho najisi’; ‘nami nitawakaribisha ndani.’” (2 Wakorintho 6:17; Isaya 52:11) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli wanaepuka kitu chochote kinachohusiana na dini za uwongo.

      17, 18. “Babiloni Mkubwa” ni nini, na kwa nini ni muhimu ‘kutoka kwake’ haraka?

      17 Biblia inaonyesha kwamba dini zote za uwongo ni sehemu ya “Babiloni Mkubwa.”a (Ufunuo 17:5) Jina hilo linatukumbusha jiji la zamani la Babiloni, ambako dini za uwongo zilianzia baada ya Mafuriko ya siku ya Noa. Mafundisho na mazoea mengi ambayo ni ya kawaida katika dini za uwongo yalianza zamani huko Babiloni. Kwa mfano, Wababiloni waliabudu miungu mitatu-mitatu. Leo, Utatu ni fundisho kuu katika dini nyingi. Lakini Biblia inafundisha wazi kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli, Yehova, na kwamba Yesu Kristo ni Mwana wake. (Yohana 17:3) Wababiloni waliamini pia kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa na ambayo inaweza kuteseka motoni. Leo, dini nyingi hufundisha kwamba nafsi au roho haiwezi kufa na inaweza kuteseka motoni.

      18 Kwa kuwa ibada ya Babiloni ya zamani ilienea duniani pote, Babiloni Mkubwa ya leo inaweza kuitwa kwa kufaa milki ya ulimwengu ya dini za uwongo. Na Mungu ametabiri kwamba milki hiyo ya dini za uwongo itaharibiwa ghafula. (Ufunuo 18:8) Je, unaona kwa nini unapaswa kujitenga na kila sehemu ya Babiloni Mkubwa? Yehova Mungu anataka ‘utoke kwake,’ yaani, Babiloni Mkubwa, haraka kabla ya kuchelewa.—Ufunuo 18:4.

      Mtu akikaribishwa katika kundi la Mashahidi wa Yehovo kutoka mataifa mbalimbali

      Utafaidika sana ukimtumikia Yehova pamoja na watu wake

      19. Utafaidikaje ukimtumikia Yehova?

      19 Huenda baadhi ya watu wakaacha kushirikiana nawe kwa sababu ya uamuzi wako wa kuacha kushirikiana na dini ya uwongo. Hata hivyo, utafaidika sana ukimtumikia Yehova pamoja na watu wake. Kama wanafunzi wa zamani wa Yesu ambao waliacha vitu vingine ili wamfuate, utakuwa na ndugu na dada wengi wa kiroho. Utakuwa sehemu ya familia kubwa ya ulimwenguni pote yenye mamilioni ya Wakristo ambao wanakupenda kikweli. Nawe utakuwa na tumaini zuri la kuishi milele “katika mfumo wa mambo unaokuja.” (Marko 10:28-30) Huenda wale ambao walikukataa kwa sababu ya imani yako wataona yale ambayo Biblia inafundisha na kuwa waabudu wa Yehova.

      20. Washiriki wa dini ya kweli wanatazamia nini wakati ujao?

      20 Biblia inafundisha kwamba hivi karibuni Mungu ataharibu mfumo huu mbovu wa mambo na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu chini ya utawala wa Ufalme wake. (2 Petro 3:9, 13) Huo utakuwa ulimwengu mzuri ajabu! Na katika mfumo huo mpya wenye uadilifu, kutakuwa na dini moja tu, aina moja ya ibada ya kweli. Je, si jambo la hekima kuchukua hatua zinazofaa ili kujiunga na waabudu wa kweli sasa hivi?

      a Unaweza kupata habari inayoeleza kwa nini Babiloni Mkubwa inawakilisha milki ya ulimwengu ya dini za uwongo katika Nyongeza “Kumtambulisha ‘Babiloni Mkubwa.’”

  • Ibada Ambayo Mungu Anakubali
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
    • WALE WANAOMWABUDU MUNGU WA KWELI

      Watu wa jamii, umri, na hali tofauti tofauti wanafuata ibada ya kweli
      • hutumia Biblia kama msingi wa mafundisho yao

      • humwabudu Yehova peke yake na kuwajulisha watu jina lake

      • wanapendana kikweli

      • wanakubali kwamba Mungu anamtumia Yesu kuwaokoa

      • si sehemu ya ulimwengu

      • wanahubiri kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu

  • Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya Kweli
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
    • SURA YA KUMI NA SITA

      Chukua Msimamo Upande wa Ibada ya Kweli

      • Biblia inafundisha nini kuhusu kutumia mifano katika ibada?

      • Wakristo huzionaje sikukuu za kidini?

      • Unaweza kuwaelezaje wengine imani yako bila kuwaudhi?

      1, 2. Baada ya kutoka katika dini ya uwongo, unapaswa kujiuliza swali gani, na kwa nini ni muhimu?

      NAMNA gani ukipata habari kwamba eneo lenu lote limetiwa sumu? Mtu fulani amekuwa akitupa kisiri takataka zenye sumu katika eneo lenu na maisha ya watu yamo hatarini sasa. Utafanya nini? Bila shaka utahama ikiwezekana. Hata hivyo, baada ya kuhama, bado utafikiria swali hili kwa uzito, ‘Je, nimeathiriwa na sumu hiyo?’

      2 Ndivyo ilivyo kuhusiana na dini za uwongo. Biblia inafundisha kwamba ibada kama hiyo imechafuliwa na mafundisho na mazoea machafu. (2 Wakorintho 6:17) Ndiyo sababu unapaswa kutoka katika “Babiloni Mkubwa,” ambayo ni milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. (Ufunuo 18:2, 4) Je, tayari umefanya hivyo? Ikiwa ndivyo, unastahili kupongezwa. Hata hivyo, kuna mambo mengi ambayo unahitaji kufanya mbali na kujitenga au kujiuzulu kutoka katika dini ya uwongo. Baada ya kutoka, unapaswa kujiuliza, ‘Je, bado mimi ninashikilia mambo fulani niliyozoea kufanya nilipokuwa katika dini ya uwongo?’ Fikiria mifano kadhaa.

      KUABUDU SANAMU NA MABABU

      3. (a) Biblia inasema nini kuhusu kutumia sanamu, na kwa nini huenda ikawa vigumu kwa wengine kukubali maoni ya Mungu? (b) Unapaswa kufanya nini ikiwa una vitu vinavyohusiana na ibada ya uwongo?

      3 Watu fulani wamekuwa na sanamu au vihekalu katika nyumba zao kwa miaka mingi. Je, wewe ni mmoja wao? Ikiwa ndivyo, huenda ukaona kwamba ni vigumu au ni vibaya kusali kwa Mungu bila kutumia vitu vinavyoonekana. Huenda hata unavipenda sana baadhi ya vitu hivyo. Lakini Mungu ndiye anayesema jinsi anavyotaka aabudiwe, na Biblia inafundisha kwamba hataki tutumie sanamu. (Kutoka 20:4, 5; Zaburi 115:4-8; Isaya 42:8; 1 Yohana 5:21) Kwa hiyo, unaweza kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli kwa kuharibu vitu vyovyote ulivyo navyo ambavyo vinahusiana na ibada ya uwongo. Kwa vyovyote vile, vione vitu hivyo jinsi Yehova anavyoviona, yaani, ni ‘vitu vinavyochukiza.’—Kumbukumbu la Torati 27:15.

      4. (a) Tunajuaje kwamba kuabudu mababu ni kazi bure? (b) Kwa nini Yehova aliwaonya watu wake wasiwasiliane na pepo kwa njia yoyote?

      4 Katika dini nyingi za uwongo, mababu pia huabudiwa. Kabla ya kujifunza kweli ya Biblia, watu fulani waliamini kwamba wafu wanaishi katika makao yasiyoonekana ya roho na kwamba wanaweza kuwasaidia au kuwaumiza walio hai. Labda ulikuwa ukijitahidi sana kuwatuliza mababu zako waliokufa. Lakini kama ulivyojifunza katika Sura ya 6 ya kitabu hiki, wafu hawana fahamu wala hawaishi popote. Kwa hiyo, ni kazi bure kujaribu kuwasiliana nao. Ujumbe wowote ambao inasemekana unatoka kwa mpendwa aliyekufa, kwa kweli unatoka kwa roho waovu. Kwa hiyo, Yehova aliwaonya Waisraeli wasijaribu kuongea na wafu au kuwasiliana na pepo kwa njia yoyote ile.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

      Kuabudu Mababu na sanamu kumefanywa kotekote dunianai

      5. Unaweza kufanya nini ikiwa zamani ulikuwa ukitumia sanamu au kuabudu mababu?

      5 Ikiwa zamani ulikuwa ukitumia sanamu au kuabudu mababu, unaweza kufanya nini? Soma na utafakari maandiko ya Biblia yanayoonyesha maoni ya Mungu. Sali kwa Yehova kila siku kuhusu tamaa yako ya kuchukua msimamo upande wa kweli, na umwombe akusaidie uwe na maoni kama yake.—Isaya 55:9.

      KRISMASI HAIKUSHEREHEKEWA NA WAKRISTO WA ZAMANI

      6, 7. (a) Krismasi inasemekana kuwa ukumbusho wa nini, na je, wafuasi wa Kristo wa karne ya kwanza waliisherehekea? (b) Wakati wa wanafunzi wa kwanza wa Yesu, sherehe za kuzaliwa zilihusianishwa na nini?

      6 Ibada ya mtu inaweza kuchafuliwa na dini za uwongo kupitia sherehe zinazopendwa. Kwa mfano, fikiria Krismasi. Inasemekana kwamba Krismasi ni ukumbusho wa kuzaliwa kwa Yesu Kristo, na karibu dini zote zinazodai kuwa za Kikristo husherehekea Krismasi. Hata hivyo, hakuna lolote linalothibitisha kwamba wanafunzi wa Yesu walisherehekea sikukuu hiyo. Kitabu Sacred Origins of Profound Things kinasema: “Kwa miaka 200 tangu Kristo alipozaliwa, hakuna mtu aliyejua siku hususa ambayo alizaliwa, na ni watu wachache tu waliotaka kujua.”

      7 Hata kama wanafunzi wa Yesu wangejua tarehe hususa ya kuzaliwa kwake, hawangeisherehekea. Kwa nini? Kwa sababu, kama vile kitabu The World Book Encyclopedia kinavyosema, Wakristo wa zamani “waliona kusherehekea sikukuu ya kuzaliwa kwa mtu yeyote kuwa desturi ya kipagani.” Sikukuu pekee za kuzaliwa zinazotajwa katika Biblia ni zile za watawala wawili ambao hawakumwabudu Yehova. (Mwanzo 40:20; Marko 6:21) Pia, sikukuu za kuzaliwa zilisherehekewa ili kuheshimu miungu ya kipagani. Kwa mfano, mnamo Mei 24, Waroma walisherehekea kuzaliwa kwa mungu wa kike aliyeitwa Diana. Siku iliyofuata, walisherehekea kuzaliwa kwa mungu-jua aliyeitwa Apollo. Hivyo, sherehe za kuzaliwa zilihusianishwa na upagani wala si Ukristo.

      8. Kuna uhusiano gani kati ya sherehe za kuzaliwa na ushirikina?

      8 Kuna sababu nyingine ambayo ingewafanya Wakristo wasisherehekee kuzaliwa kwa Yesu. Inaelekea wanafunzi wake walijua kwamba sherehe za kuzaliwa zilihusiana na ushirikina. Kwa mfano, Wagiriki na Waroma wengi wa kale waliamini kwamba roho fulani ilikuwapo wakati wa kuzaliwa kwa kila mwanadamu na ilimlinda maisha yake yote. Kitabu The Lore of Birthdays kinasema kwamba, “roho hiyo ilikuwa na uhusiano wa kichawi pamoja na mungu ambaye siku ya kuzaliwa kwake ililingana na siku ya kuzaliwa kwa mtu huyo.” Bila shaka, Yehova hawezi kufurahishwa na sherehe yoyote ambayo inamhusianisha Yesu na ushirikina. (Isaya 65:11, 12) Basi, watu wengi walianzaje kusherehekea Krismasi?

      KRISMASI ILIANZIA WAPI?

      9. Desemba 25 ilichaguliwaje kuwa siku ya kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu?

      9 Watu walitenga Desemba 25 kuwa siku ya kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu mamia ya miaka baada ya yeye kuishi duniani. Lakini Yesu hakuzaliwa siku hiyo, inaonekana alizaliwa mwezi wa Oktoba.a Basi, kwa nini Desemba 25 ilichaguliwa? Inaelekea kwamba baadaye watu fulani waliodai kuwa Wakristo “walitaka tarehe hiyo ipatane na sherehe ya kipagani ya Waroma ya ‘kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa.’” (The New Encyclopædia Britannica) Wakati wa majira ya baridi kali, jua lilipoonekana kuwa hafifu zaidi, wapagani walifanya sherehe ili kulifanya jua lirudi na kuwaletea joto na nuru. Walidhani kwamba jua lilianza kurudi Desemba 25. Katika jitihada za kuwafanya wapagani wawe Wakristo, viongozi wa kidini waliikubali sherehe hiyo na kujaribu kuifanya ionekane kuwa ya “Kikristo.”b

      10. Kwa nini watu fulani hawakusherehekea Krismasi nyakati zilizopita?

      10 Tangu zamani imejulikana kwamba Krismasi ilitokana na wapagani. Kwa kuwa ilitokana na chanzo kisichopatana na Maandiko, Krismasi ilipigwa marufuku katika karne ya 17 nchini Uingereza na pia katika koloni kadhaa za Amerika. Yeyote ambaye hakwenda kazini siku ya Krismasi alitozwa faini. Hata hivyo, punde si punde, desturi hizo za kale zikarudi, na nyingine mpya zikaongezwa. Kwa mara nyingine tena Krismasi ikawa sikukuu kubwa, na hivyo ndivyo ilivyo leo hii katika nchi nyingi. Hata hivyo, kwa sababu Krismasi inahusianishwa na dini za uwongo, wale wanaotaka kumpendeza Mungu hawaisherehekei wala hawasherehekei sikukuu nyingine yoyote iliyotokana na ibada ya kipagani.c

      JE, VYANZO VYA SIKUKUU NI MUHIMU?

      11. Kwa nini watu fulani husherehekea sikukuu, hata hivyo, ni jambo gani lililo muhimu zaidi kwetu?

      11 Watu fulani hukubali kwamba sikukuu kama vile Krismasi zilianzishwa na wapagani, hata hivyo, wanahisi kwamba si vibaya kuzisherehekea. Kwani, watu wengi wanaposherehekea sikukuu hizo hawafikirii ibada ya uwongo. Pia, pindi hizo huwezesha familia kuwa pamoja. Je, hivyo ndivyo unavyohisi? Ikiwa ndivyo, huenda sababu inayokufanya uone ugumu kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli ni upendo wako kwa familia wala si kwa dini ya uwongo. Uwe na hakika kwamba Yehova aliyeanzisha familia anataka uwe na uhusiano mzuri na watu wako wa ukoo. (Waefeso 3:14, 15) Hata hivyo, unaweza kuimarisha vifungo hivyo kwa njia ambayo Mungu anakubali. Mtume Paulo alisema hivi kuhusu jambo lililo muhimu zaidi maishani mwetu: “Endeleeni kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.”—Waefeso 5:10.

      Peremende chafu kwenye mtaro

      Je, unaweza kula peremende ambayo imeokotwa katika mtaro?

      12. Eleza ni kwa nini tunapaswa kuepuka desturi na sherehe zenye vyanzo visivyofaa.

      12 Huenda unahisi kwamba leo watu hawaadhimishi sikukuu kwa sababu ya vyanzo vyake. Je, vyanzo vya sikukuu ni muhimu? Ndiyo! Kwa mfano: Tuseme umeona peremende kwenye mtaro. Je, utaiokota na kuila? Haiwezekani! Peremende hiyo ni chafu. Sawa na peremende hiyo, huenda sikukuu hizo zinaonekana kuwa zenye kuvutia, hata hivyo, zimeokotwa mahali pachafu. Ili kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli, tunapaswa kuwa na maoni kama ya nabii Isaya, aliyewaambia hivi waabudu wa kweli: “Msiguse kitu chochote kilicho najisi.”—Isaya 52:11.

      TUMIA UTAMBUZI UNAPOSHUGHULIKA NA WENGINE

      13. Ni magumu gani yanayoweza kutokea usiposherehekea sikukuu?

      13 Magumu yanaweza kutokea unapoamua kutosherehekea sikukuu. Kwa mfano, huenda wafanyakazi wenzako wakataka kujua ni kwa nini husherehekei sikukuu fulani zinazofanywa kazini. Vipi ukipewa zawadi ya Krismasi? Je, ni vibaya kuikubali? Vipi ikiwa mwenzi wako wa ndoa ana imani tofauti? Unaweza kuhakikishaje kwamba watoto wako hawahisi kwamba wamekosa kitu fulani kwa kutosherehekea sikukuu hizo?

      14, 15. Unaweza kufanya nini ukipewa salamu ya sikukuu au ikiwa mtu anataka kukupa zawadi?

      14 Unahitaji utambuzi ili kushughulikia kila hali inayotokea. Mtu akikupa salamu za sikukuu, unaweza tu kumshukuru kwa kukutakia heri. Lakini vipi ikiwa wewe humwona au kufanya kazi na mtu huyo kila siku. Basi, huenda ukaamua kumweleza mengi zaidi. Vyovyote vile, tumia busara. Biblia inashauri: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) Uwe mwangalifu usije ukawavunjia wengine heshima. Badala yake, waeleze msimamo wako kwa busara. Waeleze waziwazi kwamba hakuna ubaya wa kutoa au kupokea zawadi na kuwa na sherehe, hata hivyo ungependa kufanya mambo hayo wakati mwingine.

      15 Vipi ikiwa mtu anataka kukupa zawadi? Inategemea hali mbalimbali. Huenda mwenye kukupa zawadi akasema: “Najua kwamba husherehekei sikukuu. Hata hivyo, ningependa kukupa zawadi hii.” Basi, huenda ukaamua kwamba kupokea zawadi hiyo si sawa na kushiriki katika sikukuu. Bila shaka, ikiwa mwenye kukupa zawadi hajui imani yako, unaweza kumtajia kwamba wewe husherehekei sikukuu hiyo. Hilo litamsaidia kuelewa ni kwa nini ingawa unakubali kupokea zawadi yake, hutampa zawadi yoyote. Kwa upande mwingine, huenda isifae kupokea zawadi ikiwa yule anayekupa zawadi hiyo anataka kuonyesha kwamba hushikamani na imani yako au kwamba unaweza kuvunja imani yako ili kupata vitu vya kimwili.

      NAMNA GANI WASHIRIKI WA FAMILIA?

      16. Unawezaje kutumia busara unaposhughulikia mambo yanayohusiana na sikukuu?

      16 Namna gani ikiwa washiriki wa familia wana imani tofauti? Unapaswa kuwa na busara. Hakuna haja ya kubishania kila desturi au sherehe ambayo watu wako wa ukoo wanaamua kusherehekea. Badala yake, heshimu maoni yao, kama vile ungependa waheshimu maoni yako. (Mathayo 7:12) Epuka mambo yoyote ambayo yangefanya uonekane kwamba unasherehekea sikukuu. Lakini utumie busara katika mambo ambayo hayahusiani moja kwa moja na sherehe za sikukuu. Bila shaka, sikuzote unapaswa kutenda kwa njia itakayokuacha ukiwa na dhamiri njema.—1 Timotheo 1:18, 19.

      17. Unawezaje kuwasaidia watoto wako wasihisi kwamba wanakosa kitu fulani wanapowaona wengine wakisherehekea sikukuu fulani?

      17 Unaweza kufanya nini ili watoto wako wasihisi kwamba wamekosa kitu fulani kwa sababu ya kutosherehekea sikukuu isiyopatana na Maandiko? Inategemea sana mambo unayofanya nyakati nyingine. Wazazi fulani hutenga nyakati za kuwapa watoto wao zawadi. Mojawapo ya zawadi bora zaidi ambazo unaweza kuwapa watoto wako ni kuwa pamoja nao na kuwaonyesha upendo.

      UNGA MKONO IBADA YA KWELI

      Picha za familia ikihubiri habari njema, wakiabudu pamoja kwenye mikutano ya Kikristo, na kupeana zawadi kwenye tafrija

      Kuunga mkono ibada ya kweli huleta furaha ya kweli

      18. Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunawezaje kukusaidia kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli?

      18 Ili kumpendeza Mungu, lazima ukatae kushiriki ibada ya uwongo na kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli. Hilo linatia ndani nini? Biblia inasema hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Mikutano ya Kikristo ni pindi za furaha ambazo unaweza kumwabudu Mungu kwa njia anayokubali. (Zaburi 22:22; 122:1) Kwenye mikutano hiyo, kuna “ubadilishanaji wa kitia-moyo” kati ya Wakristo waaminifu.—Waroma 1:12.

      19. Kwa nini ni muhimu kuzungumza na wengine kuhusu mambo uliyojifunza katika Biblia?

      19 Njia nyingine ya kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli ni kuwaambia wengine mambo ambayo umejua baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, watu wengi ‘wanaugua na kulia’ kwa sababu ya uovu unaotendeka ulimwenguni leo. (Ezekieli 9:4) Huenda unajua watu fulani wanaohisi hivyo. Unaweza kuzungumza nao kuhusu tumaini lako la wakati ujao linalotegemea Biblia. Unaposhirikiana na Wakristo wa kweli na kuzungumza na wengine kuhusu kweli nzuri za Biblia ambazo umejifunza, utaona kwamba tamaa yoyote ya kushiriki desturi za dini ya uwongo ambayo huenda bado ikawa moyoni mwako itatoweka hatua kwa hatua. Uwe na hakika kwamba utakuwa na furaha sana na utapata baraka nyingi ukichukua msimamo upande wa ibada ya kweli.—Malaki 3:10.

      a Ona Nyongeza “Je, Yesu Alizaliwa Desemba?”.

      b Sherehe ya Saturnalia pia ilichangia kuchaguliwa kwa Desemba 25. Sherehe hiyo inayomheshimu mungu wa kilimo wa Waroma ilifanywa Desemba 17 hadi 24. Katika sherehe hiyo ya Saturnalia, watu walikula na kunywa, walijitumbuiza na kupeana zawadi.

      c Unaweza kupata habari zaidi kuhusu maoni ya Wakristo wa kweli juu ya sikukuu nyingine zinazopendwa na watu wengi, katika Nyongeza “Je, Tusherehekee Sikukuu?”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki