-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
JINSI KAZI YAO ILIVYOANZA
Kazi ya watu wa Yehova ilianza jinsi gani katika eneo hilo? Masimulizi yetu yanaanza na kijana fulani kinyozi anayeitwa Franz Brand, mwenyeji wa eneo la kaskazini la Yugoslavia linaloitwa Vojvodina. Alikuwa ameenda Austria kutafuta kazi. Akiwa huko, alijifunza kweli, kisha akarudi katika mji wao mwaka wa 1925 akiwa Shahidi. Alijiunga na kikundi kidogo ambacho kilikuwa kikisoma na kuzungumzia vitabu vya kujifunzia Biblia vinavyoitwa Studies in the Scriptures, ambavyo walikuwa wamepewa na watu wao wa ukoo walio nchini Marekani.
Kikundi hicho kilitambua kwamba kinapaswa kuhubiri, na vijitabu viwili vinavyoeleza mafundisho ya Biblia vikatafsiriwa katika Kiserbia. Inahuzunisha kwamba kabla ya vijitabu hivyo kugawanywa, kikundi hicho kilitembelewa na ndugu mwenye madaraka aliyeasi tengenezo na kuanzisha dhehebu lake. Alimshawishi kila mtu aachane na Wanafunzi wa Biblia, lakini alishindwa kumshawishi Franz.
Franz alihamia Maribor, Slovenia, ambako alipata kazi kwenye saluni ya kunyoa. Alimhubiria mwenye saluni hiyo ya kunyoa, Richard Tautz, akakubali kweli. Franz na Richard waliitwa vinyozi wanaoamini Biblia, na walitumia mahali pao pa kazi kama kituo cha kuhubiri. Watu waliokuja kunyolewa walisikiliza kwa makini sana hivi kwamba hawakutaka kusogea au kuongea walipokuwa wakinyolewa! Mmoja wao alikuwa mwanasiasa, aliyeitwa Ðuro Džamonja. Mwingine aliitwa Rudolf Kalle, na alikuwa na duka la kurekebisha taipureta. Ðuro na Rudolf walifanya maendeleo ya haraka nao wakabatizwa bila kukawia. Ðuro aliacha siasa na kusaidia kuanzisha shirika la The Lighthouse Society of Bible Students katika Ufalme wa Yugoslavia. Shirika hilo la kisheria liliwawezesha akina ndugu kuhubiri na kufanya mikutano kwa uhuru.
SINEMA YA “PHOTO-DRAMA” ILIFUNGUA NJIA
Mwaka wa 1931, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika nchi ya Uswisi ilituma ndugu wawili ili waonyeshe sinema ya “The Photo-Drama of Creation” katika miji yote mikubwa huko Yugoslavia. Majumba yalijaa watu, nao walitazama kwa makini sana Ðuro alipokuwa akionyesha sinema hiyo. Sinema ya “Photo-Drama” iliwachochea wengi kupendezwa na kweli ya Biblia katika nchi yote. Wakati huo, akina ndugu walikuwa wakifanya mikutano ya Kislovenia na Kijerumani huko Maribor. Na huko Zagreb na maeneo ya karibu, vikundi vya akina ndugu vilikusanyika ili kuzungumzia vichapo ambavyo vilikuwa vimetafsiriwa katika Kikroatia.
Kisha, ndugu wakaamua kuanza kutafsiri Mnara wa Mlinzi katika Kislovenia na Kikroatia. Ilikuwa kazi ngumu sana nyakati hizo. Baada ya gazeti kutafsiriwa, dada alipiga chapa gazeti lote akitumia karatasi ya kaboni, lakini alitokeza nakala 20 tu kwa wakati mmoja. Baadaye, walipata mashini ya kunakili, wakaanza kutokeza nakala 200 za Mnara wa Mlinzi kwa wakati mmoja.
Ndugu na dada walibeba magazeti hayo na kusafiri kwa gari-moshi sehemu mbalimbali za Yugoslavia ili kuhubiri. Nyakati nyingine, ndugu wa Slovenia walikodi lori na kumwajiri dereva ambaye hakuwa Shahidi. Aliwapeleka kwenye eneo ambalo walipanga kuhubiri, kisha aliwangoja mchana kutwa mpaka walipomaliza. Siku hizo, wahubiri hao wa Ufalme hawakuwa wamezoezwa sana, na nyakati nyingine ujumbe wao ulikuwa wa moja kwa moja; hata hivyo, Yehova alibariki bidii yao kwa kuwasaidia kupata watu “waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.”—Mdo. 13:48.
Franc Sagmeister anakumbuka hivi: “Nilisikia kuhusu kweli mwaka wa 1931 kutoka kwa shangazi yangu, Terezija Gradič, na mume wake Franc. Mume wa shangazi alikuwa kati ya wahubiri wa kwanza nchini Slovenia. Hata hivyo, Franc ambaye mwanzoni alipinga dini vikali, alianza kuisoma Biblia kwa bidii. Hilo lilinivutia sana, hivyo, nikajiunga naye katika kujifunza Maandiko. Hata ingawa nilipingwa na familia yangu, nilitaka kuwafundisha wengine mambo mapya niliyojifunza. Kasisi wa parokia alipojulishwa hilo, aliniita mara moja. Akaniambia kwamba sikuruhusiwa kuwa na Biblia kwa sababu singeweza kuielewa. Nilikataa kumpa Biblia yangu. Baadaye, baba yangu alipokufa, nilikutana na kasisi huyo barabarani, naye alikasirika sana kwa sababu sikuwa nimelipia Misa hata moja ya kumwombea baba yangu. Nikamwambia, ‘Niko tayari kulipia Misa 100, hata 1,000 ikiwa zitamsaidia baba.’
“‘Zinasaidia, zinasaidia!’ akasema kasisi.
“‘Ikiwa yuko mbinguni,’ nikasema, ‘hahitaji Misa yako, na ikiwa yuko motoni, hahitaji Misa yoyote.’
“Kasisi akauliza hivi: ‘Namna gani ikiwa yuko toharani?’
“Nilimjibu hivi: ‘Bwana kasisi, unajua vizuri kwamba nina mali nyingi sana. Niko tayari sasa hivi kukupa mali yote hiyo mbele ya wakili ikiwa unaweza kunithibitishia kwa kutumia Biblia kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo inaendelea kuishi anapokufa, kwamba kuna mahali pa moto wa mateso na toharani, na kwamba Mungu ni Utatu.’
“Alinikodolea macho, akawasha sigara, na kuondoka.”
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 149]
Ndugu wakihubiri huko Slovenia wakitumia lori ambalo walikodi
-