-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
TULIKUSANYIKA KWA UMOJA HUKO UJERUMANI
Ingawa ndugu zetu huko Yugoslavia hawakuwa wametenganishwa kama wale wa nchi nyingine za Kikomunisti, walikuwa wachache na walitamani kuona upendo wa ndugu zetu wa ulimwenguni pote. Kwa hiyo, walipopata habari kwamba Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” lilipangwa kufanyika mwaka wa 1969, waliomba serikali iwaruhusu kutoka nchini ili wahudhurie kusanyiko hilo. Wazia furaha waliyohisi walipokubaliwa kusafiri!
Kusanyiko lilifanywa katika uwanja mkubwa huko Nuremberg, Ujerumani, mahali ambapo Hitler, aliyetisha kuwaangamiza kabisa Mashahidi wa Yehova, alihudhuria maonyesho ya wanajeshi wake makumi machache ya miaka mapema. Programu ilitolewa katika lugha nyingi, na wajumbe kutoka Yugoslavia walisisimuka kujua kwamba kungekuwa na programu mbalimbali katika lugha zao katika eneo lenye miti mingi karibu na uwanja mkuu. Jukwaa kubwa liligawanya uwanja huo wa michezo ili nusu ya wajumbe, walioketi upande mmoja, wasikilize programu katika Kiserbia na Kikroatia, huku ile nusu nyingine, upande wa pili wa jukwaa, wasikilize programu katika Kislovenia. Programu hiyo ya siku nane iliongeza sana ujuzi na imani ya akina ndugu.
Magari ya moshi na mabasi yalikodiwa kutoka sehemu zote za Yugoslavia ili kupeleka wajumbe Ujerumani. Ndugu mmoja kutoka Kroatia aliyesafiri kwenda Ujerumani anaeleza hivi: “Tukiwa wenye msisimko wa kuungana na ndugu na dada zetu, tulionyesha kwa fahari ishara zilizotangaza kusanyiko hilo kupitia madirisha ya gari-moshi letu.”
Ndugu walifurahi kuwaona na kuwasikiliza Nathan Knorr na Frederick Franz kutoka makao makuu ya ulimwenguni. Mjumbe mmoja anakumbuka: “Ilikuwa vigumu kwetu kuzuia furaha yetu walipokuja kwenye sehemu yetu ya uwanja ili kutusalimu.” Baraka ambazo ndugu wa Yugoslavia walipata zilipita kwa mbali jitihada nyingi walizofanya ili kuhudhuria kusanyiko hilo. Milosija Simić aliyesafiri kutoka Serbia anasema: “Ilinigharimu mishahara ya miezi miwili ili kusafiri kwenda kusanyikoni, na ilikuwa vigumu kupata siku kumi za likizo kazini. Sikuwa na uhakika ikiwa ningeendelea na kazi yangu baada ya kurudi kutoka kusanyikoni, lakini niliazimia kusafiri. Lilikuwa kusanyiko zuri ajabu! Mpaka leo hii, miaka 40 hivi baadaye, bado ninatokwa na machozi ya shangwe ninapokumbuka kusanyiko hilo.” Baada ya kujiunga na Mashahidi wenzao kutoka kila sehemu ya Yugoslavia ili kufurahia umoja wa undugu wetu wa ulimwenguni pote, akina ndugu walirudi nyumbani wakiwa wametiwa nguvu kukabiliana na matatizo yaliyokuwa mbele yao.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 184, 185]
Nyuma: Kusanyiko la Kimataifa la “Amani Duniani” la mwaka wa 1969, Nuremberg, Ujerumani; kushoto: gari-moshi la wajumbe wa kusanyiko kutoka Yugoslavia; kulia: Nathan Knorr
-