Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • MAPAINIA WATUMWA KWENYE ENEO

      Katika miaka ya 1930, wanaume na wanawake wenye bidii walifungua njia ya kuangaza nuru ya kweli katika nchi ya Yugoslavia. Kwa mfano, huko Maribor, Slovenia, Grete Staudinger, Katarina Konečnik, na baadaye Karolina Stropnik walijiandikisha katika ule uliokuja kuitwa utumishi wa upainia wa wakati wa likizo. Upande wa kusini huko Mostar, mji mkuu wa Herzegovina, kiongozi wa kikundi cha wanamuziki anayeitwa Alfred Tuček alitambua kweli naye akawa painia. Dušan Mikić, mwenye umri wa miaka 23 kutoka Zagreb, Kroatia, alipata kijitabu kinachoitwa Wafu Wako Wapi? Yeye pia alifanya maendeleo ya haraka, akabatizwa, kisha akawa painia. Muda si muda, hesabu ya mapainia iliongezeka wakati ndugu na dada wenye bidii walipokuja kutoka Ujerumani.

      Kweli ilikuwa ikitia mizizi nchini Yugoslavia, lakini ilipigwa marufuku huko Ujerumani. Ofisi ya tawi ya Uswisi ilipanga kuwatuma mapainia 20 hivi wenye uzoefu nchini Yugoslavia, kama vile Martin Poetzinger, Alfred Schmidt, Vinko na Josephine Platajs, na Willi na Elisabeth Wilke. Ingawa hawakuzungumza Kislovenia au Kiserbo-Kroatia, mapainia hao wenye kujidhabihu walihubiri kwa ujasiri wakitumia kadi za kutoa ushuhuda, wakaweka msingi wa maendeleo ya wakati ujao.

      MATATIZO WALIYOKABILI WAKIFANYA UPAINIA

      Bidii ya mapainia hao kwa ajili ya Yehova na upendo wao kwa watu uliwasaidia kushinda matatizo ya kujifunza lugha na kukosa pesa. Ilikuwa vigumu pia kusafiri kutoka eneo moja kwenda lingine. Kwa kawaida, walitembea umbali wa kilomita 40 katika milima na mabonde kukiwa na hali mbaya sana ya hewa ili kufika kwenye vijiji vilivyo mbali. Dada mmoja painia anakumbuka kwamba alivua viatu na kutembea miguu mitupu kutoka kijiji mpaka kijiji ili viatu vyake visiharibike. Martin Poetzinger, ambaye baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikumbuka sana jinsi alivyosafiri maeneo ya mashambani akiwa amebeba mgongoni mfuko uliojaa vitabu, na kuwahubiria wote waliotaka kusikiliza.

      Tatizo la kusafiri lilikwisha wakati ndugu mmoja nchini Uswisi aliponunua baiskeli na kuwapa mapainia hao waaminifu. Baiskeli hizo zilitumiwa katika huduma kwa miaka mingi.

      Ingawa watu wa Yugoslavia walijulikana kwa sababu ya ukarimu wao, kulikuwa na upinzani wa kidini na mapainia wetu walipingwa vikali. Makasisi walikuwa na mamlaka kubwa sana juu ya wafuasi wao, hasa katika vijiji vidogo. Nyakati nyingine, makasisi waliwachochea watoto wa shule wawafuate mapainia na kuwarushia mawe. Viongozi wa kidini pia waliwachochea wenye mamlaka ili wawashambulie mapainia, wachukue vitabu vyao, na kuwakamata.

      Pindi moja, Willi Wilke alipokuwa akihubiri katika kijiji kimoja cha mashambani huko Kroatia, alisikia watu wengi wenye msisimuko katika uwanja wa kijiji hicho. Yeye na mke wake, pamoja na Grete Staudinger, ambaye pia alikuwa painia, walikuwa wakiwaachia watu kijitabu (kinachoitwa Righteous Ruler, yaani, Mtawala Mwadilifu), ambacho kilikuwa na picha ya Yesu Kristo kwenye jalada. Wilke anasema hivi: “Nilishtuka sana nilipofika na kuona umati wenye hasira wa watu 20 hivi, wakiwa wamebeba mapanga ya kuvuna huku wakiwa wamemzingira mke wangu. Hapo karibu, kikundi kingine cha watu kilikuwa kikiteketeza vijitabu vyetu.”

      Mapainia hao hawakujua kwa nini wanakijiji hao wapole walikuwa wamekasirika sana hivyo, na Dada Wilke hangeweza kujua kwa nini walikasirika kwa sababu hakujua vizuri lugha yao. Hata hivyo, Grete aliongea vizuri sana Kijerumani na lugha za wenyeji hao. Alisonga karibu na kuwauliza, “Mabibi na mabwana, mnafanya nini?”

      “Hatumtaki Mfalme Peter!” wakamjibu wote kwa pamoja.

      “Hata sisi hatumtaki,” Grete akawaambia.

      Kwa mshangao, watu hao walionyesha picha iliyo kwenye jalada la kijitabu hicho na kuuliza, “Basi kwa nini mnaeneza habari zake?”

      Sasa Grete alielewa kilichowakasirisha. Mwaka uliotangulia wa 1934, Mfalme Alexander wa Kwanza wa Yugoslavia aliuawa, na mwanaye Peter alipaswa kurithi kiti chake cha ufalme. Hata hivyo, watu wa kijiji hicho walitaka kujitawala badala ya kutawaliwa na wafalme wa Serbia. Wanakijiji hao walifikiri kwamba picha ya Yesu Kristo ilikuwa ya Mfalme Peter!

      Tatizo hilo lilisuluhishwa na ushahidi kamili ukatolewa kumhusu Mfalme, Yesu Kristo. Watu fulani walioteketeza vijitabu vyao sasa walitaka vingine. Mapainia hao waliondoka kwenye kijiji hicho wakiwa na furaha, nao walihisi kwamba Yehova alikuwa amewalinda.

      Mapainia hao walihitaji pia kufikiria desturi za wenyeji. Walipokuwa wakihubiri katika vijiji vyenye Waislamu wengi huko Bosnia, walikuwa waangalifu sana ili wasiwaudhi wenyeji. Kwa mfano, kumtazama kwenye macho mwanamke Mwislamu aliyeolewa kungemkasirisha sana mume wake.

      Wakati huo, kulikuwa na makutaniko na vikundi vichache sana nchini. Kwa hiyo, baada ya kuhubiri mchana kutwa katika kijiji kilicho mbali, nyakati nyingine ilikuwa vigumu kupata mahali pa kulala usiku. Mapainia hawangeweza kukodi chumba kizuri cha kulala kwa sababu hawakuwa na pesa za kutosha. Josephine Platajs anakumbuka hivi: “Katika kijiji kimoja kila mtu alikataa kutupa mahali pa kulala kwa sababu walimwogopa kasisi wao Mkatoliki. Usiku ulikuwa umeingia tulipokuwa tukiondoka katika kijiji hicho. Njiani, tuliona mti mkubwa na majani yake makavu yalikuwa yameanguka chini—tulilala kwenye majani hayo usiku huo! Tulitumia mifuko yetu ya kubeba nguo chafu kama mto wa kulalia, na mume wangu aliifunga baiskeli kwa kamba na kuifungilia kamba hiyo kwenye mguu wake. Tuliamka asubuhi na kugundua kwamba tulilala karibu na kisima, kwa hiyo tulipata maji ya kuoga. Yehova alitulinda na pia alitimiza mahitaji yetu ya kimwili.”

      Mapainia hao waliona jinsi Yehova alivyowatunza hata katika mambo madogo. Walihangaikia kutangaza habari njema kuliko kuwa na maisha ya starehe.

      WAVUKA KUINGIA MAKEDONIA

      Alfred na Frida Tuček, ambao walikuwa mapainia, walieneza ujumbe wa Ufalme walipokuwa wakisafiri kutoka Slovenia kwenda Bulgaria. Katika mji wa Strumica, Makedonia, walimhubiria mwenye duka mmoja anayeitwa Dimitar Jovanovič, na kumwazima vitabu fulani. Mwezi mmoja baadaye, walipokuwa wakirudi kutoka Bulgaria, walimtembelea tena. Waliposikia kwamba hakusoma vitabu hivyo, walimwomba avirudishe ili wampe mtu mwingine ambaye angevithamini. Hilo lilimchochea Dimitar kuvisoma. Akawasihi wampe nafasi nyingine ya kusoma vitabu hivyo. Baada ya kuvisoma, aligundua kwamba alikuwa amepata kweli, naye akawa mtu wa kwanza kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova huko Makedonia.

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 154]

      Mapainia wa zamani walikabili matatizo mengi

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Kiongozi wa Bendi Anakuwa Painia

      Miaka mingi iliyopita katika nchi inayoitwa leo Bosnia na Herzegovina, kiongozi wa Bendi ya Royal Guards, Alfred Tuček, alipewa vichapo vinavyozungumzia Biblia na mfanyakazi mwenzake Fritz Gröger. Alfred aliwasiliana na shirika la Lighthouse Society labda mwishoni mwa miaka ya 1920, huko Maribor, akasema kwamba alitaka kuwa painia wa kawaida. Muda si muda, akawa kati ya mapainia wa kwanza nchini Yugoslavia. Hata ingawa alikuwa na kazi yenye mshahara mnono akiwa kiongozi wa bendi ya jeshi, upendo wake kwa Yehova ulimsukuma aache kazi hiyo na akaamua ‘kutotazama mambo yaliyo nyuma.’ (Luka 9:62) Mwanzoni mwa miaka ya 1930, alisafiri pamoja na ndugu mapainia kutoka Ujerumani na kuwaonyesha watu sinema ya “Photo-Drama of Creation.” Pia, alisaidia sana kuchora ramani za maeneo na kupanga kazi ya kuhubiri nchini Yugoslavia. Mwaka wa 1934, alimwoa Frida, mmoja wa mapainia waliotoka Ujerumani. Mgawo wao wa kwanza ulikuwa Sarajevo, Bosnia. Baadaye, walihubiri habari njema katika sehemu fulani za Makedonia, Montenegro, Kroatia, na Serbia. Mwanzoni walisafiri sana kwa baiskeli, lakini baadaye walitumia pikipiki. Ingawa watu hawakukubali habari njema mara moja wakati huo na kwamba kazi ya kuhubiri ilikuwa imepigwa marufuku, walitambua umuhimu wa kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki