Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • ALIKUWA MWAMINIFU MPAKA MWISHO

      Lestan Fabijan, mjenzi wa nyumba kutoka Zagreb, aliwafundisha kweli Ivan Sever, Franjo Dreven, na Filip Huzek-Gumbazir. Wote walibatizwa katika muda wa miezi sita wakaanza kuhubiri na kufanya mikutano. Jioni ya Januari 15, 1943, wanajeshi waliokuwa wakilinda doria walifika kwenye nyumba ya Ivan Sever na kumkamata pamoja na Franjo Dreven na ndugu mwingine, Filip Ilić. Walipekua nyumba yake wakachukua vitabu vyote, na kuwakamata ndugu hao.

      Lestan alipata habari kwamba walikuwa wamekamatwa, kwa hiyo akaenda pamoja na Filip Huzek-Gumbazir kumfariji mama na dada ya Franjo. Hata hivyo, wanajeshi Wakomunisti walisikia kuhusu ziara yao, wakawakamata Lestan na Filip. Ndugu hao watano walieleza wakitumia Biblia kwamba walimtumikia Yehova peke yake na kwamba wao ni askari-jeshi wa Kristo. Walihukumiwa kifo kwa sababu wote walikataa kuchukua silaha na kupigana katika vita. Basi, walishikwa mateka.

      Usiku mmoja ndugu hao watano waliamshwa usingizini, wakavuliwa nguo zote, na kupelekwa msituni. Walipokuwa wakitembea, walipewa nafasi ya kubadili maoni yao. Wanajeshi walijaribu kuvunja azimio la ndugu hao kwa kuwashawishi wakitumia upendo wao kwa familia zao. Walizungumza kuhusu mke mjamzito wa Filip Huzek-Gumbazir na watoto wake wanne. Aliwajibu kwamba alikuwa na hakika kabisa kwamba Yehova angewatunza. Franjo Dreven hakuwa na mke wala watoto, kwa hiyo, walimuuliza ni nani ambaye angemtunza mama yake na dada yake.

      Walipofika, wanajeshi hao waliwaagiza ndugu hao wasimame katika baridi kali sana. Kisha wakaanza kuwaua. Kwanza, walimpiga risasi Filip Huzek-Gumbazir. Halafu wanajeshi walingoja na kuwauliza wale wengine ikiwa walitaka kubadili msimamo wao. Hata hivyo, ndugu hao walikuwa wameazimia kubaki thabiti. Kwa hiyo, wanajeshi hao walimuua Franjo, halafu Ivan, kisha Lestan. Mwishowe, Filip Ilić, aliyekuwa amebaki, alilegeza msimamo wake akakubali kujiunga na hao wanajeshi. Hata hivyo, miezi mitatu baadaye, alirudi nyumbani akiwa mgonjwa na kusimulia yaliyotendeka. Alijaribu kuokoa uhai wake kwa kulegeza msimamo wake lakini akafa ghafula kwa sababu ya ugonjwa.

      Huko Slovenia, ndugu na dada zetu wengi waliteswa. Kwa mfano, Franc Drozg, fundi wa vifaa vya chuma mwenye umri wa miaka 38, alikataa kushiriki katika vita. Kwa hiyo, wanajeshi Wanazi walimuua huko Maribor mnamo Juni 8, 1942. Watu fulani walioshuhudia wanasema kwamba kabla hajapigwa risasi alivishwa shingoni ishara yenye maneno “Mimi si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yoh. 17:14) Imani yake yenye nguvu inathibitishwa na barua aliyoandika dakika chache kabla ya kuuawa, alisema hivi: “Rafiki mpendwa! Rupert, leo nilihukumiwa kifo. Usiomboleze kwa ajili yangu. Ninakutumia salamu zangu za upendo pamoja na wote walio nyumbani. Tutaonana katika Ufalme wa Mungu.”

      Wenye mamlaka walifanya yote waliyoweza kukomesha kazi ya kuhubiri, hata hivyo, Yehova alithibitika kuwa Mungu wa wokovu. Kwa mfano, kwa kawaida polisi walikuja ghafula na kuwapanga kwenye foleni wakaaji wote wa eneo fulani na kuchunguza vitambulisho vyao. Watu wote ambao polisi waliwatilia shaka walipelekwa gerezani. Wakati huohuo, polisi wengine walipekua nyumba za watu. Mara nyingi ndugu waliona Yehova akiwalinda kwa kuwa polisi hawakuingia katika nyumba zao huku wakifikiri kwamba tayari walikuwa wamezipekua. Angalau katika pindi mbili, nyumba za akina ndugu zilikuwa na vitabu vingi, na pia mashini za kunakili. Wale walioshiriki katika kazi ya kuhubiri nyakati hizo zenye hatari waliona tena na tena uhakikisho huu wa Biblia ukitimia: “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.”—Yak. 5:11.

      WALIHUKUMIWA KIFO

      Vita vya Pili vya Ulimwengu viliisha mwaka wa 1945, na kipindi kibaya zaidi cha umwagaji wa damu katika historia ya wanadamu kikafikia mwisho. Ndugu walitumaini kwamba kushindwa kwa Hitler na washiriki wake kungefanya vizuizi viondolewe na kwamba wangepata tena uhuru wa kuhubiri. Kulikuwa na sababu nzuri ya matumaini hayo: Serikali mpya ya Kikomunisti iliyosimamishwa iliahidi kuleta uhuru wa vyombo vya habari, uhuru wa kusema, na uhuru wa ibada.

      Hata hivyo, Septemba 1946, ndugu 15 na dada 3 walikamatwa. Kati yao ni Rudolf Kalle, Dušan Mikić, na Edmund Stropnik. Uchunguzi uliendelea kwa miezi mitano. Wenye mamlaka waliwashtaki Mashahidi kuwa wanawatendea vibaya watu na Serikali na kwamba wanahatarisha sana nchi ya Yugoslavia. Walidai kuwa kazi yetu iliongozwa kutoka Marekani na kwamba tulihubiri Ufalme wa Mungu kama kisingizio cha kuharibu usoshalisti na kurudisha ubepari. Kasisi mmoja Mkatoliki alikuwa mstari wa mbele kuwashtaki ndugu kwamba ni wapelelezi wa Marekani wanaojifanya kuwa watu wa dini.

      Mahakamani, ndugu hao walioshtakiwa walijitetea wenyewe kwa ujasiri na wakatoa ushahidi mzuri kumhusu Yehova na Ufalme wake. Ndugu mmoja kijana anayeitwa Vjekoslav Kos, alisema hivi: “Enyi mahakimu wenye hekima, nilipata dini hii na mafundisho ya Biblia kutoka kwa mama yangu, na niliabudu Mungu. Wakati wa uvamizi wa Wajerumani, mama alifungwa gerezani. Dada zangu wawili na ndugu yangu walikuwa pia washiriki wa dini ya mama yangu. Walipelekwa pia kwenye kambi ya mateso ya Dachau, ambako walipigwa risasi kwa kuwa walionwa kuwa wakomunisti kwa sababu walimwabudu Mungu. Na ni kwa sababu ya dini hiyohiyo kwamba niko hapa leo mbele ya mahakama nikishtakiwa kuwa Mfashisti.” Mahakama ilimwachilia huru.

      Hata hivyo, mahakama hiyo haikuwahurumia ndugu wengine. Watatu kati ya ndugu walioshtakiwa walihukumiwa kuuawa kwa kupigwa risasi, na waliobaki walihukumiwa kifungo cha jela kuanzia mwaka 1 mpaka miaka 15. Hata hivyo, ndugu zetu ulimwenguni pote walipinga vikali na kwa haraka sana ukosefu huo wa haki. Mashahidi wa Marekani, Kanada, Visiwa vya Uingereza, na Ulaya waliandikia serikali ya Yugoslavia maelfu ya barua za malalamiko. Walituma pia mamia ya telegramu. Hata maofisa fulani wa serikali waliandika ili kuwatetea akina ndugu. Kwa sababu ya kuungwa mkono sana hivyo, hukumu za vifo zilibadilishwa na kuwa vifungo vya miaka 20 gerezani.

      Hata hivyo, upinzani haukukoma. Miaka miwili baadaye, wenye mamlaka wa Slovenia walimkamata Janez Robas na mke wake, Marija, pamoja na Mashahidi wenzake Jože Marolt na Frančiška Verbec, kwa sababu ya kuhubiri. Shtaka lilisema hivi kwa sehemu: “‘Madhehebu ya wayehova’ . . . yaliwaandikisha washiriki wapya na kuwachochea kupinga mfumo wetu wa kijamii [na] kuwakataza kuwa wanajeshi.” Wakidai kwamba akina ndugu walijaribu kudhoofisha ulinzi wa nchi, wenye mamlaka walitoa hukumu ya vifungo vya gereza pamoja na kazi ngumu kwa muda wa miaka mitatu mpaka miaka sita.

      Mwaka wa 1952, kwa sababu ya mabadiliko ya kisiasa, wafungwa wote waliachiliwa huru; na ujumbe wa Ufalme ukaendelea kuhubiriwa. Ahadi hii ya Yehova ilithibitika kuwa ya kweli: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu.”—Isa. 54:17.

      Hata hivyo, serikali iliendelea kujitahidi kudhoofisha azimio la akina ndugu la kusimama imara katika imani. Vyombo vya habari vilisema kwamba akina ndugu ni “wagonjwa wa akili” na “watu wenye msimamo mkali wa kiwazimu-wazimu hivi.” Ndugu fulani walianza kuvurugwa na ripoti mbaya zilizoendelea kuenezwa na pia woga wa kuchunguzwa kila mara. Mashahidi waaminifu walipoachiliwa huru kutoka gerezani, wengine katika makutaniko waliwaona kuwa wapelelezi. Hata hivyo, Yehova aliendelea kuyaimarisha makutaniko kupitia ndugu washikamanifu na wakomavu.

      Josip Broz Tito alipochukua mamlaka mwishoni mwa Vita vya Pili vya Ulimwengu, ilikuwa wazi kwamba jeshi ndilo lingeongoza mambo nchini Yugoslavia. Wale waliokataa kufanya kazi katika jeshi, haidhuru sababu walizotoa, walionwa kuwa wapinzani wa serikali.

      MAJARIBU YA USHIKAMANIFU

      Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Ladislav Foro, mwenye umri wa miaka 9, kutoka Kroatia, alikuwa kwenye mkutano wa lazima wa watu wa mji huo wakati kasisi mmoja Mkatoliki alipokuwa akihubiri. Baada ya mahubiri hayo, Ladislav alitazama kwa mshangao na kuona nyuma ya pazia la jukwaa kasisi huyo akivua kanzu yake ya kasisi. Ndani ya kanzu hiyo alikuwa amevalia vazi la chama cha Ustaša, na alikuwa amejifunga kiunoni mshipi ambao ulishikilia gruneti au bomu la mkononi. Akiwa ameshika upanga wake, kasisi huyo alipanda juu ya farasi na kupiga kelele: “Akina ndugu, acheni twende tuwageuze watu wawe Wakristo! Mtu yeyote akikataa, mnajua jambo la kufanya!”

      Ladislav alijua kwamba mtu wa Mungu hakupaswa kutenda hivyo. Muda mfupi baadaye, akiwa pamoja na mjomba wake alianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi iliyofanywa kisiri-siri. Ingawa hilo liliwakasirisha wazazi wake, Ladislav aliendelea kuhudhuria mikutano na akafanya maendeleo mazuri ya kiroho.

      Alipoitwa kujiunga na jeshi katika mwaka wa 1952, Ladislav alikataa waziwazi kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutokuwamo. Maofisa walimhoji tena na tena ili kujaribu kumlazimisha kula kiapo cha kujiunga na jeshi. Pindi moja, walimpeleka kwenye kambi ya jeshi ambamo makurutu au askari wanafunzi 12,000 walikusanyika ili kula kiapo. Walimsimamisha Ladislav mbele ya askari hao wote na wakamwekelea bunduki kwenye bega lake. Papo hapo, akaitupa bunduki hiyo chini. Wakitumia vipaza-sauti ili kila mtu asikie, askari-jeshi walisema kwamba ikiwa Ladislav angeitupa tena bunduki hiyo chini, wangempiga risasi. Alipokataa kwa mara ya pili, walimpeleka na kumsukuma ndani ya shimo lenye urefu wa mita kadhaa lililochimbwa na bomu. Amri ya kumuua ikatolewa, na askari-jeshi mmoja akapiga risasi mara mbili ndani ya shimo hilo, kisha wanajeshi hao wakarudi kambini. Hata hivyo, risasi zilimkosa ndugu huyo!

      Usiku huo, maofisa wakamtoa Ladislav ndani ya shimo hilo na wakampeleka gerezani huko Sarajevo. Alipewa barua iliyosema kwamba waamini wengine wa dini yake walikuwa wakilegeza msimamo wao wakati yeye anaendelea kuteseka gerezani pamoja na wafungwa wahalifu. Maofisa hao waliendelea tena na tena kumshinikiza kupitia mazungumzo marefu kama hayo. Hata hivyo, Ladislav alifikiri hivi: ‘Je, nilikubali kumtumikia Yehova kwa sababu ya mtu fulani? Hapana! Je, niko hapa ili nimpendeze mwanadamu? Hapana! Je, uhai wangu unategemea yale ambayo wengine huenda wakasema, kufikiri, au kufanya? Hapana!’

      Kufikiri kwa njia hiyo ya kiroho kulimsaidia Ladislav kubaki mwaminifu gerezani mpaka alipoachiliwa huru miaka minne na nusu baadaye. Baada ya muda alitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko na aliungwa mkono na mke wake mshikamanifu, Anica, ambaye alikuwa mwabudu mwenzake.

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Matatizo yaliendelea. Kwa sababu ya msimamo wa kutokuwamo wa akina ndugu, wenye mamlaka waliona kazi yao ya kuhubiri kuwa njia ya kueneza propaganda. Polisi wa siri wa taifa hilo pamoja na wapelelezi walifanya iwe vigumu sana kufanya kazi ya kuhubiri. Ndugu waliopatikana wakihubiri walikamatwa na kutozwa faini. Ripoti moja ilisema hivi: “Ndugu bado wanakamatwa na kushtakiwa. Hayo ndiyo mambo yanayotendeka hasa huko Slovenia, ambako Kanisa Katoliki lina uvutano mkubwa zaidi na ambako watu wengi wa Yehova wanachunguzwa na polisi na maofisa wao, ambao wanakusudia kuwashika wakijifunza Neno la Mungu. Lakini ndugu wanaonyesha kwamba wameazimia kushinda kusudi la mateso hayo, kwa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”

      “WENYE KUJIHADHARI KAMA NYOKA”

      Walipokuwa wakihubiri katika maeneo ya mashambani ya Slovenia, ndugu waliwauliza kwanza wenye nyumba ikiwa walikuwa na mayai ya kuuza. Ikiwa bei ilikuwa nzuri, wahubiri walinunua mayai ili kuepuka kutokeza shaka. Baada ya kupata mayai ya kutosha, waliwauliza wenye nyumba zinazofuata ikiwa walikuwa na kuni. Wakati wa majadiliano kuhusu bei, wangeweza kubadili mazungumzo na kuingia katika Biblia ikiwa hilo lilionekana kuwa jambo la busara.—Mt. 10:16.

      Katika eneo linalozunguka Zagreb, Kroatia, ndugu walihubiri eneo kwa utaratibu lakini kwa uangalifu sana ili wasigunduliwe. Mbinu moja ilikuwa kuhubiri kila nyumba ya kumi. Kwa mfano, ikiwa walipewa mgawo wa kuhubiri nyumba ya kwanza, wahubiri hao walihubiri nyumba ya 1, 11, 21, 31, na kadhalika. Kupitia jitihada hizo, watu wengi walimjua Yehova. Hata hivyo, kwa sababu ya magumu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, mahubiri yasiyo rasmi yalitumiwa mara nyingi.

      Huko Serbia ndugu walikutana katika nyumba za watu binafsi. Damir Porobić anaeleza jinsi mikutano ilivyofanywa katika nyumba ya nyanya yake baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Anasema: “Watu watano hadi kumi walihudhuria. Nyumba ya nyanya yangu ilifaa kwa sababu ilifikika kwa urahisi kutoka kwenye barabara mbili. Hilo liliwawezesha wote kuja na kuondoka kisiri-siri bila kutokeza shaka.”

      Veronika Babić alizaliwa huko Kroatia, na familia yake ilianza kujifunza Biblia katikati ya miaka ya 1950. Baada ya kubatizwa mwaka wa 1957, Veronika alihamia Sarajevo, Bosnia, pamoja na mume wake. Milica Radišić, ambaye alitoka katika eneo la Slavonia, huko Kroatia, alibatizwa mwaka wa 1950. Familia yake pia ilihamia Bosnia. Zikishirikiana, familia hizo zilianza kueneza kweli ya Ufalme huko Bosnia. Kama katika sehemu nyingine za Yugoslavia, walipaswa kuhubiri kwa uangalifu. Veronika anaeleza: “Tulishtakiwa kwa polisi, na vichapo vyetu vikachukuliwa. Tulikamatwa, tukahojiwa, tukatishwa kwamba tutatiwa gerezani, na tukatozwa faini. Hata hivyo, hakuna jambo lolote lililoweza kutuvunja moyo au kutuogopesha. Badala yake, yote hayo yaliimarisha imani yetu katika Yehova.”

      Milica anakumbuka: “Siku moja, mwanamume mmoja alikuja kwenye Jumba la Ufalme na akaonyesha kupendezwa na Biblia. Alikaribishwa vizuri na hata akakaa kwa muda katika nyumba za akina ndugu. Alitoa maelezo kwa bidii kwenye mikutano. Lakini baadaye binti yetu, akiwa mahali pake pa kazi, alimwona mwanamume huyo akihudhuria mkutano wa polisi wa siri. Kisha, tukatambua kwamba alikuwa ametumwa na polisi ili kutupeleleza. Kwa kuwa uhusiano wake na polisi haukuwa tena jambo la siri, aliacha kuja.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki