Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Lina Babić, ambaye alijifunza kweli Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikikaribia kwisha na ambaye alishirikiana kwa ukaribu na ndugu na dada waaminifu anasema hivi: “Wakati huo watu walikuwa na hamu kubwa sana ya kujifunza Biblia na walifurahia kuisoma.” Anasimulia hivi: “Kwa kuwa sikuzote tulihitaji kuwa waangalifu, niliamua kunakili vitabu kwa mkono katika kijitabu changu cha kibinafsi. Kwa njia hiyo, ikiwa ningepekuliwa, ingeonekana ni kana kwamba yalikuwa maandishi yangu binafsi.”

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Alifanya Kazi Mchana, na Kuchapisha Usiku

      LINA BABIĆ

      ALIZALIWA 1925

      ALIBATIZWA 1946

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Ametumika Betheli tangu 1953, kazi ilipohalalishwa. Alisaidia katika kuchapisha na kusambaza magazeti na vijitabu. Leo anatumika kwa uaminifu katika Betheli huko Zagreb.

      BAADA ya akina ndugu kuachiliwa huru kutoka gerezani, mipango ya kuchapisha magazeti ilifanywa haraka. Lakini ndugu walikuwa wachache, na kazi ilikuwa nyingi. Nilipoona uhitaji huo, niliamua kujitolea, hata ingawa nilikuwa na kazi ya kimwili. Hata hivyo, nilitaka kusaidia. Kwa hiyo, nilifanya kazi yangu ya kimwili mchana kutwa, na karibu usiku wote nilifanya kazi ya kuchapisha magazeti.

      Wakati huo, hatukuwa na majengo ya ofisi ya tawi. Hivyo, wenzi wa ndoa waliozeeka, Petar na Jelena Jelić, waliruhusu nyumba yao yenye chumba kimoja itumiwe kwa kazi ya kuchapisha magazeti. Chumba hicho kilikuwa na upana wa mita 4.5 hivi kila upande. Makaratasi yaliyochapishwa yaliwekwa kwenye kitambaa cha kitani kilichotandazwa juu ya fremu ya mbao. Fremu hiyo iliwekwa juu ya kitanda. Mashini ya kuchapishia iliyoendeshwa kwa mikono iliwekwa juu ya meza kando ya kitanda. Tulichapisha kurasa 800 hivi kwa saa. Tulichapisha nakala chache sana ukilinganisha na nakala zinazochapishwa na mashini za kisasa, lakini tulitosheka kwamba kwa subira na jitihada nyingi sana tulichapisha vichapo vyote tulivyohitaji.

      Tuliguswa moyo sana kuona ndugu na dada Jelić wakingoja kwa subira mpaka tulipomaliza kufanya kazi na kuondoa vichapo tulivyochapisha ili waweze kulala. Hawakulalamika kamwe. Badala yake, walifurahi, na macho yao yaling’aa kwa shangwe kwa sababu walitegemeza kazi ya Ufalme kwa njia hiyo. Jelena pamoja na dada wengine waliozeeka, walisaidia kukusanya, kuunganisha, na kukunja kurasa zilizochapishwa. Msaada wao ulikuwa muhimu sana.

      Mwaka wa 1958, tulinunua mashini ya kuchapishia inayotumia umeme, hivyo, kazi ya kuchapisha ikawa rahisi zaidi. Mwaka wa 1931 tulikuwa tukichapisha magazeti 20 tu, na kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1960, tulikuwa tukichapisha magazeti 2,400 katika lugha tatu, Kikroatia, Kiserbia (Kisirili), na Kislovenia. Hata ingawa hatungeweza kuchapisha vitabu, tulichapisha vijitabu vingi. Mwaka wa 1966, tulifanya kazi kubwa ya kuchapisha kuliko wakati mwingine wowote. Mchapishaji mmoja alichapisha kitabu “Mambo Asiyoweza Mungu Kusema Uongo” katika vijitabu 12. Kila kitabu kilikuwa na seti ya vijitabu 12. Tulilazimika kuchapisha vijitabu 600,000 katika lugha tatu, yaani, vitabu 50,000.

      Leo ninatumika katika Betheli ya Zagreb. Ninafurahi ninapokumbuka miaka yangu ya utumishi na kuona jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi katika nchi zote zilizokuwa sehemu ya Yugoslavia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki