-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Ofisi ya tawi ya Uswisi ilipanga kuwatuma mapainia 20 hivi wenye uzoefu nchini Yugoslavia, kama vile Martin Poetzinger, Alfred Schmidt, Vinko na Josephine Platajs, na Willi na Elisabeth Wilke. Ingawa hawakuzungumza Kislovenia au Kiserbo-Kroatia, mapainia hao wenye kujidhabihu walihubiri kwa ujasiri wakitumia kadi za kutoa ushuhuda, wakaweka msingi wa maendeleo ya wakati ujao.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Pindi moja, Willi Wilke alipokuwa akihubiri katika kijiji kimoja cha mashambani huko Kroatia, alisikia watu wengi wenye msisimuko katika uwanja wa kijiji hicho. Yeye na mke wake, pamoja na Grete Staudinger, ambaye pia alikuwa painia, walikuwa wakiwaachia watu kijitabu (kinachoitwa Righteous Ruler, yaani, Mtawala Mwadilifu), ambacho kilikuwa na picha ya Yesu Kristo kwenye jalada. Wilke anasema hivi: “Nilishtuka sana nilipofika na kuona umati wenye hasira wa watu 20 hivi, wakiwa wamebeba mapanga ya kuvuna huku wakiwa wamemzingira mke wangu. Hapo karibu, kikundi kingine cha watu kilikuwa kikiteketeza vijitabu vyetu.”
Mapainia hao hawakujua kwa nini wanakijiji hao wapole walikuwa wamekasirika sana hivyo, na Dada Wilke hangeweza kujua kwa nini walikasirika kwa sababu hakujua vizuri lugha yao. Hata hivyo, Grete aliongea vizuri sana Kijerumani na lugha za wenyeji hao. Alisonga karibu na kuwauliza, “Mabibi na mabwana, mnafanya nini?”
“Hatumtaki Mfalme Peter!” wakamjibu wote kwa pamoja.
“Hata sisi hatumtaki,” Grete akawaambia.
Kwa mshangao, watu hao walionyesha picha iliyo kwenye jalada la kijitabu hicho na kuuliza, “Basi kwa nini mnaeneza habari zake?”
Sasa Grete alielewa kilichowakasirisha. Mwaka uliotangulia wa 1934, Mfalme Alexander wa Kwanza wa Yugoslavia aliuawa, na mwanaye Peter alipaswa kurithi kiti chake cha ufalme. Hata hivyo, watu wa kijiji hicho walitaka kujitawala badala ya kutawaliwa na wafalme wa Serbia. Wanakijiji hao walifikiri kwamba picha ya Yesu Kristo ilikuwa ya Mfalme Peter!
Tatizo hilo lilisuluhishwa na ushahidi kamili ukatolewa kumhusu Mfalme, Yesu Kristo. Watu fulani walioteketeza vijitabu vyao sasa walitaka vingine. Mapainia hao waliondoka kwenye kijiji hicho wakiwa na furaha, nao walihisi kwamba Yehova alikuwa amewalinda.
-