-
Uwe na Bidii kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova!Mnara wa Mlinzi—2009 | Juni 15
-
-
Uwe na Bidii kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova!
“Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila.”—YOH. 2:17.
1, 2. Yesu alifanya nini hekaluni mwaka wa 30 W.K., na kwa nini?
FIKIRIA hali hii. Ni wakati wa Pasaka ya mwaka wa 30 W.K. Miezi sita iliyotangulia, Yesu alianza huduma yake duniani. Sasa yuko njiani kwenda Yerusalemu. Huko, akiwa hekaluni katika Ua wa Mataifa, Yesu anawakuta “wale waliokuwa wakiuza ng’ombe na kondoo na njiwa na waliokuwa wakivunja pesa wakiwa wameketi.” Anatumia mjeledi wa kamba, na kuwatoa wanyama wote nje, na bila shaka wafanyabiashara pia wanawafuata wanyama hao. Yesu anamwaga sarafu za wale ambao wanabadili pesa na kupindua meza zao. Anawaamuru wale wanaouza njiwa wachukue vitu vyao na kuondoka.—Yoh. 2:13-16.
2 Matendo ya Yesu yanaonyesha waziwazi kwamba anahangaikia hekalu. Anawaamuru hivi: “Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!” Wanafunzi wa Yesu wanapoangalia matukio hayo, wanakumbuka maneno yaliyoandikwa na mtunga-zaburi Daudi karne nyingi mapema: “Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila.”—Yoh. 2:16, 17; Zab. 69:9.
3. (a) Bidii ni nini? (b) Tunaweza kujiuliza swali gani?
3 Yesu alitenda kwa njia hiyo kwa sababu alichochewa na hangaiko na bidii kwa ajili ya nyumba ya Mungu. Bidii ni “hamu na shauku nyingi katika kufuatilia jambo fulani.” Katika karne hii ya 21, Wakristo zaidi ya milioni saba wanaonyesha bidii kwa ajili ya nyumba ya Mungu. Tukiwa mtu mmoja-mmoja, tunaweza tukajiuliza hivi: ‘Ninaweza kuongeza bidii yangu kwa ajili ya nyumba ya Yehova jinsi gani?’ Ili kutusaidia kujibu swali hilo, acheni kwanza tuchunguze nyumba ya Mungu leo ni nini. Kisha, tutachunguza mifano ya Biblia ya watu waaminifu ambao walionyesha bidii kwa ajili ya nyumba hiyo. Mifano yao iliandikwa “ili kutufundisha sisi” na inaweza kutuchochea kuwa na bidii kubwa hata zaidi.—Rom. 15:4.
Nyumba ya Mungu—Zamani na Leo
4. Hekalu lililojengwa na Sulemani lilitimiza kusudi gani?
4 Katika Israeli la kale, hekalu huko Yerusalemu ndilo lililokuwa nyumba ya Mungu. Bila shaka, Yehova hakuwa akiishi kihalisi katika hekalu hilo. Alisema hivi: “Mbingu ni kiti changu cha ufalme, na dunia ni kiti cha miguu yangu. Iko wapi, basi, nyumba ambayo ninyi mnaweza kunijengea, na pako wapi, basi, mahali pa kupumzika kwa ajili yangu?” (Isa. 66:1) Hata hivyo, hekalu lililojengwa wakati wa utawala wa Sulemani lilikuwa kitovu cha ibada ya Yehova, mahali ambapo sala zilitolewa.—1 Fal. 8:27-30.
5. Ni mpango gani uliopo leo ambao ulifananishwa na ibada kwenye hekalu la Sulemani?
5 Leo, nyumba ya Yehova si jengo fulani la mawe huko Yerusalemu au mahali pengine popote pale. Badala yake, ni mpango unaotusaidia kumkaribia Mungu katika ibada kwa msingi wa fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo. Watumishi wote waaminifu wa Mungu duniani wanamwabudu Yehova kwa umoja katika hekalu hilo la kiroho.—Isa. 60:4, 8, 13; Mdo. 17:24; Ebr. 8:5; 9:24.
6. Ni wafalme gani wa Yudea ambao walionyesha bidii ya pekee kwa ajili ya ibada ya kweli?
6 Baada ya Israeli kugawanyika katika falme mbili mwaka wa 997 K.W.K., wafalme 4 kati ya wale 19 waliotawala Yuda, sehemu ya kusini, walikuwa na bidii ya pekee kwa ajili ya ibada ya kweli. Wafalme hao walikuwa Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia. Ni masomo gani ya maana tunayoweza kujifunza kutokana na mifano yao?
Kumtumikia Mungu kwa Moyo Wote Kunaleta Baraka
7, 8. (a) Yehova anabariki utumishi wa aina gani? (b) Ni onyo gani tunaloweza kujifunza kutokana na mfano wa Mfalme Asa?
7 Wakati wa utawala wa Mfalme Asa, Yehova alitokeza manabii ili kuliongoza taifa Lake katika njia ya uaminifu. Kwa mfano, Biblia inatueleza kwamba Asa alimsikiliza nabii Azaria, mwana wa Odedi. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 15:1-8.) Mabadiliko ambayo Asa alifanya yalileta umoja kati ya watu wa Yuda na kati ya hesabu kubwa ya watu kutoka katika ufalme wa Israeli ambao walienda kuhudhuria kusanyiko kubwa lililofanywa huko Yerusalemu. Wote pamoja walitangaza azimio lao la kumwabudu Yehova kwa ushikamanifu. Tunasoma hivi: “Wakamwapia Yehova kwa sauti kubwa na kwa sauti za shangwe na kwa tarumbeta na kwa baragumu. Na Yuda wote wakaanza kushangilia juu ya lile jambo waliloapa; kwa maana walikuwa wameapa kwa moyo wao wote nao walikuwa wamemtafuta kwa furaha kamili hivi kwamba yeye aliwaruhusu wampate; na Yehova akaendelea kuwapa pumziko kuzunguka pande zote.” (2 Nya. 15:9-15) Bila shaka, Yehova atatubariki vivyo hivyo tukimtumikia kwa moyo wetu wote.—Marko 12:30.
8 Inasikitisha kwamba baadaye Asa alikasirika sana aliporekebishwa na mwonaji Hanani. (2 Nya. 16:7-10) Tunaitikia jinsi gani Yehova anapotushauri au kututolea mwongozo kupitia wazee Wakristo? Je, tunakubali na kutumia haraka mashauri yao yanayotegemea Maandiko na hivyo kuepuka kuanguka katika mtego wa kuwa na kinyongo?
9. Ni tishio gani ambalo Yehoshafati na Yuda walikabili, na walitenda jinsi gani?
9 Yehoshafati alitawala akiwa mfalme huko Yuda katika karne ya kumi K.W.K. Yeye na wakaaji wote wa Yuda walikabili tishio la majeshi ya muungano ya Waamoni, Wamoabu, na watu wa eneo lenye milima la Seiri. Ingawa aliogopa, mfalme huyo alifanya nini? Yeye na watu wake, wakiwa pamoja na wake na watoto wao, walikusanyika kwenye nyumba ya Yehova ili kusali. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 20:3-6.) Kupatana na maneno ambayo Sulemani alisema mapema wakati wa kuliweka wakfu hekalu, Yehoshafati alitoa dua akisema: “Ee Mungu wetu, je, hutafanya hukumu juu yao? Kwa maana hakuna nguvu ndani yetu mbele ya umati huu mkubwa unaokuja juu yetu; nasi wenyewe hatujui tunalopaswa kufanya, lakini macho yetu yanakuelekea wewe.” (2 Nya. 20:12, 13) Baada ya Yehoshafati kusali, hapo “katikati ya kutaniko,” roho ya Yehova ilimchochea Yahazieli, Mlawi, kusema maneno yenye kufariji ambayo yaliwapa watu tumaini.—Soma 2 Mambo ya Nyakati 20:14-17.
10. (a) Yehoshafati na Yuda walipata mwongozo jinsi gani? (b) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini mwongozo tunaopata kutoka kwa Yehova leo?
10 Ndiyo, wakati huo, Yehoshafati na ufalme wa Yuda walipata mwongozo kutoka kwa Yehova kupitia kwa Yahazieli. Leo, tunapata faraja na mwongozo kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Bila shaka, sikuzote tunapaswa kuwaheshimu na kushirikiana na wazee waliowekwa rasmi, ambao wanafanya kazi ya uchungaji kwa bidii na kuhakikisha kwamba miongozo ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” inafuatwa.—Mt. 24:45; 1 The. 5:12, 13.
11, 12. Ni somo gani tunaloweza kujifunza kutokana na hali ambayo Yehoshafati na Yuda walikabili?
11 Kama vile tu Yehoshafati na watu wake walivyokusanyika pamoja kutafuta mwongozo wa Yehova, basi tusipuuze kuhudhuria kwa ukawaida mikutano pamoja na ndugu na dada zetu. Ikiwa nyakati fulani tunajikuta katika hali ngumu, tusijue jambo la kufanya, acheni tufuate mfano mzuri wa Yehoshafati na watu wa Yuda na kusali kwa Yehova huku tukimtegemea kabisa. (Met. 3:5, 6; Flp. 4:6, 7) Hata ikiwa tunaishi mbali na waamini wenzetu, maombi yetu kwa Yehova yanatuunganisha na “ushirika mzima wa ndugu [zetu] ulimwenguni.”—1 Pet. 5:9.
12 Yehoshafati na watu wake walifuata mwongozo uliotolewa na Mungu kupitia Yahazieli. Walipata matokeo gani? Walishinda vita na wakarudi Yerusalemu ‘wakishangilia’ huku wakipiga “vinubi na tarumbeta, kwenye nyumba ya Yehova.” (2 Nya. 20:27, 28) Sisi pia tunaheshimu mwongozo unaotolewa na Yehova kupitia tengenezo lake na tunajiunga na wengine katika kumsifu.
Tutunze Vizuri Mahali Petu pa Mikutano
13. Ni kazi gani ambayo Hezekia alianzisha mwanzoni mwa utawala wake?
13 Katika mwezi wa kwanza wa utawala wake, Hezekia alionyesha kwamba alikuwa na bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova kwa kufungua tena hekalu na kulirekebisha. Aliweka makuhani na Walawi ili waisafishe nyumba ya Mungu. Walifanya kazi hiyo kwa muda wa siku 16. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 29:16-18.) Jitihada hizo zinatukumbusha kazi tunayofanya ya kutunza na kurekebisha mahali petu pa mikutano ili pawe safi, na hilo linaonyesha kwamba tuna bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova. Je, hujawahi kusikia mambo yaliyoonwa yanayoonyesha kwamba watu wanavutiwa na bidii ya ndugu na dada zetu ambao wanashiriki katika kazi hiyo? Ndiyo, jitihada zao zinamletea Yehova sifa nyingi.
14, 15. Ni kazi gani leo ambayo imemletea Yehova sifa nyingi? Toa mifano.
14 Katika jiji fulani kaskazini mwa Uingereza, mwanamume mmoja alipinga kazi ya marekebisho iliyokusudiwa kufanywa kwenye Jumba la Ufalme lililopakana na nyumba yake. Ndugu wa eneo hilo walimtendea kwa fadhili mwanamume huyo. Kwa kuwa ukuta ulio kati ya Jumba la Ufalme na nyumba ya jirani huyo ulihitaji kurekebishwa, ndugu walijitolea kufanya kazi hiyo bila malipo. Walifanya kazi kwa bidii, na walijenga upya karibu ukuta wote. Walishughulikia hali hiyo vizuri sana hivi kwamba jirani huyo alibadili mtazamo wake. Sasa yeye ndiye anayesaidia kuangalia ikiwa uwanja wa Jumba la Ufalme uko salama.
15 Watu wa Yehova wanashiriki katika kazi ya ulimwenguni pote ya ujenzi. Wajitoleaji wenyeji wanajiunga na watumishi wa wakati wote wa kimataifa kujenga Majumba ya Ufalme na pia Majumba ya Makusanyiko na makao ya Betheli. Sam ni injinia wa vyombo vya kusambaza joto, hewa, na mashini zinazopoza hewa. Yeye na mke wake, Ruth, wamesafiri katika nchi nyingi za Ulaya na Afrika kusaidia katika miradi ya ujenzi. Popote pale wanapoenda, wanafurahia pia kuhubiri pamoja na makutaniko ya maeneo hayo. Sam anaeleza kilichomchochea kushiriki katika miradi hiyo ya kimataifa: “Nilitiwa moyo na wengine ambao walitumikia hapa katika makao ya Betheli na katika nchi za kigeni. Kuona bidii na shangwe yao kulinichochea kabisa kutaka kuingia katika utumishi huo.”
Tii Maagizo ya Mungu
16, 17. Watu wa Mungu wameshiriki kwa bidii katika utendaji gani wa pekee, na kumekuwa na matokeo gani?
16 Zaidi ya kurekebisha hekalu, Hezekia alirudisha maadhimisho ya kila mwaka ya Pasaka ambayo Yehova alikuwa ameamuru. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 30:1, 4, 5.) Hezekia na wakaaji wa Yerusalemu walialika taifa lote, na hata wakaaji wa ufalme wa kaskazini kuhudhuria maadhimisho hayo. Wakimbiaji walipeleka barua za mwaliko kotekote nchini.—2 Nya. 30:6-9.
17 Katika miaka ya hivi karibuni, tumeshiriki katika jitihada zinazofanana kidogo na hizo. Tumetumia mialiko iliyochapishwa yenye kuvutia ili kuwaalika watu wa maeneo yetu kukusanyika nasi ili kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana, na hivyo kutii amri ya Yesu. (Luka 22:19, 20) Baada ya kupokea maagizo kwenye Mikutano yetu ya Utumishi, tumeshiriki kwa bidii katika kazi hiyo. Na Yehova ametubariki sana. Mwaka jana, Mashahidi wa Yehova milioni saba hivi waligawa mialiko hiyo, na jumla ya watu 17,790,631 walihudhuria!
18. Kwa nini ni jambo la maana sana kwetu kuwa na bidii kwa ajili ya ibada ya kweli?
18 Ilisemwa hivi kumhusu Hezekia: “Alimtegemea Yehova Mungu wa Israeli; na baada yake hapakuwa na yeyote kama yeye kati ya wafalme wote wa Yuda, hata wale waliomtangulia. Naye akaendelea kushikamana na Yehova. Hakugeuka kando na kuacha kumfuata, bali aliendelea kuzishika amri zake ambazo Yehova alimwamuru Musa.” (2 Fal. 18:5, 6) Na tufuate mfano wake. Bidii yetu kwa ajili ya nyumba ya Mungu itatusaidia ‘kuendelea kushikamana na Yehova’ huku tukitazamia uzima wa milele.—Kum. 30:16.
Fuata Haraka Mwongozo
19. Ni jitihada gani za pekee zinazofanywa wakati wa Ukumbusho?
19 Yosia alipotawala akiwa mfalme, yeye pia alifanya matayarisho makubwa ya kuadhimisha Pasaka. (2 Fal. 23:21-23; 2 Nya. 35:1-19) Sisi pia tunafanya matayarisho ya pekee kwa ajili ya makusanyiko ya wilaya, ya mzunguko, na ya pekee, na pia Ukumbusho. Katika nchi fulani ndugu zetu wanahatarisha hata maisha yao ili kukusanyika pamoja kuadhimisha kifo cha Kristo. Wazee wenye bidii wanahakikisha kwamba hakuna mtu anayesahauliwa katika kutaniko. Wale waliozeeka na wagonjwa wanasaidiwa ili wawepo wakati wa tukio hilo.
20. (a) Ni nini kilichotukia wakati wa utawala wa Mfalme Yosia, na alitenda jinsi gani? (b) Tunapaswa kuchukua kwa uzito somo gani?
20 Wakati wa kazi ya kurudisha ibada safi ambayo Mfalme Yosia alianzisha, Kuhani Mkuu Hilkia ‘alikipata kile kitabu cha sheria ya Yehova kupitia mkono wa Musa.’ Hilkia alimpa Shafani, mwandishi wa mfalme kitabu hicho, naye Shafani akaanza kumsomea Yosia ujumbe wa kitabu hicho. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:14-18.) Kulikuwa na matokeo gani? Papo hapo mfalme alirarua mavazi yake kwa huzuni naye akawaamuru watu wamtafute Yehova. Kupitia nabii wa kike Hulda, Mungu alitoa ujumbe ambao ulishutumu mazoea fulani ya kidini yaliyokuwa yakifanywa huko Yuda. Hata hivyo, jitihada nzuri za Yosia za kuondoa ibada ya sanamu zilionekana wazi, naye aliendelea kuwa na kibali cha Yehova ingawa ilitabiriwa kwamba misiba ingepata taifa hilo. (2 Nya. 34:19-28) Tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo? Bila shaka, tamaa yetu ni kama ile ya Yosia. Tunataka kufuata haraka mwongozo wa Yehova na kuchukua kwa uzito onyo kuhusu hatari ya kuruhusu uasi-imani na ukosefu wa uaminifu uchafue ibada yetu. Na tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ataona na kuthamini bidii yetu kwa ajili ya ibada safi, kama tu alivyofanya katika kisa cha Yosia.
21, 22. (a) Kwa nini tunapaswa kuonyesha bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova? (b) Tutachunguza nini katika habari inayofuata?
21 Wale wafalme wanne wa Yuda, yaani, Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia, walituwekea mifano mizuri katika kuwa na bidii kwa ajili ya ibada na nyumba ya Mungu. Bidii yetu inapaswa pia kutuchochea tumtegemee Yehova na kujitahidi kwa ajili ya ibada yake. Bila shaka, ni jambo la hekima na linaloleta furaha kutii maagizo ya Mungu na kuitikia upendo wake na kukubali nidhamu tunayopewa kupitia kutaniko na wazee.
-
-
Uwe na “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”!Mnara wa Mlinzi—2009 | Juni 15
-
-
Uwe na “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”!
‘Yesu alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili atukomboe sisi kutoka katika kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.’—TITO 2:14.
1. Kunatukia nini hekaluni Yesu anapofika mnamo Nisani 10, 33 W.K.?
NI NISANI 10, 33 W.K., siku chache tu kabla ya maadhimisho ya Pasaka. Umati mkubwa wa waabudu katika eneo la hekalu huko Yerusalemu umesisimuka. Ni nini kitakachotukia Yesu anapofika? Waandikaji watatu wa Injili, Mathayo, Marko, na Luka, wote wanathibitisha kwamba kwa mara ya pili, Yesu anawafukuza wale wanaouza na kununua hekaluni. Anapindua meza za wale wanaobadili pesa na viti vya wale ambao wanauza njiwa. (Mt. 21:12; Marko 11:15; Luka 19:45) Bidii ya Yesu haijapungua tangu alipochukua hatua kama hiyo miaka mitatu mapema.—Yoh. 2:13-17.
2, 3. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu hakuwa na bidii tu ya kulisafisha hekalu?
2 Simulizi la Mathayo linaonyesha kwamba katika pindi hiyo, Yesu hakuwa na bidii tu ya kulisafisha hekalu. Aliwaponya pia vipofu na vilema ambao walimwendea hekaluni. (Mt. 21:14) Simulizi la Luka linazungumza kuhusu kazi nyingine ambazo Yesu alitimiza. ‘Yesu alikuwa akifundisha kila siku katika hekalu.’ (Luka 19:47; 20:1) Kwa hiyo, bidii ya Yesu ilionekana wazi katika huduma yake ya hadharani.
3 Baadaye, mtume Paulo alimwandikia Tito na akaeleza kwamba Yesu ‘alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili atukomboe sisi kutoka katika kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.’ (Tito 2:14) Tunaweza kuwa wenye “bidii kwa ajili ya kazi njema” katika njia gani leo? Na mifano ya wafalme wazuri wa Yuda inaweza kututia moyo jinsi gani?
Bidii Katika Kuhubiri na Kufundisha
4, 5. Ni katika njia gani wafalme wanne wa Yuda walionyesha bidii kwa ajili ya kazi njema?
4 Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia walianzisha kampeni ya kuondoa kabisa ibada ya sanamu huko Yuda. Asa ‘aliondoa madhabahu za kigeni na mahali pa juu, akazivunja nguzo takatifu na kuikata miti mitakatifu.’ (2 Nya. 14:3) Yehoshafati, akichochewa na bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova, ‘aliondoa mahali pa juu na miti mitakatifu katika Yuda.’—2 Nya. 17:6; 19:3.a
5 Baada ya sherehe ya siku saba ya Pasaka ambayo Hezekia alifanya huko Yerusalemu, “Waisraeli wote waliokuwa hapo wakaenda katika majiji ya Yuda, nao wakazivunja nguzo takatifu na kuikata miti mitakatifu na kupabomoa mahali pa juu na madhabahu kutoka katika Yuda yote na Benyamini na katika Efraimu na Manase mpaka walipomaliza.” (2 Nya. 31:1) Kijana Yosia alikuwa mfalme alipokuwa na umri wa miaka minane tu. Maandiko yanasema hivi: “Katika mwaka wa nane wa kutawala kwake, alipokuwa angali mvulana, akaanza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake; na katika mwaka wa kumi na mbili akaanza kutakasa Yuda na Yerusalemu kutokana na mahali pa juu na miti mitakatifu na sanamu za kuchongwa na sanamu za kuyeyushwa.” (2 Nya. 34:3) Hivyo, wafalme hao wote wanne walikuwa na bidii kwa ajili ya kazi njema.
6. Kwa nini huduma yetu inaweza kulinganishwa na kampeni za wafalme waaminifu wa Yuda?
6 Vivyo hivyo leo, tunashiriki katika kampeni ya kuwasaidia watu waache mafundisho ya uwongo ya dini, kutia ndani ibada ya sanamu. Huduma yetu ya nyumba kwa nyumba inatuwezesha kukutana na watu wa kila aina. (1 Tim. 2:4) Msichana mmoja kutoka Asia anakumbuka jinsi mama yake alivyokuwa akifanya matambiko mbele ya sanamu nyingi nyumbani kwao. Kwa kuwa aliwaza kwamba sanamu zote haziwezi kumwakilisha Mungu wa kweli, mara nyingi msichana huyo alisali ili apate kumjua Mungu wa kweli. Aliposikia mlango ukigongwa alifungua na akakuta kwamba ni wanawake wawili Mashahidi ambao walikuwa tayari kumsaidia kujifunza kuhusu jina la pekee la Mungu wa kweli, Yehova. Alishukuru kama nini kujua ukweli kuhusu sanamu! Sasa anashiriki kwa bidii sana katika utumishi wa shambani, na hivyo anawasaidia watu wengine kiroho.—Zab. 83:18; 115:4-8; 1 Yoh. 5:21.
7. Tunaweza kufanya nini ili kuwaiga walimu waliotumwa kotekote nchini katika siku za Yehoshafati?
7 Tunaposhiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba, tunahubiri kikamilifu kadiri gani eneo ambalo tumegawiwa? Inapendeza kujua kwamba katika mwaka wa tatu wa utawala wake, Yehoshafati aliwatuma wakuu watano, Walawi tisa, na makuhani wawili. Aliwatuma katika majiji yote ili kuwafundisha watu sheria za Yehova. Kampeni yao ilikuwa na matokeo mazuri sana hivi kwamba watu wa mataifa jirani wakaanza kumwogopa Yehova. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 17:9, 10) Tukiwatembelea watu nyumbani kwao nyakati na siku tofauti-tofauti, huenda tukafanikiwa kuzungumza na washiriki wengi wa familia moja.
8. Tunaweza kupanua utumishi wetu jinsi gani?
8 Watumishi wengi wa Mungu leo wamekuwa tayari kuacha nyumba zao na kuhama ili kutumika mahali ambapo pana uhitaji mkubwa zaidi wa Mashahidi wenye bidii. Je, unaweza kufanya hivyo? Wengine wetu ambao hatuwezi kuhama huenda tukajaribu kuwahubiria watu wanaoishi katika eneo letu ambao wanazungumza lugha tofauti. Kwa sababu ya watu wa mataifa mbalimbali ambao anakutana nao katika eneo lake, Ron aliye na umri wa miaka 81 alijifunza salamu katika lugha 32! Hivi karibuni alikutana barabarani na wenzi fulani wa ndoa kutoka Afrika na akawasalimu kwa lugha yao ya asili, Yoruba. Walimuuliza Ron ikiwa aliwahi kuwa Afrika. Aliposema hapana, walimuuliza alijua jinsi gani lugha yao. Hilo lilimpa nafasi ya kuwatolea ushahidi mzuri. Bila kusita, walikubali magazeti na hata wakampa anwani yao. Ron alituma anwani hiyo kwa kutaniko la eneo ambako watu hao waliishi ili ndugu wa huko wajifunze nao Biblia.
9. Kwa nini ni jambo la maana katika huduma yetu kusoma maandiko moja kwa moja kutoka katika Biblia? Toa mfano.
9 Walimu waliotumwa na Yehoshafati kotekote nchini walikuwa na “kitabu cha sheria ya Yehova.” Ulimwenguni pote tunajitahidi kuwafundisha watu Biblia, kwa sababu Biblia ni Neno la Mungu. Tunaonyesha kwamba Biblia ni ya maana sana katika huduma yetu kwa kujitahidi kuwasomea watu moja kwa moja kutoka katika Biblia, ili wengine waone kuwa maneno yake ni ya kweli. Mwenye nyumba fulani alimweleza Shahidi mmoja anayeitwa Linda kwamba mume wake aliyepooza alihitaji msaada wake. Mwenye nyumba huyo alilalamika hivi: “Sijui nilifanya nini hivi kwamba Mungu akaruhusu jambo hili linipate.” Linda alimuuliza hivi: “Je, ninaweza kukuhakikishia jambo fulani?” Kisha, Linda akasoma maneno ya Yakobo 1:13 na kuongezea hivi: “Mateso yote ambayo sisi na wapendwa wetu tunapata si adhabu kutoka kwa Mungu.” Aliposikia maneno hayo, mwenye nyumba huyo akamkumbatia Linda kwa shauku. Linda anasema hivi: “Niliweza kumfariji kwa kutumia Biblia. Nyakati nyingine maandiko tunayosoma kutoka katika Biblia ni yale ambayo mwenye nyumba hajawahi kamwe kusikia.” Kwa sababu ya mazungumzo hayo, mwanamke huyo alikubali kujifunza Biblia.
Vijana Wanamtumikia Mungu kwa Bidii
10. Yosia aliwawekea jinsi gani mfano mzuri vijana Wakristo leo?
10 Tukirudia mfano wa Yosia, tunaona kwamba alifuatia ibada ya kweli akiwa kijana na alikuwa na umri wa miaka 20 hivi alipoanza kampeni yake kubwa ya kukomesha ibada ya sanamu. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:1-3.) Vijana wengi leo wanaonyesha bidii kama hiyo katika utumishi wao wa Ufalme.
11-13. Ni mambo gani tunaweza kujifunza kutoka kwa vijana ambao wanamtumikia Yehova kwa bidii leo?
11 Hannah, ambaye anaishi huko Uingereza, alikuwa na umri wa miaka 13 na alikuwa akijifunza Kifaransa shuleni aliposikia kwamba kikundi cha Kifaransa kilikuwa kimeanzishwa katika mji jirani. Baba yake alikubali kumsindikiza kuhudhuria mikutano huko. Sasa akiwa na umri wa miaka 18, Hannah ambaye ni painia wa kawaida anahubiri kwa bidii katika Kifaransa. Je, wewe pia unaweza kujifunza lugha ya kigeni na hivyo kuwasaidia watu wengine wajifunze kumhusu Yehova?
12 Rachel alifurahia sana kutazama video moja (Pursue Goals That Honor God au Poursuivez Des Objectifs Qui Honorent Dieu katika Kifaransa). Anaeleza hivi kuhusu maoni aliyokuwa nayo alipoanza kumtumikia Yehova mwaka wa 1995: “Nilifikiri nilikuwa nikiendelea vizuri katika kweli.” Kisha anaongezea hivi: “Baada ya kutazama video hiyo, sasa ninatambua kwamba nilikuwa tu nikifanya mambo ya msingi kwa miaka mingi. Ni lazima nipiganie kweli, nijitahidi kabisa na kukazia akili funzo langu la kibinafsi na utumishi wangu.” Sasa Rachel anaona kwamba anamtumikia Yehova kwa bidii zaidi. Amepata matokeo gani? “Uhusiano wangu pamoja na Yehova umekuwa mzuri sana. Sala zangu ni zenye maana zaidi, funzo langu ni zuri na lenye kuridhisha zaidi, na masimulizi ya Biblia yamekuwa halisi zaidi kwangu. Kwa hiyo, ninafurahia sana huduma na ninapata uradhi wa kweli ninapoona maneno ya Yehova yakiwafariji wengine.”
13 Luke ni kijana mwingine aliyetiwa moyo na video moja (Young People Ask—What Will I Do With My Life? au Les jeunes s’interrogent—Que vais-je faire de ma vie? ya Kifaransa). Baada ya kuitazama, Luke anaandika hivi: “Ninahisi nimechochewa kuchunguza upya maisha yangu.” Anakiri hivi: “Zamani, nilisukumwa kufuatilia usalama wa kifedha kwa kutanguliza elimu ya juu na kisha kukazia fikira miradi ya kiroho. Mikazo kama hiyo haimsaidii mtu kufanya maendeleo ya kiroho; badala yake inamdhoofisha.” Enyi akina ndugu na dada vijana, kwa nini msijaribu kuona ikiwa mnaweza kutumia mambo mliyojifunza shuleni ili kupanua huduma yenu kama alivyofanya Hannah? Na kwa nini msiige mfano wa Rachel kwa kufuatilia kwa bidii miradi ambayo kwa kweli inamheshimu Mungu? Fuateni mfano wa Luke, epukeni hatari ambazo zimekuwa mtego kwa vijana wengi.
Tii Maonyo kwa Bidii
14. Yehova anakubali ibada ya aina gani, na kwa nini si rahisi kudumisha ibada hiyo leo?
14 Watu wa Yehova wanahitaji kuwa safi ili Yehova akubali ibada yao. Isaya anaonya hivi: “Geukeni, geukeni, tokeni humo, msiguse kitu chochote kilicho najisi; tokeni katikati yake [Babiloni], jiwekeni safi, ninyi mnaovichukua vyombo vya Yehova.” (Isa. 52:11) Miaka mingi kabla ya Isaya kuandika maneno hayo, Mfalme mzuri Asa aliendelea kwa bidii na kampeni ya kuondoa kabisa upotovu wa maadili katika Yuda. (Soma 1 Wafalme 15:11-13) Na karne nyingi baadaye, mtume Paulo alimwambia Tito kwamba Yesu alijitoa mwenyewe kuwasafisha wafuasi wake na kuwafanya wawe “watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.” (Tito 2:14) Leo katika jamii hii iliyopotoka, si jambo rahisi kubaki safi kiadili, hasa kwa vijana. Kwa mfano, watumishi wote wa Mungu, vijana kwa wazee, wanapaswa kupambana ili kuepuka kabisa kuchafuliwa na ponografia (picha au habari za ngono) inayoonyeshwa kwenye vibao vya matangazo, televisheni, sinema, na hasa kwenye Intaneti.
15. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuchukia mambo mabaya?
15 Bidii yetu katika kutii maonyo ya Mungu inaweza kutusaidia kuchukia mambo mabaya. (Zab. 97:10; Rom. 12:9) Tunapaswa kuchukia kabisa ponografia ili “tuepuke uvutano wake wenye nguvu sana kama sumaku,” kama alivyosema Mkristo mmoja. Ili kutenganisha vipande vya chuma ambavyo vimeshikanishwa na sumaku, mtu anahitaji kutumia nguvu zaidi kuliko nguvu ambazo zinaunganisha vipande hivyo. Vivyo hivyo, tunahitaji jitihada kubwa ili kukataa kushawishiwa na ponografia. Lakini kuelewa madhara makubwa ambayo ponografia inaweza kutuletea kutatusaidia tuichukie kabisa. Ndugu mmoja alijitahidi sana kuacha zoea lake la kutazama ponografia kwenye Intaneti. Alihamisha kompyuta yake na kuiweka mahali ambapo washiriki wote wa familia wangeweza kuiona. Pamoja na hayo, yeye mwenyewe aliazimia zaidi kuwa safi kiadili na kuwa na bidii kwa ajili ya kazi njema. Hata alichukua hatua nyingine. Kwa kuwa alihitaji kutumia Intaneti katika shughuli zake, aliamua kutumia Intaneti wakati tu alipokuwa na mke wake.
Faida ya Kuwa na Mwenendo Mzuri
16, 17. Mwenendo wetu mzuri wa Kikristo unaweza kuwa na matokeo gani juu ya wale wanaotutazama? Toa mfano.
16 Vijana wa kiume na wa kike wanaonyesha mtazamo mzuri katika utumishi wa Yehova, na hilo linawavutia kama nini watazamaji! (Soma 1 Petro 2:12.) Mtu mmoja alibadili mtazamo wake kuelekea Mashahidi wa Yehova baada ya kufanya kazi kwa siku nzima akirekebisha mashini ya kuchapisha katika Betheli ya London. Mke wake, ambaye alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Shahidi mmoja, alitambua jinsi mtazamo wa mume wake ulivyobadilika. Kabla ya hapo, mwanamume huyo hakutaka Mashahidi wafike nyumbani kwake. Lakini aliporudi kutoka Betheli alisema mambo mengi mazuri kuhusu jinsi alivyotendewa kwa fadhili. Alisema kwamba hakusikia mtu yeyote akitumia lugha chafu. Kila mtu alikuwa mwenye subira, na mazingira yalikuwa ya amani. Alivutiwa hasa na ndugu na dada vijana ambao walifanya kazi kwa bidii bila mshahara, na ambao wamejitolea kutumia wakati na nguvu zao ili kusaidia kueneza habari njema.
17 Vivyo hivyo, ndugu na dada ambao wanafanya kazi za kimwili ili kutunza familia zao wanafanya hivyo kwa nafsi yao yote. (Kol. 3:23, 24) Mara nyingi, hilo linafanya waajiri wao wathamini bidii yao ya kutoka moyoni na hawataki kuwapoteza.
18. Tunaweza kuwa wenye “bidii kwa ajili ya kazi njema” jinsi gani?
18 Kumtegemea Yehova, kutii maagizo yake, na kutunza mahali petu pa mikutano ni kati ya mambo yanayoonyesha kwamba tuna bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova. Zaidi ya hayo, tunataka kushiriki kikamilifu kadiri tunavyoweza katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. Iwe sisi ni vijana au wazee, tutapata baraka nyingi ikiwa tutafanya yote tunayoweza ili kuishi kulingana na viwango vya usafi ambavyo vinahusianishwa na ibada yetu. Na tutaendelea kujulikana kuwa watu wenye “bidii kwa ajili ya kazi njema.”—Tito 2:14.
[Maelezo ya chini]
a Huenda Asa aliondoa mahali pa juu ambapo palitumiwa kwa ajili ya ibada ya miungu ya uwongo lakini si mahali ambapo watu walimwabudu Yehova. Au huenda ikawa kwamba mahali pa juu palijengwa tena katika kipindi cha mwisho cha utawala wa Asa na kwamba paliondolewa na mwana wake Yehoshafati.—1 Fal. 15:14; 2 Nya. 15:17.
-