Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Siku ya Hukumu ya Yehova I Karibu!
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Februari 15
    • Siku ya Hukumu ya Yehova I Karibu!

      “Hiyo siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; I karibu, nayo inafanya haraka sana.”—SEFANIA 1:14.

      1. Mungu alitoa onyo gani kupitia Sefania?

      YEHOVA MUNGU atawachukulia waovu hatua karibuni. Sikiliza! Hili ndilo onyo lake: “Nitamkomesha mwanadamu . . . nami nitamkatilia mbali mwanadamu, asionekane juu ya uso wa nchi.” (Sefania 1:3) Maneno hayo ya Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu yalisemwa kupitia nabii wake Sefania, ambaye huenda alikuwa kilembwe wa Mfalme Hezekia mwaminifu. Tangazo hilo, lililotolewa siku za Mfalme Yosia mzuri, halikuashiria mema kwa waovu walioishi Yuda.

      2. Kwa nini matendo ya Yosia hayakuizuia siku ya hukumu ya Yehova?

      2 Bila shaka, unabii wa Sefania ulifanya Yosia afahamu hata zaidi kwamba kulikuwa na uhitaji wa kuondoa ibada isiyo safi nchini Yuda. Hata hivyo, matendo ya mfalme huyo ya kuondoa nchini dini zisizo za kweli hayakuondoa uovu wote miongoni mwa watu wala kufunika dhambi za babu yake, Mfalme Manase, ambaye “aliujaza Yerusalemu damu zisizo na hatia.” (2 Wafalme 24:3, 4; 2 Mambo ya Nyakati 34:3) Kwa hiyo, bila shaka siku ya hukumu ya Yehova ingekuja.

      3. Twawezaje kuwa na hakika kwamba inawezekana kuokoka “siku ya hasira ya BWANA”?

      3 Hata hivyo, watu fulani wangeokoka siku hiyo yenye kutia hofu. Kwa hiyo, nabii wa Mungu alihimiza hivi: “Kabla haijazaa hiyo amri, kabla haijapita siku ile kama makapi, kabla haijawajilia hasira kali ya BWANA, kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA. Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.” (Sefania 2:2, 3) Tunapozingatia tumaini la kuokoka siku ya hukumu ya Yehova, acheni tuchunguze kitabu cha Biblia cha Sefania. Kiliandikwa huko Yuda kabla ya mwaka wa 648 K.W.K. nacho ni sehemu ya “neno la unabii” la Mungu, ambalo sote twapaswa kusikiliza kwa moyo wote.—2 Petro 1:19.

      Mkono wa Yehova Wanyoshwa

      4, 5. Andiko la Sefania 1:1-3 lilitimizwaje juu ya waovu wa Yuda?

      4 “Neno la BWANA” kwa Sefania laanza kwa onyo lililotajwa hapo awali. Mungu atangaza: “Nitavikomesha kabisa vitu vyote, visionekane juu ya uso wa nchi, asema BWANA. Nitamkomesha mwanadamu na mnyama; nitakomesha ndege wa angani, na samaki wa baharini, na hayo makwazo pamoja na wabaya; nami nitamkatilia mbali mwanadamu, asionekane juu ya uso wa nchi, asema BWANA.”—Sefania 1:1-3.

      5 Naam, Yehova angekomesha uovu wenye kupita kiasi nchini Yuda. Mungu angemtumia nani ‘kukomesha kabisa vitu vyote visionekane juu ya uso wa nchi’? Kwa kuwa yaonekana Sefania alitabiri mwanzoni mwa utawala wa Mfalme Yosia, ulioanza mwaka wa 659 K.W.K., maneno hayo ya unabii yalitimizwa wakati Yuda na jiji lake kuu, Yerusalemu, lilipofanywa ukiwa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. Wakati huo, waovu waliokuwa Yuda ‘walikomeshwa kabisa.’

      6-8. Ni nini kilichotabiriwa kwenye Sefania 1:4-6, na unabii huo ulitimizwaje katika Yuda ya kale?

      6 Likitabiri matendo ya Mungu dhidi ya waabudu wasio wa kweli, andiko la Sefania 1:4-6 lasema hivi: “Nitaunyosha mkono wangu juu ya Yuda, na juu ya watu wote wakaao Yerusalemu; nami nitayakatilia mbali mabaki ya Baali, yasionekane mahali hapa, na hilo jina la Wakemari pamoja na makuhani; na wale walisujudiao jeshi la mbinguni juu ya dari za nyumba; na hao waabuduo, waapao kwa BWANA na kuapa pia kwa Malkamu; na hao waliorudi nyuma, na kuacha kumfuata BWANA; na hao wasiomtafuta BWANA, wala kumwulizia.”

      7 Mkono wa Yehova ulikuwa umenyoshwa dhidi ya watu wa Yuda na Yerusalemu. Alikuwa ameazimia kukatilia mbali katika kifo waabudu wa Baali aliyekuwa mungu wa Kanaani wa uzazi. Miungu kadhaa ya huko iliitwa Mabaali kwa kuwa walioiabudu walidhani kuwa miungu hiyo ina uvutano fulani katika mahali maalumu. Kwa mfano, kulikuwa na Baali aliyeabudiwa na Wamoabi na Wamidiani kwenye Mlima Peori. (Hesabu 25:1, 3, 6) Kotekote nchini Yuda, Yehova angewakatilia mbali makuhani wa Baali pamoja na makuhani Walawi wasio waaminifu ambao walikuwa wanakiuka sheria ya Mungu kwa kushirikiana na makuhani hao wa Baali.—Kutoka 20:2, 3.

      8 Pia, Mungu angewakatilia mbali wale ‘walisujudiao jeshi la mbinguni,’ ambao yamkini walikuwa wanajimu na waliabudu jua. (2 Wafalme 23:11; Yeremia 19:13; 32:29) Hasira ya kisasi cha Mungu ingewapata pia wale waliojaribu kuchanganya ibada ya kweli na dini isiyo ya kweli kwa ‘kuapa kwa Yehova na kuapa pia kwa Malkamu.’ Huenda Malkamu ni jina jingine la Moleki, mungu mkuu wa Waamoni. Ibada ya Moleki ilitia ndani kutoa watoto dhabihu.—1 Wafalme 11:5; Yeremia 32:35.

      Mwisho wa Jumuiya ya Wakristo Unakaribia!

      9. (a) Jumuiya ya Wakristo ina hatia gani? (b) Tofauti na watu wa Yuda wasio waaminifu, twapaswa kuazimia kufanya nini?

      9 Huenda yote hayo yakatukumbusha Jumuiya ya Wakristo, ambayo imekolea ibada isiyo ya kweli na unajimu. Nako kule kudhabihu mamilioni ya watu kwenye madhabahu ya vita vinavyoungwa mkono na makasisi ni jambo lenye kuchukiza kwelikweli! Na tusiwe kamwe kama watu wasio waaminifu wa Yuda, ‘walioacha kumfuata Yehova,’ wakawa wasiojali chochote na kuacha kabisa kumtafuta au kutafuta mwelekezo wake. Badala yake, na tudumishe uaminifu-maadili wetu kwa Mungu.

      10. Unaweza kuelezaje maana ya unabii wa Sefania 1:7?

      10 Maneno yanayofuata ya nabii huyo yawafaa wakosaji wa Yuda na waovu wa leo. Andiko la Sefania 1:7 lasema hivi: “Nyamaza kimya mbele za Bwana MUNGU; kwa maana siku ya BWANA i karibu; kwa kuwa BWANA ameweka tayari dhabihu, amewatakasa wageni wake.” Yaonekana kwamba “wageni wake” walikuwa Wakaldayo ambao walikuwa maadui wa Yuda. “Dhabihu” ilikuwa Yuda yenyewe, pamoja na jiji lake kuu. Hivyo Sefania alitangaza kusudi la Mungu la kuharibu Yerusalemu, na unabii huo uliashiria pia kuharibiwa kwa Jumuiya ya Wakristo. Kwa kweli, kwa kuwa siku ya hukumu ya Mungu i karibu sana leo ulimwengu wote wapaswa ‘kunyamaza kimya mbele za Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova’ na kusikia asemayo kupitia “kundi dogo” la wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu na wenzao, ‘kondoo wake wengine.’ (Luka 12:32; Yohana 10:16) Wale wote ambao hawatasikiliza na hivyo kujipanga dhidi ya utawala wa Ufalme wa Mungu wataangamizwa.—Zaburi 2:1, 2.

      Siku ya Kilio I Karibu!

      11. Ni nini maana ya andiko la Sefania 1:8-11?

      11 Kuhusu siku ya Yehova andiko la Sefania 1:8-11 laongeza kusema hivi: “Na itakuwa, katika siku ile ya dhabihu ya BWANA, nitawaadhibu wakuu, na wana wa mfalme, na watu wote waliovaa mavazi ya kigeni. Na katika siku ile nitawaadhibu hao wote warukao juu ya kizingiti, waijazao nyumba ya bwana wao udhalimu na udanganyifu. Na katika siku ile, asema BWANA kutakuwako sauti ya kilio kutoka lango la samaki, na mlio mkuu katika mtaa wa pili, na mshindo mkuu kutoka milimani. Haya! lieni, ninyi mkaao katika Makteshi, maana wafanya biashara wote wameangamia; hao wote waliokuwa na mizigo ya fedha wamekatiliwa mbali.”

      12. Inakuwaje kwamba watu fulani wanapatikana wakiwa ‘wamevaa mavazi ya kigeni’?

      12 Yehoahazi, Yehoyakimu, na Yekonia wangetawala baada ya Mfalme Yosia. Kisha Yerusalemu lingeharibiwa wakati wa utawala wa Zedekia. Ingawa walikuwa wanakabiliwa na maafa hayo, yaonekana watu fulani walitafuta kibali cha mataifa jirani kwa ‘kuvaa mavazi ya kigeni.’ Vivyo hivyo wengi leo hudhihirisha kwa njia mbalimbali kwamba wao si sehemu ya tengenezo la Yehova. Kwa kuwa wanathibitika kuwa sehemu ya tengenezo la Shetani, wataadhibiwa.

      13. Kwa kupatana na unabii wa Sefania, ni nini ambacho kingetukia wakati Wababiloni wangeshambulia Yerusalemu?

      13 “Siku ile” ambayo Yuda ilitozwa hesabu yalingana na siku ya Yehova ya kutekeleza hukumu yake dhidi ya maadui wake, kukomesha uovu, na kuthibitisha ukuu wake. Wababiloni washambuliapo Yerusalemu, kilio kingetoka katika Lango la Samaki. Huenda liliitwa hivyo kwa kuwa lilikuwa karibu na soko la samaki. (Nehemia 13:16) Magenge ya Babiloni yangeingia sehemu iitwayo mtaa wa pili, na huenda ikawa “mshindo mkuu kutoka milimani” warejezea kishindo cha Wakaldayo wanaokaribia. Wakazi wa Makteshi, yamkini sehemu ya juu ya Bonde la Tiropoa, ‘wangelia.’ Kwa nini wangelia? Kwa sababu biashara, kutia ndani biashara ya “waliokuwa na mizigo ya fedha,” ingekoma.

      14. Mungu angewachunguza kwa undani kadiri gani wale wanaodai kuwa waabudu wake?

      14 Yehova angewachunguza kwa undani kadiri gani wale wanaodai kuwa wanamwabudu? Unabii huo waendelea kusema hivi: “Kisha itakuwa wakati ule, nitauchunguza Yerusalemu kwa taa; nami nitawaadhibu watu walioganda juu ya sira zao; wasemao katika mioyo yao, BWANA hatatenda mema, wala hatatenda mabaya. Na huko utajiri wao utakuwa mateka, na nyumba zao zitakuwa ukiwa; naam, watajenga nyumba, lakini hawatakaa ndani yake; nao watapanda mizabibu, lakini hawatakunywa divai yake.”—Sefania 1:12, 13.

      15. (a) Ni nini ambacho kingewapata makuhani waasi-imani wa Yerusalemu? (b) Ni nini kitakachowapata waabudu wa dini isiyo ya kweli leo?

      15 Makuhani waasi-imani wa Yerusalemu walikuwa wakichanganya ibada ya Yehova na dini isiyo ya kweli. Ingawa waliona wako salama, Mungu angewatafuta kwa taa ambazo zingeangaza katika giza la kiroho ambamo wamejificha. Hakuna yeyote ambaye angeponyoka kutangazwa na kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu. Waasi-imani hao wasiojali walikuwa wametulia kama sira ndani ya pipa la divai. Hawakutaka kusumbuliwa na tangazo lolote la kuingiliwa na Mungu katika shughuli za wanadamu, lakini hawangeponyoka hukumu ya Mungu dhidi yao. Pia, waabudu wa dini isiyo ya kweli leo, kutia ndani wafuasi wa Jumuiya ya Wakristo hali kadhalika wale ambao wameasi ibada ya Yehova, hawataponyoka. Wakikana kwamba hizi si “siku za mwisho,” wanasema moyoni mwao, “BWANA hatatenda mema, wala hatatenda mabaya.” Lakini wamekosea kama nini!—2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4, 10.

      16. Ni nini ambacho kingetukia wakati ambapo hukumu ya Mungu ingetekelezwa dhidi ya Yuda, na kujua hivyo kwapasa kutuathirije?

      16 Waasi-imani wa Yuda walionywa kwamba Wababiloni wangepora mali zao, wangefanya nyumba zao ukiwa, na kutwaa matunda ya mashamba yao ya mizabibu. Mali za kimwili hazingekuwa na thamani yoyote wakati ambapo hukumu ya Mungu ingetekelezwa dhidi ya Yuda. Ndivyo itakavyokuwa siku ya hukumu ya Yehova itakapoujia mfumo huu wa mambo. Kwa hiyo, na tuwe na mtazamo wa kiroho na ‘kuweka hazina mbinguni’ kwa kuendelea kutanguliza utumishi wa Yehova maishani mwetu!—Mathayo 6:19-21, 33.

      ‘Siku ya Yehova Iliyo Kuu I Karibu’

      17. Kulingana na Sefania 1:14-16, siku ya hukumu ya Yehova i karibu kadiri gani?

      17 Siku ya hukumu ya Yehova i karibu kadiri gani? Kulingana na Sefania 1:14-16, Mungu ahakikisha hivi: “Hiyo siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana; naam, sauti ya siku ya BWANA; shujaa hulia kwa uchungu mwingi huko! Siku ile ni siku ya ghadhabu, siku ya fadhaa na dhiki, siku ya uharibifu na ukiwa, siku ya giza na utusitusi, siku ya mawingu na giza kuu, siku ya tarumbeta na ya kamsa, juu ya miji yenye maboma, juu ya buruji zilizo ndefu sana.”

      18. Kwa nini hatupaswi kuamua kwamba siku ya hukumu ya Yehova i mbali sana?

      18 Makuhani, wakuu, na watu wa Yuda wenye dhambi walionywa kwamba ‘siku ya BWANA iliyo kuu ilikuwa karibu.’ ‘Siku ya Yehova ingefanya haraka sana’ kwa ajili ya Yuda. Hali kadhalika leo, mtu yeyote asidhani ya kwamba kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova dhidi ya waovu ku mbali sana. Badala yake, kama vile ambavyo Mungu alichukua hatua haraka huko Yuda, ndivyo ‘atakavyoharakisha’ siku yake ya kutekeleza hukumu. (Ufunuo 16:14, 16) Utakuwa wakati wenye uchungu kama nini kwa wote wanaopuuza maonyo ya Yehova yanayotolewa na Mashahidi wake na ambao hukataa ibada ya kweli!

      19, 20. (a) Ni baadhi ya mambo gani yaliyohusika katika kudhihirishwa kwa hasira ya kisasi ya Mungu dhidi ya Yuda na Yerusalemu? (b) Kwa kuzingatia uharibifu utakaowapata watu waovu wa mfumo huu wa mambo, ni maswali gani yanayozuka?

      19 Ilikuwa “siku ya fadhaa na dhiki” wakati Mungu alipodhihirisha ghadhabu yake dhidi ya Yuda na Yerusalemu. Wavamizi wa Babiloni walisababisha mateso mengi kwa wakazi wa Yuda, pamoja na maumivu makali ya akili, wakati walipokabili kifo na uharibifu. “Siku hiyo ya uharibifu na ukiwa” ilikuwa siku ya giza, mawingu, na utusitusi, huenda si katika njia ya ufananisho tu bali pia kihalisi kwa kuwa moshi na mauaji yalikuwa kila mahali. Ilikuwa “siku ya tarumbeta na ya kamsa,” lakini maonyo yalitolewa bure.

      20 Walinzi wa Yerusalemu walikuwa hoi wakati magogo ya Babiloni yalipovunja “buruji zilizo ndefu sana.” Ngome za mfumo huu mwovu wa mambo zitakuwa bure dhidi ya silaha za vita alizo nazo Mungu mbinguni, ambazo ziko tayari kutumiwa naye hivi karibuni anapoharibu watu waovu. Je, unatumaini kuhifadhiwa? Je, umechukua msimamo imara upande wa Yehova, ‘ambaye huwahifadhi wote wampendao, na kuwaangamiza wote wasio haki’?—Zaburi 145:20.

      21, 22. Andiko la Sefania 1:17, 18 litatimizwaje wakati wetu?

      21 Siku ya hukumu inayotabiriwa katika Sefania 1:17, 18, ni siku yenye kuogofya kama nini! “Nami nitawaletea wanadamu dhiki,” asema Yehova Mungu, “hata watakwenda kama vipofu, kwa sababu wamemtenda BWANA dhambi; na damu yao itamwagwa kama mavumbi, na nyama yao kama nami [“mavi,” Biblia Habari Njema]. Fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya BWANA; bali nchi yote pia itateketezwa kwa moto wa wivu wake; maana atawakomesha watu wote wakaao katika nchi hii, naam, ukomo wa kutisha.”

      22 Kama alivyofanya wakati wa Sefania, hivi karibuni Yehova atasononesha “watu wote wakaao katika nchi hii,” wale wanaokataa kutii onyo lake leo. Kwa sababu wanatenda dhambi dhidi ya Mungu, watakwenda wakipapasa-papasa kama vipofu, wasiweze kupata ukombozi. Katika siku ya hukumu ya Yehova, damu yao “itamwagwa kama mavumbi,” kama kitu kisichofaa. Mwisho wao utakuwa wenye kufedhehesha kwelikweli, kwa kuwa Mungu atatawanya miili pamoja na viungo vya ndani vya waovu hao juu ya dunia, “kama mavi.”

      23. Ingawa wakosaji hawataponyoka “katika siku ya hasira ya BWANA,” unabii wa Sefania watutolea tumaini gani?

      23 Hakuna awezaye kuwaokoa wale wanaopiga vita dhidi ya Mungu na watu wake. Fedha wala dhahabu hazikuwaokoa wakosaji wa Yuda, kama vile mali nyingi na hongo hazitalinda wala kuponyosha Jumuiya ya Wakristo na mfumo huu wa mambo katika ‘siku ya ghadhabu ya Yehova.’ Katika siku hiyo ya kukata maneno, ‘dunia yote itateketezwa’ kwa moto wa wivu wa Mungu akomeshapo waovu. Kwa kuwa tuna imani katika neno la Mungu la unabii, tuna hakika kwamba sasa tumo katika kipindi cha mwisho kabisa cha “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Siku ya hukumu ya Yehova i karibu, na hivi karibuni atalipiza kisasi dhidi ya maadui wake. Hata hivyo, unabii wa Sefania watoa tumaini la ukombozi. Hivyo basi, twatakiwa kufanya nini ili tufichwe katika siku ya hasira ya Yehova?

  • Mtafuteni Yehova Kabla ya Siku Yake ya Hasira
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Februari 15
    • Mtafuteni Yehova Kabla ya Siku Yake ya Hasira

      “Mtafuteni BWANA . . . itafuteni haki [“uadilifu,” “NW”], utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”—SEFANIA 2:3.

      1. Hali ya kiroho ya Yuda ilikuwaje wakati Sefania alipoanza kutoa unabii?

      SEFANIA alianza kutoa unabii wakati muhimu katika historia ya Yuda. Hali ya kiroho ya taifa hilo ilikuwa imefikia kiwango cha chini sana. Watu walikuwa wakitegemea uongozi wa makuhani wapagani na wanajimu, badala ya kumtumaini Yehova. Ibada ya Baali, pamoja na sherehe zake za ibada ya uzazi, ilikuwa imeenea sana nchini humo. Viongozi wa serikali—wakuu, wenye nguvu, na makadhi—walikuwa wakiwaonea watu ambao walipaswa kulinda. (Sefania 1:9; 3:3) Ndiyo sababu Yehova aliamua ‘kuunyosha mkono wake’ dhidi ya Yuda na Yerusalemu ili kuziharibu!—Sefania 1:4.

      2. Kulikuwa na tumaini gani kwa watumishi waaminifu wa Mungu nchini Yuda?

      2 Hata hivyo, ingawa hali ilikuwa mbaya, kulikuwa na tumaini japo kidogo. Yosia, mwana wa Amoni, sasa alikuwa akitawala. Ingawa alikuwa kivulana tu, Yosia alimpenda Yehova kikweli. Iwapo mfalme huyo mpya angerudisha ibada safi nchini Yuda, hilo lingekuwa jambo lenye kutia moyo kama nini kwa wale wachache waliokuwa wakimtumikia Mungu kwa uaminifu! Huenda hata wengine wangechochewa kujiunga nao na kuhifadhiwa pia katika siku ya hasira ya Yehova.

      Matakwa ya Kuhifadhiwa

      3, 4. Ni matakwa gani matatu ambayo lazima yatimizwe ili mtu ahifadhiwe katika “siku ya hasira ya BWANA”?

      3 Je, kwa kweli watu fulani wangeweza kuhifadhiwa katika siku ya hasira ya Yehova? Ndiyo, maadamu walitimiza matakwa matatu yaliyo kwenye Sefania 2:2, 3. Tusomapo mistari hiyo, acheni tuzingatie matakwa hayo. Sefania aliandika: “Kabla haijazaa hiyo amri, kabla haijapita siku ile kama makapi, kabla haijawajilia hasira kali ya BWANA, kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA. Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki [“uadilifu,” NW], utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”

      4 Basi, ili kuhifadhiwa, mtu alipaswa (1) kumtafuta Yehova, (2) kuutafuta uadilifu, na (3) kuutafuta unyenyekevu. Twapendezwa sana na matakwa hayo leo. Kwa nini? Kwa sababu kama vile Yuda na Yerusalemu zilivyohukumiwa katika karne ya saba K.W.K., ndivyo mataifa ya Jumuiya ya Wakristo na, kwa kweli, waovu wote wanavyoelekea kukabiliana na Yehova Mungu kwenye “dhiki kubwa” inayokuja. (Mathayo 24:21) Wowote ambao wangependa kufichwa wakati huo lazima wachukue hatua madhubuti sasa. Jinsi gani? Kwa kumtafuta Yehova, kuutafuta uadilifu, na kuutafuta unyenyekevu, kabla haijawa kuchelewa mno!

      5. Ni nini kinachomaanishwa na ‘kumtafuta Yehova’ leo?

      5 Huenda ukasema hivi: ‘Mimi ni mtumishi wa Mungu, nimejiweka wakfu na kubatizwa, nami ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nimeyatimiza matakwa hayo, sivyo?’ Kusema kweli, mengi zaidi yahusika kuliko kujiweka wakfu kwa Yehova. Israeli lilikuwa taifa wakfu, lakini katika siku za Sefania watu wa Yuda hawakuwa wakiishi kulingana na wakfu huo. Kwa sababu hiyo, taifa hilo lilikatiliwa mbali hatimaye. ‘Kumtafuta Yehova’ leo humaanisha kusitawisha na kudumisha uhusiano mchangamfu wa kibinafsi pamoja naye na kushirikiana na tengenezo lake la kidunia. Kwamaanisha kupata kujua jinsi Mungu anavyoona mambo na kutilia maanani hisia zake. Sisi humtafuta Yehova tunapojifunza kwa makini Neno lake, kulitafakari na kutumia ushauri wa Neno hilo maishani. Tutafutapo pia mwelekezo wa Yehova kupitia sala ya bidii na kufuata mwongozo wa roho yake takatifu, uhusiano wetu naye huzidi kukua nasi huchochewa tumtumikie ‘kwa moyo wetu wote, na kwa roho yetu yote, na kwa nguvu zetu zote.’—Kumbukumbu la Torati 6:5; Wagalatia 5:22-25; Wafilipi 4:6, 7; Ufunuo 4:11.

      6. ‘Tunautafutaje uadilifu,’ na kwa nini jambo hilo linawezekana hata katika ulimwengu huu?

      6 Takwa la pili linalotajwa kwenye Sefania 2:3 ni ‘kuutafuta uadilifu.’ Wengi wetu tulifanya mabadiliko makubwa ili tustahili ubatizo wa Kikristo, lakini ni lazima tuendelee kutegemeza kanuni za uadilifu za Mungu katika maisha yetu yote. Watu fulani walioanza kwa bidii wamejiruhusu wachafuliwe na ulimwengu. Ni kweli kwamba, si rahisi kuutafuta uadilifu kwa kuwa twazungukwa na watu wanaoona ukosefu wa adili katika ngono, kusema uwongo, na dhambi nyinginezo kuwa mambo ya kawaida. Lakini tamaa yenye nguvu ya kumpendeza Yehova yaweza kuushinda mwelekeo wowote wa kutafuta kibali cha ulimwengu kwa kujaribu kujipatanisha nao. Watu wa Yuda walipoteza kibali cha Mungu kwa kuwa walijaribu kuiga mataifa jirani zao ambao hawakumwogopa Mungu. Basi badala ya kuuiga ulimwengu, na tuwe “waigaji wa Mungu,” tukisitawisha “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.”—Waefeso 4:24; 5:1.

      7. ‘Tunautafutaje unyenyekevu’?

      7 Jambo la tatu linalotajwa kwenye Sefania 2:3 ni kwamba ikiwa twataka kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova, ni lazima ‘tuutafute unyenyekevu.’ Kila siku, sisi huchangamana na wanaume, wanawake, na vijana ambao si wanyenyekevu hata kidogo. Wanaona kwamba kuwa na tabia ya upole ni dosari. Unyenyekevu huonwa kuwa udhaifu mkubwa sana. Wao ni wenye kudai mambo mno, wenye ubinafsi, wenye kushikilia kauli yao, na kuamini kwamba mambo wanayoyaona kuwa “haki” yao na mapendezi yao yapasa kukubaliwa na watu wote hata hali iweje. Lingekuwa jambo lenye kusikitisha kama nini iwapo tungelianza kuwa na maoni kama hayo! Huu ndio wakati wa ‘kuutafuta unyenyekevu.’ Jinsi gani? Kwa kujitiisha chini ya Mungu, kwa kukubali kwa unyenyekevu nidhamu yake na kutenda kupatana na mapenzi yake.

      Kwa Nini “Huenda” Tukafichwa?

      8. Ni nini kinachoonyeshwa na matumizi ya neno “huenda” kwenye Sefania 2:3?

      8 Ona kwamba andiko la Sefania 2:3 lasema: “Huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.” Kwa nini Sefania alitumia neno “huenda” alipokuwa akiongea na “wanyenyekevu wa dunia?” Wanyenyekevu hao walikuwa wamechukua hatua zinazofaa, lakini hawakupaswa kujitumainia. Hawakuwa wamefikia mwisho wa maisha yao wakiwa waaminifu. Baadhi yao wangaliweza kufanya dhambi. Inaweza kuwa hivyo kwetu. Yesu alisema: “Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Naam, wokovu katika siku ya hasira ya Yehova wategemea kuendelea kwetu kufanya yaliyo sawa machoni pake. Je, umeazimia kwa dhati kuendelea kufanya yaliyo sawa?

      9. Mfalme Yosia kijana alichukua hatua gani za unyofu?

      9 Yaonekana kwa kuitikia maneno ya Sefania, Mfalme Yosia alichochewa ‘kumtafuta BWANA.’ Maandiko yanasema: “Katika mwaka wa nane wa kutawala kwake, naye [Yosia] akali mchanga [akiwa na umri wa miaka 16 hivi], alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babaye.” (2 Mambo ya Nyakati 34:3) Yosia pia aliendelea ‘kutafuta uadilifu,’ kwa kuwa twasoma hivi: “Katika mwaka wa kumi na mbili [Yosia alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi] akaanza kusafisha Yuda na Yerusalemu kwa kuondoa mahali pa juu, na kwa kuondoa maashera, na sanamu za kuchora, nazo za kusubu. Wakazibomoa madhabahu za mabaali machoni pake.” (2 Mambo ya Nyakati 34:3, 4) Yosia ‘alitafuta unyenyekevu’ pia, kwa kuchukua hatua ya unyenyekevu ya kuitakasa nchi kwa kuondoa ibada ya sanamu na mazoea mengine ya dini isiyo ya kweli kusudi ampendeze Yehova. Ni lazima wanyenyekevu wengine wawe walishangilia kama nini walipoona jinsi alivyotenda!

      10. Ni nini kilichotukia Yuda mwaka wa 607 K.W.K., lakini ni nani waliohifadhiwa?

      10 Wayahudi wengi walimrudia Yehova wakati wa utawala wa Yosia. Hata hivyo, baada ya mfalme huyo kufa, wengi walirudia njia zao za kale—mazoea yasiyokubalika kwa Mungu hata kidogo. Kama vile Yehova alivyokuwa ameagiza, Wababiloni walishinda Yuda na kuharibu jiji lake kuu, Yerusalemu, mwaka wa 607 K.W.K. Hata hivyo, kuna waliosalia. Nabii Yeremia, Ebed-meleki Mwethiopia, wazao wa nyumba ya Yonadabu, na wengine waliokuwa waaminifu kwa Mungu walifichwa katika siku hiyo ya hasira ya Yehova.—Yeremia 35:18, 19; 39:11, 12, 15-18.

      Maadui wa Mungu—Tahadharini!

      11. Kwa nini si rahisi kudumu ukiwa mwaminifu kwa Mungu leo, lakini maadui wa watu wa Yehova wapaswa kuzingatia nini?

      11 Tungojeapo siku ya hasira ya Yehova dhidi ya mfumo huu mwovu, ‘tunakutana na majaribu ya namna mbalimbali.’ (Yakobo 1:2) Katika nchi kadhaa ambazo hudai kuthamini uhuru wa ibada, makasisi wenye hila wametumia uwezo wao katika mamlaka za kilimwengu ili kutokeza mnyanyaso mkali dhidi ya watu wa Mungu. Watu wasio na maadili wamewachongea Mashahidi wa Yehova, kwa kuwaita “madhehebu hatari.” Mungu anajua matendo yao naye hana budi kuwaadhibu. Maadui wa Mungu wapaswa kufikiria kilichowapata maadui wa watu wake nyakati za kale kama vile Wafilisti. Unabii wasema hivi: “Gaza utaachwa, na Ashkeloni utakuwa ukiwa; wataufukuzia mbali Ashdodi wakati wa adhuhuri, na Ekroni utang’olewa.” Majiji ya Wafilisti ya Gaza, Ashkeloni, Ashdodi, na Ekroni yangeharibiwa.—Sefania 2:4-7.

      12. Ni nini kilichopata Ufilisti, Moabu, na Amoni?

      12 Unabii huo waendelea kusema: “Mimi nimeyasikia matukano ya Moabu, na dhihaka za wana wa Amoni, ambazo kwa hizo wamewatukana watu wangu, na kujitukuza juu ya mpaka wao.” (Sefania 2:8) Ni kweli kwamba Misri na Ethiopia waliteseka mikononi mwa wavamizi Wababiloni. Lakini Mungu angehukumuje Moabu na Amoni, mataifa ambayo ni uzao wa Loti, mpwa wa Abrahamu? Yehova alitabiri hivi: “Hakika Moabu atakuwa kama Sodoma, na wana wa Amoni kama Gomora.” Tofauti na wazazi wao wa kale—wale binti wawili wa Loti, waliosalimika kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora—Moabu na Amoni yenye majivuno hawangefichwa wasipatwe na hukumu za Mungu. (Sefania 2:9-12; Mwanzo 19:16, 23-26, 36-38) Taifa la Ufilisti pamoja na majiji yake, liko wapi leo? Namna gani Moabu na Amoni ambayo wakati mmoja yalikuwa na majivuno? Hata ukiyatafuta namna gani, hutayapata.

      13. Ni uvumbuzi gani wa kiakiolojia uliofanywa Ninawi?

      13 Katika siku ya Sefania, Milki ya Ashuru ilikuwa imefikia kilele cha nguvu zake. Akifafanua sehemu moja ya jumba la mfalme ambalo alikuwa amechimbua katika Ninawi, jiji kuu la Ashuru, Mwakiolojia Austen Layard, aliandika hivi: “Paa . . . ziligawanywa na kuwa visehemu mraba, vilivyochorwa maua, au wanyama. Baadhi yake vilipambwa kwa pembe za ndovu, kila kisehemu kikiwa na mipaka na nakshi sanifu. Mihimili, hali kadhalika sehemu ya kandokando ya vyumba, ilifanywa ionekane kana kwamba ni dhahabu na fedha, au huenda hata ilifunikwa kwa dhahabu na fedha; nazo mbao adimu sana, hasa mbao za mwerezi, zilitumiwa.” Hata hivyo, kama ilivyotabiriwa katika unabii wa Sefania, Ashuru ingeharibiwa nalo jiji lake, Ninawi, lingekuwa “ukiwa.”—Sefania 2:13.

      14. Unabii wa Sefania ulitimizwaje juu ya Ninawi?

      14 Miaka 15 tu baada ya Sefania kutoa unabii huo, Ninawi lenye nguvu liliharibiwa, na jumba la mfalme lililokuwa tukufu likafanywa kuwa vifusi. Naam, jiji hilo lenye majivuno liliharibiwa kabisa. Kiwango cha uharibifu kilitabiriwa waziwazi katika maneno haya: “Mwari-nyuni na nungu watakaa juu ya vichwa vya nguzo zake [zilizoanguka]; sauti yao itasikiwa madirishani; vizingitini mwake mtakuwa ukiwa.” (Sefania 2:14, 15) Majengo ya fahari ya Ninawi yangefaa kukaliwa tu na nungu na mwari-nyuni. Makelele ya wafanya biashara hayangesikiwa tena barabarani, wala vilio vya wapiganaji, wala nyimbo za makuhani. Na kwenye barabara zilizokuwa na watu wengi wakati mmoja, kungesikiwa tu sauti ikiimba kwa woga dirishani, huenda ni sauti ya wimbo wa huzuni wa ndege au mvumo wa upepo. Adui wote wa Mungu na wakome vivyo hivyo!

      15. Tunaweza kujifunza nini kutokana na yaliyopata Ufilisti, Moabu, Amoni, na Ashuru?

      15 Tunaweza kujifunza nini kutokana na yaliyopata Ufilisti, Moabu, Amoni, na Ashuru? Kwamba: Tukiwa watumishi wa Yehova hatuna haja ya kuwaogopa maadui wetu. Mungu huona yale yanayofanywa na wale wanaopinga watu wake. Yehova aliwachukulia hatua maadui wake zamani, na hukumu zake zitatekelezwa dhidi ya dunia yote inayokaliwa leo. Lakini kutakuwako waokokaji—‘umati mkubwa kutoka katika mataifa yote.’ (Ufunuo 7:9) Unaweza kuwa miongoni mwao—iwapo tu utaendelea kumtafuta Yehova, kuutafuta uadilifu, na kuutafuta unyenyekevu.

      Ole kwa Wakosaji Wenye Ufidhuli!

      16. Unabii wa Sefania ulisema nini kuhusu wakuu na viongozi wa kidini wa Yuda, na kwa nini maneno hayo yanafafanua vizuri Jumuiya ya Wakristo?

      16 Unabii wa Sefania waelekezwa kwa Yuda na Yerusalemu tena. Andiko la Sefania 3:1, 2 lasema: “Ole wake yeye aliyeasi na kutiwa unajisi, mji wa udhalimu! Hakuitii sauti; hakukubali kurudiwa; hakumwamini BWANA; hakumkaribia Mungu wake.” Yasikitisha kama nini kwamba jitihada za Yehova za kuwatia nidhamu watu wake hazikusikiwa kamwe! Ukatili wa wakuu, wenye nguvu, na makadhi, ulikuwa mbaya kwelikweli! Sefania alaumu ukosefu wa aibu wa viongozi wa kidini, akisema: “Manabii wake ni watu hafifu [“fidhuli,” NW], wadanganyifu; makuhani wake wamepatia unajisi patakatifu, wameifanyia sheria udhalimu.” (Sefania 3:3, 4) Maneno hayo yafafanua vizuri kama nini hali ya manabii na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo leo! Kwa ufidhuli, wameliondoa jina la Mungu kutoka katika tafsiri zao za Biblia na wamefundisha mafundisho yenye kupotosha juu ya Yule wanayedai kumwabudu.

      17. Kwa nini tuendelee kutangaza habari njema hata watu wasikilize au wasisikilize?

      17 Kwa kuwajali watu wake wa kale Yehova aliwaonya juu ya hatua ambayo angechukua. Aliwatuma watumishi wake manabii—Sefania na Yeremia, na wengine—wawasihi sana watu hao watubu. Naam, “BWANA . . . hatatenda uovu; kila asubuhi hudhihirisha hukumu yake, wala hakomi.” Waliitikiaje? “Bali mtu asiye haki hajui kuona haya,” akasema Sefania. (Sefania 3:5) Onyo kama hilo latolewa leo. Ikiwa wewe ni mhubiri wa habari njema, unashiriki kutoa onyo hilo. Endelea kutangaza habari njema bila kukoma! Watu wasikilize au wasisikilize, Mungu anaona kwamba huduma yako inafanikiwa maadamu unaendelea kuitekeleza kwa uaminifu; huhitaji kuaibika unapofanya kazi ya Mungu kwa bidii.

      18. Andiko la Sefania 3:6 litatimizwaje?

      18 Kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu kutahusisha mengi zaidi ya kufanywa ukiwa kwa Jumuiya ya Wakristo. Yehova ashutumu mataifa yote: “Nimekatilia mbali mataifa, buruji zao zina ukiwa; nimeziharibu njia kuu zao, hata hapana mmoja apitaye; miji yao imeangamizwa.” (Sefania 3:6) Maneno hayo ni yenye kutumainika hivi kwamba Yehova azungumza juu ya uharibifu huo kana kwamba tayari umetimia. Ni nini kilichoyapata majiji ya Ufilisti, Moabu, na Amoni? Namna gani Ninawi, jiji kuu la Ashuru? Kuharibiwa kwa majiji hayo kwapaswa kuwa onyo kwa mataifa ya leo. Mungu si wa kudhihakiwa.

      Endelea Kumtafuta Yehova

      19. Ni maswali gani yenye kuamsha fikira ambayo huenda tukauliza?

      19 Wakati wa Sefania, hasira ya Mungu iliwapata wale ‘walioharibu matendo yao yote’ kwa uovu. (Sefania 3:7) Jambo hilohilo litatukia wakati wetu. Je, unaona uthibitisho kwamba siku ya Yehova i karibu? Je, unaendelea ‘kumtafuta Yehova’ kwa kusoma Neno lake kwa ukawaida—kila siku? Je, ‘unautafuta uadilifu’ kwa kuishi maisha safi kiadili kupatana na viwango vya Mungu? Na je, ‘unautafuta unyenyekevu’ kwa kujinyenyekeza na kuwa mtiifu kwa Mungu na mipango yake ya wokovu?

      20. Tutachunguza maswali gani katika makala ya mwisho ya mfululizo huu wa unabii wa Sefania?

      20 Tukiendelea kumtafuta Yehova, kuutafuta uadilifu, na kuutafuta unyenyekevu, tunaweza kutazamia kupata baraka nyingi sasa—naam, hata katika ‘siku hizi za mwisho’ zenye kujaribu imani. (2 Timotheo 3:1-5; Mithali 10:22) Lakini huenda tukauliza, ‘Tukiwa watumishi wa Yehova wa siku hizi tunabarikiwa kwa njia zipi, na ni baraka gani za wakati ujao ambazo unabii wa Sefania unaahidi wale watakaofichwa katika siku ya hasira ya Yehova inayokuja kwa kasi sana?’

  • Watu wa Yehova Waliorudishwa Wamsifu Duniani Pote
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Februari 15
    • Watu wa Yehova Waliorudishwa Wamsifu Duniani Pote

      ‘Nitawapa mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la Yehova.’—SEFANIA 3:9.

      1. Kwa nini ujumbe mbalimbali wa maangamizi ulitimizwa dhidi ya Yuda na mataifa mengine?

      YEHOVA alimpulizia Sefania atoe ujumbe mbalimbali wa hukumu na wenye nguvu kama nini! Ujumbe huo wa maangamizi ulitimizwa dhidi ya Yuda na jiji lake kuu, Yerusalemu, kwa sababu viongozi na watu kwa ujumla hawakuwa wakifanya mapenzi ya Yehova. Mataifa jirani pia, kama vile Ufilisti, Moabu, na Amoni, yangepatwa na hasira ya kisasi ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu yamewapinga watu wa Yehova kwa ukatili kwa karne nyingi. Serikali ya ulimwengu ya Ashuru ingeharibiwa kwa sababu hiyohiyo, isiweze kusimama tena.

      2. Yaonekana andiko la Sefania 3:8 lawahusu nani?

      2 Hata hivyo, kulikuwa na watu fulani wenye mwelekeo mzuri katika Yuda ya kale. Walitazamia kwa hamu kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu dhidi ya waovu na yaonekana kwamba maneno haya yanawahusu: “Ningojeni, asema BWANA, hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.”—Sefania 3:8.

      “Lugha Iliyo Safi” kwa Ajili ya Nani?

      3. Sefania alipuliziwa kutoa ujumbe gani wa tumaini?

      3 Naam, Sefania alitangaza ujumbe mbalimbali wa maangamizi wa Yehova. Lakini nabii huyo alipuliziwa pia kuandika ujumbe mzuri ajabu wa tumaini—ujumbe ambao ungewafariji sana watu ambao wangedumu wakiwa waaminifu kwa Yehova. Kwenye Sefania 3:9, Yehova Mungu alitangaza hivi: “Ndipo nitakapowarudishia [“nitakapowapa,” NW] mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la BWANA, wamtumikie kwa nia moja.”

      4, 5. (a) Ni nini ambacho kingewapata watu wasio waadilifu? (b) Ni nani ambao wangenufaika na jambo hilo, na kwa nini?

      4 Kungekuwa na watu ambao hawangepewa lugha safi. Unabii huo unawataja, ukisema hivi: “Nitawaondoa watu wako wanaotakabari na kujivuna, wasiwe kati yako.” (Sefania 3:11) Kwa hiyo wenye kujivuna, waliodharau sheria za Mungu na ambao walitenda mambo yasiyo ya uadilifu, wangeondolewa. Na ni nani wangenufaishwa na jambo hilo? Andiko la Sefania 3:12, 13 lasema: “Lakini [mimi Yehova] nitasaza ndani yako watu walioonewa na maskini, nao watalitumainia jina la BWANA. Mabaki ya Israeli hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya.”

      5 Mabaki waaminifu wa Israeli la kale ndio wangenufaika. Kwa nini? Kwa sababu walitenda kupatana na maneno haya: “Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”—Sefania 2:3.

      6. Ni nini kilichotukia wakati wa utimizo wa kwanza wa unabii wa Sefania?

      6 Katika utimizo wa kwanza wa unabii wa Sefania, Mungu aliadhibu Yuda isiyo na imani kwa kuruhusu Serikali ya Ulimwengu ya Babiloni kuishinda na kuteka watu wake mwaka wa 607 K.W.K. Baadhi ya watu, kutia ndani nabii Yeremia, walihifadhiwa na wengine waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova wakiwa mateka. Mnamo mwaka wa 539 K.W.K., milki ya Babiloni ilipinduliwa na Wamedi na Waajemi wakiwa chini ya Mfalme Koreshi. Miaka miwili hivi baadaye, Koreshi alitoa amri iliyowawezesha mabaki Wayahudi warudi nyumbani kwao. Baadaye, hekalu la Yerusalemu likajengwa upya, nao makuhani wakapata uwezo tena wa kuwafundisha watu Sheria. (Malaki 2:7) Kwa hiyo Yehova aliwafanikisha mabaki waliorudishwa—maadamu walidumu wakiwa waaminifu.

      7, 8. Maneno ya unabii wa Sefania 3:14-17 yaliwahusu nani, na kwa nini wajibu hivyo?

      7 Sefania alitabiri hivi juu ya watu ambao wangefurahia kurudishwa huko: “Imba, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee Israeli; furahi na kushangilia kwa moyo wako wote, Ee binti Yerusalemu. BWANA ameziondoa hukumu zako, amemtupa nje adui yako; mfalme wa Israeli, naam, yeye BWANA, yu katikati yako; hutaogopa uovu tena. Katika siku ile Yerusalemu utaambiwa, usiogope, Ee Sayuni; mikono yako isilegee. BWANA, Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; atakushangilia kwa furaha kuu, atakutuliza katika upendo wake, atakufurahia kwa kuimba.”—Sefania 3:14-17.

      8 Maneno hayo ya unabii yaliwahusu mabaki waliokusanywa kutoka utekwa wa Babiloni na kurudishwa nchi ya babu zao. Jambo hilo ladhihirishwa kwenye andiko la Sefania 3:18-20, ambapo twasoma: “[Mimi Yehova] nitawakusanya wanaousikitikia mkutano wa ibada, hao waliokuwa wa kwako; ambao mzigo uliokuwa juu yake ulikuwa fedheha kwao. Tazama, wakati huo nitawapatiliza watu wote wanaokutesa; nami nitamponya yeye achechemeaye, nami nitamkusanya yeye aliyefukuzwa; nami nitawafanya kuwa sifa na jina, hao ambao fedheha yao ilikuwa katika dunia yote. Wakati huo nitawaingizeni, na wakati huo nitawakusanya; kwa maana nitawafanya ninyi kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia, nitakapowarudisha wafungwa wenu mbele ya macho yenu, asema BWANA.”

      9. Yehova alijileteaje sifa kuhusiana na Yuda?

      9 Hebu wazia jinsi mataifa jirani waliokuwa adui za watu wa Mungu walivyoshtuka! Wakazi wa Yuda walikuwa wametekwa na Babiloni yenye nguvu, pasipo tumaini lolote la kuachiliwa huru. Isitoshe, nchi yao ilikuwa ukiwa. Lakini, Mungu alitumia nguvu zake kuwarudisha nyumbani kwao baada ya miaka 70, nayo mataifa adui yalikuwa yakikaribia kuangamizwa. Yehova alijiletea sifa iliyoje kwa kuwarudisha mabaki hao waaminifu! Aliwafanya “kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia.” Kurudishwa huko kulileta sifa iliyoje kwa Yehova na kwa wale wanaoitwa kwa jina lake!

      Ibada ya Yehova Yakwezwa

      10, 11. Unabii wa Sefania wa kurudishwa ungetimizwa lini kwa njia kubwa, nasi twajuaje hilo?

      10 Kurudishwa kwingine kulitukia katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida, wakati ambapo Yesu Kristo alikusanya mabaki ya Israeli waingie katika ibada ya kweli. Kurudishwa huko kuliashiria mambo ambayo bado yangekuja, kwa kuwa utimizo mkubwa zaidi wa kurudishwa ungetukia wakati ujao. Unabii wa Mika ulitabiri hivi: “Lakini itakuwa katika siku za mwisho, ya kwamba mlima wa nyumba ya BWANA [“Yehova,” NW] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na watu wa mataifa watauendea makundi makundi.”—Mika 4:1.

      11 Hilo lingetukia lini? Kama unabii ulivyosema, jambo hilo lingetukia katika “siku za mwisho”—naam wakati wa ‘siku hizi za mwisho.’ (2 Timotheo 3:1) Hilo lingetukia kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo wakati ambapo mataifa bado yangekuwa yakiabudu miungu isiyo ya kweli. Andiko la Mika 4:5 lasema hivi: “Mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake.” Na vipi waabudu wa kweli? Unabii wa Mika wajibu: “Na sisi tutakwenda kwa jina la BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wetu, milele na milele.”

      12. Ibada ya kweli imekwezwaje katika siku hizi za mwisho?

      12 Kwa hiyo, katika siku hizi za mwisho, “mlima wa nyumba ya Yehova u[me]wekwa imara juu ya vilima.” Ibada ya kweli ya Yehova iliyoinuka sana imerudishwa, ikafanywa imara, na kukwezwa juu ya aina nyingine zote za dini. Kama unabii wa Mika ulivyotabiri tena, “watu wa mataifa watauendea makundi makundi.” Na wale wanaofuata dini ya kweli ‘watakwenda kwa jina la Yehova, Mungu [wao], milele na milele.’

      13, 14. “Siku za mwisho” za ulimwengu huu zilianza lini, na tangu wakati huo ni nini ambacho kimekuwa kikiendelea kuhusiana na ibada ya kweli?

      13 Matukio yanayotimiza unabii wa Biblia yathibitisha kwamba “siku za mwisho” za ulimwengu huu zilianza mwaka wa 1914. (Marko 13:4-10) Historia yaonyesha kwamba Yehova alianza kukusanya tena mabaki waaminifu wa watiwa-mafuta waliokuwa na tumaini la kimbingu, waingie katika ibada ya kweli. Halafu, “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha”—watu walio na tumaini la kuishi milele duniani umekuwa ukikusanywa.—Ufunuo 7:9.

      14 Tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hadi leo, ibada ya Yehova inayotolewa na wale wanaoitwa kwa jina lake, imesonga mbele sana chini ya mwelekezo wake. Tangu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hadi sasa, idadi ya waabudu wa Yehova imeongezeka tokea maelfu machache ya watu na kufikia karibu watu milioni sita, wanaokusanywa katika makutaniko yapatayo 91,000 katika nchi 235. Kila mwaka, watangazaji hawa wa Ufalme hutumia muda wa zaidi ya saa bilioni moja wakimsifu Mungu hadharani. Ni wazi kwamba Mashahidi hao wa Yehova ndio wanaotimiza maneno ya Yesu ya unabii: “Na habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

      15. Andiko la Sefania 2:3 linatimizwaje leo?

      15 Andiko la Sefania 3:17 lasema: “BWANA, Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa.” Ufanisi wa kiroho ambao watu wa Yehova wanafurahia katika siku hizi za mwisho unatokana moja kwa moja na kuwa naye ‘katikati yao’ akiwa Mungu wao mwenye nguvu zote. Kama ilivyokuwa wakati watu wa Yuda ya kale waliporudishwa nyumbani kwao mwaka wa 537 K.W.K., ndivyo ilivyo leo. Hivyo tunaweza kuona jinsi andiko la Sefania 3:17 linavyotimizwa kwa njia kubwa wakati wetu linaposema: ‘Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia.’ Mwaka wa 537 K.W.K., neno “nyote” lilirejezea mabaki ya Wayahudi waliorudi kutoka utekwa wa Babiloni. Leo neno hilo larejezea wanyenyekevu wa mataifa yote duniani pote, wale ambao huitikia vizuri kuhubiriwa kwa Ufalme ulimwenguni pote na ambao huuendea ‘mlima wa nyumba ya Yehova makundi makundi.’

      Ibada ya Kweli Yasitawi

      16. Yaelekea maadui wetu wanahisije kuhusiana na ufanisi wa watumishi wa Yehova siku hizi?

      16 Baada ya mwaka wa 537 K.W.K., watu wengi katika mataifa jirani walishangazwa na kurudishwa kwa watumishi wa Mungu katika ibada ya kweli nyumbani kwao. Hata hivyo, kurudishwa huko kulikuwa kwa kiwango kidogo tu. Je, waweza kuwazia jambo ambalo watu fulani—hata adui za watu wa Mungu—wanasema sasa waonapo ukuzi, ufanisi, na maendeleo ya ajabu ya watumishi wa Yehova leo? Yaelekea sana kwamba baadhi ya maadui hao huhisi kama vile Mafarisayo walivyohisi walipoona jinsi watu walivyokusanyika alipokuwa Yesu. Walisema hivi kwa mshangao: “Oneni! Ulimwengu umemfuata.”—Yohana 12:19.

      17. Mwandishi mmoja alisema nini kuhusu Mashahidi wa Yehova, nao wameona ukuzi gani?

      17 Katika kitabu chake These Also Believe, Profesa Charles S. Braden alisema hivi: ‘Mashahidi wa Yehova wametoa ushahidi karibu duniani pote. Yaweza kusemwa kikweli kwamba hakuna dini nyingine ulimwenguni ambayo imeonyesha bidii na kudumu katika kujaribu kueneza habari njema ya Ufalme kuliko Mashahidi wa Yehova. Yaonekana dini hiyo itazidi kuwa na nguvu.’ Hakukosea hata kidogo! Alipoandika maneno hayo miaka 50 iliyopita, kulikuwako Mashahidi 300,000 hivi waliokuwa wakihubiri ulimwenguni. Angesema nini leo, wakati ambapo idadi ya wanaohubiri habari njema imeongezeka karibu mara 20—kufikia milioni sita hivi?

      18. Lugha safi ni nini, naye Mungu amewapa nani lugha hiyo?

      18 Kupitia nabii wake, Mungu aliahidi: ‘Nitawapa mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la Yehova, wamtumikie kwa nia moja.’ (Sefania 3:9) Katika siku hizi za mwisho, Mashahidi wa Yehova ndio wanaoliitia jina la Yehova, ndio wanaomtumikia kwa umoja katika kifungo kisichoweza kuvunjika cha upendo—naam, ndio wanaomtumikia “kwa nia moja.” Hao ndio watu ambao Yehova amewapa lugha safi. Lugha hiyo safi hutia ndani kumwelewa kikweli Mungu na makusudi yake. Yehova tu ndiye humpa mtu uelewevu huo kupitia roho yake takatifu. (1 Wakorintho 2:10) Yehova amewapa nani roho yake? ‘Wale tu wanaomtii yeye akiwa mtawala.’ (Matendo 5:32) Mashahidi wa Yehova peke yao ndio wana nia ya kumtii Mungu akiwa Mtawala wa vitu vyote. Ndiyo sababu wao hupokea roho takatifu ya Mungu na kuzungumza lugha safi, ile kweli juu ya Yehova na makusudi yake ya ajabu. Wao hutumia lugha hiyo safi ili kumsifu Yehova ulimwenguni pote kwa kiwango kikubwa kinachozidi kuongezeka.

      19. Kuzungumza lugha safi humaanisha nini?

      19 Kuizungumza lugha safi kwamaanisha kuamini kweli na kuifundisha wengine na pia kupatanisha mwenendo wako na sheria na kanuni za Mungu. Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa mstari wa mbele katika kumtafuta Yehova na kuinena lugha safi. Hebu wazia mambo ambayo yametimizwa! Ingawa idadi ya watiwa-mafuta haifiki 8,700, karibu watu wengine milioni sita, wenye tumaini la kidunia, wanaiga imani yao kwa kumtafuta Yehova na kusema lugha safi. Hao ndio umati mkubwa unaozidi kuongezeka kutoka katika mataifa yote ambao hudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu na kutoa utumishi mtakatifu katika ua wa kidunia wa hekalu la kiroho la Mungu, nao wataokoka “dhiki kubwa” ambayo hivi punde itaupata ulimwengu huu usio na uadilifu.—Ufunuo 7:9, 14, 15.

      20. Watiwa-mafuta waaminifu na wale wa umati mkubwa wanatazamia mambo gani?

      20 Umati mkubwa utaingizwa katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Yesu Kristo na wale watiwa-mafuta 144,000, ambao wanafufuliwa kuishi mbinguni ili watumikie wakiwa wafalme na makuhani pamoja naye, ndio watawala wapya wa dunia. (Waroma 8:16, 17; Ufunuo 7:4; 20:6) Waokokaji wa dhiki kubwa watafanya kazi ya kuifanya dunia iwe paradiso na wataendelea kuzungumza lugha safi waliyopewa na Mungu. Kimsingi, maneno haya yanawahusu: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi. Utathibitika katika haki.”—Isaya 54:13, 14.

      Kazi Kubwa Zaidi ya Kufundisha Katika Historia

      21, 22. (a) Kama ionyeshwavyo na andiko la Matendo 24:15, ni nani watakaohitaji kufundishwa lugha safi? (b) Ni kazi gani ya kufundisha isiyo na kifani ambayo itafanywa duniani chini ya utawala wa Ufalme?

      21 Kikundi kikubwa sana cha watu ambao watapewa fursa ya kujifunza lugha safi katika ulimwengu mpya ni wale wanaotajwa kwenye andiko la Matendo 24:15, lisemalo: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Wakati uliopita, mabilioni ya watu wameishi na kufa kabla ya kupata ujuzi sahihi juu ya Yehova. Atawafufua kwa utaratibu fulani. Nao waliofufuliwa watahitaji kufundishwa ile lugha safi.

      22 Litakuwa pendeleo lililoje kushiriki katika kazi hiyo kubwa ya kufundisha! Hiyo ndiyo itakayokuwa kazi kubwa zaidi ya kufundisha katika historia ya wanadamu. Yote itatimizwa chini ya utawala mwema wa Kristo Yesu akiwa na mamlaka ya Ufalme. Hatimaye wanadamu wataona utimizo wa andiko la Isaya 11:9, lisemalo hivi: “Dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”

      23. Kwa nini unaweza kusema kwamba sisi tuna pendeleo kubwa sana tukiwa watu wa Yehova?

      23 Tuna pendeleo lililoje siku hizi za mwisho la kufanya matayarisho kwa ajili ya wakati huo mzuri ajabu ambapo kwa kweli ujuzi juu ya Yehova utaijaza dunia! Na tuna pendeleo lililoje sasa hivi la kuwa watu wa Mungu ambao wanaona utimizo wa maneno ya unabii yaliyo kwenye Sefania 3:20! Hapo twaona uhakikisho wa Yehova: “Nitawafanya ninyi kuwa sifa na jina, miongoni mwa watu wote wa dunia.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki