-
Je, Kuunganisha Ulimwengu Kutatatua Matatizo Yetu Kweli?Amkeni!—2002 | Mei 22
-
-
Je, Kuunganisha Ulimwengu Kutatatua Matatizo Yetu Kweli?
‘Ulimwengu wetu ulio kama mtaa, una matatizo chungu nzima. Wakazi wake wengine hutendewa vibaya; wengine hawapati njia za kufanikiwa maishani. Mamilioni ya watu hawapati mahitaji yao hivi kwamba hawawezi kuamini kuwa wao ni sehemu ya jamii fulani.’—“OUR GLOBAL NEIGHBOURHOOD.”
FATIMA, anayeishi katika jiji moja kubwa la Afrika, anajiona kwamba amebarikiwa. Angalau ana friji. Lakini familia yake huishi katika banda la mabati lililo karibu na makaburi matatu yaliyotengenezwa kwa marumaru. Sawa na wakazi wengine nusu milioni, yeye huishi katika eneo kubwa la makaburi. Na hata eneo hilo la makaburi linaendelea kujaa. Fatima anasema hivi: “Watu wengi sana wanahamia katika eneo hili, hasa huku kwenye makaburi.”
Kilometa 15 hivi kutoka kwenye nyumba ya Fatima, kuna nyumba mpya za anasa zilizo na mikahawa ya fahari na uwanja mkubwa wa kuchezea gofu. Bei ya kucheza gofu mara moja inazidi mshahara wa wastani kwa kila mtu mmoja katika nchi hiyo ya Afrika. Jiji hilo limekumbwa na umaskini sikuzote, lakini viwanja vya gofu—ambavyo hutumiwa na watu wa hali ya juu—vinaanza kutokea na vinawaudhi watu. Kuna ufanisi na umaskini ulimwenguni na mambo hayo hayapatani.
Bonde la Hadhramaut ni njia ambayo ilitumiwa na wasafiri hapo kale na ina majiji ya kale hapa na pale. Bonde hilo hupita kwenye ardhi kame ya Yemeni katika Mashariki ya Kati. Mtu asipotazama eneo hilo kwa makini atafikiri kwamba hakuna mabadiliko ambayo yamefanywa huko. Lakini hiyo si kweli. Katika jiji la Saywūn lililoko karibu, jumba la makumbusho limemwomba msichana mmoja aliyehitimu chuo kikuu kutayarisha habari kwenye kompyuta zinazoorodhesha vitu vyote vyenye thamani katika jumba hilo. Ijapokuwa msichana huyo alizaliwa katika eneo hilo, alisomea huko Ohio, Marekani. Siku hizi, watu wanaweza kusafiri kokote ulimwenguni na kujifunza mambo kuliko hapo zamani.
Maelfu ya kilometa upande wa magharibi, katika jangwa la Sahara, malori matatu yanasonga polepole kwenye barabara katika eneo lililojitenga huku yakielekea kusini. Dereva mmoja, anayeitwa Mashala, anasema kwamba anasafirisha televisheni, vifaa vya kurekodi video, na vifaa vya kupokea ishara za televisheni kutoka kwenye setilaiti. Yeye hufahamu matukio ya karibuni ya ulimwengu kwa kutazama vituo vya habari vya Marekani. Anasema kwamba katika mji wa kwao “kila mtu ana vifaa vya kupokea ishara za televisheni kutoka kwenye setilaiti.” Ni sehemu chache tu duniani ambazo haziwezi kupokea habari za ulimwengu.
Kuenea daima kwa watu, mawazo, habari, fedha, na tekinolojia kotekote ulimwenguni, kumetokeza jamii mpya ya ulimwenguni pote ambayo inaweza kuleta faida. Utandaridhi unawasaidia watu kusambaza utamaduni wa kienyeji huko Yemeni na unamsaidia Mashala kuchuma dola 3,000 za Marekani kila anapoenda safari ya majuma matatu. Lakini sio watu wote wanaopata fedha nyingi. Fatima na majirani zake huwaona watu wachache wakifurahia faida za utandaridhi, huku wakibaki katika umaskini.
Ijapokuwa ulimwengu wetu haujawa mahali pazuri, yaelekea kwamba matokeo ya utandaridhi hayawezi kufutika. Je, watu wanaweza kuacha kutumia televisheni zao, kutupa simu zao za mkononi, kuharibu kompyuta zao, na kuacha kusafiri katika nchi nyingine? Je, mataifa yatajaribu kujitenga na mataifa mengine ya ulimwengu, kisiasa na kiuchumi? Yaonekana mambo hayo hayawezi kutukia. Hakuna mtu ambaye angependa kutupilia mbali faida za utandaridhi. Lakini vipi juu ya matatizo ambayo yametokea? Yanasababisha wasiwasi mwingi, na yanaathiri kila mtu. Hebu tuchunguze kwa ufupi baadhi ya matokeo mabaya zaidi ya utandaridhi.
Tofauti Inayozidi Kuongezeka
Sikuzote kumekuwa na matajiri na maskini ulimwenguni pote, lakini utandaridhi wa kiuchumi umeongeza ile tofauti kati ya matajiri na maskini. Ni kweli kwamba inaonekana nchi fulani zinazoendelea zimefaidika tangu zilipoingia katika biashara ya ulimwenguni pote. Wataalamu wanasema kwamba katika miaka kumi iliyopita, idadi ya watu maskini huko India ilipungua toka asilimia 39 hadi asilimia 26 na kwamba maendeleo kama hayo pia yamekuwako katika bara lote la Asia. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba kufikia mwaka wa 1998, asilimia 15 tu ya watu huko Asia Mashariki ndio walioishi kwa dola 1 kwa siku, ikilinganishwa na asilimia 27 miaka kumi mapema. Hata hivyo, hali ulimwenguni pote si nzuri hivyo.
Katika eneo lililoko kusini mwa jangwa la Sahara huko Afrika na katika maeneo fulani mengine yanayoendelea, mapato yameshuka katika muda wa miaka 30 iliyopita. Kofi Annan, katibu-mkuu wa UM, anasema hivi: “Jumuiya ya kimataifa . . . inakubali watu wapatao bilioni 3—karibu nusu ya wanadamu wote—kuishi kila siku kwa dola 2 za Marekani au chini ya hapo katika ulimwengu wenye utajiri mwingi sana.” Ubinafsi katika biashara ni jambo moja kuu linalosababisha tofauti hiyo kubwa ya kijamii. Larry Summers, aliyekuwa waziri wa fedha wa Marekani anasema hivi: ‘Ulimwenguni pote, taasisi za watu binafsi zinazoshughulika na mikopo na fedha za kigeni huwapuuza maskini hohehahe. Benki kubwakubwa hazianzishwi katika sehemu zenye umaskini—kwa sababu hazitapata faida.’
Tofauti hiyo kubwa katika mapato ya matajiri na maskini huwafanya watu na nchi mbalimbali kugawanyika. Muda mfupi uliopita, mali za yule mtu tajiri zaidi huko Marekani zilizidi jumla ya mali halisi za Wamarekani wengine zaidi ya milioni 100. Utandaridhi pia umesaidia makampuni tajiri ya kimataifa kuimarika na kudhibiti kwa kadiri kubwa biashara ya bidhaa fulani ulimwenguni. Kwa mfano, mnamo mwaka wa 1998, makampuni kumi tu ndiyo yaliyodhibiti asilimia 86 ya biashara ya mawasiliano ya simu ambayo ina thamani ya dola bilioni 262 za Marekani. Mara nyingi, makampuni hayo ya kimataifa huwa na uwezo mkubwa kuliko serikali mbalimbali na, kama vile shirika la Amnesty International linavyosema, makampuni hayo “hayatilii maanani haki za binadamu na za wafanyakazi.”
Mashirika ya haki za binadamu yanahangaikia jinsi watu wachache wanavyomiliki mali nyingi, na hilo linaeleweka. Je, ungependa kuishi mahali ambapo matajiri, ambao wanafanyiza asilimia 20 ya idadi ya watu, wanachuma mapato yanayozidi yale ya maskini kwa mara 74? Na kupitia televisheni, watu hao maskini, ambao wanafanyiza asilimia 20 ya idadi ya watu, wanafahamu vyema jinsi matajiri wanavyoishi, ijapokuwa hawana njia ya kuboresha maisha yao. Ukosefu huo mwingi wa haki katika ulimwengu wetu huchochea sana fujo na mfadhaiko.
Utamaduni Unaenea
Hangaiko jingine pia linahusu mgongano wa utamaduni na kuenea kwa tamaa ya mali. Utandaridhi unaeneza sana dhana mbalimbali, na Internet ni mfano bora wa jambo hilo. Kwa kusikitisha, Internet haitumiwi tu kueneza habari zinazofaa, utamaduni, na biashara. Vituo fulani vya Internet huonyesha picha chafu na kuendeleza ubaguzi wa rangi, au kamari. Vingine hata hueleza waziwazi jinsi mtu anavyoweza kujitengenezea mabomu. Kama vile Thomas L. Friedman anavyosema, ‘ni rahisi sana kupata habari hatari kwenye Internet. Unaweza kujikuta mahali ambapo watu wanapanga njama au kuona picha chafu na hakuna mtu wa kukuzuia wala kukuelekeza.’
Televisheni na filamu huathiri sana maoni ya watu. Mara nyingi filamu hutayarishwa huko Hollywood, ambayo ndiyo biashara kuu ya kutengeneza filamu ulimwenguni. Mara nyingi, biashara hiyo kubwa ya filamu huonyesha mambo yanayoendeleza tamaa ya mali, ujeuri, au ukosefu wa adili. Huenda mambo hayo yasipatane kabisa na utamaduni wa nchi nyingi ulimwenguni. Hata hivyo, mara nyingi serikali, walimu, na wazazi hushindwa kuzuia filamu hizo.
Mkazi mmoja wa Havana, huko Kuba, alimwambia hivi mgeni mmoja kutoka Amerika Kaskazini: ‘Tunapenda utamaduni wa Marekani. Tunajua mabingwa wenu wote wa Hollywood.’ Utamaduni wa Magharibi pia huwafanya watu wapende vitafunio na soda zao. Mfanyabiashara mmoja huko Malasia alisema hivi: “Hapa watu wanapenda kitu chochote ambacho kimetoka katika nchi za Magharibi, hasa Marekani. . . . Wanataka kula vyakula vyao na kuwa kama wao.” Mkuu wa chuo kimoja cha Havana alisema hivi kwa huzuni: “Kuba si kisiwa tena. Visiwa vimetokomea. Kuna ulimwengu mmoja tu.”
Utamaduni wa Magharibi ambao unaenea sana unaathiri matazamio na matamanio ya watu. Kichapo cha Human Development Report 1998 kilisema hivi: ‘Watu wameacha kushindana na majirani zao na wanataka kuishi kama matajiri na watu mashuhuri ambao wanaonyeshwa kwenye filamu na kwenye vipindi vya televisheni.’ Kwa wazi, wanadamu wengi hawataweza kamwe kuwa na maisha kama hayo.
Je, Suluhisho Ni Kuunganisha Ulimwengu?
Sawa na miradi mingi ya wanadamu, utandaridhi umeleta faida na hasara. Umewawezesha watu fulani kufaidika kiuchumi, na kuleta maendeleo katika mawasiliano ya ulimwenguni pote. Hata hivyo, unawafaidi matajiri na watu wenye uwezo kuliko maskini. Wahalifu wametumia faida za utandaridhi vizuri kuliko serikali mbalimbali. Na virusi vinavyosababisha magonjwa vimeenea kwa sababu ya utandaridhi.—Ona masanduku kwenye ukurasa wa 8 na 9.
Utandaridhi umeongeza sana matatizo ulimwenguni. Badala ya kusuluhisha matatizo hayo, utandaridhi umechangia matatizo. Migawanyiko na mfadhaiko umeongezeka katika jamii. Serikali ulimwenguni pote zinajaribu kutumia faida za utandaridhi huku zikiwazuia raia wasiathiriwe na athari zake mbaya. Je, serikali hizo zitafanikiwa? Je, inawezekana kwamba suluhisho ni kuunganisha ulimwengu kwa njia ya kuwajali wanadamu wengine? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8, 9]
KUENEA KWA UHALIFU NA UGAIDI
Kwa kuhuzunisha, mbinu za kuendeleza biashara zaweza kutumiwa kwa urahisi na wahalifu. Kichapo cha Human Development Report 1999 kinasema hivi: ‘Mashirika ya kimataifa yamejitahidi kubuni mbinu za kusitawisha biashara ulimwenguni pote na magenge ya wahalifu ya kimataifa yanatumia mbinu hizo.’ Magenge ya wahalifu yamefaidikaje kutokana na utandaridhi?
Magenge ya kuuza dawa za kulevya yamegundua njia nyingi za kufanya biashara yao ya mabilioni ya dola kuonekana kuwa halali. Kwa kuwa vizuizi vingi vya forodha vimeondolewa na wasafiri wameongezeka, ni rahisi magenge hayo kusafirisha dawa za kulevya kutoka nchi moja hadi nyingine au kutoka bara moja hadi jingine. Katika miaka ya 1990, utengenezaji wa kokeini uliongezeka mara mbili na wa kasumba uliongezeka mara tatu. Magenge ya wahalifu ya kimataifa pia yamesitawisha biashara ya ukahaba inayotokeza faida kubwa. Kila mwaka, wanawake na wasichana wapatao 500,000 husafirishwa kwa meli hadi Ulaya Magharibi kwa kusudi hilo—wengi wao wakipelekwa huko kwa lazima.
Sawa na mashirika ya kimataifa, magenge ya wahalifu yameungana pia katika miaka ya hivi majuzi. Magenge mengi yanafanya kazi ulimwenguni pote, na kwa jumla magenge hayo hupata dola trilioni 1.5 za Marekani kwa mwaka—fedha nyingi kuliko jumla ya pato la taifa la Ufaransa.a
Internet pia imetumiwa vibaya na wataalamu wakora wa kompyuta. Mnamo mwaka wa 1995, mtaalamu mmoja mlaghai wa kompyuta aliiba habari zilizokadiriwa kuwa zina thamani ya dola milioni 1 za Marekani pamoja na nambari 20,000 za kibinafsi za kadi za mikopo. José Antonio Soler, Mhispania ambaye ni mkurugenzi wa benki, alisema hivi: “Kuiba kwa kutumia tekinolojia mpya si hatari sana na kunatokeza faida kubwa.”
Magaidi pia hutumia faida za utandaridhi. Kwa kuwa vyombo vya habari husambaza habari ulimwenguni, magaidi wanaweza kuwateka nyara watalii kadhaa wa nchi za Magharibi katika nchi ya mbali ili kutangaza haraka malalamiko yao ya kisiasa.
VITU VIBAYA VINAVYOENEA
Watu na vilevile magonjwa yanaweza kuenea ulimwenguni pote, na baadhi ya magonjwa hayo ni hatari. Profesa Jonathan M. Mann, mtaalamu wa magonjwa ya kuambukiza, anasema hivi: ‘Magonjwa yameenea hasa kwa sababu kuna ongezeko kubwa la wasafiri, bidhaa zinazosafirishwa, na mawazo yanayoenea ulimwenguni pote. Sasa, magonjwa mapya ya kuambukiza na yale ya zamani yanatokea na kuenea kwa urahisi ulimwenguni.’
Jambo hilo linaonyeshwa wazi na ugonjwa wa UKIMWI ambao sasa unasababisha vifo vya watu milioni tatu hivi kila mwaka. Katika nchi fulani za Afrika, wafanyakazi wanaotoa huduma za afya wanahofu kwamba hatimaye ugonjwa huo utaua theluthi mbili ya vijana. Ripoti moja ya Mradi wa Umoja wa Mataifa Kuhusu UKIMWI inasema hivi: “Ijapokuwa kwa karne na miaka kumekuwa na magonjwa ya kuambukiza, vita na njaa, hakuna wakati mwingine wowote ambapo vijana wengi hivyo wamekufa.”
Mbali na viini na virusi, kuna vitu vingine vinavyoenea ulimwenguni. Wanyama, mimea, na wadudu wametoroka mazingira yao ya asili na kuingia katika mabara mengine. Aina fulani ya nyoka wenye sumu kutoka Australia wamevamia Visiwa vya Pasifiki. Yaonekana waliingia huko kwa kujificha ndani ya ndege. Nyoka hao wamewamaliza karibu ndege wote wa msituni huko Guam. Gugu-maji kutoka Amerika Kusini limeenea katika nchi 50 za kitropiki, ambako linaziba mifereji na kuharibu vidimbwi vya samaki. Gazeti la International Herald Tribune linasema hivi: “Viumbe wanaovamia sehemu nyingine za ulimwengu wanasababisha hasara ulimwenguni pote kila mwaka ambayo huenda ina thamani ya mamia ya mabilioni ya dola na kueneza magonjwa na kuharibu sana mazingira.”
[Maelezo ya Chini]
a “Jumla ya pato la taifa” ni thamani ya bidhaa na huduma zote ambazo nchi hutoa kwa mwaka.
[Picha]
PESA ZINAZOSAFIRISHWA KIHARAMU
Zikiwa zimefichwa ndani ya shehena ya wanasesere
KUSAFIRISHA KOKEINI KIHARAMU
Kokeini yenye thamani ya dola 4,000,000 za Marekani ilipatikana mpakani ndani ya gari moja la kwenda safari
UGAIDI WA KIBIOLOJIA
Maaskari watafuta virusi vya kimeta huko Capitol Hill, Washington, D.C.
MASHAMBULIZI YA MABOMU
Bomu lililotegwa kwenye gari lalipuka huko Israel
KUENEA KWA UKIMWI ULIMWENGUNI POTE
Ugonjwa wa UKIMWI umeenea sana huko Afrika Kusini hivi kwamba hospitali fulani za umma hazikubali wagonjwa zaidi
VIUMBE WANAOVAMIA MAZINGIRA MAPYA
Nyoka-mti wenye rangi ya kahawia wako karibu kuwamaliza ndege wote wa msituni huko Guam
GUGU-MAJI
Mmea huu huziba mifereji na kingo za mito katika nchi 50 hivi
[Hisani]
Kusafirisha pesa na kokeini kiharamu: James R. Tourtellotte and Todd Reeves/U.S. Customs Service; ugaidi wa kibiolojia: AP Photo/Kenneth Lambert; basi linaloungua: AP Photo/HO/Israeli Defense Forces; mtoto: AP Photo/Themba Hadebe; nyoka: Photo by T. H. Fritts, USGS; gugu-maji: Staff CDFA, California Dept. of Food & Agriculture, Integrated Pest Control Branch
[Picha katika ukurasa wa 7]
Utandaridhi wa kiuchumi umeongeza tofauti kati ya matajiri na maskini
[Hisani]
UN PHOTO 148048/ J. P. Laffont - SYGMA
[Picha katika ukurasa wa 10]
Internet inatumiwa kuendeleza ugaidi
-
-
Njia ya Kuunganisha Ulimwengu Ambayo ItakufaidiAmkeni!—2002 | Mei 22
-
-
Njia ya Kuunganisha Ulimwengu Ambayo Itakufaidi
“Ili utandaridhi ufaulu, ni lazima uwafaidi maskini na matajiri kwa usawa. Ni lazima watu wapate haki zao kama wanavyopata mali. Ni lazima utokeze haki na usawa katika jamii sawa na ufanisi wa kiuchumi na maendeleo ya mawasiliano.”—KOFI ANNAN, KATIBU-MKUU WA UMOJA WA MATAIFA.
KAMA vile Kofi Annan alivyosema, ili utandaridhi ufaulu, ni lazima uboreshe maisha ya watu wote ulimwenguni. Lakini hali ya maisha haijawa nzuri katika miaka ya hivi majuzi. Kumekuwa na ufanisi mwingi wa kiuchumi na maendeleo ya kitekinolojia kuliko maendeleo katika haki za binadamu na usawa katika jamii.
Tatizo kuu ni kwamba utandaridhi wa kiuchumi unachochewa hasa na tamaa ya kupata mali. Watu wanaoongozwa na tamaa hiyo hawawafikirii maskini wala kutilia maanani masilahi ya siku zijazo ya dunia. Dakt. David C. Korten anasema hivi: “Biashara ya ulimwenguni pote isiyodhibitiwa ambayo inaongozwa na mashirika ambayo yanazingatia tu kupata fedha haiwezi kuwa thabiti . . . na inawafanya wanadamu kuwa maskini katika njia nyingine.”
Je, serikali za ulimwengu zitaweza kudhibiti biashara ya ulimwenguni pote ili itokeze haki katika jamii? Inaonekana hilo haliwezekani. Kufikia sasa, serikali zimeshindwa kutatua matatizo yoyote ulimwenguni—iwe ni uhalifu wa kimataifa, ongezeko la joto duniani, au umaskini ulimwenguni pote. Annan anasema hivi: ‘Watu wanahitaji kushirikiana kutunza masilahi ya ulimwenguni pote, lakini katika ulimwengu huu wa utandaridhi mbinu za kufanya kazi hiyo ya ulimwenguni pote ni za hali ya chini sana.’
Licha ya mbinu za kushughulikia matatizo ya ulimwenguni pote, kuna mambo mengine yanayohitajiwa. Tume ya Usimamizi wa Ulimwengua inasema kwamba maadili mazuri yanahitajiwa ulimwenguni. Ripoti ya tume hiyo inasema hivi: ‘Bila maadili ya ulimwenguni pote, migogoro itaongezeka ulimwenguni; bila mwongozo, hata mikakati na mashirika yaliyopangwa vizuri hayataweza kufaulu.’
Walipendekeza maadili gani kwa ajili ya ulimwengu wote? Ripoti hiyo ilisema hivi: “Watu wanapaswa kuwatendea wengine kama wanavyotaka kutendewa.” Yesu Kristo, kiongozi mkuu zaidi aliyewahi kuonekana ulimwenguni, alifundisha kanuni hiyo miaka elfu mbili hivi iliyopita. (Mathayo 7:12) Lakini kanuni hiyo bado inafaa hali za leo. Bila shaka, kuunganisha ulimwengu kwa kutumia kanuni hiyo kutafaidi kila mtu. Je, hilo linaweza kutukia?
Suluhisho Tofauti la Matatizo Ulimwenguni Pote
Biblia inatabiri kwamba hivi karibuni serikali ya ulimwenguni pote isiyokuwa na ubinafsi itawaunganisha wanadamu pasipo kutumia fedha wala tekinolojia. Serikali hiyo itafaulu kwa sababu ina uwezo na mbinu za kuwasaidia wanadamu wote ulimwenguni pote. Yesu Kristo alikazia serikali hiyo ya ulimwenguni pote alipowafundisha wafuasi wake kusali ‘Ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yatendeke duniani.’—Mathayo 6:10.
Ufalme wa Mungu, serikali ya mbinguni inayoongozwa na Yesu Kristo, utaleta maadili mapya ulimwenguni pote, maadili yaleyale ambayo Yesu alifundisha alipokuwa duniani. Kumpenda Mungu na jirani ndizo kanuni zitakazoongoza. (Mathayo 22:37-39) Unabii mwingi katika Biblia unaonyesha mambo ambayo yatafanywa na serikali hiyo mpya. Biblia inaahidi hivi kuhusu Mtawala wa serikali hiyo, Yesu Kristo: “Atawapatia haki watu maskini, atawaamulia sawasawa wanyonge nchini.” (Isaya 11:4, Biblia Habari Njema) Matajiri na watu wenye uwezo hawatawadhulumu watu wasio na uwezo. Yesu “atamhurumia aliye dhaifu na maskini . . . Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu.”—Zaburi 72:13, 14.
Matatizo yanayokumba mazingira yataondolewa haraka. Badala ya majangwa kuenea, “nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi.” (Isaya 35:1) Badala ya upungufu wa chakula, ‘kutakuwepo wingi wa nafaka.’—Zaburi 72:16.
Ufalme wa Mungu huwaunganisha watu wa jamii zote. ‘Nitawaleta pamoja kama kondoo katika zizi,’ Mungu anaahidi. ‘Nitawarudishia lugha iliyo safi, wanitumikie kwa nia moja.’ (Mika 2:12, BHN; Sefania 3:9) Hiyo ‘lugha safi,’ ambayo inatia ndani kanuni za kiadili na za kidini zinazowahusu wote, inawaunganisha watu hata sasa.
Kwa sababu ya vyombo vya usafiri ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova hufanya makusanyiko makubwa ya kimataifa kwa ukawaida, ambayo huunganisha watu wa jamii, mataifa, na utamaduni mbalimbali. Makusanyiko hayo yanaonyesha wazi jinsi watu wanavyoweza kuunganishwa wawe na moyo mmoja na akili moja, badala ya kupitia tekinolojia na biashara. (Ona sanduku.) Mwanatheolojia mmoja Mhispania ambaye amehudhuria baadhi ya makusanyiko hayo aliandika hivi: ‘Nilitoka huko nikiwa nimejengwa, si tu kwa hotuba za Kimaandiko zenye kuelimisha bali pia kwa sababu ya umoja uliopo kati ya watu hao, maadili yao mazuri sana, na tabia yao njema.’
Mashahidi wa Yehova pia hutumia vizuri faida nyingine za utandaridhi ili kuendeleza kazi yao ya kuhubiri habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Kwa mfano, gazeti la Amkeni! hutafsiriwa katika lugha zaidi ya 80 na watafsiri wengi ulimwenguni pote ambao wanatumia programu za kompyuta na njia za mawasiliano ya kompyuta. Vyombo hivyo huwasaidia Mashahidi wa Yehova kueneza programu yao ya elimu ya Biblia ulimwenguni pote. Kwa wazi, vifaa vya utandaridhi vyaweza kutumiwa kuleta faida au hasara.
Vivyo hivyo, badala ya kuleta matatizo kama vile njia ya wanadamu ya kuunganisha ulimwengu ilivyofanya, serikali ya ulimwenguni pote iliyosimamishwa na Mungu italeta masuluhisho. Tuna kila sababu ya kuwa na uhakika katika utawala huo wa mbinguni. Mungu anaahidi hivi: ‘Naumba nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa. Furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.’ (Isaya 65:17, 18) “Nchi mpya” ya Mungu itawafaidi watu kabisa ulimwenguni pote.
[Maelezo ya Chini]
a Tume hiyo, ambayo ina viongozi mashuhuri wa ulimwengu 28, ilitayarisha ripoti ndefu katika mwaka wa 1995, yenye kichwa “Our Global Neighbourhood.” Katika ripoti hiyo viongozi hao walitaja mapendekezo yao ya kuboresha usimamizi ulimwenguni.
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
WAMEUNGANISHWA LAKINI BADO WAMEGAWANYIKA
Ijapokuwa tekinolojia imewaunganisha watu ulimwenguni pote, bado kuna migawanyiko. Televisheni, simu za mkononi, na Internet zimewawezesha watu kuwasiliana lakini hazijawawezesha kuwa kitu kimoja. Biashara ya ulimwenguni pote na kumalizika kwa uhasama kati ya mataifa yenye uwezo kumepunguza vita kati ya Nchi mbalimbali, lakini vita katili za wenyewe kwa wenyewe zinaendelea kuwaua na kuwalemaza mamia ya maelfu ya watu kila mwaka.
Kwa nini? Kwa sababu bado kuna chuki kati ya vikundi vya kikabila, vya kijamii, na vya kidini—kisababishi cha vita za wenyewe kwa wenyewe. Na biashara mbalimbali ulimwenguni pote na magenge ya wahalifu huuza silaha nyingi za bei rahisi kwa vikundi vinavyopigana. Umoja wa kweli hauwezi kutokezwa na mashine za elektroniki. Wala ongezeko la faida katika soko la hisa haliwezi kutokeza haki katika jamii.
Katika njia fulani, utandaridhi wa kiuchumi unaweza kusababisha mgawanyiko. Uchumi unapoanza kuzorota baada ya kuimarika sana, wanasiasa wakatili wanaweza kutumia nafasi hiyo ili kujifaidi na kuwanyanyasa maskini wasio na uwezo. Basi suluhisho ni nini? Kichapo cha Human Development Report 1999 kinasema hivi: “Ni lazima kuwe na usimamizi mpya katika mataifa na ulimwenguni pote—na hangaiko kuu liwe kuleta usawa na kuwawezesha watu kufanya maendeleo.” Ufalme wa Mungu utafanya hivyo hasa.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Programu ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova imewaunganisha watu wa jamii zote
-