Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Musa Aliamua Kumwabudu Yehova
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Binti ya Farao anampata mtoto Musa huku Miriamu akiwatazama kwa karibu

      SOMA 17

      Musa Aliamua Kumwabudu Yehova

      Katika nchi ya Misri, watu wa familia ya Yakobo walikuja kuitwa Waisraeli. Baada ya Yakobo na Yosefu kufa, Farao mwingine alianza kutawala. Aliogopa kwamba Waisraeli wangekuwa wengi na hivyo kuwa na nguvu kuliko Wamisri. Kwa hiyo, Farao huyo aliwafanya Waisraeli kuwa watumwa. Aliwalazimisha kutengeneza matofali na kufanya kazi ngumu kwenye mashamba. Lakini kadiri Wamisri walivyowalazimisha wafanye kazi ngumu, ndivyo walivyozidi kuongezeka. Kwa kuwa Farao hakufurahia jambo hilo, aliagiza wavulana wote Waisraeli wauawe mara tu wanapozaliwa. Je, unaweza kuwazia jinsi Waisraeli walivyoogopa?

      Mwanamke Mwisraeli aliyeitwa Yokebedi, alijifungua mtoto wa kiume mwenye sura nzuri. Kwa sababu alitaka kumwokoa, aliamua kumweka ndani ya kikapu, na kumficha kwenye matete yaliyo kandokando ya Mto Nile. Miriamu, dada ya mtoto huyo, alikaa karibu ili aone kitakachotokea.

      Binti ya Farao alienda kuoga mtoni na akaona kikapu hicho. Ndani ya kikapu hicho, aliona mtoto akilia, naye akamsikitikia. Miriamu akamwuliza: ‘Ungependa nikutafutie mwanamke atakayemnyonyesha mtoto huyu kwa niaba yako?’ Binti ya Farao alipokubali, Miriamu akamleta Yokebedi, mama yake. Binti ya Farao akamwambia hivi: ‘Mchukue mtoto huyu uninyonyeshee, halafu nitakulipa.’

      Musa akikimbia

      Mtoto alipokuwa mkubwa, Yokebedi akamleta kwa binti ya Farao, naye akamwita Musa na kumlea kama mtoto wake. Musa alilelewa kama mtoto wa mfalme na angeweza kupata chochote alichotaka. Lakini Musa hakumsahau Yehova. Alijua kwamba yeye alikuwa Mwisraeli, si Mmisri. Na aliamua kumtumikia Yehova.

      Alipokuwa na umri wa miaka 40, Musa aliamua kuwasaidia Waisraeli wenzake. Alipomwona Mmisri akimpiga mtumwa Mwisraeli, Musa alimpiga kwa nguvu Mmisri huyo na kumuua. Halafu akamficha ndani ya mchanga. Farao alipogundua jambo hilo, alijaribu kumuua Musa. Lakini Musa akakimbilia nchi ya Midiani. Yehova alimtunza alipokuwa huko.

      “Kwa imani, Musa . . alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kuteswa pamoja na watu wa Mungu.”​—Waebrania 11:24, 25

      Maswali: Waisraeli walitendewaje walipokuwa Misri? Kwa nini Musa alikimbia kutoka Misri?

      Mwanzo 49:33; Kutoka 1:1-14, 22; 2:1-15; Matendo 7:17-29; Waebrania 11:23-27

  • Kichaka Kinachowaka Moto
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Musa akiwa karibu na kichaka kinachowaka moto

      SOMO LA 18

      Kichaka Kinachowaka Moto

      Musa aliishi Midiani kwa miaka 40. Alioa na kupata watoto. Siku moja alipokuwa akichunga kondoo karibu na Mlima Sinai, aliona kitu chenye kustaajabisha. Kichaka kilikuwa kikiwaka moto lakini hakikuteketea! Alipokikaribia ili aone kwa nini hakikuwa kikiteketea, alisikia sauti kutoka kwenye kichaka hicho ikisema: ‘Musa! Usikaribie zaidi. Vua viatu vyako kwa sababu mahali ambapo umesimama ni ardhi takatifu.’ Yehova ndiye aliyekuwa akizungumza kupitia malaika.

      Musa aliogopa, kwa hiyo akauficha uso wake. Sauti hiyo ilisema hivi: ‘Nimeyaona mateso ya Waisraeli. Nitawakomboa kutoka kwa Wamisri na kuwapeleka kwenye nchi nzuri. Wewe ndiye utakayewaongoza watu wangu kutoka Misri.’ Je, unafikiri jambo hilo lilimshangaza Musa?

      Musa akauliza hivi: ‘Watu wakiniuliza ni nani aliyenituma, niwaambie nini?’ Mungu akamjibu hivi: ‘Waambie kwamba Yehova, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo amekutuma.’ Kisha Musa akasema hivi: ‘Vipi ikiwa watu hao hawatanisikiliza?’ Yehova alimpa Musa uthibitisho kwamba atamsaidia. Alimwambia Musa atupe fimbo yake chini, nayo ikawa nyoka! Musa alipomkamata nyoka huyo kwenye mkia, akageuka kuwa fimbo. Yehova akasema hivi: ‘Ukiwafanyia muujiza huu, utathibitisha kwamba nimekutuma.’

      Musa akasema: ‘Mimi si msemaji mzuri.’ Yehova akamwahidi hivi: ‘Nitakufundisha mambo unayopaswa kusema, nami nitamtuma Haruni, ndugu yako, ili akusaidie.’ Akiwa na uhakika kwamba Yehova alikuwa pamoja naye, Musa akamchukua mke na watoto wake, na kurudi Misri.

      “Msihangaike kuhusu jambo mtakalosema au jinsi mtakavyolisema, kwa sababu mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo.”​—Mathayo 10:19

      Maswali: Musa aliona nini alipokuwa akichunga kondoo? Yehova alimwagiza Musa afanye nini?

      Kutoka 3:1–4:20; Matendo 7:30-36

  • Mapigo Matatu ya Kwanza
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Musa na Haruni wamesimama mbele ya Farao

      SOMO LA 19

      Mapigo Matatu ya Kwanza

      Waisraeli walilazimishwa kufanya kazi ngumu wakiwa watumwa. Yehova aliwatuma Musa na Haruni wamwambie hivi Farao: ‘Waruhusu watu wangu waondoke ili wakaniabudu huko nyikani.’ Kwa kiburi, Farao akasema hivi: ‘Mimi sijali Yehova anasema nini, na sitawaruhusu Waisraeli waondoke.’ Kisha Farao akawalazimisha wafanye kazi ngumu hata zaidi. Yehova angemfundisha Farao somo. Unajua alifanya nini? Alileta Mapigo Kumi juu ya Misri. Yehova alimwambia hivi Musa: ‘Farao amekataa kunisikiliza. Kesho asubuhi atakuwa kwenye Mto Nile. Nenda ukamwambie, kwa kuwa amekataa kuwaruhusu watu wangu waondoke, maji yote ya Mto Nile yatageuka kuwa damu.’ Musa alitii na akaenda kwa Farao. Farao alimwona Haruni akipiga maji ya Mto Nile kwa fimbo yake, nayo yakageuka kuwa damu. Samaki wakafa, mto ukaanza kunuka, na hakukuwa na maji safi ya kunywa kutoka kwenye Mto Nile. Lakini bado Farao alikataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke.

      Baada ya siku saba, Yehova alimtuma tena Musa kwa Farao akamwambie hivi: ‘Usipowaruhusu watu wangu waondoke, vyura watajaa katika nchi yote ya Misri.’ Haruni akainua fimbo yake na vyura wakaanza kujaa na kuifunika nchi. Kulikuwa na vyura katika nyumba za watu, vitandani, na kwenye vyombo. Vyura walikuwa kila mahali! Farao alimwambia Musa amwombe Yehova akomeshe pigo hilo. Akaahidi kwamba angewaruhusu Waisraeli waende. Kisha Yehova akakomesha pigo hilo, na Wamisri wakawakusanya vyura hao mafungu-mafungu. Nayo nchi ikaanza kunuka. Lakini kwa mara nyingine tena, Farao hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.

      Baada ya hapo, Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Mwambie Haruni apige mavumbi ya dunia kwa fimbo yake, nayo yatakuwa mbu, au wadudu wadogo wanaouma.’ Papo hapo, mbu wakajaa kila mahali. Baadhi ya watu wa Farao walimwambia hivi: ‘Pigo hili limetoka kwa Mungu.’ Lakini bado Farao hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.

      Mapigo matatu kati ya mapigo kumi nchini Misri: damu kwenye Mto Nile, vyura, na mbu

      “Nitawafanya wajue nguvu zangu na uwezo wangu, nao watalazimika kujua kwamba jina langu ni Yehova.”​—Yeremia 16:21

      Maswali: Taja mapigo matatu ya kwanza. Kwa nini Yehova alileta mapigo hayo?

      Kutoka 5:1-18; 7:8–8:19; Nehemia 9:9,10

  • Mapigo Sita Yaliyofuata
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Makundi ya nzige

      SOMO LA 20

      Mapigo Sita Yaliyofuata

      Musa na Haruni walienda kumwambia Farao ujumbe huu kutoka kwa Mungu: ‘Ikiwa hutawaruhusu watu wangu waende zao, nitatuma nzi juu ya nchi yako.’ Makundi makubwa ya nzi yakaanza kuvamia nyumba za Wamisri, matajiri kwa maskini. Nchi yote ikajaa nzi. Lakini katika eneo la Gosheni, ambako Waisraeli walikuwa wanaishi, hakukuwa na nzi. Pigo la nne na yale yaliyofuata yaliwapata Wamisri peke yao. Farao akamsihi hivi Musa: ‘Mwombe Yehova kwa niaba yangu aondoe nzi hao, kisha watu wako wanaweza kuondoka.’ Hata hivyo, Yehova alipowaondoa nzi, Farao alibadili mawazo yake. Unafikiri Farao angejifunza kutii?

      Yehova alisema hivi: ‘Ikiwa Farao ataendelea kukataa kuwaruhusu watu wangu waende zao, mifugo ya Wamisri itapatwa na ugonjwa na kufa.’ Siku iliyofuata, mifugo ikaanza kufa. Lakini mifugo ya Waisraeli haikufa. Lakini bado Farao aliendelea kuwa na moyo mgumu na hakutaka kuwaruhusu waondoke.

      Kisha Yehova akamwambia Musa arudi kwa Farao na kurusha majivu angani. Majivu hayo yakawa vumbi na kujaza nchi yote na kuwafunika Wamisri. Mavumbi hayo yakasababisha majipu juu ya Wamisri na wanyama wao wote. Ingawa hivyo, Farao alikataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke.

      Mapigo ya Misri kuanzia pigo la 4 hadi la 6: nzi, mifugo inakufa, majipu

      Yehova akamtuma tena Musa kwa Farao amwambie hivi: ‘Bado unakataa kuwaruhusu watu wangu waondoke? Kesho mvua kubwa sana ya mawe itanyesha juu ya nchi.’ Siku iliyofuata, Yehova akafanya mvua kubwa ya mawe inyeshe, pia kukawa na ngurumo, na moto. Wamisri hawakuwa wamewahi kuona mvua kubwa kama hiyo. Miti yote na mimea iliharibiwa isipokuwa katika eneo la Gosheni. Farao akasema: ‘Msihi Yehova ili mvua iache kunyesha! Kisha nitawaruhusu mwende.’ Hata hivyo, mara tu mvua ilipoacha kunyesha, Farao alibadili mawazo yake tena.

      Kisha Musa akasema hivi: ‘Sasa nzige watakula mimea yote iliyobaki baada ya mvua ya mawe kunyesha.’ Makundi ya nzige wengi wakala kila kitu kilichobaki shambani na kwenye miti. Farao akamsihi Musa hivi: ‘Mwombe Yehova awaondoe nzige hawa.’ Lakini hata baada ya Yehova kuwaondoa nzige, bado Farao aliendelea kuwa na moyo mgumu.

      Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Nyoosha mkono wako kuelekea angani.’ Papo hapo, giza zito likatokea katika nchi yote. Kwa siku tatu, Wamisri hawakuweza kuona kitu chochote. Waisraeli tu ndio waliokuwa na mwangaza katika nyumba zao.

      Mapigo ya Misri kuanzia pigo la 7 hadi la 9: mvua kubwa, nzige, giza

      Farao akamwambia Musa: ‘Wewe na watu wako mnaweza kwenda. Lakini waacheni wanyama wenu.’ Musa akasema: ‘Lazima twende na wanyama ili tukamtolee Mungu wetu dhabihu.’ Farao alikasirika sana. Akamwambia hivi Musa kwa hasira: ‘Toka hapa! Nikikuona tena nitakuua!’

      “Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.”​—Malaki 3:18

      Maswali: Yehova alileta mapigo gani baadaye? Mapigo hayo yalitofautianaje na yale matatu ya kwanza?

      Kutoka 8:20–10:29

  • Pigo la Kumi
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Mwanamume Mwisraeli akipaka damu juu ya mlango wake

      SOMO LA 21

      Pigo la Kumi

      Musa alimwahidi Farao kwamba hangeenda kumwona tena. Lakini kabla hajaondoka, alimwambia Farao hivi: ‘Katikati ya usiku, kila mzaliwa wa kwanza nchini Misri, kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao mpaka mzaliwa wa kwanza wa watumwa, atakufa.’

      Yehova aliwaambia Waisraeli watayarishe mlo wa pekee. Alisema hivi: ‘Chinjeni kondoo dume au mbuzi wa mwaka mmoja, kisha mpake damu yake kwenye mlango wa nyumba zenu. Chomeni nyama hiyo na kuila pamoja na mkate usiotiwa chachu. Vaeni nguo na viatu na muwe tayari kuondoka. Nitawakomboa usiku wa leo.’ Hebu wazia jinsi Waisraeli walivyofurahi!

      Katikati ya usiku, malaika wa Yehova alienda katika kila nyumba nchini Misri. Mzaliwa wa kwanza katika nyumba yoyote ambayo haikuwa imepakwa damu mlangoni, alikufa. Lakini malaika huyo alipita nyumba zilizokuwa zimepakwa damu. Kila mzaliwa wa kwanza alikufa katika familia zote nchini Misri, iwe ni za matajiri au maskini. Lakini hakuna mtoto hata mmoja wa Mwisraeli aliyekufa.

      Hata mwana wa Farao mwenyewe alikufa. Farao hangeweza kuvumilia tena. Papo hapo akawaambia Musa na Haruni hivi: ‘Simameni. Ondokeni hapa. Nendeni mkamwabudu Mungu wenu. Chukueni wanyama wenu na mwende!’

      Usiku huo, kukiwa na mwezi mpevu, Waisraeli waliondoka Misri wakiwa wamepangwa kulingana na familia na makabila yao. Kulikuwa na wanaume Waisraeli 600,000, pamoja na wanawake wengi na watoto. Pia, watu wengine wengi waliambatana nao ili wamwabudu Yehova. Hatimaye, Waisraeli walikuwa huru!

      Ili kukumbuka jinsi ambavyo Yehova aliwakomboa, kila mwaka wangetayarisha mlo huo wa pekee. Mlo huo uliitwa Pasaka.

      Waisraeli wakitoka Misri

      “Kwa sababu hii nimekuacha ubaki: ili nionyeshe nguvu zangu kuhusiana na wewe na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.”​—Waroma 9:17

      Maswali: Pigo la kumi lilikuwa lipi? Waisraeli walipaswa kufanya nini ili kujilinda wakati wa pigo la mwisho?

      Kutoka 11:1–12:42;13:3-10

  • Muujiza Katika Bahari Nyekundu
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Farao na jeshi lake

      SOMO LA 22

      Muujiza Katika Bahari Nyekundu

      Muda mfupi tu baada ya kusikia kwamba Waisraeli wameondoka Misri, Farao alibadili mawazo yake kuhusu kuwaruhusu waondoke. Aliwaamuru hivi mashujaa wake wa vita: ‘Tayarisheni magari ya vita ili tuwafuate! Hatukupaswa kuwaruhusu waondoke.’ Farao na wanaume wake wakaanza kuwafuata Waisraeli.

      Yehova alikuwa akiwaongoza watu wake kupitia wingu wakati wa mchana na nguzo ya moto wakati wa usiku. Aliwaongoza hadi kufikia Bahari Nyekundu, na kuwaambia wapige kambi.

      Kisha Waisraeli wakaona Farao na jeshi lake wakiwafuatilia. Walijikuta wakiwa wamenaswa kati ya bahari na jeshi la Wamisri. Wakaanza kumlilia Musa na kusema, ‘Tutakufa! Ni bora ungetuacha Misri.’ Lakini Musa akawaambia: ‘Msiogope. Simameni imara muuone wokovu wa Yehova.’ Kwa kweli Musa alimtumaini Yehova, sivyo?

      Yehova akawaambia Waisraeli wavunje kambi. Usiku huo, Yehova akalihamisha wingu na kuliweka katikati ya Wamisri na Waisraeli. Kukawa na giza upande wa Wamisri, lakini upande wa Waisraeli kukawa na mwangaza.

      Yehova akamwambia Musa aunyooshe mkono wake juu ya bahari. Kisha Yehova akafanya upepo wenye nguvu uvume usiku kucha. Bahari ikagawanyika na kukawa na njia katikati yake. Idadi kubwa ya Waisraeli wakapita katikati ya bahari juu ya nchi kavu, huku maji yakiwa kama ukuta kando yao nao wakaelekea upande wa pili wa bahari.

      Waisraeli walipita katikati ya bahari juu ya nchi kavu, huku maji yakiwa kama ukuta kando yao

      Jeshi la Farao likawafuata Waisraeli ndani ya bonde la bahari. Kisha Yehova akavuruga jeshi hilo. Magurudumu ya magari yao ya vita yakaanza kutoka. Wanajeshi hao wakapiga kelele na kusema: ‘Tuondoke hapa, kwa kuwa Yehova anawapigania Waisraeli!’

      Yehova akamwambia Musa: ‘Nyoosha mkono wako juu ya bahari.’ Ghafla kuta za maji zikaangukia jeshi la Wamisri. Farao na wanaume wake wote wakafa. Hakuna hata mmoja aliyeokoka.

      Ng’ambo ile nyingine ya bahari, umati mkubwa ulikuwa ukimsifu Mungu kwa kuimba hivi: “Mwimbieni Yehova, kwa maana amekwezwa sana. Farasi na mpandaji wake amewavurumisha baharini.” Watu walipokuwa wakiimba, wanawake walikuwa wakicheza dansi wakiwa na matari. Kila mtu alikuwa na furaha kwa sababu sasa walikuwa huru kabisa.

      “Ili tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?’”​—Waebrania 13:6

      Maswali: Ni nini kilichotokea kwenye Bahari Nyekundu? Yehova aliwaokoaje Waisraeli?

      Kutoka 13:21–15:21; Nehemia 9:9-11; Zaburi 106:9-12; 136:11-15; Waebrania 11:29

  • Waisraeli Wamtolea Yehova Ahadi
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Waisraeli wamesimama kwenye sehemu ya chini ya Mlima Sinai

      SOMO LA 23

      Waisraeli Wamtolea Yehova Ahadi

      Miezi miwili hivi baada ya Waisraeli kutoka Misri, walifika kwenye Mlima Sinai na kupiga kambi. Yehova akamwita Musa, naye akapanda juu mlimani, kisha Yehova akamwambia hivi: ‘Mimi niliwaokoa Waisraeli. Ikiwa watanitii na kushika sheria zangu, watakuwa watu wangu wa pekee.’ Musa akashuka kutoka mlimani na kuwaambia Waisraeli maneno ambayo Yehova alikuwa amesema. Waliitikiaje? Walisema hivi: ‘Tutafanya mambo yote ambayo Yehova anatuambia tufanye.’

      Musa akapanda tena juu mlimani. Akiwa huko, Yehova akamwambia: ‘Baada ya siku tatu, nitazungumza nawe. Waonye watu wasijaribu kupanda juu kwenye Mlima Sinai.’ Musa akateremka kutoka mlimani na kuwaambia Waisraeli wajitayarishe kusikiliza kile ambacho Yehova atasema.

      Waisraeli wanaona radi na wingu zito juu ya Mlima Sinai

      Siku tatu baadaye, Waisraeli waliona radi na wingu zito kwenye mlima. Pia, walisikia sauti kubwa sana ya mingurumo na pembe. Kisha Yehova akashuka kwenye mlima katika moto. Waisraeli wakaogopa sana na kutetemeka. Mlima wote ulitetemeka sana na kufunikwa na moshi. Sauti ya pembe ikazidi kuwa kubwa. Kisha Mungu akasema: ‘Mimi ni Yehova. Msiabudu miungu mingine.’

      Musa akapanda tena juu mlimani, na Yehova akampa sheria ambazo zilionyesha jinsi watu walivyopaswa kumwabudu na jinsi walivyopaswa kujiendesha. Musa akaandika sheria hizo kisha akawasomea Waisraeli. Wakaahidi hivi: ‘Tutafanya mambo yote ambayo Yehova ametuambia tufanye.’ Naam, Waisraeli walimtolea Mungu ahadi. Je, wangeitimiza?

      “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.”​—Mathayo 22:37

      Maswali: Ni nini kilichotendeka kwenye Mlima Sinai? Waisraeli waliahidi kufanya nini?

      Kutoka 19:1–20:21; 24:1-8; Kumbukumbu la Torati 7:6-9; Nehemia 9:13, 14

  • Walivunja Ahadi Yao
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Waisraeli wakiimba na kucheza kuzunguka ndama wa dhahabu

      SOMO LA 24

      Walivunja Ahadi Yao

      Yehova alimwambia Musa hivi: ‘Njoo kwangu juu mlimani. Nitaandika sheria yangu juu ya mabamba ya mawe halafu nitakupa.’ Musa akapanda juu mlimani na kukaa huko kwa siku 40. Alipokuwa huko, Yehova akaandika zile Amri Kumi juu ya mabamba mawili ya mawe na kumpa Musa mabamba hayo.

      Musa akitupa chini mabamba ya mawe

      Baada ya muda, Waisraeli wakafikiri kwamba Musa alikuwa amewaacha. Wakamwambia Haruni hivi: ‘Tunataka mtu wa kutuongoza. Tutengenezee mungu!’ Haruni akasema: ‘Nipeni dhahabu yenu.’ Akaiyeyusha dhahabu na kuifanya kuwa sanamu ya ndama. Watu wakasema hivi: ‘Huyu ndiye Mungu aliyetutoa Misri.’ Wakaanza kuabudu ndama huyo wa dhahabu na wakafanya sherehe. Je, hilo lilikuwa kosa? Ndiyo, kwa kuwa watu hao walikuwa wameahidi kumtumikia Yehova peke yake. Lakini sasa walikuwa wanavunja ahadi hiyo.

      Yehova aliona kilichokuwa kikitendeka, naye akamwambia Musa hivi: ‘Shuka urudi kwa watu. Wameacha kunitii na wanaabudu mungu wa uwongo.’ Musa akashuka haraka kutoka mlimani, akiwa amebeba yale mabamba mawili.

      Alipoikaribia kambi, Musa akawasikia watu wakiimba. Kisha akawaona wakicheza dansi na kuiinamia sanamu ya ndama. Musa akakasirika sana. Akatupa yale mabamba mawili chini, nayo yakavunjika vipande-vipande. Akaiharibu sanamu hiyo mara moja. Kisha akamuuliza Haruni hivi: ‘Watu hawa walikuambia nini ili ukubali kufanya jambo hili baya?’ Haruni akasema: ‘Usikasirike. Wewe unajua jinsi watu hawa walivyo. Walitaka niwatengenezee mungu, kwa hiyo nikatupa dhahabu yao ndani ya moto na sanamu hiyo ya ndama ikatokea!’ Haruni hakupaswa kufanya hivyo. Musa akarudi juu mlimani na kumsihi Yehova awasamehe watu hao.

      Yehova aliwasamehe wale waliokuwa tayari kumtii. Je, umeona kwa nini ilikuwa muhimu kwa Waisraeli kufuata uongozi wa Musa?

      “Wakati wowote unapoweka nadhiri kwa Mungu, usikawie kuitimiza, kwa maana hapendezwi na wapumbavu. Unapoweka nadhiri, itimize.”​—Mhubiri 5:4

      Maswali: Waisraeli walifanya nini Musa alipokuwa ameondoka? Musa alifanya nini aliporudi?

      Kutoka 24:12-18; 32:1-30

  • Maskani ya Ibada
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Maskani na ua wa maskani

      SOMO LA 25

      Maskani ya Ibada

      Musa alipokuwa kwenye Mlima Sinai, Yehova alimwambia ajenge hema la pekee linaloitwa maskani, ambapo Waisraeli wangemwabudu Mungu. Wangeweza kuibeba maskani waliposafiri.

      Yehova alisema hivi: ‘Waambie watu watoe michango ya kujenga maskani.’ Waisraeli wakatoa dhahabu, fedha, shaba, mawe yenye thamani, na vito. Pia, walitoa sufu, vitambaa vya kitani, ngozi za wanyama, na vitu vingine vingi. Walitoa kwa ukarimu sana hivi kwamba Musa akalazimika kuwaambia hivi: ‘Tumepata michango ya kutosha! Msilete zaidi.’

      Waisraeli wakileta zawadi ili kujenga maskani

      Wanaume na wanawake wengi wenye ustadi walisaidia kujenga maskani. Yehova aliwapa hekima ili waweze kufanya kazi hiyo. Wengine walisokota nyuzi, wakatengeneza mavazi, au wakafanya kazi ya kutarizi. Wengine walifanya kazi kwa kutumia mawe, dhahabu, na mbao.

      Watu wakajenga maskani kama tu Yehova alivyokuwa amewaambia. Wakaweka pazia maridadi ili kutenganisha maskani katika sehemu mbili, Patakatifu na Patakatifu Zaidi. Katika Patakatifu Zaidi kulikuwa na sanduku la agano lililotengenezwa kwa mbao za mshita na dhahabu. Katika Patakatifu kulikuwa na kinara cha taa cha dhahabu, meza, na madhabahu ya kufukiza uvumba. Katika ua kulikuwa na beseni ya shaba na madhabahu kubwa. Sanduku la agano liliwakumbusha Waisraeli kuhusu ahadi yao ya kumtii Yehova. Je, unajua agano ni nini? Ni ahadi ya pekee sana.

      Yehova aliwachagua Haruni na wanawe wafanye kazi kwenye maskani wakiwa makuhani. Walipaswa kuitunza na kumtolea Yehova dhabihu. Ni Haruni peke yake ambaye aliruhusiwa kuingia Patakatifu Zaidi kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa kuhani mkuu. Aliingia humo mara moja kwa mwaka ili kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zake, dhambi za familia yake, na dhambi za taifa lote la Israeli.

      Waisraeli walikamilisha ujenzi wa maskani mwaka mmoja baada ya kutoka Misri. Sasa walikuwa na mahali pa kumwabudu Yehova.

      Yehova akaijaza maskani utukufu wake na akafanya wingu litande juu yake. Wingu lilipoendelea kukaa juu ya maskani, Waisraeli hawakuondoka mahali walipokuwa wamepiga kambi. Lakini wingu lilipoinuka, walijua ni wakati wa kuondoka. Wangebomoa maskani na kufuata wingu hilo.

      “Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.’”​—Ufunuo 21:3

      Maswali: Yehova alimwambia Musa ajenge nini? Yehova aliwapa Haruni na wana wake majukumu gani?

      Kutoka 25:1-9; 31:1-11; 40:33-38; Waebrania 9:1-7

  • Wale Wapelelezi Kumi na Wawili
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Wanaume Waisraeli wakiipeleleza nchi ya Kanaani

      SOMO LA 26

      Wale Wapelelezi Kumi na Wawili

      Waisraeli waliondoka Mlima Sinai na kusafiri kwenye nyika ya Parani hadi eneo linaloitwa Kadeshi. Wakiwa huko, Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Tuma watu 12, mmoja kutoka kila kabila, wakaipeleleze nchi ya Kanaani, nchi nitakayowapa Waisraeli.’ Kwa hiyo, Musa akachagua watu 12 na kuwaambia hivi: ‘Nendeni kwenye nchi ya Kanaani mkachunguze kama inafaa kwa ajili ya kupanda chakula. Angalieni kama watu wa nchi hiyo ni dhaifu au wana nguvu na kama wanaishi katika mahema au majiji.’ Wapelelezi hao 12, kutia ndani Yoshua na Kalebu, wakaenda Kanaani.

      Waisraeli wanalalamika na kuvunjika moyo

      Baada ya siku 40, wapelelezi hao wakarudi, wakiwa na tini, makomamanga, na zabibu. Wapelelezi hao wakasema hivi: ‘Ni nchi nzuri, lakini watu wanaokaa katika nchi hiyo ni wenye nguvu na majiji yake yana kuta ndefu sana.’ Naye Kalebu akasema hivi: ‘Tunaweza kuwashinda. Twendeni mara moja!’ Je, unajua kwa nini Kalebu alisema hivyo? Ni kwa sababu yeye na Yoshua walimtegemea Yehova. Lakini wale wapelelezi wengine kumi wakasema: ‘Hapana! Watu hao ni wakubwa sana, kama majitu! Sisi tulikuwa kama panzi tulipojilinganisha nao.’

      Waisraeli walivunjika moyo. Wakaanza kulalamika na kuambiana hivi: ‘Tuchague kiongozi mwingine ili turudi Misri. Kwa nini twende kwenye nchi hiyo halafu tuuawe?’ Yoshua na Kalebu wakasema hivi: ‘Msimwasi Yehova, wala msiogope. Yehova atatulinda.’ Lakini Waisraeli hawakusikiliza. Hata walitaka kuwaua Yoshua na Kalebu!

      Yehova alifanya nini? Alimwambia Musa hivi: ‘Ingawa nimewafanyia Waisraeli mambo mengi, bado hawanitii. Kwa sababu hiyo watakaa katika nyika hii kwa miaka 40, nao watakufa hapa. Watoto wao, Yoshua, na Kalebu ndio tu watakaoishi katika nchi niliyoahidi kuwapa.’

      “Kwa nini mnaogopa sana, ninyi wenye imani ndogo?”​—Mathayo 8:26

      Maswali: Ni nini kilichotendeka baada ya wapelelezi 12 kurudi kutoka Kanaani? Yoshua na Kalebu walionyeshaje kwamba wanamtegemea Yehova?

      Hesabu 13:1–14:38; Kumbukumbu la Torati 1:22-33; Zaburi 78:22; Waebrania 3:17-19

  • Walimwasi Yehova
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
    • Kora na wanaomuunga mkono wakiwa mbele ya Musa na Haruni

      SOMO LA 27

      Walimwasi Yehova

      Muda fulani baadaye Waisraeli walipokuwa bado nyikani, Kora, Dathani, Abiramu, na watu wengine 250 walimwasi Musa. Walimwambia hivi: ‘Imetosha! Kwa nini wewe uwe kiongozi wetu na Haruni awe kuhani mkuu? Yehova yuko katikati yetu sisi sote, si wewe na Haruni tu.’ Jambo hilo halikumfurahisha Yehova. Aliona kwamba walikuwa wakimwasi yeye!

      Musa akamwambia Kora na watu waliokuwa wakimuunga mkono hivi: ‘Kesho njooni kwenye maskani, na mje na vyetezo vilivyojaa uvumba. Yehova atatuonyesha amemchagua nani.’

      Siku iliyofuata, Kora na wale wanaume 250 wakaenda kukutana na Musa kwenye maskani. Wakafukiza uvumba kana kwamba wao walikuwa makuhani. Yehova akamwambia Musa na Haruni: ‘Jitengeni na Kora na wanaume hawa.’

      Ingawa Kora alikuwa ameenda kukutana na Musa kwenye maskani, Dathani, Abiramu, na familia zao walikataa kwenda. Yehova akawaambia Waisraeli wajitenge na mahema ya Kora, Dathani, na Abiramu. Mara moja, Waisraeli wakajitenga nao. Dathani, Abiramu, na familia zao wakasimama nje ya mahema yao. Ghafla nchi ikapasuka na kuwameza! Kwenye maskani, moto ukashuka na kumteketeza Kora na wale wanaume 250 waliokuwa pamoja naye.

      Ardhi ikipasuka na kuwameza Dathani, Abiramu, na familia zao

      Kisha Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Chukua fimbo moja kutoka kwa kiongozi wa kila kabila, na uandike jina lake juu ya fimbo hiyo. Lakini kwenye fimbo ya kabila la Lawi, uandike jina la Haruni. Uziweke ndani ya maskani, na fimbo ya mtu nitakayemchagua itachipuka maua.’

      Siku iliyofuata, Musa akatoa nje fimbo zote na kuwaonyesha viongozi. Fimbo ya Haruni ilikuwa na maua yanayomea na lozi zilizoiva. Kwa njia hiyo, Yehova akathibitisha kwamba alikuwa amemchagua Haruni kuwa kuhani mkuu.

      “Watiini wale wanaoongoza kati yenu na mnyenyekee.”​—Waebrania 13:17

      Maswali: Kwa nini Kora na wale waliomuunga mkono walimwasi Musa? Tunajuaje kwamba Yehova alimchagua Haruni kuwa kuhani mkuu?

      Hesabu 16:1–17:13; 26:9-11; Zaburi 106:16-18

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki