-
Alifarijiwa na Mungu WakeMnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
-
-
Yehova alishughulikia jinsi gani woga na mahangaiko ya Eliya? Malaika alimwambia Eliya asimame kwenye mlango wa pango. Alitii, bila kujua yale ambayo yangetokea. Ghafla, upepo wenye nguvu ukavuma! Ni lazima upepo huo ulikuwa na kelele kubwa, kwa sababu ulivuma kwa nguvu sana hivi kwamba ulipasua milima na miamba. Hebu wazia Eliya akijaribu kukinga macho yake huku aking’ang’ana kushikilia vazi lake gumu lenye manyoya wakati upepo huo ulipokuwa ukivuma. Pia, alihitaji kuangalia asianguke, kwa kuwa ardhi ilianza kutikisika na kusukasuka kwani eneo hilo lilikumbwa na tetemeko! Kabla hajaelewa vizuri kilichokuwa kikiendelea, moto mkubwa ulipita, ukimlazimisha arudi ndani ya pango ili asiunguzwe na joto kali.—1 Wafalme 19:11, 12.
Katika kila moja ya matukio hayo, simulizi hilo linatuambia kwamba Yehova hakupatikana katika maonyesho hayo yenye kustaajabisha ya nguvu za asili. Eliya alijua kwamba Yehova si kama mungu wa kuwaziwa, kama vile Baali, ambaye alitukuzwa na waabudu wake waliodanganywa kuwa yeye ni “Mwendeshaji wa Mawingu,” au mleta mvua. Yehova ndiye Chanzo halisi cha nguvu zote zisizo na kifani zinazopatikana katika vitu vya asili, lakini pia ni mkuu sana kuliko kitu chochote alichoumba. Hata mbingu haziwezi kumtosha! (1 Wafalme 8:27) Hayo yote yalimsaidia Eliya jinsi gani? Kumbuka kwamba alikuwa na woga. Akiwa na Mungu kama Yehova, mwenye nguvu nyingi sana, Eliya hakupaswa kuwaogopa Ahabu na Yezebeli!—Zaburi 118:6.
Baada ya moto kupita, kimya kilitokea na Eliya akasikia “sauti tulivu, ya chini.” Ilimkaribisha ajieleze tena, naye akafanya hivyo, akieleza mahangaiko yake yote kwa mara ya pili.b Labda hilo lilimtuliza. Bila shaka, Eliya alitulizwa hata zaidi na maneno ambayo ile “sauti tulivu, ya chini” ilifuatia kusema. Yehova alimhakikishia Eliya kwamba alikuwa mwenye thamani sana. Jinsi gani? Mungu alimfunulia mengi kuhusu makusudi yake ya wakati ujao kuhusiana na vita vyake dhidi ya ibada ya Baali nchini Israeli. Kwa wazi, kazi ya Eliya haikuwa ya bure, kwa kuwa makusudi ya Mungu yalikuwa yakitimia bila kuzuiwa. Zaidi ya hayo, Eliya alikuwa na sehemu katika utimizo wa makusudi hayo, kwa kuwa Yehova alimtuma tena, akimpa maagizo hususa.—1 Wafalme 19:12-17.
-
-
Alifarijiwa na Mungu WakeMnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
-
-
b “Sauti tulivu, ya chini” inaweza kuwa ya yule malaika aliyetumiwa kupeleka “neno la Yehova” anayetajwa katika 1 Wafalme 19:9. Mstari wa 15 unamtaja “Yehova” ambaye anawakilishwa na, malaika huyo. Huenda tukakumbuka mjumbe kutoka kwa Yehova ambaye alitumiwa kuwaongoza Waisraeli nyikani na ambaye Mungu alisema hivi kumhusu: “Jina langu limo ndani yake.” (Kutoka 23:21) Bila shaka, hatuwezi kusema kwa hakika kabisa kuhusu hilo, hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba kabla ya kuwa binadamu, Yesu alitumika akiwa “Neno,” Msemaji maalumu wa Yehova kwa watumishi wake.—Yohana 1:1.
-