-
“Agizo la Yehova” Haliwezi KushindwaMnara wa Mlinzi—2004 | Julai 15
-
-
Mataifa Yana Fujo
4. Unawezaje kueleza kwa ufupi mambo makuu katika Zaburi 2:1, 2?
4 Akirejelea matendo ya mataifa na watawala wao, mtunga-zaburi aanza tungo yake kwa kuimba: “Kwa nini mataifa yamekuwa na fujo na vikundi vya mataifa vimeendelea kusema jambo la upuuzi? Wafalme wa dunia wanachukua msimamo wao nao maofisa wakuu wamejikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.”—Zaburi 2:1, 2.a
5, 6. Ni ‘jambo gani la upuuzi’ ambalo “vikundi vya mataifa vimeendelea kusema”?
5 Ni ‘jambo gani la upuuzi’ ambalo vikundi vya mataifa ‘vimeendelea kusema’? Badala ya kumkubali Mtiwa-Mafuta wa Mungu, yaani, Masihi au Kristo, mataifa ‘yameendelea kusema,’ au kutafakari juu ya kuendeleza mamlaka yao. Maneno hayo ya zaburi ya pili pia yalitimizwa katika karne ya kwanza W.K., wakati wenye mamlaka Waroma na Wayahudi waliposhirikiana kumuua Mfalme-Mteuliwa wa Mungu, Yesu Kristo. Hata hivyo, utimizo ulio mkuu ulianza 1914 wakati Yesu alipowekwa kuwa Mfalme wa kimbingu. Tangu wakati huo, hakuna serikali yoyote duniani ambayo imemtambua Mfalme wa Mungu aliyetawazwa.
6 Ni nini maana ya swali hili la mtunga-zaburi: ‘Kwa nini vikundi vya mataifa vimekuwa vikisema jambo la upuuzi’? Kusudi la vikundi hivyo ndilo la upuuzi; ni la ubatili na halitafanikiwa. Haviwezi kuleta amani na upatano duniani. Na bado, vinafikia kiwango cha kuupinga utawala wa Mungu. Kwa kweli, vimechukua msimamo wa pamoja wenye uhasama, navyo vimejikusanya pamoja kumpinga Aliye Juu Zaidi na Mtiwa-Mafuta wake. Huo ni upumbavu ulioje!
Mfalme wa Yehova Mwenye Ushindi
7. Wafuasi wa mapema wa Yesu walitumiaje Zaburi 2:1, 2 katika sala?
7 Wafuasi wa Yesu walitumia maneno ya Zaburi 2:1, 2 kumhusu. Walipoteswa kwa ajili ya imani yao, walisali hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu [Yehova], wewe Ndiye uliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo, na ambaye kupitia roho takatifu ulisema kwa kinywa cha babu yetu Daudi, mtumishi wako, ‘Kwa nini mataifa yakawa yenye fujo na vikundi vya watu vikatafakari juu ya mambo matupu? Wafalme wa dunia walichukua msimamo wao nao watawala wakajikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.’ Ijapokuwa hivyo, Herode [Antipasi] na pia Pontio Pilato pamoja na watu wa mataifa na pamoja na vikundi vya watu wa Israeli kwa kweli walikusanyika pamoja katika jiji hili dhidi ya mtumishi wako mtakatifu Yesu, ambaye ulimtia mafuta.” (Matendo 4:24-27; Luka 23:1-12)b Ndiyo, katika karne ya kwanza kulikuwa na njama dhidi ya Yesu, mtumishi wa Mungu aliyetiwa mafuta. Hata hivyo, zaburi hiyo ingetimizwa tena karne nyingi baadaye.
8. Zaburi 2:3 inahusuje mataifa ya siku hizi?
8 Waisraeli wa kale walipokuwa na mfalme wa kibinadamu, kama Daudi, mataifa na watawala wapagani walikusanyika pamoja dhidi ya Mungu na mtiwa-mafuta wake aliyetawazwa. Lakini namna gani wakati wetu? Mataifa ya siku hizi hayataki kutimiza matakwa ya Yehova na Masihi. Hivyo, yanaonyeshwa yakisema: “Na tuzikate pingu zao na kuzitupa kamba zao mbali nasi!” (Zaburi 2:3) Watawala na mataifa wangepinga vizuizi vyovyote vinavyowekwa na Mungu na Mtiwa-Mafuta wake. Bila shaka, jitihada zozote za kukata pingu hizo na kutupa kamba hizo hazitafanikiwa.
-
-
“Agizo la Yehova” Haliwezi KushindwaMnara wa Mlinzi—2004 | Julai 15
-
-
a Mwanzoni, Mfalme Daudi ndiye aliyekuwa “mtiwa-mafuta,” nao “wafalme wa dunia” walikuwa watawala Wafilisti waliojikusanya pamoja dhidi yake.
b Maandishi mengine katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pia yanaonyesha kwamba Yesu ndiye Mtiwa-Mafuta wa Mungu anayetajwa katika zaburi ya pili. Jambo hilo linakuwa wazi tunapolinganisha Zaburi 2:7 na Matendo 13:32, 33 na Waebrania 1:5; 5:5. Ona pia Zaburi 2:9 na Ufunuo 2:27.
-