Mfurahieni Yehova na Kushangilia
SIKUZOTE, kukamilishwa kwa mradi wowote ule wenye manufaa huwa ni pindi ya kushangilia. Kwa hakika, shughuli ya kuhitimu iliyofanywa Machi 13, 1999, katika Kitovu cha Kielimu cha Watchtower huko Patterson, New York, ilikuwa pindi yenye shangwe kwa wale wanafunzi 48 wa darasa la 106 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower.
Maneno ya kufungua ya Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, mhitimu wa darasa la saba la Gileadi, na pia mwenyekiti wa programu ya kuhitimu, yalikazia maneno ya Zaburi 32:11: “Mfurahieni BWANA [“Yehova,” NW]; shangilieni, enyi wenye haki.” Akieleza kwa nini yafaa wote washangilie kwenye pindi hiyo, alisema hivi: “Twashangilia kwenye pindi kama hii kwa sababu ya mambo ambayo Yehova anatimiza akitumia watu walio wanyofu wa moyo, kutia ndani wanafunzi wetu wa Gileadi.” Ingawa wanafunzi walifanya mipango ili wahudhurie Shule ya Gileadi, nao walijitahidi kwa bidii ili wastahili utumishi wa mishonari, Yehova ndiye aliyewezesha mambo yote yakamilike kwa mafanikio. (Mithali 21:5; 27:1) Ndugu Jaracz alikazia kwamba hiyo ndiyo sababu ya ‘kumfurahia Yehova.’
Washiriki wa familia za wanafunzi na wageni wao waliotoka nchi 12 walikuwa miongoni mwa watu waliokuwa kwenye ukumbi wa Patterson ili kushuhudia pindi hiyo yenye shangwe. Wahudhuriaji 5,198—pamoja na washiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn, ya Patterson, na ya Wallkill, waliosikiliza na kuona kupitia televisheni—walipokuwa wakingojea programu kwa hamu, ilikuwa dhahiri kwamba roho yenye shangwe ilienea kotekote.
Wahimizwa Wadumishe Roho ya Shangwe
Ndugu Jaracz alipokuwa akimalizia maneno yake ya kufungua, alimkaribisha msemaji wa kwanza kati ya watano, waliokuwa wametayarisha shauri la Kimaandiko lenye kutia moyo wenye kuhitimu na pia wahudhuriaji.
Msemaji wa kwanza alikuwa William Malenfant, mhitimu wa darasa la 34 la Gileadi, ambaye sasa anatumikia kwenye Halmashauri ya Kufundisha ya Baraza Linaloongoza akiwa msaidiaji. Kuhusiana na kichwa chake “‘Mambo Yote’ Si Ubatili!” kinachotegemea Mhubiri 1:2, alizusha swali hili: “Je, kwa kweli Solomoni alimaanisha kwamba mambo yote, kwa maana kamili ya neno hilo, ni ubatili?” Akajibu: “La. Alikuwa akimaanisha kwamba kazi za binadamu zinazopuuza mapenzi ya Mungu, ufuatiaji usiotia ndani mapenzi ya Mungu—mambo hayo yote ni ubatili.” Kinyume cha hilo, si ubatili kumwabudu Mungu wa kweli, Yehova; wala si ubatili kujifunza na kuwafundisha wengine Neno la Mungu, Biblia. Mungu hasahau jitihada hizo zinazofanywa na watumishi wake. (Waebrania 6:10) Kwa hakika, hata maafa yakiwapata wale wanaopendelewa na Mungu, wao “[wa]tafungwa katika furushi ya uhai pamoja na BWANA.” (1 Samweli 25:29) Jambo hilo lapendeza kama nini! Kukumbuka mambo hayo kwaweza kuwasaidia waabudu wote wa Yehova kudumisha roho yenye shangwe.
John Barr, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alilitia moyo darasa lenye kuhitimu kwa hotuba yake “Pendezwa na Mgawo Wako wa Umishonari.” Alionyesha kuwa utumishi wa mishonari ni jambo ambalo Yehova Mungu amelithamini sikuzote. “Ni jambo ambalo lilikuwa sehemu muhimu ya jinsi ambavyo Yehova alionyesha upendo wake kwa ulimwengu. Alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee aje duniani. Yesu alikuwa mishonari mkuu kuliko wote.” Ingawa wenye kuhitimu wangeweza kuchanganua kwa makini mabadiliko ambayo Yesu alipaswa kufanya ili afanikiwe katika kazi yake duniani, manufaa ya utumishi wa mishonari wa Yesu yangali yapatikana kwa wote wanaoamua kuyatumia kwa faida yao. Kwa sababu, kama alivyosema Ndugu Barr, Yesu alipendezwa na kufanya kazi ya Mungu, naye aliwapenda wanadamu pia. (Mithali 8:30, 31) Ndugu Barr aliwasihi wenye kuhitimu wadumu katika migawo yao, si kwa kuvumilia tu, bali kwa sababu wanapenda kufanya hivyo. “Mtegemee Yehova; naye hatakuacha,” akasihi darasa hilo.—Zaburi 55:22.
Msemaji aliyefuata, Lloyd Barry, mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza, alichagua kichwa, “Kutembea Katika Jina la Yehova Milele.” Ndugu Barry, aliyetumikia hapo awali akiwa mishonari kwa zaidi ya miaka 25 nchini Japani baada ya kumaliza darasa la 11 la Gileadi, alisimulia mambo kadhaa yaliyoonwa ya baadhi ya wamishonari wa mapema na kusimulia magumu waliyolazimika kukabili. Je, ni shauri gani lenye kutumika alilotolea darasa lenye kuhitimu? “Zaidi ya mambo yote, dumisheni hali yenu ya kiroho. Pia, jifunzeni lugha na utamaduni. Dumisheni ucheshi wenu. Nanyi mdumu katika kazi; msiwe wanyong’onyevu wala msichoke kabisa.” Ndugu Barry aliwaambia wenye kuhitimu kwamba kwenye migawo yao katika nchi za kigeni, watakutana na watu wengi wanaotembea katika jina la miungu mbalimbali, naye akawakumbusha juu ya maneno haya ya Mika: “Mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake, na sisi tutakwenda kwa jina la BWANA [“Yehova,” NW], Mungu wetu, milele na milele.” (Mika 4:5) Bila shaka kielelezo cha wamishonari wa zamani ni kichocheo kikubwa kwa watumishi wote wa Mungu ili waendelee kutembea katika jina la Yehova na kumtumikia kwa uaminifu.
Aliyefuatia kwenye programu ni mfunzi wa Gileadi, Lawrence Bowen. Kichwa cha hotuba yake kilizusha swali, “Wewe Utathibitika Kuwa Nani?” Alionyesha kwamba kupata mafanikio katika utumishi wa Mungu hutegemea kuwa na imani na tumaini katika Yehova. Mfalme Asa alipomtegemea Yehova kabisa, alipata ushindi mkubwa dhidi ya jeshi la adui lenye watu milioni moja. Ingawa hivyo, alikumbushwa na nabii Azaria juu ya uhitaji wa kuendelea kumtegemea Mungu: “BWANA yu pamoja nanyi, mkiwa pamoja naye.” (2 Mambo ya Nyakati 14:9-12; 15:1, 2) Kwa kuwa jina la Mungu, Yehova, lina maana ya kwamba yeye huthibitika kuwa chochote kile kihitajiwacho ili kutimiza kusudi lake—iwe yamaanisha kuwa Mwandaaji, Mlindaji, au hata Mfishaji—wamishonari wanaomtegemea Yehova na kufanya kazi kupatana na kusudi lake watafanikiwa katika migawo yao. (Kutoka 3:14) “Msisahau kamwe,” Ndugu Bowen akamalizia, “kwamba maadamu mwalifanya kusudi la Yehova kuwa kusudi lenu, atawafanya mwe chochote kihitajiwacho ili kutimiza mgawo wenu.”
Msemaji wa mwisho katika sehemu hiyo ya programu alikuwa Wallace Liverance, aliyekuwa mishonari hapo awali na sasa ni msajili wa shule hiyo. Hotuba yake yenye kichwa “Dumisheni Neno la Mungu Likiwa Hai na Lenye Kutenda Kazi Ndani Yenu,” ilikazia ujumbe wa Mungu, au ahadi yake isiyoweza kushindwa na ambayo husonga mbele daima kuelekea ukamilisho. (Waebrania 4:12) Neno la Mungu hubadili maisha ya wale wanaolikubali. (1 Wathesalonike 2:13) Neno hilo laweza kudumishwaje likiwa hai na lenye kutenda kazi maishani mwetu? Kupitia funzo la Biblia lenye bidii. Ndugu Liverance aliwakumbusha wenye kuhitimu juu ya mbinu za kujifunza Biblia walizojifunza katika Gileadi, zilizotia ndani kusoma na kufafanua maana na matumizi ya Neno la Mungu. Alinukuu maneno ya Albert Schroeder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza aliyetumikia akiwa mwenyekiti wa halmashauri iliyoanzisha Shule ya Gileadi zaidi ya miaka 50 iliyopita: “Kwa kutumia muktadha, mtu aweza kupata nguvu kamili, iliyo sahihi, ya roho inayoandaliwa na Mungu katika Neno lake.” Mtindo huo wa kujifunza Biblia hudumisha Neno la Mungu likiwa hai na lenye kutenda kazi.
Mambo Yaliyoonwa na Mahojiano Yenye Shangwe
Baada ya hotuba hizo, wahudhuriaji waliburudishwa kwa mambo yaliyoonwa kadhaa yenye shangwe yaliyosimuliwa na wanafunzi. Kikundi cha wanafunzi, kikielekezwa na Mark Noumair, aliyekuwa mishonari hapo awali na sasa ni mfunzi wa Gileadi, kilionyesha jinsi walivyojitahidi kutoa ushahidi katika hali mbalimbali. Baadhi yao walifaulu kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia na watu katika eneo kwa kuangalia kwa makini hali mbalimbali na usemi wa watu, na kwa kupendezwa nao kibinafsi. Kwa hiyo wanafunzi hao ‘walikuwa wakikazia uangalifu kwao wenyewe na kwa kufundisha kwao,’ nao walipendezwa kikweli kuwasaidia wengine wapate wokovu.—1 Timotheo 4:16.
Madokezo mengi yenye kutumika yalitolewa, na shangwe ya utumishi wa mishonari ilionyeshwa wazi na ndugu kadhaa wenye ujuzi waliokuwa wakizoezwa katika shule ya washiriki wa halmashauri ya tawi iliyofanyiwa katika Kitovu cha Kielimu cha Watchtower. Ndugu Samuel Herd na Robert Johnson wa makao makuu waliongoza mahojiano yenye uchangamfu wakiwa na wawakilishi kutoka katika ofisi ya tawi ya Bolivia, Zimbabwe, Nikaragua, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Dominika, Papua New Guinea, na Kamerun.
Baada ya mambo yaliyoonwa na mahojiano, Gerrit Lösch, aliyehitimu katika darasa la 41 la Gileadi, ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya mwisho juu ya kichwa hiki chenye kuamsha fikira “Je, Wewe Ni ‘Mtu Upendwaye’?” Kwanza, Ndugu Lösch aliwakumbusha wenye kuhitimu kwamba Yesu, Mwana mkamilifu wa Mungu, hakupendwa na watu, bali “alidharauliwa na kukataliwa na watu.” (Isaya 53:3) Kwa hiyo haishangazi kwamba katika sehemu nyingi za ulimwengu leo, wamishonari huonwa kuwa watu wasiokubalika, wala kukaribishwa. Kwa upande mwingine, mara tatu kupitia malaika, Muumba alimwita Danieli “upendwaye sana” katika kile kipindi cha miaka mingi Danieli alipokuwa akitumikia huko Babiloni. (Danieli 9:23; 10:11, 19) Ni nini kilichomfanya Danieli awe hivyo? Hakuridhiana kamwe kanuni za Biblia alipokuwa akifanya mabadiliko ili kufaana na utamaduni wa Babiloni; alikuwa mwaminifu katika mambo yote, pasipo kamwe kutumia cheo chake kupata manufaa ya kibinafsi; naye alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu. (Danieli 1:8, 9; 6:4; 9:2) Pia alisali kwa Yehova kwa ukawaida, naye hakusita kamwe kumpa Mungu utukufu kwa matimizo yake. (Danieli 2:20) Watumishi wa Mungu, wakifuata kielelezo cha Danieli, waweza kuthibitika kuwa wapendwao, si lazima wapendwe na ulimwengu, bali na Yehova Mungu.
Akimalizia programu hiyo yenye kujenga kiroho, mwenyekiti alisoma baadhi ya telegramu na jumbe zilizotoka sehemu mbalimbali ulimwenguni. Kisha, wenzi wa ndoa zote 24 wakapokea diploma zao, na nchi ambayo waligawiwa ikatangazwa. Hatimaye, mwakilishi wa darasa alisoma barua iliyoandikiwa Baraza Linaloongoza na familia ya Betheli, ikionyesha shukrani ambazo darasa lilitoa kwa ajili ya mazoezi na matayarisho waliyokuwa wamepata katika miezi mitano iliyopita.
Programu ilipokuwa ikifikia mwisho, ‘furaha pamoja na shukrani’ zingeweza kusikiwa miongoni mwa umati uliokuwa ukiondoka.—Nehemia 12:27.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Takwimu za Darasa
Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 10
Idadi ya nchi walikogawiwa: 19
Idadi ya wanafunzi: 48
Idadi ya wenzi wa ndoa: 24
Wastani wa umri: 33
Wastani wa miaka katika kweli: 16
Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13
[Picha katika ukurasa wa 25]
Darasa la 106 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower
Katika orodha ifuatayo, nambari za safu zaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.
(1) Deakin, D.; Puopolo, M.; Laguna, M.; Davault, S.; Dominguez, E.; Burke, J. (2) Gauter, S.; Vazquez, W.; Seabrook, A.; Mosca, A.; Helly, L.; Breward, L. (3) Brandon, T.; Olivares, N.; Coleman, D.; Scott, V.; Petersen, L.; McLeod, K. (4) McLeod, J.; Thompson, J.; Luberisse, F.; Speta, B.; Lehtimäki, M.; Laguna, J. (5) Gauter, U.; Dominguez, R.; Helly, F.; Smith, M.; Beyer, D.; Mosca, A. (6) Scott, K.; Seabrook, V.; Speta, R.; Coleman, R.; Breward, L.; Davault, W. (7) Smith, D.; Lehtimäki, T.; Petersen, P.; Thompson, G.; Vazquez, R.; Beyer, A. (8) Luberisse, M.; Deakin, C.; Brandon, D.; Puopolo, D.; Olivares, O.; Burke, S.