Kuifunua Wazi Sura ya Yule Nyoka
“llikuwa, siku moja ambayo hao wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha mbele za BWANA [Yehova, NW], Shetani naye akaenda kati yao.”—AYUBU 1:6.
1. (a) Ni nini awali na maana ya jina “Shetani”? (b) Neno “Shetani” linaonekana mara ngapi katika Maandiko, na ni maswali gani yanayotokea?
NI NINI awali ya jina Shetani? Hilo linamaanisha nini? Katika mazingira yalo ya Kibiblia, limefanyizwa kutokana na herufi tatu za Kiebrania ש (Sin), ט (Tehth), נ (Nun). Kwa kutumia nukta za vokali zazo, herufi hizi zinafanyiza neno “Shetani,” ambalo, kulingana na mwana-chuo Edward Langton, “limetolewa kutokana na mzizi unaomaanisha ‘kupinga,’ au ‘kuwa au kutenda kama mpinzani.’” (Linganisha 1 Petro 5:8, NW.) Ingawa jina “Shetani” linaonekana kama mara 52 katika Biblia, hilo linatukia mara 18 tu katika Maandiko ya Kiebrania na hapo tena ni katika vitabu vya 1 Nyakati, Ayubu, na Zekaria. Kwa hiyo maswali yanatokea, Ni lini mwanadamu alipokuja kufahamu juu ya uasi na utendaji wa Shetani? Ni lini Shetani anapofunuliwa wazi mara ya kwanza katika Maandiko ya Kiebrania?
2. Ni swali gani lililotokea baada ya uasi wa Adamu na Hawa?
2 Biblia inaeleza kwa njia rahisi lakini yenye maarifa ya kina kirefu juu ya jinsi dhambi na uasi zilivyokuja kuwako duniani, katika iliyokuwa bustani ya kiparadiso katika Mashariki ya Kati. (Ona Mwanzo sura 2 na 3.) Ingawa mwendelezaji wa kutotii kwa Adamu na Hawa anatambulishwa kuwa nyoka, hakuna kidokezi cha mara hiyo kinachotolewa kuonyesha ni nani aliyekuwa yule mwenye nguvu na ueledi ambaye hasa ndiye aliyechochea sauti iliyotokezwa na nyoka yule. Hata hivyo, Adamu alikuwa na wakati mrefu wa kuyafikiria katika Edeni matukio yaliyoongoza kwenye kufukuzwa kwake kutoka bustani hiyo ya kiparadiso.—Mwanzo 3:17, 18, 23; 5:5.
3. Ingawa hakudanganywa, ni jinsi gani Adamu alitenda dhambi, na tokeo lilikuwa nini kwa aina ya kibinadamu?
3 Ni wazi kwamba Adamu alijua kuwa wanyama hawaneni wakiwa na ueledi wa kibinadamu. Yeye alijua pia kwamba Mungu hakuwa amenena kwake kupitia mnyama ye yote kabla ya kishawishi cha Hawa. Kwa hiyo ni nani aliyekuwa ameambia mke wake kutotii Mungu? Paulo alisema kwamba hata ingawa mwanamke alidanganywa kweli kweli, Adamu hakudanganywa. (Mwanzo 3:11-13, 17; 1 Timotheo 2:14) Labda Adamu aling’amua kwamba kiumbe fulani asiyeonekana alikuwa akitoa njia tofauti ya kufanya mambo badala ya kutii Mungu. Hata hivyo, ingawa yeye mwenyewe hakufikiwa na yule nyoka, yeye alichagua kufuatana pamoja na mke wake katika kutotii. Kitendo cha kutotii kwa Adamu kwa makusudi na kwa kujipendea mwenyewe kilivunja ule mfinyango wa ukamilifu, kikatokeza ile kasoro ya dhambi, na kuongoza kwenye shutumu la kifo lililotabiriwa. Na hivyo, akitumia uwakilisho wa nyoka, Shetani akawa ndiye mwuaji wa hapo awali.—Yohana 8:44; Warumi 5:12, 14.
4, 5. (a) Ni hukumu gani ya kiunabii iliyopewa dhidi ya nyoka? (b) Ni vitendawili gani vilivyohusishwa na unabii huo?
4 Uasi katika Edeni ulitokeza hukumu ya kiunabii kutoka kwa Mungu. Hukumu hiyo ilihusisha ndani “siri takatifu” ambayo maelfu ya miaka yangehitajiwa ili kuifumbua kabisa. Mungu alisema hivi kwa nyoka: “Mimi nitaweka uadui kati ya wewe na yule mwanamke na kati ya mbegu yako na mbegu yake. Huyo aliye wa kiume atakuponda wewe katika kichwa na wewe utamponda katika kisigino.”—Waefeso 5:32; Mwanzo 3:15, NW.
5 Unabii huo muhimu unaingiza ndani vitendawili kadhaa. Ni nani kwa kweli aliyemaanishwa na “yule mwanamke”? Je! ilikuwa ni Hawa, au ilikuwa ni mwanamke wa ufananisho aliye wa umaana mkubwa zaidi ya Hawa? Pia, ni nini kilichomaanishwa na ‘mbegu ya mwanamke’ na ‘mbegu ya nyoka’? Na ni nani kwa kweli aliyekuwa “nyoka” ambaye mbegu yake ingekuwa kwenye uadui pamoja na mbegu ya mwanamke? Kama vile tutakavyozungumzia baada ya muda mfupi, kwa uwazi Yehova aliamua kwamba maswali hayo yangepata jibu kamili zaidi katika wakati unaofaa.—Linganisha Danieli 12:4 na Wakolosai 1:25, 26.
Ithibati Zaidi ya Uasi Katika Mbingu
6. Ni nini kionyeshi kilichofuata cha kwamba kulikuwa na uasi katika mbingu?
6 Wakati historia ya Biblia inapoendelea-endelea, kinafunuliwa kionyeshi kingine cha kwamba uasi ulitokea kwenye kiwango cha maisha yaliyo juu zaidi ya yale ya wanadamu muda mfupi tu kabla ya Gharika, kama miaka 1,500 baada ya kuanguka kwa mwanadamu ndani ya dhambi. Usimulizi wa Biblia unatuambia kwamba “wana wa Mungu wa kweli walianza kutanabahi binti za wanadamu, kwamba wao walikuwa wenye sura nzuri; na wao wakaenda wakijichukulia wake kwa ajili yao wenyewe, yaani, wote ambao wao walichagua.” Wazao mahuluti wa miungano hiyo isiyo ya kiasili walijulikana kuwa “Wanefili” walio “wenye uweza ambao walikuwa wa zamani, wale wanaume wenye umaarufu.” (Mwanzo 6:1-4, NW; linganisha Ayubu 1:6 ili upate utambulisho juu ya “wana wa Mungu wa kweli.”) Kama miaka 1,600 baadaye Yuda alitoa elezo fupi juu ya tukio hili alipoandika hivi: “Na malaika ambao . . . waliacha makao yao wenyewe yanayofaa amewaweka akiba wakiwa katika vifungo vya milele chini ya giza zito mno kwa ajili ya hukumu ya ile siku kubwa.”—Yuda 6; 2 Petro 2:4, 5, NW.
7. Ujapokuwako ubaya wa mwanadamu, ni ukosefu gani wenye kuamsha udadisi ambao tunapata katika vingi vya vitabu vya kihistoria vya Biblia?
7 Lakini, hata penye hatua hii ya kabla ya Gharika ambapo ‘maovu ya mwanadamu yalikuwa makubwa duniani na kila kusudi alilowaza moyoni mwake lilikuwa baya tu sikuzote,’ katika kitabu cha Mwanzo chenye uvuvio Shetani hakutambulishwa wazi kuwa ndiye ule uvutano wenye nguvu nyingi uliochochea uasi wa kimalaika na uovu wa mwanadamu. (Mwanzo 6:5) Na muda wote wa historia ya mataifa ya Israeli na Yuda, yenye kurudi-rudi daima kuingia katika ibada ya sanamu na ibada bandia, Shetani hatajwi kamwe katika vitabu vya Biblia vilivyovuviwa vya Waamuzi, Samweli, na Wafalme kuwa ndiye ule uvutano usioonekana uliochochea matukio hayo, hata ingawa yeye alikuwa ‘akizunguka-zunguka duniani.’—Ayubu 1:7; 2:2.
8. Je! hapo kwanza Ayubu alikuwa na habari juu ya sehemu iliyotimizwa na Shetani katika mteseko wake? Tunajua hivyo jinsi gani?
8 Hata wakati tunapofikiria ule usimulizi ulio wa maana sana wa Ayubu na majaribu yake, tunaona kwamba Ayubu hamhesabii kamwe mpinzani huyo, Shetani, sifa ya kuyasababisha. Inaonekana kwamba wakati huo yeye hakuwa na habari ni suala gani lililotegemea tokeo la mwenendo wake. (Ayubu 1:6-12) Yeye hakung’amua kwamba Shetani alikuwa ameporomosha jambo hilo la umaana mkuu kwa kushtaki ukamilifu wa Ayubu mbele za Yehova. Hivyo, wakati mke wa Ayubu alipomkemea rasmi kwa maneno haya, “Bado wewe unaushika imara ukamilifu wako? Laani Mungu na ufe!”, yeye alijibu kwa urahisi tu, “Je! sisi tukubali kilicho chema tu kutoka kwa Mungu wa kweli na tusikubali pia kilicho kibaya?” Akiwa hajui chanzo cha kweli cha majaribu yake, inaonekana yeye aliyaona kuwa yenye kutoka kwa Mungu na kuwa yalipasa kukubaliwa. Kama yasingalikuwa hivyo yasingalikuwa mtihani wa kweli wa ukamilifu wa Ayubu.—Ayubu 1:21; 2:9, 10, NW.
9. Ni swali gani la kadiri inayofaa linaloweza kutokezwa kuhusu Musa?
9 Sasa swali linatokea. Ikiwa, kama vile sisi tunavyoitikadi, Musa ndiye aliyeandika kitabu cha Ayubu na kwa hiyo alijua kwamba Shetani alikuwa akizunguka-zunguka duniani, imekuwaje yeye haneni juu ya Shetani kwa kumtaja jina katika cho chote cha vile vitabu vya Pentateuki, ambavyo ni yeye pia aliyeviandika? Naam, kwa nini Shetani anatajwa mara chache sana katika Maandiko ya Kiebrania?a
Kule Kufichuliwa Kidogo tu kwa Shetani
10. Ni jinsi gani Shetani alivyofichuliwa kidogo tu katika Maandiko ya Kiebrania?
10 Hata ingawa alikuwa anatoa malawama ya wazi juu ya utendaji wenye kuvuviwa na roho wabaya, inaonekana kwamba kwa hekima yake Yehova alikuwa na sababu nzuri za kuhakikisha kwamba Mpinzani wake, Shetani, alipaswa kufichuliwa kidogo tu katika Maandiko ya Kiebrania. (Walawi 17:7; Kumbukumbu 18:10-13; 32:16, 17; 2 Nyakati 11:15) Hivyo, ingawa ni lazima iwe kwamba waandikaji Waebrania walikuwa na maarifa ya kadiri fulani juu ya shetani na fungu lake la uasi katika mbingu, wao walivuviwa ili wafafanue na kufichua dhambi za watu wa Mungu na za mataifa yaliyowazunguka tu na kuhimiza dhidi ya uovu wayo. Jina la Shetani lilitajwa mara haba.—Kutoka 20:1-17.
11, 12. Ni jinsi gani sisi tunajua kwamba waandikaji Waebrania wa Biblia hawakukosa kujua juu ya Shetani na uvutano wake?
11 Kulingana na matukio yaliyotukia Edeni, na kuharibika tabia kwa “wana wa Mungu wa kweli,” na yale maandishi ya kikumbukumbu katika kitabu cha Ayubu, waandikaji Waebrania wa Biblia waliovuviwa hawakukosa maarifa juu ya ule uvutano mwovu wa Shetani, unaozidi nguvu za mwanadamu wa kiasili. Nabii Zekaria, aliyeandika mwishoni-mwishoni mwa karne ya sita K.W.K., alipata njozi juu ya kuhani mkuu Yoshua na “Shetani akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume ili kumkinza. Ndipo malaika wa Yehova akasema kwa Shetani hivi: ‘Yehova akukemee wewe, O Shetani, ndiyo, Yehova, akukemee wewe.’” (Zekaria 3:1, 2, NW) Pia, mwandishi Ezra, akiandika historia ya Israeli na Yuda katika karne ya tano K.W.K., alitaarifu kwamba ‘Shetani alisimama juu ya Israeli, akamshawishi Daudi kuwahesabu Israeli.’—1 Nyakati 21:1.
12 Hivyo, kufikia wakati wa Zekaria, roho takatifu ilikuwa ikiacha fungu analotimiza Shetani liwe wazi zaidi katika Maandiko. Lakini karne nyingine tano zingepita kabla ya kiumbe huyu mwovu kufichuliwa wazi kabisa katika Neno la Mungu. Tukiwa na msingi wa Biblia, tunaweza kufikia-fikiaje kuamua ni sababu gani iliyofanya kufichuliwa kabisa kwa Shetani kupangiwe muda huo?
Ufunguo wa Kutegua Kitendawili Hicho
13-15. (a) Ni kweli gani za msingi zilizo ufunguo wa kuelewa ni kwa nini Shetani alifichuliwa kidogo tu katika Maandiko ya Kiebrania? (b) Yesu alipokuja, ni jinsi gani Shetani alitokezwa peupe?
13 Kwa Mkristo aliye na imani katika Neno la Mungu, ufunguo wa msingi kwa maswali hayo na yale ambayo tumetangulia kutokeza haupatikani katika uchambuzi wa juu zaidi, kama kwamba Biblia ni kitabu tu cha maarifa makuu, kilichotokezwa kwa umahiri wa kibinadamu tu. Ufunguo wenyewe unafunuliwa katika kweli mbili za kimsingi za Biblia. Kwanza, kama vile Mfalme Sulemani alivyoandika, “Kijia cha waadilifu ni kama nuru nyangavu ambayo inaendelea kunurika zaidi na kunurika zaidi mpaka ile siku ipate kuthibitishwa kwa imara.” (Mithali 4:18; linganisha Danieli 12:4; 2 Petro 1:19-21, NW.) Ukweli unafunuliwa pole kwa pole katika Neno la Mungu kwenye wakati wa Mungu, kwa kupatana na uhitaji na uwezo wa watumishi wake wa kuufyonza ukweli huo akilini,—Yohana 16:12, 13; linganisha Yohana 6:48-69.
14 Ukweli wa pili ulio wa msingi umo katika yale ambayo mtume Paulo aliandikia Timotheo mwanafunzi Mkristo: “Andiko lote ni lenye kuvuviwa na Mungu na lina manufaa kwa kufundisha, . . . ili mtu wa Mungu apate kuwa na uwezo wa kutosha, aliye tayari kabisa kwa kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17, NW) Mwana wa Mungu, Yesu, angemfichua Shetani na jambo hilo lingetiwa kumbukumbuni katika Andiko, hivyo akitolea kundi la Kikristo habari za kulitayarisha kusimama imara dhidi ya Shetani kwa kuunga mkono enzi kuu ya Yehova.—Yohana 12:28-31; 14:30.
15 Kwa kutegemea misingi hiyo, vile vitendawili vya Mwanzo 3:15 vimeondolewa polepole kile kisetiri chenye kuvificha. Chini ya mwelekezo wa roho takatifu ya Mungu, au kani ya utendaji, Maandiko ya Kiebrania yalitoa vimulimuli vya nuru kuhusu yule Mesiya, au Mbegu, mwenye kuja. (Isaya 9:6, 7; 53:1-12) Kwa usambamba na jambo hilo, maandiko hayo yamekuwa kwa muda mfupi na mifyatuko-fyatuko ya nuru juu ya fungu ambalo Shetani anatimiza akiwa Mpinzani wa Mungu na adui ya aina ya kibinadamu. Lakini Yesu alipokuja, Shetani alitokezwa peupe kabisa kwa kuwa alichukua hatua ya kufanya ufidhuli wa wazi na wa moja kwa moja dhidi ya ile “mbegu” iliyoahidiwa, Yesu Kristo. Matukio yalipokuwa yakiendelea-endelea kufunuka katika hiyo karne ya kwanza ya muda wa kipindi cha Kikristo, fungu lenye kutimizwa na “yule mwanamke,” tengenezo la Yehova la roho wa kimbingu, na ile “mbegu,” Yesu Kristo, lilieleweshwa wazi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Wakati uo huo, fungu lenye kutimizwa na Shetani, “yule nyoka wa awali,” lilitokezwa peupe kwa ukamili zaidi.—Mathayo 4:1-11; Wagalatia 3:16, 4:26; Ufunuo 12:1-9, NW.
Siri Takatifu Yaondolewa Kisetiri
16, 17. “Ile siri takatifu ya Kristo” ilihusisha nini ndani?
16 Mtume Paulo aliandika kwa wingi juu ya “ile siri takatifu ya Kristo.” (Waefeso 3:2-4; Warumi 11:25; 16:25, NW) Hii siri takatifu ilihusika na “mbegu” ya kweli ambayo mwishowe ingeponda-ponda yule nyoka wa awali, Shetani Ibilisi. (Ufunuo 20:1-3, 10) Siri hiyo ilihusisha ndani uhakika wa kwamba Yesu alikuwa ndiye mshiriki wa kwanza na wa kimsingi wa Mbegu hiyo, lakini kwamba angeungwa na wengine, “warithi waungani,” kwanza kutokana na Wayahudi halafu kutokana na Wasamaria na watu wasio Wayahudi, ili kukamilisha ile hesabu ya mbegu hiyo.—Warumi 8:17; Wagalatia 3:16, 19, 26-29; Ufunuo 7:14; 14:1.
17 Paulo anaeleza hivi: “Katika vizazi vingine siri hii haikujulishwa kwa wana wa wanadamu kama vile ambavyo sasa imefunuliwa kwa mitume watakatifu wake na wanabii kwa roho.” Na siri hiyo ilikuwa nini? “Yaani, kwamba watu wa mataifa wapaswe kuwa warithi waungani na washiriki-wenzi wa ule mwili na watwaaji pamoja nasi wa ile ahadi katika muungano pamoja na Kristo Yesu kupitia zile habari njema.”—Waefeso 3:5, 6; Wakolosai 1:25-27, NW.
18. (a) Paulo anaonyesha jinsi gani kwamba wakati ulihitajiwa ili kufunua maana ya “ile siri takatifu”? (b) Ni jinsi gani ufunuzi huu ungeathiri uelewevu juu ya yule “nyoka wa awali”?
18 Paulo aliguswa sana fikira na jambo la kwamba eti mtu wa namna yake angetumiwa kutangaza “zile habari njema juu ya utajiri usiopimika kina wa Kristo na kupaswa kufanya wanadamu waone jinsi inavyotekelezwa ile siri takatifu ambayo kutoka wakati uliopita usio dhahiri imekuwa ikifichika katika Mungu ambaye aliumba vitu vyote.” Au kama vile yeye alivyoweka wazo hilo kwa Wakolosai: “Ile siri takatifu iliyofichwa kutoka kwenye mifumo ya mambo iliyopita na kutoka kwenye vizazi vilivyopita. Lakini sasa imefanywa idihihirike kwa watakatifu wake.” Tukichukua mambo kiakili, ikiwa siri inayohusu ile “mbegu” ilifunuliwa kabisa hatimaye, hiyo ingehusisha ndani pia kuifunua wazi sura ya yule Mpinzani Mkuu, “yule nyoka wa awali.” Inaonekana wazi kwamba Yehova hakuchagua kufanya lile suala lake pamoja na Shetani liwe ndilo jambo kuu zaidi mpaka Mesiya aje. Na ni nani mwingine angefaa zaidi kuifunua wazi sura ya Shetani isipokuwa Mbegu hiyo, Kristo Yesu mwenyewe?—Waefeso 3:8, 9; Wakolosai 1:26, NW.
Yesu Amfichua Yule Mpinzani
19. Yesu alimfichua yule Mpinzani jinsi gani?
19 Mapema katika huduma yake, Yesu alimkataa Mshawishi huyo kabisa kabisa kwa maneno haya: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima wewe uabudu, na ni kwake peke yake ambako ni lazima wewe utoe utumishi mtakatifu.’” (Mathayo 4:3, 10, NW) Katika pindi tofauti, Yesu aliwafichua adui zake wachongezi wa kidini waliokuwa na madhumuni ya kumwua kwa kumlaumu wazi mwenye kuwasukuma kufanya hivyo na kumfichua kuwa ndiye nguvu iliyochochea yule nyoka katika Edeni, akisema, “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo [uongo].”—Yohana 8:44.
20. Yesu alikuwa na msingi gani wa kufichua Shetani?
20 Yesu angewezaje kuwa na uhakika mwingi jiivyo wa kumlaumu wazi Shetani? Yeye angewezaje kumjua vizuri hivyo? Ni kwa sababu yeye alikuwa amekuwa pamoja na Shetani katika mbingu! Hata kabla ya huyo kuasi kwa kiburi dhidi ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, Yesu, akiwa ndiye yule Neno, alikuwa amemjua. (Yohana 1:1-3; Wakolosai 1:15, 16) Yeye alikuwa ameona vitendo vyake vya kiufundi vilivyotendwa kupitia yule nyoka katika Edeni. Yeye alikuwa ameona uvutano wake wa werevu sana juu ya Kaini mwenye kuua ndugu yake kimakusudi. (Mwanzo 4:3-8; 1 Yohana 3:12) Baadaye, Yesu alikuwa katika ua wa kimbingu wa Yehova wakati ambapo “wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha . . . Shetani naye akaenda kati yao.” (Ayubu 1:6; 2:1) Oh, ndiyo, Yesu alimjua mpaka kwenye kiini cha utu wake na alikuwa tayari kumfichua aonekane jinsi alivyo—mwongo, mwuaji, mchongezi, na mpinzani wa Mungu!—Mithali 8:22-31; Yohana 8:58.
21. Ni maswali gani yanayobakia kujibiwa?
21 Akiwako adui mwenye nguvu nyingi hivyo anayetolea uvutano aina ya wanadamu na historia yao, maswali sasa ndiyo haya, Ni kwa kadiri gani zaidi Shetani anafichuliwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? Na ni jinsi gani sisi tunaweza kukinza mbinu zake za kiufundi na kudumisha ukamilifu wetu wa Kikristo?—Waefeso 6:11, Kingdom Interlinear.
[Maelezo ya Chini]
a Profesa Russell anataarifu katika kitabu chake The Devil—Perceptions of Evil From Antiquity to Primitive Christianity: “Uhakika wa kwamba Ibilisi anakuwa hajaonyeshwa kwa ukamili kabisa katika Agano la Kale si msingi wa kukataa kuwako kwake katika theolojia ya ki-siku-hizi ya Kiyahudi na Kikristo. Kuukataa kungekuwa ni kuwa na wazo lile lenye makosa ambalo limekuwapo tangu zamani—wazo la kwamba ukweli wa neno—au dhana fulani—unapatikana katika namna yalo iliyo ya mapema zaidi. Badala ya hivyo, ukweli wa kihistoria unaonekana wakati jambo linapoendelea-endelea kufanyika kwa kadiri muda unavyopita.”—Ukurasa 174.
Je! Wewe Unakumbuka?
◻ Ni vitendawili gani vinavyohusiana na Mwanzo 3:15 vilivyohitaji kuelezwa?
◻ Katika Maandiko ya Kiebrania mna ithibati gani juu ya uasi katika mbingu?
◻ Ni kweli gani mbili zinazotusaidia kuelewa ni kwa nini Shetani anatajwa kwa uhaba katika Maandiko ya Kiebrania?
◻ “Ile siri takatifu ya Kristo” ina uhusiano gani na kufunuliwa kwa Shetani na fungu analotimiza?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Uvutano wa Shetani ulionekana wazi miongoni mwa aina ya wanadamu katika ulimwengu ule wa kabla ya Gharika
[Picha katika ukurasa wa 10]
Shetani—mtu halisi—ndiye aliyetolea Mungu mwito wa ushindani kuhusu ukamilifu wa Ayubu