Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 15
    • Kufanya Kazi Chini ya Nira

      9, 10. Hapo zamani nira ilikuwa ishara ya nini, na kwa nini Yesu aliwaalika watu wachukue nira yake?

      9 Je, uliona kwamba katika maneno yaliyonukuliwa kutoka katika andiko la Mathayo 11:28, 29, Yesu alisema: “Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu.” Wakati huo, huenda mtu wa kawaida alihisi kana kwamba alifanya kazi chini ya nira. Tangu zamani, nira ilikuwa ishara ya utumwa. (Mwanzo 27:40; Mambo ya Walawi 26:13; Kumbukumbu la Torati 28:48) Wengi wa vibarua ambao Yesu alikutana nao walitumia nira halisi kubebea mizigo mizito kwenye mabega yao. Nira ingeweza kubebeka kwa urahisi au kuchubua shingo na mabega ikitegemea jinsi ilivyotengenezwa. Kwa kuwa Yesu alikuwa seremala, huenda alitengeneza nira, na alijua jinsi ya kutengeneza nira “ya fadhili.” Labda alifunga kwa ngozi au vipande vya nguo sehemu za nira ambazo ziligusana na mwili ili kuifanya iwe rahisi zaidi kubebeka.

      10 Yesu aliposema, “Chukueni nira yangu juu yenu,” huenda alikuwa akijifananisha na mtu aliyeuza nira zilizotengenezwa vizuri ambazo zingekuwa zenye “fadhili” kwa shingo na mabega ya mfanyakazi. Hivyo, Yesu aliongeza kusema: “Mzigo wangu ni mwepesi.” Hilo lilimaanisha kwamba nira hiyo ilikuwa rahisi kubeba, nayo kazi haikuwa ya kitumwa. Ni kweli kwamba kwa kuwaalika wasikilizaji wake wakubali nira yake, Yesu hakuwa akitoa kitulizo cha papo hapo kutokana na hali zote zenye kulemea wakati huo. Hata hivyo, maoni yake tofauti kuhusu nira yangeleta burudisho kubwa. Kurekebisha mtindo wa maisha yao na njia yao ya kufanya mambo kungewaletea kitulizo pia. Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba tumaini hakika na lenye nguvu lingesaidia kupunguza mkazo katika maisha yao.

      Unaweza Kupata Burudisho

      11. Kwa nini Yesu hakuwa akipendekeza tu ubadilishaji nira?

      11 Tafadhali ona kwamba, Yesu hakusema kwamba watu wangebadilisha nira yao. Roma ilikuwa bado inatawala nchi hiyo, kama vile serikali za leo zinavyotawala nchi ambako Wakristo wanaishi. Kodi iliyotozwa na Waroma katika karne ya kwanza haingeondolewa. Magonjwa na matatizo ya kiuchumi yangeendelea kuwepo. Hali ya kutokamilika na dhambi zingeendelea kuathiri watu. Hata hivyo, wangepata burudisho kwa kukubali mafundisho ya Yesu. Sisi pia tunaweza kupata burudisho kwa kufanya hivyo.

      12, 13. Yesu alikazia jambo gani ambalo lingeleta burudisho, na wengine waliitikiaje?

      12 Matumizi muhimu na yaliyo wazi ya mfano wa Yesu wa nira yalihusiana na kazi ya kufanya wanafunzi. Hapana shaka kwamba kazi kuu aliyofanya Yesu ni kuwafundisha wengine, huku akikazia Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:23) Kwa hiyo aliposema, “Chukueni nira yangu juu yenu,” hapana shaka kwamba kuchukua nira yake kungemaanisha kufanya kazi hiyohiyo. Maandishi ya Injili yanaonyesha kwamba Yesu alichochea watu wanyofu wabadili kazi zao, ambazo zilionwa na wengi kuwa muhimu sana maishani. Kumbuka mwito wake kwa Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana: “Nifuateni, nami nitawafanya nyinyi kuwa wavuvi wa watu.” (Marko 1:16-20) Aliwaonyesha wavuvi hao jinsi ambavyo wangeridhika kama wangefanya kazi aliyotanguliza maishani mwake, wakifanya hivyo chini ya mwongozo na msaada wake.

      13 Baadhi ya Wayahudi waliomsikiliza walielewa mafundisho ya Yesu na kuyafuata. Hebu wazia mambo yaliyokuwa yakifanyika kando ya bahari kama tunavyosoma kwenye Luka 5:1-11. Wavuvi wanne walikuwa wamemenyeka usiku kucha lakini hawakuvua samaki wowote. Kwa ghafula nyavu zao zikajaa! Jambo hilo halikutokea tu lenyewe; Yesu ndiye aliyelisababisha. Walipotazama ufuoni, waliona watu wengi waliopendezwa sana na mafundisho ya Yesu. Jambo hilo liliwasaidia kuelewa yale Yesu aliyowaambia wavuvi hao wanne: ‘Tangu sasa na kuendelea mtakuwa mkivua watu wakiwa hai.’ Waliitikiaje? “Wakarudisha hizo mashua kwenye nchi kavu, na kuacha kila kitu wakamfuata.”

      14. (a) Tunawezaje kupata burudisho leo? (b) Yesu alitangaza habari njema zipi zenye kuburudisha?

      14 Hata wewe unaweza kuitikia vivyo hivyo. Kazi ya kufundisha watu kweli ya Biblia bado inaendelea. Mashahidi wa Yehova wapatao milioni sita ulimwenguni pote wamekubali mwaliko wa Yesu wa ‘kuchukua nira yake juu’ yao, nao wamekuwa “wavuvi wa watu.” (Mathayo 4:19) Wengine hufanya kazi hiyo wakati wote; huku wengine wakiifanya kulingana na uwezo wao. Wote wanaburudishwa na kazi hiyo, kwa hiyo maisha yao hayana mkazo sana. Kazi hiyo inahusisha kufanya jambo wanalofurahia, yaani, kuwahubiria wengine habari njema—“habari njema za ufalme.” (Mathayo 4:23) Sikuzote inafurahisha kuzungumza kuhusu habari njema, hasa habari njema za ufalme. Biblia ina habari za msingi tunazohitaji ili kuwasadikisha wengi kwamba wanaweza kuishi maisha yasiyo na mkazo mwingi.—2 Timotheo 3:16, 17.

      15. Unaweza kunufaikaje na mafundisho ya Yesu kuhusu maisha?

      15 Kwa kadiri fulani, hata watu ambao wameanza kujifunza juu ya Ufalme wa Mungu hivi karibuni wamenufaika na mafundisho ya Yesu kuhusu jinsi ya kuishi. Wengi wanaweza kusema kwa unyofu kwamba mafundisho ya Yesu yamewaburudisha na kuwasaidia kubadili maisha yao kabisa. Unaweza kuthibitisha jambo hilo kwa kuchunguza kanuni fulani kuhusu maisha zilizotajwa katika masimulizi ya maisha na huduma ya Yesu. Masimulizi hayo yanapatikana hasa katika vitabu vya Injili ambavyo viliandikwa na Mathayo, Marko, na Luka.

      Njia ya Kupata Burudisho

      16, 17. (a) Unaweza kupata wapi baadhi ya mafundisho makuu ya Yesu? (b) Ni nini kinachohitajiwa ili kupata burudisho kwa kufuata mafundisho ya Yesu?

      16 Katika masika ya mwaka wa 31 W.K., Yesu alitoa hotuba ambayo inajulikana sana hata leo. Hotuba hiyo inaitwa Mahubiri ya Mlimani. Imeandikwa kwenye kitabu cha Mathayo sura ya 5 hadi 7 na kitabu cha Luka sura ya 6. Sura hizo zinaeleza kwa ufupi mengi ya mambo aliyofundisha. Unaweza kupata mafundisho mengine ya Yesu katika sura nyinginezo za vitabu vya Injili. Mengi ya mambo ambayo Yesu alisema ni rahisi kueleweka, ingawa inaweza kuwa vigumu kuyatenda. Mbona usisome sura hizo kwa makini? Nguvu za mawazo ya Yesu na ziongoze fikira na mtazamo wako.

      17 Ni wazi kwamba mafundisho ya Yesu yanaweza kupangwa katika njia mbalimbali. Na tupange mafundisho makuu ili tuwe na fundisho moja kila siku katika mwezi, tukiwa na lengo la kuyafuata maishani. Jinsi gani? Usiyapitie kijuujuu tu mafundisho hayo. Kumbuka yule mtawala tajiri aliyemwuliza Yesu Kristo hivi: “Ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Yesu alipotaja matakwa muhimu ya Sheria ya Mungu, mtu huyo alijibu kwamba tayari alikuwa anayatimiza. Hata hivyo, alitambua kwamba alihitaji kufanya mengi zaidi. Yesu alimwambia ajitahidi zaidi kufuata kanuni za Mungu kwa matendo na awe mwanafunzi mwenye bidii. Yaonekana mwanamume huyo hakutaka kufanya hivyo. (Luka 18:18-23) Hivyo, yeyote anayetaka kujua mafundisho ya Yesu leo anahitaji kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kukubali, na kufuata mafundisho hayo na hivyo kupunguza mkazo.

      18. Onyesha jinsi unavyoweza kutumia kwa manufaa sanduku lililoonyeshwa.

      18 Kama hatua ya kwanza ya kuchunguza na kufuata mafundisho ya Yesu, tazama fundisho la kwanza kwenye sanduku lililoonyeshwa. Fundisho hilo larejezea Mathayo 5:3-9. Naam, yeyote kati yetu anaweza kutafakari kwa muda mrefu ushauri mzuri unaotolewa kwenye mistari hiyo. Hata hivyo, unapotazama mistari hiyo kwa ujumla, unaweza kusema nini kuhusu mtazamo? Iwapo kwa kweli unataka kushinda madhara ya mkazo unaopita kiasi katika maisha yako, ni nini kitakachokusaidia? Unaweza kufaidikaje kwa kukazia uangalifu zaidi mambo ya kiroho? Je, kuna jambo linalokuhangaisha maishani ambalo unahitaji kulipuuza na badala yake kukazia uangalifu zaidi mambo ya kiroho? Ukifanya hivyo, utakuwa mwenye furaha zaidi sasa.

      19. Unaweza kufanya nini ili upate ufahamu na uelewevu zaidi?

      19 Kuna jambo jingine unaloweza kufanya. Mbona usizungumzie mistari hiyo na mtumishi mwingine wa Mungu, labda mwenzi wako wa ndoa, jamaa wa karibu, au rafiki? (Mithali 18:24; 20:5) Kumbuka kwamba mtawala huyo tajiri alimwuliza mtu mwingine—Yesu—juu ya jambo lililohusiana na habari waliyokuwa wakizungumzia. Jibu alilopata lingezidisha matarajio yake ya kupata furaha na uhai wa milele. Mwamini mwenzako unayezungumza naye kuhusu mistari hiyo hatakuwa sawa na Yesu; lakini, mazungumzo kuhusu mafundisho ya Yesu yatawanufaisha nyote wawili. Jaribu kufanya hivyo haraka iwezekanavyo.

      20, 21. Unaweza kufuata programu gani ili kujua mafundisho ya Yesu, na unawezaje kupima maendeleo yako?

      20 Tazama tena sanduku, “Mafundisho ya Kukusaidia.” Mafundisho hayo yamepangwa ili angalau uweze kufikiria fundisho moja kwa siku. Kwanza unaweza kusoma mambo aliyosema Yesu kwenye mistari iliyoonyeshwa. Kisha fikiria maneno yake. Tafakari jinsi unavyoweza kuyatumia maishani mwako. Ukiwa unahisi kwamba tayari unafanya hivyo, tafakari uone ni mambo gani zaidi unayoweza kufanya ili uishi kupatana na fundisho hilo la Mungu. Jaribu kutumia fundisho hilo siku hiyo. Ukiona ni jambo gumu kulielewa au kujua jinsi ya kulitumia, litafakari siku nyingine. Hata hivyo, kumbuka kwamba si lazima ulielewe kabisa ndipo utafakari fundisho jingine. Unaweza kufikiria fundisho jingine siku inayofuata. Mwishoni mwa juma, unaweza kuangalia uone jinsi ambavyo umefanikiwa kuyatumia mafundisho manne au matano ya Yesu. Juma la pili fikiria mafundisho zaidi, siku kwa siku. Ukiona kwamba umeshindwa kutumia mafundisho fulani, usivunjike moyo. Kila Mkristo atahisi hivyo. (2 Mambo ya Nyakati 6:36; Zaburi 130:3; Mhubiri 7:20; Yakobo 3:8) Endelea kufanya hivyo katika juma la tatu na la nne.

      21 Baada ya mwezi mmoja hivi, huenda ukafaulu kuchunguza mafundisho yote 31. Vyovyote vile, utahisije? Je, hutakuwa mwenye furaha zaidi, labda mwenye kustarehe zaidi? Hata kama hali yako itakuwa imeboreka kidogo, yaelekea mkazo utapungua, au angalau utashughulika na mkazo huo vizuri zaidi, na utajua jinsi ya kuendelea kufanya hivyo. Usisahau kwamba kuna mafundisho mengine mazuri ya Yesu ambayo hayakuorodheshwa kwenye sanduku. Kwa nini usitafute baadhi ya mafundisho hayo na kujaribu kuyafuata?—Wafilipi 3:16.

      22. Tunaweza kupata matokeo gani kwa kufuata mafundisho ya Yesu, lakini ni mambo gani mengine yanayostahili kuchunguzwa?

      22 Unaweza kuona kwamba nira ya Yesu ina fadhili kweli ingawa ina uzito fulani. Mzigo wa mafundisho yake na uanafunzi ni mwepesi. Baada ya kujionea mambo kwa zaidi ya miaka 60, mtume Yohana aliyekuwa rafiki mpendwa wa Yesu, alikubaliana na jambo hilo kwa kusema: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Wewe pia unaweza kuwa na uhakika kama huo. Kadiri unavyozidi kufuata mafundisho ya Yesu, ndivyo utakavyotambua kwamba maisha yako hayatakuwa na mkazo sana kama maisha ya watu wengi leo. Utaona kwamba umepata kitulizo kikubwa. (Zaburi 34:8) Hata hivyo, kuna jambo jingine unalohitaji kufikiria kuhusiana na nira ya Yesu yenye fadhili. Yesu pia alitaja kwamba yeye ni “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni.” Sifa hiyo inahusianaje na kujifunza na kumwiga Yesu? Tutachunguza jambo hilo katika makala ifuatayo.—Mathayo 11:29.

  • “Mjifunze Kutoka Kwangu”
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 15
    • “Mjifunze Kutoka Kwangu”

      “Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—MATHAYO 11:29.

      1. Kwa nini kujifunza kutoka kwa Yesu kunaweza kupendeza na kuthawabisha?

      SIKUZOTE Yesu Kristo alifikiri, akafundisha, na kutenda inavyofaa. Hakuishi muda mrefu duniani, lakini alifurahia kazi yenye kuthawabisha na yenye kuridhisha, na aliendelea kuwa mwenye furaha. Aliwakusanya wanafunzi wake na kuwafundisha jinsi ya kumwabudu Mungu, kuwapenda wanadamu, na kuushinda ulimwengu. (Yohana 16:33) Alijaza mioyo yao tumaini na ‘kutoa nuru juu ya uhai na kutoharibika kupitia habari njema.’ (2 Timotheo 1:10) Iwapo wewe ni mmoja wa wanafunzi wake, unafikiri inamaanisha nini kuwa mwanafunzi? Kwa kuchunguza mambo ambayo Yesu anasema kuhusu wanafunzi, tunaweza kujua jinsi ya kuboresha maisha yetu. Hiyo inamaanisha kukubali maoni yake na kufuata kanuni fulani za msingi.— Mathayo 10:24, 25; Luka 14:26, 27; Yohana 8:31, 32; 13:35; 15:8.

      2, 3. (a) Mwanafunzi wa Yesu ni nani? (b) Kwa nini ni muhimu kujiuliza, ‘Mimi nimekuwa mwanafunzi wa nani?’

      2 Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno linalotafsiriwa “mwanafunzi” linamaanisha hasa mtu anayekazia akili jambo fulani, au mtu anayejifunza. Neno linalohusiana na hilo linapatikana kwenye andiko letu la msingi, Mathayo 11:29: “Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Naam, mwanafunzi ni mtu anayejifunza. Kwa kawaida vitabu vya Injili hutumia neno “mwanafunzi” kurejezea wafuasi wa karibu wa Yesu, ambao walisafiri naye alipohubiri, na waliofundishwa naye. Huenda wengine walikubali tu mafundisho ya Yesu, wakifanya hivyo kisiri. (Luka 6:17; Yohana 19:38) Waandikaji wa vitabu vya Injili pia waliwataja “wanafunzi wa Yohana [Mbatizaji] na wanafunzi wa Mafarisayo.” (Marko 2:18) Kwa kuwa Yesu aliwaonya wafuasi wake ‘wajiangalie na fundisho la Mafarisayo,’ tunaweza kujiuliza, ‘Mimi nimekuwa mwanafunzi wa nani?’—Mathayo 16:12.

      3 Ikiwa sisi ni wanafunzi wa Yesu na tumejifunza kutoka kwake, basi wengine wanapaswa kuhisi wameburudika kiroho wanapokuwa nasi. Wanapaswa kutambua kwamba tumekuwa wenye tabia-pole zaidi na wenye hali ya chini moyoni. Iwapo sisi ni wasimamizi kazini, au ni wazazi, au ni wachungaji katika kutaniko la Kikristo, je, wale walio chini ya uangalizi wetu wanahisi kwamba tunawatendea kama Yesu alivyowatendea wale waliokuwa chini ya uangalizi wake?

      Jinsi Yesu Alivyowatendea Watu

      4, 5. (a) Kwa nini si vigumu kujua jinsi Yesu alivyowatendea watu waliokuwa na matatizo? (b) Ni nini kilitukia kwa Yesu alipokuwa akila nyumbani mwa Farisayo mmoja?

      4 Tunahitaji kujua jinsi Yesu alivyowatendea watu, hasa wale waliokuwa na matatizo makubwa. Si vigumu kujua jambo hilo kwa kuwa Biblia ina ripoti nyingi kuhusu jinsi Yesu alivyowatendea wengine, ambao baadhi yao walikuwa na matatizo. Na tuone pia jinsi viongozi wa kidini, hasa Mafarisayo walivyowatendea watu wenye matatizo. Ulinganisho huo utatufunza mambo fulani.

      5 Katika mwaka wa 31 W.K., wakati Yesu alipokuwa katika safari ya kuhubiri huko Galilaya, “mtu mmoja wa Mafarisayo alifuliza kumwomba ili ale mlo-mkuu pamoja naye.” Yesu alikubali mwaliko huo. “Basi akaingia katika nyumba ya huyo Farisayo na kuegama kwenye meza. Na, tazama! mwanamke aliyejulikana katika jiji kuwa mtenda-dhambi akapata habari kwamba alikuwa akiegama kwenye mlo katika nyumba ya Farisayo, naye akaleta chupa ya alabasta iliyo na mafuta yenye marashi, na, akichukua kikao nyuma kwenye miguu yake, akatoa machozi na kuanza kulowesha miguu yake kwa machozi yake naye akawa akiyafuta kwa nywele za kichwa chake. Pia, alibusu miguu yake kwa wororo na kuipaka mafuta yenye marashi.”—Luka 7:36-38.

      6. Huenda ni kwa nini mwanamke aliyekuwa “mtenda-dhambi” alikuwa nyumbani kwa Farisayo?

      6 Hebu wazia jambo hilo. Kitabu kimoja cha marejezo chasema: “Mwanamke huyo (mstari wa 37) alitumia pindi hiyo ambayo kidesturi watu wenye uhitaji waliruhusiwa kuwepo kwenye karamu hizo ili kuchukua chakula kilichobaki.” Hilo linaonyesha jinsi ambavyo mtu angeweza kuingia kwenye karamu kama hiyo bila kualikwa. Huenda kulikuwa na wengine waliotazamia kuchukua mabaki baada ya mlo huo. Hata hivyo, tabia ya mwanamke huyo haikuwa ya kawaida. Yeye hakutazama mambo tu akiwa pembeni, akingojea wakati wa mlo uishe. Alikuwa “mtenda-dhambi” mwenye sifa mbaya, aliyejulikana sana, hivi kwamba Yesu alisema kuwa alizijua “dhambi zake, ingawa [zilikuwa] nyingi.”—Luka 7:47.

      7, 8. (a) Tungetendaje kama tungekabili hali kama zile zilizoripotiwa katika Luka 7:36-38? (b) Simoni alitendaje?

      7 Hebu wazia kwamba uliishi wakati huo na ulikabili hali kama hiyo aliyokabili Yesu. Ungetendaje? Je, ungekuwa na wasiwasi kukaribiwa na mwanamke huyo? Hali hiyo ingekuathiri namna gani? (Luka 7:45) Je, ungeudhika au kushtuka?

      8 Kama ungekuwa mmoja wa wageni hao, je, ungekuwa na maoni kama ya Farisayo aliyeitwa Simoni? “Kwa kuona hayo yule Farisayo aliyemwalika [Yesu] akajisemea ndani yake mwenyewe: ‘Mtu huyu, kama angekuwa ni nabii, angejua ni nani na ni wa aina gani mwanamke anayemgusa, kwamba ni mtenda-dhambi.’” (Luka 7:39) Tofauti na Farisayo huyo, Yesu alikuwa mwenye huruma nyingi. Alielewa shida za mwanamke huyo na kufahamu jinsi alivyoteseka. Biblia haisemi jinsi alivyoanza maisha yake ya dhambi. Ikiwa kwa hakika yeye alikuwa kahaba, yaonekana watu wa mji huo, ambao walikuwa Wayahudi waliojitoa kwa Mungu, hawakumsaidia.

      9. Yesu alitendaje, na yaelekea matokeo yalikuwa nini?

      9 Lakini Yesu alitaka kumsaidia mwanamke huyo. Alimwambia: “Dhambi zako zimesamehewa.” Kisha akaongeza kusema: “Imani yako imekuokoa; shika njia yako uende kwa amani.” (Luka 7:48-50) Masimulizi hayo yanaishia hapo. Huenda mtu akabisha kwamba Yesu hakumsaidia sana mwanamke huyo. Alimbariki tu na kumwambia aende zake. Je, unafikiri aliendelea na maisha yake yenye kusikitisha? Ingawa hatuwezi kujua kwa hakika hali ilivyokuwa, ona maneno ya Luka yanayofuata. Alisema kwamba Yesu alisafiri “kutoka jiji hadi jiji na kutoka kijiji hadi kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme.” Luka pia aliripoti kwamba “wanawake fulani” walikuwa pamoja na Yesu na wanafunzi wake. Wanawake hao ‘waliwahudumia kutokana na mali zao.’ Kuna uwezekano kwamba mwanamke huyu mwenye kutubu na mwenye uthamini alikuwa miongoni mwa wanawake hao, na aliishi maisha yanayompendeza Mungu akiwa na dhamiri safi, kusudi maishani, na upendo mwingi kwa Mungu.—Luka 8:1-3.

      Tofauti Kati ya Yesu na Mafarisayo

      10. Kwa nini inanufaisha kufikiria masimulizi juu ya Yesu na yule mwanamke kwenye nyumba ya Simoni?

      10 Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo yenye kuvutia? Yanachochea hisia zetu, sivyo? Hebu wazia ukiwa nyumbani kwa Simoni, ungehisije? Je, ungetenda kama Yesu, au ungehisi kidogo kama yule Farisayo aliyemkaribisha? Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, hivyo hatuwezi kuhisi na kutenda sawa kabisa na alivyotenda. Kwa upande mwingine, huenda hatungependa kuwa kama Simoni, aliyekuwa Farisayo. Ni watu wachache sana ambao wangejivunia kuwa Farisayo.

      11. Kwa nini hatungetaka kufananishwa na Mafarisayo?

      11 Kwa kuchunguza uthibitisho wa Kibiblia na wa kilimwengu, tunaweza kukata kauli kwamba Mafarisayo walijivuna kuwa waangalizi wa masilahi ya umma na ya taifa. Sheria ya Mungu ilikuwa wazi na yenye kueleweka kwa urahisi lakini hawakutosheka na jambo hilo. Walipoona kana kwamba Sheria haikueleza mambo fulani waziwazi, walijaribu kuongezea maelezo yao kuifanya iwe wazi zaidi ili kusiwe na uhitaji wa kutumia dhamiri. Viongozi hao wa kidini walijaribu kubuni sheria za kuongoza mwenendo wa watu katika kila jambo, hata mambo madogo-madogo.a

      12. Mafarisayo walijionaje?

      12 Mwanahistoria Myahudi Josephus wa karne ya kwanza anaonyesha wazi kwamba Mafarisayo walijiona kuwa watu wenye fadhili, wapole, wenye haki, na waliostahili kabisa kwa kazi yao. Hapana shaka kwamba baadhi yao walikuwa na sifa zinazokaribiana na hizo. Huenda ukamkumbuka Nikodemo. (Yohana 3:1, 2; 7:50, 51) Baada ya muda, baadhi yao waliukubali Ukristo. (Matendo 15:5) Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi fulani, kama vile Mafarisayo: “Wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Hata hivyo, vitabu vya Injili vinaonyesha jinsi watu wa kawaida walivyowaona. Waliwaona kuwa watu wenye majivuno, wenye kiburi, wenye kujiona kuwa waadilifu, wenye kutafuta-tafuta makosa, wenye kushutumu, na kuwadharau wengine.

      Maoni ya Yesu

      13. Yesu alisema nini kuhusu Mafarisayo?

      13 Yesu aliwakemea waandishi na Mafarisayo kuwa wanafiki. “Wao hufunga mizigo mizito na kuiweka juu ya mabega ya watu, lakini wao wenyewe hawataki kuisogeza kwa kidole chao.” Naam, mzigo ulikuwa mzito, nayo nira ambayo watu walibebeshwa haikuwa ya fadhili. Yesu aliwaita waandishi na Mafarisayo “wapumbavu.” Mtu mpumbavu husumbua jamii. Yesu pia aliwaita waandishi na Mafarisayo “viongozi vipofu” na kusisitiza kwamba ‘walipuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.’ Hakuna mtu ambaye angetaka Yesu amlinganishe na Farisayo.—Mathayo 23:1-4, 16, 17, 23.

      14, 15. (a) Yesu anafunua nini kuhusu Mafarisayo kupitia jinsi alivyomtendea Mathayo Lawi? (b) Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na masimulizi haya?

      14 Karibu wasomaji wote wa masimulizi ya vitabu vya Injili wanaweza kuona kwamba Mafarisayo walikuwa wachambuzi. Baada ya Yesu kumwalika Mathayo Lawi, aliyekuwa mkusanya-kodi, awe mwanafunzi wake, Lawi alimwandalia Yesu karamu kubwa. Masimulizi hayo yanasema: “Ndipo Mafarisayo na waandishi wao wakaanza kunung’unikia wanafunzi wake, wakisema: ‘Ni kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya-kodi na watenda-dhambi?’ Yesu aliwajibu hivi: ‘. . . Nimekuja kuita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi waje kwenye toba.’”— Luka 5:27-32.

      15 Lawi mwenyewe alielewa jambo jingine ambalo Yesu alisema wakati huo: “Nendeni, basi, na mjifunze kile ambacho hili lamaanisha, ‘Mimi nataka rehema, wala si dhabihu.’” (Mathayo 9:13) Ingawa Mafarisayo walidai kwamba waliamini maandishi ya manabii Waebrania, wao hawakukubali maneno hayo kutoka katika andiko la Hosea 6:6. Waliona ni afadhali washikilie mapokeo kuliko kuonyesha rehema. Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza, ‘Je, mimi nina sifa ya kusisitiza sheria fulani zifuatwe, kama zile zinazounga mkono maoni yangu binafsi au njia za kawaida za kushughulikia mambo? Au je, wengine wanaona kwamba mimi ni mwenye rehema na mwema?’

      16. Mafarisayo walikuwa na mazoea gani na tunawezaje kuepuka kuwa kama wao?

      16 Mafarisayo walikuwa na mazoea ya kuwachambua wengine. Walitafuta kila kasoro—iwe ya kweli au ya kuwaziwa tu. Walishutumu watu kila wakati na kuwakumbusha kasoro zao. Mafarisayo walijivuna kwa kutoa sehemu ya kumi ya mimea iliyo midogo zaidi kama vile mnanaa, dili, na jira. Kwa mavazi yao walijionyesha kuwa watu wenye kumcha Mungu na walijaribu kuliongoza taifa. Kwa kweli, ili matendo yetu yapatane na kielelezo cha Yesu, ni lazima tuepuke mwelekeo wa kutafuta na kutia chumvi kasoro za wengine.

      Yesu Alishughulikaje na Matatizo

      17-19. (a) Eleza jinsi Yesu alivyoshughulika na hali ambayo ingekuwa na matokeo mabaya sana. (b) Ni nini kilichofanya hali hiyo iwe yenye wasiwasi na isiyopendeza? (c) Kama ungekuwepo wakati mwanamke huyo alipomfikia Yesu, ungetendaje?

      17 Yesu alishughulika na matatizo kwa njia tofauti kabisa na Mafarisayo. Fikiria jinsi Yesu alivyoshughulika na hali ambayo ingekuwa na matokeo mabaya sana. Ilihusu mwanamke mmoja aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka kumi na miwili. Unaweza kusoma masimulizi hayo katika andiko la Luka 8:42-48.

      18 Masimulizi ya Marko yanasema kwamba mwanamke huyo ‘aliogopa na kutetemeka.’ (Marko 5:33) Kwa nini? Bila shaka ni kwa sababu alijua kwamba alikuwa amevunja Sheria ya Mungu. Kulingana na andiko la Mambo ya Walawi 15:25-28, mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu usio wa kawaida angeendelea kuwa asiye safi wakati wa mtiririko na hata juma moja baada ya mtiririko huo kuisha. Kila kitu alichogusa na kila mtu aliyemgusa angekuwa mchafu. Ili kumfikia Yesu, ingembidi mwanamke huyo ajikakamue kupita katikati ya umati. Tusomapo masimulizi hayo miaka 2,000 baadaye, tunamhurumia mwanamke huyo kwa tatizo lake.

      19 Kama ungalikuwako siku hiyo, ungeonaje hali hiyo? Ungesema nini? Ona kwamba Yesu alimtendea mwanamke huyo kwa fadhili, upendo, na kwa kumjali, bila hata kutaja matatizo yoyote ambayo huenda alisababisha.—Marko 5:34.

      20. Kama andiko la Mambo ya Walawi 15:25-28 lingekuwa takwa la Kikristo leo, ungekuwa na tatizo gani?

      20 Je, tunaweza kujifunza jambo lolote kutokana na tukio hilo? Tuseme wewe ni mzee wa kutaniko la Kikristo leo. Isitoshe, tuseme andiko la Mambo ya Walawi 15:25-28 ni takwa la Kikristo leo na kwamba mwanamke Mkristo amelivunja takwa hilo kwa sababu ya kufadhaika na kutojua la kufanya. Ungetendaje? Je, ungemwaibisha mbele ya watu kwa kumshauri vikali? “Ah, mimi singeweza kamwe kufanya hivyo! Kwa kufuata kielelezo cha Yesu, ningejitahidi niwezavyo kuwa mwenye fadhili, upendo, ufikirio, na mwenye kujali.” Sawa! Lakini tatizo ni kuonyesha sifa hizo, kuiga kielelezo cha Yesu.

      21. Yesu aliwafundisha watu nini kuhusu Sheria?

      21 Kwa kawaida, watu walihisi wameburudishwa, wamechangamshwa, na kutiwa moyo na Yesu. Sheria ya Mungu ilipotaja mambo waziwazi, ilimaanisha tu kile ilichosema. Kama haikutaja mambo waziwazi, basi watu wangetumia dhamiri zao zaidi na wangeonyesha upendo wao kwa Mungu kupitia maamuzi yao. Sheria haikuwa na vizuizi vingi kupita kiasi. (Marko 2:27, 28) Mungu aliwapenda watu wake, akijishughulisha daima kwa manufaa yao, na alikuwa tayari kuwaonyesha rehema walipokosea. Yesu alikuwa hivyo pia.—Yohana 14:9.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki