Wakati wa Mavuno!
KWA nini historia ya “Ukristo” imekuwa isiyo na mfano wa Kristo hivyo? Watu wengi wenye kufikiri huuliza swali hilo, lakini Yesu alilijibu karibu miaka 2,000 iliyopita katika mfano mmoja. Alisema juu ya “mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake.” Kisha, “adui yake akapanda magugu katikati ya ngano.” Mbegu zilipochipuka, wafanyakazi waliyaona magugu wakataka kuyang’oa. Lakini mtu huyo akasema: “Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno.” Wakati wa mavuno, ngano ingetenganishwa na magugu.—Mathayo 13:24-30.
Akieleza mfano huo, Yesu alisema kwamba yeye mwenyewe ndiye mtu aliyepanda “mbegu njema”—Wakristo wa kweli. Adui alikuwa Shetani, aliyepanda “magugu” katikati—akipenyeza Wakristo wa mwigo ndani ya kutaniko. Yesu aliruhusu Wakristo bandia na wale wa kweli waweko pamoja—lakini hadi wakati wa mavuno tu. Kisha wangetenganishwa.—Mathayo 24:36-44.
Kwa hiyo, hatustaajabu tunapojifunza kwamba muda wa karne zote zilizopita matengenezo ya “Kikristo” yamemvunjia Mungu heshima kwa kukubali mafundisho ya kipagani, wakiachilia ukosefu wa adili, wakitegemeza vita vya ushindi, na kuongoza mabaraza yenye ukatili ya kuhukumu wazushi. Katika hayo twatambua ile mbegu mbaya iliyopandwa na Shetani. Hata hivyo, tunaposoma juu ya watu mmoja-mmoja waliopatwa na kifungo cha gerezani au kifo badala ya kuridhiana kanuni za Biblia, twaona kwamba mbegu njema haikufutiliwa mbali.
Yesu alisema kwamba wakati wa mavuno ulikuwa “umalizio wa mfumo wa mambo.” (NW) Kwa kuwa tunaishi katika umalizio wa mfumo wa mambo wa ulimwengu uliopo, lazima huu uwe ndio wakati wa mavuno! Kwa hiyo ni lazima iwe kwamba kutenganisha kwa Wakristo wa kweli na bandia kumetukia tayari. Leo, ni lazima kuweko watu walio kikundi, si watu mmoja-mmoja tu waliotawanyika, wanaofaana na simulizi la Yesu la Wakristo wa kweli—wanaojitiisha kwa Ufalme wa Mungu na kuhubiri habari njema juu yao, ambao huendeleza adili zenye msingi wa Biblia na kukatalia mbali mafundisho ya kipagani kwa kupendelea kweli ya Biblia, ambao hudhihirisha jina la Mungu na si sehemu ya ulimwengu.—Mathayo 6:33; 24:14; Yohana 3:20; 8:32; 17:6, 16.
Twakuhakikishia kwamba, watu hao wako! Je! wewe watamani kumtumikia Mungu kwa njia inayokubalika? Basi watafute watu hao, na umtumikie Mungu pamoja nao.